Unajua kuwa kuna mambo ukiguswa, hata kAma upo na ujasiri gani, utatikisika
tu, unaweza ukajibaragua lakini moyoni, utakuwa na vishawasha vya uoga,
kiukweli nilianza kuogopa, ..kwanza nikaanza kujishuku mwenyewe, je kweli mimi nipo
sahihi….nikajikuta nikijilaumu kuwa mwenendo wangu usio mnzuri, ndio maana haya
yananitokea..
Ikafika nikaamua niongee na familia tuweze kuuza sehemu ya ardhi
tuliyokuwa nayo..tuliwahi kununua mashamba, na mwenzngu yeye aliuza uza maeneo
yake ili kupata pesa ya matibabu. Kutokana na hali ngumu, nikaona na sisi ni
wakati muafaka wa kuuza sehemu ya shamba,…
Wanafamilia hawakulipinga hilo ombi langu, ila hawakufahamu kuwa mimi
pamoja na hayo nina ajenda ya siri…sikuwa na namna nyingine ya kupata pesa,
tukauza eneo, na pesa ilipofika mkononi, nafsi ikaniambia hii pesa ni jasho la
familia, usiigawa bure, ..nyingine ikaniambia, fanya uliyoagizwa, utakuja
kuumbulia na kazi , umauurufu wako wote utaingia nyongo, na wakati nawazia hayo
mara simu yangu ikaita, kuangalia mpiigaji
ikawa ni ile namba isiyo na namba..
‘Haya niambie unataka nini tena..?’ nikauliza
‘Hiyo pesa ifikishe kwa muuza duka yule chotara, mwambie ni deni la kijana wa marehemu rafiki
yako atakuelewa…’akakata simu, hata kabla sijaweza kuongea lolote.
Oh, sasa akili ya kiaskari
ikaanza kufanya kazi, ukitaka kumshika mwizi, kwanza anza na yule unayemshuku,
huyo anaweza kuwa ni njia ya kumpata mwizi wako, kwahiyo mimi moja kwa moja
nikamuendea muuza duka kwa vitisho..
‘Mzee mbona unanichanganya,…mimi mwenyewe nimepokea ujumbe kuwa wewe
mwenyekiti utanileta pesa, ya sehemu ya deni ninalimdai huyo jamaa’ akasema.
‘Kwahiyo mpo kundi moja…’nikasema.
‘Mzee ni hivi huyo jamaa mimi namdai sana, pesa nyingi tu,…na sijui
kwanini isku hizi hanilipi kama zamani, alikuwa mwaminifu sana, anakopa
analipa……….na jana ananitumia ujumbe wa maneno, tana sijaufuta kuwa wewe
utakuja kuniletea hizo pesa yeye kasafiri, nashukuru sana kama umekuja
kupunguza hilo deni..
‘Unamdai shilingi ngapi…?’ nikamuuliza
‘Milioni mbili…’ akasema.
‘Milioni mbili!!! …wewe, alikopa pesa zote za nini hizo..?’ nikamuuliza,na
yeye akaanza milolongo mrefu, kumbe deni hilo limeanzia kipindi baba yake akiwa
hai , yeye derva alikuwa akifika hapo, na kukopa bila baba yake kujua, kwa
ajili ya kununua dawa,..au mahitaji amengine, akawa analiendeleza hilo deni, akipata pesa
anapunguza, ikafika muda anakopa tu…mara hiki au kile…
‘Kumbe hata hiyo ajenda ya kuwa anadaiwa ada ilikuwa ni sababu tu ya
kupata pesa ili kupunguza hilo deni, na mara ya
mwisho ndio akaja kukukopa kwa ajili ya safari…na wewe ukamkubalia tu,
kwanini ukubali na deni unaliona ni kubwa sana..?’ nikamuuliza.
‘Bosi mimi namuamini sana huyu mtu, analipa,..huwa anakopa analipa,
..sina wasi wasi na yeye, sema kwa sasa hivi naona kafikwa…sijui ana tatizo
gani, kwani hata alipokuja kuniona alionekan hana raha…’akasema.
‘Na alikuambia anafanya kazi …maana kukopwa pesa nyingi hivyo, utakuwa
na uhakika kutokana na kazi anayoifanya…?’ nikamuuliza.
‘Mimi sijui kazi yake,….ila anakuwaga na pesa nyingi, na siku nyingine
anakuwa hana pesa kabisa, ndio anaishia kukopa…’akasema.
‘Sasa nataka uniambie ukweli, la sivyo nitawapeleka polisi…’nikasema
kwa ukali.
‘Kwa kosa gani mzee, kwa mimi
kudai haki yangu,..?’akasema akishangaa.
‘Kudai haki yako kwangu mimi, kwani mimi nilikuja kwako kukopa, au
kuwa madhamini, wa huyo tapeli mwenzako …’nikasema.
‘Mzee mimi kama kuja kwako ningelifika kukuuliza tu, kutokana na taarifa hii ya ujumbe wa simu,
vinginevyo, ningemsubiria tu mwenyewe akija, mimi sina shaka naye, nina uhakika jamaa atakuja
kunilipa pesa yangu, mimi sijui kwanini kasema wewe ndiye utamlipia, hayo ni juu yako wewe na yeye…’akasema
‘Kwahiyo mnafahamiana naye sana..?’ nikamuuliza.
‘Ndio..nafahamiana naye kama mteja wangu..alikuwa akifanya shughuli zake anakuja dukani kwangu
anakopa, analipa, yeye ni fundi mnzuri wa magari, na mimi napeleka gari langu
analitengeneza vizuri,…namkopa, namlipa tumejuana hivyo tu, lakini undani wa
maisha yake mimi sijui…’akasema.
‘Unamwaminije mtu kama huyo ambaye hujui wapi anapotoka maisha yake
yapoje..nahisi kuna kitu kati yako na yeye..’nikasema.
‘Mzee,..mimi sina zaidi, najua ipo siku atakuja kunilipa deni langu,
kama alikosea kukutaja wewe kuwa ndiye utamsaidia, kulipa, basi samahani mzee,
hakuna shida, mimi ninayemdai ni yeye, sio wewe…ila aliniambia nitazipata
kutokea kwako…’akasema
‘Alikupatia picha uniletee mimi..?’ nikamuuliza
‘Picha!...mzee picha gani …mara ya mwisho kuonana naye ni kipindi
alisema anasafiri, na hakuwahi kunipa picha zozote, mzee. samahani je hizo pesa
unazo, au huna, nilitaka kupunguza deni kwenye dafutari la madeni…’akasema
akiwa anafungua fungua hilo daftari, nikalichukua hilo daftari, nikaanza
kulikagua kweli niliona mtiririko wa hilo deni, tokea tarehe za nyuma,
linalipwa linaongezeka..
Kiukweli, ikabidi nitoe pesa, japokuwa sio kwa kiwango hicho alichodai
yeye…, lakini, zilinitoka, nikasema ahueni kumba nasaidi kitu ambach hata
rafiki yangu angelikuwepo ningakifanya…baada ya kutoa pesa hiyo,..nilipofika
nyumbani nikapokea ujumbe wa kushuru, na hali ikapoa,…ila moyoni nikaahidi kulifuatilia hilo mpaka nijue mwisho wake, hawawezi kuchukua pesa yangu hivi hivi tu...
Kiukweli badae kukapoa, sikuwahi kuona rabsha nyingine kutoka kwa huyo kijana hadi
karibia mwaka mnzima, kuonyesha kweli alikuwa kasafiri,...Tatizo kubwa lilikuwa kati yangu na mke wangu, familia yangu hatuongei na huko kwa shemeji nako
nikawa najiiba siku moja moja..nikifika huko kuna wakati naambulia matusi, kuna
wakai tunaongea..siku zinakwenda.
************
Muda ukafika Soldier akaja nyumbani kuoa…
'Ehe, unataka kuoa mchumba unaye tayari au tukusaidie kutafuta?' nikamuuliza
'Ninaye tayari keshakubaliana na mimi..nilionana naye kwenye safari zangu...'akasema
'Wa huku huku au huko maeneo mengine?' nikamuuliza
'wa huku huku mzee..'akasema
'Ni nani au anatokea familia gani..?' nikamuuliza.
'Ni kutoka familia ya Matatizo,...'akasema
'Nani...wewe una laana...'nikasema kwa mshangao, tulikuwa tunakuala hamu yote ya kula ikaisha..Maana hiyo familia, haina maelewano na familia yetu tokea kizazi na kizazi,...ila huyo binti yao, alikuwa msichana mnzuri tu...mwenye tabia nzuri wengi wanamfahamu.
‘Kijana..hilo unalolitaka ni laana, unajua mababu watatulaani, maana
haijatokea hata siku moja familia yetu kwenda kuoa huko au wao kuja kuoa kwetu, ni mwiko....ni wewe wa kwanza..’nikamwambia.
‘Basi mshukuru kuwa mimi nimeondoa hilo tatizo,..hayo ni mambo yenu ya kizamani, tufike mahali tuachane na tabia hizo za chuki...sasa tuwe
marafiki…’akasema.
Pamoja na sisi kukubali, upande wao ilikuwa nishida, kuna kaka yake na huyo binti, ni aadui mkubwa sana wa familia hii, na waliwahi kugombana na soldier, na uhasama wao ukawa wa kudumu, haya mwanangu anataka kuoa huko..ilikuwa ni kazi kweli, lakini watoto wameshapendana, utafanyaje..
Huku na huko ikafikia hatua, inabidi maadui wakae meza moja,…kujadili maswala ya ndoa huku tumekunjiana sura…huwezi amini, tukaja kukubaliana na tendo hilo likafanya familia yangu na familia ya huyo adui yangu wa siku nyingi, tuweze kusahau ugomvi wetu na kuwa kitu kimoja, kwa ajili ya kufanikisha sherehe ya watoto wetu..ila huyo mtoto wao mkubwa, alisema moja kwa moja yeye, na familia hii ni kama maji na mafuta..
Kiukweli hata mimi nilikubaliana na familia hiyo, ilimradi tu yaishe, kumrizsiha kijana wetu maana alishafikia sehemu kijana wetu hataki kuoa tena, sasa alipokuja na ombi hilo, tukamkubalia, ila pale alipotaja ni nani anataka kumuoa kutoka kwa familia gani, hapo, ilikuwa ni kazi kutushawishi.
Familia hiyo tulikuwa hatuelewani nayo tokea enzi, kisa ni ardhi, mipaka, na huko nyuma mababu zetu waliwahi kupigana na kumwaga damu, kwahiyo kukajengeka visasi…
Mwisho wake, tukakubali tu, watoto
wakaoana,..na haikupita muda, mara taarifa inakuja, kuwa Soldier ni miongoni
mwa watu waliochaguliwa kwenda vitani kwa kupitia mikataba ya kimataifa,..safari
hizo wengi wa maaskari wanazitaka sana kijana wetu alikuja kutupatia hiyo
taarifa akiwa na furaha nyingi tu…, maana japokuwa ni hatari lakini ukirudi
angalau unaweza kuitwa mtu..
Ilikuwa sio furaha kwetu kama wazazi, hasa mimi ninayefahamu ni nini
maana ya vita, lakini moyoni, kimaongezi, nilikuwa nawaambia watu huo ni
uzalendo. Na ukumbuke ndio kijana wetu katokea kuoa, hata miezi mitatua
haijaisha,..tuliombea angalau atupatie mjukuu, sasa ndio anamuacha mkewe mikononi
mwetu, anakwenda vitani, na vita ni vita…mama yake alikataa kata kata, lakini
atafanyaje, mwisho wa siku tulikaa pamoja kama familia tukamuombea duwa,
akapata baraka zetu, akatuachia mkewe…
************
Mwaka ukapita , na sasa familia ya mkewe kijana wetu ikawa inaleta
malalamiko , kwanini tumemuoa mtoto wao anakaa tu na wakwe, kwani sisi ndio
tulimuoa,… mume wake yupo wapi,… kama kafa huko vitani kwanini hatusemi, binti
yao arudi kwao,....ikawa ni shida kweli…lakini tunamshukuru mungu kwani mkwe
wangu, binti huyu alijitahidi sana
kuvumilia kwani alikuwa akimpenda sana mume wake..
Mimi kama kawaida yangu nilijitahidi kuwa karibu naye, inafika sehemu
najifanya sio mkwe, ilimradi tu asijisikie mpweke, nahisi tabia kama hiyo, yeye
na wengine, ndio wakaanza kuitafsiri vibaya, lakini ndio tabia yangu ya
ucheshi,....ndio siwezi kukataa, kuwa katabia kwa kuchepuka sikuweza kukazuia..lakini
sio mkwe wangu!
Basi mwaka wa pili tukapokea taarifa kuwa kikosi kilichopelekwa huko,
kimevamiwa na kuna baadhi ya askari wetu wameuwawa….hapo tukawa tumbo joto,
tukawa tunawasiliana na makao makuu, laki hakukuwa na taarifa rasmi…, lakini
tetesi zikaja kuwa miongoni mwa waliouwawa ni mwanangu…siku hiyo ilikuwa ni
kilio..nyumba ikabadilika,..mama, mke wa kijana wangu….mimi kiukweli niliiona
taarifa hiyo kama sio kamilifu.
Nilijua akilini mtoto wangu hajafa, na kama ameuwawa, basi amekufa
kishujaa,..si yupo vitani…ndio nitaumia sana moyoni, lakini ndio mungu kapanga
iwe hivyo utafanyaje…, lakini hata hivyo, jambo kama hilo likitokea ni lazima
tutapewa taarifa iliyo rasmi,hatukuwahi kupokea taarifa kama hiyo, ni tetesi tu,
uvumi tu..siku zikaenda..
Siku moja,…nikapata safari ya kwenda nchi ya jirani,.. jirani yetu ana
wakimbizi wengi wa vita, unajua vita vinavyoendelea huko, kwahiyo huko kuna
kambi za wakimbizi, ..nilifika huko kwa mualiko, kama kiongozi mmojawapo,..na
tulipofika huko nikawa mmoja wa waongeaji, …mimi ni mpiganaji mstaafu kwahiyo
nafahamu mambo ya kivita..ndio maana walinipatia nafasi hiyo...
Baada ya vikao, ..kukutana na watu ikafika muda wa kujipumzisha,
kwahiyo nikaelekea hotelini kwangu,..nilipofika nikahisi nywele
zinanisisimuka,..ni hulka yangu tu, ikitokea hivyo, naweza kukutana na kitu
kisicho kuwa cha kawaida, ningekuwa vitani, ningechukua ‘cover..’ kujihami, lakini nipo uraiani,..nikajipa moyo,
..nikaangalia huku na kule,..baadaye nikajirizisha, na kuelekea hotelini
kwangu.
Nikiwa natembea kwenye corido za hiyo hoteli,..mbele ya chumba changu
niliona mtu kakaa nje ya mlangoni wa chumba changu,..kwanza nilitaka kurudi
kuwauliza mapokezi, ni nani huyo, ..akili ya hatari imeshanicheza, lakini
nikasema labda ni muhudumu tu, nikatembea kwa tahadhari hadi pale mlangoni.
Kwanza nilihisi mwili ukinicheza,…ni mtu au ni jinni…kafikaje hapo,
kapitaje kule mapokezi, maana kuna sheria ngumu hapo hotelini, huwezi kuja
kumuona mtu hapo mpaka huyo mwenyeji apewe taarifa, akubali, na wanapingwa sana
kuingia humo hotelini ni wakimbizi, na jinsi nilivyomuona huyu mdada,
yawezekana akawa na mkimbizi, vinginevyo, basi sio binadamu!
Nilijiuliza maswali mengi kichwani huku natembea mwendo wa taratibu,
kuvuta muda, kabla sijafika pale mlanngoni, nikajiuliza ni kwanani wakati nachukua
ufunguo pale mapakozi, wahudumu hawakuniambia kwua nina mgeni, labda sio mgeni
wangu, sasa ni kwanini aje kukaa kwenye mlango wangu..…yawezekana ni mtego…hapo
nikasimama kidogo..
Lakini baadae nikaanza kutembea kumkabili huyo mtu, kwani ni
mwanamke..nilivyomuona kwa mbali..hiyo hoteli ni kubwa,…ina vyumba vingi vya
wageni,…nikasogea hadi kwenye chumba changu, nikamuangalia huyo mtu…
Alikuwa mdada, kajifunika kitu kama shuka nyeupe, imechakaa,..na kuna
sehemu ya nyingine kwenye hiyo shuka ni kama imeungua,…na kuna alama za damu
damu, hapo mwili ukazizima, damu zimetokea wapi, na ule mkao ni wa masikitiko, mtu anakaa
miguu inakuja karibu na kichwa, kainama hataki kuniangalia… inatia huruma
kumuona, ..
Na kitu kilichonivuta hisia zangu zaidi ni pale nilipoangalia pembeni yake,
kuna kitoto kichanga..
NB: Tuendelee baadae.
WAZO LA
LEO: Kuna watu maisha yao ni Ujanja ujanja, kuwarubuni watu, kuhadaa
kudanganya, kutumia mbinu za mdomo kupata kipato kutoka kwa wengine..ukimuuliza
anasema, anatumia elimu yake, anatumia ujuzi wake kupata riziki…huo ni wizi,
tujaribu kupata kipato halali, kwa njia halali, zisizo za hadaa, mtu alipwe
kutokana na huduma, tusiweke mitego, mfano utakuta watu wanaandika, mwishoni masharti
kuzingatiwa wakiwa wameka mitego kuwa ukikosea kidogo, pesa yako imeliwa.
JAMANI tumuogope mungu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment