Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, July 27, 2015

RADHI YA WAZAZI-23


Ni Njagu!

Profesa aliposikia hivyo akakumbuka jinsi alivyosikia habari za huyu mpelelezi wa kujitegemea,ilikuwa siku ile wakijipongeza wakiwa na mtaalamu wa dili na mitandao.

‘Katika kazi hizi zetu kuna watu wanasifika sana kupekenyua, I mean wapelelezi,  idara hiyo ina wapelelezi wa namna nyingi...siogopi sana, polisi....’akatulia

‘Polisi nimeshawasoma,na najua jinsi gani ya kupambana nao, ili mradi tu, kusitokee mauwaji...’akasema

‘Ila kuna hawa, wapelelezi binafsi, hawa njaa mbaya,....hawa ni wabaya sana, hasa katika upelelezi wa hizi dili zetu...kuna mtu mmoja mbaya sana,..., mtu huyu wanamuamini sana,...kiukweli kazi hiyo anaiwezea sana kuwafichua watu wa mlungula,....’akasema

Ni nani huyo...?’ akauliza

‘Ni askari mmoja njaa kali, anaitwa Njagu...’akasema Mtalaamu siku wakisherehekea fungu la kwanza kutoka kwa mtu wao.

‘Njagu, ndiye huyo...?’ akauliza kama vile hamfahamu

‘Ndiye huyo huyo aliyepewa kazi hiyo na mama mtemi, mpaka akakupata ....unajua ni kwanini..?’ akawa kama anauliza

‘Hapana ..hata mimi nilishangaa sana...maana mambo yangu yalikuwa ni siri kubwa sana, sikumhusisha mtu....’akasema

‘Hukuhusisha watu, hahaha, wewe hukuenda kuwauliza baadhi ya watu kuhusu maisha ya huyo mama, ukapita huku na kule, unajua mimi huyo mama namfahamu, na kwa vile namfahamu sitaki kabisa kumuingilia, tunajuana na hatuingiliani, unasikia sana, sasa kwanini ulimfuata huyo mama.....?’ akauliza

‘Nilikuwa sijui,...unajua kila ninapofanya kazi kwa mtu nikipata sababu ya kupata pesa, huwa siangalii huyu ni nani...ndio hivyo tu,...kwahiyo nilipopata nafasi hiyo ikabidi nidadisi kupata uhakika...’akasema

‘Basi kwa kufanya hivyo, ulijichora, uliweka nyayo za miguu yako kila ulipopita..’akasema

‘Mhh...nilikuwa makini sana, sikuuliza kinamna ya kujiweka wazi...’akasema

‘Kwa mtu kama njagu, dalili ndogo tu, inamfanya ajue mengi...namuamini sana kaika upelelezi,..unajua polisi walifanya makosa kumsimamisha mapema huyu mtu, wangemfunda, na kumtumia katika kuwatafuta watu kama nyie...’akasema

‘Eti watu kama sisi, wewe je....eeh,Ina maana aliachishwa kazi idara ya polisi...?’ akauliza

‘Alikuwa askari mpelelezi wa ngazi za juu..., akafanya makosa mengi tu, wakamsimamisha kwa mujibu wa sheria..lakini sio kwa kumfukuza, kilichotumika ni yeye kujiuzulu...ilitumika hekima fulani aonekane hakufukuzwa....na ndio maana wakampa kibali cha upelelezi wa kujitegemea...’akasema

‘Mhh, mtu mkosaji lakini bado wampe leseni, ....hapo siamini....’akasema

‘Polisi ni wajanja, wao wanataka kumtumia kama mpini kwenye shoka,...na ni kweli kwakupitia yeye wameweza kuwakamata wahalifu wengi tu, kwa vile yeye alishahusishwa na makundi ya wahalifu,na nia yao kwasasa ni kutaka kuja kumkamata hata yeye lakini wanatafuta ushahidi wenye mshiko....’akasema

‘Kwanini sasa wamuogope...?’ akauliza

‘Sio kumuogopa...kama ulivyosikia, nyuma kulikuwa na kundi baya la wahalifu, na ni kipindi hicho Njagu alikuwa kashika usukani, ...idara ya polisi , katika kuchunguza wakagundua kuwa, alikuwa na mahusiano kwa namna moja au nyingine na haya makundi....’akasema

‘Kwa vipi...?’ akauliza

‘Huyu jamaa ana tamaa, alikuwa akipata pesa kutoka kwa wakuu wa haya makundi, japokuwa haikuonekana moja kwa moja....na mmoja wa wakuu wa hayo makundi anafahamika, ni huyo mama mtemi,...ndio maana unaona wapo sambamba....huyo mama anafahamu makundi yote ya mitaani, na huyo Njagu, halikadhalika....’akatulia

‘Mhh, kumbe.....’akasema

‘Kwahiyo uwe mbali na hawa watu wawili, huwezi kuwaficha kitu kuhusu ujambazi, kuhusu mlungula, kuhusu......wanajua kila kitu...’akaambiwa

‘mhh kumbe, Ningelijua...’akasema

‘Hahaha..ungelijua, kama uliingia anga zao, ujue unao..ujue  unalo,..hasa huyo mama hatakubali mpaka ahakikisha haupo,... unapotea, au unakwenda kuozea jela, na huko jela ana watu wake, ukiingia huko wewe ni maiti mtarajiwa....’akasema

Alipoyakumbuka hayo, ndio maana akauliza swali hilo kwa mashaka;

Oh,...ina maana kumbe keshamtafuta mpelelezi tayari,  na ni nani huyo mpelelezi,ni...Njagu  nini...?’ profesa akauliza

*********
‘Ndio ni huyo huyo,NJAGU...unakuambuka nilishakuonya kuhusu huyo mtu...’akasema
‘Nakumbuka ndio maana naogopa sana....’akasema
‘Hata hivyo kwangu mimi simuogopi sana huyo mpelelezi ...’akasema mtaalamu
‘Kwanini, na wewe uliniamba kuwa huyo mpelelezi anayafahamu makundi yote ya wakorofi hapa mjini na ni mtu makini sana, tofauti ni kuwa ana tamaa sana...’akasema
‘Ni kweli, ila mimi ni mjanja zaidi yake,...mtalaamu wa mambo yote yanatokea , yeye mwenyewe  ananifahamu kwa hilo , ...ananifahamu na namfahamu...., ‘akasema
‘Kwahiyo...?’ akauliza profesa
‘Ila ikibidi nitaongea naye, ila kwa jinsi alivyo na tamaa, na njaa yake kali, atahitajia pesa hapo ndipo nampatia.... huyo mtu yupo mkononi mwangu,hanitishi kabisa lakini kuwe na pesa ya kutosha, unaona ilivyo, iabidi nitumie pesa nyingi sana wakati mwingine, ila kwa huyu nafahamu sehemu gani ya kumpatia, hanitishi.....’akasema mtaalamu
‘Unataka kusema nini sasa...?’ akauliza Profesa
‘Huyo mtu nimeshamsaidia sana,... vinginevyo angelishakamatwa kwa makosa ya uuaji, unajua katika kuziba mapengo yake alijaribu sana kuwanyamazisha wale wote waliotaka kutoa taarifa zake,...nina skendo zake nyingi tu, ana mauchafu yake mengi nimeyahifadhi,....hata hivyo kwa sasa nataka nione nyendo zake...anataka kufanya nini..., najua mwisho wa siku atanijia kutaka taarifa fulani fulani..’akasema
‘Mhh kumbe....nimekuelewa,kumbe hata hao watu wanakuja kwako..’akasema kwa kuonyesha mshangao
‘Huyu mtu ni mjanja sana yeye anawashinda watu wa usalama kwa vile anauma huku na huku, anachua vichochoroo vyote vya watu wakorofi, anakula nao,unasikia sana.....ile ukijifanya kumuendea kwa kasi anaweza kukushushua ukajiona mjinga,..mimi sio mjinga, mimi ni mjanja, na kwahiyo nahitaji njia za kumbana....’akasema
‘Kwahiyo utanisaidia au sio maana hii sasa inahitajia utaalamu wako au sio....?’ akauliza
‘Nitakusaidia...hahaha kwa vipi, mimi nazungumzia upande wangu, kama atapewa kazi na huyo mtu, najua mwisho wa siku anaweza kunifikia mimi,....sasa...nitapambana naye...nina hamu sana ya kupambana  na huyu mtu maana kila akipewa kazi anajaribu kunipima, anataka kupambana na mimi ili nionekane mimi mjinga.....’akasema
‘Mhh, mimi hata sikuelewi, ina maana unafanya mzaha...hii sio kazi ya kupimana ujanja, ...huyo ni mpelelezi, na hana tofauti na watu wa usalama,sema ni kwa vile anaifaya kibinafsi, au sio, sasa hapo hapataki mzaha ....’akasema
‘Hahaha,ukiwa kwenye anga zangu, wakati mwingine, unahitajia changamoto, unapopata changamoto, unaongeza utaalamu zaidi, unajua kipi kimepungua ili ukitafutie ujuzi zaidi, sijapata changamoto kwa muda sasa, akili yangu imelala, .....’akasema
‘Mhh, ...hapo sitakuelewa...’akasema
‘Sio kazi yako kunielewa,...wewe fanya yako yanayokuhusu....mimi najua jinsi gani ya kujilida,....hili eneo lipo kwenye anga zangu, nawaona wote mchana mkihangaika na usiku mkitenda yasiyotakiwa,na mimi  hapo ndio nawashindia watu wangu, usiwaone watu wamevalia masuti mchana, usiku ni watu wabaya sana...’akasema.
‘Mhh, ungekuwa kwetu ungeitwa mchawi...’akasema profesa
‘Mhh,lakini mchawi wa utaalamu wa kisasa......sasa eeh, unataka nini zaidi...?’ akasema
‘Najua kuwa hii sio kazi yako, lakini kumbuka unachezea shilingi chooni, pesa hiyo tunaweza kuikosa na ni pesa nyingi, ...tukiiachia, kwa kutaka kupimana na huyo mtu, itakuwa ni hasara...’akasema

‘Kwangu mimi sio hasara,...sifanyi kazi ya hasara....najua ni nini ninachokifanya...’akasema

‘Sasa huoni kuwa kuna kukamatwa na watu wa usalama kwa makosa kama hayo...wewe unabuni dili za kuwadhulumu watu haki zao kwa kutengeneza uchafu wao na kuwatishia nao, kwa minajili ya kupata pesa...’akasema profesa

‘Mimi siwadhulumu watu, mimi natumia ujuzi wangu kwa manufaa ya kuzalisha, ujuzi ninao, sasa niupeleke wapi,....nitangaze dini, hahaha, nikuambie kitu, mimi siogopi kukamatwa, hasa nai mtu kama njagu....huyo ndiye kabisa haniwezi kunikamata kwa kosa lolote, ....mimi ni mtaalamu bwana....’akasema huku akicheka

‘Mhh,....’profesa akaguna tu

‘Njagu,...anajua hilo, ila anaweza kuwakamata watu kama nyie, watu ambao anafahamu hawawezi kupambana na yeye..., hilo ndugu yangu siwezi kukuficha,huyo jamaa akiamua atawatia hatiani...lakini  sio mtu kama mimi ...’akasema

‘Kwanini na wewe ndiye unayetupa hizo dili....?’ akauliza profesa

‘Unajua sheria wewe, ...wewe ni mtoto mdogo, uambiwe ukaibe, ukaue,...hna unajua ni kitu kibaya, ufanye halafu useme nilielekezwa na yule.....haiji ....’akatulia

‘Halafu mtu mwenyewe yule pamoja na ujanja wake wote wakati mwingine ananitegemea mimi, hapo ndipo mimi namshidia, mimi ni mjanja...hahaha’ akacheka kwa dharau

‘Hata hivyo,.... ni lazima nifanye jambo,maana dili hii ina pesa nyingi, na huyu jamaa akianza kazi ya kuchunguza, ni lazima atanusa , atajua kuwa dili hii ina pesa, na akijua hilo, mhhh, atazing’ang’ania, unaona eeh,.... sasa mikono itakuwa mingi na hapo sizani kutakuwa na kitu cha maana, pesa itapungua sana....’akasema

‘Umeonaeeh, tutapata pesa ndogo kwa kugawana watu wengi au sio...sasa hakikisha unanisaidia, ...si unaliona hilo,....sasa tusaidiane,wewe wabane hao watu, hasa huyo mpelelezi, ili niwewe kucheza na huyu mtu wetu au sio...’akasema

‘Kiukweli hii pesa itakuwa ndogo sana,vinginevyo watu wapungue ....sasa ni nani atoke.....’akawa kama anauliza

‘Nani atoke.....?’ akauliza profesa

‘Kwanza ukumbuke kwa mimi kulifanya hili inakubidi wewe uongeze kiwango changu cha ushuru, hicho ni kitu baki kabisa....sasa kama unataka niendelee kukufuatilia mambo yako, hayo ni makubaliano mengine ..kwani hiyo ilikuwa ni kazi yako, subiri nipige mahesabu kidogo hapa eeh,....’akasema huku akiwa anafanya mahesabu yake.

‘Mtaalamu wewe nakuaminia,kwa hivi sasa inabidi iwe hivyo,ila kwanza kumbuka ombi langu ni muhimu sana, nipate pesa kwa ajili ya huyo mama...na...mtu kama Njagu, siwezi kupambana naye sijui mengi sana kumuhusu yeye,...hilo nakuachia wewe au sio...’akasema

‘Kwa mtaji huo , itabidi Njagu aingie kwenye mgawo,....sasa tutakuwa watu wengi,...mhh, kipato kitakuwa kidogo, aah, haitoshi lazima watu wapungue,....’mtalaamu akawa anaendelea kupiga mahesabu yake.

‘Mimi hapo unaposema kupungua ni nani wa kupungua maana sote ni washika usukani, utamtoa nani, ....hebu nambie...sikuelewi hapo kabisa....’akasema profesa.

‘Huwezi kunielewa...lakini mwisho utasema....’akasema profesa

‘Na ukumbuke pia, huyu mtu wetu pia, kama ulivyoshauri, ....sijafika kwake kwa muda sasa, ningekuwa nafika pale nyumbani kwao, ningelijua ni nini anachokifanya,unaona hilo,kwahiyo hapo nakutegemea wewe pia kujua kinachoendelea ili nikiongea naye asije kuniona tapeli...’akasema

‘Tapeli, tapeli mara ngapi.....mmh, ukimweka njagu hapa....’ilionekana mtaalamu alishazama kwenye mahesabu ya pesa.

‘Lakini mtaalamu, wewe umezama kwenye mahesabu ya pesa, Je kweli huyo jamaa atazitoa hizo pesa....usipige mahesabu ya pesa wakati hujajua kuwa zitapatikana kweli wakati mkewe keshaziingilia, hilo kwanini hulioni...’akasema profesa

‘Poaaah, sasa.....nimeona kitu, ila  zitakutoka pesa nyingi sana, kwasababu Njagu ni lazima aingizwe kwenye mgawo...na usikie kabisa mimi sina pesa kwa ajili ya huyo mama mtemi, kwahiyo sitaki kabisa hilo wazo lako la kuwa mimi nikukopeshe pesa kwa ajili ya huyo mama, hiyo pesa hapa kwenye mahesabu naiondoa haipo....’akasema

‘Lakini sasa nitapatia wapi pesa za kumpooza huyo mama, namfahamu alivyo, nikimpa kitu kidogo, atalainika...., na kiukweli bila kuwa na pesa huyo mama ataniweka kubaya, atanifunga, na mimi siwezi kwenda jela, najua nikienda  huko wataniua...’akasema profesa

My, my.....ok, sasa.....mhh, pesa itakuwa ndogo sana, ...ngoja nione cha kufanya,....kwa hali hiyo, ukitoa ushuru wangu, kitakachobakia ni nusu kwa nusu,nuusu kwa nusu eeh, nusu kwa yap...’akasema

'Nusu kwa nusu....!?' akauliza profesa hakuwa anaelewa mwenzake anafanya nini huko, hakujua kuwa mwenzake akili yake imezama kwenye mahesabu

‘Unaona hapo, na nusu yako sasa, itabidi ugawane na Njagu,... na wala sio nusu kwa nusu, maana hao kwanza, ....mmh hii ni kutoka kwenye nusu yako, au sio,..utakuwa na deni langu, halafu itakayobakia unagawana na Njagu,...sasa hapo sawa....huku kwako, kunaisha,..., sijui kama wewe utakibakia na kitu,..sizani ngoja tuone...mmmh huyu Njagu atalalamika ...vinginevyo, wewe u-o-ndo-ke,....mmh, sijui...’akasema mtaalamu

‘Haiwezekani, unasema nini... hapo utaniumiza nitawezaje kulipa madeni ya watu, unajua mimi nadaiwa sana, mama mtemi, kuna madeni mengine, nilikuwa nakaa hotelini, kwani si unajua tena, sina pa kuishi.....’akalalamika profesa

‘Haya kama unaona utaweza kufanya kazi kazi mwenyewe,... basi,beba mzigo wako mwenyewe, ila...mmh hapana , utaharibu kabisa hii dili nikikuachia mwenyewe, unajua unaniharibia mahesabu yangu,..halafu naona kwa jinsi ilivyo, wewe sasa utaniletea kiwungu -cheusi,sijui niifanye hii kazi mwenyewe, na Njagu, wewe ni gharama tu, hasara tupu ...’akawa anasema

‘Peke yako kwa vile imeshafikia sehemu ya kuchuma ndio unataka kunisaliti au sio, ujue pesa haijapatikana bado na mimi ndiye atakayefanya ipatikane...unaona hapo, sasa mimi nakuwa gharama kwa vipi, wakati ndiye mtafutaji...wewe nisaidie hao watu unasikia mtaalamu, usije kufanya ujanja ujanja wako....nakuelewa wewe ,umeshaanza tamaa zako....’profesa akawa analalamika

‘Unajua umeiharibu sana hii dili, sikupenda, ulivyoendesha hii dili, unajua nilikuamini sana, lakini umeharibu kabisa, umefanya mambo utakavyo wewe....unajua ulichofanya...unajua ulichokifanya mpaka naingia gharama nyingi zaidi...unajua au nikuambie?’ akauliza

‘Kwani nimefanya nini kibaya zaidi, au unanitafutia visa ili niachane na hii dili...ni huko kukuomba pesa ndio imekuwa ni tatizo...kuna kosa gai jingine nimefanya, acha tamaa na roho mbaya ...?’ akauliza

‘Kwanini ulimuhusisha huyu jamaa jambazi,kwenye hii dili,sikukuambia umuweke, na hilo ni kosa kubwa sana, kwanini ulifanya hivyo....?’ akauliza

‘Jamaa gani huyo, ni jambazi gani huyo, mbona ...zaidi ya yule binti ambaye alikuwa ni...ndiye kitega uchumi chetu, hakuna mtu mwingine kwa upande wangu, wengine walikuwa wakisaidia tu...na ni kazi yao,mtu kalewa, inabidi kubebwa,kuwekwa sehemu...ndio hivyo tu...sasa ni nani mwingine...’akasema

‘Huyu jambazi kaka wa huyo mdada, kwanini ukamuhusisha kwenye hii dili, unamfahamu sana huyo mtu...umeongeza gharama....unaona hapo....’akasema

‘Kaka yupi huyo, mbona unanichanganya,...mbona mimi sijafanya hivyo...kaka yupi una maana kaka wa huyo msichana tuliyemtumia kwenye hii dili..hapana mimi wala sijawahi kuongea naye..., kwanini unasema hivyo?’ profesa akahisi mwili  ukimcheza  kwa wasiwasi

‘Usijifanye huelewi, usinifanye mimi ni mjinga...huyu mtu ni mbaya sana...katika watu nisiopenda kufanya kazi nao, huyo ni wa mwisho kutoka juu,...yaani hafai, haaminiki,ni tapeli, hatosheki,  ni muuaji, jambazi,...ukifanya naye kazi ni lazima akuzunguke, ....sasa hivi kwa taarifa yako huyo mtu anakufuatilia kwa karibu sana, sijui utamkwepaje, maana ni kupe...’akasema mtaalamu

‘Yupo wapi...?’ profesa akasema huku akigeuka nyuma, alijisahau kuwa yupo kwenye kibanda cha simu

‘Mimi nijuavyo, huyu mtu aliondoka na dada yake , kwani yeye ndiye mlinzi  wa huyo mdada, na hawezi kumuacha huyo dada peke yake, ndivyo  alivyonielezea huyo mdada...au unataka kusema nini, una uhakika umemuona huyo jamaa akinifuatilia...nambie ukweli,....ananifuatilia kwa lipi...eeh?’ akauliza na kugeuka huku na kule,....

‘Na hata hivyo mimi sikumshirikisha kabisa, hakuwepo kabisa kwenye hilo tukio....’akalalamika profesa

‘Ok,ok...mimi kwa hilo halinihusu,....hilo utalibeba wewe mwenyewe,...kama unahisi nakudangaya, basi, after all, I have finished with you,....’akasema

‘Una maana gani kusema hivyo,....umemalizana na mimi kwa vipi....?’ akauliza

‘Kiukweli, nimeshachoka na wewe, ...ila kwa kukupa tu angalizo,  ukipata kiasi chako, kama kweli utapata, kama kweli utabakiwa na kitu, ujue huyo jamaa unaye, huyo ni kupe keshakuganda...sijui mtagawanaje...’akatulia

‘Sa-sa-sa kwanini.....?’ akauliza

‘Usije ukasema sikuku-tahadharisha, ....unanifahamu sana, mimi sisemi kwa kukisia, nakupa tu kama angalizo,...huyo mtu unaye,  na ukumbuke huyu mtu ni muuaji, na hasiti kuua pale kunapokuwa na pesa.....na alivyo, ...ni tabia yake haiachi, ni lazima akuzunguke kwenye kazi yoyote, akijua una mshiko,  hata kama haimuhusu, he is a master in double crossing....utakuja kuniambia....’akaambiwa

‘Mhh, lakini...anaingiliaje ,anahusikaje...maana kiukweli nilishamuhisi vibaya, nilipoongea na yule mdada, nikamkanya kabisa kuwa huyo jamaa simtaki, na huyo mdada akasema huyo jamaa hatahusika, yeye ni mlinzi wake tu........’akasema

‘Ok,...its over, tumalizane kwa haya mazungunzo,nenda kawajibike, ....hakikisha unafanya yale tu niliyokuelekeza, .....sijui kama  umenielewa....ok’akasema

‘Nambie ukweli, kuhusu huyo mtu je umemuona akinifuatilia,...?’ akauliza profesa

‘Mimi sipendi kurudia rudia mambo, naona wewe huniamini, wewe ni mtu pekee asiyeniamini.....na mtu kama wewe sitaweza kuendana naye kabisa.....sijui kama nitafanya dili na wewe tena....’akasema

‘Sio kwamba sikuamini, ila kiukweli, mimi nilimwambia huyo mdada sihitaji mtu mwingine, hususani huyo kaka yake,....kwahiyo kama umeona anahusika, labda ni kwa vile umemuona akiwa karibu na huyo mdada,kama mlinzi wake au sio....ulimuona lini akinifuatilia...?’akasema na kuuliza

‘Sawa hamna shida....’akasema profesa akisikika kwenye simu akiongea na watu wengine.

‘Mtaalamuu hebu niambie ukweli kama umemuona huyo mtu hivi karibuni, au ni kiona mbali chako tu kinhisi hivyo...na wewe kwa ramli bwana, ...’akalalamika

‘Ramli eeh,.mimi naiga ramli eeh, ....Ok, but nakuambia ukweli,  my brother wewe upo kubaya,huyo mtu unaye, utakuja kuniambia, ....anyway, its yu’baby,....na sina la kufanya kwa hilo...huyo ni ndumila kuwili, double crosser, jambazi, muuaji,....na .....sijui utafanyaje,...sijui...na sitaki kujua, ...’akasema

‘Oh,...ina maana ni kweli.....?’ akauliza profesa

‘Unajua ....nimekuchoka,..hivi wewe ni nani kwangu, na nitakubeba kiasi gani kiukweli my brother hubebeki, na sijui...i wish, niimalizie hii dili mwenyewe...maana hata ikiisha naona wewe utakuwa ni mzigo kwangu....,kwa mahesabu yangu, naona huna chako kabisa, hutabakia na kitu,....am’ sory to tell you that..’akaambiwa na simu ikakatika.

Profesa akahisi mwili ukimcheza kwa woga, hasira,  ...akihisi kuzungukwa na maadui kila upande, akajua sasa keshatapeliwa, hata hiyo kazi sasa hatapata kitu,lakini hana jinsi anahitajika kuimaliza hiyo kazi ili kupata pesa... ..

‘Hahaha, hawanijuau hawa watu eeh, mimi ni mtoto wa mjini, nimekulia manzese.....hahaha, tutaona...wanataka kunidhulumu, tutaona....ila mhh...kupe, ...ina maana kweli ananifuatilia,....’akasema huku akitoka kwenye kile kibanda cha simu.

Na ni kipindi kile wakati profesa anatoka kwenye kibanda cha simu,.....

Akiwa na mawazo mengi, akiwa hana uhakika wa kupata pesa, na akiwa keshatishiwa kuwa ana kupe keshamganda. Mara ghafla wakati anatoka nje ya kibanda, akajikuta anagongana na jamaa,....

Huyu jamaa alikuwa akija kwenye hicho kibanda kwa kasi, kama vile anawahi nafasi au...na wakajikuta wanagongana bega kwa bega, profesa akajikuta akipepesuka na huyo jamaa akamuwahi kumdaka,...

Kama isingelikuwa huyo jamaa kumdaka mkono profesa, basi profesa angelidondoka vibata sana,...na ile hali ya kugongana bega kwa bega,profesa alihisi maumivu makali kwenye bega, na maumivi hayo yakasambaa mwili mzima, yaonekana jamaa huyo ana mwili mgumu kama chuma.

‘Mhh....’akajikuta akigugumia kwa maumivu

Akainua uso kumuangalia huyo jamaa,  hajawahi kugongwa hivyo na kuhisi maumivu makali hivyo, ni heri angeligongana na chuma chenyewe,... akataka kuhakikisha kuwa huyo mtu ni mtu kweli au ni roboti la chuma,...akainua kichwa kumuangalia huyo jamaa, wakati huo ameshikiwa mkono, ili aweze kusimama vyema.

Mtu huyo huyo alikuwa kavaa kofia pana,kama vile kuficha uso, na mawani meusi machoni...

‘Oh... am’ sory....nilikuwa nawahi kupiga simu ....’huyo jamaa akasema, akiyavua yale mawani yake, na kumtupia jicho profesa, na macho yao yakakutana,....

Profesa  akahisi moyo ukimlipuka kwa mshituko, badala ya maumivu sasa mwili ulitawaliwa na woga, akahisi miguu ikimtetemeka kama aliyeshikwa na ubaridi wa ghafla,....., hakutegemea kukutana na huyu mtu kabisa...akabakia kaduwaa,mdomo wazi..

Huyu jamaa akajifanya hajali, akimuachia profesa mkono huku akisema;
Its you again...hahaha....’akasema na kuingia kwenye kibanda cha simu, kama vile hana habari na profesa.

NB: Ni nani huyu


WAZO LA LEO: Mipango mizuri ya haki na ukweli, ya mambo ya heri, hutokana na malengo yenye fanaka na matarajio yake ni matunda yenye neema...., lakini kama mipango hiyo ni kuhusu dhuluma, hata mikakati yake huwa na kasoro, na mwisho huishia kutapeliana,  na kunyang’anyana hicho kilichopatikana, maana pato la dhuluma kamwe halina baraka.
Ni mimi: emu-three

No comments :