Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, May 17, 2017

MPENZI WA FACEBOOK-29



‘Mkuu,… msaidizi wangu ananihitajia sana….’akasema docta.

‘Msaidizi wako bado yupo ICU...'akajibiwa

‘Una uhakika na hilo..?’ akauliza docta.

‘Kwanini unasema hivyo..?’ akauliza mkuu 

Mkuu alipopiga simu kwa watu wake huko hospitalini, akaambiwa ndio na wao walikuwa wanataka kumpigia baada ya kutafuta kila kona, ..msaidizi wa docta hajulikani wapi alipo, na wana uhakika asingeliweza kutoka, kwanza alikuwa hajaweza hata kutembea...pili ulinzi, na hadi kutoka nje, kuna sehemu mbali mbali angelipita, sasa alipitaje, wao wanahisi bado yupo humo ndani...

Mpelelezi, akamuangalia docta kwa macho ya kuuliza, akiwa kajaa hasira, hakuweza hata kuongea na mtu wake huyo akatoka nje kwa haraka na kuelekea ofisini kwake,

Mpelelezi, hakuamini..mpaka alipowapigia watu...

Tuendelee na kisa chetu..

*************

Mpelelezi alipoona bosi wake katoka akiwa kabadilika akajua kuna jambo limetokea , na kwa jinsi amjuavyo bosi wake, basi siku hiyo iakuwa ngumu sana, na huenda kukatokea tamko kali baadae…na yeye bila kuongea kiti na docta , kwa haraka akatoka nje kama vile anamfuata huyo bosi wake, lakini alipofika nje, akasimama na kuanza kuwasiliana na watu wake;

‘Vipi imekuwaje..?’ akauliza, na kusikiliza kwa makini baadae akasema;

‘Mtafuteni haraka, haiwezekani, ina maana alipitia wapi,…kabisa hamkumuona akitoka, haiwezekani,.. au ni ujanja wa hawa watu wamemuhamisha kwa….ngoja nitaona…’akasema na baadae alipomaliza kuongea na watu wake akarudi kwa docta.

‘Haya docta mpiga ramli, hebu tuambie msaidizi wako yupo wapi…?’ akauliza

‘Hata kama ningelijua wapi alipo, nisingelikuambia,..lakini sijui wapi alipo na hilo linanipa mashaka makubwa sana, najua ni watu wenu wanafanya hivyo…’akasema docta.

‘Watu wangu wetu kwa vipi, …nimeongea nao na wao wanashangaa kwa jinsi gani alivyoweza kutoka bila kujulikana,…haiji akilini…’akasema mpelelezi.

‘Ndio sasa mjue kuwa mnachocheza nacho sio jambo rahisi kama mnavyodhania, nazidi kukusihi ndug yangu…., jirudi…, hao watu sio wema, huko ulipoingia ni kubaya sana, nakujua na najua hatari zake..’akasema docta.

‘Docta, nakuelewa sana,… lakini hata ramli wakati mwingine zinakosea, na hiyo uliyopiga dhidi yangu umekosea sana…, sivyo hivyo unavyonifikiria mimi ,wewe, kuwa ndivyo nilivyo, kamwe siwezi kuisaliti nchi yangu na watu wangu, kamwe, lakini hutaweza kunielewa…’akasema mpelelezi.

‘Lakini binti yako alikuwa na matatizo kweli si kweli…?’akauliza na mpelelezi akageuka upande mwingine akawa kama nataka kuondoka halafu akasema;

‘Ndio hilo nalikubali sana..binti yangu alikuwa na matatizo, ,..lakini mmh, mbona wapo wengi wana matatizo kama hayo, utasema na wao wanajihusisha na makundi hayo haramu…’akasema kama anauliza sasa akiwa amempa mgongo docta.

‘Naju mlihangaika sana,…mpaka mkakutana na jamaa fulani,..na mipangpo tu ilipangwa iwe hivyo,…huyo jamaa ndio akakushauri jambo,.. ukamwambia, upo tayari kwa lolote lile..sawa ni sawa..?’ akauliza

‘Sasa ukiwa unaguliwa, na mtoto wako akaja mtu akakushauri dawa..utasemaje, pesa ni nini bwana..siwezi kusema nina uwezo, lakini …nilimuambia hivyo nikiwa na maana nitajitahidi niwezavyo…’akasema

‘Sawa, nataka kuhakiki jambo tu…maana sio mimi, ..lakini mimi kama docta nataka kuhakiki kila kitu, ..je alikuuliza nini, baadae, ..si alisema,…una uhakika, upo tayari,..?’ akauliza.

‘Mhh..yah, alisema hivyo, nikajua kuwa anataka kuhakikisha kuwa nipo tayari hata kwa kutibiwa kienyeji, ….’akasema docta

‘Na wewe ukamjibuje…?’ akauliza

‘Nilimuambia …ndio…ningesemaje hapo…’akasema

‘Ndio hapo akakuelekeza wapi uende,…na ukaenda na huko, ukaelekezwa madawa na kwenda makaburini,..sijui tambiko ..nini na nini, au sio… ukafanya hivyo, au sio, ..nijibu ili niwe na uhakika…?’ akasema docta.

‘Ndio nilifanya hivyo…’akasema mpelelezi, sasa akimgeukia docta.

‘Na kweli ulipofanya hivyo, mtoto wenu akapona,…na wewe na mkeo mkafurahi sana, hata mlitaka kufanya sherehe na mlipokwenda kwa jamaa kumualika akawaambia msifanye hivyo…’akaambiwa.

‘Oh…docta..umejuaje…’akasma

‘Ila ukapewa masharti ya kutoa makafara la damu..kwanini damu, na tena damu ya mtu, unakumbuka…?’ akaulizwa na hapo mpelelezi akageuka kumpa mgongo docta.

‘Docta, …kuna mengine siwezi kukujibu, nielewe tu…’akasema

‘Nakueleze hilo, ili uone wapi walipokutegea, na iwe fundishi, kwanini kafara , kwanini damu, kwanini..makaburini, kwanini..huyo ni shetani anawachezea, ungelikuwa na imani ya dini, ungejua jinis gani ya kujilinda…’akasema docta.

‘Wewe hujapata matatizo ambayo yanakugusa sehemu ambayo huwezi ku…huku mtoto, huku mke hakuelewi,..unajua, we acha tu,…’akasema

‘Swali je ulikubali kuyafanya hayoo..?’ akauliza

‘Hivi..unaelewa jibu lake docta…’akasema

‘Jibi ni kuwa ulikubali, kumbuka ulishasema upo tayari kwa lolote lile,kwao kauli hutunzwa, kama ushahidi,..kwahiyo …ukakubali, jibu ni ndio..’akasema docta.

‘Ningefanyaje…’akasema mpelelezi.

‘Ndio tatizo lilianzia hapo…’akasema docta.
‘Docta tatizo halikuanzia hapo…lilianzia kipindi mtoto wangu alipoanza kuumwa, ukisema lilianzia hapo unakosea…’akasema

‘Nina maana kuwa tatizo la wewe kuingia kwenye mtego wao …mtoto angelipona, kwa njia za halali tu..sema ndio hukuelewa, hukumuweka mungu mbele, elimu ya dini kwenu ni shida…mbona mimi nilishapata matatizo , nilikuwa nimechanganyikiwa kabisa, ..naokota makopo..unajua…lakini imani ya dini, mitihani hii hukufika ili kujaribiwa,…’akasema docta.

‘Sawa bwana…’akasema mpelelezi.

‘Hawa watu walikuwa wanakutafuta, ulipohamia eneo hili wakagundua nyota yako ni kali sana…wakaanza kukutengenezea mitihani,..na wewe, najua…ukaingia kwenye anga zao,…siku moja akakujia jamaa mwingine lakini hao hao, kwa shauri la kutafuta kipato,…’akasema

‘Docta hayo mengine ya nini,achana nayo…’akasema

‘Sio mengine ni hao hao…walishaanza kukuharibu akili wewe hujui tu…’akasema docta.

‘Hapana akili yangu inafanya kazi, najua mitihani hiyo ilinipeleka kubaya, lakini sikuwahi kuokota makopo…’akasema.

‘Huyo jamaa alikuja kwako wakati huo huna mbele wala nyuma,, umekopa pesa ofisini, unadaiwa, ulikuwa na pesa ya kikundi ya mkeo mkaitumia, …nyuma ina deni..huku mtoto bado anahitajia dawa…anasoma, huna pesa, ulifanya nini hapo, na ukumbuke akili yako ilishachezewa…’akasema docta.

‘Mhh…kweli wewe unajua kupiga ramli…’akasema mpelelezi sasa akionyesha kuwa huru kuongea.

‘Ukakubali na mikakati yake ya kuingiza kipato, maana hukuwa na jinsi,..ni mbinu zao hizo, kama sio kwenye kukutegea ugonjwa, watakuingiza kwenye umasikini uliokithiri, madeni.., yeye akakupigia mahesabu ukakubali ..lakini ukiwa na mashaka,.’akaambiwa.
‘Ok,…’akasema hivyo tu.
‘Na ghafla mtoto akaanza kuumwa tena, na mtoto na unakumbuka mtoto alidai nini ili apone….’akasema docta

‘We acha tu…’akasema hivyo.

‘Akawa anahitajia vitu vya thamani sana…unakumbuka,..kesho yake ukakutana na jamaa akakuuliza una tatizo gani, ikabidi umwambia ndio akakukumbushia yale mliyoongea ya kuongeza kipato..ukaona huna jinsi..ukakubali, ukaingia kwenye mradi..sawa si sawa…’akasema na mpelelezi akabakia ameduwaa.

‘Lakini msharti baba..ukaambiwa nini ..kafara, sasa kubwa zaidi…ulifanyaje, hapo utajaza mwenyewe,…’akasema docta.

‘What…docta umejua…aje hayo, …docta sikutanii, sasa upo chini ya ulinzi, sasa nakubali kabisa kuwa wewe umetumwa…sasa sikiliza binti yangu akiumwa tena, ama zako ama zangu…nimechoka nimechoka, unajua kiasi gani napata taabu…’akasema sasa akionyesha kuchanganyikiwa, achue hatua kama anavyotaka au akubaliane na docta.

‘Afande..fanya kazi yako….kama nipo chini ya ulinzi au…unisikilize…’akasema docta. Na mpelelezi akawa sasa kashika kichwa, na kuna hisia zinamchezea kichwani, akamuangalia docta na docta akasema;

‘Sasa hivi utapigiwa simu…binti anaumwa,…’akasema docta.

‘Ni kweli huwa nikijisikia hivi, ….haipiti muda…nina shida docta…’akasema

‘Hahaha….sasa nikuambie ukweli, sijapiga ramli wala nini,…ndivyo nilivyoambiwa, mimi,  kila likitaka kutokea jambo linalonigusa najiwa na njozi, sijui inakuwaje, hata mimi inafikia mahali nashindwa kuelewa ni nani huyo ananiambia hayo yote,ndio maana nikaamua kufanya uchunguzi huu….unielewe hapo, mimi sio mpiga ramli, mimi sio kwamba napenda haya mambo..lakini kwa vile yanasaidia watu, kwanini nisifanye…’docta akasema

‘Sasa utanisaidiaje…’akasema mpelelezi, na  hapo docta akapumua kimoyo moyo akajua sasa mtu keshaingia kwenye anga zake…
‘Ni hivi…jana nilijiwa na hiyo njozi..na ikanionyesha tukio lako lote, tokea ulipohamia hapa…ulihamia hapa na moto mkali sana, maana serikali ilikuamini, na ukaona hiyo ni sehemu ya kukupandisha daraja,….ukasahau kupiga hodi..’docta akatabasamu.

‘Bosi wako ukawa unamwambi hiki na kile, lakini bosi wako akawa hata hakusikilizi….mkawa sasa hamuelewani,  …sijui, nahisi alishayajua mazingiza ya hapa, akaamua kufanya kama mazingiriza yalivyo,…najua unalifahamu hilo..’docta akasema.

‘Sawa nakuelewa, eleza jinsi gani nitamuokoa binti yangu, nachanganyikiwa docta,  ndio maana hata kazi nashindwa kufanya, bosi wangu hapa amesha nishtukia, sitaki nikosane naye, lakini nitafanyaje, hebu fikiria mtoto wako anapoumwa, ..hebu fikiria, mke naye hamuelewani….aah, hata sijui nikuambieje…’akasema.

‘Kiukweli mke wako walishamteka mapema tu,…huna la kufanya juu yake…’akasema.

What…una sema nini…’akasema sasa akishika simu.

‘Sio kumteka kumchukua, hapana, walishamweka kwenye mikono yao..si unajua wakina mama wengine walivyo rahisi kurubuniwa hasa inafikia kwenye mtoto wake…huyo sasa hivi hata akiambia akumalize anakumaliza..ila nakuomba, unielewe, usije kulichukulia hili kwa pupa, mke wako ni mwema sana, lakini keshachoka,..matatizo ya mtoto yamemfika shingoni, sasa atafanyaje…’docta akatulia

‘Kwahiyo…’akauliza mpelelezi.

‘Kwahiyo ni wewe tu….haya hata mkuu hayajui,..nimekuambia wewe ili ujua jinsi gani ya kujitoa huko..na kujitoa kwako, ni kushirikiana na…mimi au mkuu, lakini kwa njia ambayo..hata sijui..maana umeshajiweka kubaya…’akasema docta.

‘Docta ningelikuwa namfahamu huyo mtu, nakuhakikishia ningelichukua machine gun, na kwenda kumiminia risasi,….nimechoka,..lakini nimejitahidi kumtafuta sana, lakini sijawahi kuonana naye, na wala simjui kabisa…’akasema.
‘Kwa vipi…?’ akauliza docta

‘Ni hivi, …lakini tuyaache hayo, sitaki kumuingiza mtu kwenye matatizo najua walivyo hao watu…’akasema

‘Mimi nimeshaingia kwenye vita na hao watu, wananifahamu,…usiogope kuhusu mimi…’akasema docta.

‘Huwa wameshanipa masharti yao,…’akasema

‘Kuwa ukiongea utakufa, au binti yako atakufa,…haya ngoja tusubirie ufe..’akasema docta.

‘Wewe unafanya mzaha…’akasema mpelelezi.

‘Endelea….’akasema docta.

‘Mimi kwa ujanja wangu wote, ..imefikia sehemu nafuata masharti yao tu…nimefanya kila niwezalo, …sijampata huyo mtu…wananjia kila mahali, kwenye facebook, ..nyumbani…yaani kila mahali natembea nao, nimechanganyikiwa docta..kila ninalolifanya wanalijua….’akasema mpelelezi.

‘Hahaha, kwahiyo hata haya mazungumzo yetu wanayajua…au sio, ndio wasiwasi wasi wako…’akasema docta na mpelelezi akawa kama anaangalia hewani.

‘Sijui…’akasema

‘Nakuhakikishia, hapa umefika..hawajui lolote,…viona mbali vyao, vimegota, haviwezi kuniona mimi kamwe, wanalijua hilo,…sasa hivi wapo matumbo joto, hawaamini…’akasema docta

‘Kwa vipi…?’ akauliza mpelelezi.

‘Muda sasa umefika wa kulimaliza hilo kundi, najua sio kazi rahisi, na wewe ndio njia,..unatakiwa ujitolee muhanga kwa ajili ya familia yako na taifa lako..unielewe vyema, njozi imeniambia hivyo, wewe ndio njia ya kufika huko kwenye uwanja wa mapambano…msaidizi wangu alikuwa nauli..alikuwa sehemu ya kunivuta hadi hapa, sasa kazi iliyobakia ni kupitia kwako,…’akasema docta.
‘Sijui….na sielewi kwa vipi…?’ akauliza

‘Wewe unawasilianaje na hao watu..?’ akaulizwa .

‘Kwa hivi sasa wameshaniondolea vile viona mbali vyote..hawaniamini tena, ilikuwa kwa simu au kwa ishara, naenda mahali nakutana nao, napata maagizo..au kupitia kwa binti yangu, wananitesea sana binti yangu…ndio maana nasema kama ningelijua jinsi ya kumpata huyo mtu…naapa, ningelimumaliza kwa risasi…’mpelelezi akasema.

‘Hao watu wanajua kuwa wewe ni njia yao ya mafanikio fulani..njia ya kupata taarifa kutoka huku kwenu, njia ya kuingia kwenye mtando wa serikali,….unanielewa, wanajua wewe una kipaji fulani…unanielewa, wewe ni mlenga shabaha mashuhuri unanielewa….’akasema na hapo mpelelezi akashtuka na kusema;

‘Oh..docta…sijamuua mimi , najua unapotaka kuelekea, hapo hunipati kamwe..’akasema.

‘Sikiliza, mimi sijasema ni wewe..ila wao wametumia taswira yako wakaiweka kwa mtu mwingine, na mtu huyo akaweza kulifanya lile jambo, ambao ulitakiwa wewe ulifanye..uone jinsi hao watu walivyo wa hatari, kwasababu wameshachukua kivuli chako, taswira yako, akili yako,…wewe hapo ulipo ni mtumwa wao, kuna kitu wamekupandikizia,…’akasema docta.

‘Kitu gani, na nitafanyaje ili kiondoke…?’ akauliza

‘Ni kweli kuwa wewe ni mlenga shabaha mashuhuri,…kweli si kweli?’ docta akauliza

‘Ni kweli,  lakini mimi sijamuua huyo mtu,…naapa, mimi sijafanya hilo tendo, nimefika pale..unielewe kwa maagizo, na baadae nikaambiwa utakuja, nifanye moja mbili tatu, ukifika wewe ndio utaonekana umeua…nikafanya hivyo…na wakati naingia ndani ndio nikasikia mlio wa risasi , kwa uzoefu wangu nikajua ni nini kimtokea, nikaingia ndani kama walivyoniagiza, unapofikia kufanya maagizo yao, sijui inakuwaje,..huelewi kitu…

‘Ehe…nakuelewa ikawaje?’ akauliza.

‘Ndio nikakuta mtu keshadondoka chini, kwa haraka ..unajua tena, nikafanya walivyotaka, nikatoka nje, lakini nilijua kabisa walivyotaka wao haiwezekani, …haiji akilini, nilijua utofauti wa bunduki, nilijua swala la muda..nilijua..kwa mtaalamu atagundua kuwa haiwezekani..lakini wao walitaka iwe hivyo ningelifanyaje…’akasema.

‘Kwahiyo unakiri kuwa mimi sijaua…?’ akauliza docta.

‘Docta unalijua hilo sana…na unajua kabisa kuwa hiyo ilikuwa ni set up..hata mkuu analijua hilo..lakini wao wana maana yao, na sijaijua ni ipi…hawafanyi jambo ki..zembe, kila jambo, unaweza kuliona la makosa lakini wana maana yao kubwa…nimejaribu kuwachunguza nimeshindwa…na zaidi ni kwasababu wameniweka kwenye ndoana yao…nimechoka,..nimeshaamua …’akatulia

‘Tulia usiamua vibaya, kujiua ndio lengo lao,  …usichukulie pupa, hili jambo linahitajia umakini wa hali ya juu..niamini mimi,…nimekuwa nikilifuatilia hili jambo hata kabla, nilioteshwa kuwa atakuja mtu atanionyesha njia,…sasa nimefika sehemu …natakiwa niimalize hii kazi, …sasa nataka ufanye jambo moja kubwa…’akasema docta.

‘Jambo gani docta, ila lisiathiri familia yangu,…docta, familia yangu ni kila kitu, nipo tayari kufa kwa ajili ya familia yangu…’akasema mpelelezi.

‘Leo, au sijui..utaitwa..utaelekezwa..najua, wanakutafutia mwanya wa kukumaliza, sasa ni wewe au wao…je utafanyaje, ..mimi sijui..ila unatakiwa ujitolee mhanga, …usijali athari yake kwako, ..najua unaipenda sana familia yako, lakini huwezi kuipenda kama bado ipo hatarini…’akasema docta

‘Mimi ninataka wewe uje kukivaa hiki kidude mwilini mwako,..sijui utafanyaje…wapi ambapo una uhakika hutagundulikana..sijui..nataka nione nyendo zako,moja hadi mwisho…mengine niachie mimi…’akasema.

Ilikuwa kitu kama unywele mndefu, mpelelezi huyu alishindwa hata kuelewa, auweke wapi…anajua akiitwa mahali na hao watu, anapekuliwa hadi kwenye chupi, sasa atafanyaje..

‘Je utaweza hilo, wewe ni mpelelezi, ni askari…una mbinu za kila aina,…sasa sehemu iliyobakia ni hii kumjua huyo mtu ni nani..tunataka tufike kwenye makao yao makuu,..tutafikaje, wewe utafikishwa leo,….sasa tutakupataje…?’ akauliza docta.

‘Hata sijui..anyway, nipo tayari kufa kwa ajili ya familia yangu, niachie ..nitajua jinsi gani ya kufanya…’akasema

Docta akatoka kitu kwenye vifaa vyake,
‘Nipe kidole chako…’mpelelezi kwa mashaka akanyosha kidole chake, na docta akamchoma sindano kama zile za kutolea damu kwenye kidole kwa ajili ya kupima malaria, na mpelelezi akahisi maumivu makali, …na ghafla akadondoka chini.

 Docta akampekua kila mahali na kuhakikisha hakuna kitu mwilini mwake, na baadae akampigia simu mkuu;

‘Tayari unaweza kuja…’akasema na mara mkuu akafika.

‘Ok, umefanya ulichotaka..?’ akauliza na docta akamuonyesha mpelelezi aliyekuwa kalala sakafuni, na mkuu akatikisa kichwa kukubali.

‘Sasa huyu mtu ni wetu..watamshuku sana.., na hatujui hatima yake itakuwaje,..muhimu kwa sasa ni kuweka watu wako tayari…vita imeanza…na vita hii haihitaji silaha sana ila ikibidi…hasa hapa, ni utaalamu wa kidigitali, ulichanganyikana na …nguvu za giza…zinaitwa hivyo lakini wenzetu wameshaziiingiza kwenye mtandao,..’akasema docta.

‘Sasa huyu msaidizi wako yupo wapi..?’ akauliza mkuu.

‘Hata mimi sijui..ila nahisi bado wanamvuta , kama walivyomvuta binti, nia yao ilikuwa kuwakutanisha, na huyo binti, halafu wanamumaliza....na ile dhamira yao, ya ..mpenzi wa ….wa mtandao, ikamilike, kuna ka mchezo wamecheza, ..ni kama majaribio…bado hawajafanikiwa…, ambayo yakifanikiwa,..watu watakuwa matatani…’akasema docta.

‘Kwa vipi…?’ akauliza

‘Mpenzi wako wa facebook, huyo huyo anaweza kuwa ni adui wako,…Itafikia muda, tutaogopa hata kugusa mitandao, maana unaweza ukahisi mtu , au picha,..kumbe sio mtu au picha..taswira zinachukuliwa na kuchezewa kama wanga wanavyochezea watu usiku…unajua wachawi wanavyofanya kwenye majumba ya watu usiku, ….sasa hawa wameamua kuyaweka kidigitali..ni hatari, …achana na wazungu …’akasema docta.

‘Mhh, mimi hayo sielewi…na sitaki kuyaelewa…..naogopa, na wameanza kunitisha..lakini nimeaga kwetu…’akasema mkuu.

‘Hawajataka tu,… huna nyota ya mambo yao, wanachunguza nyota…na bahati yamtu, kuna watu wana nyota, nzuri,… na vitu kama hivyo, wakikuona hufai hawawezi kupoteza muda na wao, ila wakikuona ni mzigo, au ni kikwazo kwao, watakumaliza, na nahisi mkuu wako alilijua hilo ndio maana akawa hashughuliki nao…’akasema docta.

‘Achana na mtu huyo…arubaini zake zinakuja…’akasema msaidizi huyo huku akimuangalia mpelelezi aliyekuwa sasa akizindukana..

*************
Mpelelezi, alisimama kwa haraka na kuhakikisha nguo zake zipo sawa, akawa kama hajui alipo baadae akasema;

‘Docta umenifanya nini mimi mbona nipo hivi..…?’ akauliza

‘Nimekufanya nini…?’ docta akauliza akionyesha kushangaa..

‘Hata sielewi,…nahisi binti yangu anaumwa..nataka kufika nyumbani…’akasema mpelelezi akitaka kuondoka, na docta akamuashiria mkuu amuache tu aondoke,…na mpelelezi akasita halafu akageuka nyuma, na kumuangalia docta akatikisa kichwa kama kukubali, halafu akamgeukia mkuu wake, na kusema;

‘Mkuu naomba ruhusa nikamuone binti yangu, nilikuambia jinsi gani anavyoumwa, sasa hisia zinanituma kuwa anaumwa…’akasema

‘Lakini hawajakupigia simu…’akasema mkuu

‘Najua tu…’akasema

‘Ok, unaweza kwenda lakini uwe na tahadhari, nakutegemea sana wewe …’akasema mkuu.

‘Sawa afande, tupo pamoja…’akasema na kwa haraka akaondoka na docta na mkuu wakaangaliana bila kusema neno, mkuu akatoka nje akikimbilia ofisini kwake, na docta akaingia kwenye chumb chake na kutoa komputa yake ndogo…

NB: Hii imekaaje!!!, hata sielewi, nasubiria comments zenu kwa wingi…


WAZO LA LEO: Kila mtu kabarikiwa kipaji chake na muumba wake, wengine hujua jinsi gani ya kuviendeleza vipaji vyao na kuvifanya mtaji, wengine kama walivyo wezi, wanaamua kutumia vipaji vya wengine kwa manufaa yao, huo ni wizi , HIYO NI DHULUMA,……kama unajua kipaji cha mtu fulani kinaweza kuzalisha kwanini usimwambie huyo mtu, mkaja kushirikiana naye ..kitakachopatikana mkatafuta njia ya kugawana,..Tukumbuke kuwa, siku ya malipo, kila kitu ulichofanya utaulizwa tuweni makini sana.
Ni mimi: emu-three

No comments :