Nikasogea mezani na kuchukua ile barua, taratibu nikaitoa
kwenye bahasha, na maandishi ya kwanza niliyoyaona, ni….’ninasikitika…’ kichwa
kikaanza kuuma, nikawa sioni maandishi..mara giza…nilichokumbuka ni kauli …
‘NISAMEHE MAMA, sikufanya makusudi…’, nikazama kwenye giza!
Nilipoteza fahamu,………..
Nilijikuta nipo hospitalini…nikatibiwa siku kadhaa baadaye
nikatoka, na nilipofika ofisini, kama barua ilivosema, mimi sasa sitakuwa bosi
tena, na nafasi yangu ataichukua mwenzangu, na mimi nitakuwa msaidizi wake,
..huku uchunguzi ukiendelea, na ikibainika kuwa ni uzembe wangu, hatua zaidi
zitachukuliwa, nikawa sina jinsi ….
Basi siku zikaenda, nikakubaliana na hiyo hali…
Siku moja narudi
nyumbani jioni, mtoto wangu kipenzi
analalamika macho yanamuuma,..hapo nimechoka na kazi za ofisini ambazo
zinanichanganya sana bosi wangu ananifanyia vitwimbi, lengo niondoke kabisa…sasa
nimerejea nyumbani sijaweka hata mkoba, mtoto analalamika macho, …kwahiyo hilo
la mtoto kulalamika macho, nikalidharau tu, na sio kawaida yangu, mimi huwa
nawajali sana watoto wangu, lakini siku hiyo nilichoka sana.
Nikajilaza kwenye kochi, kausingizi ka mang’amu ng’amu,…namuona
mtoto wangu ananililia anatoa machozi ya damu…ilikuwa ndoto fupi tu, nikafunua
macho,..kweli mtoto alikuwa kasimama pembeni ya sofa, analia..macho, mama macho…
Nikamnawisha, na kumweka dawa ya macho, nikijua ni matatizo
tu ya kawaida, huenda kaingiwa na michanga…
Inafika usiku mtoto wangu analia,…anasema haoni vizuri..nikaanza
kupaniki, hapo sasa nikawa sina ujanja, ikabidi nimkimbize hospitalini usiku
huo huo..,..walimuangalia, wakaona hakuna tatizo..akapewa dawa, tukarudi
nyumbani akalala hadi asubuhi..nikajua akimuaka atakuwa safi..
Kesho yake mtoto analalamika haoni vizuri…unajua,kuchanganyikiwa…
nilianza kuwaza mbali, kwanza kazini kuna matatizo, sasa shida ya
mtoto….nilianza kulia, …nililia, nikikumbuka kuwa nina tatizo jingine mimi na
mume wangu hatuelewani kabisa, na imefikia kama tumetengana naye, anaishi kwake
na mimi kwangu, hapo sina mtu wa kunisaidia…! Utaona umuhimu wa mume kipindi
kama hiki cha shida…
Hapa naingia natoka….nifanyeje.
Na siku hiyo kazini kulikuwa na kikao muhimu sana, nikikosa
kufika siku hiyo, nitaeleweka vibaya sana,..na huenda nikafukuzwa kazi kwani
nimeshaonywa mara nyingi kwa barua, na utakuta makosa yenyewe sio makosa hasa
ni uzembe wa watu wengine nabeba mzigo wa lawama mimi,…baadaye sijui kwa vipi…nikakumbuka…
Iilinijia tu kama fikira… , nikamkumbuka yule mama aliyekuja
ofisini siku ile,…sijui ilikujaje mpaka nikamkumbuka…,
Unajua nilichofanya, nikasema hayo ya mwanangu namuachia
mungu,, nikaondoka kwenda kazini, nikamuachia mfanyakazi wangu maagizo ya
kumuhudimia mwanagu,…nikawahi ofisini…, nilipofika ofisini tu.., nikaitafuta
ile barua ya yule mama, nikaanza taratibu za kufuatilia kuhakikisha yule mtoto
anasoma…nikamwandikisha ‘private candidate…’
Pamoja na kipato changu kidogo… , lakini nilimsomesha huyo
mtoto , bila ya hata yeye kujua, au wazazi wake kujua hadi akafikia chuo kikuu…wao
wanajua labda ni huduma za hiyo ofisi,…ofisi isingeliweza kumsaidia, kwani
alishafeli….mimi nikatumia gharama zangu akasoma hadi chuo kikuu, huko
nikamuachia mungu, maana alifanikiwa kuwa miongoni mwa wanafunzi waliopewa mkopo…
Sasa tukirudi kwa mtoto wangu hali ya macho ilimtesa
sana..nilihangaika naye, ikafikia sehemu nikakakata tamaa kabisa kabisa..,
maana,..alishafikia sehemu haoni, ni kama kipofu…anaona kidogo sana….basi ikawa
mimi na ibada tu kumuomba mungu tu…
**********
Siku moja nipo nyumbani mara mtoto wangu anakuja, keshakuwa
mkubwa kiasi, yupo kidato cha nne, anakaribia kufanya mitihani…nashangaa
mwanangu anafuraha ya ajabu, nikamuuliza ni nini kilichomfurahisha hivyo, maana
yeye muda wote ilikuwa kulalamika tu.., kwanini mama, kwanini imekuwa hivyo,
ina maana mimi sitaona tena…maneno ya kunitesa tu,..sina la kufanya mimi ni
kulia tu.
Sasa leo anakuja na furaha tele,…nikamuuliza ‘mwanangu
umefanikiwa nini huko shuleni,..?’
‘Mama mimi naona kabisa…’akasema kwa kujiamini.. na kwa
kunihakikishia, akaanza kunisomea kwenye kitabu chenye maandishi ya kawaida,…sikuamini,
nikamuuliza imekuwaje…maana kusoma ilibidi atumie lenzi kubwa anaishikilia mkononi
ndio asome….
Akasema; Alikuja kijana mmoja, yeye anasoma chuo kikuu, ni
mtu wa dini sana, …akasema yeye anaombea watu wenye matatizo ya macho maana
hata yeye alitibiwa kwa kuombewa, na alimuomba mungu ampe kipaji hicho cha
kuwaombea watu wengine..na kweli mungu akamjalai akapata hicho kipaji, kwahiyo yeye
sasa anapita mashuleni kila akipata nafasi, kuwaombea wenye matatizo kama hayo, ndio
kaniombea na mimi nimepona mama…ahsante mungu…’akasema binti yangu.
‘Anaitwa nani…?’ nikamuuliza nikiwa na furaha moyoni, unajua
furaha…
Akanitajia jina,…nikamkumbuka yule kijana niliyemsomesha,
jina lake ni hilo hilo…nilimwambia mwanangu twende kwa huyo kijana, ..ukumbuke
muda huo sijawahi kukutana naye, na wala hajui kuwa mimi nilijitolea kumsomesha
hadi akamaliza kidato cha sita…na sikutaka afahamu kabisa, maana nilikuwa
nalipa dhambi nilizozifanya..
Unajua mpaka leo,
sijaonana na huyo kijana, maana
alisafiri kwenda nje, kwani alipata msaada zaidi wa kusoma nje, …ila bado
natafuta siku nije nionane naye…nina hamu sana ya kumuona, hasa mama yake pia
angalau niwaombe msamaha..’ akamaliza.;
‘Kwahiyo hayo yaliyokupata usikate tamaa, mkabidhi mungu,
yeye anajua ni kwanini imetokea hiyo, kama wamekufanyia hujuma,…mungu mwenyewe
anajua cha kufanya,..muombe mungu tu…na amini nikuambiayo, malipo ni hapa hapa
duniani..na kamwe haki ya mtu haipotei bure, hata aweje, hata yule unayemuona hafai, ana haki yake, usiwe wewe ndiwe chanzo cha kumfanya ateseke.....’akamalizia.
WAZO LA LEO: Enyi
mlio kwenye madaraka, ogopeni kuwatendea vibaya wenye madhaifu ambayo
hawakupenda yawapate,..ogopeni kuidhulumu nafsi ya mja…waja wa mungu nikiwa na
maana wale wenye madhaifu ambayo hawakupenda yawapate, ….kuwatendea ubaya watu
kama hao, ni madhambi makubwa sana,…na adhabu yake huanzia hapa hapa duniani,…utazaa,
au wewe mwenyewe yatakukuta,..timiza wajibu wako, lakini usije kuweka chuki
yako kwa waja wa mungu, ogopeni sana dhambi hiyo ya kiburi na dharau…!
NIMEWAKILISHA TUKIO NA UJUMBE HUO
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment