Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, August 10, 2015

RADHI YA WAZAZI-29



Ni kituo cha polisi, ofisa mpelelezi alifika kwa mkuu wake akiwa na makabrasha ya kazi zake, na wakati wanamsubiria muendesha mashitaka, ikawa ni kazi ya ofisa huyu kumuelezea mkuu wake kazi ilivyokwishafanyika, akijua kuwa kuna mambo ambayo yanaweza kuja kuleta utata...

'Ehe endelea na maelezo yako,...kuna mauji,...kwanini imefikia huko..?' akauliza mkuu

'Ni kweli mtu mmoja kauwawa, ....na ....'akawa anaendelea kuelezea

‘Kwahiyo sasa ni kesi ya mauaji, sipendi hivi kabisa,....’akasema mkuu akisoma moja ya makabrasha.

‘Ndio mkuu....’akasema mpelelezi.

‘Na kwahiyo sasa imefikia hatua mbaya,...siwezi kukupa tena muda,...sasa nataka kujua wapi ulipofikia,...tulimalize hili jambo, huko juu nalaumiwa sana...’akasema

‘Mkuu, ..hata hivyo sihitajii muda tena kwani kazi niliyokuwa nikifuatilia imeshakamilika,...’akasema

‘Ok, kwahiyo kumbe  leo umakuja na kila kitu, nasema hivyo, kwa vile, hata mimi nakabiliwa na shinikizo kutoka juu kwa wakubwa,..na tatizo hili,  sasa limeinua hisia kubwa, hasa kwenye vyombo vya habari, kwa wananchi...sasa nambie kila kitu,...'akasema na mpelelezi akawa anatoa makabrasha yake kwenye mkoba wake.

'Si umesema upo tayari,...?’ akaulizwa na mkuu wake.

‘Ndio mkuu nipo tayari,...maana kama ujuavyo, walikamatwa hata watu wa habari,waendesha mitandao ya kijamii ambao hawaendani na maadili na ,nia na lengo ni kujaribu kuzuia hili jambo lisije kupotoshwa zaidi...hawa waliokamatwa kwa sasa wanatumiwa,ndio maana kumekuwa na sintofahamu nyingi....’akasema

‘Ukisema hili jambo, una maana gani, ni hili la hii kesi.?’ akaulizwa

‘Ndio, ....ni kuhusu hii kesi, mkuu...’akasema

‘Ok, endelea....’akasema

‘Katika hii kesi, kuna watuhumiwa wawili, kuna huyu ambaye tumeshamkamata tayari ni raia wa nchi za nje..., yeye ni wakala wa milungula, na kuna mwingine ambaye hatujamkamata, ni raia wetu....yeye anatumia sana watu wanamitandao, na kueneza propaganda za kuonyesha au kujenga chuki, katika jamii.....’akasema

‘Mhh.....hebu niambie zaidi kuhusu huyo mtu anayetumia watu wa mitandao, je kuna mahusiano ya  hayo mauaji na huyu mtu, na je alikuwa akishirikiana na huyo mshukuwa wa haya mauji?’ akaulizwa.

‘Mwanzoni tuligundua kuwa hawana mahusiano, kutokana na uchunguzi wa mwanzo, lakini tulipofanya uchunguzi wa kina tumekuja kugundua kuwa watu hawa wawili walikuwa wanafanya kazi pamoja,....’akasema.

‘Ok, swali langu muhimu kabla hautajaendelea je kundi hili lina mahusiano na yale makundi haramu yaliyokuwepo kipindi kile cha nyuma?....

‘Hapana...’akasema na kabla hajafafanua mkuu wake akasema

‘Unakumbuka yale makundi ya nyuma yalivyoharibu huu mji, na watu, hasa vyombo vya habari, wamefikia kusema kuwa  haya ni mabaki ya yale makundi haramu....na wanafikia kusema sisi watu wa usalama tulidanganya kuwa tumelimaliza hilo kundi,sasa iweje wimbi hili la mlungula, mauaji limeibuka tena....?’ akauliza mkuu.

‘Hili sio kundi kubwa...kama wanavyovumisha watu wa habari,na tutalimaliza haraka iwezekanavyo...na halihusiania kwa vyovyote  vile na makundi yaliyopita...ni kwa vile mbinu au kazi wanayoifanya inafanana fanana tu, na yale makundi ya zamani.....hawa ni vijana chipikizi kabisa.....’alikuwa ofisa mpelelezi akitoa taarifa kwa mkuu huyu ambaye alikuwa kasafiri, na aliporudi akataka kusikia wapi kazi hiyo imefikia.

‘Mbona dalili zake,...na harakati zake zinafanana sana na makundi yale yaliyopita...yawezekana hilo hamlikuliona?’ akaulizwa mpelelezi.

‘Hili kundi limejitokeza tu hivi karibu, ni chanzo chake ni athari za vijana kukosa ajira za uhakika, wamesoma, na utaalamu wanao, lakini hakuna ajira za uhakika..na wengi walisoma wakiwa na mategemeo ya kuajiriwa...’akasema

‘Hilo ni kweli....’akasema mkuu wake akitikisa kichwa kwani ana kijana wake msomi, kasomea mambo ya komputa, na ana uwezo mkubwa, lakini bado hajapata kazi, na katika kuhangaika, ...kijana wake akasema kagundua kuwa kuna mtu anaweza kumsaidia, yeye ni mtaalamu wa hali ya juu kwa mambo hayo...

Alikumbuka siku moja alipokuwa na kijana wake wakiongea, na alitaka ikiwezekana amuingize kijana wake kwenye kazi za uaskari, kama yeye, lakini kijana wake alikuwa hapendeleo kazi hizo,kijana wake alijikita zaidi kwenye mitandao na komputa.

‘Baba usiwe na wasiwasi,...nimehangaika na sasa nimempata mtu wa kunisaidia, kwani anasaidia watu wengi sana...’akasema

‘Yeye..ni nani, ni mtu, wa namna gani na  atakusaidia kwa vipi, ana kampuni au anafanya nini huyo mtu...?’ alimuuliza kijana wake

‘Ndio yeye ana kampuni yake mwenyewe, na sio kampuni moja tu..japokuwa wengi wanahisi hivyo kuwa ana kampuni moja,...ni mtu ana ujuzu wake mkubwa, na kaamua kuutumia ujuzi wake, sio kwake tu, pia kwa wengine...’akasema

‘Hivyo ndio inatakiwa,..elimu yako iwe na manufaa kwa watu wengine pia, ukiwa na ujuzi au utaalamu uwe ni sababu ya kusaidia na wenzako, na kuleta maendeleo, tunahitaji watu wa namna hiyo...’akasema baba mtu.

‘Kampuni yake inajihusisha na nini zaidi,....?’ akauliza

‘Yeye zaidi kampuni zake zote, japokuwa anajitanua zaidi kwa mambo mengine ili kuendana na wakati, lakini hasa, kwa kisaisi kikubwa anajishughulisha na mitandao, na biashara za komputa na vifaa vyake, anauza vifaa vyote vya kisasa vya komputa,kuweka mitandao majumbanina fani kama hizo....’akasema

‘Umeshaongea naye au nikaongee naye mimi mmwenyewe..?’ akamuuliza

‘Nimeshaongea naye na nimeshaanza kazi kabisa, nimepata ujuzi mkubwa kutoka kwake,....nilianza muda, sema sikutaka kuwaambia kwanza mpaka nihakikishe nina uhakika na ajira hiyo...’akasema

‘Vizuri sana, nataka hivyo, uwe unajisumbua mwenyewe, ila uwe makini,sio makampuni yote yanaweza kukusaidia kwa maisha yako ya baadaye....mengine yanakutumia wakifanikiwa wanakutupa.....nina uzoefu sana wa mambo ya ajira....’akasema

‘Ndio baba usiwe nashaka, kwa hilo....najua ni kitu gani ninakifanya, muhimu kwa sasa napata mahitajio yangu yote bila kukutegemeeni, na nikijaliwa na mimi nitaanzisha shughuli zangu binafsi...’akasema

‘Hiyo kampuni inamilikiwa na nani...?’ akaulizwa

‘Mhh,...huyu mtu, .... yeye anajulikana zaidi kwa jina moja tu, la Mtaalamu...japokuwa ana majina yake mengine..’akasema

‘Mtaalamu...mtaalamu....mmh, kwa kumbukumbu zangu huyu mtu, kama namfahamu.....’akasema

‘Ndio anafahamika sana, anasaidia sana watu,....anasaidia sana taifa kwenye maendeleo yake.....’akasema

‘Ok,.....sina uhakika kama ni huyo ninayemfahamu mimi,...unajua kijana wangu kulikuwa na jamaa mmoja alijulikana kwa jina hilo, ...Mtaalamu mtundu, akawa na kampuni kubwa sana,..tulikuja kumgundua kuwa alikuwa na biashara haramu ndani yake,.....’akasema

‘Baba, sio huyo....’akasema kijana akiangalia saa yake.

‘Najua sio huyo, nakuambia tu, kulikuwa na mtu kama huyo tukamgundua na tukaja kumfunga na kampuni zake, zimeshakufa....sasa uwe makini sana....’akasema

‘Huyu ana ujanja ujanja wa komputa, mitandao...au yupoje, maana wengine huamua kuutumia utaalamu wako,nia kubwa sio hasa kupata lakini kwa kisai kikubwa sio kwa njia za halali, wanatumia utaalamu wao kuiba, kuibia serikali....yeye kampuni yake ipoje...?’ akaulizwa

‘Baba, huyo sio mjanja mjanja ....ni mtu na fani yake, ni mtaalamu kweli, na ujuzi alio nao, sio wa kubahatisha...kausomea hadi ngazi za juu,...na aliona kuwa kuajiriwa hakumlipi, na ndio maana akaja kuanzisha kampuni yake mwenyewe,......na kampuni hiyo ikawa inajitanua....mimi napenda sana juhudu zake......’akasema

‘Ok....’akasema baba yake akimuangalia kijana wake kwa makini, anampenda sana kijana wake, na hataki aje kujiingiza kwenye matatizo....kilichomshangaza ni jinsi gani kijana wake akapata kazi, na akakaa kimia bila kumuarifu yeye mwenyewe,lakini hakuwa na shaka.

‘Dad, huyu mtu kawasaidia, vijana wengi walikuwa wakihangaika na ajira, ...si unamsiki anavyotoa msaada, ...sasa hivi kaanzisha kampuni ndogo ndogo nyingi, na kuwaajiri watu wengi....huyu anafaa hata kuwa kiongozi wa nchi, maana ni msaada mkubwa kwa taifa...’akasema

‘Mhh, kama ni hivyo, ....hata mimi nimeliona hilo, anaweza kuwa kiongozi mnzuri kwa maendeleo ya taifa, ...nitamtembelea ofisi kwake nione tutakavyoweza kumsaidia,...anafanya kazi nzuri....vizuri sana kijana wangu.....’akasema sasa baba mtu akifurahia kuwa sasa angalau mtoto wake atakuwa kwenye ajira yenye faida kwake na baadaye ataweza kuwekeza zaidi.

*******

Wakati anawaza hili,....mwenzake alikuwa akiendelea kumuelezea tatizo hili la ajira linavyowakabili vijana..

‘Kwahiyo kama unavyoona mkuu,...taifa na sio taifa hili sasa ni tatizo la dunia nzima, kuna tatizo la ajira.... ajira hakuna japo kweli vijana wapo wengi wanajiobidisha kusoma, elimu zinazotolewa ni za misingi ya kuajiriwa, sasa vijana wanaomaliza shule, vyuo, ni wengi, hebu niambia watakwenda wapi,.’akasema

Mkuu wake alitaka kumwambia kuwa kijana wake keshapata ajira ya uhakika, lakini akaona haina haja kumuelezea hilo kwa sasa...akawa anasikiliza tu.

‘Mkuu,na hata wale walioajiriwa wamejikuta wengine wakiachishwa kazi, kwani makampuni waliokuwa wakifanyia  yameshindwa kupambana na ushindani wa kibiashara,....hili ni tatizo jingine....’akatulia

‘Kampuni zinapokuwa nyingi, kama uonavyo wengi nao waliamua kujiajiri, wakaanzisha kampuni zao, kampuni zinaongezeka, kuongezeka kwa kampuni ni tatizo kwani kunatokea ushindani wa kutafuta masoko,....utaalamu unakuwa, na sehemu yenye watu wengi, wanahitajika watu wachache, wengi wanaondolewa....

Ina maana gani hapo,... makampuni mengi sasa yanaamua kupunguzwa wafanyakazi, kwa visingizio mbali mbali, wengine wakidai wanabana matumizi..... kwahiyo tunajikuta tuna wataalamu, na wasomi ...wengi  tu,wasiokuwa na ajira wapo mitaani,hawana kazi, ogopa kuwa na wasomi wengi, na wasiwe na ajira, wasiwe na malengo yoyote, kama huko Nigeria....’akasema

‘Sasa wale waliopunguzwa,wanakuja mitaani, wana utaalamu wao,wameshaonja pesa...wakifika mitaani, wanakutana na upinzani mnzito, kuna wenzao walishajiajiri tayari,....

'Na ukumbuke pia kujiajiri nako kuna changamoto zake, maisha ni magumu, hawa walitoka maofisini, hawana maandalizi yoyote, na ukumbuke huko walipokuwa wameajiriwa kipato kilikuwa kidogo,sasa hawajui waanze vipi maisha mapya ya kujiajiri...tatizo linaanzia hapo’akatulia

Wengine wanafanikiwa, lakini ndio wanajikuta katika kunyang’anyana wateje...tatizo juu ya tatizo...unaliona hapo mkuu....’akasema na mkuu wake akatikisa kichwa kukubali, huku kwa mbali akimuwazia kijana wake.

‘Kwa hali kama hiyo,...mwisho wake ndio hapo wanabuni njia mbadala ya kujipatia kipato, kwa kutumia migongo ya utaalamu wao,.njia zenye  muelekeo hasi ili kupata kipato,..na hizo njia nyingi,ni njia zisizo sahihi,na ndio chanzo cha haya makundi ya sasa...’akasema

‘Mhh, nimekuelewa, kweli,...hii kweli ni shida,maana mzazi umejitahidi umetumia gharama nyingi ukitegemea mafanikio kwa mtoto wako, lakini inafikia hatua unasema sasa mtoto kamaliza shule, anakwenda kupata ajira...lakini kazi hakuna, ajira sahihi hakuna, au mbinu za kujiajiri hakuna..kwakweli hilo ni tatizo....’akasema mkuu,

‘Ndio hivyo mkuu,...’akasema

‘Natumai utakuwa na ushahidi wa hayo yote kwani itafika wakati tutatakiwa kukutana na wana siasa,....’akasema akizama kwenye mawazo mazito

‘Hilo tutaliona huko baadaye....’akasema

‘Sasa swali hapo ni je ushahidi tulio nao watatuelewa, je utaweza kuwa..kamata hawa watu, au tutafute njia za kuwasadia, maana kama unavyoona watu hawa ni msaada mkubwa kwa vijana wetu na taifa kwa ujumla....’akasema

‘Mkuu,  huu sasa sio msaada kwa taifa, ni mnzigo....kama watu wanaamua kutumia mbinu chafu, hilo sio tegemeo, hilo ni kututengenezea janga, sijui umenielewa mkuu..’akasema

‘Nimekuelewa, sana, sana...ila nataka hili walione hawa viongozi wetu, na tusije kujenga uhasama..badala ya kusaidia jambo,..na pia wasije kukimbilia kutulamu sisi, kuwa  watu wa usalama ni chanzo cha vurugu......ni kazi kubwa sana kazi yetu ikihusisha na watu wa siasa, si umeliona hili, sasa mimi kama kiongozi natakiwa kuwa na hekima ya kila jambo...’akasema

‘Kwa ushahidi tulio nao watatuelewa, kwani athari zake zinawagusa hata wao wenyewe, wana vijana wao hawana kazi pia nalielewa hilo, kama tulivyo sisi... na wengine walioguswa na watu hawa, kwenye shughuli zao kabisa,kwani mambo yao ya chini kwa chini yaligunduliwa na hawa watu,..yakawa ni mtaji kwa hawa watuhumiwa...’akasema.

‘Ni kweli...’akasema na kutabasamu

‘Japokuwa wengine wakiingia kwenye mitego ya hawa watu hawataki kuja kwetu moja kwamoja,wanasubiria mpaka balaa litokee .....lakini wapo kwenye shida, hawana amani....na chanzo ni hawa watu wanaondesha hizi biashara haramu...’akasema mpelelezi

‘Kwahiyo kwa namna fulani,...hizi shughuli za hawa watu, zliwabana hawa watendaji waovu, wenye mambo ya chini kwa chini, ambao wanatumia siasa za mdomoni, kuwahadaa wananchi kumbe chini kwa chini wana mambo yao mabaya....?’ akauliza

‘Ukiweka kihivyo, unaweza kusema imesaidia, lakini kwa njia isiyo halali,....hawa wataalamu, waliwasoma hawa watendaji,....ni kweli, wakagundua kuwa uzaifu wao pia unaweza kuwa ni soko kwao, ...ndio maana mlungula umeshika hatamu sana, biashara ya udaku, umeshamiri....’akasema

‘Mkuu,..blackmail.. sasa ni hatari,kwani wanaofanyiwa hivyo nao wanajaribu kujihami kwa njia yoyote, hata ikibidi kuua, maana mtu anajiona anavuliwa nguohadharani, anajua atafirisiwa, ...hebu fikiria mtu kahangaika kupata pesa zake,leo anakuja mtu anamtaka azitoe .... ‘akasema

‘Lakini ni kwauzembe wao,kwanini wanaogopa kuja kutoa taarifa polisi..’akasemamkuu wake

‘Ni kutokana na vitisho,  ama watoe pesa au wayatangaze hayo machafu yao hadharani...ni njia isiyo halali,...lakini pia wao wanaogopa kujiabisha, wakija polisi, ina maana hayo machafu yao, hayana siri tena....una ona hapo....’akasema

‘Naelewa hilo,ika kitu ninachochelewa, hawa watu wana washabiki wao, hasa wana siasa...au sio,..., na huku kwenye hawa wahalifu wanaotumia mitandao, nao wana wapenzi wao, ...’ akatulia

‘Jambo kama hili, tunahitajika kuwa na ushahidi wa kutosha, hasa tukifika mahakamani, tuhakikishe tunashida,vinginevyo, tutaharibu kazi zetu....’akasema

‘Hilo mkuu usiwe na shaka,....’akasema

‘Shaka ni kuwa, hawa watu wana pesa watawatumia mawakili wajanja,...watatumia vyombo vya habari, watawashawishi watu ...kwahiyo tunahitajia ushahidi wa kutosha kuhakikisha tunalimaliza hili tatizo,....’akasema mkuu.

‘Ndio maana, tumechukua, muda....watu watafikiri tumeanza baada ya haya mauaji,..hapana mkuu,ulipo nipa hii kazi, niliamua kuifanya kwa undani zaidi, ndio maana kila mara nilikuwa nakuambia, bado,nipo muda....’akasema

‘Sawa kabisa...ndio maana hata mimi sikutaka kukulazimisha, kukuhimiza, ili tatizo liishe kabisa, lisije kujirudia tena..je hilo mumelifanyia kazi...?’ akaulizwa mkuu akionyesha kufurahiwa na kazi nzuri ya mpelelezi wake.

‘Ndio tunao ushahidi wakutosha, hatuna shaka na hilo mkuu, ...hilo tumelifanyia kazi, na kuna jambo jingine mkuu, nitaliongezea kwenye ushahidi wetu....’akasema

‘Jambo gani....maana nataka tumalizane na hili tatizo kwanza, je hilo linahusiana nah ii kesi yetu? akauliza kwa mshangao

‘Japokuwa hatutaeleweka kwa hilo,.... lakini sasa hili limekuwa ni tatizo, ni kuhusu hawa wahamiaji...hawa wahamiaji wamekuwa ni tatizo, kwani wanakuja na tabia zao, wengine ni wakorofi huko walipotoka,..na wengine walikuja wakitarajia maisha mazuri, ....lakini wamejikuta kwenye maisha magumu...ndio hapo wanaamua kujiunga kwenye haya makundi machafu, wanatumiwa...’akasema

‘Sasa hilo tutaongea na wenzetu wa uhamiaji...wahakikishe wanaoingia wana sababu muhimu, wakague uhalali wa hawa watu,..hilo lina uzito wake, lakini tutaona jinsi gani ya kufanya ni kikutana na wenzangu....’akasema mkuu

‘Ndio maana sikuliweka kwenye ushahidi wetu, ni jambo la kujitegemea....’akasema

‘Sasa, .. kwahiyo  inahitajika wote wanaohusika wakamatwe...’ akasema akishika simu akawa anaongeajambo na mkuu wake huku akikagua makabrasha yake.

‘Ndio hivyo mkuu....’akasema

‘Ok, kibali kimeshatoka, kwahiyo watuhumiwa wote wanatakiwa kukamatwa na kufikishwa mbele ya mahakama.., au wameshakamatwa,,?’ akauliza mkuu

‘Leo sijaonana na msaidizi wangu,nilimwambia ukiwa tayari, kama sijarudi afanye kinachowezekana....je hili zoezi lakuwakamata wahusikawote limeshafanyika?’ akaulizwa

‘Limefanyika mkuu, lakini sio wote tuliowakamata..., kuna ambao hawajakamatwa, ikisubiriwa kibali chako,....’akasema

‘Kwanini, maka kibali changu...?’ akauliza kwa mshangao

‘Kwa mfano kuna huyu mmoja ambaye tulikuwa tunamshuku siku nyingi,....ni mfanyabiashara mkubwa wa mitandao, na msaidizi wako alisema hatuwezi kumkamata mpakatupate kibali chako, na tulichofanya ni kumtumia, kwa hivi sasa yupo na watu wetu, nia ni kutaka kuhakikisha kila alichokifanya kinajulikana....’akasema

‘Ni nani huyo....?’ akauliza akikunja uso kwa mashaka

‘Huyu mfanyabiashara unamfahamu sana,ni muwekezaji mnzuri, ..’akasema akifungua makabrasha

‘Ndio ni yupi huyo, ...?’ akaulizwa mkuu akiinama kuangalia lile kabrasha.

‘Ni jamaa mmoja ....eeh, huyu hapa,...’ akawa anaonyesha picha yake, na kuendelea kusema

‘Yeye anajulikana  sana kwa jina moja la Mtaalamu...’akasema

‘Mtaalamu!..mtaalamu!,...una maana...haiwezekani, ina maana ni huyu, huyu mwenye kampuni kubwa ya mitandao...anayesaidia watu wasio na ajira...huwa anajitahidi sana kuwaajiri vijana wasio na kazi,,...haiwezekani?’ akauliza huku akonyesha usio kukubaliana na hilo.

‘Ndio huyo huyo mkuu ndio maana tukasubiria kibali chako, ikizingatiwa kuwa katika safari zako ulisema unakwenda kuangalia jinsi gani watu kama watakavyoweza kusaidiwa na serikali,kwa vile wanasaidia vijana, lakini kwa ushahidi ni mmoja wa mafisadi, waendesha biashara ya mlungula....’akaambiwa na mpelelezi,mpelelezi  alishangaa kumuona mkuu wake akikuna kichwa mara nyingi....

‘Haiwezekani....’mkuu akasema huku akisimama, na mara mlango ukafunguliwa na muendesha mashitaka akaingia.

WAZO LA LEO: Taifa likianza kujenga matabaka la wasio kuwa nacho na wenye nacho, elimu ikatolewa kwa misingi hiyo hiyo, wenye nacho wanapata elimu nzuri, na wasio nacho hawapati elimu sawa na wasio nacho, na kwahiyo hata ajira zikawa zinaelekea kwa misingi hiyo hiyo,...na kwahiyo hata viongozi wakawa wanagawana madaraka kwa misingi hiyo hiyo, siasa ikaingiliwa na wenye nacho hapo unategemea nini....rejea misingi ya ubepari.

Mimi najaribu kutafakari kwa maono,  umma wa walio wengi ambao ndio wasio kuwa nacho watafanya nini, ...nahisi amani itakuwa ni kitendawili, au , huoni kuwa umma wa waliowengi utakuwa na kinyongo, hasira na visasi vitajaa moyoni, na ikitokea kuwepo na sababu kidogo tu, inaweza kuwa ni chanzo cha machafuko yasiyo na kikomo, hivi sisi ni tofauti na huko kunaotokea vurugu, wananchi  ni sugu kiasi hicho....tumuombe sana mungu.

Ni mimi: emu-three

No comments :