Tulifika kwenye nyumbani
ya huyo mzee aliyoikimbia, tulitarajia kuwakuta polisi kama walivyoahidi,
lakini tulipofika huko, hatukuwaona, walikuwa hawajafika…, tukaulizana
tufanyeje,
Tuligonga mlango lakini
hakukuwa na dalili ya mtu, mzee akasema kama hakuna mtu tuingie
ndani maana ni nyumba yake, kwa muda huo mlango ulikuwa umefungwa..
‘Mimi nina ufunguo wa
akiba…’akasema mzee, kwahiyo tukatumia ufungu huo wa akiba na mzee akaukabili
mlango na kuanza kufungua mlango..
‘Sijui kaenda wapi huyu
mtu…, lakini..hamsikii, harufu mbaya..’akasema huku akiweka ufungua kwenye
kitasa.
‘Ni kweli…hata mimi
naihisi hiyo harufu...mhhhhfuuh’nikasema.
Mzee akaufungua
mlango,…duuh, ilibidi tushike pua, harufu mbaya ajabu, kama kitu kimeoza,..
‘Kuna harufu mbaya kama
ya mzoga…ni kitu gani hiki, mmh..’akasema mwenye nyumba.
‘Nahisi ni zaidi ya
mzoga,mhh, humu hakukaliki. Lakini tulipofika hapa hakukuwa na harufu kama
hiyo, ilikuwa harufu ya mafukizo tu. …’akasema docta.
‘Kuna kitu kimekufa…isije
ikawa mtu wako kafa..lakini kama ni kufa atakufaje kwa muda huoo mfupi na
kuanza kunuka , masaa mangapi yamepita, tangia tuachane naye,..’nikasema.
‘Sizani kama ni
yeye..kuna kitu kingine,... je tutaweza kuingia humo ndani na harufu kama hiyo,
?’ akauliza docta.
‘Kwanini, tusiingie,
tuzibe pua, tuingie…tu…’akasema mzee, akitangulia kuingia ndani.
Tukaingia ndani kila
mmoja akiwa kashikilia pua, na tukafika chumba cha maongezi pale tulipokuta
vile vitu awali, kulikuwa hakuna kitu, nyumba ilikuwa kimia, na mimi mwili
ulikuwa unanisisimuka,..tukaangalia huku na kule hakuna kitu.
‘Sasa hii harufu
inatokea wapi…?’ nikauliza.
‘Hebu twendeni chumba
chake…’akasema mwenye nyumba.
Na kabla
hatujaenda huko mara tukasikia gari likisimama nje, lilikuwa gari la polisi,
ikabidi tusubirie kidogo, sote tulikuwa tumeshikilia pua,…polisi wakaingia na
wao wakashikilia pua..
‘Mhh..kuna kitu gani
kimekufa…?’ akauliza polisi.
‘Hatujui ndio na sisi
tumefika tukawa tunalizana…’akasema mzee.
‘Ok, naambieni, ni nini
dhumuni lenu, maana hiyo harufu, sio ya mnyama wa kawaida..kuna kesi hapa, hiyo
itakuwa ni harufu ya mtu aliyekufa,…akaanza kuoza,..’akasema polisi.
‘Oh, sisi tumeingia, …na
zaidi ya mimi hakuna mwingine aliyegusa kitu, eti si ndio hivyo…’akasema mzee.
‘Ok, sawa, kwahiyo, huyo
mpangaji wako hujamkuta..au …isije ikawa ndio kafa humu ndani..lini mlionana
naye..?’ akauliza
‘Leo mbona tulikuwa
naye, haiwezekani akawa ndio yeye…’akasema mzee.
‘Kwahiyo
hamjagundua hiyo harufu inatoka wapi..?’ akasema akianza kufuatilia kwa pua..
‘Bado…’akasema mzee.
‘Itakuwa inatokea
huku…’akasema askari mwingine.
‘huko mtaenda
wenyewe..’nikasema sasa nikitaka kutoka nje, na docta akanishikilia mkono kuwa
nisubirie.
‘Ooohoooh…’alikuwa
askari aliyeingia ndani, alirudi akionyesha kutaka kutapika, na sisi hapo
tukazidi kushikilia pua.
‘Mkuu, hapa mpaka tupate
kitu cha ziada, aitwe docta..’akasema askari, wakapigiana simu na wenzao ili
madakitari wafike, na sisi tukatoka nje kwa haraka maana harufu ilizidi
maradufu.
************
Ilichukua muda, baadae
waligundua kuwa kuna viungo vya wanadamu, vilikuwa vimefungwa kwenye kiroba,….
‘Hatuwezi kuvitambua,
lakini yaonekana ni maiti zilifukuliwa zikakatwa viungo, sizani kama walivikata
kwa watu walio hai...ni vingi sana,...na vingi vya viungo hivyo ni vya
wanawake..’akasema huyo docta wao..
Baadae uchunguzi
ukatufanya twende hadi makaburini, na huko ndio ikagundulikana kuwa makaburi
mengi yalifukuliwa…ikabidi wachimba baadhi ya hayo makaburi, wakagundua kweli
sehemu nyingi za maiti hizo zimekatwa viungo.
‘Hawa watu ni mashetani,
eeh…’polisi akashangaa.
‘Inaonekana kila maiti
ikizikwa wao wanawahi mapema kufukua na kukata viungo, sasa huo mzigo ulikuwa
unasubiria kupelekwa,...sasa sijui imekuwaje,…’akasema askari mmojawapo
‘Ni nani anafanya hii
kazi…?’ akauliza askari mwingine akituangalia sisi, na sisi hatukuw ana jibu la
kuwaambia.
‘Huyu mtu wako anayeishi
hapa yupo wapi….?’ Akauliza askari, kiongozi wao.
‘Hatujui, kama
tulivyokuambia, nia ni kukutana naye, kumuhoji, sasa ndio tunakutana na mambo
kama haya…’akasema mzee.
‘Ok, sasa hii kazi
tuachieni sisi, tutampata tu huyu mtu au kama ni kundi la watu litapatikana
tu…’akasema polisi.
‘Itakuwa kama kazi ile
ya awali, mpaka sasa hamjamgundua huyo aliyesababisha binti yangu
kujiua...'akalalamika mzee.
‘Unajua kazi hizi ni
ngumu, hazina ushahidi, hatuwezi kumkamata mtu kwa hisia tu..ila hili sasa
limetupatia namna ya kuandaa kesi, ..hapa tuna ushahidi, na huyu mtu tutambana
sana, mpaka atatuambia ukweli….haya ni mambo ya imani za kichawi, unanielewa
mzee.’akasema huyo askari.
‘Lakini kama ni yeye,
asingeliweza kuacha kitu kama hicho humu ndani, nahisi wenyewe kwa wenyewe
wanachomeana, hii ni kumkamatisha huyu mtu ili aonekane anafanya hii
kazi…’akasema docta.
‘Tutaligundua,
unafikiri, ngoja tumkamate, atatuambia kila kitu…’akasema polisi
Wakati tupo pale
mara tukasikia watu wakipiga kelele…
‘Ajali ajali…’
*************
‘Mnasikia huko kuna, kelele
nahisi kuna ajali, imetokea…’akasema askari, akachukua sismu yake na kuanza
kuwasiliana na wenzake waliopo huo bara barani,,…
‘Kuna nini huko..over?’
akauliza wakitambulishana kwa maneno yao
‘Kuna mtu kagongwa na
gari, yupo taabani,..’sauti nyingine ikasema.
'Ni ajali tu, au kwa
makusudi..?’ akauliza.
‘Huyo aliyemgonga
hakusimama, na hali ya huyu mtu ni mbaya sana,sizani kama atapona, …’akasema
askari mwenzake.
‘Mumeweza kumtambua huyo
mtu ni nani..?’ akauliza.
‘Ni nani huyo..’akauliza
tena huyo askari. Tukawa hatusikii wanachoongea na huyuu askari akasema;.
‘Oh, ndio tupo hapa
nyumbani alipokuwa akiishi , kama ni huyo mtu, na humu ndani tumekuta mambo ya
ajabu kweli, nahsi huyo mtu atakuwa akifanya biashara za miili ya watu,
muwahisheni hosp na ulinzi mkali, na mjaribu kumhoji hoji asije akafa tukakosa
ushahidi..’akasema huyo askari.
Yule askari alipomaliza
kuwasiliana na wenzake, akatugeukia na kusema;
‘Huyo mtu mliyemfuata
huku, yupo taabani kagongwa na gari...'akasema
'Kwahiyo hawezi kuongea
kabisa..?' nikamuuliza
'Hawezi, ..kagongwa
vibaya sana..askari wangu wanasema kila wakimuuliza swali anachojibu ni kusema,... ni
mkuu, ni mkuu..hivyo tu basi…’akasema docta.
'Mkuu...'nikajikuta
nimesema hivyo.
'Mnamfahamu huyo
mkuu..?' akauliza polisi
‘Hapana, kama
tulivyokuambia awali, hata sisi alituambia hivyo, kuwa anayemtuma ni mkuu, sasa
huyo mkuu ni nani, hata sisi hatumfahamu…’akasema mzee
‘Ok…tutamgundua tu…ila
huyu jamaa labda asipone, akipona ana kesi kubwa ya kujibu, watu kama hawa ndio
tunawatafuta…’akasema huyo askar akipiga simu kuwasiliana na watu wake.
Ikawa sisi hatuna la
kufanya,, tuliwaachia askari wafenye kazi yao, na hatukuruhusiwa kuingie tena
kwenye hilo jengo,..hata hivyo ni nani angeliingia na hiyo harufu,
tukaambiwa tukae sehemu ambayo itakuwa rahisi kwao kutupata maana tulihitajika
kutoe maelezo polisi, baadae tukawa tunajiuliza wenyewe kwa wenyewe....
‘Docta sasa
tufanyeje..maana hii ishakuwa kesi, na polisi watakuwa wakitusumbua kama sisi
ndio wahalifu?’ nikasema.
‘Ni kazi yao waache
wafanye, …na safari hii lazima watagundua kitu….’akasema mzee.
‘Ni mpaka…nahisi bado
kuna tatizo..’akasema docta.
‘Kwanini…?’ akauliza
mzee.
‘Usicheze na watu wenye
pesa, biashara hizi na za madawa ya kulevya, zina mitihani mingi
sana..sijui..lakini nimeshaanza kuhisi jambo, ..kwann huo mzigo wa hivyo viungoi
vya binadamu ikaletwa na kuweka humo…huoni kuna kitu…’akasema docta.
‘Polisi wenyewe
watagundua…’akasema mzee.
‘Sawa tusubirie, lakini
sisi hatuwezi kuwasubiria polisi kazi yetu inaendelea, ..’akasema docta.
‘Tutakuwa tunaingilia
kazi ya polisi…’akasema mzee.
‘Hapana hatutaingilia
kazi yao, ila tutawasaidia,..wewe utaona tu…’akasema docta.
‘Kwa vipi…?’ nikauliza.
‘Sijui kama
tutaweza,kupata nafasi ya kumuhoji huyo mtu, kama bado yupo hai ingelikuwa ni
bora zaidi, tukaipata hiyo nafasi, huyo ndiye msaada wetu
mkubwa,..’akasema docta
‘Sasa utafanyaje, na
wakati huyo mtu atakuwa hospitali na huko atakuwa kwenye ulinzi mkali…’akasema
mzee.
‘Usijali, mimi huko ni
nyumbani kwangu…’akasema docta.
**********
Basi baadae docta
akasema twende huko hospitalini,
'Na tukifika huko,
mengine muniachie mimi....'akasema
'Utafanyaje.. kuingia
kumuona...?'nikauliza
'Hilo niachieni
mwenyewe..'akasema
Kiukweli mimi sikuwa na
hamu tena ya kuendelea na hili tatizo, nilitaa hata snisiende huko, lakini
baadae nikaingiwa na hamu ya kujua ni nini kitakachoendeela, kwahiyo
nikajiunga, na moja kwa moja, tukaenda huko hospitalini, ambapo huyo majeruhi
kalazwa..
Tuliambia huyo majeruhi
kapelekwa chumba cha wagonjwa mahututi, na docta kwa uzoefu wake wa kidakitari
akapata nafasi ya kuingia huko ndani na baadae akatoka, akasema;
‘Bado kazi ni ngumu…ila
kuna neno kalisema nahisi linaweza kuwa ni msaada kwetu, kwanza aliniomba
nimsaidie kama sijakichoma kile kibuyu chake cha uchawi, nikamwambia akipona
nitampatia;
‘Utakipata wapi…?’
nikauliza huyo docta.
‘Ikibii tutamtengezea
kingine..’akasema docta.
‘Kwani hatajua kuwa
umetengeza kibuyu kingine.…’nikasema.
‘Ok, najua hilo
haliwezekani, hata hivyo, huyo mtu sio wa kupona, nilijaribu sana kumdadisii…'
'Kasema nini zaidi..?'
nikamuuliza
'Yaani inachukua muda
kuongea, ...yaonekana hawakutaka huyu mtu apone, hutaamini nasikia polisi
wanadai hawajaweza kulipata hilo gari lilimgonga...'akasema
'Huyo majeruhi
alisemaje...?' nikazidi kumuuliza docta
'Yeye kwanza anakiri
kuwa kweli kakosea na anatubu madhambi yake...; akasema
'Makosa gani kafanya..?'
nikauliza
'Nilimuuliza hivyo,
kakosea nini, na atafanyaje ili toba yake iwe sahihi maana anatakiwa kutubia
kwa aliowakosea, ...akawa anaongea kwa shida, akisema;
'Najua
nimeshachelewa,..ila nakuomba wewe unisaidie kuniombea msamaha..'akasema
'Kwa nani sasa..mimi
siwajui uliowakose...?' nikamuuliza
'Kwa, kwa....wote tu,
...si, si... yaani ikawa hivyo tu, ., hakuweza kusema neno, nashangaa
nikimuuliza mambo mengine anaweza kujibu mengine anakuwa mnzito
kujibu...'akasema docta
'Kwahiyo alisema ni nani
kamtuma, ...au ni nani ukamuombee msamaha kwa ajili yake..?' nikauliza
'Aliyemtuma anadai ni
mkuu,..na huyo mkuu hamjui, wanawasiliana tu kwenye simu, hajawahi kukutana
naye uso kwa uso..., yeye akimaliza kazi anatumiwa pesa zake kwa njia ya
simu,…akasema zaidi tukitaka twende kwenye facebook,…’
‘Kwenye facebook,,,,?'
nikauliza kwa mshangao.
'Ndio kasema hivyo ndio
nikamuuliza huyo mtu anatumia jina gani, ?’ nikamuuliza
‘Mkuu,…au..ana wakala
zake…mashetani..’akasema.
‘Mashetani,...huyo mtu
wa ajabu sana, utawasilianaje na mashetani...'nikauliza kwa mshangao.
'Ndivyo alivyosema, na
nilimuuliza hivyo hivyo, akasema wamo humo kwenye facebook, ni wengi na huyo
mkuu ana mawakala wake wengi, wenye asili ya namna hiyo..'akasema
'Sasa sisi kama sisi
tutawajuaje..?' nikauliza
'Nilimuuliza hao
mawakala wake kama ni mashetani, sisi tutawajuaje...akasema hivi;
‘Wapo wengi tu…wanawake
kwa ajili ya kuwapata wanaume na wanaume kwa ajili ya kuwapata wanawake…sifa
yao kubwa ni uzuri, mvuto…na wengine..walishakufa ila wanatumiwa vivuli
vyao..kuwavuta watu wapya kujiunga na kundi lao
’akaniambia hivyo.
‘Oh….ina maana
..’nikasema.
‘Ndio
hivyo,..ulinaswa..’akasema docta alipogundua nataka kusema nini.
‘Haiwezekani..’nikasema.
‘Kama haiwezekani yupo
wapi huyo mtu.., mpaka leo ulishawahi kumuona sura yake huyo mtu..’nikasema.
‘Ni nani huyo..?’
akauliza mzee
‘Kuna mtu anamdanganya
kwenye mitandao,…kama rafiki, ndio namkanya kuwa watu hao hawaaminiki…’akasema
docta,akijaribu kudanganya, sikujua kwanini doct aanamua kufanya hivyo.
‘Ndio maana nilikuwa
nawakanya sana mabinti zangu wasiendekeze mitandao ya kijamii, hasa hiyo
facebook, wao wanadai kuwa humo unaweza kumpata rafiki wa kuaminika…hata
wazungu wanafanya hivyo...’akasema mzee.
‘Kwahiyo walikuwa na
marafiki huko kwenye facebook,..?’ akauliza docta
‘Sijui...ndivyo
walivyokuwa wakidai,....hayo ni mambo yao vijana..’akasema mzee.
‘Sasa huyo majeruhi
katusaidia nini…?’ nikauliza.
‘Nilipomaliza kumuhoji,
akapoteza fahamu, na sijui kama aataamuka tena…sasa huko kwenye facebook,kuna
nini…ni nani anaweza kutusaidia kwa hili…’akasema docta.
Labda binti yako
mzee..’nikasema.
‘Kwa vipi, kwani wewe
haupo kwenye facebook, wengi wapo huko, huyo binti yangu ndio anaweza kusaidia
nini..hapana msimsumbue binti yangu…’akasema mzee.
‘Hili jambo linahitajia
utaalamu wa ziada, watu wanaosshughulika na hii mitandao, wanaowekea watu
akaunti zao, au …wepesi wa kubuni picha nak….sasa sijui ni nani hapa jirani
mnayemfahamu..?’ akauliza docta.
‘Huyo jamaa anayemiliki,
super market ni mtaalamu wa mambo kama hayo, kwanza kabisa ndio ilikuwa kazi
yake alipofika, baadae ndio akaajiri watu huku akijishughulisha na biashara
hiyo ya supermarket,…sijui kama anaweza kutusaidia..’akasema mzee.
‘Huyo anaweza akawa
nyuma ya haya mambo, ukimuendea ni kama umejipeleka mwenyewe, kufichua siri
zako,…cha muhimu hapa, ni turudi nyumbani tuone pa kuanzia..’akasema docta, na
kweli tukarudi nyumbani kwa Mzee
****************
Mama na bint yake
walikuwa wakitusubiria kwa hamu sana,na walipotuona ikawa swali kubwa,
kumetokea nini huko..
‘Huyo mtu yupo taabani
hospitalini, kagongwa na gari…’akasema mumewe
‘Umeona hao watu
walivyo, hawaogopi kuua,…’akasema bint.
‘Watu gani, hao ?’
nikamuuliza na yeye akaniangalia kwa macho ya kushangaa, na kusema;
‘Si ndio hao
mnaowafuatilia…..au ningesemaje..’akasema huyo bint.
‘Bint nikuulize
kitu,..unamfahamuje huyo mtu anayemiliki super market, ulisema uliwahi kuongea
na wewe, akasema anataka kumuoa dada yako,…na alipoona dada yako kafariki
akakugeukia wewe, hebu tuambie tunawezaje kuongea naye, au..’akasema docta
‘Wewewewe..acha hiyo
usimtumbukize binti yangu kwenye hayo majanga…kama sisi wenyewe hatuwezi basi,
tuyaache, tuwaachie polisi…’akasema mzee
‘Sio hivyo mzee…nahis
huyu binti yako, anaweza kuwa msaada mkubwa kwa hili jambo, huyo jamaa alitokea
kuwapenda mabinti zako, tukimtumia huyu bint…tunaweza tukagundua
mengi..’akasema docta.
‘Hapana hilo siwezi
kukubaliana nalo kamwe…’akasema mzee.
‘Mzee
mimi..nawahakikishia kuwa binti yenu atakuwa salama…mimi nitamlinda, muhimu
natafuta jinsi ya kuingia kwenye himaya ya huyo mtu, lakini siwezi kumuingili
hivi hivi…binti upo tayari, au unaogopa…?’ akamuuliza binti.
‘Tatizo docta, mimi
sitaki tena kuhatarisha maisha ya familia yangu, sitaki kuongea na huyo mtu ,
kwanza namuogopa, ukimuangalia usoni, utahisii kuwa sio mtu wa
kawaida…’akasema.
‘Unavyoongea ni kama
unawafahamu fahamu kazi zao…sasa sijui, hebu nikuulize huko kwenye mtandao
huwasiliani na hao watu..?’ akauliza docta.
‘Wa nini..kwanini
niwasiliane nao…?’ akauliz ahuyo binti.
‘Labda uliwahi kuwa na
urafiki nao, wengi wanafanya hivyo, …hebu niambie huyo mkuu hujawahi kuwa na
mawasiliano naye..?’ akauliza docta.
‘Sina mawasiliano naye,
, na sijazoeana naye, nimeshakuambia hata kuonana naye uso kwa
usomnaogopa…’akasema.
‘Kuogopa ndio
tatizo…’akasema docta na mara simu ya huyo binti ikaita. Binti kwa haraka
akaichukua na kusikiliza..
‘Ni nani, kafa..?’
akauliza
‘Oh, jamani
masikini…’akasema
‘Hapana, siwezi,
tafadhali siwezi, nilishawaambia, mimi siwezi na sitaki, sitaki.......’akakata
simu akionyesha kakasirika
‘Ni nani kafa..?’
akauliza mzee
‘Huyo mpangaji wako,
masikini jamani..’akasema kwa masikitiko.
‘Ni nani huyo kakupatia
hiyo taarifa..?’ akauliza docta.
‘Ni rafiki yangu
mmoja…’akasema na docta aliposikia hivyo, akashika kichwa kama anawaza
jambo halafu akasema;
‘Oh, ngoja nimpigie
huyo docta anipe taarifa kamili..’akasema na akawa anapiga namba..
‘Mhh..salio
limekata…sijui ..nani naweza kutumia simu yake..?’ akauliza na mimi nikajaribu
kupiga simu yangu, ikawa haina salio, nikasema;
‘Hata mimi salio
limekata, labda tukope..’nikasema
‘Mzee…simu yako ina
salio..?’ nikamuuliza.
‘Oh,..ngoja tuagize
vocha..’akasema mzee akijipapasa mfukoni, mimi naikagundua kitu, nikasema
nikimuangalia huyo binti..
‘Binti kwani simu
yako haina salio..?’ nikamuuliza na yeye kwanza akaonekana kusita,
halafu baadae akasema;
'Mhh..sina uhakika,
lakini ngoja nijaribu kuangalia...'akasema akiweka namba za kuangalia salio,
baadae akasema
‘Ndio…’akasema huku
akiniangalia usoni,
‘Lakini ..sio jingi
sana, kwani ulitaka kumpigia mtu wa mtandao gani akasema;
Docta akamtajia namba,
na kusema;
‘Usijali, utarejeshewa
salio lako….’akasema
‘Ok, hamna shida, ila ….ok,
sawa hiyo hapo inaita…’akasema na kumkabidhi docta, docta akasema;
‘Samahani kidogo,
akageuka upande wa pili akawa anaongea na huyo mtu, ambaye docta wa hiyo
hospitali.
‘Unasema
keshafariki..ooh, sory, ..lakini je kuna jamaa yake yoyote aliyewahi kufika hapo,
kuulizia labda…?’ akauliza na akajibiwa, baadae akatulia akiwa kageuka upande
mwingine baadae akageuka na kumkabidhi simu binti.
‘Sasa sisi tutawaacha
kidogo, ila tutarudi baada ya muda mfupi...’akasema docta.
‘Mnakwenda wapi askari
walisema watatukuta hapa sote msiondoke mnajua mimi ndio nimechukua dhamana
yenu…’akasema mzee
‘Mzee usijali, tunarudi
sasa hivi…’akasema docta.
‘Mimi nina wazo docta…nipo
tayari kuonana na huyo anayemiliki supermarket, kama kweli itasaidia..’akasema
huyo binti.
‘Kwanini..?’ akauliza
baba yake kwa mshangao.
‘Kwasababu baba,…naona
nisipofanya hivi, kuna hatari ya matatizo..baba, hao watu wanavyoonekana sio
watu wema, watu wanaongea mengi…hasa huyo anayemiliki hiyo supermarket, wanadai
kuwa huenda anashirikiana na hao wanaoitwa friimason…’akasema na kutulia
‘Watu wanasema tu, kwa
vile kawa tajiri au…?’ akauliza baba
‘Lisemwalo lipo baba,
mimi naogopa sana,…na jingine angalia kilichomkuta dada, naogopa kisije kutokea
kwenye familia yetu tena, ni bora mimi nijitolee mhanga kwa ajili ya familia
yetu…’akasema
‘Hapana hilo sikubali
binti yangu, mimi ndio wakujitolea muhanga, sio nyie, hata mama yako hawezi
kukubali, hivi kaenda wapi…’akasema baba
‘Yupo jikoni..’akasema
binti
‘Baba hili usimwambie
mama, mimi nitashirikiana na hawa watu mpaka kieleweke, najua, ni kazi ya
hatari…lakini, sitaweza kutuliza akili yangu, na kichwa changu, kama hatutaweza
kulipiza kisasi cha dada yangu,..mimi nimefikiria sana, na sasa nimeamua, nipo tayari kujitolea,…’akasema
‘Mimi kama baba yako
nimesema hapana, …’baba yake akasema kwa hasira na mama akatokea, na kukuta
baba mtu akifoka hivyo.
‘Vipi tena, kuna
nini..umesema hapana kwa jinsi gani , kuna nini kinachoendelea, mniambia,
sitaki kufichwa kitu hapa…’akasema mam
‘Mama hakuna kitu…mimi
nataka niende kwenye huo msiba..’akasema
‘Msiba gani..?’ akauliza
mama
‘Si huyo mpangaji wetu…’akasema
‘Tutakwenda wote, tusubirie
utaratbu utakuwaje…’akasema mama,
‘Sawa,…mimi nipo tayari,
mkiwa tayari mniambie, nipo chumbani kwangu mara moja..’binti akasema akiondoka
kuelekea chumbani, na mimi na docta tukabakia pale, na docta akasema;
‘Binti anajua jambo…na
hivi sasa huenda anawasiliana na hao watu, najua kwanini anafanya hivyo, lakini
tumpe muda, hata hiyo ya kusema atashirikiana na sisi, sio kweli anachofanya ni
kuvuta muda,…sasa sijui kwann…kuna hii namba walimpigia, nataka tuipige , tujue
ni nani kabla hajawasiliana nao..’akaniambia kwa sauti ya chini, na kuanza
kutoka nje, mimi nikabakia na mara binti akaja akiwa na haraka..
‘Docta kaenda wapi…?’
akauliza akionyesha wasiwasi mkubwa
‘Yupo kaenda kujisaidia…’nikasema
‘Hapana nimeshamjua,….kachukua
namba ya simu anataka kupiga,…’akasema sasa akitaka kutoka nje
‘Wewe binti niambie kuna
nini unaficha…’baba akasema kwa ukali
‘Hakuna kitu baba,
nafanya haya kuwalinda nyie…baba, ni hatari, …’akasema huku akikimbilia nje,
baba akamuangalia mkewe, na mkewe hakupoteza muda, mbio akatoka nje kumfuatilia
binti yake…..
NB: Je binti anaweza
kulifanya hili.
WAZO LA LEO:Ukiuona
uhalifu, ukiuona ubaya, na una uhakika nao kuwa ni ubaya kuwa ni uahalfu,…wewe
ukanyamaza kimia, na ukijua uhalifu huo utaleta madhara kwa jamii au kwa
mwenzako, ujue na wewe utakuwa umehusika kwa namna moja au nyingine.
Tumeambiwa, ukiuona ubaya, tuuondoe kwa mikono yetu, yaani tuchukue hatua, au
tuukemee, au tukishindwa kabisa tuuchukie, lakini kuchukia tu moyoni ni
udhaifu, ni vyema tukachukua hatua, tukaisaidia jamii.
Ni mimi: emu-three
No comments :
Post a Comment