Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, May 25, 2015

UKITAKA KUJUA TABIA YA MTU NGOJA KWANZA APATE


 Jana nilikuwa nawapa kuku wangu chakula, kuna kuku wawili wanatembea pamoja, japokuwa mmoja ni mkubwa kuliko mwingine, huwa mmoja akimkosa mwenzake utaona akilia huku na huku akimtafuta mwenzake wakiamuka asubuhi mbio mbio kwenye kuchakarua majalalani... Lakini cha ajabu nilipowatupia mchele, wa kutosha tu yule mkubwa akawa anamdonoa mwenzake, badala ya kula akawa anafanya kazi ya kumfukuza mwenzake , nikajiuliza ‘hivi ule urafiki umekwenda wapi, mbona nimewatupia mchele mwingi tu…

‘Na huyu kuku anayemfukuza mwanzake  si yule kuku  kama mwenzake hayupo anakuwa akilia huku na kule akimtafuta mwenzake,....' nikajikuta nikiongea mwenyewe, ... mhh, nikakumbuka ule usemi usemao ukitaka kujua tabia ya mtu ngoja apate…

Wakati naliwaza hili mawazo yangu yakarejea kwenye ile zawadi au bashishi iliyotokana na pesa ya RADA, nahisi wengi wameshaanza kuisahau , ila kwa kukumbushia tu ni kuwa kuna fungu lilitolewa kutokana na ile pesa iliyotolewa kwenye kadhia ile ya RADA, kutokana na hiyo pesa serikali iliona iitumie hilo fungu kwa manufaa ya watu wake, ikalipeleka hilo fungu wazarani na wizara kwa nia yake njema ikapanga kuwa pesa hiyo inunulie vitabu vya shule kwa ajili ya shule za msingi, na kweli nia njema hiyo ikafanyika, na mapesa yakagawanywa kwa wachapishaji wa vitabu ambao walikuwa na vitabu vingi kwenye maghala yao. soma hapa: http://www.pesptz.org/index.php/home?lang=swahili

Nakumbuka kwenye kasheshe hiyo kuna makampuni makubwa yaliyokuwa na kesi mbali mbali yalikataliwa kupewa hilo fungu, ..Mimi niliandika nakala moja kulalamika kuhusu hilo kuwa huenda katika kufanya hivyo itakuwa haijatendea haki makampuni hayo, nikayaita makala hayo, `mnyonge mnyongeni lakini haki yake mpeni…’ niliandika nikijua katika kufanya hivyo, sio tu hayo makampuni yatapata hasara, lakini pia hatukuwa tumewatendea haki watu wengine wasiohusika, tunawapa adhabu hata wale wasiostahiki , yaani wafanyakazi na familia zao, watungaji wa vitabu nk.

Nakumbuka wengi wa wafanyakazi wa hizo kampuni walikesha kwa kuomba, wakafunga ,huku wakimlilia mola wao kuwa je hiyo ni haki, kwanini na wao wasifikiriwe kwani wameteseka vya kutosha, wameishi  katika mazingira magumu, kwani mishahara yao ni midogo sana, na ilikuwa hata hiyo mishara yenyewe inalipwa kwa shida, maana biashara za vitabu hakuna, sasa tangazo hilo kuwa pesa ya RADA italipwa kwenye hayo makampuni, ikawa ni neema, lakini tena wanaambiwa nyie hamtapata kwasababu mna kesi.. mmmh!

Wavuja jasho hawa hawakukata tamaa, wakazidi kukesha na kuomba huku sheria zikifuatiliwa, na Mungu akasikia kilio chao, na baadhi ya kampuni zikaonekana hazina hatia, serikali kwa nia safi ikasema hapana wote wanaostahiki watapata hilo fungu ili waweze kuvitoa hivyo vitabu vinavyoharibika maghalani, mabilioni yakatumwa kwa hizo kampuni.

Wavuja jasho, wanamaombi, waomba dua, wafanyakazi, walalahoi, waliokuwa wakikesha kwa kuomba, wakasikia taarifa hiyo, ikawa ni shangwe na vigelegele, kupongezana na kujikweza kwa wakubwa ili kuwapa mikono ya ushindi, mungu hapo akasahaulika,…ndivyo wanadamu tulivyo tukipata hatusemi ahsante mungu tunakimbilia kumuona mwanadamu mwenzetu ndiye mtoaji wa hiyo riziki.

‘Mhh, sasa ni mwendo wa mkao wa kula..’ mmoja wa wafanyakazi wa siku nyingi akasema, na wengine wakionyesha mfano wa mapaja ya kuku kuwa sasa yapo mezani, akasema

‘Mapaja ya kuku sasa yapo mezani…..’ walisema hivyo wakiwazia hayo mabilioni kuwa ni sawa na mapaja ya kuku na ya kuwa angalau… muajiri kwa kuwaonea huruma atawawezesha na wao wafanyakazi waondokane na dimbwi la umasikini kwa uvumilivu na kuvuja jasho kwao huku wakipokea mishahara midogo sana kwa siku nyingi.

Lakini pia waliwazia mbali kuwa kutokana na pesa hizo ajira itakuwa bora zaidi, watawekeza kwa kuzalisha vitabu bora zaidi, na hata kugundua njia bora zaidi na matokea yake ni kuwaboreshea kipato chao, ikiwa na maana mishahara itapanda ili kuondokana na dimbwi la umasikini.

Haikutosha hapo serikali kwa nia njema tena  ikasema fungu bado lipo nitatoa zaidi, chapisheni vitabu zaidi, visambazwe mashulani (BAE tender)…na ikafanyika hivyo kwa haraka sana, maana makapuni haya yana utaalamu wa muda mrefu, mmmh mungu awape nini wafanyakazi wakajua sasa hakuna shaka tena, kampuni itawafikiria hasa katika mishahara maana pesa ipo mtaji upo, na wakitumia utaalamu wao waataboresha kampuni yao na kuwa bora zaidi.

Nilipofikia hapa kuwaza hilo nikawaangalia wale kuku wangu, nikawarushia tena mchele fungu la pili kubwa zaidi, kazi ikawa ile ile kuku wakawa wanapigana na kukimbizana, mkubwa  anamuonea mdogo, mdogo hana haki, japokuwa fungu limetolewa kwa wote, lakini mkubwa anasema `changu, changu …’ akitafuta kila mbinu za kuhakikisha mwenzake hapati,…mmh,

Nikiacha kuwawazia wale kuku akili yangu ikarejea kwenye hili tukio maana najiuliza hivi kweli hilo fungu la kwanza na hilo fungu la pili, hivi kampuni itatetereka tana, hivi kwa pesa hizo waajiri hawataweza kuwafikiria wavuja jasho,  hawa waliokuwa wakiomba na kukesha, wakiishi kwa shida na mshahara mdogo, wakiombea kuwa ipo siku mungu atajalia neema iwashukie, ..ni kweli neema imeshuka, lakini je wamepata nini…mmmh ukitaka kumjua mtu tabia yake ache apate..

Mara boooom….

Serikali ikasema kuwa sasa hivi itakuwa ikichapisha vitabu vyake wenyewe, …kauli hii  ikawa ndio kisingizio,  mapaja ya kuku, yaliyokuwa sahanini, yaliyokuwa yakiwatoa mate walioandaliwa, mwenye nacho akataka zaidi, na yule asiye nacho akawa ananyosha mkono, sasa kauli ya hiyo ya serikali, ikawafanya mawazo yageuke..wasiwasi, ukawaingia wawekezaji,  na ilivyo mwenye nacho atakuwa ka neemeka,  na muwekezaji kwa kauli hiyo, japokuwa ana mapaja mezani,lakini kwa tabia na hulika, atageuka huku na kule, akiwaangalia wenzake ambao wanaendana naye, hapo tena hataki jasho, wale wavuja jasho, wananuka, hawafai tena keshapata kisingizio…mmh badala ya kumshukuru mungu moyo unakengeuka, ubinafsi unatawala zaidi, akili inakuwa sio ile tena…

‘Jamanieeh mumesikia, serikali yenu ilivyosema…..kazi hakuna, na siwezi kuendeleaa kuishi nanyi, najua mumeteseka sana, mumevumilia sana, lakini nitawalisha nini…nimewapa kidogo, kinatosha,..kwahiyo naona mwisho wa mwezi huu niwape haki zenu kisheria muende mkapumzike majumbani kama kukitokea kazi nitawaita…’ ni kauli ya mshitukao, ni kauli ambayo haikutarajiwa.. kila mtu alipigwa  na butwaa, huku mate yakiwa bado hayajakauka mdomoni, mate yakitamani yale mapaja ambayo yanayeyuka sasa, ina maana hatupati tena kitu hapa, ina maana hata mifupa hakuna…ukumbuke mishahara yao haijaboreshwa, na kisheria haki zao zinalipwa kutokana na mishahara yao,…mwezi mmoja wa notice, na mwezi mmoja wa bye bye, kafe na umasikini wako.

Ni ukweli usiopingika kuwa kwa muajiri akiambiwa kazi inayokuzalishia haitakuwepo tena, inamvunja nguvu, anakuwa hana jinsi akifikiria gharama za uzalishaji na mara nyingi anachokimbilia kuangalia ni gharama za rasilimali watu, wengi hawaangalii gharama za uendeshaji kama mafuta magari nk, maana magari na mafuta ni kwao wao wenyewe wakubwa, yeye anachoangalia ni rasilimali watu, kile anachowalipa wafanyakazi ni mzigo kwake, sasa je serikali kwa kutangaza hivyo haioni kuwa inawatelekeza watu wake, wale waliokuwa wameajiriwa na haya makampuni je watakwenda wapi, au wana jinsi gani ya kuwabeba hawa watu. Basi wawachukue kwenye hayo makampuni yao waliyopanga kuwa yatazalisha vitabu .

Mabilioni yale yatakuwa hayana maana kwa wafanyakazi hao na familia zao, ina maana watoto wao hawataweza kusoma tena…maana elimu sasa inahitaji pesa, kama huna pesa mtoto wako hatakwenda na wakati,…kama wafanyakazi hawa watakosa ajira, basi hata kule walipokuwa wamewapeleka watoto wao kusoma inabidi wawaondoe, wakawasomeshe kwenye shule za kawaida…huyu mtoto alishazoea huko alipokuwa sasa anarudishwa sehemu nyingine, kwa mtoto kuelewa ni kugumu…yote ni kwa vile mzazi wake sasa hana ajira yote haya ni kutokana changamoto ya hilo fungu la rada, badala ya neema kwa wengi limekwenda kuwa neema kwa wachache.

Kilio cha wavuja jasho ni kuwa serikali iangalie upya hili zoezi, la kuondo a uchapishaji wa vitabu kutoka kwa makapuni binafsi, kwani inaua makampuni ya uchapishaji makampuni makongwe yenye kujua vyema vitabu vyenye manufaa kwa wanafunzi, na pia mkumbuke kuwa mkiyaua haya makampuni mnawakosesha ajira watu wenu, je wao watakwenda wapi,…watoto wao watasoma wapi..

Ndio mtachapisha vitabu vyenyewe, lakini mkumbuke serikali imeshashindwa kuendesha shughuli zake wenyewe nyingi tu ikawapa watu binafsi, na hawa wamekuwa wakizifanya hizo kazi  kwa ubora zaidi. Tuangalie hili kwa mapana zaidi, kwa nia njema ya kuwawezesha watanzania wajiingize kwenya ajira hii ya uchapaji wa vitabu kwa manufaa ya taifa, na vitabu view vingie vyenye mawazo tofauti.

Cha msingi ni kuangalia ubora na hili litawezekana kama kutakuwa na idara maalumu ya wataalamu waliobobea wa mitaala , na ubora wavitabu hivyo, wao wavipitie na kuona kama kweli vinastahiki, na utofauti wa vitabu ndio chachu ya kuwezesha mtoto kufikiria zaidi, kwani yeye anapata mawazo kutoka vichwa tofauti, na unamjenga huyo mtoto kupenda kusoma vitabu tofauti tofauti, lakini kama tutakuwa na mawazo ya kichwa kimoja tu, aina moja ya kitabu tu, bado tutafika mahali tutakuja kuona kuwa kumbe mawazo hayo yana walakini…..tuangalie haya kwa mapana zaidi kuliko kuangalia yale mapaja yaliyoandaliwa mezani.

Mhh ama kweli ukitaka kujua tabia ya mtu, ..msubirie akipata….


Ni mimi: emu-three

No comments :