Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, September 5, 2014

DUNIA YANGU-28



Inspecta akiwa na wasiwasi aliingia chumbani kwake,na alijua atamkuta mkewe akiwa kitandani, akiwa kalala, na lengo lake ni kumkurupusha kwa hasira na kutoa kipigo cha aina yake, lakini hasira zile na dhamira ile aliyokuwa nayo  ilinywea ghafla, kwani kwanza alihisi mwilini hali isiyo ya kawaida. Yeye huwa mwili wake unatabia ya kuhisi jambo, hasa likiwa ni la hatari, mwili humsisimuka au nywele kusimama.

Alipohisi hiyo hali, akili ikamtuma kuwa kuna tatizo, hapo hapo mwili ukajenga hali ya tahadhari, na kama angekuwa na silaha angeitoa na kuwa nayo mkononi, lakini hapo hakuwa na silaha, alichoweka akilini ni kuwa huenda mkewe atakuwa kwenye matatizo.

Hapo hapo hali ile ya hasira ikabadilika na kujenga hisia za wasiwasi, huruma, na moyoni akawa anaombea kusiwe na baya lolote kwa mkewe, alianza kukumbuka siku zake za nyuma, jinsi alivyompenda mkewe hadi wakafikia kuoana, na katika maongezi yao mara kwa mara kila mmoja alikuwa anaomba atangulie yeye kufa, ili asije kupata machungu ya kumkosa mwenzake.

Maisha ni kitu cha ajabu sana, leo imefikia hatua wanasalitiana, wanafanya yale waliyoapa kuwa hawatafanya, ..

‘Natubu kwa mola wangu hili kosa sitarudia tena, ni lazima nimpende mke wangu kwa moyo wangu wote, na nitatubu kwake na kumuelezea yale yote yaliyotokea, kwani hayo yote yamefanyika sio kwa dhamira yangu…’akawa anajisemesha moyoni huku machoni akihisi hali ya machozi.

Huruma ikazidi kuongezeka, akavuta hatua, lakini hali ile mwili kusisimu na nywele kusimama ikazidi, na na hapo akajua ni lazima kuna jambo baya limetokea, akawa sasa  anaharakisha ili kama kuna lolote aweze kuchukua hatua za haraka, akashikilia simu yake tayari kwa kuomba msaada ilibidi, ndio silaha pekee aliyokuwa nayo mkononi.

Akatupa jicho kitandani,hakuona kitu,..ohoo, kaenda wapi huyu, akajiuliza na akahisi mwili ukinywea, miguu ikaanza kuishiwa nguvu, lakini kwa ujasiri wa kiaskari akajikaza, na akatupa jicho na macho yake yakiwa na hisia za kiaskari, yakawa yamepeleleza eneo lote la chumba, na sakafuni mwa kitanda akaona shuka limedondoka, kidogo, akahisi nguvu, kuwa huenda mkewe kaenda kuoga au chooni.

Akavua shati na kubakiwa na vest ya ndani,akijua sasa anahitaji kupambana na lolote lililopo mbele yake, akatupa jicho chini,akaona kitu,…leso

Kuna leso yenye alama za damu,….akaisogelea na kuiangalia, sio damu nyingi, ni kama mtu alipatwa na jereha, akafutia, hiyo sio leso ya mkewe, mkewe ana tabia ya kununua leso aina fulani,…

‘Hii itakuwa ni leso ya nani…’akajiuliza akataka kuinama kuichukua, lakini akasita, akakagua kitandani, akaangalia huku na kule, kunaonyesha dalili zote kuwa mkewe alilala hapo…hisia nyingine za wivu, kuwa huenda kulikuwa na mtu mwingine, akakumbuka maneno ya muhudumu wa hoteli, alivyosema;

`…Huyo shemeji yake ….aah, unajua siruhusiwi kuongea zaidi, ila ndio alikuja baadaye, na alipoona hiyo hali, akamshawishi huyo mwanamke, na baadaye akakubali wakaondoka naye…
‘Ina maana walikuja pamoja, wakatumia kitanda change…hapana, lakini nitajua tu..’akasema sasa hali ikibadilika tena, akasogea hadi kitandani.

Kwanza alisita kukaa kama vile atajichafua, aliona kitanda chake kama ni kichafu, kimechafuliwa..lakini hali ile ya mwanzo ya kuwa huenda mkewe yupo matatani ikamrejea, sasa akajipweteka kitandani, akashika kichwa, akiwaza kwa muda, halafu akainua na kuandalia huku na kule kama anahisi jambo.

Kulikuwa kimiya kabisa kama hakuna uhai, ni kama vile dunia iliamua kutulia kwa muda, hakuna hata kitu kinatikisika, ile hali ya matumaini ikaanza kunywea, akaona kwanini aandikie na mate wakati wino upo, akainuka kitandani na kuanza kutembea kuelekea chooni…huko ndipo kuna bafu pia, akasogea, kwanza alitaka kupiga hodi, lakini akasita
Akashika kitasa cha mlango wa kuingilia huko, na kwa nguvu akafungua na kusukuma, na kwa haraka akawa keshaingia ndani...

Kulikuwa kimiya,..na ile hali ya kusisimukwa mwili ikamrejea, akahisi ubaridi mkali, akaona asipoteze muda, akafungua mlango wa kuingilia chooni, ulipofunguka, akakuta hakuna kitu…kuna karatasi za chooni, sakafuni, akaona kipande kidogo kidogo, kina alama nyekundu….damu

Machale sasa yakamcheza, bila kuchkua tahadhari, akakimbilia mlango wa bafuni, akafungua kwa haraka, na hapo, akasimama, akaduwaa, …lakini macho kama gololi yakawa yamesoma eneo lote,na kujua ni nini kipo wapi.

Ndipo akatupa macho sasa kwa makini, pale kwenye beseni la kuogea, mkewe alikuwa kalala , kuonyesha alikuwa anaoga, lakini kwa hali aliyokuwa nayo sio ya kuoga, …
Mkewe alikuwa kalala kwenye beseni lililokuwa limejazwa maji, mkono mmoja umejikunja na ulikuwa umefunikwa na maji, ulikuwa umshikilia tumboni, …hapo akaona rangi ya maji ikiwa imebadilika,…damu, damu….

Kwa haraka akakimbilia pale, na kuinama kumuangalia mkewe, huku mwili sasa ukiwa sio wake, ni mwili wa kiaskari, akapeleka mkono shingoni kwa mkewe,…akahisi mapigo ya damu kwa mbali, akajua bado yupo hai..

Sasa akatupa macho ndani ya maji, kwanini maji ni mekundu, ….hapo akaishiwa nguvu, alichosema ni..

‘No, no….sio kweli, haiwezekani, ….’akashusha mkono hadi ndani ya maji, akagusa kitu, …kwasababu maji yalishabadilika rangi, na mwanga mle ndani ulikuwa nihafifu, hakuweza kuona ni kitu, ila alichogusa akajua ni kitu gani, hapo akili ikaanza kuchanganyikiwa, akaacha kuchukua tahadhari za kiaskari, akawa amekigusa hicho kitu,na alipogundua hilo kosa ikawa keshachelea

‘Mu-mu-mu-me, wangu ni-ni-ni-sa-ame-he……’ilikuwa sauti ya mkewe akiongea kwa shida,, akamsogelea na kumshikilia kichwani, alionekana yupo kwenye hali mbali, akafunua macho kidogo kwa shida, na Inspecta alipoona hivyo, akasema;

‘Mke wangu, umefanya nini,..kwanini umeamua kujiua…’akasema Inspecta.

‘Si-we-zi, ku-ku-za-li-li-li-ka,..rafi-ki , y-ya-ko , du-ni-a aaah, -ya-ya-ngu….’akasema na mara shingo ikalegea, akawa kimiya..Inspecta akaanza kuchanganyikiwa, ule ujasiri wa uaskari ukamuishia.

‘No…hapana, utapona tu mke wangu….usife mke wangu ukaniacha, kumbuka ahadi yetu,....ooh,’akasema sasa akihangaika kutaka kumtoa pale ndani ya maji, na mara kwa nje akasikia mlango ukigongwa kwa kasi…

‘Fungua mlango sisi ni askari…’akasikia

Akajua sasa kuna tatizo, akainama kwanza kuangalia afanye nini, akashusha mikono yote sasa, ili aweze kumbeba mkewe na kumtoa kwenye maji, mara kwa nyumba mlango ukafunguliwa kwa kasi, na haikupita muda, hao askari wakawa waeshafika eneo hilo la chooni,

‘Yupo huku afande…’sauti ikasema na mara sauti ya uali ikasema nyuma yake;

‘Tulia hivyo hivyo, upo chini ya ulinzi…’sauti kali ya askari ikasema, na yeye akageuza kichwa haraka na kusema;

‘Ita dakitari haraka, mke wangu,yupo mahututi,....’akasema, na alipomshika mkewe na kwa jinsi alovyolegea, akaishiwa nguvu kabisa, akawa sasa anajaribu kumtoa kwenye lile beseni lililojaa maji.

‘Tumekuambia tulia, kabisa, mtieni pingu huyu,…’sauti kali ya askari ikasema.

Akashikwa kwa nyuma na askari na hapo akawa hawezi kumshikilia tena mkewe, na akageuka kumuangalia mkewe, na machozi yakaanza kumtoka, akaanza kulia,

‘Haiwezekani, kwanini,…kwanini…haiwezekani, mke wangu hawezi kufa,….ha…’akasema na askari wakawa wanahangaika kumtia pingu

‘Kwanini mnapoteza muda, muiteni dakitari haraka…’akasema

‘Dakitari keshafika, usitie shaka, ila wewe upo chini ya ulinzi, usivuruge ushahidi…’akasema huyo askari.

‘Kwa kosa gani?’ akauliza

‘Kumuua mke wako…’akasema

‘Mimi nimuue mke wangu, mna akili kweli nyie…’akasema

‘Umesikika ukitoa kauli hiyo mbele ya mashahidi wengi, na ndio maana tukawa tunakufuatilia, na kweli hilo umelifanya, kwahiyo upo chini ya ulinzi…’akasema huyo askari
Askari wengine wakaingia wakiwa wamevalia vifaa mikononi, wakaanza kukagua, na mmoja akasema;

‘Tunaomba nafasi tufanye kazi yetu, …’akasema askari na docta akasogea pale alipolala mke wa Inspecta, akaweka vipimo vyake na kuanza kutimiza wajibu wake, na mara akageuka kumuangalia yule askari aliyekuwa na cheo cha Inspecta, na akatikisa kichwa kama kukubali, kwa muda ule Inspecta hakuelewa ishara ile ina maana gani.

Inspecta alishanga huyu askari kaja lini, mbona ni sura ngeni kwake, akatulia kwanza akitaka kusikia kauli ya docta.

‘Mtupe nafasi kwanza tuweze kufanya kazi yetu…’akasema huyo docta badala ya kusema lolote kuwa mke wake yupo vipi, akili yake haikukubali kuwa amekufa, yeye alijua kapoteza fahamu tu,....

‘Docta mbona huendeleo kumsaidia mke wangu, …bado yupo hai huyo, mnapoteza muda…’akasema na docta akageuka kumuangalia, na macho yalipokutana naye, akahisi kitu, akajiuliza huyu aliwahi kumuona wapi, kuna jicho kama la dharau, au kitu fulani ambacho Inspecta hakukielewa wakati huo.

‘Usijali,…kazi itafanyika, ila tunahitaji nafasi…’akasema na Inspecta alipoona kama vile hao watu wanapoteza muda, akaanza kuleta fujo.

‘Hivi hamuoni mnapoteza muda, mke wangu hajafa huyo..kwanini docta…’akakatizwa na askari aliyekuwa akimshikilia, akamkata ngwala, akadondoka chini

‘Mtie pingu, asiendelee kufanya lolote…’ na Inspecta aliposikia kauli hiyo, akasema;

‘Kwanini mnafanya hivyo, kwanini mnanifanyia hivyo, nyie hamuoni kuwa mke wangu yupo kwenye hatari ya kupoteza uhai,…’akasema

‘Wewe tulia,….ulipofanya hivyo hukujua utaua,…..’akasema askari ambaye hakuweza kumtambua kwa muda ule ni nani.
‘Unajua mimi ni nani unayeongea naye, kwanza wewe ni askari gani, sikutambui…?’ akauliza
‘Mimi ni askari wapya walioletwa, ……nafahamu wewe ni Inspecta, lakini hapa tunatimiza wajibu wetu, jambo ulilofanya halistahiki, tunawajibika kukutia pingu,na kuanzia sasa wewe upo chini ya ulinzi…’akasema huyo askari, alikuwa na cheo sawa na yeye, akakumbuka, kuwa kesho, yaani leo asubuhi, alihitajika kukutana na askari wapya wawili ambao walitumwa kuja kuungana naye kupambana na hali iliyokuwa ikiendelea
Alikumbuka kauli ya mkuu wake, akiongea naye kwa simu, mkuu huyo alimwambia;
‘Nitakutumia nguvu mpya ambayo utasaidiana nayo kuhakikisha hali ya usalama inarejea mahali pake….’aliambiwa na ilifanyika hivyo pale alipomwambia mkuu huyo kuwa anahitaji kikosi maalumu cha kupambana na kundi ambalo analiona ni hatari, kundi lililojipanga vyema.

‘Kwani kuna nini kinachoendelea?’ akaulizwa

‘Kwa uchunguzi wangu, kuna kundi kubwa, ambalo limejijenga ipasavyo, bado nafuatilia, nikikamilisha uchnguzi wangu nitawaambia…’akasema

‘Basi kuna kikosi kipya kimerudi kutoka mafunzoni, nitakutumia nikikamilisha uhamisho wao…’akasema mkubwa wao

‘Sawa afande…’akasema, na ilipita muda bila askari hao kufika, na usiku wa jana akaambiwa wameshafika, kwahiyo atakutana nao…

‘Ndio nyie askari wapya waliofika…?’ akauliza

‘Ndio sisi…’akasema huyo Inspecta

‘Ok, ila nawaambia mke wangu akifa mkononi mwenu kwa kupoteza muda, mtawajibika, …’akasema

‘Afe mara ngapi afande, hebu tuache tufanya kazi yetu…’akasema docta.

‘Eti nini, hapana, haiwezekani haiwezekani, mke wangu hajafa…..’ Inspecta akawa analia kwa uchungu, lakini askari hawakumjali, wakamkokota hadi nje, na walipofika nje, akamuona Inspecta rafiki yake akiwa kakaa kwenye sofa, akiwa kashikilia shavu,….

NB: Kwa leo nimeweza kumalizia sehemu hii iliyobakia kutoka sehemu iliyopita


WAZO LA LEO: Tuweni makini sana na kauli zetu, ulimi unaweza kukuponza, ukakutia hatiani hata kama huna makosa, mara nyingi hali hii inatokea pale tunapokuwa na hasira. Ukikutwa na jambo la kukukasirisha, au kutaharuki jaribu kuwa na subira, chunga sana matamshi yako kwani sio watu wote wana nia njema na wewe, wanaweza kutumia kauli yako kukuangamiza kwa masilahi yao.

Ni mimi: emu-three

No comments :