KESI-HITIMISHO-2
Hakimu
aliwauliza hao watu wao ni akina nani..lakini watu hao walikuwa kama bubu,
hawakutaka hata kuongea neno moja na muheshimiwa hakimu akatoa amri kuwa watu
hao waondelewe hizo ngozi bandia walizojivika mwilini…, kama walivyoelezea
waendesha mashitaka, …na muda huo wakili upande wa utetezi, walibakia kimia, ni
nani atampinga hakimu..
Tuendelee
na kisa chetu…..
*******************
Wa
kwanza kufanyiwa utaratibu huo wa kuondolewa ngozi bandia alikuwa kiongozi…
‘Huyu
ndiye alikuwa mtendaji mkuu , kiongozi anayesimamia shughuli zote za kila siku
kwenye hilo kundi, lakini yeye sio kiongozi mkuu, kiongozi mkuu mtakuja kumuona
baadae, kitu cha kushangaza pamoja na ya kuwa huyu ndiye aliyekuwa anasimamia
shughuli za kila siku, lakini hata siku moja hakuwahi kuonekana ofisini mchana,
ni kwanini..
‘Hii
kwanini ndio iliyonifungulia njia ya kugundua mengi….
‘Wakati
naendelea na utafiti wangu, huku nikichunguza, ndio nikagundua kuwa huyu mtu
anafanya hivi kwa vile mchana anakuwa kwenye majukumu mengine, muhimu huenda ni
ya kiserikali zaidi, na kama ujuavyo, sio rahisi mkono mmoja ukaweza kufanya
shughuli mbili kwa wakati mmoja, …uwe sehemu hii na muda huo huo uonekane
sehemu nyingine.
‘Huyu
mtu atakuwa ni mtu anayefanya shughuli mahali fulani, na ni mtu maarufu sana,
kicheo na labda hata kihali za kimaisha,....nikajiuliza huyu mtu anaweza kuwa
nani…nilikuwa tayari na orodha ya watu ninaowashuku,…’akasema docta.
‘Kwahiyo
wewe umeshamfahamu kuwa huyu mtu ni nani…?’ muendesha mashitaka akamuuliza docta,
na docta akasema;
‘Kiukweli
bado sijawa na uhakika wa moja kwa moja, ngoja tuifanye hii kazi, ili kuupata
uthibitisho huo…’akasema docta akianza kualika, laptop yake ili ianze kufanya
kazi, na mara yule mtu aliyewekewa huo waya, ulioungana na laptop, akaanza
kufutuka, sehemu ya kichwa hadi mabegani, ….mpaka ikafika sehemu fulani,
ikatulia, na mara …ikafunuka taratibu kama mtu anayefungua zipu, ikufunguka
kitia sehemu ya karibu na sikio,..
Ilikuwa
ni kama unaangalia,katuni fulani inavyoweza kuondoa sehemu ya uso, kutoka sura
moja kwenda sura nyingin..na baadae, docta akasogea pale aliposimama huyu mtu,…na
kumalizia kazi iliyobakia kwa mkono, na sasa akatokea mtu mwingine tofauti na
sura ile ya awali…
Watu
wakashika mdomo, wengine wakapiga ukelele, wengine wakasimama..hata muheshimiwa
hakimu hakuamini, alijikuta akishika mdomo, akatikisa kichwa, akahema, na
baadae akageuka huku na kule akiwaangalia wenzake, waendesha mashitaka, kama
kuwauliza na nyie mumeona..akatikisa kichwa tena na tena!
‘Haiwezekani,
yaani ndio wewe…siwezi kuku-bali, siamini macho yangu, wenzangu mumeliona hili,
kiukweli…’hakimu aliishiwa hata na kauli.
Na
mara kutoka kwa watu waliofika humo ndani, kukatokea sauti, na vurumai kidogo,
na mtu mmoja alitokeza na sasa akawa anaelekea kumkabili huyo mtu, na walinzi
wakamuwahi kabla hajamkaribia…
‘Yaani
ni wewe , unatuhadaa kuwa …huku unanitesa mimi na familia yangu, siwezi
kukusamehe kabisa,…siwezi,…’huyo mtu akasema…watu wengi walioumizwa kwasababu
moja au nyingine walijawa na hasira zilizopitiliza, na kila mmoja alikuwa na
lake, ikawa ni zogo, hata hakimu hakutaka kuwatuliza kwa haraka, na mwingine
aliyeshindwa hata kujuzuia, akataka kwenda huko mbele alikuwa ni mpelelezi,
akiwa kavalia kiraia.
Ilibidi
polisi wafanye kazi ya ziada, kuwazuia watu, na kuwatuliza, ilishangaza, kwani
kwa muda wote huo hakimu alikuwa kimia, hakugonga rungu lake kuwatuliza watu.
Mwingine
aliyeonakana kutokuamini kabisa alikuwa msaidizi wa mkuu wa kituo, yeye kwa
muda huo alikuwa ndio kaingia..inaonekana awali hakuwepo, alikuwa kwenye
majukumu mengine, na sasa ndio alikuwa karudi, na kwa muda huo, alikuwa
anatafuta sehemu ya kukaa…na mara ndio akamuona huyo mtu,…na alipomuona huyo
mtu hakuamini..akashikwa na bumbuwazi…, akabakia amesimama, akawa kakodoa macho
tu haamini…..
‘Kiukweli,
sikudhania kabisa kama huyo mtu ni huyu muheshimiwa…kiukweli hakuwepo kabisa kwenye orodha za watu niliokuwa
nikiwashuku, nijuavyo, huyu mtu alisafiri nchi za nje, au sio....nilikuwa
namfikiria mtu mwingine kabisa..’akasema docta, na muendesha mashitaka,
akashika kichwa, na baadae hakimu akasema;
‘Haya
wewe,…ina maana wewe uliyepewa dhamana ya kusimamia mambo ya serikali, ulikuwa
una…aah, ….docta, ulijuaje haya..?’ hakimu akamgeukia docta, na docta akasema;
‘Muheshimiwa
hakimu,..hii ni kazi ya muda mrefu sana, ..lakini mungu ndiye aliyetuongoza
hadi kufika hapa tulipofikia, sio kazi
rahisi kama watu watakavyofikira, ni kazi ngumu ya kuumiza kichwa na
kujitoa mhanga, na kiukweli sio kwa ujanja wetu, ni mungu peke yake
aliyetuongoza na kutulinda, hadi siri hii kubwa ikafichuka…’akasema docta,
na muheshimiwa hakimu akamgeukia tena
huyo mshitakiwa namba mbili, na kuumuuliza;
‘Haya
wewe…sasa utajibu maswali yangu, maana sasa upo chini ya jamuhuri, nataka
unijibu swali langu, nililokuuliza awali wewe ni nani…?’
Mshitakiwa
huyu, akainua kichwa, maana muda wote alikuwa kainamisha kichwa kwa aibu, au
kwa kuogopa watu wasimuangalie,..lakini sasa akainua kichwa na kuwakabili
wanachi…akataja jina lake kwa marefu yake.
watu wakacheka waliocheka, wakaguna walioguna,wakazomea walizomea….na
walipotulia muheshimiwa hakimu akamuuliza swali jingine.
‘Kazi
yako..?’ akaulizwa nay eye bila kusita akaitaja,
‘Mkuu
wa kituo …’akasema, na aliptaja hivi watu sasa wakamzomea, na hapo hakimu
akagonga rungu lake , na kusema watu wanyamaze, kwani sasa yupo kazini,
alishawapa muda wa kutoa hasira zao moyoni, sasa sheria inataka ifanye kazi.
‘Wewe
kazi yako ni Mkuu wa kituo, … mkuu uliyepewa dhamana kubwa ya kusimamia usalama
wa kituo, umakuwa msaliti wa nchi yako na raia wako, umetutia doa sisi
tuliopewa dhamana kama hiyo, inasikitisha sana, ni kwanini, …?’ akauliza hakimu na kabla hajajibiwa mara
kukatokea ghasia ..na hakimu akainua rungu lake akitaka kuligonga, lakini
akakatisha.
Mama
mmoja alishajitoa mikononi mwa polisi na alikuwa sasa keshafika sehemu ya
mbele, huku kashika kichwa, polisi wakamfuata, lakini hakimu akawazuia, na kusema;
‘Wewe
mama una shida gani..?’ akaulizwa
‘Nilikuja
kuthibitisha,….maana huyu mtu nilijua ni kaka yangu aliyepotea, nilijua ndio
yeye anatutesa mimi na familia yangu…, kumbe sio yeye,..ina maana awali huyu
mtu alivalia sura ya ndugu yangu, na sasa akavalia sura ya mtu mwingine, kumbe
wewe sio ndugu yangu, ndugu yangu, kanipigia simu sasa hivi…yupo huko alipo
anaumwa, alipotea watu wakajua kafariki, sasa kaonekana akiwa na hli mbaya sana…na
nimemuona kwenye simu mbashara, ulimfanya nini ndugu yangu…’akasema huyo mama.
‘Kwahiyo
huyu sio ndugu yako, wewe si ulisema awali kuwa huyu huenda akawa ndio ndugu
yako, aliyepotea..?’ kaulizwa na muendesha mashitaka..
‘Huyu
sio ndugu yangu kabisa,…’akasema huyo mama.
‘Ndugu
yangu ni huyu hapa,….’akaonyesha picha kwenye simu yake.
‘Wewe ehe, …hebu tuambie hiyo yote ni kazi
yenu, ni kwanini ulifanya hivyo..?’ akaulizwa;
Wakati
huo mshitakiwa namba moja alikuwa kakaa kwenye kitu, katulia, kaegemea
kiti,…akiangalia juu…na watu wengi wakawa sasa wanamuwazia yeye, atakuwa ni
nani…na huyu mshitakiwa namba mbili akaanza kujielezea..
**************
‘ Ndugu muheshimiwa hakimu, wengi wataniona mimi ni mnyama, au
mimi ni shetani, kama wengi walivyosikika wakisema,..yote ni sawa kwa uoni wao,
lakini hakuna anayejiuliza ni kwanini mpaka mtu ufikie hatua hiyo,…hilo kwasasa
hakuna anayejaribu kurejesha akili yake nyuma, akajiuliza…’akasema.
‘Kwanini sasa ukafanya hayo uliyoyafanya,…?’ akaulizwa.
‘Nitasema kila kitu, msiwe na shaka,..najua mwisho wa haya
yote umefika, lakini nafahamu haya nitakayoyaongea yanahitajika kusikiwa na
kila mtu, ili ukweli uwe bayana, kuwa mtu sio mnyama, unyama unakuja baada ya
kutendwa, hasa kama tulivyotendwa sisi,….’akatulia.
‘Huyo mwanamke hapo mbele ni ndugu yangu..kwa vipi, hajui….’akasema na huyo
mwanamke akasema;
‘Wewe sio ndugu yangu sikujui kabisa….’akasema.
‘Hutaweza kunijua,…lakini yoyote anaweza kuwa ndugu ya
yoyote , sisi sote ni watoto wa adamu, na hawa, basi hiyo haitoshio kuwa sisi
ni ndugu, sawa, kwa vile sisi hatukuwa na baba, basi hatuna ndugu, baba yetu
alitukana, basi wewe hutoshi kuwa ndugu yangu, hunionei huruma, nisiye na baba,
...najua hutapenda kuwa na ukaribu na sisi, ndio maana tukatumia ndugu yako
uliyemfahamu,…’akasema na watu hapo wakatulia, na kutega sikio.
‘Sikulaumu kamwe, maana nyie mlikuwa watoto wa geti kali,
lakini sisi tulikuwa machokoraa, omba omba..tulikosa nini….hayo ni maelezo ya
awali tu, ya kukufunulia akili yako ujue sisi tumetokea wapi, na kwanini tukawa
hivyo,..sasa hebu sikia chimbuko la sisi, ombaomba, chokoraa..watoto wa haramu,
tulipatikanaje, unalijua hilo, sasa leo utalijua…’akatulia.
‘Kiukweli mimi sio huyo ndugu yako aliyepotea, tulifikia
hatua ya kulitumia jina lake na sura yake kwasababu ya kukamilisha haya…najua
wewe unayemfahamu ni huyo ndugu yako na ndugu zako wengine, ...wewe uliyeolewa
na mwanamume tajiri, aliyekuwa askari, mtoto wa askari…na kwa cha baba yake
mumeo, aliwahi hata kunifunga mimi, nikiwa mdogo tu, hakutaka hata
kunisikiliza…
‘Sawa hauna makosa, sawa, hata mume wako hana makosa, makosa
anayo, huyo aliyesabibisha mimba ikatunga tumboni kwa mama yangu….huyo ndiye
chanzo cha haya yote…’akasema
‘Sasa fungueni masikio, nieleze ni kwanini tulifikia kuayafanya haya yote,..
kabla ya kujibu hilo swali, niwakumbushe kitu kidogo,…’akawageukia wazee
waliokuwa wamekaa mbele kama wazee Mahakama, kuna wawili walikuwa wazee kweli
‘Samahanini wazee waheshimiwa, nashukuru, mpo kwenye
mahakama hii, maana wazee, wa mahakama, siku hizi ni vijana tu, ila hapa mpo
nyie ambao mtakuwa shahidi wangu, je mnakumbuka kipindi fulani nyuma,
alipatikana mama mmoja aliyekufa peke yake kwenye nyumba, iliyokuwa imeezekwa
kwa makuti, nyumba ya udongo…?’ akauliza.
Wale wazee wawili wakasema wanakumbuka..
‘Safi kabisa….Nyumba hiyo ilikuwa imejengwa hapo walipojenga
huyo mnayemuita mzee , ambaye mabinti zake wamejikuta kwenye mkasa huu,…mzee
ambaye ndiye mume wa huyu mama, ..mzee ambaye ndiye alinunua eneo hilo kutoka
kwa ndugu wa mke wake. Je ni kweli huyo ndugu alilipata eneo hilo kihalali…hakuna
anayelijua hilo!
Nawakumbusha kuwa eneo hilo ilikuwa mali halali ya mama yangu, eneo la urithi
kutoka kwa wazazi wake, ..lakini alikufa bila kulifaidi, alikufa ndani ya banda
bovu, akiwa peke yake, huku mwanaume aliyempa mimba, tena kwa kumbaka akiwa tajiri,
akiwa anakula raha na wanawake wake wa ndoa…hataki hata kumsikia.
Mnafahamu mama yangu alikuwaje,…nyie wazee, waheshimiwa huyo
mama aliyekufa kwenye hilo banda alikuwaje, kihali yake,..mnajua sana…, ila
hamjui kuwa huyo mama ndiye alikuwa mama yetu…’akatulia
‘Na wengine hapo wapo, wanafahamu kabisa ni kitu gani kilitokea
kwa huyo mama, lakini ni nani atafungua mdomo wake, wakati ilipigwa marufuku
kuliongelea hilo, eti mnamkashifu muheshimiwa, eti anasingiziwa, na
atakayeongea ataishia jela kama huyo bibi,..nani alimjali huyo bibi
alipofungwa, ni nani..,..alijitokeza kumtetea, ni nani, nani atamtetea, bibi
mchawi..si ndivyo mlivyodanganywa..!
‘Nilishalia sana,..siku nasimuliwa maisha ya mama yangu na
bibi yake…, nililia sana…sikuamini,..na nilipothibitisha hayo kuwa ni kweli,,..nikaapa
kuwa sitalia tena…kilio changu kitakuwa kulipiza kisasi, ndio maana nilijiunga
na kazi ambayo itanijenga ujasiri…
‘Unajua kwa historia yangu nisingeliweza kujiunga
huko,…historia ya uchokoraa, mtukutu, mwizi…lakini niliweza kusoma na kujiunga
na jeshi, askari polisi..ni nani aliyenisaidia hadi kufika huko…mimi nadiriki
kusema ni mizimu ya mama yangu…’akatulia.
‘Na kweli nikiwa huko, niliweza kusahau ya nyuma, nikawekeza
akili yangu kwenye taaluma hiyo,lakini kwa siri, nilikuwa na ajenda,…na
hutaamini kila nikipata kazi ngumu ya kufanya namkumbuka mama yangu,
nilivyosimuliwa,,..napambana na hilo tukio , kama ni kazi ngumu kama ni
zoezi,..nalifanya hilo jambo, kama vile napambana na huyo aliyemfanyia hivyo
mama yangu…’akatulia
‘Najua hata nikilia sasa,… ni nani atanisikiliza…watu
huangalia mwisho wa jambo, hawapendi kuangalia chimbuko lake..mwisho huwa mtamu
au mchungu kuliko mwanzo wake,…, ndivyo ilivyokuwa hivyo, hata pale mama wa
mama yangu alipokwenda kushitaki,ni nani angelimsikiliza, alionekana muongo,
mchochezi…’akatulia akimuangalia hakimu.
‘Hakuna haki kwenye hii dunia kwa mnyonge..’akasema
akimuangalia hakimu.
‘Muheshimiwa hakimu labda ilikuwa enzi hiyo, utasema
hivyo,.. mnatetea, haki za kila mtu utasema hivyo..lakini kwangu mimi,
niliposikia yaliyompata mama, yaliyotupata sisi, nasema ..sio kweli, nyie watu, anaposhitakiwa mnyonge ndio mnajifanya mnajua
sheria, lakini akishitakiwa tajiri, kiongozi mwenye heshima, mnajifanya kuwa na
makengeza..ndivyo ilivyotokea kwa mama yangu.
‘MAMA YANGU, ALIBAKWA, na tena alikuwa ni kiwete, mama yake alikuwa
mzee, masikini hana mbele wala nyuma,..kaenda kushitaki, anaishia kufungwa…
‘Niliapa kuwa ni lazima nitalipiza kisasi,..sitajutia kwa
hilo kamwe,..najua mtanifunga, mtaniua, sawa…lakini afadhali kidogo, afadhali
kidogo, angalau nimeweza kutimiza nadhiri yangu…’akasema kwa akitikisa kichwa.
Sasa sikilizeni kumuhusu huyo mama ..aliyekuwa mlemavu wa
miguu, ila mzuri wa sura, …’akasema akitabasamu kidogo,
‘Ni mnzuri wa sura, ukiangalia usoni…anafanana, na haha, ndio maana tulikuja na wazo hilo ka
kutumia sura yake, kama…’mpenzi wa facebook’…hahaha, ‘hapo akacheka,
‘Ni nani angeliiona hiyo sura yake ya uso, akaacha kuvutika
naye, sura hiyo nikaitumia kama ulimbo kuwanasa maadui zangu..wale wote
wanaostahiki kuingia kwenye mtego wa kulipiziwa kisasi wakaingia ndani…
‘Sasa ngoja niwasimulie yaliyomkuta mama yangu na hadi sisi
tukazaliwa, naomba mnivumilie…nitachukua muda wenu, lakini masimulizi haya
yataaidia kurahisha kesi yenu hii, na mkiondoka hapa mtajua ni kwanini haya
yote yalitokea, tofauti na uvumi, na mengi yaliyowahi kusimuliwa huko, hayo
yaliyosimuliwa, ilikuwa ni propaganda, tuliyoiunda, na kweli ikanasa..
Nijua mimi sina haki tena..kama alivyoikosa haki bibi yangu
na mama yangu, ..lakini haya nataka kila mtu ayasikie, na hata hapo, pumzi
yangu ikikatika nijue kila mtu ni shahidi ya haya, mnawaona mayatima ,
chokoraa, mnawapuuza, wengine hamjui wametoka wapi, wengine walikuwa ha haki ya
majumba na mgorofa yanaoota kama uyoga, ni nani atalijua hilo…’akatulia.
‘Mama yangu alipewa mimba kwa kubakwa,..waheshimiwa wazee
mliambiwa atakayeongea huo uwongo, maana uligeuzwa na kuitwa uwongo, atafungwa,
kweli si kweli..sitaki mnijibu msije kufungwa,..ila moyoni mnalifahamu hilo, ni
nini kilitokea kwa mama yangu,mama ambaye alikuwa hajiwezi, miguu imepooza, ..sawa
si sawa…’akawa kama anauliza.
‘ Mama yangu alikuwa kapooza miguu yote miwili anatembea kwa
kujiburuza..ikatokea siku jamaa mmoja muheshimiwa, akapita sehemu ambapo mama
hufanya kazi ya kuomba omba, tamaa bwana,..jamaa huyo akavutika na sura ya
binti huyo, maana mama muda huo ni binti, na jamaa huyo …tamaa zake za kupenda
wanawke wazuri, zikamvuta..akashindwa kulala
‘Haya naongea yalitokea, sio uzushi, kama nazua, waulizeni
hao wazee…jamaa hakuweza kulala, au kutimiza majukumu yake akiikumbuka sura ya
mama yangu..
‘Siku moja akashindwa kuvumilia, akafunga safari kwa siri
hadi nyumbani kwa mama yangu , wakati huo bibi hayupo kaenda shambani,..alipofika
hapo akiwa na zawadi, akamataka mama kimapenzi,..sio kumuoa, anamtaka mama kimapenzi..ni
nani angemuoa kiwete…’akatulia.
Mama kalelewa, japokuwa ni masikini, lakini yeye alikuwa
anajali utu wake, heshima yake, mama alikataa, akimuambia, yeye hawezi kuzalilishwa,
hata akipewa pesa zinazojaa hii dunia,..alijua huyo jamaa nia yake ni kumzalilisha
tu, hataweza kumuoa..ana mke wake mnzuri, japokuwa sura yake haimfikii hata
nusu ya sura aliyokuwa nayo mama yangu, …huyo jamaa ana wake wengine wa nje,
lakini atawezaje kumfanya huyu awe mke wake wa nje, wakati huyo mama kalemaa
miguu…masikini, hajasoma…
‘Jamaa huyo, kwa vile kipindi hicho alikuwa na mamlaka, hajawahi kukataliwa,
akiwataka wanawake,wanajipeleka wenyewe… akaamua kutumia nguvu, akambaka mama
yangu…, mama ambaye, alipooza miguu, mama ambaye ni masikini asiyeweza
kujitetea...'jamaa akatikisa kichwa, alijizuia kutoa machozi, lakini yalimlenga
lenga….
‘Jamaa alipomaliza shughuli yake akamtupia mama pesa, na hizo mama hakuwahi
kuzitumia,….alizichoma moto..lakini mama aliachiwa kitu kingine, uja uzito,
...ujauzito uliomtesa mama, hadi tunazaliwa sisi, ni kwanini mama aliteseka na
huo ujazito, musikie sasa nyie wazee, maliojua siri hiyo mkabakia
kimia…’akasema.
‘Jamaa huyo si alitumia nguvu, tendo hilo la kutumia nguvu, lilimpa mama jeraha
kubwa jeraha ambalo halikuweza kupona,
kwa vile mama alikuwa akijiburuza kwa kuegeme upande mmoja ambao ndio huo
ulikuwa na jeraha..jeraha likawa linafumuka kila akitaka kutembea..huwezi
kuijua hiyo hali mpaka ikukute..’akatulia.
Jereha hilo likaja kutengeza usaha,, likaoza..atajitibiaje, akinda
hospitalini..anaona aibu, ni sehemu ya siri…akawa anatumia dawa za kienyeji,
hadi alipozidiwa sana, ndio ikabidi ajitokeze kwa dakitari, muda huo donda
limekuwa donda ndugu....nataka mlielewe hili, japokuwa mimi na ndugu yangu
hatukupenda kuliongelea hili, tulipanga,tulipize kisasi kimia kimia, na mambo
yaishe kama yalivyo…lakini muda umefika jamii mlisikie hili, na hata
tukinyongwa mjue tulifanya hivyo,kwasababu gani..
.
Mama akabeba mimba kwa shida…bibi ndiye anahangaika, ..alijitahidi awali
kumgundua ni nani kamfanyia hivyo binti yake alipogundua kuwa ni muheshimiwa
akamuendea,…hahaha, siku hiyo alisitiriwa, akapewa vijisenti, ili eti azibe
mdomo wake.
Baadae akafuatwa na walinzi, akaambiwa asije kuonekana tena
eneo hilo la muheshimiwa,…akawauliza kwanini, hiyo ni damu yake, yeye ndiye
aliyesababisha hayo, kampa binti yake mimba, bibi akajitetea hivyo,…..alipotamka
hivyo, ukazushiwa uvumi,…
Alizushiwa uvumi, ulioenea kama vumbi jangwani, …eti huyo
bibi ni mchawi, huyo bibi anataka kumloga muheshimiwa..ok,..huyo bibi
walimzuishia uchawi …ndivyo walivyosingizia huyo bibi, ….kwa vile walimzushia
huyo bibi wakati kweli hakuwa mchawi, sisi ndio tukajiwa na wazo hilo,..kama
yeye alizushiwa, basi katika sehemu yetu ya kulipiza kisasi, sisi tuwe ni
wachawi wa kiukweli..bibi au mama hawakuwa machawi kabisa,..wala hawajui hata
dawa za kienyeji, zinatengezwaje.. lakini sisi ndio tukaamua kuwa
wachawi…’akatulia akijaribu kutabasamu.
‘Uchawi wetu ni wa kusomea…sio wa kurithi…kama alivyo kua
yule mzee kigagula…’akasema hivyo.
Mpaka mama anafikia
hatua ya kujifungua, lile donda, lilikuwa sehemu ya siri, limekuwa kubwa, na
likawa linamtafuna, si unajua tena, kidonda kisichopona,…kwa jina jingine
kansa…mnasikia, mama alikuwa na kansa…ndio aliyomtesa mama, ni kansa
iliyotokana na kubakwa na huyo jamaa…
Siku mama anajifungua, ndio kipindi kidonda kimekuwa ni
tatizo, kinamuuma kweli kweli,..hadi uchungu unamshika, akajua hatapona, unajua
alichowaambia madocta, hasa yule mama aliyemsaidia kujifungua, ..hao madocta
mkitaka waiteni wawathibitishie hili…wapo, hadi leo…
‘Mama yangu alisema hivi;-
'Nataka muhakikishe, ninazaa hao watoto mapacha,…maana aliambiwa watoto ni
mapacha, nataka, watoto waje kulipiza kisasi, maana mimi ni mnyonge, mimi ni
kilema, mimi sina ndugu, ndugu yangu ni bibi yangu ambaye hajiwezi,…wamemfunga,
ili kum-maliza asije kutoa hii siri…, sasa watoto hao mje kuwaambia siri hii,
..akawasimulia yote ilivyotokea, na huyo mama akawa kaandika kwenye karatasi,
yote aliyosimuliwa, karatasi hiyo ipo, hadi leo…’akatulia.
‘Ninajua mama yangu,akisikia mimi nimekufa, na yeye hataishi
tena, hao watoto wapeni wenye uwezo wa walee, na wakiwa wakubwa wasimulieni huo
ukweli wote…’ ndivyo mama alisema, akiwasimulia hao manesi na madocta
walishughulikia, kuhakikisha sisi tunazaliwa salama...
‘Najua wengine watasema huenda ni uwongo ulizushwa, wengine
watasema tuna uhakika gani, waulizeni wazee waliowahi kuitambua hiyo familia, kama
wanamuogopa mungu, watayakinisha haya maneno yangu, kawaulizeni hao madocta, na
huyo mama ambaye alikuwa mkunga, kipindi hicho, sasa hivi ni mama mzee..’akatulia
akiwaangalia wale wazee.
‘Kama nyie wazee mnaifahamu hiyo familia,..kama haya
ninayoongea sio kweli, basi,, simameni mkanushe, kuwa nazua uwongo…’akatulia
akiwaangalia hao wazee, na hakuna aliyesimama
‘Mama alijifungua kwa shida sana, ingelikuwa ni ….angelifanyiwa upasuaji, sasa
mtu hana pesa…basi tena, akajifungua kwa njia ya kawaida,… akiugulia maumivu
makali, mungu mwenyewe ndiye anajua ulikuwa uchungu wa kiasi gani…pimeni,
fikirieni, wazeni, aina gani ya maumivu aliyokutana nayo mama..
************
Sisi tulizaliwa mapacha, mimi na ndugu yangu..siwezi kumtaja
huyo ndugu yangu,. na kwa vile ilishagundulikana kuwa mama hatapona, sisi
wawili tuligawiwa kwa wasamaria wema…tukiwa vichanga tu…’akatulia
‘Na hata hao waliotuchukua, walikuja kutushindwa, kwani
walikuja kuwa na familia zao, wakawa hawana uwezo, tukatupwa mitaani, tukawa
chokoraa…mnajua maisha hayo yapoje, siwezi kuwasimulia, hayo maisha yalikuwaje,
maana ni hadithi ndefu ya kusikitisha....ninachotaka ni kusimulia kilichotokea
kwa mama, ambacho ndicho kilituvuta mimi nije kulipiza kisasi…
Nasikia mama hakuweza kumaliza mwezi akafariki, na bibi ambaye ndiye mlezi
wake, aliposikia kuwa mjukuu wake kafariki na yeye hapo hapo akafiriki akiwa
gerezani, hebu fikirieni, nyie watu mnaojifanya ni malaika, maana sisi ni
mashetani, nyie ni nani ni malaika, si ndio, huyo bibi alifungwa kwa kosa
gani,..…’akawageukia wazee, halafu watu, watu walikuwa kimia.
Mama alifariki akiwa peke yake kwenye hilo banda la matope, lililoezekwa kwa
makuti, kama wapo wazee wa siku nyingi waulizeni…walifanya nini kumsaidia huyo mama,
mama anaumwa, hajiwezi, anaishia kula wadudu..acheni tu….’hapo akashindwa
kuvumilia na kulia.
Nawauliza wazee ni nani aliyasababisha yote
haya…nijibuni….’akawageukia hao wazee, na hakuna mzee aliyesema kitu.
‘Najua hamtasema kwa sababu mnaogopa kufungwa, kama
alivyofungwa bibi, si ndio hivyo, lakini mungu anawaona…..’akatulia
Akamgeukia huyo mama aliyekuwa kasimama hatua chache, mbele
ya watu waliokuwemo humo, …
‘Sasa nikuulize wewe unyejifanya kuwa sio ndugu yangu,
unamfahamu huyo aliyembebesha mama yangu huo uja uzito, …najua, lakini sina
uhakika, uliwahi kusimulia na bibi yako wakati anataka kukubadhi mkoba,..
‘Hapo utajifanya hukumbuki, na je, kuna tukio lilitokea,..nikiwa
mdogo chokoraa, niliwahi kukuibia, wewe ulikuwa mtoto,..mimi kijana kijana …nikaja
kufungwa jela ya watoto, kisa nimekuibia wewe mtoto wa muheshimiwa,..kipindi
hicho sijajua wewe ni nani, na mimi nimetokea wapi, nilikuambiaje,..ipo siku
nitajua ukweli wa wazazi wangu, na nitakuja kulipiza kisasi, niliongea tu, wala
sijaujua huo ukweli…nilifungwa jela ya watoto,
Nashukuru sana nikiwa jela ya watoto ndio nikaanza kujifunza
maisha, na nilipotoka hapo ndio, nikaanza kujitambua, nikasoma..na hapo ndio
ikaja wazo la kutafuta ukweli , mimi ni nani, na kwanini ilitokea nikawa hivyo,
sina baba , wala mama, wala ndugu yoyote…nitawasimulia hilo…
.
‘Sasa nakuuliza wewe mwanamke, je unajua ni nani,..aliyembaka
mama yangu, akasababisha hilo jeraha…nijibu wewe mwenyewe kwa kinywa chako ili
niweze kuendeela na maelezo mengine…’akamuangalia huyo mama, lakini huyo mama
alibakia kimia.
‘Ninajau mna hamu ya kufahamu kwa jinsi tulivyoweza
kubadilika, na kufanya tuliyoyafanya tuliwezaje, na tulifanyaje, hayo
nitayaeleza yote kila mtu afahamu, hadi akatokea binti mrembo wa facebook,…huyo
alikuwa ni nani, tulimtengezaje,…nitawasimulia, lakini kwanza nataka huyu
mwanamke anijibu je anafahamu huo ukweli, je ni nani alimbaka huyo mama
aliyefia kwenye hilo banda peke yake,,…’akamuangalia huyo mama, akisubiria
jibu, mahakama ilikuwa kimiaa.
NB: Kidole kinauma, tutaendelea sehemu ijayo
WAZO LA LEO: Binadamu ana utu wake, kama mwana-adamu..ila madhila yakiwa
mengi, dhuluma zikazidi,..kukawa na kuteseka kwingi, hali hiyo, humfanya
binadamu akageuka kuwa mnyama..na ndio maana viongozi wanatakiwa kusimamia
kwenye haki na ukweli, wakahakikisha kuwa mnyonge hadhulimiwi na mwenye nacho, …Tumuombe
mungu atujalie, tuwe waadilifu, wachamungu, na tunaotenda haki na yaliyohaki,
na tuwe na viongozi waadilifu, ili tuwe
na maisha mema hapa duniani na kesho ahera.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment