Ile sura niliyoiona kwa huyo mama, ilinitosha kuwa ni ujumbe
kwangu, mimi nikanywea, nikasubiria kauli itakayotoka, kiukweli nilishajiandaa
kuondoka, lakini sikujua wapi pa kwenda, ila nilitamani tu kuondoka hapo,…na
huko ninapokwenda nitaishije, hayo kwangu akilini yalikuwa hayapo, lakini kama
tuliishi mimi na mama yangu kwa kuomba, kwanini nije kushindwa kuishi. Mungu
mwenyewe anajua!
‘Hii ni zawadi yako, au sio…?’ huyo mama alianza kuniuliza
hivyo, huku akiwa kainua mfuko wenye kitu ndani, ni mifuko unayowekewa kitu
ulichonunua madukani hasa supermarket,…hata sikujua ni kitu gani, au kimetoka
wapi.
Nikajua labda ni zawadi ya kuondoka nayo, sikusema kitu wala
kusimama kuipokea, nikawa nimetulia tu kimia, akilini nikiwa nashindwa hata
kuwaza, mambo mengi yamepita akilini , na kichwa hapo kinaanza kuuma, lakini
nikajitahidi kujituliza.
‘Nakuuliza hii zawadi ni yako, au unaogopa kusema sasa, hii
zawadi amekuletea mume wetu, kakuletea wewe bi mdogo wake, ichukue, …’akasema akinirushia
na mimi sikusogea kuichukua, nikawa nimetulia tu. Nilikumbuka maneno ya mama,
akinikanya nisigombane na watu, aliwahi kuniambia;
‘Binti yangu, ukiona
mwenzako kakasirika anaongea kwa jaziba wewe tulia mpe muda amalize jaziba
yake, halafu akitulia ndio unaweza kufikiria jambo la kumjibu. Mara nyingi mtu
kama huyo ukimjibu ghadhabu zake huongezeka, na inaweza kutokea madhara makubwa!
‘Utashangaa nimeipata wapi hii zawadi yako, na mletaji
kashangaa nimeipataje,…mimi nilikuja mapema tu, nikijaribu kuchunguza
kinachoendelea, …’akasogea ndani na kusimama, akageuka kuangalia mlangoni, huku
anaongea.
‘Nimesikia mengi kutoka kwa majirani, ..sikutaka kuchukulia
haraka, …nilijua ipo siku tu , nitawanasa,…sasa leo nimewanasa, na nimegundua
kuwa ni kweli, wewe ni nyumba ndogo ya mume wangu,…unajua mimi ni mvumilivu
sana, lakini uvumilivu una mwisho wake, siwezi kuvumilia tena, maana haya yametokea
mara nyingi,…sasa nasem basi, umesikia nitakuachia huyo mume, lakini sio kuwa
nitawaachia, make humu, hapana wewe na yeye mkatafute wapi pa kuishi..huo ndio
uamuzi wangu….’akasema na aliponiona nipo kimia, akanigeukia.
‘Unajua,…mama yako, alinikabidhi wewe, akasema nikulee kama
mwanangu, nikulee kama binti yangu, kumbe nimechukua nyoka ndani ya nyumba
yangu, siwezi hata kuamini,..unajifanya mpole, unajifanya hujui kitu, kumbe,
umekubuhu….huwezi kusema kitu maana mimi mwenyewe, nimejionea kwa macho
yangu..halafu ulipogundua kuwa nimewafuma, ukajifanya kukurupuka na kukimbia,
ujanja w kitoto…’akasema.
‘Sasa nimekuambia mwenzako, afungashe, na wewe nimekuja
kukuambia ufungashe…mkatafute pa kuishi, hii nyumba ni yangu ni mali ya wazazi
wangu, …nina mamlaka nayo,…kama ulifikiri kuwa ni mali ya mume ..umenoa, huyo
mume hana kitu hapa…unisikie vyema, mtaenda kutafuta sehemu ya kupanga, muanze
maisha yenu, mjifunze maisha,….unanielewa…’akasema akiniangalia na mimi nikawa
kimia, ni kama sikuyasikia hayo maneno.
Machozi yalikuwa yakinitoka,..yanatiririka kama maji, lakini
sikuweza kutoa sauti ya kulia, kilio kilikuwa ndani ya moyo, nasononeka,
..naomboleza, ..lakini ni nani atalijua hilo, ni nani atamuonea huruma binti
masikini…
Mara akatokea kijana wake,..akaja na kusimama mlangoni,
akasema
‘Mama mbona unachukulia haya mambo kwa jaziba, ….’akasema na
mama yake akamuangalia kwa macho yaliyojaa hasira,
‘Hayakuhusu haya,…’mama akasema.
‘Mama,…., kwanza naomba samahani, kuwaingilia …ila mama una
uhakika na unachokisema, ….?’ Akauliza, sasa akiingia ndani kabisa.
‘Uhakika gani ninao-uhitajia mimi…., hebu niambie mwanangu,
nimemfuma huyu Malaya akiwa chumbani kwetu na mume wangu, akiwa kavalia khanga
moja, wapo wana, hapo unahitajia ushahdi gani mwingine, niambie wewe
unayejifanya mkubwa sasa, …..yaani nasikia hata kutapika…’akasema.
‘Mama umuogope mungu, hivi kweli mama, huyu anaweza kufanya
kitu kama hicho kweli mama, nakuomba mama urejeshe moyo wako nyuma, wewe ndiye
uliyesema huyu ni binti wa kijijini hajui lolote, tumuongoze, leo hii unasema
kayafanya hayo, mama mimi siamini hayo, hajafanya hayo unayoyasema….’akasema
huyo kijana na mama yake akamuangalia huyo kijana usoni akiwa katahayari,
akasema;
‘Ina maana mimi naongopa, ina maana mimi macho yangu hayaoni
siku hizi, nimekulea nikakuonyesha njia, sasa umeota mapembe,…sikiliza wewe mtoto,
wewe bado mdogo, haya hayakuhusu kabisa…, na hujui uchungu nilio nao mimi….subiria
muda wako utafika, utaoa, na utafanyiwa hivyo ndio na wewe utajua ni kwanini
ninasema haya…’akasema.
‘Mama nayasame haya kwa vile mimi namfahamu sana huyu mdada,
hawezi kuyafanya hayo, na unakumbuka siku moja nilikuambia kuwa huyu mdada
alishikwa na baba…alishikwa na baba
akitaka kukimbia….’akatulia akimuangalia mama yake.
‘Mama, huyu mdada ana matatizo makubwa, anapata shida,
anaweweseka usiku, na wakti mwingine anadondoka na kupoteza fahamu….je ulimpa
nafasi baba akuelezee kama huyo mdada hakudondoka akapoteza fahamu na baba
alikuwa akijaribu kumrejesha katika hali yake, ..je mama angelikuwa ni binti
yako, ungelifanyaje,…mama wewe ulitufundisha tumuogope mungu, kwa kusingiziana
uwongo, je kama unachomsingizia mwenzako sio kweli, utasemaje mbele ya mungu...’kijana
akasema.
‘Wewe mtoto, wewe unataka kusema nini kuwa mimi namsingizia
uwongo huyu mwanamke…, kama namsingizia uwongo kwanini hajitetei…aseme yeye mwenyewe
kama sio kweli…kama sio kweli sikumkuta akiwa kalala chini akiwa uchi, na mume
wangu yupo juu yake, …asema yeye mwenyewe kama sio kweli….’akasema na mimi
nikaendelea kukaa kimia.
‘Eti ni kweli hayo dada…?’ akaniuliza huyo kijana
akiniangalia moja kwa moja, na mimi nikawa nimeinama chini, nikuendelea kukaa
kimia, na mama akaonyesha ishara kama kusema
‘Unaona…’ lakini hakutamka neno….na kijana akaniangalia kwa
mshangao, na kusema;
‘Sema ukweli wewe mdada, jitetee, shauri lako…, ukikaa kimia ni nani
atakusaidia….’akasema, na mama akasemaa;
‘Usimlazimishe kukana maovu yake, kukaa kwake kimia,
inaashiria nini, kuwa ni kweli, na moyoni anaona haya….kwa uchafu walioufanya
na ….huyo baba yako….’akasema mama.
‘Mama…usiseme hivyo, una uhakika….’akasema kijana
‘Si huyo hapo,….umemuuliza kakujibu nini, kakaa kimia, maana
ukweli unauma…ni ..hata sijui niseme nini, ashukuru mungu siku hizi hasira
zangu zimeenda likizo…’akasema mama.
