Yule mdada alipoondoka, kwanza kulipita ukimia fulani, kama
vile watu wameambiwa watulie, na baadae kiongozi wa dini akasema;
‘Kuna mambo mengine yakitokea unajiuliza ni kweli au sio
kweli, ..lakini kwenye hii dunia lisemwalo lipo, na uchawi upo, hata kwenye
vitabu vya dini vimesema hivyo, na tatizo ni jinsi gani ya kupambana nao, au
kujikinga nao, wengi hukimbilia kwenye shirki, badala ya kumuendea yule
aliyewaumba. Ndugu zanguni, niliwaambia awali nimehisi hapa kuna tatizo, na hata
kabla ya kuja huyo mdada, nikahisi kuna kitu zaidi ya maelezo…’akatulia
‘Unataka kusema umeamini hicho alichoongea huyo mdada..?’
akauliza mama mwenye nyumba.
‘Kuamini au kutokuamini, ni nyie wawili, ambao mumeyashuhudia
hayo, na mnapata mitihani hiyo, ukijua kuwa yote hayo ni mitihani, lakini
vyovyote iwavyo nimewashauri jambo moja kubwa ni kujirudi, na kuwa kitu kimoja,
ili muweze kupambana na hilo tatizo mkiwa na nguvu moja, maana nyie ni kitu
kimoja mke na mume na familia kwa ujumla,…’akatulia.
‘Mara nyingi adui ili ashinde hupenda kuwagawa,
kutenganisha, kuwagombanisha…na hiyo ndio kazi ya shetani…kujenga fitina,..ili
wanandoa wakosane, wanandugu wafarakane, majirani wasielewane…huyo ni adui yetu
tupambane naye, lakini kwa njia sahihi….’akatulia, na mama mwenye nyumba
akachukua nafasi hiyo na kuanza kuongea;
‘Mimi nilisema kuwa mume wangu anakwenda kwa huyo binti na
nilisema nina video yenye ushahidi huo…lakini mume wangu akanikatalia,..sasa
tumuulize yeye anasemaje ..?’ akasema mama mwenye nyumba na mume akabakia
kimia, alikuwa kama kamwagiwa maji, hakusema kitu…hakumuangalia mke wake
alionekana kuwa mbali kimawazo.
‘Huna cha kuongea…’akasema baba yake.
‘Nitaongea nini tena baba hapo…, haya yamenikuta, na
kiukweli bila ya huyo mdada kuyasema hayo, nilikuwa siamini, …hata mpaka sasa
bado sijaamini, lakini nifanyeje, nitajitetea vipi,..kama ni kweli, basi ni
kweli…’akasema.
‘Kwahiyo unasemaje?’ akaulizwa.
‘Niseme nini hapo…kwasasa mimi namsikiliza mke wangu ..maana
kiukweli itakuwa imemuumiza sana, najaribu kufikiria kama mimi ndio yeye,…lakini
kiukweli mimi sijui hayo mambo, na kama kweli nilikuwa nafanya hivyo, ooh,
mbona ni mtihani huu, yaani mimi kiukweli sijaamini bado…’akasema.
‘Nikuulize kitu, hali kama hiyo ilishawahi kukutokea kabla?’
akauliza kiongozi wa dini na kuwafanya watu sasa wamuangalia kiongozi huyo
wakijiuliza ana maana gani.
‘Hali hiyo ya …..hapana, au una maana gani kiongozi,
umesikia alivyosema, na hili kwangu ni jipya, yaani ningebisha mpaka kesho…hata
hivyo, bado, jamani, yaani nitoke hivi hivi, mguu kwa mguu nisijitambue, hivi
kweli nyie mnaamini hayo…!’akasema kama anauliza lakini akionyesha uso wa
kutahayari.
‘Kwanini unauliza hivyo mkuu..?’ sasa akauliza mzee mmojawapo.
‘Mimi mawazo yangu, hayakuwa mbali na hilo aliloliongea huyo
bint, ni kweli yanaweza kuwa ni ya ukweli kwa mtizamo wa huyo binti, kama
nilivyosema awali , uchawi upo…, lakini pia, tusikimbilie huko moja kwa moja ,
kwa vile bado kuna utaalamu wa kihospitalini….’akasema
‘Hayo mambo yana matibabu hospitalini…?’ akauliza mzee.
‘Kuna jambo jingine nilitaka kuliongea kabla, na japokuwa
nilikuwa na walakini mbili, sasa…hili limetokea likanifanya nijiuliza mara
mbili, je ni mambo ya shirki, au ni tatizo la ugonjwa..’akasema kiongozi.
‘Kwani kuna ugonjwa kama huo, mimi naona ni mambo ya nguvu
za giza, na hospitalini kamwe hawawezi kuyaamini hayo au una taka kusema nini
kiongozi wa imani…?’ akauliza mzee.
‘Ndio, lakini hao wanatibia, madocta nk, ni wanadamu kama
sisi, na hata wao wanakumbana na matatizo kama haya, je hamjawahi kuhangaika na
mgonjwa wenu ikafikia sehemu huyo docta anakushauri ujaribu njia mbadala….?’ akauliza.
‘Ipo sana…..’akasema mzee.
‘Unajua mimi ni kiongozi wa dini wa eneo hili, lakini kabla
ya hapo nilisomea udakitari, kuna tatizo linaitwa ‘somna-mbulism’
sijui kama nimelitamka sawa…ni neno la kitaalamu, wanajua wenyewe wazungu
kwanini wakatumia neno hilo…’akatulia akiwaangalia kila mtu kwa waakti wake.
‘Ni nini hiyo…ni..ok, nimewahi kusikia kitu
kama hicho, ….’akasema mzee mwingine.
‘Yaani… mtu anaota na kutenda, huku akiwa
usingizi, ….na mara nyingi anachofanya hakikumbuki, anaweza akaota, akaenda
kuchota maji, au kufanya kazi, na baadae akarudi akalala..bila kujijua….ndio
maana nikamuuliza baba mwenye nyumba hii ni mara yake ya kwanza kumtokea
hivyo…?’ akauliza kiongozi huyo wa dini.
‘Mhh…uajua umeonga jambo, ukanikumbusha
kitu….’aliyesema hivyo ni mke mtu, akawa kama anawaza jambo, na kiongozi wa
imani akamuuliza.
‘Kitu gani, tuambie ndio maana nilitaka
mfunguke, muelezee kila kitu, huenda ikajileta yenyewe, ni kitu gani,
umekikumbuka…?’ akauliza.
‘Mume wangu unakumbuka,…’ akageuka kumuangalia
mume wake, ambaye bado alionekana kuwa mbali kimawazo.
‘Nini….hapana, sikumbuki….’akasema akitikisa
kichwa
‘Kuna kipindi fulani humu ndani kulikuwa
kunatokea maajabu, ..nilikuwa nikiamuka asubuhi, nakuta vyombo vyote vimeoshwa,
kumefagiliwa kumepigwa deki, na kila kitu kimepangwa vyema kabisa, hatukuwa na
mtu mwingine humu ndani, nikamuuliza mume wangu, ni nani kafanya hivyo, hata
yeye akawa anashnga tu, na ilitokea mara kwa mara kipindi hicho,…’akasema.
‘Unakumbuka kwanini ilitokea hivyo..?’
akaulizwa.
‘Kipindi hicho, nilikuwa nalalamika kazi
zimekuwa nyingi, na tukiongea na mume wangu anasema tuwe na subira maana hali
sio nzuri kiuchumi, basi, nikawa sina raha, na hayo yakaanza kutokea, unajua,
nilijua ni mume wangu anafanya kuni-shtukizia, lakini yeye akawa anashangaa, na
kuniuliza, …’akasema mke mtu.
‘Mhh…nakumbuka, lakini …sio mimi, niliyekuwa
nafanya hivyo..inawezekana ulikuwa ni wewe…ulipitiwa tu, maana ule usafi na
jinsi ya vitu vilivyokuwa vinapangwa ni utaalamu wa aina yake, na anayeweza
hivyo ni mwanamke…’akasema.
‘Yah,
ulikataa hivyo hivyo, kama ulivyokataa hili….na sasa unajiuma uma…inawezekana
ni wewe, inabidi kweli tumtafute docta,…ndio sasa naanza kukumbuka,
inawezekana, sasa huyo docta tutampataje kiongozi wetu wa imani..?’ akauliza
mama mwenye nyumba.
‘Lakini sioni kwamba hilo lina ukweli ndani…na
hata kama lipo, mimi sina tatizo hilo…’akasema baba mwenye nyumba
akizidi kujitetea.
‘Kama huna tatizo hilo, ina maana ulifanya
makusudi,…kama ulikusudia tuambie tujua, utubu dhambi zako…’akasema mama mwenye
nyumba, na baba mwenyenyumba akabakia kimia.
‘Sasa kabla ya kufikia maamuzi hayo, kuna mambo
mawili ya kufanya, kwanza, nyie wawili mshuke chini, muombeane msamaha, maana
mola hukubali toba za yule alietubia madhambi yake, akawa hana kinyonga na mtu,
akasamehe ili na yeye aweze kusamehewa, na la pili, ndio hapo tutamkabidli yeye
muumba, tutaomba kwa pamoja, ili tupate radhi zake, ulizi wake, na kama kuna
jambo la shiriki, basi mwenyezi mungu aliondoe, na kuweka ulinzi wake, …sawa..?’akasema
kiongozi wa imani akiwaangalia wanandoa hao.
‘Sawa kabisa…’wakasema wazee wale wawili na
kijana akawa wa kwanza kusimama akiwasubiria wazazi wake, kwa uso wenye furaha.
‘Unasemaje baba mwenye nyumba, bado una mashaka
na hilo..?’ akaulizwa na wazee
‘Mimi nilitaka nione hiyo video kwanza, nihakikishe
kwa macho yangu maana mimi sijaamini hilo…’akasema
‘Kama ni kuiona hiyo video, basi mtaiona mkiwa
nyie wawili, kama ni muhimu kwenu…, ila mimi ningelishauri muiharibu kabisa
hiyo video…, isje kuleta chuki nyingine…’akasema kiongozi wa dini.
‘Ni kweli, hebu ilete hapa tuiharibu…’akasema
mzee akimuangalia mama mwenye nyumba.
‘Hapana siwezi kuiharibu kwa sasa… bado nataka
kuifanyia kazi…’akasema mama mwenye nyumba.
‘Kazi gani tena..?’ akauliza baba mwenye nyumba
akimuangalia mke wake.
‘Nataka kuhakiki kama alichosema huyo mdada ni
cha u- kweli,…’akasema
‘Kwa vipi..?’ akauliza mumewe.
‘Kuna mtaalamu mmoja, yeye kasomea, mambo ya
mitandao, lakini pia ana utaalamu wa nguvu za giza, anasema yeye anapambana na
hayo mambo, yeye, hatai kuitwa mganga wa kienyeji, bali anapendelea akiitwa
mtaalamu, maana hapigi ramli, au…sijui tunguli, hapana, yeye anatumia mitandao…alisema
yeye anaweza kupiga picha, na kwenye picha kunaweza kukawa na mtu zaidi ya
mmoja,..labda, nikamuuliza kwa vipi.
‘Akasema, duniani kuna viumbe vingine
havionekani, kama majini mashetani, na usiku kuna wachawi, sasa unaweza ukapiga
picha bila kujua kuwa viumbe hao wapo karibu yako,..kwenye picha hawataonekana,
lakini yeye akiingalia, akaweka kwenye vipimo vyake anaweza kuona vitu kama hivyo…’akasema
‘Kwanini alikuambia hayo…?’ akauliza mumewe
‘Ilitokea tu, wakati tunaongea, rafiki yangu
alinitambulisha kwake, …ni mumewe….’akasema
‘Ok….kama ni hivyo sawa…’akasema baba mwenye
nyumba.
‘Lakini huo ndio mwanzo wa kuamini mambo hayo,
au unataka uhakikishe kitu gani sasa..?’ akaulizwa
‘Kama alichosema huyo mdada ni kweli, ina maana
mume wangu alipokuwa huko chumbani, alikuwa pamoja na huyo mtu mwingine lakini,
huyo mtu mwingine alikuwa haonekani, kwa kauli yake au sio…sasa kama haonekani,
kwa ujuzi wa huyo mtu atamuona, kwahiyo tutagundua ukweli wa maneno ya huyo
mdada, kama kweli hatudanganyi…’akasema mama mwenye nyumba.
‘Unajua ukianza kupekenyua, pekenyua hayo
mambo,.. ndio mwanzo wa kujiingiza kwenye shirki, kitu ambacho ndicho
tunakikwepa hapa, au sio jamani wazee wangu…’akasema kiongizi wa dini.
‘Mimi siwezi kuingia kwenye shirki hata siku
moja… imani yangu ni thabiti, ndio maana hata hao mnaowaita wachawi sijui,
hawajaweza kunichezea mimi,…hilo la mume wangu kufanya hayo, akilini mwangu
kuwa ni uchawi sijaliafiki,…ila nilishagundua kuwa kuna tatizo kwa mume
wangu,sasa sikuwa na uhakika ni tatizo gani,…kama alivyosema kiongozi wa dini, kuwa
kuna hali hiyo ya kutembea kwenye ndoto, hapo naweza kuamini kidogo,…sasa mimi
nahitajia muda, kuyachunguza haya…’akasema.
‘Kwahiyo bado huniamini mimi…?’ akauliza mume
wake.
‘Kukuamini au kutokuamini, kunahitajia mambo
mengi, na mojawapo ninalotaka kulifanya ni hilo, la pili…ni hilo la kumtafuta
dakitari, na la tatu ni kumuelekea mwenyezimungu, mimi hayo yote nayapitisha,
ila hilo la uchawi, bado sijaliamini, labda huyo mtu anionyeshe huyo mchawi
kwenye hizo picha, …’akasema.
‘Atakuonyeshaje sasa..?’ akaulizwa.
‘Hilo niachieni mimi..sio kwamba nitaamini,
lakini kama kasema anaweza kumgundua mchawi hata kama kajificha ,basi
ataligundua na hilo..alisema hata picha kama kuna kitu kisichoonekana lakini
kimechukuliwa na picha atakiona, alinionyesha pich alizopiga usiku akiwa piga
wachawi, lakini ukiziangalia hivi huoni kitu, yeye anakiona hicho kitu,…na ana
namna ya kusafisha hizo picha kwa utaalamu wake, na hizo sura za wachawi
zikaonekana kabisa…..’akasema.
‘Oh, unaamini hayo..? akaulizwa na mumewe.
‘Kuamini au kutokuamini kutakuja baada ya
ugunduzi huo..mimi tabia yangu ni kufanya utafiti kwanza, ndio maana nilikwenda
shule…, na nikigundua basi, nitakuwa nimegundua jambo ambalo nilikuwa silijui,
akili yangu itaongeza ujuzi huo, japokuwa kwangu mimi bado nayaona mambo hayo
kama nguvu za giza tu, mambo ambayo hayahitajiki kwetu sisi wanadamu…’akasema.
‘Sawa, sasa mnasemaje..mpo tayari kushikana
mikono na kuyamaliza haya mambo..?’ akauliza kiongozi wa dini.
‘Samahanini wazee wangu…..nisema ukweli wangu,
hata kama nitakubali hapa, kuwa nimesamehe, nimshike mkono, utakuwa ni unafiki
tu, bado mimi sijawa na imani
…sijakubaliana na hili jambo kuwa ni kweli, mume wangu alikuwa hajui mambo yote
hayo, kuwa hakuna kitu kwenye moyo wa mume wangu, kumtamani huyo binti, …hawa
mabinti, maana hata huyu kasema hay ohayo yamekuwa yakimtokea, sijafuatilia
hili, ila nilishaanza kufuatilia…’akasema.
‘Sasa unataka kusema nini..?’ akaulizwa.
‘Nasema hivi, nahitajia muda wa kulifanyia kazi
hili na..nikijirizisha basi , nitawaambia, lakini sio kwamba,..nimekasirika au
nina nia yoyote mbaya,..naomba mnielewe hivyo, kwasababu,..nilipoona hiyo
video, moyo wangu ulikufa ganzi, na mimi sio jiwe, penzi nililokuwa nalo moyoni, silioni tena…aah,
nisameheni tu, na mwenyezimungu anisamehe pia…’akasema.
‘Oh…lakini mwenyezimungu katuambia, kamwe
tusiweke kinyongo moyoni, au tusiwe na kisasi au chuki moyoni, maana umauti
ukikukuta ukiwa bado na kinyongo hicho, au chuki hizo,..kuuona ufalme wa
mbingu, kuingia peponi kwako itakuwa ni mtihani, na mwenyezimungu anajua
zaidi..ni bora msameheane,..hata kama moyoni bado una hasira, ile kusamehe,..huku
unamuomba mungu, mungu mwenye atailanisha nafsi yako, nahasira na chuki hizo,
zitayeyuka kidogo kidogo,…muhimu ni kumuomba mwenyezi mungu awasaidie, maana
haya mambo bila muongozo wa mola wetu bado yatakuwa ni mazito kwetu,…’akasema.
‘Kiongozi,..hata kama moyoni, au kwenye nafsi
yangu bado sijarizika, nikubali tu…hapana mimi bado nina ..duku duku,…kwani jamani, siruhusiwi kujirizisha
kwanza.niongoze kiongozi wangu, mimi ninachotaka ni kufany autafiti,
nijirizishe, maana mume niliyemjua sio huyu tena….’akasema.
‘Hata hivyo,…mimi niliona ni vyema mkasameheana
kwa leo, huku mkiendelea na michakato mingine kama nilivyosema, huku mnamuomba
mungu awasaidie, maana haya yote sio kwa ujanja wetu, na hatjui ya kesho,
hatujui uhai wetu upo kiasi gani….ni muhimu tukalitambua hilo…’akasema kiongozi
wa imani.
Basi wote wakakubaliana tukaanza ibada ya
kumuomba mwenyezimungu na kuomba hayo yote yaliyopo humo kwenye nyumba kama ni
ya kibinadamu au kama ni ya kishetani..yaondoke na nyumba ibakie kwenye amani…na
tuliomba mwenyezimungu atupe kinga yake, na kutuongoza kwenye njia sahihi,
baada ya hapo wanandoa hao wakashikana mikono, na kijana alionekana kufurahi
sana.
‘Kabla hatujaondoka nina ombi jingine na hili
sitaki likataliwe, na sitarudi nyuma tena, kwa uamuzi huo…’akasema mama mwenye nyumba.
‘Ombi gani tena..?’ akauliza mume mtu akionekana
kuwa na mashaka zaidi.
‘Ni kuhusu huyu mfanyakazi wa ndani tuliye naye
sasa…’akasema.
‘Ehe, unatakaje au naye ana nini..?’ akaulizwa.
Huyo
mama hakutaka hata kuniangalia machoni, akasema…
‘Mume wangu, ..hili ninataka wewe ulifanyie
kazi, ..utajua wewe mwenyewe kwa jinsi gani, …’akatulia.
‘Niambie mke wangu nipo tayari, kukubalia
lolote lile, najua nimekukosea sana, na sitaki niendelee kukukosea, nataka
nikuonyesha kuwa mimi ninakupenda sana mke wangu...’akasema baba mwenye nyumba
akitamani hata kupiga magoti.
‘Najua kwasasa utasema hivyo, siwezi kukulaumu..nimekuzoea…,
ila hili, nimeliwazia sana nikaona ni bora iwe hivyo, hata kama watu wataniona
mimi ni mtu wa ajabu sana…’akasema mama mwenye nyumba.
‘Sawa uamuzi ni wako, kama mnataka muongee
wawili basi mturuhusu sisi tuondoke…’akasema kiongozi wao wa imani.
‘Hapana hili nitaka niliongee hapa hapa ili
kila mtu alisikie na lifanyiwe kazi , ….’akasema sasa akimuangalia mume wake
machoni, halafu akageuka kuniangalia mimi, na hapo moyo wangu ukaanza kudunda,
nikahisi kuna jambo kubwa linakuja,..lakini siweza kubahatisha ni jambo gani!
NB: Hatimaye nimefanikiwa kuandika sehemu hiyo
hivyo….kama nilivyosimuliwa na mwenyewe, tusihie hapa kwa leo.
WAZO LA LEO: Riziki
haigombewi, kwani kila mja ana fungu lake.
Lakini pia riziki haupewi, ukilala na
kusubiri fanI zake.
Jibidishe kwa amali hata kupiga kiwi, ufanye
ibada na kila kitu kwa mahala pake.
Mola ni
mwingi wa rehema, atampa kila mja fungu lililo lake.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment