Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, May 2, 2017

MPENZI WA FACEBOOK-20



Tulifika kwenye nyumbani ya huyo mzee aliyoikimbia, tulitarajia kuwakuta polisi kama walivyoahidi, lakini tulipofika huko, hatukuwaona, walikuwa hawajafika…, tukaulizana tufanyeje,

Tuligonga mlango lakini hakukuwa na dalili ya mtu,  mzee akasema kama hakuna mtu tuingie ndani maana ni nyumba yake, kwa muda huo mlango ulikuwa umefungwa..

‘Mimi nina ufunguo wa akiba…’akasema mzee, kwahiyo tukatumia ufungu huo wa akiba na mzee akaukabili mlango na kuanza kufungua mlango..

‘Sijui kaenda wapi huyu mtu…, lakini..hamsikii, harufu mbaya..’akasema huku akiweka ufungua kwenye kitasa.

‘Ni kweli…hata mimi naihisi hiyo harufu...mhhhhfuuh’nikasema.

Mzee akaufungua mlango,…duuh, ilibidi tushike pua, harufu mbaya ajabu, kama kitu kimeoza,..

‘Kuna harufu mbaya kama ya mzoga…ni kitu gani hiki, mmh..’akasema mwenye nyumba.

‘Nahisi ni zaidi ya mzoga,mhh, humu hakukaliki. Lakini tulipofika hapa hakukuwa na harufu kama hiyo, ilikuwa harufu ya mafukizo tu. …’akasema docta.

‘Kuna kitu kimekufa…isije ikawa mtu wako kafa..lakini kama ni kufa atakufaje kwa muda huoo mfupi na kuanza kunuka , masaa mangapi yamepita, tangia tuachane naye,..’nikasema.

‘Sizani kama ni yeye..kuna kitu kingine,... je tutaweza kuingia humo ndani na harufu kama hiyo, ?’ akauliza docta.

‘Kwanini, tusiingie, tuzibe pua, tuingie…tu…’akasema mzee, akitangulia kuingia ndani.

Tukaingia ndani kila mmoja akiwa kashikilia pua, na tukafika chumba cha maongezi pale tulipokuta vile vitu awali, kulikuwa hakuna kitu, nyumba ilikuwa kimia, na mimi mwili ulikuwa unanisisimuka,..tukaangalia huku na kule hakuna kitu.

‘Sasa hii harufu inatokea wapi…?’ nikauliza.

‘Hebu twendeni chumba chake…’akasema mwenye nyumba.

 Na kabla hatujaenda huko mara tukasikia gari likisimama nje, lilikuwa gari la polisi, ikabidi tusubirie kidogo, sote tulikuwa tumeshikilia pua,…polisi wakaingia na wao wakashikilia pua..

‘Mhh..kuna kitu gani kimekufa…?’ akauliza polisi.

‘Hatujui ndio na sisi tumefika tukawa tunalizana…’akasema mzee.

‘Ok, naambieni, ni nini dhumuni lenu, maana hiyo harufu, sio ya mnyama wa kawaida..kuna kesi hapa, hiyo itakuwa ni harufu ya mtu aliyekufa,…akaanza kuoza,..’akasema polisi.

‘Oh, sisi tumeingia, …na zaidi ya mimi hakuna mwingine aliyegusa kitu, eti si ndio hivyo…’akasema mzee.

‘Ok, sawa, kwahiyo, huyo mpangaji wako hujamkuta..au …isije ikawa ndio kafa humu ndani..lini mlionana naye..?’ akauliza

‘Leo mbona tulikuwa naye, haiwezekani akawa ndio yeye…’akasema mzee.

 ‘Kwahiyo hamjagundua hiyo harufu inatoka wapi..?’ akasema akianza kufuatilia kwa pua..
‘Bado…’akasema mzee.

‘Itakuwa inatokea huku…’akasema askari mwingine.

‘huko mtaenda wenyewe..’nikasema sasa nikitaka kutoka nje, na docta akanishikilia mkono kuwa nisubirie.

‘Ooohoooh…’alikuwa askari aliyeingia ndani, alirudi akionyesha kutaka kutapika, na sisi hapo tukazidi kushikilia pua.

‘Mkuu, hapa mpaka tupate kitu cha ziada, aitwe docta..’akasema askari, wakapigiana simu na wenzao ili madakitari wafike, na sisi tukatoka nje kwa haraka maana harufu ilizidi maradufu.

************

Ilichukua muda, baadae waligundua kuwa kuna viungo vya wanadamu, vilikuwa vimefungwa kwenye kiroba,….

‘Hatuwezi kuvitambua, lakini yaonekana ni maiti zilifukuliwa zikakatwa viungo, sizani kama walivikata kwa watu walio hai...ni vingi sana,...na vingi vya viungo hivyo ni vya wanawake..’akasema huyo docta wao..

Baadae uchunguzi ukatufanya twende hadi makaburini, na huko ndio ikagundulikana kuwa makaburi mengi yalifukuliwa…ikabidi wachimba baadhi ya hayo makaburi, wakagundua kweli sehemu nyingi za maiti hizo zimekatwa viungo.

‘Hawa watu ni mashetani, eeh…’polisi akashangaa.

‘Inaonekana kila maiti ikizikwa wao wanawahi mapema kufukua na kukata viungo, sasa huo mzigo ulikuwa unasubiria kupelekwa,...sasa sijui imekuwaje,…’akasema askari mmojawapo

‘Ni nani anafanya hii kazi…?’ akauliza askari mwingine akituangalia sisi, na sisi hatukuw ana jibu la kuwaambia.

‘Huyu mtu wako anayeishi hapa yupo wapi….?’ Akauliza askari, kiongozi wao.

‘Hatujui, kama tulivyokuambia, nia ni kukutana naye, kumuhoji, sasa ndio tunakutana na mambo kama haya…’akasema mzee.

‘Ok, sasa hii kazi tuachieni sisi, tutampata tu huyu mtu au kama ni kundi la watu litapatikana tu…’akasema polisi.

‘Itakuwa kama kazi ile ya awali, mpaka sasa hamjamgundua huyo aliyesababisha binti yangu kujiua...'akalalamika mzee.

‘Unajua kazi hizi ni ngumu, hazina ushahidi, hatuwezi kumkamata mtu kwa hisia tu..ila hili sasa limetupatia namna ya kuandaa kesi, ..hapa tuna ushahidi, na huyu mtu tutambana sana, mpaka atatuambia ukweli….haya ni mambo ya imani za kichawi, unanielewa mzee.’akasema huyo askari.

‘Lakini kama ni yeye, asingeliweza kuacha kitu kama hicho humu ndani, nahisi wenyewe kwa wenyewe wanachomeana, hii ni kumkamatisha huyu mtu ili aonekane anafanya hii kazi…’akasema docta.

‘Tutaligundua, unafikiri, ngoja tumkamate, atatuambia kila kitu…’akasema polisi

 Wakati tupo pale mara tukasikia watu wakipiga kelele…

‘Ajali ajali…’

*************

‘Mnasikia huko kuna,  kelele nahisi kuna ajali, imetokea…’akasema askari, akachukua sismu yake na kuanza kuwasiliana na wenzake waliopo huo bara barani,,…

‘Kuna nini huko..over?’ akauliza wakitambulishana kwa maneno yao

‘Kuna mtu kagongwa na gari, yupo taabani,..’sauti nyingine ikasema.

'Ni ajali tu, au kwa makusudi..?’ akauliza.

‘Huyo aliyemgonga hakusimama, na hali ya huyu mtu ni mbaya sana,sizani kama atapona, …’akasema askari mwenzake.

‘Mumeweza kumtambua huyo mtu ni nani..?’ akauliza.

‘Ni nani huyo..’akauliza tena huyo askari. Tukawa hatusikii wanachoongea na huyuu askari akasema;.

‘Oh, ndio tupo hapa nyumbani alipokuwa akiishi , kama ni huyo mtu, na humu ndani tumekuta mambo ya ajabu kweli, nahsi huyo mtu atakuwa akifanya biashara za miili ya watu, muwahisheni hosp na ulinzi mkali, na mjaribu kumhoji hoji asije akafa tukakosa ushahidi..’akasema huyo askari.

Yule askari alipomaliza kuwasiliana na wenzake, akatugeukia na kusema;

‘Huyo mtu mliyemfuata huku, yupo taabani kagongwa na gari...'akasema

'Kwahiyo hawezi kuongea kabisa..?' nikamuuliza

'Hawezi, ..kagongwa vibaya sana..askari wangu wanasema kila wakimuuliza swali anachojibu ni kusema,... ni mkuu, ni mkuu..hivyo tu basi…’akasema docta.

'Mkuu...'nikajikuta nimesema hivyo.

'Mnamfahamu huyo mkuu..?' akauliza polisi

‘Hapana, kama tulivyokuambia awali, hata sisi alituambia hivyo, kuwa anayemtuma ni mkuu, sasa huyo mkuu ni nani, hata sisi hatumfahamu…’akasema mzee

‘Ok…tutamgundua tu…ila huyu jamaa labda asipone, akipona ana kesi kubwa ya kujibu, watu kama hawa ndio tunawatafuta…’akasema huyo askar akipiga simu kuwasiliana na watu wake.

Ikawa sisi hatuna la kufanya,, tuliwaachia askari wafenye kazi yao, na hatukuruhusiwa kuingie tena kwenye hilo jengo,..hata hivyo ni nani angeliingia na  hiyo harufu, tukaambiwa tukae sehemu ambayo itakuwa rahisi kwao kutupata maana tulihitajika kutoe maelezo polisi, baadae tukawa tunajiuliza wenyewe kwa wenyewe....

‘Docta sasa tufanyeje..maana hii ishakuwa kesi, na polisi watakuwa wakitusumbua kama sisi ndio wahalifu?’ nikasema.

‘Ni kazi yao waache wafanye, …na safari hii lazima watagundua kitu….’akasema mzee.

‘Ni mpaka…nahisi bado kuna tatizo..’akasema docta.

‘Kwanini…?’ akauliza mzee.

‘Usicheze na watu wenye pesa, biashara hizi na za madawa ya kulevya, zina mitihani mingi sana..sijui..lakini nimeshaanza kuhisi jambo, ..kwann huo mzigo wa hivyo viungoi vya binadamu ikaletwa na kuweka humo…huoni kuna kitu…’akasema docta.

‘Polisi wenyewe watagundua…’akasema mzee.

‘Sawa tusubirie, lakini sisi hatuwezi kuwasubiria polisi kazi yetu inaendelea, ..’akasema docta.

‘Tutakuwa tunaingilia kazi ya polisi…’akasema mzee.

‘Hapana hatutaingilia kazi yao, ila tutawasaidia,..wewe utaona tu…’akasema docta.

‘Kwa vipi…?’ nikauliza.

‘Sijui kama tutaweza,kupata nafasi ya kumuhoji huyo mtu, kama bado yupo hai ingelikuwa ni bora zaidi, tukaipata hiyo nafasi,  huyo ndiye msaada wetu mkubwa,..’akasema docta

‘Sasa utafanyaje, na wakati huyo mtu atakuwa hospitali na huko atakuwa kwenye ulinzi mkali…’akasema mzee.

‘Usijali, mimi huko ni nyumbani kwangu…’akasema docta.


**********

 Basi baadae docta akasema twende huko hospitalini, 

'Na  tukifika huko, mengine muniachie mimi....'akasema

'Utafanyaje.. kuingia kumuona...?'nikauliza

'Hilo niachieni mwenyewe..'akasema

Kiukweli mimi sikuwa na hamu tena ya kuendelea na hili tatizo, nilitaa hata snisiende huko, lakini baadae nikaingiwa na hamu ya kujua ni nini kitakachoendeela, kwahiyo nikajiunga, na moja kwa moja, tukaenda huko hospitalini, ambapo huyo majeruhi kalazwa..

Tuliambia huyo majeruhi kapelekwa chumba cha wagonjwa mahututi, na docta kwa uzoefu wake wa kidakitari akapata nafasi ya kuingia huko ndani na baadae akatoka, akasema;

‘Bado kazi ni ngumu…ila kuna neno kalisema nahisi linaweza kuwa ni msaada kwetu, kwanza aliniomba nimsaidie kama sijakichoma kile kibuyu chake cha uchawi, nikamwambia akipona nitampatia;

‘Utakipata wapi…?’ nikauliza huyo docta.

‘Ikibii tutamtengezea kingine..’akasema docta.

‘Kwani hatajua kuwa umetengeza kibuyu kingine.…’nikasema.

‘Ok, najua hilo haliwezekani, hata hivyo, huyo mtu sio wa kupona, nilijaribu sana kumdadisii…'

'Kasema nini zaidi..?' nikamuuliza

'Yaani inachukua muda kuongea, ...yaonekana hawakutaka huyu mtu apone, hutaamini nasikia polisi wanadai hawajaweza kulipata hilo gari lilimgonga...'akasema

'Huyo majeruhi alisemaje...?' nikazidi kumuuliza docta

'Yeye kwanza anakiri kuwa kweli kakosea na anatubu madhambi yake...; akasema

'Makosa gani kafanya..?' nikauliza

'Nilimuuliza hivyo, kakosea nini, na atafanyaje ili toba yake iwe sahihi maana anatakiwa kutubia kwa aliowakosea, ...akawa anaongea kwa shida, akisema;

'Najua nimeshachelewa,..ila nakuomba wewe unisaidie  kuniombea msamaha..'akasema

'Kwa nani sasa..mimi siwajui uliowakose...?' nikamuuliza

'Kwa, kwa....wote tu, ...si, si... yaani ikawa hivyo tu, ., hakuweza kusema neno, nashangaa nikimuuliza mambo mengine  anaweza kujibu mengine anakuwa mnzito kujibu...'akasema docta

'Kwahiyo alisema ni nani kamtuma, ...au ni nani ukamuombee msamaha kwa ajili yake..?' nikauliza

'Aliyemtuma anadai ni mkuu,..na huyo mkuu hamjui, wanawasiliana tu kwenye simu, hajawahi kukutana naye uso kwa uso..., yeye akimaliza kazi anatumiwa pesa zake kwa njia ya simu,…akasema zaidi tukitaka twende kwenye facebook,…’

‘Kwenye facebook,,,,?' nikauliza kwa mshangao.

'Ndio kasema hivyo ndio nikamuuliza huyo mtu anatumia jina gani, ?’ nikamuuliza

‘Mkuu,…au..ana wakala zake…mashetani..’akasema.

‘Mashetani,...huyo mtu wa ajabu sana, utawasilianaje na mashetani...'nikauliza kwa mshangao.

'Ndivyo alivyosema, na nilimuuliza hivyo hivyo, akasema wamo humo kwenye facebook, ni wengi na huyo mkuu ana mawakala wake wengi, wenye asili ya namna hiyo..'akasema

'Sasa sisi kama sisi tutawajuaje..?' nikauliza

'Nilimuuliza  hao mawakala wake kama ni mashetani, sisi tutawajuaje...akasema hivi;

‘Wapo wengi tu…wanawake kwa ajili ya kuwapata wanaume na wanaume kwa ajili ya kuwapata wanawake…sifa yao kubwa ni uzuri, mvuto…na wengine..walishakufa ila wanatumiwa vivuli vyao..kuwavuta watu wapya kujiunga na kundi lao
’akaniambia hivyo.

‘Oh….ina maana ..’nikasema.

‘Ndio hivyo,..ulinaswa..’akasema docta alipogundua nataka kusema nini.

‘Haiwezekani..’nikasema.

‘Kama haiwezekani yupo wapi huyo mtu.., mpaka leo ulishawahi kumuona sura yake huyo mtu..’nikasema.

‘Ni nani huyo..?’ akauliza mzee

‘Kuna mtu anamdanganya kwenye mitandao,…kama rafiki, ndio namkanya kuwa watu hao hawaaminiki…’akasema docta,akijaribu kudanganya, sikujua kwanini doct aanamua kufanya hivyo.

‘Ndio maana nilikuwa nawakanya sana mabinti zangu wasiendekeze mitandao ya kijamii, hasa hiyo facebook, wao wanadai kuwa humo unaweza kumpata rafiki wa kuaminika…hata wazungu wanafanya hivyo...’akasema mzee.

‘Kwahiyo walikuwa na marafiki huko kwenye facebook,..?’ akauliza docta

‘Sijui...ndivyo walivyokuwa wakidai,....hayo ni mambo yao vijana..’akasema mzee.

‘Sasa huyo majeruhi katusaidia nini…?’ nikauliza.

‘Nilipomaliza kumuhoji, akapoteza fahamu, na sijui kama aataamuka tena…sasa huko kwenye facebook,kuna nini…ni nani anaweza kutusaidia kwa hili…’akasema docta.
Labda binti yako mzee..’nikasema.

‘Kwa vipi, kwani wewe haupo kwenye facebook, wengi wapo huko, huyo binti yangu ndio anaweza kusaidia nini..hapana msimsumbue binti yangu…’akasema mzee.

‘Hili jambo linahitajia utaalamu wa ziada, watu wanaosshughulika na hii mitandao, wanaowekea watu akaunti zao, au …wepesi wa kubuni picha nak….sasa sijui ni nani hapa jirani mnayemfahamu..?’ akauliza docta.

‘Huyo jamaa anayemiliki, super market ni mtaalamu wa mambo kama hayo, kwanza kabisa ndio ilikuwa kazi yake alipofika, baadae ndio akaajiri watu huku akijishughulisha na biashara hiyo ya supermarket,…sijui kama anaweza kutusaidia..’akasema mzee.

‘Huyo anaweza akawa nyuma ya haya mambo, ukimuendea ni kama umejipeleka mwenyewe, kufichua siri zako,…cha muhimu hapa, ni turudi nyumbani tuone pa kuanzia..’akasema docta, na kweli tukarudi nyumbani kwa Mzee

****************
Mama na bint yake walikuwa wakitusubiria kwa hamu sana,na walipotuona ikawa swali kubwa, kumetokea nini huko..

‘Huyo mtu yupo taabani hospitalini, kagongwa na gari…’akasema mumewe

‘Umeona hao watu walivyo, hawaogopi kuua,…’akasema bint.

‘Watu gani, hao ?’ nikamuuliza na yeye akaniangalia kwa macho ya kushangaa, na kusema;

‘Si ndio hao mnaowafuatilia…..au ningesemaje..’akasema huyo bint.

‘Bint nikuulize kitu,..unamfahamuje huyo mtu anayemiliki super market, ulisema uliwahi kuongea na wewe, akasema anataka kumuoa dada yako,…na alipoona dada yako kafariki akakugeukia wewe, hebu tuambie tunawezaje kuongea naye, au..’akasema docta

‘Wewewewe..acha hiyo usimtumbukize binti yangu kwenye hayo majanga…kama sisi wenyewe hatuwezi basi, tuyaache, tuwaachie polisi…’akasema mzee

‘Sio hivyo mzee…nahis huyu binti yako, anaweza kuwa msaada mkubwa kwa hili jambo, huyo jamaa alitokea kuwapenda mabinti zako, tukimtumia huyu bint…tunaweza tukagundua mengi..’akasema docta.

‘Hapana hilo siwezi kukubaliana nalo kamwe…’akasema mzee.

‘Mzee mimi..nawahakikishia kuwa binti yenu atakuwa salama…mimi nitamlinda, muhimu natafuta jinsi ya kuingia kwenye himaya ya huyo mtu, lakini siwezi kumuingili hivi hivi…binti upo tayari, au unaogopa…?’ akamuuliza binti.

‘Tatizo docta, mimi sitaki tena kuhatarisha maisha ya familia yangu, sitaki kuongea na huyo mtu , kwanza namuogopa, ukimuangalia usoni, utahisii kuwa sio mtu wa kawaida…’akasema.

‘Unavyoongea ni kama unawafahamu fahamu kazi zao…sasa sijui, hebu nikuulize huko kwenye mtandao huwasiliani na hao watu..?’ akauliza docta.

‘Wa nini..kwanini niwasiliane nao…?’ akauliz ahuyo binti.

‘Labda uliwahi kuwa na urafiki nao, wengi wanafanya hivyo, …hebu niambie huyo mkuu hujawahi kuwa na mawasiliano naye..?’ akauliza docta.

‘Sina mawasiliano naye, , na sijazoeana naye, nimeshakuambia hata kuonana naye uso kwa usomnaogopa…’akasema.

‘Kuogopa ndio tatizo…’akasema docta na mara simu ya huyo binti ikaita. Binti kwa haraka akaichukua na kusikiliza..

‘Ni nani, kafa..?’ akauliza

‘Oh, jamani masikini…’akasema

‘Hapana, siwezi, tafadhali siwezi, nilishawaambia, mimi siwezi na sitaki, sitaki.......’akakata simu akionyesha kakasirika

‘Ni nani kafa..?’ akauliza mzee

‘Huyo mpangaji wako, masikini jamani..’akasema kwa masikitiko.

‘Ni nani huyo kakupatia hiyo taarifa..?’ akauliza docta.

‘Ni rafiki yangu mmoja…’akasema na docta aliposikia hivyo, akashika kichwa kama anawaza jambo halafu akasema;

‘Oh, ngoja nimpigie huyo docta anipe taarifa kamili..’akasema na akawa anapiga namba..

‘Mhh..salio limekata…sijui ..nani naweza kutumia simu yake..?’ akauliza na mimi nikajaribu kupiga simu yangu, ikawa haina salio, nikasema;

‘Hata mimi salio limekata, labda tukope..’nikasema

‘Mzee…simu yako ina salio..?’ nikamuuliza.

‘Oh,..ngoja tuagize vocha..’akasema mzee akijipapasa mfukoni, mimi naikagundua kitu, nikasema nikimuangalia huyo binti..

‘Binti kwani simu yako haina  salio..?’ nikamuuliza na yeye kwanza akaonekana kusita, halafu baadae akasema;

'Mhh..sina uhakika, lakini ngoja nijaribu kuangalia...'akasema akiweka namba za kuangalia salio, baadae akasema 

‘Ndio…’akasema huku akiniangalia usoni,

‘Lakini ..sio jingi sana, kwani ulitaka kumpigia mtu wa mtandao gani akasema;

Docta akamtajia namba, na kusema;

‘Usijali, utarejeshewa salio lako….’akasema

‘Ok, hamna shida, ila ….ok, sawa hiyo hapo inaita…’akasema na kumkabidhi docta, docta akasema;

‘Samahani kidogo, akageuka upande wa pili akawa anaongea na huyo mtu, ambaye docta wa hiyo hospitali.

‘Unasema keshafariki..ooh, sory, ..lakini je kuna jamaa yake yoyote aliyewahi kufika hapo, kuulizia labda…?’ akauliza na akajibiwa, baadae akatulia akiwa kageuka upande mwingine baadae akageuka na kumkabidhi simu binti.

‘Sasa sisi tutawaacha kidogo, ila tutarudi baada ya muda mfupi...’akasema docta.

‘Mnakwenda wapi askari walisema watatukuta hapa sote msiondoke mnajua mimi ndio nimechukua dhamana yenu…’akasema mzee

‘Mzee usijali, tunarudi sasa hivi…’akasema docta.


‘Mimi nina wazo docta…nipo tayari kuonana na huyo anayemiliki supermarket, kama kweli itasaidia..’akasema huyo binti.

‘Kwanini..?’ akauliza baba yake kwa mshangao.

‘Kwasababu baba,…naona nisipofanya hivi, kuna hatari ya matatizo..baba, hao watu wanavyoonekana sio watu wema, watu wanaongea mengi…hasa huyo anayemiliki hiyo supermarket, wanadai kuwa huenda anashirikiana na hao wanaoitwa friimason…’akasema na kutulia

‘Watu wanasema tu, kwa vile kawa tajiri au…?’ akauliza baba

‘Lisemwalo lipo baba, mimi naogopa sana,…na jingine angalia kilichomkuta dada, naogopa kisije kutokea kwenye familia yetu tena, ni bora mimi nijitolee mhanga kwa ajili ya familia yetu…’akasema

‘Hapana hilo sikubali binti yangu, mimi ndio wakujitolea muhanga, sio nyie, hata mama yako hawezi kukubali, hivi kaenda wapi…’akasema baba

‘Yupo jikoni..’akasema binti

‘Baba hili usimwambie mama, mimi nitashirikiana na hawa watu mpaka kieleweke, najua, ni kazi ya hatari…lakini, sitaweza kutuliza akili yangu, na kichwa changu, kama hatutaweza kulipiza kisasi cha dada yangu,..mimi nimefikiria sana, na sasa nimeamua,  nipo tayari kujitolea,…’akasema

‘Mimi kama baba yako nimesema hapana, …’baba yake akasema kwa hasira na mama akatokea, na kukuta baba mtu akifoka hivyo.

‘Vipi tena, kuna nini..umesema hapana kwa jinsi gani , kuna nini kinachoendelea, mniambia, sitaki kufichwa kitu hapa…’akasema mam

‘Mama hakuna kitu…mimi nataka niende kwenye huo msiba..’akasema

‘Msiba gani..?’ akauliza mama
‘Si huyo mpangaji wetu…’akasema

‘Tutakwenda wote, tusubirie utaratbu utakuwaje…’akasema mama,

‘Sawa,…mimi nipo tayari, mkiwa tayari mniambie, nipo chumbani kwangu mara moja..’binti akasema akiondoka kuelekea chumbani, na mimi na docta tukabakia pale, na docta akasema;

‘Binti anajua jambo…na hivi sasa huenda anawasiliana na hao watu, najua kwanini anafanya hivyo, lakini tumpe muda, hata hiyo ya kusema atashirikiana na sisi, sio kweli anachofanya ni kuvuta muda,…sasa sijui kwann…kuna hii namba walimpigia, nataka tuipige , tujue ni nani kabla hajawasiliana nao..’akaniambia kwa sauti ya chini, na kuanza kutoka nje, mimi nikabakia na mara binti akaja akiwa na haraka..

‘Docta kaenda wapi…?’ akauliza akionyesha wasiwasi mkubwa

‘Yupo kaenda kujisaidia…’nikasema

‘Hapana nimeshamjua,….kachukua namba ya simu anataka kupiga,…’akasema sasa akitaka kutoka nje

‘Wewe binti niambie kuna nini unaficha…’baba akasema kwa ukali

‘Hakuna kitu baba, nafanya haya kuwalinda nyie…baba, ni hatari, …’akasema huku akikimbilia nje, baba akamuangalia mkewe, na mkewe hakupoteza muda, mbio akatoka nje kumfuatilia binti yake…..


NB: Je binti anaweza kulifanya hili.

WAZO LA LEO:Ukiuona uhalifu, ukiuona ubaya, na una uhakika nao kuwa ni ubaya kuwa ni uahalfu,…wewe ukanyamaza kimia, na ukijua uhalifu huo utaleta madhara kwa jamii au kwa mwenzako, ujue na wewe utakuwa umehusika kwa namna moja au nyingine. Tumeambiwa, ukiuona ubaya, tuuondoe kwa mikono yetu, yaani tuchukue hatua, au tuukemee, au tukishindwa kabisa tuuchukie, lakini kuchukia tu moyoni ni udhaifu, ni vyema tukachukua hatua, tukaisaidia jamii.

Ni mimi: emu-three

No comments :