Na mimi kwanza nilikaa kimia, nikiwazia haya mambo kwa
undani zaidi, sikuwa na la kujibu, nilishindwa nijubu nini maana hayo
anayoyasema huyo mama, siyaelewi, na sijui yametoka wapi, baadae sijui
ilikuwaje nikajikuta nasema haya maneno;
‘Mungu pekee ndiye anayejua ukweli wa hayo yote, kama
umeamua kuamini hivyo, hata nifanyeje siwezi kubadilisha imani yako, ila
mwenyezimungu peke yake ndiye anayeweza kufanya hivyo….’nilipotamka maneno
hayo, nilihisi kichwa kikitulia maumivu, na hapo nikaingiwa na nguvu y akuongea
zaidi, nikasema;
‘Mimi sina uwezo wa kuwafanya nyie muamini ukweli ulivyo…ila
mungu anaweza. Lakini ni bora niseme ukweli,…, mimi sijui hicho
ninachosingiziwa nacho,…sijui mama unaongea nini, mpaka sasa naona kama umeamua
kunitungia uwongo, labda ili uweze kutimiza unachokitaka….’niliposema hivyo
huyo mama akataka kunikatiza, lakini sikumpa nafasi nikaendelea kuongea.
‘Mama…kilichotokea,…. mimi nilidondoka, na kupoteza fahamu…’niliposema
hivyo, mama akacheka kwa kebehi, akijua labda nimesema hivyo kwa vile kijana
wake alisema hivyo.
‘Mimi nilidondoka, … baada ya kuisoma barua iliyotokea
kijijini kuwa mama yangu amefariki….’niliposema hivyo, machozi yakawa yananitoka
utafikiri maji yana mwagwa, na mama akabakia mdomo wazi, kanikodolea macho
utafikiri kasikia jambo gani, hakutarajia hilo kabisa, huenda hata hiyo barua,
labda aliiona mume wake na hakuweza kumuambia mkewe kuwa mimi nimeugundua
ukweli.
‘Mama, wewe umesema kuwa umenichukua mimi kama muwe kama wazazi
wangu, kwa vile mama alikuomba ufanye hivyo, ..je ungeyafanya haya kwa mtoto
wako,…, najiuliza ni kwanini mkanifanyia mimi hivyo, au ni kwa vile, …’nikasema
hivyo bila kumalizia.
‘Mama nyie …mlipata
taarifa hiyo mkakaa kimia…’nikasema na huyo mama sasa akabadilika sura. Kutoka
kwenye hasira na kurejea kwenye kushangaa…binadamu sura hujieleza ukimuangalia
kwa makini.
Mama sasa akawa anatafuta njia ya kujitetea, kwanza akahema
kama mtu aliyepo kwenye usingizi akibadili pumzi kwa nguvu. Akamtupia jicho
kijana wake , na kijana wake akawa kainama chini, sasa ikawa zamu yao, kuhisi
unyonge, maana ukweli huuma!
Lakini kama ujuavyo, mwenye uwezo, tajiri, watawala hata
wakikosa hawakosi neno la kujitetea, huyo mama akasema;
‘Ni nani alikuambia upekue pekue huko ndani kwangu..si
nilishakuambia kuwa wewe kazi yako ni kufanya usafi tu huko ndani…na
nilishakuambia kama baba yako yupo wewe usiingie kabisa huko ndani…kwanini sasa
unajiamini mpaka unaanza kupekua pekua huko unatafuta nini, je nikipotolewa na
kitu utakataa kuwa wewe hujahusika, na kumbe wewe ndiye unamtia mshawasho mume
wangu kwa kuingi ahuko chumbani na khanga moja,…niambie ni kwanini ukafanya
hivyo?’
‘Mama, mimi sikupekua pekua vitu vyenu nilikuwa nakung’uta
vitabu mavumbi, na kwa bahati mbaya ndio hiyo barua ikadondoka, na kufunguka,…na
mama sijawahi kuingia ndani akiwepo baba kwa utashi wangu, kama niliingia, ni
kwa muito wa baba….’nikasema na hapo akakunja uso kama anataka kusema neno, na
mimi sikumpa nafasi nikaendelea kusema;
‘Wakati nakugung’uta vitabu, ndio hiyo barua ikadondoka,…na
ilipodondoka, ikafunguka,…na ndio nikaona maelezo ya kutoka kijijini, na macho
hayana pazia,..kuona maneno hayo,…nikavutika kuyasoma yote,…na ndio hapo
nikagundua hilo,… kama ni kosa, hapo nimefanya kosa, kwa kusoma barua yako,…naomba
mnisamahe, lakini najua ni mungu alitaka kunifunulia ukweli,..mlitaka kunificha
mungu akataka kunifunulia ukweli…. sasa nauliza ni kwanini mumenifanyia
hivyo…’nikasema
Huyo mama sasa akanywea, akahema, akageuka kumuangalia
mwanae, kama vile anataka amsaidie kujitetea, lakini kama nilivyosema watu hawa
wenye uwezo, hawakosi neno,…akasema;
‘Sikiliza, wewe binti, hatukuwa na nia mbaya kwako,…nia yetu
ilikuwa ni njema kabisa, ya kuwa tukikuambia huo ukweli, kwanza
utachanganyikiwa, utashindwa kufanya kazi, na wewe hujadunduliza kiasi cha fedha
cha kukuwezesha maisha, na kwanini tulifanya hivyo, tulijua ukiambiwa utataka
kwenda nyumbani, na ukienda huko unaweza usirudi kwa hali ilivyo...'akasema
'Kwanini jamani....'nikasema hivyo.
'Sisi tunaona mbali zaidi yako...hebu jiulize ungeenda hivyo kiharaka hivyo, nani angelusaidia, hpo kuna nauli..kuna matumizi, na huko je.... huko
ungeenda kuishie, na maisha yalivyo huko sio kama ulivyoondoka, ..huko sasa hivi, huko
kijijini eeh, we usikie tu, hali ni mbaya sana hakuna chakula watu wanakufa kwa
njaa…, na isitoshe, hali ni hatari, watu wanauwawa ovyo, tuliogopa ukienda huko
na wewe utauwawa…sasa nikuulize je hivyo tulifanya vibaya...’akatulia.
'Mimi najiuliza kame ingelikuwa ni wewe umefiwa, na tena mama yako, ungelifanyiwa hivyo ungelifurahi...yaani hata..hapana mimi bado sijaridhika na hilo, lakini nitafanyeje, mimi naweza kusema nini kwenu, mliamua kwa vile....'hapo sikumalizia, na huyo mama akanidakia kwa kusema.
‘Mama yako alinikabidhi wewe akasema nikulinde, na nihakikishe
upo mikono salama, na ndicho tulichokifanya,…hata kama hutaelewa,…na hata
hivyo, kwa mfano tungekuambia, uende…ungeenda huko ungelifanya nini, maana hata
sisi wenyewe taarifa hiyo tuliipata imechelewa walikuwa wameshazika kutokana na
hali ilivyokuwa huko…, mama yako aliungua sana….umenielewa, pole sana, na
tuliza kichwa chako…’huyo mama akasema alipoona mimi ninalia kwa kwikwi.
‘Sasa pamoja na hayo
najua sasa hivi upo kwenye majonzi,….wenzako sasa wameshasahau wa
kusahau…lakini ni lazima nihakikishe mambo fulani, japokuwa umeweza kujitetea
kihivyo,..kwa hayo yaliyotokea, nataka uniambie ukweli, ..ukweli ndio
utanifanya na mimi nitulize moyo wangu, nataka unijibu bila kuogopa, …je mume
wangu amekuwa akikufanyia hivyo mara ngapi…?’ akauliza na kijana akataka
kuingilia lakini mama yake akamuashiria anyamaze.
‘Kunifanyia hivyo kw vipi, sijakuelewa mama..?’ nikauliza
nikimuangalia huyo mama naye akawa kanikazia macho, na kwa hali hiyo mimi
nikatizama chini.
‘Nilimkuta anakuwekea mdomo wake kwenye mdomo wako….unaelewa
ni nini maana yake hiyo, unieleze hayo anakufanyia, hivyo ….je ni mara ya ngapi
kakufanyia hivyo…?’akasema na mimi nikashtuka na kusema;
‘Kwanini afanye hivyo,…mama, mimi sijui unachoongea, kwanini
afanye hivyo, hata sielewi…mimi nilipozindukana nilimkuta baba kachuchumaa,
kaniinamia, kama vile yupo juu yangu, akiwa hivyo, kwa haraka nilipozindukana,,..nilijua
anataka kunifanyia kitu kibaya, ndio maana nikaanza kupiga ukelele na kukimbia…’nikasema.
‘Kwahiyo yote aliyokufanyia baba yako hukuyaona, unataka
kunidanganya eeh?’ akaniuliza.
‘Kwani alinifanyia nini..mama mimi sijui hayo unayoyaongea,
..sikumuona akinifanyia hivyo, maana wakati nadondoka humo ndani nilikuwa peke
yangu, hata sijui huyo baba alikuja saa ngapi…’ nikasema sasa nikiwa na hamu ya
kutaka kujua.
‘Wewe…unajifanya hujui, nakuuliza ni mara ngapi kawahi
kukufanyia hivyo, au vitendo kama hivyo…wewe sio mtoto mdogo utake nikuffanulie
kila kitu, haya labda nisema, kakulazimisha hivyo, mara ngapi, ….?’ Akauliza.
‘Mama kwakweli sijui unachotaka kukisema, kama ni hivyo,
kupoteza fahamu, na labda, mimi sijui kama alifanya nini, ..sijawahi kufikia
hatua hiyo, …ni huo mshutuko ulionifanya nidondoke na kupoteza fahamu….sijua
lolote baadae mpak niliposhituka na kumkuta hivyo…’nikatulia nikisita kuelezea
tukio lile lililopita.
‘Nakuuliza tena, maana isije ikatokea tatizo ukajuta, ..mimi
ni mtu mnzima, nawafahamu sana wanaume, leo na au kesho kutwa, nije kusikia
kuwa una mimba, nakuapia, utatoka humu ndani ukiwa huna sura, nitakurarua,
mpaka unijue kuwa mimi ni nani…’akasema kwa hasira.
‘Mimba !!!...mama mimba itoke wapi….mimi siwezi kufanya kitu
kama hicho…, kwa vipi mama,..mimi sijui kitu,….mama mimi sijui hayo mambo…sijawhi
na sitaki kujihusisha na mambo hayo , mama alinikataza kabisa…’nikasema na
akanisogelea kama kuninong’onezea kitu ili kijana wake asisikie…, akaniuliza
jambo, sikumsikia vyema, au sikumuelewa alikuwa na maana gani, lakini nikahisi
tu, na kusema;
‘Mama mimi hayo siyafahamu kabisa,…mama alinikanya sana kufanya
urafiki na wanaume, hayo unayoyaongelea kwangu ni mageni kabisa siyajui mama…’nikasema.
Mama akaniangalia
machoni kwa makini kama ananipa kuwa kweli niliyosema ni sahihi au najaribu
kumuhadaa, halafu akasema;
‘Sawa…ila nakuonya tena na tena, huo mwili na kupendeza usije
kukudanganya, watakuambia wewe ni mnzuri, unapendeza na mambo kama
hayo…..watafikia hata kukupatia zawadi,.. na ujanja wa wanaume, ili kukufanya
ujione wana kupenda, wengi wao huanzia kwenye kukupa zawadi,….’akasema
‘Mama mimi sijachukua zawadi ya mtu yoyote, wakinipa huwa
nakataa…’nikasema.
‘Na hiyo zawadi aliyokuletea mume wangu ilikuwa ni ya nini,
kama sio mlishaanza urafiki…’akasema.
‘Zawadi gani mama, baba hajawahi kunipa zawadi nikiwa peke
yangu, mara nyingi akileta zawadi, anakupa wewe ndio unanpa mimi,…kweli si
kweli…?’nikasema na kumuuliza.
Mama akahema kidogo,
halafu akageuka kumuangalia kijana wake, kuna kitu alitaka kuniuliza lakini
kuwepo kwa kijana wake, akashindwa kuongea, akaniangalia na kusema;
‘Haya mimi nakuambia tu…usije kudanganyika ukaingilia ndoa za
watu, usije kudanganyika ukaanza mapenzi na kijana wangu, huyu kijana wangu, sio
hadhi yako, usije kukudanganya kuwa anaweza kukuoa, hilo halipo na
sitakukubalia hata siku moja, na…. usije kudanganyika ukaanza umalaya huko nje,
ukaniletea mimba humu ndani au magonjwa, ukumbuke hayo, usije kunilaumu na kuniona
mbaya,..’akasema.
Mimi nikakaa kimia, aliponiona sisemi kitu akasema;
‘Nikuambie ili kama angalizo, kuanzia sasa hivi, nitakuchunguza hatua kwa hatua, ole wako,
unasikia ole-wako, nije kugundua kuwa kuna kitu kinachoendelea kati yako wewe
na mume wangu au kijana wangu….’akasema kwa hasira.
‘Mama mimi naomba niondoke humu ndani, haya ya humu ndani
siyawezi,…kwani yaonekana wewe huniamini tena…, nilijua nyie ni kama wazazi
wangu, sasa nageukwa,…’nikasema.
‘Uondoke , uende wapi… na ni nani anakugeuka, unaona kauli
yako, nahisi kuna kitu unanificha, sema ukweli, nikusaidie, je kuna lolote
kakufanyia mume wangu..?’ akaniuliza
‘Hapana, mimi naona ni bora nirudi kwetu kijijini…’nikasema
‘Hahaha, eti urudi kwenu kijijini, wenzako huko
wanapakimbia, wanakuja huku , wengine wanatafuta sehemu ya kwenda wewe..unataka
kwenda huko , sawa kama unataka kurudi kwenu kijijini, mimi nitakupatia nauli
yako uende, lakini ukiondoka hapa ndio bye bye…waulize waliokuwepo hapa mimi
sina muda wa kubembeleza mtu,…’akasema
‘Kwanza usiku mimi silali…nateseka na …sijui kuna nini humu
ndani…’nikasema na hapo akashtuka na kusema
‘Kuna nini kinatokea usiku…haya anza kuongea maana nilikuwa
nasubiria hilo, usiku unaona kitu gani, kunatokea nini..?’ akauliza na mara
kukasikika mngurumo wa gari, mume wa huyo mama alikuwa karudi na wageni, ..
‘Nona kuna wageni, tutaliongelea hilo baadae…nataka uje kunielezee
vizuri kabisa, …kwasababu kuna mwenzako alikuwa akiishi humu ndani kabla yako,
alivumisha mambo mabaya sana, eti humu ndani kuna mashetani, hayo mashetani
aliyaleta yeye, mbona sisi hatuyaoni hayo mashetani, acheni mambo ya
kishirikina….sasa jiandae kuniambia ukweli wote …’akasema akigeuka kuondoka.
Alipoondoka, kijana wake akasema;
‘Kwanini umemuambia hayo mama yangu..?’ akauliza
‘Kwasababu ndio ukweli ulivyo, mimi usiku nateseka, silali,
kwanini nisimuambie…’nikasema
‘Una uhakika kuwa kweli kuna mashetani humu ndani, mbona
mimi sijawahi kuyasikia hayo mahetani …yapoje,…., au kunitokea nini…halafu
kwanini iwe ni wewe, na huyo mwenzako aliyekuja leo na kuondoka…msitake
kuwachanganya wazazi wangu…’akasema.
‘Mimi hayo siyajui kwasababu nimeanza kuyapatia hapa,…sijawahi
kusikia hivyo nikiwa huko kwetu kijijini,…’nikasema.
‘Unasikia,….uwe makini na kauli zako, mama ni mjanja sana,
anatafuta njia ya kumuona baba ana makosa, nina uhakika kuwa baba hana makosa
mimi namfahamu sana baba yangu, na ikithibiti kuwa kuna kitu kinahusiana na
baba, na mama akasikia kutoka kwako,…utavuruga ndoa yao,…na hapo hutapata
mtetezi tena, baba ndiye mtetezi wako, na alipanga mambo mengi ya kukusaidia,
…’akasema
‘Kwahiyo wewe ulitakaje,…kuwa mimi nikae kimia huku napata
shida, ….hapana mimi nitasema ukweli, hata kama ukweli huo utaniumiza
mimi,lakini siwezi kudanganya…’nikasema.
‘Mbona hujamuambia mama kuhusu hicho kijitabu cha huyo mdada,
kama kweli wewe ni mkweli…, au kuhusu huyo mdada aliyekuja kuchukua mizigo
yake, alikuambia nini..?’ akaniuliza.
‘Alinisimulia alivyopata taabu, akiwa humu ndani, mpaka
akaamua kuondoka…’nikasema
‘Hivyo tu…?’ akaniuliza
‘Ndio, na kwanini na wewe unayaingilia haya, au na wewe una
kitu kinakuhusu…?’ nikamuuliza
‘Mimi najaribu kukusaidia wewe, na kuisadia familia yangu,
siwezi kunyamaza kama kuna tatizo linaigusa familia yangu, hao ni wazazi wangu,
sitafurahi wakikosana, na mimi nimekuwa nikikusaidia hata wewe…tangia ufike
hapa,mengine ..ya..ya… kukuomba urafiki ni kawaida tu, …wala usije kunifikiria
vibaya…’akasema.
‘Ulisema utafanya juu chini mpaka unipate, nakumbuka sana
kauli yako hiyo, nakutilia mashaka na kauli hiyo…’nikasema
‘Unanitilia mashaka, kwa nini unitilie mashaka, …najua huyo
mdada kakuhadaa kwa maneno yake ya uwongo,….’akasema
‘Maneno gani ya uwongo….?’ Nikauliza.
‘Hayo, tuyaache kwasasa,… muhimu ni hali hii inayoendelea
hapa, ni bora uwe makini na unachokiongea, ukiongea jambo la kumfitinisha baba,
ukasababisha wao wakosane na mama. …sijui …na hata hivyo, huyo mdada alichokuambia,
mimi simuamini, ..kuna mambo yake mengi alikuwa kiyafanya, na sikuwahi
kuwaambia wazazi wangu, maana niliona hayana maana…’akasema
‘Kama mambo gani..?’ nikamuuliza.
‘Huyu mdada ni mshirikina..uwe makini sana na kauli zake,
ukimuendekeza atakuharibu, na ukiishirikiana naye, ….utakuja kuingia kusipofaa,
na mama atakugundua tu,………..’akasema.
‘Mimi sijui hayo, mimi nazungumzia hayo yanayotokea kwangu,
na ambayo kumbe yalitokea na kwake, kwanini yanitokee hivyo kila siku kukabwa,
kusumbuliwa, sipati usingizi….na yeye aliniambia hali ilikuw ahivyo hivyo, je
hayo ni mambo ya kishirikina…?’nikasema.
‘Mimi nikushauri jambo…’akasema na mara baba na mama
wakafika, na tukakatiza mazungumzo, na baba akasema;
‘Ni bora tukayaongelee chumba cha maongezi…sio huku
chumbani…’akasema baba na kuondoka na mama akaingia na kusema;
‘Haya, sasa jiandae uje kuna maongezi, nataka uje uelezee
kila kitu, ukinificha, basi shauri lako, ..yatakayokutokea usije
kunilaumu..mimi nawafahamu sana hawa wanaume, ..unanisikia, mimi nataka
nikusaidie wewe haya yasije kutokea tena…unanielewa…, kwahiyo sema kila kitu
kinachotokea humu ndani, na kama uliwahi kufanyiwa jambo lolote na mume wangu, uliongee,
huu ndio wakati wako…’akasema na kuondoka kumfuata mume wake.
Na kabla sijaondoka kijana akaja ka haraka, akionyesha kuwa ana jambo anataka kuniambia, lakini kabla hajaanza kuongea mara mzee mwenyewe akatokea, na kwa nyuma yake nikamuona mama akiwa kasimama,...
.
NB: Haya mambo ya familia hayo, ngoja tuone itakuwaje kwenye
hicho kikao cha familia.
WAZO LA LEO:
Matatizo yakitokea kukawa na msigishano, uwe wa wanandoa au uwe wa viongozi au
ujirani nk… hekima na busara ni kila mmoja kukubali kushuka, na kukubali kukaa
mezani na kuongea, ili muweze kujadili yale yenye sintofahamu. Kiubinadamu, tabia
hutofautiana, kutokana na hisia na utashi wa kufikiri, na usipokubali kuwa kuna
utofauti huo, utashindwa kushirikiana na mwenzako au kuvumiliana kwenye mambo
ya kila siku. Hala hala, ili kuondoka mgongano, jambo jema ni kukubali kukaa na
kuongea kwa kusikilizana, kila mmoja atoe duku duku lake, ili mwisho wake kuje
kupatikana suluhu..Suluhu hujengwa kwa maridhiano, sio ubabe
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment