Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, August 26, 2014

DUNIA YANGU-23


‘Usitumie kisingizio cha kazi yako kufanya mambo yenu, nawafahamu sana nyie wanaume mnapenda sana kujiendekeza kwa visingizio mbali mbali, unadai una kazi za ziada kama hivyo kumbe una mambo yako mimi nitakuja huko huko unapokwenda kukutana na huyo aliyekuita....’.

‘Kuja...kufanya nini....?’

Tuendelee na kisa chetu...

***********
Inspecta hakuwa na amani, lakini aliona ni vyema kwenda huko alikoambiwa aende, kuonana na mdada wa urembo, alijua kuwa kwa kufanya hivyo inaweza kuwa ni sehemu ya kupata hicho anachokitaka kukijua, japokuwa kwa namna nyingine, anazidi kujiingiza kwenye mtihani mkubwa;

‘Moja ya kazi yangu ni mitihani, kwahiyo ngoja niende tu,....’akasema na kwanza akabadili nguo zake, ili aonekane toauti kidogo, akaliacha koti lake na kubakiwa na shati,...mtanashati kidogo, akatoka nje ya ofisi na alipofika kwenye gari kichwa akawa anasikia sauti ya mkewe ikimwambia;

‘Kila laheri, sina zaidi, utanijulisha mkielewana na mwenzako,kuwa niende au nisiende..kama sitakwenda basi mimi nitakuja huko huko unapokwenda kukutana na huyo aliyekuita...’

‘Mhh, sasa huu ni mtihani, inaweza kweli mke wangu anaweza kuja huko, ...?’ akajiuliza huku akiingia kwenye gari, na moyoni akawa kama anakanywa asiende huko anapotaka kwenda, akawa anahisi hali isiyo ya kawaida,...

‘Hali kama hii inaniashiria hatari...lakini kwanini, kwani huko kuna hatari gani, huu sasa ni uoga...’akasema

Akaanza kuendesha gari, na alipofika kati kati ya bara bara , mara akahisi kuna mtu nyuma yake , akaangalia kiyoo cha  juu kinachoonyesha nyuma, kile kiyoo kilikuwa kimegeuzwa na tofauti na kinavyotakiwa kiwe, akajua kuna mtu kafanya hivyo kwa makusudi, akapiga mahesabu, jinsi ya kufanya.

Alihisi kwa vyovyote kuna mtu nyuma yake, je huyo mtu ana malengo gani, akatupa jicho kwenye kiyoo cha runinga ndogo iliyopo hapo mbele ambapo kuna kiyoo kinachoweza kuakisi kitu cha nyuma,kinaonyesha mandhari ya nyuma, lakini hakuona mtu, kuna kitu kama kitambaa kinapepea, hakumbuki kuweka kitambaa nyuma, lakini muoshaji jana alisahau kitambaa chake.

‘Nahisi kabisa kuna mtu nyuma sijui kakaa vipi kiasi kwamba siwezi kumuona...’akawa anaongea komoyo moyo

‘Hili ni kosa kubwa nimefanya, kwanini sikuwa muangalifu wakati naingia ndani ya gari....’akawa anajilaumu

‘Kama ni mtu kaingiaje kwenye gari langu, wakati eneo la ofisi lote kuna usalama wa magari, ..?’ akawa anajiuliza bila jibu.

‘Huyu atakuwa mtu wa ndani, sasa ni nani...’akaendelea kujiuliza huku akitauta njia ya kugeuza kicha aangalia nyuma, lakini inakuwa vigumu, kwani kama ni mtu atakuwa nyuma yake kabisa, na kumuangalia ni mpaka usimamishe gari.

Akawa anaendesha gari hivyo hivyo, akijifanya hana wasiwasi, lakini kwa mashaka hadi akafika sehemu ambayo anajua hakuna hatari inayoweza kutokea, hata kama atakabliana na huyo mtu, ni sehemu ya watu, akapunguza mwendo kutaka kusimamisha gari, mara akahisi hatari...

‘Kwanini unasimamisha gari...’sauti ikasema na mara akahisi chuma kikigusa kwenye kisogo, akajua hiyo ni bastola

‘Wewe ni nani na kwanini umeingia ndani ya gari langu bila rushusa na kuharibu utaratibu wa viyoo vya usalama, huoni unaniweka kwenye hatari ya kuleta ajali...?’ akauliza

‘Hilo lisikusumbue, cha muhimu ni kuelekea huko huko ulipotakiwa kwenda...’sauti ikasema

‘Wapi?’ akauliza

‘Kwani uliambiwa uende wapi, hukumbuki uliambiwa nini ,kuwa ukakutane na nani...?’ akaulizwa

‘Sijui unachokisema, wala sikuelewi, niambie wewe unataka nini kwenye gari langu,....’akasema

‘Kwahiyo unataka nikukumbushe...au sio, mimi sio kazi yangu, lakini ukinilazimisha nitaweza kufanya hivyo...’sauti ikasema

‘Sijakuelewa...’akasema

‘Hapa nyuma nina sindano ya virusi vya magonjwa, nikuchome nayo, au...?’ akaulizwa

‘Usinitishe bwana, kama ni kwenda huko nitakwenda kwa hiari yangu, kwani nilipanga kwenda huko ninapokwenda, sasa sijui huko unapotaka wewe ni wapi, au kuna sehemu gani nyingine unayotaka mimi niende, nielewe wewe...’akasema Inspecta

‘Huko huko unakoelekea ni sahihi, twende kazini...ile sauti ikasema na kile chuma kisogoni kikaondolewa,  ambacho Inspecta alijua ni mdomo wa bastola, na hapo Inspecta akapumua akijua angalau sasa anaweza kuendesha bila mashaka. Katika vitu ambavyo anajitahidi katika kazi yake kuwa na tahadhari navyo, kimojawapo ni silaha, kwani alishahudia mtu akiuwawa kwa bahati mbaya tu, kwa mzaha kama huo...

‘Umeingiaje kwenye gari langu....?’ akauliza Inspecta,  lakini kukawa kimiya, hakusikia jibu lolote kutoka kwa huyo mtu ambaye alijua kabisa bado yupo nyuma yake, kulikuwa kimiya kama hakuna mtu.

‘Nataka kuweka gari langu mafuta , huwa nina kawaida ya kuongeza mafuta kila ninapotoka ofisini, kwahiyo nataka kuingia kituo cha mafuta...’akasema Inspecta

‘Hilo limeshafanyiwa kazi, ukifika hapo unapokwenda utajaziwa mafuta yako, hayo yaliyopo yatakufikisha sehemu unayotakiwa bila kuisha, ...’akaambiwa

‘Ina maana umechunguza kila kitu, kwanini umefanya hivyo, au ni nani kakutuma?’ akauliza, akitaka aendelee kusikia sauti ya huyo mtu huenda akaweza kumtambua, maana ni lazima awe mtu wa ndani ambaye anaweza kuingia ndani ya gari lake bila kuhisiwa vibaya.

‘Yah, ...kila kitu...’akasema na kutulia

‘Unajua mimi ni askari, na sipendi hicho unachonifanyia, hapa naweza kufanya lolote, lakini sitaki shari, kwanini tusielewane, tuongee na tujuane, ....’akasema Inspecta

‘Usijali, ..’sauti ikasema na kunyamaza

‘Binti wa urembo, au jembe, unajuana naye kivipi?’ akauliza na sauti kama ya kuhema nyuma ikasema

‘Endesha gari, ...’Mara akahisi kitu, na haruu ya dawa za hospitalini ikasambaa ndani ya gari, na mara sindano yenye dawa au kitu ndani ikapitishwa mbele kidogo kupitia sikioni, ...

‘Unaona hii humu ndani kuna virusi, sijui vya ugonjwa gani mimi nimepewa maagizo kuwa ulileta ubishe nikudunge nayo...kwahiyo endesha gari na kaa kimiya....’sauti ikasema
Ilikuwa onyo kwa Inspecta, na akilini akawa anawaza, inawezekana kweli ni kuna virusi, au ni vitisho tu,lakini hakutaka kubahatisha, akaona ni bora kufuata anavyotaka huyo mtu, akaendesha gari taratibu hadi hoteli ya Paradise, ...

Alipofika maeneo haya mara akasikia mlango wa nyuma wa gari ukifunguliwa, na baadaye kukawa kimiya, alipoona kimia kingi, na hakuna lolote linaloendelea akageuka kuangalia nyuma, kwenye kiti cha nyuma yake, ambapo huyo jamaa alikuwepo, hakuona dalili ya mtu.

Alijua ameshateremka,..basi akafungua mlango na kutoka nje ya gari, akafungua mlang  nyuma na kukagua akaona kitambaa kinachofanana na viti vya gari lake kikiwa kimetandikwa kama shuka ina maana huyo jamaa wakati yeye anaingia kwenye gari, alijilaza sambamba na viti akajiunika hicho kitambaa kama shuka..

Akakitoa na kukikunja akakiweka kwenye sehemu nyuma ya gari,na alipohakikisha kuwa gari lake lipo vyema, akalifunga, na kuweka kufuli ya mtandao, ina maana hakuna mtu yoyote anayeweza kulifungua mpaka awe na neno la siri.

Akatoka na kuanza kutembea kuelekea sehemu ya mapokezi ya hiyo hoteli, na mara simu yake ikaita, akaangalia, alikuwa mkewe...

*****
‘Unasema kweli, uliwaona lini...?’ akaulizwa

‘Siku hiyo nilikuwa zamu kwa mdada mmoja....’akasema

‘Hapana huyo sio mume wangu ninayemfahamu mimi, ...hajawahi kunifanyia hivyo hata siku moja...’alikuwa mke wa Inspecta Moto akilalamika kwa uchungu, na mwenzake akamuangalia kwa jicho la pembeni huku akichekelea kwapani

‘Nilikuambia wanaume hawaamaniki, wewe ooh, mume wangu ni muadilifu, oooh, mume wangu ni mcha mungu, sasa kipo wapi, ipo siku nitakuletea picha zao utawaona `live’ wakifanya vitu vyao...’akasema

‘Lakini wewe uliyajuaje hayo, na ulimuona wapi akifanya hivyo?’ akaulizwa

‘Mimi ni mfanyakazi katika nyumba ya huyo binti Urembo,wanayemuita jembe, ni mfanyakazi wake wa ndani, na siku hiyo, nilikuwepo huko kwenye nyumba yake ya Msasani, japokuwa sifanyi pale nyumbani kwake mara kwa mara, huwa nafanyia kwenye nyumba yake nyingine, ana nyumba yake mwenyewe kuacha hiyo ya kupanga...’akasema

‘Huyo binti Urembo au Jembe sijui hana mume au mchumba?’ akauliza

‘Ana mchumba, lakini wanawake kama hao watakuwa na mume bwana...hao wanawake hawahitaji mume wa kudumu, leo ana huyu kesho ana yuke, ndio maisha yao yalivyo, nilisikia tu akisema ana mchumba wake anasoma nje, mimi sijawahi kumuona...’akasema

‘Ningelimjua huyo mume wake au mchumba wake...ohoooh..’akakatiza huyo mke wa Inspecta

‘Ina maana na wewe ungalimfanyizia au sio,...hahaheeeh?’ akauliza huyo shoga yake na kucheka kwa dharau

‘Sasa na hiyo ya kukutana na huyo mwanamke huko hotelini, mnasema inaitwa hoteli gani sijui umesema...?’ akauliza

‘Paradiso, au paradise humo kuna starehe za kila namna, ukumbi za mikutano, vyumba vya kupanga, na kila aina ya jambo unaloweza kulihisi linapatikana humo, hiyo hoteli ni kubwa na ina eneo kubwa, huwezi amini, kuna mpaka nyumba za ibada humo, ...’akasema

‘Humo humo ndani kuna nyumba za ibada!? Za nini na wakati inavyoonekana ni hoteli ya ufusuka?’ akaulizwa

‘Wenzetu hawa ni wajanja, wao wana kila mbinu ya kuingiza pesa, huyo mtu anataka kila aina ya shughuli inayoingiza senti aifanye yeye kwenye miradi yake, kila aina ya kipaji, ikiwemo hiyo ya karama, maombi sijui....anataka zote awe nazo...’akasema na kutulia kidogo.

‘Ni kuambie ukweli, hizo nyumba za Ibada ni vitega uchumi vyake, kuna watu wanajiita wana karama, za kutibu kuponya, kuombea, basi wao ndio wanaendesha hizo shughuli, wanapata chao na mwenye jengo au kitega uchumi anapata chake....’akasema

‘Hiyo sasa ni kumkufuru mungu...’akasema

‘Wao wanasema wameambiwa watafute riziki, na wasiofanya kazi hawatakiwi kula au sio, sasa wanye kazi za kumtumikia mungu watapata wao kula yao kumbuka hao wapo kwenye nyumba za ibada kuwasubiri waumini au sio...hebu jiulize watapata wapi kula yao, kama wasiokusanya kinachoitwa sadaka, ....ina maana wao hawahitaji maisha mazuri, kuoa, kuzaa, kutembelea magari mazuri, wao kama binadamu wanahitaji hivyo vitu vyote au sio...’akawa kama anauliza

‘Hiyo sio kweli, huko ni kujidanganya kwa mungu, na mungu hadanganyiki...’akasema mke wa Inspecta.

‘Hahaha, wao wana malengo yao, bwana...sikio,  kumbe, kuna watu hao wenye karama, ambao huonyesha miujiza yao, na watu wanaikubali, iwe hata mazingaumbwe, yeye akaona ohoo, kumbe nako huku kunalipa..., akakibuni hicho kitengo, akajua kumbe watu wakitoka makazini wakapitia hapo hotelini kwake, wakala, wakastarehe, lakini bado wanamuhitajia mungu wao, wanahitaji kuombewa, kutubu dhambi zao, basi wanaingia kwa hao wataalamu wake wa maombezi, wanaombewa...hahaha...jamaa mjanja huyo...’akasema huyo shoga na kucheka

‘Sasa yeye anapata nini hapo?’ akauliza

‘Hutaamini, sehemu hizo zinaingiza pesa kama nini, kuna wataalamu wa kutoa maneno ya mvuto, wana mbinu za kumpagawisha mtu, mpaka anatoa senti zote alizokuwa nazo mfukoni, ...watu hao wamefundishwa nchi za nje, walikwenda huko huko kunakosifika kwa hizo dini, wengine wametoka huko Nigeria, unakufahamu kwa sifa zake, wengine wapi huko sijui, wanakopigana vita kila siku, wengine mashariki ya kati, wanajua lugha za huko za ushawishi kama wamezaliwa na hizo lugha ..’akatizama saa yake

‘Kwahiyo kwa vile wabongo wengi hawakusoma, na hawataki kusoma wakisikia hizo lugha wanajua ni kweli,eeh ...ndivyo wanavyofanya hivyo eeh...?’ akauliza

‘Kama ulikuwepo, hao jamaa wanajua kila lugha za kimataifa, na hapo ukimkoga mbongo kwa lugha za nje, ooh, wewe waonekana msomi kweli, wewe unajua dini kweli, wewe unajua..yaani we acha tu, wakichanganya na  mazingaombwe yao, watu wakapagawa,...sijui wanafanyeje bwana, watu wenye mapepo, wanapandisha, eeh, na utaona wenye mapepo wanapona kabisa....’akasema

‘Hahaha, hao basi wana mapepo makubwa ambayo yanagopa hivyo vipepo vidogo, ni yale yale ya mtu kwenda kwa mganga wa kienyeji, waganga wa kienyeji wengi ni wachawi, wanachofanya ni kutoa na kupandikiza, unapona leo kwa uchawi wa mwanzo , na kesho unaumwa kwa uchawi wake aliokuwekea ili urudi tena...mimi siamini hayo, lakini yote ni ushirikina tu...’akasema

‘Sasa wenzako wakajua kuwa huko nako kuna namna ya kupata vijisenti, watu wanafika na magari ya kifahari kuombewa, kufanyiwa makafara ya kupata utajiri, na sijui inakuwaje, kesho na kesho kutwa, unawakuta watu hao ni matajiri kweli,...pia wana namna ya kujitangaza, kwahiyo hutaamini wanaohudhuria hapo kwenye nyumba hizo za ibada zao ni watu wakubwa, matajiri, na nasikia wana chama chao, wana nembo yao, ipo kama dunia hivi....’akasema

‘Kama dunia kwa vipi?’ akauliza mke wa Inspecta

‘Niliiona wakati nafagia kwa huyo mdada mrembo, ipo dunia inazunguka, ina ramani za nchi, kama ile wanayotumia watoto mashuleni, si unaifahamu dunia ya kusomeshea watoto shuleni ilivyo,....’akasema

‘Lile tufe la dunia linalozunguka?’ akauliza

‘Eheeeh, hilo hilo, basi hiyo ndio nembo yao, halafu mara kunatokea mikono mbali mbali, ile mikono ni fani za watu, vipaji vyao, maana inaonyesha mkono ule una komputa, ule una vifaa vya hospitali, ule una watu wa dini, waheshimiwa, akina mama warembeshaji na kila aina ya kazi...inakuwa mikono mingi, ambayo baaaye inakuja kukutana kwenye lile tufe inashikilia lile tufe...na sauti ya ya kutisha, inasema

‘Dunia yangu...’  na maandishi hayo ya dunia yangu, yanakuja na kuizungua ile dunia, halafu anatokea jamaa mmoja kakaa kwenye kiti, akiiangalia hiyo dunia yake, nasiki huyo ndiye tajiri mwenyewe....’akasema

‘Yupo wapi huyo tajiri mwenyewe?’ akaulizwa

‘Mimi sijui, ...maana sijawahi kumuona,wengine wanasema yuko nchi za nje, wengine wanasema ni marehemu lakini mizimu yake ndiyo inafanya kazi, wengine wanasema yupo humu humu nchini, lakini hajulikani ni nani...hata mimi simjui...’akasema

‘Nikuulize umefanya kazi kwa huyo mdada kwa muda gani?’ akaulizwa

‘Nina miaka mitano kwa huyo mdada, kabla ya hapo, nilikuwa nafanya kazi kwa mama mmoja ambaye tulikuja kukosana naye maana mtoto wake ni muhuni, alikuwa akitaka kutembea na wafanyakazi wa humo ndani, mimi nikaona siwezi kuzalilika, nikaondoka zangu..’

‘Mama gani huyo?’ akaulizwa

‘Aaah, hata sina haja naye tena, japokuwa sasa ni tajiri kweli, ..nasikia ana hisa kwenye hiyo hoteli ya Paradise, sasa sijui kwa vipi, ..’akasema na kuangalia saa kwenye simu yake

‘Shoga yangu unajua natakiwa kuingia kazini, nina zamu ya usiku, mimi naondoka, ila ninachokushauri, kama unataka kuthibitisha hayo niliyokuambia kumuhusu mume wako, nenda jioni hii, jifanye unapita, au unashida kwenye hiyo hoteli, utamuona mume wako akiwa na huyo kimwana...’akaambiwa

‘Mimi sitaki wala kumfuatilia, ataniumiza kichwa changu bure, kama ni umalaya wake, aendelee nao tu, na mimi nitajua ni kitu gani cha kufanya, nataka nianzishe miradi yangu, ..ile uliyonishauri, kuna rafiki yake huyo mume wangu, kasema anaanzisha miradi ya kuwasaidia akina mama , sasa nataka nijiunge na mimi..’akasema

‘Hapo umelenga kwenyewe, hata mimi nimesikia na mimi nitajiunga huko huko, tutakutana huko huko.....’akasema

‘Lakini mume wangu hataki...’akasema

‘Ndio hayo hayo niliyokuambia, ....mimi naondoka, kama upo tayari tuongazane maana mimi hiyo hoteli naifahamika sana, nitakuelekeza wapi pa kumpata huyo mume wako ushuhudie mwenyewe kwa macho yako, akila raha na huyo mrembo...’akasema

‘Ooh, kweli eeh, utanisindikiza eeh, hilo neno,...kama ni hivyo ngoja nijiandae twende...nikajionee mwenyewe na nikimuona ama zake ama zangu,...utaona vumbi langu...’akasema na kuingia ndani kujiandaa na huyo shoga yake akachukua simu yake na kuandika ujumbe wa maneno

‘Keshaingia kwenye mtego, anakuja kazi kwenu...’

WAZO LA LEO:Unaposaidia mtu, kwa jambo lolote lile, hutakiwi kumtangaza kuwa umemsaidia huyo mtu, au kuja kumyanyapaa tena kuwa wewe ndiye umemsaidia kama sio wewe asingelifanikiwa kwa jambo fulani au angelikua njaa, au asingelipona na vitu kama hivyo.


Pia unapofanya jambo lenye manufaa kwa jamii kama msaada, haina haja ya wewe kujitangaza na kujinadi kuwa wewe ni mfadhili wao, kama usingelikuwa wewe hilo jambo lisingelifanyika, huo sio uungwana, huo sio msaada tena hiyo ni biashara yenye masharti. Msaada wa kweli hauna masharti, msaada wa kweli ni kama sadaka, ambayo inatakiwa ukiitoa kwa mkono huu, mwingine usifahamu. 
Ni mimi: emu-three

No comments :