Ilikuwa usiku sana, watu
wengi walishaondoka, na ndipo Soldier akapata nafasi ya kwenda chumbani kwake,
kulala,…mkewe akawa bado anashughulika na wenzake, bada ya muda mkewe akafika,…alitaka
kumuongelesha, lakini alikumbuka mkewe alivyomuomba kuwa leo hataki kuongea
kitu chochote,…kibusara akaona sawa, ngoja avute subira tu, lakini ikafika muda
akaona anashindwa kuvumilia,alimuangalia mkewe alivyolala, akatamani kumuamusha
waongee, lakini akasita…akasema.
‘Kesho itafika,….mtaniambia kila kitu la sivyo…’akasema na kujigeuza
upande mwingine, ...macho yalikuwa manzito sababu ya usingizi, lakini kila
akijaribu kulala anajikuta akiwaza hili na lile, kichwa kilikuwa hakina amani
kabisa
‘Kwanini mama hajaniambia kitu…sasa anaumwa, sijui anaumwa nini…mke
wangu naye hataki kuongea, halikadhalika baba, wote wanasema kesho kesho ..kuna
nini hapa..?’ akajiuliza, hakuzoea mambo ya kusubiria,…akajiinua pale
kitandani, na kusimama, akachungulia nje dirishani,…
‘Natamani nitoke nje….’akasema, lakini akaona akitoka nje,
anaweza kuondoka na kwenda sehemu nyingine na huenda akajikuta akifanya mambo
ambayo hakutaka kuyafanya…’sitaki nije kushawishika kulewa….’ Akasema na kurudi
kitandani…
Tuendee na kisa chetu…
************
Alipofika kitandani akasogeza mkono akitaka kumuamusha mkewe, ili
angalau waongee kidogo…lakini akasita, mkewe anapenda kulala sana, akiweka
ubavu kitandani usingizi tayari, na hapendi kuamushwa…akasita kufanya hivyo,
kwa vile alijua mkewe alikuwa kachoka sana, kazi walizofanya siku nzima ya leo,
ni lazima takuw akachoka sana,…na wakati anamuangalia mkewe, mawazo yakarudi
nyuma, akakumbuka alipokwenda kuonana na mama yake kwenye shughuli, pale
alipomfikia na kumkuta analia, alimsalimia akaitikiwa,…lakini baada ya salamu,
mama yake hakutaka kuongea zaidi.
‘Mama anaonekana ana jambo nzito sana, ni jambo gani..ni kuhusu
mke wangu na mtoto, je ni kuhusu baba….mmh, hata sijui, lakini lazima nifahamu,
na najua nisipoingilia kati mama ataumia
sana…lakini kwanini baba anafanya hivi…mimi sijui baba anafaidikka nini na hali
hii…?’ akawa anawaza..
‘Ngoja nijaribu kulala…’akasema kwa sauti ndogo, na kuanza
kuutafuta usingizi, …na mara taswira ya mama yake ikamjia akiongea….
****************
‘Mwanagu nashukuru umerudi salama, najua kuna mengi umekutana
nayo huko ulipotoka na sasa unahitajia muda wa kupumzisha kichwa chako….kapumzike
mwanagu, mengine yaacha kwanza kama yalivyo….nafahamu kabisa una maswali mengi na
unahitajia majibu na ufafanuzi…, lakini nakuomba kwa leo usiniulize kitu,..hapa
nilipo sina amani,..unielewe hivyo,…’mama yake akasema na kusimama
‘Mama lakini siwezi kuwa na amani nikikuona katika hali kama hiyo…kuna
nini, na kwanini unalia?’ akamuuliza mama yake akimuangalia usoni, na mama yake
akawa anamkwepa wasiangaliane.
‘Hata mimi siwezi kuwa na amani nikikuona katika hali hiyo, mimi
ni mama yako, japokuwa umekuwa mkubwa, lakini bado hisia za umama zipo ndani
yangu…naumia nikikuona, …ila nielewe tu, amani yako ndio itanifanya mimi
nitulie…’akasema
‘Mama kuhusu mimi usijali, nimeshakuwa mkubwa sasa, .na kama
kuna matatizo nina haki ya kuyafahamu, maana matatizo ni sehemu ya maisha,
nimetoka vitani, huko ilikuwa ni kufa kupona, sembuse hapa, …hapa hakuna
milipuko ya mabomu au bunduki, zijazungukwa na maadui, kwahiyo mama, nawaomba….mama
nakuomba kuhusu mimi usiwe na shaka…’Soldier akajaribu kkumpoza mama yake, japokuwa
moyoni alijua hana amani.
‘Mwanangu, ya vita ni mengine,..hayo yanaonekana na yana mwanzo
na yana mwisho wake…, ila haya ya hapa sijui kama yatakuja kwisha, nimechoka
nayo ….oh, hebu kwanza niache, nikapumzike kidogo…wewe nawe kampumzike tutaonana
kesho mungu akituamsha salama…’mama yake akasema akianza kuondoka.
‘Lakini mama, mimi nakutegemea wewe, uniambie kinachoendelea,
tuongee kwanza kabla hujalala, unajua mama tukiweza kuyaongea matatizo ndio
inakuwa mwanzo wa kujua jinsi gani ya kupata ufumbuzi, ..baba kaniambia ..’
kabala hajaendelea mama akamgeukia na kumkatiza maneno…
‘Sitaki kusikia maswala ya baba yako hapa….sitaki hata kuongea
naye leo,..huyo achana naye, isingelikuwa ni wewe, ..na huyo mkeo, na…na mtoto,
ningelisharudi kwetu, lakini mimi ni mama, mimi ni mwanamke, nimeumbwa kupata
mateso na kuyavumilia,..mangapi tunaumia nayo, ya maumbile na hata ya
kimaisha,..haya ndio maisha yetu, uchungu, kuumia na kuvumilia, yanapita na tunayasahau,
ndio maana nimevumilia ili kupatikane muafaka kwanza,kabla sijaamua la kufanya…’akaanza
kuondoka.
‘Mama..mama…inaonekana kuna tatizo kwanini unasema hivyo..’Soldier
akawa anamfuata mama yake kwa nyuma,… lakini kabla hajafika mbali, akashikwa began
a mtu…hakumuona alipotokea, maana sehemu ile kulikuwa ni varanda ya kuelekea
sehemu ya vyumba….alihisi maumivu kutokana na huo mkono ulimshika, ulikuwa kama wa chuma, na huyo mtu aliyemshika
anaonekana hana amani naye, …Soldier akageuza kichwa kwa hasira kumuona huyo
mtu …
‘Vipi mbona unanishika….’akasema na kabla hajamaliza uso wake
ukakutana na uso wa shemeji yake, kaka wa mke wake,Mshari…
‘Karibu kijijini kwetu, …mimi Mshari, umenisahau…’akaambiwa,
sasa wakiangaliana uso kwa uso.
‘Ahsante, lakini,…tutaongea baadaye nataka kuongea na mama
kwanza…’Soldier akasema akitaka kuondoka lakini jamaaa akamshika mkono, …huyu
jamaa mkono wake ni mkavu, una nguvu, na akikushika lazima uhisi maumivu, ..
‘Mama hawezi kukusaidia , najua kuna tatizo, lakini matatizo
mengine huwezi kumkimbilia mama, wewe ni mwanaume,pambana kiume, usidekedeke
hapa kwa mama…’akasema shemeji mtu.
‘Sikuelewi…unataka kusema nini, na tafadhali sitaki kuivuruga
siku yangu, unajua umuhimu wa siku hii…’akasema Soldier, maana anamfahamu huyo
jamaa kila wakikutana wanaishia kugombana.
‘Aaah..nani kasema anataka vurugu,..mimi nipo nyumbani kwenu,
mimi ni mgeni tu hapa,…sikupenda kuja hapa ni bab tu kanisihi, ..na hasa
aliposema mdogo, hana raha, ninajua kweli hana raha….sasa mimi sitaki kuvunja
heshima ya ugeni, ila ikibidi sitaacha kufanya lolote, na sitajali kuwa wewe ni
askari, uaskari wako ni huko huko…unanielewa, ninachotaka kuuambia ni
hiki..…’akawa sasa akimtoboa toboa kwa kidole kifuani, ..mpaka soldier akahisi
maumivu, na kusoge nyuma huku mkono mwingine ukitaka kuzuia mkono wa huyo jamaa
asiendelee kumtoboa toboa na kidole.
.
‘Unataka kusema nini…?’ akauliza Soldier, sasa akiwa tayari kwa
lolote, alishaona jamaa anataka kumkalia kichwani.
‘Ni kuhusu mdogo wangu… namuona hana raha, hataki kuniambi ana
tatizo gani,…mimi sipendi…unasikia, kwanza ni kwanini ….unajua mdogo wangu alitoweka
mwaka na kitu, hatujui yupo wapi,…, anarudi na mtoto,…ok, sijui, na kwa ile alikuwa na mama yako, sikuwa na
shaka sana…sasa tunahisi humu kwenu kama nilivyowahi kuwaambia awali ndugu
zangu, dada hana amani…mimi namuheshimu sana mama yako, nilishataka kuleta
vurugu, nimchukue dada yangu ‘akatulia
‘Kwanini umchukue…?’ Soldier akauliza
‘Nisikilize kwa makini, mimi sitaki kujua ni nini kinachoendelea
kati yako wewe na dada yangu au kati ya dada yangu na familia yako, hasa baba
yako…mimi simuamini baba yako kamwe kama nisivyokuamini wewe, wakati wote nyie
wawili nai maadui zangu….unanisikia sana…nikipata mwanya tu, moto utawaka…’akajitutumia
kifua.
‘Mhh..sielewi kitu, na uadui wako huo usioo maana
haunistishi,..unasikia, ushari wako wa kishamba, hauna maana kwangu, kwahiyo
tuachane…’Soldier akasema.
‘Hata baba yako alitamka maneno hayohayo..mtasema hivyo hivyo,
hamuelewi kitu huku mnatesa dada yangu, sawa ushari wangu ni wa kishamba,
sijasoma, si ndio maana yake hiyo ila mimi nakuambia hivi hatua nitakayochukua
mtakuja kuniona mbaya, nimeshamuambia baba yangu…, niliwaonya mapema tu..leo
wanataka msaada wangu…niliwaambia kabisa, nyie watu hamfai kumuoa mdogo wangu,
hamfai…lakini baba hakunisikia, sasa haya yanatokea wameanza kuyakumbuka maneno
yangu..’akasema
‘Lakini kwani kuna tatizo gani hebu tuongee kuna tatizo gani,
mama na baba yangu wana, kuna nini….?’Soldier akataka kujua zaidi.
‘Sitaki kusikia kudeka deka kwako,..mimi sidekewi,..kamdekee
mama yako ..maana naona unamuhitajia sana, wewe ni mwanaume pambana na matatizo
yako kama mwanaume,..achana na kutegema familia yako ooh mama , oo mama, kila
kitu mama, kila baba ..mpaka lini,..unaniona mimi, …simtegemei baba wala mama,
ninaishi kwangu , mbali kabisa na familia,..kwanini, sababu..mimi ni mwanaume
wa shoka..’akasema sasa akitaka kurusha ngumi kama kawaida yake mkono wake ni
mwepesi kupiga, na Soldier anamfahamu jamaa, akasogea pembeni.
‘Hahaha…mama, mama…gangamala mwanaume...’akageuka kuondoka na
Soldier akaona asimuachie kuondoka hivi hivi bila kumjibu neno, akasema;.
‘Lakini shemeji sikiliza, hayo maneno yako mimi siyapendi,
kwanza mimi sideki, pili mimi siwategemei wazazi wangu kama unavyofikiria
wewe,..nimeshakuwa mkubwa nina familia yangu ndio maana nikamuoa dada yako, na
tatu, dada yako na mimi tulioana kwa kupendana, hakuna kulazimishana hapo, na
dada yako hana matatizo, na kwa ufupi ni hivi, mimi nimerudi nitahakikisha yote
yamekwisha…kwahiyo sipendi wewe kuingilia maisha yangu na familia yangu, wewe
una family yko na mkeo sijawahi hata siku moja kukuingilia, kuwa mstaarabu na..kaa
mbali kabisa na mimi na familia yangu.unanielewa….’Soldier akasema na jamaa aliyeanza
kuondoka ghafla akasimama.
‘Unasema….?’ Akauliza bila kugeuka
Soldier alijua jamaa
akigeuka hapo atamjia kama mbogo, aliyejeruhiwa,..anamfahamu huyu jamaa
alivyo.., hawezi kuachana naye kabla hajaanzisha shari,…na hii shari ya sasa
kainzisha yeye, kwani jamaa alishaamua kuondoka,..hakutaka iwe hivyo, ila
aliona bila kusema neno, ataonekana mjinga,…Soldier akajiandaa kwa mapambano,
anamjulia, jamaa huwa anakuja bila mipangilia, …, na kabla jamaa hajageuka mara
mke wake akatokea, na kusema;
‘Oh, kaka, uko huku , baba anakutafuta wanataka kuondoka wenzako…’akasema
na kaka mtu akahema kama mtu aliyeshusha mzigo mnzito…
‘Waambie nakuja…’akasema kwa hasira.
Na dada mtu akahisi kuna
tatizo, anafahamu wawili hao wakikutana ni vurugu, akaona njia pekee ni
kuhakikisha wanatengana, akasogea hadi kwa mumewe na kumshika mkono.
‘Twende, kuna wageni Wanaka kukuaga…’akasema akimshika mumewe
mkono na kaka yake akiguna akatembea mwendo wa kasi kuondoka eneo hilo
‘Vipi kuna nini tena,..najua nyie wawili mkikutana hamuishi
kugombana mnagombea nini jamani, mbona hamkui…?’ mkewe akamuuliza.
‘Hatujagombana tulikuwa tunaongea tu..’akasema Soldier.
‘Unafikiri mimi ni mtoto mdogo sio nimewaona muda tu, na
niliwahi kumuondoa kaka hapo nikijua kitakachofuata ni nini..na mama naye hayupo
vizuri, …sijui ana tatizo gani..?’ akasema mkewe
‘Mama hayupo vizuri..?, ana tatizo gani , anaumwa..?..yupo
wapi…?’ Soldier akauliza maswali mengi akiwa na mashaka
‘Sasa hivi kaenda kulala, hataki kuongea na mtu…’akasema mkewe
‘Ok ….sasa , kabla hatujaenda huko, nikuulize kitu,...’ akasema
akimshika mkewe mabegani na wakawa wanaangaliana uso kwa uso, na kwa haraka
Soldier akasema.
‘Hebu niambie kuna nini hapa nyumbani….ni nini kinachoendelea
hapa nyumbani,…nataka majibu ya haraka kabla kichwa changu hakijapasuka kwa
mawazo?’ akamuuliza mkewe akimuangalia kwa macho makali,mpaka mkewe akashikwa
na butwaa,..kama kutahayari, hakupenda jinsi mumewe alivyomshika,watu wanaweza
kuwaona, akaondoa mikono ya mumewe mabegani na kusogea pembeni..
Mkewe kwanza alibakia kimia kwa muda, halafu akasema;
‘Hata mimi nina maswali kama hayo hayo…..nilimuuliza mama, hakuweza
kunipatia majibu, akaishia kulia…na wewe unaniuliza mimi, aah, inafikia najuta,
kwanini niliolewa,…ooh, sitaki kuyaongea sasa hivi,…na sitaki kuyaongea kabisa,
mimi naona kwasasa wa kukupatia majibu hayo ni baba yako, na mimi sitaki
uniulize zaidi, nimejitahidi kuvumilia ili urudi, na sasa umerudi, subiria muda
muafaka utapatiwa majibu na baba yako, na ninajua baada ya hapo, hutakiwa na
shaka na mimi, nitaondoka zangu…’akasema
‘Utaondoka zako…!!? Una maana gani kusema hivyo! Kuondoka …,
kwenda wapi.? Na , na…Baba anahusikanaje na mtoto, baba anahusikinaje..na na…hebu
niambie haraka, kabla sijabadilika….niambie…’kabla hajamaliza mara baba yake
akatokea…
Kokorikooooh…..kumekucha!...
NB: Bora niishie hapa,
WAZO
LA LEO: Hakuna kitu kinatesa kama mawazo, mawazo yasiyokuwa na
ufumbuzi wa haraka,na mwazo yakizidi sana, inageuka kuwa ni ugonjwa, na madhara
yake huweza kuwa makubwa zaidi ya mawazo yenyewe! Ni muhimu sana kutafuta
suluhu ya mawazo kabla hayajageuka kuwa ni tatizo..Ni kweli mtu mwenyewe
unaweza ukasema nitayamaliza tu, lakini kuna shinikizo la nje,..ni kwanini
mbona nk…haya kama hakuna subira na uvumilivu, haya..ndio yanayofikia kuwaumiza
watu hadi kufikia kupatwa magonjwa ya shinikizo la damu. Tumuombe mungu sana
atulinde na matatizo ya mawazo!
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment