Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, May 20, 2013

WEMA HAUOZI -9



 Niliposikia mlango ukigongwa, na wakati huo yule mwanamke kaanguka chini , na alianza kwanza kupiga piga miguu, na baadaye akatulia, nikajua sasa ni balaa. Nikashika kichwa kuashiria kuchanganyikiwa, na nikageuka kumwangalia babu yako, lakini cha ajabu yeye hakuonekana kujali,…

Mlngo ukazidi kugongwa na sauti iliyosikia sio ya mtu mwingine, bali ilikuwa ni sauti ya mume wa huyu mwanamke rafiki yangu, ..hapo nikageuka kuangalia pale alipolala yule rafiki yangu, na kwa muda huo alikuwa katulia kimiya, kuashiria kuwa huenda kapoteza fahamu au keshafariki,….

‘Oh, kafariki, hapana, hajafariki, atakuwa kazimia tu,….’nikawa najiuliza mwenyewe akilini, …mungu wangu, sikutaka wazao hilo la kufariki liniingie akilini, na liliponijia nikajaribu kuliondoa kwa haraka akili mwangu, lakini athari za hilo wazo, zilishaingia akilini mwangu na kuathiri mwilini wangu maana nilihisi mwili mzima ukisisimuka, na miguu kuishiwa nguvu.

Usiuone huu mwili ukajivunia kuwa mimi nina nguvu, mimi sina matatizo, kitu kidogo tu, hasa mawazo, hasa mshituko, hasira, au kuchanganyikiwa, kinaweza kikaubadili mwili wako na kuwa kitu kingina kabisa, ndio maana unakuta mtu anashikwa na shinikizo mara moja,….na hata kiharusi, wakati alikwua hana tatizo lolote, …..hai hiyo ilikuwa kidogo inipate.

Mawazo ya haraka yakanija, nikachukua khanga yangu na kumfunika yule mwanamke, ili kama mtu akiingia usigundue kwa haraka kuwa kuna mtu kalala, au…, na kwa haraka nikageuka kumwangalia babu yako, kama anaweza kutoa msaada wowote, lakini yeye alikuwa kasimama, kashikilia panga, mwili mzima ukimtetemeka kwa hasira, na nilijua kama huyo mwanamke angeamuka, na kuanza maneno yake, ….angejikuta akicharazwa mapanga.

Kwa haraka bila kumjali babu yako nikakimbilia mlangoni, nia ni kumuwahi huyo aliyepiga hodi asiweze kuingia ndani, kwani kama angeliingia, mengi yangelitokea, ama kutoka kwa babu yako, au vyovyote vile kusingelikalika humu ndani, na lolote lingelitokea, kwahiyo niliona niepushe shari kwa haraka iwezekanavyo

Nikaukabili mlango, huku nikiomba msaada wa mungu, aniepushia balaa hilo, na kunipa busara ya kuongea na huyo mume wa huyo rafiki yangu,nikafungua mlango...na macho kwa macho, nikakutana na mwanaume. Ilionekana alikuwa kasimama hapo mlango kwa muda kidogo, sasa sijui alikuwa kasikia nini, lakini sikujali kwa muda huo.

Kitu nilichogundua kwa haraka, ni kuwa huyo jamaa alikuwa tayari anataka kufungua mlango, na alionekana kama alikuwa akisikiliza ….kwani aliponiona alikuwa kama kashikwa na mshituko, akaniangalia kwa macho yaliyojaa udadisi, na hata bila kusalimia akauliza;

‘Mke wangu nimesikia yupo hapa, nataka kuonana na yeye…’akasema huyo mwanaume huku akikunja uso kwa hasira, na mimi akili ikafanya kazi haraka, hasa kutoka na kauili yake ya kusema `nimesikia yupo hapa, kumba hana uhakika ….’nikamjibu.

‘Mke wako hayupo hapa, aliondoka hapa muda mfupi uliopita, nahisi mumepishana kidogo,..’nikamdanganya, na yule mwanaume akapepesa macho ya kuonyesha mshangao, …akabenua mdomo wa tabasamu la kukebehi, halafu akageuka huku na kule kama anakwepa kuniangalia usoni moja kwa moja akasema;

‘Haiwezekani,….wewe mwanake, unataka kusema nini… nimeambiwa bado yupo humo ndani kwenu,….’akasema na kujaribu kuangalia ndani kupitia kwenye mpenyo wa mlango, lakini haikuwa rahisi kwani nilikuwa nimesimama kati kati ya mlango, huku nimeshikilia mlango, ili usifunguke wote.

‘Na kwanini hunikaribishi ndani, ndio adabu zenu hizo….’akasema.

‘Kwasababu kama unavyoniona,..nipo peke yangu, siwezi kukukaribisha mwanaume ndani , wakati mume wangu hayupo….na..hata hivyo karibu, ….’nikasema huku nikivunga, ial sikusogea pale niliposimama.
Akiwa ameshikwa na kitu kama mshituko wa kushangaa, akukunja uso kuashiria kukasirika,na kama vile haamini kile ninachomwambia, na huenda alijua kuwa namtania, akawa kama anageuka kutaka kuondoka, lakini hakuondoka, akaguna kiume….kama anataka kumeza fundo la hasira, halafu akasema;.

‘Wewe mwanamke, mimi sio mtu wa msihara sihara, mnanijua nilivyo, na unanifahamu jinsi gani nilivyo na uhasama na mume wako, sitaki hili liwe chanzo cha kufumua hasira yangu dhidi yake, sitojali kuwa wewe ni mwanamke,….nitakufumua, niambie huyu mke wangu yupo wapi…. mimi  nina haraka…. , nataka kwenda safari zangu, najua kabisa yumo humo ndani, …kama mumepanga na yeye kuwa useme hayupo, ohoo…..’akasema na sikutaka kumpa mwanya wa kuongea sana, nikasema;

‘Ndio alikuwemo humu kwangu sitakati, ….alifika hapa kusalimia, …., tukaongea kidogo, halafu baadaye,….  akaondoka kwa haraka, akidai anakuja kukuwahi…’nikamdanganya na kauli yangu iliozaa matunda, maana aliniangalai mara ,moja usoni, na akageuka kutaka kuondoka, lakini hakuondoka.

Moyoni nilikuwa niomba dua, ….nikiomba huyu mtu aondoke, maana …..nimeshadanganya na hili litaweza kuleta madhara baaadaye, haya akiondoka,  kwani akijua kuwa kama litatokea lolote akajua kuwa nilimdanganya, moto wake utakuwa mkali sana. Huyu jamaa ni miongoni wa wanakijiji wanaoogopewa kwa kuwa na hasira na haraka haraka.

Alishagombana na mke wake, akampiga karibu ya kumuua, na walipoamuliwa akaingia ndani na kuchunkua panga, hapo kile aliyekuwepo alipata jeraha, na mkewe ambaye kwa muda huo alikuwa hajiwezi, kwa kipigo alichopata, akajaribu tena kumsihi mumewe, na hapo, akawa kajichongea, akajikuta na yeye anakatwa mapanga, na aliponea chupuchupu, kwani hadi leo ana makovu mawili ya usoni, sehemu ambapo alishinwa nyuzi kutokana na kukatwa na mapanga, hajali yeye hasira zikimpanda anaweza hata kuua

Huyu jamaa alishawahi kugombana na mume wangu wakiwa kwenye ulevi wao, na ugomvi wao uliishia kukatana mapanga, na hata walipofikishwa mbele ya mjumbe, jamaa huyu alikuwa hashikiki, hadi pale aliposhikwa na wanaume watano wenye nguvu, na ni baada ya kupambana nao kwa muda mrefu, na aliapa kuwa siku akipata mwanya wa kugombana na mume wangu, atautumia kuhakikisha anamtoa roho yake.

‘Mimi huyu mtu namdai pesa nyingi, kabla hajaiba na kukimbia, sasa karudi anakana kuwa nilikuwa simdai….sasa sikilizeni, hizo pesa zisitaki tena, …nitahakikisha nazipata kwa kumharibu sura yake, na siku yeye au familia, yake wakinikorofisha kidogo, ….hasira zangu zitaishia kubaya….mnanijua mimi …katika familia yetu huruhusiwi kuapa uongo…sasa naapa siku wakinikorofisha yeye au mkewe, ….nitaitoa hii hasira kwao…na mnajua ni nini nitakifanya…..’akasema baada ya kusuluhishwa.

Mume wangu waliposuluhishwa na huyu jamaa alijitahidi sana kutokugombana na huyu jamaa, kwani kweli anamfahamu sana huyo jamaa, maana wamekua pamoja, na historia ya familia yao anafahamu vyema, kuwa wao wakiapa kuwa watafanya jambo fulani, ni lazima walifanye, wana imani kuwa ukiapa uongo, basi wewe sio mwanaume.

Yule jamaa akageuza kiwchwa kwa haraka na kuniangalia, akiwa keshakunja uso , uso wa ugomvi, akakunja ngumi, kama kujizuia hasira zake, halafu akatembea hatua mbili mbele, akasema;

‘Haya, kwa vile nina haraka zangu, sitaki kubishana na wanawake….lakini ….haya sisemi mengi,….ninakuamini shemeji, hujawahi kunidanganya, ila mume wako siwezi kumwamini hata siku moja, …. nilimwambia mke wangu asiwe karibu na familia yenu, maana hatuna mahusiano mazuri, na sitaki mimi nionekane mkotofi kwenu,….haya…mimi nakwenda,…’akasema na kuanza kuondoka lakini ghafla akasimama na bila kugeuka akasema.

‘Huyu mwanamke atakuwa kapitia wapi,…mimi nilimwambia kuwa nina safari, na sikutarajia angelichelewa kiasi hicho, huyu mwanamke kwa umbea…naona kasahau hasira zangu, na kwanini kabadilika kiasi hiki…., yaani kila nyumba anataka apite kumwaga sera zake za kuamini mambo ya kishirikina…..sasa kaenda wapi……' akawa anaongea kwa sauti ya hasira, na akasema;

'Hili nitahakikisha nalimaliza leo hii, na ninaweza kuiharisha hii safari kwa ajili yake, na nikifanya hivyo…..mtasikia….na shemeji hatujamalizana, kama wewe ndiye unayemuharibu mke wangu, leo hakutakalika hapa kijijini....’akawa anachezesha mguu, haku kakunja ngumi, kuashiria kuzuia hasira.

'Sio kweli shemji,...'nikasema, kumbe nisingesema kitu, nilitakiwa nikae, kimiya,wao wanaamini kuwa mwanaume akiongea huruhusiwi kujibu kitu, mpaka upewe idhini ya kuongea, ..hapo nikawa nimeharibu, maana...

Na mara akageuka na kuanza kunijia pale niliposimama, uso ulikuwa umeshambadilika, na aliponifikia tu, akasimama,…nilishaanza kuetetemeka, na hata hoja ndogo ingelitoka, lakini nikajipa moyo na kumuomba mungu, huku nikisema kama angeliinua mkono wake, ningelimuita babu yako,….babu yako ni miongoni mwa wazee waliokuwa wakiheshimiwa sana…

Akasimama mbele yangu huku anatetemeka kwa hasira, akaguna na kwa haraka akgeuka na kuondoka, na mimi nikasema;

‘Shameji huenda mke wako sasa hivi yupo nyumbani anakusubiria….kwanini nikufiche’nikasema na yule jamaa akaondoka akionyesha kukasirika, na nilikuwa na uhakika kuwa akifika huko kwake, halafu amkose,basi anaweza akarudi kwangu kama mbogo aliyejeruhiwa, nikaomba mungu mambo hayo yaishe yasije kuwa makubwa mkononi mwangu.
***************

Nikakumbuka jinsi babu alivyonimabia kuhusiana na huyo mwanamke aliyeanguka ndani kwa mama yangu, na wakati ananismulia haya, alikuwa akikunja uso kuonyesha hasira, ….akasema;

Nilikuwa nimezamiria kupambana na wale wote walioshiriki kumfanya mke wangu azaniwe ni mchawi, kwani nilijua kabisa hizo zilikuwa ni fitina na umbea wa wale wasiompenda kwa sababu zao wenyewe, na nilipoona watu wanaanza kupata madhara, …..nilijua kweli sasa haki itatendeka.

Nilipofika ndio lile vugu vugu la wale vijana, kupatwa na mdhara, lilikuwa limeanza, na sikuwahi kwenda moja kwa moja, kwenye makazi niliyokuwa ninanishi …nyumbanii kwa mama yako, nilifikia eneo langu ambalo kwa muda huo lilikuwa likiendelea na ujunzi, na hapo, nikaweka makazi yangu ya muda, kabla sijajipanga vyema kupambana na hawo waliosababisha kifo cha mke wangu.

Hasira zangu kubwa zilikuwa kwa wale vijana ambao walikuwa wakijifanya walinzi wa kijiji, na kumbe walikuwa nyuma ya huyo wanayemuita `mtaalamu,..’ na habari za kuungua kwa nyumba yake, na yeye mwenyewe kupotea, zilikuwa zimesambaa kwa haraka sana, ……nikajua sasa mambo yameiva, iliyobakia ni kusafisha jina la mke wangu.

Nilifika eneo la nyumba ya yule mtaalamu, kwani kulikuwa na msiba mwingine, kwahiyo nikaona nikajionee mwenyewe ni nini kimetokea, na hapo nikamuona mmoja wa wale vijana akiwa amelala katikati ya sehemu ile iliyokuwa na nyumba ya huyo mtaalamu, sehemu hiyo ilikuwa kama imesakafiwa.

Nikasubiri kidogo kuskiliza watu wanaongea nini, kwani kila mmoja alikuwa akiongea lake, wengine ambao bado walikuwa waumini wazuri wa huyo mtaalamu, walisema hawoo vijana huenda walikosea miiko, ndio maana yamewakuta, hawo na huyo mtaalamu, aliamua kuhama hapo,na hakutaka makazi yake yabaki kama yalivyo, ndio maana akaamua kupaunguza na moto.

Wengine walidai kuwa huenda mizimu imekasirika , wengine walikuwa wakisema ni malipizo ya wale watu waliodhulumiwa nafsi zao…ilimradi kila mmoja alikuwa akiongea lake.

Haraka nikarudi kwenye makazi yangu ya muda, sikutaka kurudi kule nyumbani kwa mama yako, maana nilikuwa na mambo yangu ya kufanya, na nisingelipanda kumuhusisha mama yako. Lakini baadaye wazo likanijia , nikukumbuka kuwa niliondoka bila kuaga, na huenda wazazi wako watakuwa wamehangaiak kunitafuta , nikfika  nyumbani kwa mama yako, kwa nia ya kumwambia nipo, asisumbuke kunitafuta.

Na nilipofika hapo, nyumbani kwa mama yako, ndio, mara nikasikia sauti za watu wakiongea, nikajua ni mama yako anaongea ni mgeni, ….mara nikasikia maneno yaliyoniumiza moyo wangu…

‘Na haya yote ni uchawi wa huyo mwanamama wenu, hamjaushughulia, ….unakumbuka alivyokuambia yule mtaalamu, …wewe ukapuuzia, ….mtoto hajambo sasa, lakini akianza kuumwa na yeye mtatafuatana, sasa hivi ni zamu ya mumeo…..hangaikeni, huyo mwanamama, kaondoka lakini mtaondoka naye,….alikuwa mwanga kiukweli kweli…nawaambia ukweli, huyo atawamaliza wote..’

Mkononi nilikuwa nimeshikilia panga,…nilijikuta nikitetemeka mwili mzima, hasira zikanipanda, na sikutaka kuendelea kusikia zaidi, bila kupiga hodi nikausukuma mlango na kuingia ndani, na jicho langu la kwanza likakutana na huyu mwanamama….

`Ahaa, huyu ndiye mbaya wangu, kwanza nilikuwa namtafuta siku nyingi, ni mchonganishahi, mkubwa, bila kumuondoa hapa kijijini hakutakuwa na amani,..'nikawa nasema kimoyomoyo, huku panga likiwa tayari linaanza kuinuliwa, huku nikisonga mbele, .....

Akaniona, na macho yetu yalipokutana, akahisi hatari,...nilimuona akionyesha kuogopa, na alitaka kuinuka lakini mwili wake ulikuwa kama umekufa ganzi, …na wakati huo mama yako alikuwa kanipa mgongo, kwahiyo hakugundua kuwa ni mimi niliyeingia....

********

Mama akaendea kuongea;

Nilipohakikisha kuwa yule mwanaume, keshaondoka, kwa haraka nikarudi ndani, na nilipofika, nilimkuta babu yako, ndio anamsogolea yule mwanamke, na panga likiwa limeinuliwa juu, na yule mwanamke , rafiki yangu alikuwa kapiga magoti, huku kainua mikono juu, akiomba msamaha..…

NB: Hapa hata mimi naogopa kuendelea...kidogo lakini kikubwa....., dola na muda umekwisha tukijaliwa tutaendelea sehemu hii....

WAZO LA LEO: Tunapokuwa na masahibu yanayoweza kutupandisha hasira, yawe ni mauzi, ugomvi, kuibiwa, kufumaniana …..na hata kufanyiwa mabaya ambayo yanaweza hata kuleta vifo, kwanza inabidi tutulize hasira zetu, kwani shetani hapo hachezi mbali,….

Tukishatulia na kuyakabidhi hayo kwa mola wetu, kinachofuatia ni kututumia hekima, kwa kupambanua ukweli wa hali halisi, kwani huenda hilo tukio lilikuwa na sababu ya kutuashiria jambo jema, lakini kama tutalichukulia kwa hasira za haraka, linaweza likatutia hatiana, na kutupeleka kubaya zaidi. Tukumbuke kuwa hasira mara nyingi huleta hasara.


Ni mimi: emu-three

1 comment :

Anonymous said...

Tremendous things here. I'm very happy to peer your post. Thank you so much and I am looking ahead to touch you. Will you please drop me a e-mail?

my homepage revitolproducts.weebly.com