Mama mkunga alipofungua
mlango, akijua ni mmoja wa majirani kaja kuta taarifa ya mtu wake, labda yupo
tayari kujifungua au ana matatizo ya uzazi, kwahiyo akafungua mlango akiwa hana
wasiwasi.
Mlango ulipofunguka,
akajikuta anakutana na mtu wa ajabu, mtu ambaye uso umevimba na kuleta sura ya
ajabu, na sehehemu nyingine nyama zinaonekana, kama mtu alikuwa akikwangua uso
na kitu chenye ncha kali.
Ilikuwa ni sura ya
kutisha, hata hutamani kuiangalia mara mbili, ..uso umevimba, hata macho
hayaonekani vyema, ni kama dude lenye kichwa na matundu ya macho, kifuani
kumelowana damu,...
Mama huyu mkunga alipoona
hivyo akahisi huy ni shetani, na kwa vile alishasikia watu wakiongelea
mashetani wala watu, akahisi hilo ni mojawapo limekuja kumuingilia,…..akataka
kupiaga yowe…lakini aliposhusha macho kumuangalia huyo mtu wa ajabu, akashangaa mtu huyo ni mja mnzito, au kama
sio mja mnzito basi ni shetani limeshiba nyama za watu….
Japokuwa mama huyu mkunga ana ujasiri, kazoea
kucheza na damu za watu, lakini sura aliyoiona mbele yake ilimtisha sana
akataka kufunga mlango kwa haraka, lakini mama alishaingiza mguu mmoja ndani na
alikuwa sasa anayumba yumba akitaka kudondoka.
Yule mama mkunga akataka
kupiga yowe la msaada ili kibidi mume wake aje, lakini kabla hajafanya hivyo,
huyo mama akayumba na akawa sasa anataka kudondokea ndani kilichokuwa kimemzuia
ni huo mlango……mama mkunga akawa bado kashikilia mlango, akili ikawa inashindwa
kuamau afanye nini, na hapo akawa kachelewa.........
Mama yule akadonokea ndani
, mama mkunga hakuweza hata kumshikilia bado akili ilikuwa inaogopa, ...
Tuendelee na kisa chetu
**********
Mama mkungwa alimtizama huyu mama, pale sakafuni
alipodondokea, kwa tahadhari, Aliogopa hata kumsogelea, lakini baadaye akapiga
moyo konde, akamjongelea, alipomkaribia,akamgusa kwa mguu, akaona mama katulia,
akainama na kuweka kidole shingoni, akaona mapigo ya moyo yanafanya kazi akajua
bado mzima,
Kwa tahadhari
akamchunguza, hadi akili yake iliporizika kuwa huyo ni mwanadamu, ila kwa hali
aliyo nayo, anahitajia usafi wa haraka, alichofanya mama huyu,ni kutafuta maji
ya haraka, akapitia jikoni na kwa bahati nzuri kulikuwa na jiko bado lina moto,
walikuwa wameka sufuria kubwa kwa kwa ajili ya maji yao ya kunywa.
Akachota maji, yalikuwa
bado na uvuguvugu,….akaongeza kuni jikoni, akachukua yale ya uvuguvugu, na
kurudi kwa mgonjwa. Akajaribu kumgeuza vyema huyo mama,
‘Hapa nahitaji msaidizi,
lakini kwa hali aliyo nayo, hatamaniki, ngoja ni msafishe, sijui hii mimba ina
muda gani,...’akawa anajiuliza huku akipitisha mkono tumboni, na akasikia mguno
wa maumivu,
‘Mhh, hii sio kazi ndogo, ……’akasema
na kujaribu kumweka vyema alichokuwa akisikia kwa sasa ni mguno wa maumivu,
mama alikuwa kigugumia kuashiria maumivu makali.
‘Hebu niambie wewe ni
nani, na umepatwa na nini?’ akamuuliza, lakini hakupata jibu, mama akawa
anatumia yale maji ya uvugu vugu kujaribu kumsafisha, akaona hayo hayafai
yanahitajika maji mengi ya moto kidogo.
Maji yaliyokuwa jikoni
yakawa yameshapata moto wa kutosha, akachukua kitambaa na kuanza kumfanyia
usafi wa mwili mzima, nguo alizokuwa kavaa huyo mama,ni vitambaa, tambaa tu , vimeraruka.
Huyu mama mkunga akaingia ndani na kutafuta moja ya nguo zake, akarudi nayo
akamfunika huyo mama,
‘Sasa huu ni mtihani…hii
mimba ni ya muda gani?’ akawa anajiuliza lakini hakupata jibu. Mama mkunga
akaendelea na kazi ya kumsafisha huyo mama kadri alivyoweza
Alipomaliza kazi hiyo
akajua kuwa huyo kweli ni mwanadamu, uso kidogo ukaanza kunywea, na kuonekana
kama mtu, ‘ sasa kidogo anatizamika’ akasema na, sasa akataka kumchunguza vyema,
ili aweze kukisia hali ya mimba je ipo na muda gani, kwa utaalamu wake ni
rahisi kujua, dalili zote za kujifungua zikaonekana
‘Mhh, sasa huu ni mtihani,
kwa hali uliyo nayo, tuombe mungu....’akajisemea mwenyewe
‘Kwanza huyu mtu umefanya
nini, kuna madhila gani yamemkuta huyo mama hadi uso kuharibiwa kiasi hicho.....?’
akawa anajiuliza
‘Hilo sio muhimu sana kwa
sasa, muhimu ni huo uja uzito, huyu mama anahitaji msaada wa haraka…nifanyeje.’akasema
huku akigeuka huku na kule, na akili ikikumbuka agizo la serkali kuwa ukunga wa
mila marufuku, kwani kulitokea tatizo hapo nyuma akaishia jela.
‘Mhh, jele nyingine hiyoo
inanukia, lakini nitafanyaje kwa hili…’akasema huku akiangalia huku na kule kuona kama anaweza kupata kitu
cha kusaidia, akili yake ilishajawa na utu. Akaona amuarifu mume wake, waone
watafanya nini, haraka akamuita mume wake, na mume wake akatoka akiwa bado na
usingizi, akauliza.
‘Vipi kuna nini?’ akauliza
mume wake huku akipiga miayo na akakatiza huo muayo, pale alipotupa macho
pembeni na kumuona huyo mama kalala sakafuni.
‘Mhh kuna mgonjwa!!....na-na-na
huyo, mbona kalala sakafuni…?’ akauliza mumewe kw kigugumizi, usingizi wote
ukamuishia
‘Usiulize zaidi kawaite
wale akina mama wanaonisaidia hii kazi, hii kazi sio yangu peke yangu
sitaiweza, huyu mama inaonekama keshafikia muda wake wa kujifungua na hali
aliyo nayo sizani kama anaweza kufika kituo cha zahanati….’akasema
‘Eti nini, umesahau eeh,….hapana
hili huwezi kulianya kwenye hii nyumba, ’akasema mume wake akionyesha wasiwasi.
‘Wewe unafikiri hapa tutafanya
nini, fikiria kama ndio wewe, au mkeo yamemkuta haya, …ubinadamu unahitajika
hapa…., ‘akasema
‘Mke wangu unakumbuska,
uliwekwa ndani kwa mambo haya haya, huruma yako itakuponza,….huyu tumtoe nje
kabisa…..’akasema huku akimsogelea.
‘Haya mtoe….’akasema mama
mkunga akimuangalia mume wake ambaye alikuwa akionyesha wasiwasi hata wa
kumsogelea.
‘Unaona hali aliyo nayo….hatuna
ujanaj hapa, najua kabisa kwa hali aliyo nayo kujiungulia hapa ni hatari,
lakini waite wenzangu tuone tutafanyaje..maana kwa hali kama hiyo hata mimi sijui
tufanyeje…mimi naona bora tujitahidi afike angalau kituo cha zahanati kwa
ushahidi...’akasema huyo mama
‘Wewe nakuona umesahau,…
unataka kuleta kesi nyingine hapa nyumbani hujasahau onyo ulilopewa na serikali,
hawakujali kuwa ulijitolea kuanya ubinadamu, wakakuweka ndani….halafu huyu ni
mtu gani mbona uso umeharibika hivyo....?’ akauliza mume mtu
‘Kimbia kawaite
wasaidizi..hii sio swala lako tena na muda hapa ni mali....’akasema mama mkunga,
na mume wake akatoka nje kwa haraka kwenda kuwaita wanawake wasaidizi ambao
wanaishi nyumba za jirani.
Walipofika, walimkuta mama
huyo akiwa kashikilia kitambaa akiendelea kumsafisha huyo mama, akiwa na baadhi
ya vifaa vyake vya kazi, na wenzake walipofika na kumkaribua huyo mgonjwa kila
aliyemtupia jicho, akawa anashituka, na kurudi nyuma.
‘Mhh, huyu ni mwanadamu
gani, mbona uso umekuwa hivyo…’wakauliza
‘Ni heri kwa sasa
nilipomkanda na maji ya moto na dawa kidogo uvimbe umepungua, ungelimuona
mwanzoni,….sijui kaanyiwa ukatili huo na nani…’akasema mama mkunga.
‘Sasa hii sio kesi ya
polisi…’akasema mwingine
‘Kwa hali aliyo nayo mpaka
tuwaite polisi, tutapoteza mtu,….’akasema mama mkunga
‘Sasa tufanyeje….tunakusikiliza
wewe uliyetuita….’akasema mama mwingine
‘Mimi nimeshindwa hata
kumweka mahali pazuri, …hebu sogeza huo mkeka, tumuweke hapo, …’akasema
‘Kile kitanda kipo wapi,
maana alivyo , na anavyolalamika naona kama anakaribia kujifungua…’akasema
‘Ndio hivyo, wasiwasi
wangu, kapoteza damu nyingi, nilijaribu kumnywesha yale maji ya kuongeza damu, ….lakini
anakunywa kwa shida, unaona mdomo ulivyovimba,….’akasema huku wakimkagua kagua.
‘Una uhakika huyu ni
binadamu…’mmoja aliyekuwa kimiya wakati wote akauliza kwa kunong’ona.
‘Hakikisha mwenyewe….’akasema
mama mkungwa, wale akina mama na wao wakamsogelea tena, wakawa wanamshika huku
na kule
Walipomkagua na kuona ni
mtu kweli wakajaribu kumhoji, lakini mama alikuwa akijaribu kuinua mdomo
kuongea, mdomo ulikuwa haufunguki, ulikuwa mzito kwasababu ya uvime,
‘Jamani huyu mtu anahitaji
huduma ya haraka., leteni maji ya moto mengine yaliyochanganywa na chumvi, na
yale majani ya kutuliza maumivu..’ mama mkunga akatoa amri kwa akina mama
waliokuwepo humo. Mambo hayo yakafanyika harahaharaka na huduma ya kwanza
ikafanyika kwa mama.
‘Jamani hapa tukifanya
mchezo tutampoteza huyu mtu, mnakumbuka serikali ilivyotangaza juzi, ukunga wa
jadi ni mwiko, na hali ya huyu mama haitamaniki, na naona kama mtoto amekaa
vibaya tumboni, na inaonekana hayo majeraha aliyoyapata yatakuwa yamepoteza damu
nyingi, hili sio swala letu kabisa, hili ni swala la hospitali, sasa tufanyeje…’
akasema yula mama mkunga.
‘Na hizi mvua barabara
inaendeka kweli, tungeliazima hata baiskeli, awepo mwanaume wa kuendesha, sisi
tufuatilie kwa nyuma....’akasema mmojawapo
Ukumbuke huko ni kijijini
hakuna magari ya kukodi, magari yapo maeneo ya mbele kidogo, na kwa hali livyo
hakuna ambaye angekubali gari lake like eneo hilo na hospitali ipo mbali sana,
wakashauriana kuwa itafutwe baiskeli haraka iwezekanavyo.
Baiskeli ikapatikana
ambayo ilikuwa na kitu nyuma kama mkokoteni, na safari ya kwenda hospitali
ikaanza. Haikuchukua muda Mama akaanza kuvuja damu, na mama mkunga akamuangalai
mwenzake kwa ishata kuonyesha hali ya hatari.
Wenzao wengine walikuwa
wakija kwa nyuma, lakini walikuwa mbali kidogo, wao wawili walikaa kwenye huo
mkokoteni kwa ajili ya msaada, kazi ilikuwa kwa kumuendeshaji.
‘Damu inavuja, hii ni
ishara mbaya….na tukijaliwa kufika huko hospitali salama, kutahitajika damu,
hatujui ndugu zake, mjiandae kujitolea damu….’akasema mama mkunga.
‘Mhh, mimi sina damu ya
kutosha kutoa….’akasema mwenzake
‘Sijui wenzetu, lakini
yote tutajulia huko mbele, tuombe tufike salama…’akasema mama mkunga.
Walipofika hospitali
ambayo ni kituo kidogo tu, Ile hospitali wakaogopa kabisa kumpokea yule mgonjwa
kutokana na hali aliyokuwa nayo. Walisema lazima kuwe na barua ya polisi, kwani
inavyoonekana huyo mama kapigwa na hawajui kapigwaje, je watasema nini kama
akipoteza maisha , hasa kwa jamaa zake.
‘Lakini mfanyieni huduma
ya kwanza, mnaona hali aliyo nayo….’akasema mama mkunga lakini wale madakitari
pale waliogopa hata kumshika, mmojawapo akajitolea na kutoa dawa za huduma ya
kwanza, huku akisema;
‘Tafuteni usafiri, huyu
mtu yupo kwenye hali mbaya…’akasema na wakati anaongea mara dakitari mkuu wa
hiyo hospitalia katokea na gari lake, akamuona huyo mgonjwa.
‘Huyu mgonjwa sio wa
kucheleweshwa, awahishwe hospitali kuu….’akasema huy dakitari mkuu.
‘Usafiri…’akasema mama
mkungwa
‘Oh, …..’akaguna huyo
dakitari, akaingia kwenye gari lake, na kusema;
‘Haya muingizeni
tumfikishe huko hospitalini,
Ikatoka hiyo Bahati, na mama akaingizwa kwenye gari, ikawa safari
ya kwenda hospitali ya wilaya.
Alipofikishwa hospitalini
ya wilaya hali ya mama ilizidi kuwa mbaya kwani damu nyingi ilishapotea,
majeraha ya miba yalimuharibu sana usoni na sehemu nyingine za mwili, na vile
vipigo vilikuwa vimeathiri tumboni.
Madakitari wa Wilaya, nao
wakaogopa, walihitajia barua ya polisi, lakini kwa hali aliyokuwa nayo mama, wakaona
wamuhudumie kwanza,huku barua ya polisi ikitafutwa. Hospitali ile ya wilaya
ikachemsha, vifaa walivyo navyo ni duni, na wataalamu wa operesheni kama ile
hakuna,….kwani kwa hali aliyokuwa nayo mama, hatakuwa na uwezo wa kujiungua kwa
njia ya kawaida, wakashauri apelekwe hospitali ya rufaa, …
‘Tutapawa wapi gari, maana
aliyemleta mgonjwa alishaondoka kurudi kazini kwake...wakaangaliana, usafiri wa
haraka upo wapi, je kuna jamaa wa huyu mama anaweza kusaidia, wakaulizwa
waliomleta na wao wakasema;
‘Sisi hata hatumjui
tumejitolea tu kama wasamaria wema…..’wakasema.
Huku na huku na ya mungu
mengi likapatikana gari ambalo lilikuwa likielekea huko mjini, mwenye gari
akawa tayari kutoa msaada, hadi hospitali ya rufaa na huko kwa bahati nzuri
walimkuta mtaalamu wa akina mama ambaye alikuwepo hapo kwa muda, mtaalamu huyu
alipomchunguza mama huyo akasema kuna mawili mama au mtoto mmoja atapoteza
maisha
‘Hapa ni mtihani,
mpelekeni chumba cha upasuaji haraka....’akasema dakitari huyo.....
Kazi kweli kweli…sasa
ilikuwaje vile, ngojeni nijaribu kukumbuka, simtajua kisa hiki ni cha muda
kidogo.
Tuendee kuwepo, tuishie
sehemu hii, mambo yanakuja msijali …
WAZO LA LEO: Utu wa mtu mtu haupimwi kwa hali ya
mtu aliyo nayo, awe ni masikini au tajiri utu wake upo pale pale. Kama unawajibika kusaidia, kuongoza,
kuhudumia, usiangalie hali ya mtu, wewe angalia utu na wajibu wako kwake.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment