‘Mzee hilo peke yake la kuwa ulifanya hivyo ni kashfa kwako, ulifanya
nini na mke wa mwenzako , tena rafiki yako,..ni swali ambalo litakuharibia sifa
yako, ...je ni kwa makubaliano, kama ni kwa makubaliano mbona mama hajui....au ulimuhadaa baba, kwa vile mnafanana naye,..haingii akilini...'akatulia
Sasa hilo ni tisa, kumi , hili....hili la sasa mzee, sijui utaiambiaje jamaii, mzee, utakufa kwa presha,…fikiria sana, lakini nipo kijana wako nipo, nitakusaidia , ila…’
akasema.
‘Acha nife…’nikasema nikiwa natamani kusema maneno mabaya lakini
sikuwa na ujanja, huyu kijana anajua jinsi gani ya kumshika mtu pabaya, nishaanza kumuogopa,...na umri huu tena, sikutaka changamoto za namna hii...ningekuwa na bastola, lolote lingelitokea...kanimaliza....
‘Mzee usiseme hivyo, wanaoo tunakupenda, …. ndio maana nataka
kukusaidia,...'alisema.
Kweli msaada aliotoa ulikuwa wa namna ya kumfanya huyo mtoto aweze kupata maziwa, yaya wa kumlea, tiketi zao..lakini najua gharama hizo nitakuja kuzibeba mimi, najua kuna jambo lipo mbele yangu..nikawa nasubiria, hata nikiwa kwenye ndege, nikajua kuna mtego, hilo la kupewa huyo mtoto nk..ni sehemu tu, ni lazima kuna jambo kubwa litatokea huko mbele, sijui ni jambo gani
Tuendelee na kisa chetu…
**************
Mtoto alipoanza kulia tu, mara mwanadada mmoja akatokea, akiwa na kikapu..ndani yake kuna vifaa vya mtoto, maziwa nk...akanisalimia, na kujitambulisha,... sikuwa na zaidi, nikafungua mlango wangu na kuingia ndani, baadae naye akaingia...
Mipango ya mtoto kuondoka na mimi ilishapangwa na Dereva, ajabu kabisa,
na hata huyo yaya aliyeletwa huo usiku alikuwa keshakatiwa tiketi yake…kweli
jamaa alijiandaa, alikuwa na uhakika kuwa hayo yote yatafanyika na mimi
nitakubaliana nayo,..na najua ana maana yake, na gharama hizo nitakuja kuzililipa, sijui kwa vipi..
Hata hivyo nilishukuru, maana ningelifanyaje na huyo mtoto, na alishaanza kulia…
Huyo yaya…alipofika tu, akamnywesha huyo mtoto maziwa aliyoyatengeza kwa muda mfupi tu, naona alikuwa kaisomea hiyo kazi...,
mtoto akanywa na hatimae akalala…,
‘Kwahiyo huyo mtoto utakwenda kulala naye chumbani kwako…’nikamwambia
‘Wapi bosi, ...?' akaniuliza
'Hakukuambia aliyekutuma...?' nikamuuliza
'Hapana yeye kasema nije hapa, nianze kazi ya kumhudumia mtoto na mengine yatafuata , ndio nasubiria,....bosi 'akasema
'Haya mimi najipumzisha, sasa wewe ...utalala wapi, ...?' nikauliza
'Mimi nitakaa hapa hapa kwenye sofa,...kwasababu, nasubiria maagizo, yenu....'akasema
'Sawa...'nikasema nikiliza kichwa kwenye mto.
Mawazo mawazo..usingizi wa mang'amu ng'amu, tunasubiria,....muda ukafika, tukaondoka kwenda uwanja wa ndege, taxi ilishafika, ...
Tuliondoka hapo kama kawaida na kufike maeneo ya kwetu, na nilipoteremka
uwanja wa ndege tu haraka, nikachukua usafiri wa kuelekea huko kijijini
anapoishi mke wangu, sikutaka kufika kwangu na huo ugeni, nitasemaje watu
wakiniona na huo ugeni na watu ni wepesi sana kunasa mambo.
Haya haraka tukafika ukweni, na uzuri huko nilikuwa na nyumba yetu niliyojenga
na hapo ndipo mke wangu alikuwa akiishi, ni hatua kidogo kutoka hapo ndio
makazi ya wazazi wa mke wangu.
Mke wangu aliponiona, alinipokea tu kama mgeni, huku akionyesha macho
ya mshangao na huo ugeni, hakusema kitu, akahakikisha huduma muhimu zipo, hasa
kwa mtoto,…mimi nilikuwa nimekaa sehemu ya nje kwenye mti, sikutaka hata
kuingia ndani.
‘Mbona huingii ndani..?’ akaniuliza
‘Kuna mambo nataka tuyaongee kabla sijaingia huko…’nikasema
‘Ina maana unaondoka leo hii..?’ akaniuliza
‘Ndio, nahitajika…kufikisha kile nilichotumwa huko ….leo hii,
…’nikasema, akilini nikijua nina mambo yangu natakiwa kuyaweka sawa, na
nikiendelea kukaa hapo, maswali yatakuwa mengi, ambayo sina majibu yake. Na ….
Mara mke wa Soldier akatokea….
‘Hee huyu mke wa Soldier yupo
huku….?’ Nikamuuliza mke wangu, na moyoni nikawa nakumbuka maneno ya Dereva…
‘’….Ndio maana nimekuambia wewe
ulifanye hivyo, kwa kukusaidia,..mchukue huyo mtoto maana ni damu yako, rudi
naye kijijini kamtafute mke wako…na huko utamkuta mke wa kijana wako
ameshafika,kwanza muulize alikuwa wapi…’’
‘Ndio amekuja huku, anaogopa kuishi na wewe , umemfanyia vituko vya
aibu…hata sijui wewe mwanaume wa namna gani…hata mke wa mwanao…..’akasema.
‘Amefika tokea lini…’ nikamuuliza bila kujali hicho alichoongea, maana
kweli nikilewa nakuwa ….hata sielewi.
‘Sio muda mrefu, lakini hana raha kabisa, nimejaribu kumuuliza ana
nini hataki kuniambia…nafikiri ni mambo yako, hebu niambie ulimfanya nini..?’
akaniuliza.
‘Mke wangu mimi sijamfanya kitu, na wala sielewi, kuna muda nilikuwa
nalewa..kuondoa mawazo, sasa sijui…..naombe mke wangu unisaidia…nahitajia
msaada wako mkubwa sana…’nikasema.
Pamoja na yote ninayoyafanya, mke wangu ananipenda sana, ni mwanamke
mwenye huruma, sana, na nilivyoongea hivyo akawa keshanielewa kuwa nipo katika
hali gani. Kukawa na ukimia kidogo, halafu mimi nikasema;
‘Oh…kumbe ni kweli..’nikasema, na wakati huo mke wa mwanagu alikuwa
anakuja kunisalimia.
‘Kweli kuhusu nini, kwanza hebu niambie huyo binti na mtoto mchanga
umetokea wapi, usiseme umempa mwanamke mwingine mimba na unataka kuniletea
mizigo huku…huyo mtoto mchanga mnafanana naye….uniambie ukweli, ili tuachane
kwa amani…’akasema
‘Huyo ni mtoto wa Soldier..’nikasema kwa kujiamini.
‘Eti nini…?’ aliyeuliza hilo swali ni mke wa Soldier alishafika mbele
yangu kunisalimia.
‘Eti nini…mtoto wa nani,…?’ akauliza mke wangu, sasa naye akianza
kuchanga changanya macho, najua sasa anamuhofia mke wa Soldier, atalichukuliaje hilo...na huenda moyoni atakuwa akinilaumu kwanini nimeongea hilo mbele ya mke wa Soldier
Tukasalimiana na mke wa mwanangu, halafu yeye akasogea pembeni
akisubiria maelezo, na mimi sikutaka kuongea naye kwa muda huo, nilitaka kwanza
niongee na mke wangu , niyaweke mambo sawa, hata hivyo, bado nilikuwa na
maswali muhimu kwa huyo mkwe wangu:
‘Ngoja niongee na mama yako, atakuja kukuambia kinachoendelea, msijali
tutayamalizia haya mambo ambayo yametokea huko…, sijiu kinachoendelea mpaka
sasa…maana habari ni nyingi sana, muhimu tuzidi kumuomba mungu mtoto wetu awe
salama..unasikia, muombee sana mume wako…’nikasema
‘Kwani ulisikiaje…?’ akauliza huyo mke wa Soldier.
‘Mengi tu…..atakuja kukuambia mama yako, nikimaliza kuongea naye, au
unasemaje,..?’ nikamuuliza mke wangu.
‘Sawa, hata sielewi, umeshanichanganya….’akasema mke wangu.
‘Ile mke wa mwanangu, nakuomba sana, ufanye utakavyoagizwa, kuna mambo
nitakubaliana na mama yako, ujitahidi kuyafuata …vinginevyo, sijui itakuwaje,
mume wako anaweza kuwa matatani..’nikasema
‘Mhh…mimi sielewi…mambo yenu, nimekuja mara moja tu kumsalimia mama,
nitaondoka…’akasema
‘Kwani wewe ulikuwa wapi muda wote huu, mwaka na kitu...hujui wewe umeolewa...?' nikamuuliza
‘Nilikuwa kwa wajomba zetu, nchi ya jirani…’akasema
‘Nchi ya jirani, huko wanapoishi wakimbizi…!!!?’ nikamuuliza na
kichwani nikaanza kuhisi huenda aliyoyaongea Dereva yana ukweli, lakini
..haiwezekani kuwa kulewa kwangu niliweza kumfanyia ….hapana, siwezi, huwa
kweli nalewa, mpaka napitiwa, lakini…oh, mbona ni aiabu hii…!
‘Lakini mbona hukutuambia,unajua bado upo kwenye mamlaka yetu,
ulitakiwa ukisafiri umbali huo tujue, unajua kiasi gani nilivyohangaika
kukutafuta…nikipiga simu kwenu hawataki kupokea…, mtu umeondoa
nyumbani..unasema una kwenda kwenu, kwenu haupo, kuna nini ulikwenda
kufanya,huko…?’ nikamuuliza na niliombea kama kuna ukweli wowote asije kuusema
mbele ya mke wangu.
‘Baba, ..ilibidi niondoke, ..wewe mwenyewe unajua, nisingeliweza
kuvumilia, …na kuna jambo muhimu nilitakiwa kwenda kulifanya huko kwa
wajomba..nilikuwa sina jinsi…’akasema.
‘Mambo gani..?’ akaulize mke wangu kwa hasira kidogo.
‘Siwezi kuyasema,…mama nilishakuambia, muda ukifika nitayasema yote,
lakini sio sasa, naombea huyo mume wangu arudi salama, akiwepo, ….ndio
nitaongea,…naombeni mnielewe hivyo…’akasema.
‘Ulikuwa na nani huko nchi za jirani…?’ nikamuuliza, na akawa kimia,
mke wangu ikabidi aingilie kati na kusema;
‘Mimi naona hayo niachie mimi, nitaongea na mwanangu, najua anahitajia
muda, sisi wanawake tukikwazika, huwa hatutakiwi kulazimishwa…ila kama kuna
lolote uelifanya kwa mwanangu hapa, tafadhali, …ujue itakuwa haina mjadala,
hivi sasa nipo tu, sijaweza kuyaongea yote kwa wazazi wangu….’akatulia.
‘Ina maana umewaambia wazazi wako kuhusu matatizo yetu...?' nikamuuliza.
‘Niwaambie nini, ..huo uchafu wako, kama wengelisikia, sizani kama
wangelinikubalia tena, nirejee kwako, nasubiria muda muafaka mwanangu arudi,
akirudi, ..hapo nitatoa kauli yangu ya mwisho…’akasema.
‘Mke wangu unajua tumetoka mbali, unanifahamu sana , na siwezi kuishi
bila yaw ewe, mengi yanayotokea ni kwa vile upo mbali na mimi..nakuomba sana,
usije kunifanya nikapoteza maisha,…ooh…’nikataka kupiga magoti mbele ya mke
wangu, lakini nilipogundua kuwa mkwe wangu bado yupo hapo, nikasita.
‘Samahani ….naomba faragha…’nikasema na huyo mke wa mwanangu akaondoka
shingo upande, najua alikuwa na mambo …na alikuwa hakafahamu kuwa kuna ugeni
mwingine, mtoto…alikuwa hajaonana nao hadi muda huo.
‘Nasikia kama kuna sauti ya mtoto mchanga..’akasema akimuangalia mke
wangu.
‘Ndio,…sijajua ni nani hao, nitakuja kukuelezea, nenda wapo chumba cha
wageni…’akasema mke wangu.
Baada ya mke wa Soldier kuondoka,….nikakimbilia kupiga magoto mbele ya
mke wangu, yeye akageukia upande mwingine akisubiria maelezo.
‘Mke wangu mimi nitakueleza kila kitu, muhimu ni subira, tuombe mungu mtoto
wetu arudi salama maana taarifa za huko hazieleweki,…lakini pamoja na hayo, nakuomba
sana, univumilie mke wangu, naapa kuanzia sasa nitabadilika…...’nikasema.
‘Hayo ulishayaongea sana..utabadilika ndio wimbo wako ukikosea, sasa
yabidi na mimi nichuke hatua, nasema mtoto wetu akirudi, hutaamini
nitakachokifanya, na…hilo …la huyo mtoto, kama ni wako, ndio itakwua ushahidi
wa uchafu wako,…..’akasema.
‘Huyo ni mtoto wa Soldier, hunielewi…’nikasema.
‘Na huyo mke wa Soldier ulimfanya nini…?’ akauliza
‘Je kuna kitu kakuambia kuwa nimemfanya lolote?' nikamuuliza kwa kujihami, nikiombea kusiwepo na kitu kama hicho...labda sio kweli, labda..labda..hata mimi sijui ukweli halisi!
**********
Ilikuwa kazi kubwa ya kumshawishi mke wangu kuwa huyo mtoto ni wa
Soldier, na haijulikani alimpataje, kwahiyo yeye afanye juhudi za kuhakikisha
mke wake anampokea huyo mtoto kama wake na kumlea, na afanye hivyo,..mpaka hapo
mume wake atakaporudi, na yoyote atakaye muuliza aseme huyo ni mtoto wake…
Mimi ikabidi niondoke nirudi nyumbani kwangu,…
Wakati nakaribia nyumbani kwangu nikaona mtu amekaa kwenye kiti changu
cha enzi, kuna kiti changu nimekitengeza kwa magogo, huwa napumzika hapo nikiwa
napunga upepo, na huyo mtu alikuwa kava kofia kubwa, kama la yule mtu
niliyemuona kule hotelini.
Nilihisi mwili ukiniisha nguvu…nikahisi hatari, nikahisi mashaka…ni nani
huyu, ni yule jamaa, nikazidi kusogea, na mara yule mtu akajua ni mimi,
akajigeuza na kunielekea, akavua kofia, na kusema;
‘Shikamoo mzee, nimekusubiria sana….’akasema.
Alikuwa ni Dereva, mtoto wa
rafiki yangu, alikuwa nje ya nyumba akinisubiria, utafikiri alijua kuwa
nitarudi siku hiyo…unajua imefikia hatua nikimuona huyu mtu naanza kuingiwa na
mashaka, shinikizo la damu linaongezeka,…ananipa shida kweli, natamani nifanya
jambo…nim-malize, keshakuwa ni adui yangu moyoni.
'Hiyo kofia uliyovaa, ni kama yule mtu uliyemtuma kule hotelini....'nikasema
'Yah, ...ni kofia zetu, za kujikinga na jua...'akasema
Na kiukweli kwa hali niliyokuwa nayo, sikutaka kuongea na mtu, lakini
niliona niongee naye ili nihakikishe mambo fulani fulani,..niujue ukweli na ni
ni dhamira yake, kwahiyo nikawa mnyonge.
‘Umefika saa ngapi..?’ nikauliza.
‘Mzee, nimefika tokea asubuhi,…niliwasili…na ndege ya pili, baada ya
nyie kuondoka na mimi niakingia ndege ya pili yake…kuna mambo muhimu nmekuja
kuyaweka sawa… nilikuwa na mama nyumbani nimemalizana naye…, baadae nikaja hapo
kwako, nikasema siwezi kuondoka mpaka tuongee…’akasema.
‘Haya sasa umekuja na kipi
kingine, maana nia yako ni kutaka kunimaliza, si ndio..unimalize kimaisha,
nifiriskike,….si ndio hata nikifa ni sawa kwako…’nikasema.
‘Mzee, nilitarajia wewe ungenipongeza kwa juhudi niliyoifanya, kwanza
nikuulize mama (mke wako) na mke wa Soldier wamesemaje..?’ akaniuliza, najua
anafahamu nimetokea huko.
‘Watasemaje,…mambo hayo umezua wewe, na haijulikani ukweli wake ni
upi..’nikasema
‘Mzee, hivi kweli huyo sio mtoto wako,..niambie ukweli mzee, maana
nikitaka kuutafuta huo ukweli nitaujua tu, na si unanielewa zangu..’akasema
akiniangalia usoni.
‘Unajua uwe na heshima, mimi nawezaje kutembea na mke wa mwanagu,
nimelogwa…’nikasema
‘Haaah, labda ulikuwa umelewa ukapitiliza...mimi hata sielewi..ni aibu
sana mzee, ni jambo ambalo unatakiwa ucheze karata vyema vinginevyo ,
utaumbuka,…sasa hayo yapo mikononi mwako
kwa hivi sasa,mimi nimejitahidi kufanya hivyo ili kukusaidia,…’akasema
‘Kunisaidia au kuniangamiza….?’ Nikauliza
‘Mzee, utaelewa tu, ila,…kuna kitu nimekuja nacho hapa…’akasema
‘Kitu gani tena…?’ nikauliza
‘Ile nakala ya DNA, unayo..?’ akaniuliza
‘Nimeichana..’nikasema, ni kweli niliichana-chana kwa hasira.
‘Hahaha, …nilijua kuwa utafanya hivyo, ile ni nakala tu, halisia yake
bado ninayo…lakini ulichofanya ni sahihi kabisa…sasa nimekuja na nakala
nyingine ya DNA, ya kuthibitisha jambo jingine,…’akasema.
‘Ya nani, ya mtoto…?’ nikauliza sasa miguu ikinicheza cheza, na wakati
huo, jamaa alikuwa akiitoa kwenye kibegi chake, taratibu.
‘Usiwe na wasi wasi mzee, unajua nilishakuambia mimi ni mtoto wa
mjini,..na kila jambo kwetu ni dili..umeonaeeh, sasa, utaniamini kuwa mimi
sijazaliwa leo, naona mbele na nyuma, na ujue, kuwa mimi sifanyi mchezo,
nikuakuambia jambo ujue nimeshalifanyia kazi..’akasema.
‘Ohh..kijana...unanitafuta sana, hatasijui nisemeje,...lakini we ngoja tu...'nikasema na yeye akatabasamu tu.
‘Usichoke mzee..ngoja tuyamalize haya kwanza, halafu utakwenda kulala,
upumzishe kichwa chako ukiwazia, ni nini ufanye, …’akasema.
‘Hii hapa ni nakala ya DNA,….’akasema akinikabidhi.
‘Ya nani tena….?’ Nikauliza huku nikisita kuipokea,
NB: HAYA, NINGELIENDELEA LKN MUDA, NA SALIO.
WAZO LA
LEO:Ulevi ni mbaya, ulevi huondoa akili ya kawaida ya kufikiria kihekima,
na wengine huchanganyikiwa kabisa,…na wanaweza kufanya mambo ambayo wakiwa na akili
zao za kawaida hawawezi kufanya… na wengine wanajitetea kuwa wanakunywa ili
kupunguza mawazo. Hivi unapunguza mawazo au unayasubirisha mawazo…ulevi ni moja
ya silaha ya shetani,..ukiingia kwenye shabaha yake umeangamia!
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment