‘Mama mimi nimechelewa kikaoni…’nikasema sasa nikianza
kufunga funga vitu vyangu ili niweze kuondoka. Lakini yule mama ni kama hakunisikia,..na pale ofisi
kulishajaa harufu ya jasho lake,…nikasogea kwenye kipozoe na kukiwasha, sikuwa na nia mbaya ya kumzarau..lakini ofisi ni ofisi, huyo mama alipoona hivyo akasema;
‘Najua unakerwa na jasho langu, jasho hilo lina thamani kubwa mbele ya mungu na ni ushahidi kwako, ili ujue ninavyoteseka, uone kuwa nimetembea maili nyingi hadi kufika hapa sina nauli nitafanyaje..….'akasikitika kwa kutikisa kichwa
'Lakini hayo
hayana maana kwako, maana utafikiria nimekuja kukuomba, hapana ninachotaka ni haki yangu, haki ya mtoto wangu, na najua imeshachelewa kama ulivyosema, lakini hata kama imechelewa, nataka wewe usikie hii kauli yangu kwako…..
Muda huo mimi nimeshakasirika,....sikutaka hata kumsikiliza nilitaka
atoke, ili nione nitafanya nini, maana nilishachelewa hata hicho kikao,...nitafute namna ya kumdanganya bosi wangu kama atanielewa....namfahamu sana huyo bosi mkuu, kwake muda ni kitu muhimu sana,hapotezi hata sekunde moja, ukichelewa dakika moja tu, keshafunga
kikao, kitakachofuata hapo ni barua…
‘Nisikilize kwa makini, najua sana kuwa sisi watu wa chini
hatuna maana kwenu, tunanuka mijasho na tutasema nini, ndio maana hatutakiwi
kuja kwenye ofisi zenu, sawa nashukuru..., lakini hata hivyo tuna sehemu ya
kimbilio letu, ..huyu hawezi kamwe kututupa, na kauli yangu na ujumbe wangu ni
kituma kwake yeye, asiyeangalia mwili au mijasho yetu,... mola ..kwa mola wangu..….’
Akanikazia macho na huku anainua mikono juu.
Wakati huo nilishasimama mlango kumuashiria atoke, nifunge
mlango, yeye akawa kasimama pale pale, na kuendelea kuongea;-
`Kauli yangu ni hii….
‘Kama kweli barua hiyo haikuwahi kufika kwako…, wewe ni mzazi kama mimi
wewe ni mama kama mimi, unazaa kama mimi, mungu anaona,…hakuna anayefahamu
uchungu wa mtoto zaidi ya mzazi, hasa mama….’akaweka mikono hivi kama
atafanyaje.
‘Nasema hivi , kama kweli haijafika kwako, basi nisamehe,..lakini kama
kweli ilifika kwako ukafanya uzembe, ukadharau, maana unaona huyo ni kilema tu,
anafaa nini,..mungu anakuona…mimi sasa naondoka,..samahani sana kwa kukupotezea
muda wako…’
Hayo ndio maneno aliyatamka huyo mama kabla hajaondoka,
halafu alipomaliza taratibu akaanza kuondoka, kwanza, nilibaki nimeduwaa,
nikakumbuka kikao, nikakurupuka lakini kabla sijafungua mlango mara katibu
muhutasi wangu ananijia kwa kasi akisema;
‘Samahani bosi mimi sikumuona huyo mama akiingia….alipitia
wapi, ooh, nilikuwa nimekwenda maliwatoni, samahani bosi…’akasema na mimi
sikumjibu kitu..ila aliposema…..
‘Na…bosi mkuu amepiga simu anasema anakuja…’aliposema hivyo,
mwili mzima ukanywea, maana hicho kikao kilikuwa kinakwenda kufanyikia ofisi
kwake, sasa nimechelewa,…lishapita nusu saa sijafika huko, ..niliangalia simu
yangu, nikakuta missing call tano, simu nilikuwa nimezima kutoa sauti...nikajua
sasa kimenuka, ajira haipo tena!
Nikataka nitoke tu, nimuwahi huyo bosi kabla hajafika,....na
kabla sijafunga mlango, mara mlango wan je ukafunguliwa, na aliyeingia alikuwa
bosi mkuu… kakunja uso utafikiri sio yeye..alikuja moja kwa moja kwangu pale
nilipokuwa nimesimama..
‘Kwanini hujafika kwenye kikao…?’ akaniuliza, na kabla
sijamjibu vyema, akasukuma mlango wangu, ukafunguka, akawahi kuingia ofisini
kwangu, na hakukaa, akanibwagia barua mezani, nilijua ni barua ya nini….nikashika
kichwa,…
Huyo bosi hakusema zaidi, akatoka, na hakuaga, akatoka nje,
kuondoka zake,…sikuisoma ile barua kwanza,…akili yangu ilinituma kuhakikisha
jambo fulani kwanza, kwahiyo nikaliendea trei langu la barua zinazotoka, na
kuingia nikawa nakagua sehemu ninapoweka barua za kuja kwangu,…haikuwa mbali, nikaiona ile barua.
‘Oh..’nikaguna, hapo ndio nikaikumbuka tatizo la huyo mama
na barua iliyotumwa kwangu, kumbe ndio huyo mama…
‘Kiukweli…, ile barua niliwahi kuisoma, kukawa na
ucheleweshaji fulani, katika kufuatilia kumbukumbu zake, hazikuwa zimekamilika
na ilifika ikiwa imechelewa mezani kwangu,…na mimi nilitingwa na kazi nyingine…,
mpaka muda ukapita, nilipoiona tena, muda ulishapita,..hatungeliweza kufanya
lolote,… kwahiyo tukaacha kama ilivyo,….leo hii huyu mama amekuja na maneno
kama hayo..Ilinipa wakati mgumu sana, lakini sikuwa na la kufanya!
Nikageukia mezani, barua aliyoleta bosi ipo mezani, huenda
ndio ya kufukuzwa kazi,..sasa nikaanza kukumbuka mbali…
‘Unajua kwanza niliwazia watoto wangu,..ile kauli ya huyo
mama ililenga haswaa…mimi kama mama ilinigusa pale pale,..mama ukitaka kumpata
gusia watoto wake,..laana ya huyo mama imeshaanza kufanya kazi, kwanza
nimeshafukuzwa kazi, ya pili sijui itakuwaje…mimi nina imani sana ya dini,..lakini
hapo nilitikisika kiimani… nilijikuta nikalia,..nilifikiria, sina nitawakleaje
hao watoto,..
Nikasogea mezani na kuchukua ile barua, taratibu nikaitoa
kwenye bahasha, na maandishi ya kwanza niliyoona, ni….’ninasikitika…’ kichwa
kikaanza kuuma, nikawa sioni maandishi..mara giza…nilichokumbuka ni kauli …
‘NISAMEHE MAMA, sikufanya makusudi…’, nikazama kwenye giza! Nilipoteza
fahamu,………..
NB: Kwa wale wanaotaka kujua ni nini duwa ya mja inafanya
kazi soma kisa hiki, tuonane sehemu nyingine mungu akipenda.
WAZO LA LEO:
Usimdharau mja wa mola..hata kama kakosea, hata kama wewe ni mubwa namna gani,
kipato chako cheo chako, hakina thamani mbele ya muumba, ambaye anajua ni
kwanini kamuumba mja wake hivyo..
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment