Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, January 31, 2013

Uchungu wa mwana Aujuaye ni mzazi-53




‘Ofisi yako itakuwa hii hapa, …..’ Maua hakuamini siku hiyo alipofika mjumbe toka kwa tajiri, mjumbe huyo alitumwa kuja kumuonyesha ofisi mpya iliyofunguliwa kwa ajili yake. Mwanzoni aliogopa, na hakujuwa nini akafanye, japokuwa kuandika na hesabu za kawaida hazimpi shida, lakini ile hali ya kuambiwa kuwa sasa wewe ndiye bosi wa hii ofisi ilikuwa kama miujiza kwake,…

‘Usiwe na wasiwasi binti, wewe ukifika asubuhi, cha kwanza , unafungua simu yako,….hii hapa’akapewa simu, na kujikuta akizidi kuchanganyikiwa kwa miujiza hiyo..

‘Ina maana hii ni simu yangu?’ akauliza.

‘Ya kwako kwa ajili ya kazi,…..’yule jamaa akamwambia, huku akimkabidhi hiyo simu.

‘Cha kwanza na ni muhimu sana, ukifika, ofisni hapa, kwanza unaangalia meseji ulizotumia, kuna watu wanahitaji mizigo yao, kuna watu wanahitaji kulipwa, na ….mengine utayazoea kidogo kidogo……’akaelekezwa, na kujikuta akiwa kakaaa kwenye meza ya thamani kubwa, na kiti, kama meneja wa kampuni,…akatabasamu.

‘Nilikuambia mwanangu, bahati haiji mara mbili, hii ndio bahati yako, inabidi unishukuru sana, na cha muhimu ni kufuatilia kila ninalokuelekeza..ukivurunda, shauri lako….’akasema mama yake mdogo, walipokuwa wakiongea.

‘Lakini mama, mbona kazi za ofisini sijawahi kusomea, huoni kuwa ….’akalalamika.

‘Shule sio lazima uingie darasani,….shule nyingine unajifunza kutokana na mazingira….sasa anza kusoma, na mimi nitakuwa mwalimu wako….kwanza anza kujifunza, jinsi gani ya kuvaa, hizo nguo za kijijini achana nazo,…na unahitajika, kujiremba….’akaanza kufundwa.

Kwakeli Ilikuwa kama mchezo wa kuigiza, Maua hakutegemea kuwa ataweza kukaa kwenye ofisi na kuitwa mfanyakazi, akijilinganisha na maisha ya huko alipotoka na darasa lake la saba, …hakujua yote hayo yana sababu, hakujua kuwa huenda huo ni mtego wa panya,…huenda ukaja kumnasa.

‘Mwanangu naona mambo yalivyojileta , nilikuwambia hapa mjini, ….fuata ninavyokualekezea, sasa mungu akupe nini, iliyobakia ni akili kichwani mwako, …’ mama yake akaendelea kumfunda.

‘Akili kichwani mwangu kwa vipi mama kuna nini zaidi ya hiyo kazi, ….?’akauliza Maua.

‘Unamuona mtu mwenyewe alivyo, hajatulia, na anahhitaji mtu wa kumtuliza, huwezi kushangaa makamo kama hayo hajaoa, anaruka huku na huku kama jogoo, sasa huenda bahati ikaangukia kwako’ mama mdogo akamwambia Maua.

‘Kwa umri kama huo alio nao, ina maana hajaoa….?’ Akauliza kwa mshangao akikumbuka siku ile alivyomuona akiongea na simu.

‘Mbona nimesikia akiongea na mke wake…na akawa anamwambia kuwa anampenda sana..’akasema Maua.

‘Hana mke huyo,….eti anampenda sana…hahahaheee…’akacheka yule mama kwa kicheko kikubwa.

‘Huyo, kila mwanamke anamwambia hivyo hivyo, hizo ni lugha za wanaume za ulaghai, na akimkuta bwege, akiambiwa hivyo, anajiona kweli keshapendwa, lakini akimkuta mjanja kama mimi, …’akasema huku akijiangalia, na Maua akawa anamwangali mama yake huyo kwa mshangao.

‘Usionione hivi mwanangu, mimi hapa nilipo ni kama msomi wa chuo kikuu…..lakini …..mmh, wewe usijali, nitakufundisha,…cha muhimu ni wewe kusikiliza maelekezo yangu ninayokuambia….’akamshika mabegani huku akimwangalia moja kwa moja usoni.

‘Maisha ni mazuri sana, ukiyajulia, na ni mgumu sana, ukiyakatia tamaa…na usiona watu wanajenga, wana maisha mazuri, ukazania walipata hivi hivi tu, kuna njia walifanya, wengine wanahangaika sana,…na hawapati,  na kuhangaika huko kupo kwa namna nyingi, kuna wengine wanatumia njia za mikato, kuna wengine wanafikia hata kujitolea mihanga, kuna wengine wajanja, wanatumia mbinu za  kudanganyana…ili mradi ni akili kichwani kwako…’akamshika shavuni, akipitisha mkono taratibu, kama mtu anayempaka mtoto mafuta.

‘Wewe ni mrembo kweli kweli…..una umbo zuri, unavutia, na ukitumia hizo hazina ulizopewa na muumba, unaweza ukasahahu kabisa kuwa ulizaliwa kwenye shida, …sasa nataka nianze kukufundisha maisha ya dunia yalivyo, …..nahisi wakati sasa umefika, ‘akatulia na kugeuka kuangalia nje.

‘Yule jamaa nimejuana naye siku nyingi, na ……sio mbaya, maana hata mimi muda huo nilikuwa nikitafuta, na bahati mbaya, sina umbo la mvuto kama la kwako, ingelikwua hivyo, nakuhakikishai sasa hivi ningelikwua siishi kwenye nyumba hii ya kupanga..’ akawa anaangalia huku na kule kama kuitizama ile nyumba.

‘Lakini hata hivyo, ….ipo siku , na najua tukiwa na wewe mambo yatakuwa safi, maisha yatabadilika,…wewe ni jembe, lakini jembe bila mlimaji sio mali kitu….lazima litumikishwe, na mimi nitahakikisha hatuitupi hii bahati’akageuka na kumwangalia Maua. Alimwanglia kwa muda akawa anashusha macho na kumwangalia kifuani, halafu akamwangalia usoni na kusema;

‘Hebu niambie umewahi kuwa na rafiki wa kiume?’ akauliza huku akimsogelea na akawa anapitisha mkono kifuani , sio kwa karibu sana, alikuwa kama anaupitisha ule mkono hewani, lakini karibu na kushika sehemu ya kifuani ya Maua. Maua akawa anashangaa, akawa anajiuliza huyo mama ana nini kwanini anamfanyia vituko vyote hivyo…, akatizama chini, hakujibu lile swali, …akatulia

‘Usiogope kuniambia, mimi ni mama yako, na nichukuliea kama rafiki yako, na usinihukuliea kama mtu mzima, nichukulie kama mwenzako, wa umri kama wako….niambie kila kitu, ili niweze kukusaidia..’akamshika begani na kumwangalia usoni akasema;.

‘Unaonekana bado hujaguswa ehe….’akasema huku akiwa kama anamtekenya sehemu ya nyonga, na Maua akasogea mbali, na yeye, na safari hii akakunja uso, na kumwangali mama yake huyo kwa hasira, akasema.

‘Mama kwanini unaniuliza mambo kama hayo, na kwanini unafanya kama….’akatulia na kugeuka pembani akakumbuka maneno ya mama yake, na vitendo kama hivyo, ambavyo yeye alishaambiwa kuwa wanaume wana tabia kama hiyo kuwafanyia wanawake, na hakutegemea mama yake huyo angemfanyia kama hivyo, akasema;

‘Mama yangu hapendi,…..mambo kama haya, …na mimi sina rafiki yoyote wa kiume…’akatulia kwa muda halafu akawa kama kakumbuka jambo akageuka na kumwangali mama yake. Akashangaa kumuona akitabasamu, na akamuuliza swali ambalo alitaka kumuuliza mapema;

‘Hivi kama mimi nigelikuwa mtoto wako wa kuzaa, ungelinifanyia haya unayonifanyia au kwa vile mimi sio mtoto wako wa kunizaa..?’ akauliza.

Yule mama akatabasamu, na akawa kama anawaza, ….na uso ukakunjamana, na taswira ya usoni ikabadilika, kiwingu cha huzuni kikatanda usoni, …akainama chini na kusema;

‘Mtoto…..ningelijaliwa kupata mtoto ningelifurahi sana, lakini nimechelewa…’akawa anaongea kwa huzuni.

‘Nasikitika kuwa,….na najuta, lkini majuto ni mjukuu huja baada ya matendo… hakuna mtoto aliyebahatika kukaa tumboni mwangu, …kila aliyejaribu kuingia tumboni mwangu nilimtoa, nikiogopa kuharibu usichana wangu, na sasa sizani kama ninaweza kupata mtoto tena…’akasema kwa uchungu.

‘Kwanini ulikuwa unafanya hivyo, ulimtoa kwa vipi….ina maana mama huwezi kupata mtoto tena?’ Maua akawa anauliza maswali mengi kwa wakati mmoja.

‘Usiulize maswali mengi, ukkiuliza sana utashindwa hata kuifanya hiyo kazi, mengine hayasimuliwi , yanakuja tu,….na umri unavyokwenda ndio unaanza kujuta,…..mimi nasikitika kuwa sitapata mtoto tena,…na ….’akawa anatoa machozi, na Maua akawa anamwangalia wa simanzi, hakujua afanye nini, baadaye akamsogelea na kumshika kama vile anamkumbatia, akasema;

‘Pole mama sikujua kuwa una matatizo, lakini sielewi kwanini usipate mtoto….’akasema Maua.

‘Nitapataje mtoto na mimi sina kizazi….’akasema huyo mama kwa hasira na kuondoka , akimuacha Maua akiwa kaduwaa…

NB: Japo kwa shida pokea sehemu hiyo ndogo, uone uhondo wa uchungu wa mwana, je kama huyo mama angelikuwa na mtoto, akajua uchungu wa uzazi angelimfanyia hivyo Maua, ….tuwepo pamoja.

WAZO LA LEO: Usijaribu kuharibu majaliwa ya muumba, kwani kuna ambao wamediriki kuua watoto, kuwatupa majalalani, kutoa mimba…na mwishowe wakaharibu hata kizazi, …..baadaye wanajuta ,tukumbuke majuto ni mjukuu

Ni mimi: emu-three

No comments :