Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, October 17, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-9


‘Kumpenda kwasababu hizo,…mhh…naomba uwe na stahimili…sitaki nikujibu swali lako kihivyo…hilo la kupenda lipo wazi,…maana mengine yanaweza kuja kuwa kuni,…lakini si wewe mwenyewe umetaka, na nataka nikisafiri niwe na amani, au sio…sasa mimi nakuomba unisikilie kwa makini…nikuelezee ilivyotokea, …tafadhali…’akasema

‘Sawa uonavyo wewe uwanja ni wako, au sio…..lakini mimi nimeshajua kuwa ni nani unayemzungumzia, ni nani baba wa mtoto wako, hilo sina shaka,..na hata mume wangu japokuwa hataki kuliongelea hilo, eti anadai hayo ni mambo yetu hayamuhusu, lakini kwa namna fulani, anakubaliana na wazo langu….’nikasema.

‘Ina maana mlinijadili, ..si ulisema hutaongea naye sana kuhusu siri zetu…?’ akaniuliza

‘Tuliongea, yale ya kawaida, si lazima mtu aulize baba wa mtoto wako ni nani, na lazima wengi wataniuliza mimi, kwa vile mimi ni rafiki yako, na nimeshajipanga jinsi gani ya kuwajibu,..lakini kwa mume wangu nilitaka nichukue tahadhari, jinsi gani ya kumjibu, umenielewa hapo…’nikasema

‘Ok, sawa…’akasema

‘Kwani hajafika kukuona…alisema akipata muda atafika kwako, hajafika…?’ nikamuuliza

‘Keshafika…’akasema

‘Mhh, alikuuliza….kuhusu mtoto…?’ nikamuuliza

‘Mhh…ndio…lakini …tuliongea, …’akasita

‘Najua, …mume wangu sio muongeaji, sana, hawezi kukudadisii kivile, baba yake ni nani, una matarajio  gani, mengi anajua tumeshaonge, namfahamu sana..’nikasema


‘Sawa….utakuja kuelewa huko mbele ya maelezo yangu, kama utavuta subira…’akasema

‘Aaah, kama leo umeamua kunisimulia ukweli, nipo tayari kuvumilia mpaka umalize, nitafurahi sana…moyo wang utatulia,…’nikasema;

Tuendelee na kisa chetu…

***********

‘Basi siku ile, ya tukio la kwanza ilikuwa kama bahati mbaya, au ndio niseme ilipangwa itokee hivyo, kwani siku ile kulikuwa na sherehe ya kampuni yetu, huwa tunafanya hivyo mara kwa mara kwa namna ya kujitangaza, na kuwapa pongezi wafanyakazi kwa kazi fulani iliyofanikiwa….’akasema

‘Na sherehe kama hizo, familia inawajali sana familia na wafanyakazi, maana bila ya wao, wafanyakazi hawawezi kufanya kile walichofanya, tuna msemo hapo kazini kwetu kuwa juhudi ya mtu huanzia, nyumbani kwake…waingereza wanajua sana kuwale wafanyakazi wao…wajanja sana….’akasema

‘Ni kweli hata mimi najitahidi kuwafanyia hivyo wafanyakazi wangu….’nikasema

‘Basi kila mtu alipewa nafasi ya kuwaalika wanandoa wenza wao, na kama huna mwanandoa mwenzako, basi uje na mpenzi wako anayetambulikana, sio muhuni tu,…na wengi wanajulikana, hakuna siri hapo kazini kwetu,..au kama huna hata mpenzi, basi tulipewa nafasi ya kuja na hata ndugu yako..ilimradi kuwe na namna ya kupongezana kifamilia, na kijamii zaidi…’akasema.

‘Na wewe ukamualika nani, …hahaha, najua ulimualika yeye,  au sio…?’ nikajikuta nimemuuliza hivyo…nitamani asema ndio, ni yeye, lakini haikuwa hivyo….ila akilini mwangu nilishajua kuwa ndio huyo ninayemfikiria mimi.

‘Sasa cha ajabu siku hiyo sikuwa na mtu wa kumualika,..unajua tena wapenzi wangu walishaoa,..na nilikuwa kivyangu zaidi,…na siku hiyo,..sikuhitajia mtu, nilikuwa na yangu kichwani…’akasema

‘Mhh..kweli hilo…’nikasema

‘Kabisa kabisa sikutaka kuwa na mtu, nilikuwa nimetingwa na mawazo yangu maana siku zinakwenda, lile zoezi tulilolipanga halifanikiwi,…naona kama wanaume wannikwepa, na ninaokuwa karibu nao, siwezi kufanya nao…yaani ikawa shida, na  sikutegemea kuwa itakuwa vigumu hivyo.

‘Yah..kiu ukikidhamiria inakuwa hivyo…’nikasema

‘Ila kwa siku hiyo, kiukweli… nilitaka nisiwe na mtu karibu yangu anayeweza kunigusa…kunipa mawazo..nilitaka niwe peke yangu …, nilitaka hata kuwepo nisiwepo kwenye hiyo shughuli…, lakini ningeonekanaje na mimi ni mmoja wa mabosi wa vitengo, hapo nilipoajiriwa,,

Kwahiyo siku hiyo nikaingia kwenye ukumbi kivyangu, sikuwa muongeaji siku hiyo niliwaambia wenzangu kuwa sitaongea kabisa, ..niliwaambia naumwa, …najisikia vibaya, na wenzangu walinielewa, wao wakaongea, walichoongea, na akili haikuwa hapo kabisa....’akasema.

‘Wakati nimekaa naongea na wafanyakazi wenzangu, ..kikiwa ni kipindi cha kula na kunywa,…wenzangu wakawa  wananitambulisha familia zao, na wale waliokuja na watoto wao wakawa wananionyesha watoto wao,..basi hapo ndio nilikuwa sipataki…sio kwamba siwapendi watoto, wewe mwenyewe unanielewa, ila hisi fulani ndani kwa ndani…’akatulia

‘Nakuelewa sana…’nikasema

‘Mtu akiwa ana familia, ..anaweza hata kujingiza kwenye shirki, sio kwamba anataka,…maana inaumiza ndani kwa ndani, na huwezi kuelezea hilo labda liwe limeshakufika…

Basi, wakawa wakinionyesha watoto wao, najitahidi kuwaonyesha ile hali yangu ya kupenda watoto lakini moyoni naumia,…na mpaka ikafika muda…, najiuliza ni kwanini, wote hapo tupo umri mmoja wana familia zao, na wengine nimewazidi, lakini wameshabahatika kuwa na familia zao, kwanini mimi....kwakweli niliumia sana, hadi nikajikuta machozi yananitoka,...na kabla sijaonekana nikainuka …

‘Nilikimbilia washroom, kunawa nikiwa na maana nikitoka huko, sirudi tena kwenye sherehe, naondoka zangu kulala, na siku hiyo sikutaka kabisa kugusa kilevi, nilishadhamiria kuacha kilevi kabisa, niwe huru, niwe tofauti..…,

Sijui nilikaa muda gani, ila nililia sana,…sijui,..nilimlilia mungu wangu..sana, na kama mtu angeliingia akanigusa,..sijui…nilikuwa sio mimi… na nilipohakikisha machozi yamekwisha, nikatoka mle ndani,…, nikarudi pale mezani kwangu kwa nia ya  kuchukua mkoba wangu, niondoke zangu…lakini haikuwezekana.

‘Kwanini…?’ nikamuuliza

*********
‘Wakati nimetoka chumb cha kunawa, niliona mtu mgeni mezani kwangu…’akasema

‘Mhh, hapo hapo,….’nikasema

‘Tulia basi…’akasema

‘Kwasababu alinipa mgongo sikuweza kumtambua kwa haraka, na akilini mwangu sikutaka …kuongea na mtu, kwahiyo sikutilia maanani, nikawa nakwenda mwendo wa haraka kwenda kuchukua mkoba wangu, na sikutaka kuaga…’akasema

‘Ok…’nikasema

‘Pale nilihisi machozi kama yanataka kunitoka tena,..nikajikaza ki-kike…na..niliposogea nikashikwa na butwaa, sikutarajia kabisa,…’akasema

‘Una maana  ni …huyo bwana’ko...?’ nikajikuta nimemuuliza maana kwa muda ule nilikuwa nimetekwa na hisia za huruma, kama nilivykuambia awali rafiki akiumizwa na jambo ni kama mimi niliyeumizwa, kwahiyo hata mimi pale nilitamani kulia, lakini nikawa namuuliza maswali ilikupotezea….

Kiukweli usichanani kwetu ilikuwa hivyo, ikitokea tatizo la kuumia, kulia, kuhis jambo kwa mwenzangu na mimi nakuw ahivyo hivyo..sijui ilikuwaje, kwa watu wasiotufahamu wakituona walihisi sisi ni mapacha…maana  kama ni tukioa la kulia, tutalia sote…mmoja akiwa na furaha, basi tunafurahi sote, …kwahiyo maneno yake hayo hapo yalinifanya nitoe machozi na mimi….sasa uone kiasi gani tulivyokuwa tumeshibana.

Yeye hakujibu hilo swali mara moja…, muda huo alikuwa kimia kidogo, nahisi alikuwa akiwazia mbali,..basi ili kumpa unafuu, nikauliza swali la kumtoa hapo alipo

‘Si huyo bwanako mliozaa naye, au…?’ nikauliza hivyo kumchochea, nafahamu hapendi kuambiwa hivyo, na kweli, akainua kichwa na kuniangalia huku akisema kwa jaziba;

‘Huyo sio bwanangu bwana,…mume wa mtu atakuwaje bwana’ngu, …!’akasema kwa sauti ya kukereka…!

‘Nauliza ni huyo aliyekupa huo ujauzito,  au huyo unayefikiria kuwa ndiye aliyekupa mimba…, maana awali umesema huna uhakika,…na mpaka sasa hujaelewa, nakushangaa, ina maana ulipewa madawa ya kulevya au ilikuwaje …..hahaha  mtu wewe, yaani wanificha hata mimi,  haya ngoja tuone unataka nini ….?’ Nikamuuliza, hapo akatikisa kichwa tu.

‘Sio hivyo rafiki yangu, hujui nipo kwenye wakati gani sasa, unajua ..nilijua baada ya kumpata huyu mtoto, akili yangu itatulia,…nilijua kila kitu kitakwenda sawa,..lakini nashangaa sana,…nakuwa na wakati mgumu kuliko…lakini yote haya ni sababu ya ….anataka mambo ambayo …we acha tu…’akasema

‘Una maana gani hapo…?’ nikamuuliza

‘Nitakuja kukuambia tu…., wewe si unataka nikuambie…u-ukweli, subiria sasa, ila nakuomba tafadhali uwe na subira,…tafadhali sana, wewe ni rafiki yangu na hili tulilipanga pamoja, au sio..’akasema

‘Kwanini unasema hivyo..?’ nikamuuliza nikimuangalia moja kwa moja usoni, yeye akanikwepa na kuangalia pembeni.

‘Lakini si wewe umeamua tuvunje yale makubaliani yetu moja baada ya jingine…ulisema iwe siri, sasa unataka nikuambie ukweli, haya, au niache…?’ akaniuliza akiniangalia kwa macho ya kutia huruma

‘Ndio, nataka uniambie kila kitu,…wewe ndiye ulianza kuharibu, sasa endelea, nautaka sana huo ukweli,…, wewe ni rafiki yangu nilijua utaniambia tu,…huwezi kunificha jambo hata siku moja, … au sio....ila kauli yako inanipa mashaka, nahsi kuna jambo baya lilikutokea unaogopa kuniambia kuwa labda na mimi nitaumia, usijali, wewe niambie tu..…haya endelea, mimi sina wasiwasi na wewe, wewe ni ndugu yangu, kama kuna jambo limekutokea, siwezi kukutupa kamwe, niambie tu ilikuwaje…’nikasema

‘Mhh, wewe wasema tu, kwa vile hujausikia huo ukweli…lakini sina jinsi inabidi nikuambie tu…ila sitakuambia ni nani , ni wewe mwenyewe utamfahamu…kutokana na maelezo …sasa utakaloamua, sina jinsi…’ akasema na kugeuka pembeni.

Niliwaza huyu mtu ana maana gani, nikajikuta nasema

‘Wewe endelea bwana…acha kuniweka roho juu…’nikasema

‘Kumbe mjamaa alishafika muda, kwani nilimkuta anakula, sikujua kuwa nilichelewa sana chomba cha kunawia mikono, ni kweli nilichelewa nikiwa nimezama kwenye mawazo, mawazo ya mitihani niliyo nayo…ok, ndio hivyo….’akasema

‘Basi nikamkuta jamaa anakula...pembeni kilevi…nikajua ehee…kazi ipo leo,..sijui ni nani alimualika, maana mimi sijafanya hivyo, …japokuwa wengi pale ofisini walishaniona nikiwa naye, na wanajua ni nani kwangu, …na sijawahi kusikia mtu akiniongelea vibaya dhidi yake, maana wanamuheshimu sana…na, wanamfahamu kuwa ni mtu mstaraabu tu…’akasema

‘Yule..hahaha, mstaarabu, au maana ya ustaraabu hamuijui nyie, acha bwana, hata wewe unamuita hivyo,…hahaha, ..labda , kwasabbu ulishapenda, utasemaje, ukipenda chongo utaita kengeza au sio, hahaha, hata hivyo sikulaumu,…’nikasema

‘Ndio kupenda, nilipenda, kama nilivyowahi kukuambia awali lakini nilishaweka mpaka, kwa vile ni mume wa mtu..nielewe hapo….’akasema

‘Nakuelewa sana, mimi ninachokataa ni kumuita eti mstaarabu,…hana hiyo sifa kabisa,…labda, maana mtizamo wa watu, unatofautiana,…nikuambia kitu, na nilishawahi kukuambia, unakumbuka nilikuwambia huyo jamaaa alifanya nini kwangu…ananitongoza mimi, shemeji yake mke wa kaka yake, nilichomuambia hajawahi kurudia tena…’nikasema.

‘Mhh…sawa nakuelewa, ulishaniambia  bwana, hayo tuyaache, …ngoja niendelee au…?’ akaniuliza

‘Sawa endelea, …lakini usimvike sifa hiyo ya ustaarabu, hamtoshi….’nikasema

‘Utakuja kuelewa tu kwanini nasema hivyo…’akasema

‘Sawa endelea….’nikasema


‘Kwanza, nilitaka nigeuze , niondoke, ..kabla hajaniona, lakini macho ya watu, waliniona na yeye alipoona watu wanaangalia upande wangu, akageuka akaniona..ikawa haina jinsi, …nikasalimiana naye, naye akanikaribisha nikae utafikiri yeye ndio mwenyeji, mimi nikamwambia najisikia vibaya nataka kuondoka.

‘Aaah,…mimi nipo nitakupa dawa…’akaanza utani wake, unajua kuna kitu kimoja nilimpendea, anajua kumfariji mtu…na hata kama ulikuwa huna raha, utatulia tu, mna bahati sana mlioolewa….’akasema

‘Hata mume wangu ana tabia hiyo, ila kuna muda, akiwa na mambo yake, …hataki kusema, anaumia ndani kwa ndani, yeye akikuona upo huna raha, atakudadisi mpaka basi, lakini yeye, akiwa hana raha, ngumu kujua labda awe anataka kukuambia, anasema kuna mambo mengine ya kiume, sio lazima kumsumbua mkewe, basi, mimi najionea sawa tu, ila kiukweli hatufichani, …ndio hivyo tena, siku hizi, sijui uzee…’nikasema

‘Eti uzee, unanitisha mimi, una uzee gani….’akasema

‘Mkiishi sana na mwenzako, unajionea kawaida, hata ile …raha ya usichana inakuwa haipo, utaolewa utajionea wewe mwenyewe…’nikasema

‘Basi mimi nikazidi kumsihi kuwa najisikia vibaya yeye aendelee tu, …mimi naondoka kurudi nyumbani,…unajua alisema nini….’akawa kama anauliza

‘Yaani hiyo tabia gani,…mimi mgeni wako nimekuja, kwa ajili yako…, mwenyeji wangu unataka kuondoka, haiwezekani, kaa angalau kidogo, nimalize kinywaji, ..na hiki chakuka, ..au niaviache…?’ akauliza akiashiria kwa mkono pale mezani, uzuri pale mezani hakukuwa na mtu mwingine, watu walishajichanganya huku na kule,

‘Hapana wewe endelea tu wapo wengine mtaendelea nao, usiwe na shaka jisikia upo nyumbani…’nikasema sasa nikidhamiria kweli kuondoka.

‘Mimi wengine siwajui, nimekuja kwa ajili yako…nimekuja kukupongezeni, …na mimi ninayemfahamu hapa ni wewe…au nimekosea kuja, basi kama unaondoka, nikuombe kitu kimoja, wewe si unaumwa, subiri nimalizie hiki kinywaji nitakupeleka nyumbani kwako, vinginevyo ukae, au…?’ akaniuliza

Basi nikaona sio vizuri..nikaa kidogo, na yeye akaendelea kunywa,    nilishangaa kumuona shemeji akinywa kwa pupa siku hiyo ,… sio kawaida yake, ni kama alikuwa na kitu kinamkera,…hata sielewi… mpaka nikaingiwa na wasiwasi , kwanini anakunywa hivi.…’akasema

‘Lakini yule ni mlevi, anakunywa sana, hata kaka yake aliniambia, labda akiwa kwako ndio anajivunga, haya  ikawaje, …?’ nikamuuliza


‘Nikamtahadharisha kuwa kunywa kwa namna ile mimi sikupendi, anaweza akazidiwa ikawa shida kwangu, nikamwambia mimi naondoka,….akanizuia, akisema hii moja basi, hii moja basi..basi moja baada ya nyingine…’akasema.

‘Hapana shemeji…mbona leo hivi….?’ nikamuuliza

‘Usijali, siku moja moja, nafanya hivi, ili akili yangu iwe sawa,…nataka nikirudi nyumbani sisumbui kichwa changu tena, nalala tu, sitaki shida,..na leo sijisikii kwenda nyumbani, sitaki, na..na mambo yangu ya kufanya mengi ofisini, ikibidi nitenda kulala ofisini…’akasema

‘Shemeji mimi nakuhofia wewe, imetosha…’nikasema

‘Mhh, wanaume jamaani…., mimi sioni ajabu hata mume wangu kuna kipindi ilikuwa hivyo, mpaka nikawa sielewani naye, hasemi tatizo ni nini, anarudi kalewa, na ilikuwa sio kawaida yake, sijui, wakati mwingine najilaumu maana hizi kazi zinanifanya nakuwa mbali na mume wangu, ndio hivyo…’nikasema

‘Mhh, yawezekana, ndio maana ilitokea hivyo...’akaguna na kusema hivyo

‘Endelea na kisa chetu, nilitaka tu kukuambia kuwa hayo ya ulevi ni kawaida ya wanaume, hasa waliopo kwenye ndoa ...usijali sana, na wala usimwazie sana mtu kama huyo, kama kakupa ulichokitaka mpotezee, haya niambie ikawaje baadae naona muda umekwenda sana, ..’ nikasema.

‘Basi, aliendelea kunywa, na mimi sijui ikatokeaje, akanishawishi, nilianza na mimi kunywa kidogo, kidogo ooh… akawa ananiongelesha kunichkesha, utani, nakunywa, nakunywa,..weeeh, akili ikabadilika, nikawa nami nazipupia, …japokuwa kiukweli nilijitahidi kujizuia,…’akatulia

‘Mhh, kumbe…naanza kuipata picha….’nikasema
‘Basi bwana, ikafikia muda nikaanza kujisahau na mimi nikawa nakunywa kupitiliza, ila nikabakiwa na akili kidogo ya kukumbuka, hapo nikaingiwa na shaka..huyu mtu kalewa hivi atakwendaje nyumbani, sikujijali mimi, maana najua nitapara msaada kwa wenzangu, huwa wanafanya hivyo wakiona mmoja kazidiwa kwa kilevi,a pombe mbaya jamani...’akasema.

‘Nikatoka kidogo, kwenda `wash-room’ …nikampigia ndugu yake mmoja, ili kama akizidiwa ahakikishe anamchukua na kumfikisha nyumbani kwake…’akasema

‘Ok, namfahamu sana yule ndugu yake, wanasema eti ni mapacha,  sio mapacha ila wamepishana kidogo sana, kama miezi tisa hivi au pungufu ya hapo kidogo…, sijui ilitokeaje mama yao alishika mimba mapema, ..ndio hivyo tena, bahati mbaya, kwahiyo wanakaribiana sana, sio mapacha wale…’nikasema.

‘Nikampigia simu…kumbe alikuwa naye karibu tu, …akasema anatuona nisiwe na wasiwasi...’akasema.

‘Mhh, hata mume wangu akilewa mara nyingi anamuita mdogo wake aje amchukue...hilo ni kawaida kwa wanaume wengi, na wadogo zake kuna kipindi wanakosana na kaka yao kuna kipindi wanaelewana, damu ni nzito bwana asikuambie mtu ....’nikasema.

‘Ndio..naelewa hayo sana…’akasema

‘Ok, sasa ikawaje...?’ nikamuuliza.

‘Yaani baada ya kurudi mezani, akili hayo iliganda, sijui nilikunywaje,..sijui ilitokeaje, mengi nimekuja kuhadithiwa,…maana ninachokumbuka ni wewe kuwa kichwani mwangu na wazo lako hilo, kila mara unanighasi, ukisemaa…sasa fanya lile jambo wakati ndio huu… usimwachie huyu ..mshawishi, ...ukishindwa hapo basi tena..’

‘Mimi nipo kichwani mwako….?’ Nikamuuliza kwa kushangaa

‘Nakuona mbele yangu, ….nakusikia kichwani mwangu, unanishurutisha, nifanye kile tulichopanga nikifanye,…..akili ilikuwa sio yangu,…pombe mbaya, jamani..sitaweza kulisahau hilo…na yaliyotokea hapo, hapana….’akashika kichwa

‘Ikawaje sasa….?’ Nikauliza nikiangalia saa yangu

‘Nilijikuta nipo kitandani kwangu, nilivyofika, sijui…na wakati nazindukana, mara mlango unagongwa,…nikasema nikiwa nimejichokea ‘nani wewe, fungua mlango…mlango upo wazi,’

Mara mlango unafunguliwa taratibu, anayefungua anaonekana kama anaogopa,..halafu kama ana uhakika, akafungua mlango kabisa,

Mtu niliyemuona pale mlangoni, alinifanya nipandwe na hasira, sijui kwanini, nikasimama kwa hasira nikitaka kumfukuza, ..oh, najikuta nipo kama nilivyozaliwa..

‘Nani sasa…yeye, kwanini umkasirikie, na …ina maana hukukumbuka kilichotokea usiku….?’ Nikamuuliza

‘Sasa subiri kwanza, unajua ni kwanini nilikasirika, na huyo aliyeingia unamfahamu ni nani…?’ akaniuliza

NB: Naishia hapa kwa leo, kili imechoka kidogo


WAZO LA LEO: Kiukweli pombe kwa wanyaji huwezi kuwaambia kitu, lakini pombe ni sababu kubwa ya maasi,…imekuwa ni kichocheo cha kuharibika maadili, kuharibu ndoa..na kuharibu afya za watu, …wengi wanasema kuna faida ndani yake, lakini ukilinganisha faida na hasara , hasara ni nyingi zaidi. Nawausia wenzangu na kujiusia mwenyewe tuachane na ulevi…ewe kijana ewe mwanandoa, kulewa sio suluhisho la matatizo, bali ni kuahirisha tu tatizo kwa muda, tusijidanganye kuwa pombe inaondoa mawazo.
Ni mimi: emu-three

No comments :