‘Halloh …sijui
nikuiteje, manake mwanzoni ulikuwa dada yangu, rafiki yangu mpendwa, lakini kwa hivi sasa,
nashindwa nikuiteje,.....lakini hilo tuliache,….’akatulia muongeaji kwenye
simu, na mpokeaji akawa kimia tu...
‘Nimeamua
nikupigie simu tu, ili nikueleze yaliyopo moyoni mwangu,…nimekuwa nikijiuliza
iweje haya yatokee, …je ni mpango wa nyie watatu au ni mpango wa wawili, na
wewe ukawa mtendwaji…na sijui unajisikiaje moyoni mwako, ukiyafanya hayo
unayoyafanya sasa, ni ujanja au kunikomoa mimi…sijui, labda ndivyo wanawake
tulivyo kusahau,… labda…
‘Sasa mimi ninakuomba
unisikilize tu…, najua mtendewa hawezi kuuhisi uchungu,kama yule
aliyeathirika...kwani aisifuye mvua imemnyea, na siri ya mtungu aijuaye ni kata…'
Mpokeaji sio kwamba hawezi kujibu,,..anajua sana kujibishana, hata mpigaji wa simu anamfahamu kuwa yeye ni hodari wa kuongea, na mpigaji hamuwezi kabisa kwenye kubishana, lakini mpokeaji akaona ni vyema kubakia kimia tu, kusikiliza tu....
‘Mwanzoni nilipoambiwa una mtoto anafanana na mtoto wangu, nilijua ni kawaida tu,
maana hata wanaume wetu wanafanana,..nilifurahi kuwa urafiki wetu umekomaa, na
maneno ya watu nikawa nayapuuza…nikijua wewe ni rafiki yangu huwezi kamwe
kufanya kitu kama hicho..lakini…
‘Nasema lakini
maana haya yamekuja kujitokeza baaadaye, na baada ya kujitokeza ndio
nikakumbuka jambo, siku za nyuma kuna mtu aliwahi kuniambia, kuhusu mume wako…’akatulia
‘Yeye aliwahi
kufanya kazi hospitali, ambayo mume wako alikuwa akitibiwa, na yeye alikuwa
kitengo cha vipimo, na siku moja aliona vipimo vya mume wako, kuwa ana matatizo
…na kwa utaalamu wake, aliyagundua hayo matatizo kuwa ukiwa nayo huwezi kuzaa
tena…’akatulia.
‘Kuna kipindi
fulani nilikupigia simu, nikitaka tuongee, lakini kukawa na sintofahamu nyingi,
tukashindwa kuongea, na hata ulipofika huko kijijini, nilikuambia hebu tafuta
muda tuongee, lakini ikawa hawezekani, na nilishangaa umebeba mimba, unakumbuka
niliwahi kukuambia mume ni mwingi wa rehema kaamua kuwaumbua watu na vinywa
vyao,…nilikuwa na maana hiyo kuwa huyo aliyesema mume wako hazai ni mwongo,…’akatulia.
‘Kiukweli
matatizo aliyokuwa nayo mume wako, yasingeliwezekana yeye kuzaa…liniambia
ukweli maana hayo nimekuja kuyajua tena baadae…’akatulia
‘Baadae sasa umejifungua
mtoto, na mtoto huyo anafanana na mume wangu…kama nilivyokuambia nilipoambiwa
kuhusu hilo nilipuuzia,..sikuwa na akili ya kufikiria hayo maelezo ya awali…kiukweli
sikulikumbuka hilo kabisa, nikajua mtoto wako, ni wangu pia, nikajawa na furaha…’akatulia
‘Watu wakazidi
kunisakama, kwa hilo..mpaka kero..basi ikafikia muda nikawaambia,,,kama
imetokea hivyo, mtoto wako anafanana na mtoto wangu, basi ni bahati nzuri, maana wewe ni rafiki yangu, na hayo
wanayoyasema ni uzushi, maana wewe huwezi kamwe kunisaliti…na kama imetokea
kufanana, basi ..yaishe…nikijua ipo siku tutakutana utaniambia ukweli…’akatulia.
‘Nilitamani
nije tukae, nikufariji tu, tuyaache tu yapite…kama yalivyo maana mtoto wako ni
wangu, ndivyo tulivyokuwa tukiishi, na…nikashukuru mungu, lakini moyoni nikawa
najiuliza iweje hilo lifanyike nyuma ya mgongo wangu, kwanini usiniambie…’akatulia
‘ Nilijua kwa
vile wewe ni mwanake kama mimi, utalijutia hili, ukatubu. Nilijua wewe ni
rafiki yangu, dada yangu, tuliyeshirikiana nawe, utakuja kuniambia ukweli..,
nimesubiri wee, lakini haijatokea na baadae ndio ukweli ukaanza kudhihiri, kuwa
kumbe haikuwa bahati mbaya, kumbe wewe na mume wangu mlikuwa na ajenda yenu ya
siri…’akatulia.
‘Kwanini isiwe
hivyo, mtenda kosa hutenda mara moja, akirudia kakusudia, je hujawahi kutembea
na mume wangu tena na tena..kama hiyo ya kwanza ilikuwa ni bhati mbaya…,
nikuulize, lakini kwasasa sitaki jibu , maana nimewaona wewe na mume wangu mara
nyingi tu, yeye anajitetea kuwa anakuliwaza, haya anakuliwaza mpaka
kitandani,..., nimewaona kwa macho yangu..hebu niambie kama ingelikuwa wewe
ungelijisikiaje, urafiki upo mpaka kuchangia waume, mbona mimi sijawahi
kutembea na mume wako kama ingelikuwa ni hivyo…’akatulia
‘Tuyaache hayo
labda mimi ni mjinga,nakumbuka sana kauli yako, uliwahi kuniambia awali, kuwa mume akitembea nje, basi mke umeshindwa
kazi…labda mimi nimeshindwa kazi, kazi unaijua wewe…lakini kumbuka wewe ni
mwanamke kama mimi, …kumbuka haya yanayotokea leo, yaweza kutokea kwako, kwa
watoto wako …kumbuka hilo…’akatulia
'Nakupigia simu
hii sikuwa na nia ya kukushutumu, najua kama umedhamiria, hata nikuambieje
hutanielewa, maana sikio la kufa halisii dawa, ila natoa neno muhimu kwako, sisi ni wanadamu
tu, hapa duniani ni mapito…, wangapi waliyafanya hayo wakaishi milele, hakuna….
tutayafanya hayo na mwisho wake tutarejea kwa muumba wetu,hakimu wa mahakimu…na
hata hapa duniani, muumba anaweza kutoa adhabu yake, sikuombei mabaya,..hapana
, sivyo mungu alivyotuusia,ila elewa, mateso gani ninayoyapata ..elewa hilo….
‘Na sasa
nakuusia wewe na kujiusia mimi mwenyewe, kuwa tumuogope mungu..najua ipo
siku...haki itatendeka...
' Jingine ni
hili, nimesikia mwanao ameamua kudai haki yake,…unaona yaliyokuwa ya siri sasa
yanaanza kuwa dhahiri, yanaanza kututesa sisi wenyewe, nasikia kuwa kijana wako
ameanza kumfuata mume wangu na kumfanyia visa, ili ikiwezekana mali yote
aichukue yeye..je hamjui kuwa hiyo ni dhuluma, mnawanyang'anya hata wale wenye
haki yao...
Nakuelezea
hili, ninajua wewe ni mzazi kama mimi, mwanangu anarudi mungu akipenda, hivi
karibuni, na haya yanaweza kuzua vita, mimi sitaki vita, mimi sitaki
ugomvi..kama lengo lenu ni mali, basi fanyeni taratibu stahiki…, mje mchukue,
kama ni haki yenu, ilimradi tu mtuachie amani...nawaomba tena sana, mimi sitaki
fujo…umenisikia hilo njooni kwa utaraibu mseme mnataka hiki na hiki, basi
mchukue..si haki yenu mnayodai…au mnatakaje!
‘Na kama wewe
unamtaka mume niambie, kwanza mimi nilishaondoka hapo nyumbani ili niwaachie
nafasi,..mume huyo hapo nyumbani mchukue, na mliweke hilo hadharani kuwa wewe
sasa ni mke wa mume wangu, ..au mnataka nini , mimi siwaelewi,...hamtosheki
jamani!
‘Dada, au mke
mwenzangu, nayaongea haya maana yanazidi kuwa mabaya kila kukicha,..sasa
nisipoongea leo, labda huko kesho nitakuja kulaumiwa,…mueleze mwanao, kama
anahitajia hiyo haki yake,basi ajitambulishe rasmi, kwa wahusika, kuwa yeye ni
mtoto wa mume wangu na anahitajia kadha wa kadhaa, au sio..tulielewe hilo,
lakini sio kwa hivyo anavyofanya yeye, anatuumiza na sisi tusiokuwemo kwenye
mambo yenu..
‘Yeye anapita
akiimba wimbo wake, kuwa kitanda hakizai
haramu…wenye akili tulishamuelewa, …sasa muulize anataka nini…..umenisikia,
muulize, kama lenu ni moja, haya njooni kwa utaratibu unaofaa mseme mnataka
nini…..’simu ikakatika.
Mama dereva
akabakia ameshikilia simu masikioni, akahisi vitu vikimpanda na kushuka,
akahisi kutapika,akihisi kulia…lakini mwili ukawa kama umekufa ganzi, akabakia
vile vile kwa muda…
*********
Wakati mama anaongea
na simu, mtoto wake alikuwa kasogea na
kusimama kwenye dirishani akawa anaangalia huko nje, akibuni mambo yake, na
kuyaweka sawa kichwani, alijua mipango yake imeshakamilika iliyobakia ni muda
tu, akiwasili wakili wake anakwenda kumaliza kazi,…
‘Mama ananiwekea
kiwungu tu, lakini atanielewa, hili ni lazima lifanyike, apende mama, asipende,
yeye atakuja kujua mengine baadae…’akasema kwa sauti ndogo, na hapo akageuka
kumuangalia mama yake, na kumkuta akiwa kaganda..kashikilia simu sikioni,
lakini haonekani kama yupo sawa, akahisi kuna tatizo
‘Mama ina maana
bado unaongea na simu..bado unaongea na mama yake Soldier..?’ akauliza, lakini
hakupata jibu, mama katulia tuli.
Dereva
akamsogelea mama yake, na kuichua ile simu mkononi mwa mama yake, simu haikuwa
hewani, akamshika mama yake mara mama huyo anadondokea sakafuni..
‘Hee mama vipi
tena..’ akasema huku akili ikianza kuchanganya, akajua mama yake hayupo sawa,
akamshika shingoni kuhakikisha kama mapigo yapo sawa…
' Mama
nini...umepatwa na nini mama…?'akamtikisa tikisa..lakini mama alikuwa kimia..
Haraka
akachukua simu yake na kumpigia docta anayemfahamu, akamuelezea dakitari jinsi
ilivyo kwa mama yake, na dakitari akamuelekeza ni nini afanye kama huduma ya
kwanza, akajitahidi kufanya hivyo na,
baadae mama yake akafungua macho.
'Mama kumetokea
nini?'akauliza, lakini mama yake
hakufungua mdomo…alikuwa kimia tu.
Dereva
akachukua simu ya mama yake na kuangalia huyo mtu aliyekuwa akiongea na mama
yake, alijua kuwa ni mama yake Soldier.
Akaipiga ile
namba huku hasira zikimchemka, akilini anatafuta maneno makili ya kuongea, mtu
anaymemuumiza mama yake kamuumiza yeye…
‘Halloh, mimi
ni dereva, umeongea nini na mama'akauliza kwa hasira.
,
'Muulize
mwenyewe,… kwani hawezi
kuongea?'akaambiwa
'Mama alikuwa akiongea
na wewe, na alipomaliza kuongea na wewe, akapoteza fahamu, umemfanya nini mama
yangu, unajua hali yake lakini…sasa umemfanya nini mama yangu...'akawa anaongea
kwa hasira
'Sikiliza
dereva, nasikia wewe ndiye mshawishi mkubwa kwa mama yako, lengo na nia, ni
kuhakikisha mumemfirisi mume wangu...kweli si kweli?…sasa hayo yanayompata mama
yako , kwa hivi sasa sababu kubwa ni wewe…jiulize wewe mwenyewe umefanya nini….'akatulia
‘Nimefanya nini…nilishawahi
kuongea na wewe kukuambia lolote..?’ akauliza
'Sasa ni hivi,..mama
yako nimemuambia hivi, kama lengo lenu
ni mali, si ndio unataka hayo, mali…sasa fanyeni hivi, tafuteni utaratibu mnzuri tu, kama ni wakili,
kama ni wazee mje kwa ustaarabu, mseme mnataka nini…mnataka hiki na kile,…mtapatiwa,..au
kama mnataka mali yote, sawa mtachukua,.. si ndio unalolitaka hilo, ndio
nimemuambia mama yako kama kashikwa na kihoro, cha fuaraha au nini sijui...'akaambiwa
.
'Mama mimi
sijawahi kuongea na wewe kuhusu mali, mimi naongea na mzee, nisingelipenda wewe
uingilie hayo kati, maana wewe na mama yangu hapa, nawaheshimu sana, nafahamu
kabisa nyie wawili hamna hatia, na yote yaliyotokea ni sababu ya wazee wetu,…marehemu
na mume wako..lengo langu ni kuwaweka kwenye mstari sahihi..baba hayupo duniani
ni marehemu lakini mume wako yupo, aubebe mzigo wake...'akasema.
‘Je katika
kuubeba huo mzigo unahisi anauweza kuubeba mwenyewe, wakati ana familia, unajua
fika wakipigana mafahali zinazoumia ni nyasi, unafikiri ni nani anayeahirika na
hayo yote,…sasa tusipoteze muda, kama mama yako keshaamuka, yupo sawa, mwambie
mpange siku mje, ….unasikia, na jingine kunaweza kuwepo na sherehe ya
kuwakaribisha waliokwenda huko vitani ,hakikisha kuwa unakuwepo wewe na mama
yako…’akataka kusema lakini mara simu yake ikachukuliwa wangu wangu, na mama
yake.
Mama yake kumbe
alikuwa kazindukana vyema, na akaja kwa nyuma na kumnyang’anya Dereva simu,..
Na kwa haraka
akaanza kuongea na mama yake Soldier.
‘Wewe mwanamke
wewe…., nimekusikia, sitaki tena neno kutoka kwako…achana na mimi , achana na
mwanagu, sitaki kuongea na wewe tena, na wala sitaki, siwataki,
nawachukia..nyote nyie siwataki tena …umenisikia…’akasema
‘Ni…’mwenzake
akataka kuongea.
‘Na mume wako
asikanyage tena hapa kwangu, akija nitamnywesha sumu,…mwambia hivyo, unanisikia, naona akiwa hai atazidi kunifuata
fuata, je niliwahi kuja huko kwako kumfuata mume wako…yeye ndio kila siku kiguu
na njia kuja hapa kwangu..nilimuita, kama umeshindwa kumuhudumia mume wako
mwambie akatafute wanawake wengine, wapo wengi mitaani, kwanini ananing’ang’ania
mimi..umesikia…’akasema
‘Hahaha..naona
sasa umeshapona, kauli yangu ni hiyo hiyo, ..kama mnataka mali, njooni kwa
utaratibu , mwambie mwanao…mje,..na kama wewe unamtaka mume wangu, niambie..usijifanye huhusiki,
usijifanye kuwa yeye ndiye anakufuata fuata, kwanini kama anfanya hivyo
usiniambie mimi mwenyewe, lenu moja,,…’mwenzake akasema na mama mtu akaitupa
simu chini…na kuanza kutembea, akielekea nje…
‘Mama unakwenda
wapi……
NB: Haya ya
akina mama yakianza …
WAZO LA LEO:
Mnapoingia kwenye ugomvi,mkawa hamuelewani, muhimu kwenye ni kuvuta subira,
kila mmoja atulie sehemu yake atafakari kwanza ni nini faida ya ugomvi huo, na
nini athari zake, na ikizidi sana watafuteni wenye hekima wawasuluhishe,
msizidi kujengeana chuki, visasi,…na uhasama, kwani kwa kutenda hayo mnazidi
kumfurahisha ibilisi na mwisho wa yote nyote mtaadhibiwa mbele ya mola.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment