Ilikuwa ni kipindi
cha chai ya asubuhi, wanandoa wawili hawa walikuwa mezani, aliyekuwa wa kwanza
kufika mezani alikuwa mke, alipofika mezani mume alikuwa nje akijibaragua, baadaye kidogo akaingia ndani, na kumkuta
mkewe tayari akiwa kaandaa kila kitu, akafika na kuanza kunywa chai, mwanzoni, kukatanda
ukimia fulani, kila mtu akimtegea mwenzake kuanza neno, na mke akawa wa kwanza
kuongea;
‘Mume wangu kama
nilivyokuambia jana, nina mazungumzo muhimu leo mimi na wewe...’akaanza kuongea
mke huku akimkagua mumewe kama yupo sawa, au alizidamkia za asubuhi, kupoteza
malengo.
‘Sawa mke
wangu, hakuna shida, ...tuongee tu nipo safi, ila samahani kwa jana, niliamua
kunywa kuondoa stress, unajua hizi kazi
zetu za wavuja jasho, kiujumla unapokua kwenye ngazi ya kutumwa, wewe sio bosi,
tunaseka sana, unajituma sana kazini, lakini watu hawaoni unachokifanya, kila
ukifanyacho chenue faida,bosi ndiye anayeonekana wewe mchumia juani, huthaminiki,...’akasema
‘Mhh ni
kawaida...’akasema mke mtu akitafuta jinsi ya kuanza yale yake, hakutaka
kumuharakisha, kwani ni muhimu kuhakikisha anaupata ukweli wote.
‘Angalia kwa
mfano, kinaharibika kitu kazini, hapo habebi lawama sio za bosi, lawama ni
kwako wewe mtendaji, lakini kukiwa na mafanikio, wewe mtendaji umafanya jambo
likaleta mafanikio wewe tena huonekani, wewe uliyevuja jasho, hadi ukafanikisha
hilo, huonekani, anayeonekana ni bosi, ....faidia na ziada yote, anapewa bosi...,
wewe utaambulia tu ahsate na sifa nyingi za maneno...’akaendelea kuongea
kupoteza muda
‘Ndivyo
ilivyo, sio kwenu tu, haki na ukweli huwa haupewi nafasi, hata majumbani,
unaonaeeh....’akasema mkewe
‘Na hali
hiyo,inamfanya mfanyakazi wa kawaida kuwa kama mchumia tumbo tu, angalia, ...mshahara
mdogo haukidhi haja muhimu, ni wa kula nusu tumbo, hauwezi kukuletea maendelea
hata siku moja,...lakini huyu mnyonyaji anayeitwa bosi yeye anapewa gari,
mshahara mkubwa na marupurupu yote,...na bado hatosheki...’akatikisa kichwa
‘Ila wewe uneyeumia mshahara mdogo,...huna hata
angalau kitu cha kujikumu, kuwekeza, ...huna kabisa, ni kunyonywa kwa kwenda
mbele....sasa ukiwazia hayo unaona bora kunywa , nimekunywa pombe wee kupoteza
mawazo, lakini mhh, napo sijapoteza mawazo, zaidi ya kuyapumzisha tu...ni
taabu, ni majeraha...’akasema
‘Umeonaeeh,taabu
na majeraha, ...’akasema mkewe akiongeza chai
‘Ni taabu
kweli mke wangu, na ni kujipa majeraha, hebu angalia, sasa nina madeni, na sio
madeni ya maendeleo, madeni ya kubambikiwa,...ukiona mimi sina kosa, ni ajali
za kazini, hayo habebeshi bosi, hayo unayabeba wewe mwenyewe, kwa anuani ya
uzembe..,’akashika kichwa
‘Sasa mke
wangu usione nakunywa, usione nipo hivyo, ni maisha, tu...’akasema
‘Ndio maana
nawazia, ikiwezekana nitafute sehemu nyingine ya kazi...nibadili sehemu ya
kupata riziki, maana riziki ni popote, au sio mke wangu....’akasema sasa
akimtupia mkewe macho ya kujiiba
‘Pole sana
mume wangu ndio mitihani ya kazi hiyo, wengi wa binadamu wapo hivyo, na watu
kama hao wanajiona wanachofanya ni sahihi, kwa vile umimi, ubinafsi na roho
mbaya imeshatanda kwenye mioyo yao...wao kuishi kiujanja ujanja ni ufahari,
...na wanaweza hata kujinadi, sasa tuyaache hayo ,...’akasema mkewe na kuona
anapotezewa muda, kulisema alilolitaka.
‘Eeeh, ni
kweli kabisa mke wangu kwahiyo naomba unisamehe sana, ....sasa ulikuwa
unasemaje, umesema ulikuwa unataka
tuongee, haya tunaongea au sio, maisha yetu, tufanyeje, tukianzia na hilo la
mimi kutafuta kazi sehemu nyingine au unasemaje...?’ akauliza sasa akiona kuwa
hakuna tatizo.
‘Mume wangu pamoja
na hayo, kuna mambo naona kwanza tuyaweke sawa, nimeona hayo tusipoyamaliza,
yatakuja kuleta ufa mbaya kwenye ndoa yetu,...na ni muhimu sana katika
mipangilio yetu ya kimaisha humu ndani, na nimeona nikikaa kimia sijui kama
tutafika..’akasema na mume akataka kukatiza na mke akanyosha mkono na kusema
‘Naomba kwanza
unisikilize kwa makini...ili tuelewane’akasema mkewe, kwani alioa akimuachia
mumewe kuongea muda utakwisha nay ale aliyopanga yaje kufanyika hayatapata muda.
‘Aaa ok, ok,nakusikiliza,
sina neno, leo nipo nyumbani nataka tukae mimi na wewe,...si unajua mke wangu, sitaki
watu watusumbue, leo mimi na wewe, unajua nakupenda sana mke wangu...wewe hujui
tu...nimewaza sana nikaona hakuna haja ya mimi kwenda kulewa huko, na kumuacha
mke ndani...kwanza natafuta nini,....’akasema akijichekesha
‘Nashukuru
kusikia hivyo, na hiyo kauli ya kuwa unanipenda naisikia kwa mara ya kwanza tangu
tufike huku ulaya, na inaonyesha kuna shinikizo fulani,...lakini usijali, hata
mimi nakupenda sana mume wangu, ndio maana nataka tuyaongee haya...tuelewane
...’akasema mke sasa akiwa kakunja nne.
‘Mhh, kweli
mke wangu,najua kabisa sisi tunapendana sana, tangu nifike hapa watu wanatuonea
wivu,...japokuwa ulaya ni ulaya, kila mtu na hamsini zake, ...eeh, hebu sema
hilo la moyoni mke wangu,...nakusikiliza
mke wangu mrembo...’akasema huku akicheka cheka
‘Kwanza
tuanzie kule, katika swala la kuaminiana, na kuambizana ukweli, hili lilikuwa
ombi langu toka mwanzo...unakumbuka nilipokubali kuwa tufunge ndoa mimi na
wewe,...nilikuambia hilo, kuwa tuwe tunaaminiana, kila kitu chetu kiwe
wazi,changu kiwe chako na chako kiwe changu,tuwe hatufichani mambo....’akasema
mke
‘Ni sawa
kabisa mke wangu....nakumbuka sana hilo, na kwa ujumla hilo tumelifanya, na
tumefanikiwa au sio, kila kitu changu kipo wazi kabisa kwako,...sijui kama kuna
kitu nimekuficha,...hakuna, nina nini cha kukuficha, si unanijua nilivyo ,
unanifahamu kuwa sikuwa na kitu zaidi na hivi tulivyochuma sote....na
nisingelipenda kurejesha historia nyuma, au sio mkewangu...sasa tusonge
mbele....au unasemaje...?’akasema
‘Una uhakika
kuwa umekuwa mkweli kwangu,kuwa kila kitu chako umekiweka wazi kama
tulivyokubaliana,..huna kitu ambacho umekiacha kama chako na sio chetu...labda
una sababu za msingi, kama zipo niambie nisikie,.., ?’ akauliza
‘Kila kitu
changu nimeshakiweka wazi, sina changu, vyote ni vyetu...sina shaka na hilo mke
wangu,na mungu ni shahidi,..kwanza mimi nina nini cha kukuficha, siwezi
kukuficha kitu mke wangu,wewe na watoto wetu ni kitu hiki...kimoja...mengine
labda yawe ni majungu..’akasema
‘Mume wangu
kwanza nikuambie kitu, wewe unavyofanya sio sahihi, mfano huko kwenda kuelewa,
kwenda kushika shikwa kwenye bar, wakati k e.mke nyumbani unajivunjia heshima
yako....hivi nikuulize hao wanawake huko wana nini zaidi ya mke wako
nyumbani..?.’akasema na mume wake akasimama kujinyosha.
‘Mke wangu
wewe una tofauti kabisa na hao, wewe ni mke wangu,mrembo, huwezi kujilinganisha
na hao..na nakupenda sana....’akamwendea na kukaa karibu yake, kwanza alitaka
kupitisha mikono nyumba ya shingo ya mkewe kama kumkumbatia, lakini akasita
‘Sikiliza,
haina haja ya kujibaragua kwa haya, maana mimi sio mtoto mdogo, tuna miaka
mingi ya ndoa mimi na wewe,nakufahamu zaidi ya unavyojifahamu wewe, kwahiyoo
kujiigiza kinafiki hapa hakusaidii kitu....’akasema kwa sauti ya juu kidogo
‘Mke wangu,
kwanini...mimi nataka tuwe pamoja, na hata kama siku mbili tatu, nimekuwa mbali
na wewe, sasa nataka tuwe kama ilivyokuwa awali, kama ndio tunaoana,...’akasema
‘Tusipoteze
lengo, nilianza kwa kauli ya kuaminiana, na kuelekezana ukweli, nikakuuliza kama
kweli una uhakika kuwa chako, ni chetu, na hakuna chako ambacho hujakiweka
wazi, na kama kipo huenda una sababuu ya msingi,....sasa mimi, nataka kujua
ukweli..ukiniambia ukweli hapo nitajua kweli unanipenda, ’akasema
‘Mhh, ukweli
upi tena mke wangu...?’ akauliza
‘Je una
uhakika kuwa kweli chako ni changu na changu ni chako,una uhakika kuwa kweli
huna jambo au mambo unayonificha, ambayo unayafanya kibinafsi kinyume na
makubaliano yetu, je una uhakika kuwa huna mahusiano nje....’akasema na hapo
mume akanywea
‘Mke wangu,
siwezi hata siku mja kuwa jambo kinyume na makubaliano yetu,....hebu toa
mfano,na kwanini tuzunguke niambie kitu gani ambacho sijawahi kukuambia,
au....eeh ni kuhusu ile akaunti ..nilishakuambai ukweli wote...au sio...’akasita
‘Wewe ulidai
kuwa hiyo akaunti yako, haitumiki, na ulikuja kuitumia wakati unapokea malipo
ya kazini tu, na haijawahi kuingiza pesa zako binafsi, au sio, huo ndio ukweli
wako au sio....?’ akauliza na mume mtu kwanza alitulia halafu akasema
‘Ndio
hivyo...kwani kuna tatizo gani hapo, kama kungekuwa na kitu kingine
ningekuambia, achana na hiyo akaunti haina lolote muhimu, na pesa iliyopo humo
ni ya watu, nitaitoa ibakia kama ilivyokuwa....’akasema
‘Una uhakika
na unachokisema....?’ akauliza
‘Kwanini
unanitilia mashaka ka hilo,...,sikuelewi mke wangu hicho ni kitu kidogo tu,
hakina maana mbele ya ndoa yetu, au sio....’akasema
‘Mume wangu,
hapo hapo umeshanitilia mashaka,kama unanificha ukweli kwa hilo najua kuna
mengi unayafanya, na,huenda yamekwisha kukufika kubaya, ndio maana unalewa tu,
na hayo ya kazini kwako ni kisingizio tu, na ndio maana leo umeamua kujifanya
upo karibu na mimi....niambie ukweli’akasema
‘Sio kweli,
kama ni hilo la akaunti hiyo...ili uwe na uhakika twende pamoja benki,mimi
nitaitoa hiyo pesa yote ya watu, halafu uone kama kutabakia kitu...’akatulia
‘Mume
wangu,...nilikuonyesha barua ya kutoka benki, ukasema ni barua ya kutaka kujua
kama hiyo akaunti unaihitajia au waifunge, kweli si kweli...?’ akauliza
‘Hapana,
...nilikuambia kuwa akaunti hiyo mwanzoni ilikuwa haitumiki, na benki wakaniuliza
hivyo, basi ili kuifanya iendelee nikawa naweka pesa za malipo ya watu, ili
iweze kufanya kazi, sasa benki wakawa wanataka baadhi ya nyaraka ndio
wakaniletea hiyo barua...’akasema
‘Na hiyo
akaunti yako haijawahi kuingiza pesa zako binafsi, .....?’ akauliza
‘Pesa zangu
binafsi kama zipi, maana pesa zangu ni zako...’akasema
‘Je mshahara
wako huwa unapitia benki, uliniambia awali kuwa kwa vile mshahara wako ni
mdogo, hauitii benki, unakumbuka hilo, au umesahau...?’ akamuuliza
‘Aaah, kumbe
ni hilo, ndio, kuna wakati napitishia huko, si unajua, kuwavunga watu wa kazini
wasijue kuwa mshahara wangu upoje, leo naweka hapa kesho hapa....hilo lisikupe
shida...ni kitukidogo tu...’akasema
‘Na je mshahara
ulionitajia awali ndio huo huo unaingia benki au ...?’ akauliza hapo mume
akashituka akasema
‘Mshahara,
...ooh, kwani ...mmh, mke wangu, kuna tatizo kuhusu mshahara wangu, kila mwezi
naleta pesa yote tunapigiana mahesabu, kama unvyofanya wewe...kuna tatizo gani
kuhusu mshahara wangu...?’akasema na kuuliza
‘Naomba
unipe salary slip yako....’akasema
mkewe
‘Ya nini,
una maana leo huniamini mke wangu, ....kwanza hiyo nyaraka ya nini, mimi
sichukuagi, haina maana kwangu...’akasema
‘Kwasasa
siwezi kukuamini,kiukweli maswali machache hayo niliyokuuliza yamenifanya
nisikuamini kabisa, .....na kwa vile unataka twende kihivyo hamna shida....’akasema
mke mtu
‘Kwanini mke
wangu, nimeshakuambia kama unataka twende pamoja benki,uone kama hiyo akaunti
ina chochote..na pili hiyo salary slip
nitakueleta kesho, kama unaihitaji, si huniamini mke wangu, mbona vitu vidogo
sana hivyo mke wangu....’akasema
‘Yah...,najua
yote hayo umeshajipanga, huko benki huenda umeshazichukua hizo pesa,
ukazihamisha au unataka kufanya hivyo, ...na hiyo salary slip unaweza kwenda kuibadili ukaweka unavyotaka wewe ,...’akasema
‘Kwanini
nifanye hivyo,mbona unajibebesha mzigo
ambao haujatua kichwani mwako,....mke wangu niamini, mimi nipo wazi
kwako,...siwezi kukuficha hata mara moja....’akasema
‘Je hizo
pesa ulizotoa leo ulizipeleka wapi....?’ akaulizwa
‘Pesa
gani,...ok,hizo nilikwenda kulipia lile deni la kazini, na nyingine nitakwenda
kulipia watu wengine niliowakopa ili kulipa hilo deni la kazini ....hata hivyo
umenikumbusha,..hapa nilitaka kutoka,...nikawakilishe hizo pesa za watu ...hivi
sasa ni saa eeh, ngoja,....’akasimama kama anafikiri jambo.
‘Ulisema leo
upo nyumbani mimi na wewe au sio,sasa hiyo safari inatoka wapi?’ akaulizwa
‘Nilisahau,..kuna
pesa natakiwa kuzipeleka mahali,...’akasema
‘Mume wangu
tulia, naona tusipotezane muda, kiukweli hiyo akaunti yako inatumika,na umekuwa
ukiitumia tangu tufike hapa ulaya, umekuwa ukipitishia mshahara wako,na nusu ya
huo mshahara ndio unaleta hapa nyumbani ukidai ndio mshahara wako wote,
...’akasema
‘Na karibuni
ukatoa pesa benki kiasi kikubwa tu, sijui ulikuwa unazipeleka wapi, sasa mimi
ninachotaka ni kujua ukweli hizo pesa ulikuwa unapeleka wapi, ukinijibu ukweli,
mimi sina tatizo,...’akaambiwa
‘Hizo pesa
nilikuwa napeleka kulipia hilo deni,na kuna mtu mwingine nilimkopa, ndio maana
nikakumbuka,unajua mambo mengi kichwani, umenikumbusha kitu cha muhimu sana
...’akaangalia saa
‘Mume wangu
hizo pesa za deni la kazini unampelekea nani hasa mhasibu au unamlipa nani...?’
akauliza
‘Kuna
mfanyakazi mmoja nilimkopesha, yeye anatoa pesa kwa riba...’akasema
‘Je kazini
una deni kiasi gani, ...?’ akamuuliza
‘Deni gani,
ohoo, lile la uharibifu wa vifaa,...sikumbuki ni kiasi gani mpaka sasa,maana
wenzangu waliniunga mkono, hilo mpaka nikamuulize muhasibu..’akasema
‘Mume wangu,
sikuamini tena na sitaweza kukuamini tena, wewe ni muwongo,na unachofanya hapa ni
kujidanganya mwenyewe...hayo niliyokuuliza yote nimeshayafahamu ukweli wake,
nilikuwa nakupima tu...’akasema
‘Kwanini
usiniamini....?’ akauliza
‘Ninachotaka
kujua kwasasa ni kuhusu hizo pesa nyingi ulizitoa ulizipeleka wapi..?’
akamuuliza
‘Nimeshakuambia
ukweli wote mke wangu,...labda kama una lako jambo, naona unataka kuniumbua tu,
kwa vile...labda umenichoka,...’akasema
‘Hahaha eti
nimekuchoka,...’ akasema mke wake
‘Mke wangu
nilishakuambia, hii ni akaunti nilikuwa nayo tu, haikuwa na pesa awali,...,na nikaja
kutumia kwa dharura, na pesa humo sio zangu, na kama ni mshahara unapitia tu,,
naweka baadaye nazitoa, kuzikabidhi kwa
walengwa au kama ni mshahara naleta hapa nyumbani, tatizo lipo wapi...’akasema
kwa sauti ya ukali
‘Nimeshakuambia
kuwa yote niliyokuuliza hapa nimeshayafanyia kazi,na ukweli wote nimeshaupata,
na nilitaka kuhakiki kutoka kwako, ili nione kama umejirudi, maana binadamu hukosea
na baadaye anatambua kuwa kakosea na hujirudi, sasa nataka kujua pesa uliyotoa
uliipeleka wapi....?’ akaulizwa
‘Nimeshakuambia
nilitoa na kuzipeleka kwa wadai wangu....hunielewi..’akasema
‘Hii hapa nyaraka
ya benki inayonyesha pesa uliyotoa....sasa ili tuelewane niambie ukweli wote...’
akasema mke wake akimkabidhi mumewe ile nyaraka ya benki, na mume akaipokea
akionyesha kushangaa
‘Nimeshakuambia
kuwa sehemu yake ni pesa ya kazini,
ilipitia kwangu nikawa nimechelewa kuipeleka, na walikuwa wakiihitaji...tatizo
likawa ni benki waliniambia akaunti
yangu haijafanyiwa uhakiki, ila wakakubali nitoe kiasi tu...’akasema.
‘Mume wangu
,mimi nakufahamu sana kuliko unavyofikiria wewe, nakufahamu ukibadilika,
nafahamu ukiwa na matatizo...tulipofika hapa ukawa unachelewa chelewa kurudi
nyumbani,, nikajua labda unajiburudisha kujichanganya na wenzako ili uzoee,
lakini uhuru huo umepita mipaka...’akasema mkewe
‘Mke wangu
niamini, hakuna tatizo kabisa , kama ni hayo tu naona tuyamalaze kwa leo,
nataka kuwahi mahali,huyu mtu atakuwa kanisubiria sana....’akasema
‘Hatujamalizana
mume wangu...kwa vile akaunti zangu zote zipo kwenye makubaliano, na wewe
akaunti yako hiyo haipo kwenye makabaliano, leo wakili anakuja turekebishe
makubaliano yetu..hutaweza kuchukua pesa bila sahihi ya wawili, yangu na yako
’akasema
mkewe
‘Lakini hiyo
dhamana naitumia kwa malipo ya kazini, huoni kuwa italeta usumbufu kila mara nikikuomba
tukae kujadili....’akasema
‘Mimi sioni
usumbufu, kama kweli ni jambo sahihi, kwanini nione usumbufu, muhimu kuwe na
nyaraka sitahiki, sizani mtu atalipa tu bila nyaraka, au kama ni kazi umefanya
binafsi basi hilo ni swala la kifamilia nahitajia na mimi kulifahamu...’akasema
‘Kama ni
hilo hakuna shida....ngoja niende nikirudi tutakaaa....’akasema
‘Wakili
anakuja nilimuambia apitie benk kuzuia malipo yote , ....’akasema
‘Eti nini....sasa
nitachukuaje hizo pesa zawatu....na benki hawawezi kuruhusu kitukama hicho
mpaka mwenyewe niwepo, ...’akasema akionyesha kukasirika
‘Ndio maana
nataka tukae tuongee, tuweke mambo sawa, kuwa kuanzia sasa hiyo akaunti iwe
kama tulivyokubaliana, ....na hilo ni kuanzia sasa,...’akasema mke
‘Tunapoteza
muda bure, acha nimalizane na hao watu kwanza, halafu hayo mambo mengine
baadaye....’akasema
‘Tunaanzia
sasa hivi, wakili anakuja hawezi kufika hapa halafu akusubirie,...’akasema
‘Hapana mke
wangu,..hilo haliwezekani, subiri kwanza nichukue pesa ya watu ndio tuingie
kwenye makubaliano hayo...’akasema
‘Pamoja na
hilo kuna mengine nataka yaingie kwenye makubaliano yetu, nataka tuingize kila
kitu, maana sasa hakuna kuaminiana tena...’akasemamkewe
‘Mengine
yapi, kuna nini kwani, unataka kusema nini...?’ akauliza mumewe akionyesha
wasiwasi na kama kukerwa
‘Nyendo zako zinanitia mashaka, ...sikuamini
tena mume wangu...’akasema
‘Kwanini..?’
akauliza mume akiwa kakunja uso ,lakini moyoni akihisi wasiwasi fulani,
akikumbuka kauli ya wale watu;
‘Kama unabisha ngoja tumuonyeshe mke
wako picha ya uchafu wako..’
NB: Naona
tuishie hapa kwa leo
WAZO LA LEO: Wanandoa, tujitahidini sana kuwa
waaminifu, kuna mambo mnaweza kuyafanya nje kwa kificho yakaja kuathiri
familia, lakini kama mngeshauriana mkawa kitu kimoja hilo lisingelitokea.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment