Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, February 23, 2017

HAKI YA MJA HAIPOTEI BURE-1


Ni kisa amenisimulia bosi wangu mmoja, nilipokuwa naongea naye maswala ya mtoto wangu..,…akaniambia,…

‘Ndugu yangu wewe muombe mungu wako tu…, utafanikiwa, kama njia hiyo imefungwa ipo nyingine itafunguliwa..nikuambie ukweli, haki ya mja haipotei bure….’akatikisa kichwa na akawa kama anakumbuka jambo…

‘Nikuambie tukio lililonikuta mimi mwenyewe…’akanigeukia kuniangalia usoni.

‘Sijamsimulia mtu…’akageuka kuangalia huku na kule kama kuhakikisha kuwa hakuna mtu anayemsikiliza.

‘Mimi niliwahi kuwa bosi sehemu,..nikawekwa kwenye kitengo cha kuwasaidia watoto wenye matatizo mbali mbali ambao wanahitajia kusaidiwa kwa namna moja au nyingine. Nia hasa ni kuwawezesha na wao waweze kusoma, maana bila hivyo hawatasoma, jamii haina wema na watu wenye matatizo…hasa unapogusia kwenye swala la elimu, sanasana uwaamabie michango ya harusi, watakuchangia sana.

Basi mimi kwa elimu yangu nikawa mkuu wa kitengo hicho na baadaye nikateuliwa kuwa mkurugenzi wa kampuni nzima,…na moja ya kazi zetu ni kuhakikisha watoto wenye mapungufu fulani, ..ulemavu, matatizo ya macho, nk…wanapatiawa huduma maalumu ya kuweza kufanya mitahani yao vyema..kama vile kupewa maandishi maalumu..,na vitu kama hivyo,…’akatulia kidogo.

‘Siku hiyo nilikuwa nimefika ofisini asubuhi…kama kawaida yangu. Na hata sijakaa vyema kwenye kiti changu, ghafla mlango ukafunguliwa na akainga mama mmoja, ni mtu mnzima, nilishangaa yeye kuruhusiwaje kuja kuniona maana enzi zangu, kuja mpaka unifikie mimi kuna hatua kidogo, sio kwamba nilitaka iwe hivyo, hapana ni utaratibu wa kazi ulivyo, kiutandaji,..wapo wadogo zangu ki vyeo, inabidi wao kwanza wafanye hizo kazi, kabla hazijanifika mimi…

Sasa asubuhi hiyo na mapema hata sijajiweka vyema…na ilitakiwa kabla mtu hajafika kwangu nipigiwe simu,…na nadra watu kuletwa kwangu, maana shughuli nyingi zinamalizwa na walio chini yangu…lakini kama ni lazima mtu kuniona inatakiwa apangiwe siku na mimi niwe nimeshapitia mlolongo mzima wa matatizo yake….sasa siku hiyo ikawa ni ajabu ya aina yake…na haijawahi kutokea.

Basi huyo mama, akiwa kasimama,  akaanza kutoa machozi,…nilihisi ana tatizo labda la kufiwa, au… ni omba omba tu maana hapo ofisini tulikuwa tunakutana na mitihani mingi, watu wenye shida ni wengi sana, huwezi hata kuamini, lakini hawaruhusiwi kufika kwangu….mimi kwa tahadhari, nikasogeza mkono ili nishike simu niwapigie mapokezi , niwaulize kulikoni,…lakini hata kabla sijafanya hivyo huyo mama akasema;

‘Usihangaike mdogo wangu,…najua wewe ni bosi mkubwa sana hapa, najua wewe kukufikia ni shida, najua wewe ni muheshimiwa, lakini kwanza jiulize nimewezaje kukufikia wewe…lakini hiyo sio hoja yangu , ila ninaomba dakika tano tu, nikufikishie huu ujumbe, ….’akasema na kutulia, na mimi nikareejsha mkono wangu na kutulia.

‘Kuna barua yangu nilikutumia, nina mtoto wangu, yeye ni mlemavu, ..ana matatizo mengi, ni mtihani wa maisha tu umetukuta,…nami siwezi kulalamika sana…mtoto wangu, ana ulemavu wa viungo, pia ana matatizo ya macho hayaoni vyema ..haya  hata kusikia kwake ni kwa shida,lakini anatakiwa na yeye asome, ndio maana kukawa na maidara kama haya, ya kuwasaidia watoto kama hao, na nyie mkapewa dhamana hiyo, mnalipwa kwa ajili hiyo…mtoto anasoma kwa shida sana,anateseka,..lakini nitafanya nini…’akatulia.

Mimi pale ninatakiwa kujiandaa na vikao, nahitajika nitayarishe muhutasari wa kazi zetu , ..huyu mama hajui hilo,lakini nashindwa kumtoa, …akilini hasira zinachemka, hasira kwa watendaji wangu wa chini, wanajua majukumu niliyo nayo….

‘Lakini namshukuru mungu, mola kamjalia angalau ana akili..huko nyuma kajitahidi sana,…lakini tatizo mtihani huu wa mwisho,…wa kumaliza kidato cha nne,… sikuwahi kupata msaada kama nilivyoomba, kwasababu yenu….wewe ukiwa bosi wao…’akasema akininyoshea kidole.

‘Sasa mwanangu hajaweza kufanya mitihani yake, atfanyaje wakati hakutayarishiwa kama ilivyo kawaida yake, sababu nasikia umesema vithibitisho havikukamilika..vithibitisho gani, wakati miaka yote anasoma, miaka yote anapata hizo huduma, leo hii….hapana, wewe huna uchungu,….’akawa anatoa machozi.

Pale nikaangalia saa, nimebakiwa na muda mchache tu niondoke, sijatayarisha chochote, na kikao hicho kilikuwa cha migogoro ya kikazi nilitakiwa kwenda kujieleza..

‘Nyie kwenye maelezo yenu awali, mlisema tutasaidiwa kila kitu tukaorodhesha majina ya watoto wetu kumbe nia yenu ni ili mfaidike kwa kupitia migongo yetu,…mtoto wangu hajafanya mitihani, nyie ndio mumesababisha hayo……’akasema kwa huzuni..

‘Lakini mama samahani sana, nina kikao maalumu naomba tafadhali…’nikaanza kujitetea, lakini hakunipa nafasi akawa anaongea tu.

‘Nikuambieni ukweli, mwanangu hakuomba yeye awe hivyo…hii ni mitihani tu, hata uwe tajiri au masikini haya yaliyomkuta mwanangu yanaweza kukuta hata wewe, hata mtoto wako,…au nyie kwasababu ni matajiri, hayo hayawezi kuwakuta au sio…niwaulize maana mimi sijui…nimewakosea nini jamani, umasikini wetu ndio tunapata adhabu kama hii…..’akawa analia.

‘Mama samahani kidogo…’sasa nikashindwa kuvumilia…na yeye akawa anazidi kuongea…

‘Labda, mnaona atakuwa na fadia gani kwenye hii dunia.., mwili wenyewe umelegea, macho hayaoni,..atafanya kazi gani..au sio…, si ndivyo mnavyofikiria au sio…..ndio maana mnatufanyia hivi sisi watu wa hali ya chini..hamjui jinsi gani tunavyohangaika na haya maisha, mnafikiri tumeomba…’akajifuta machozi.

‘Mama, mimi nina kikao..nina matatizo makubwa, nielewe kwanza…’nikasema lakini hakutaka kunisikiliza akaendelea kuongea…

‘Sasa nikuambie ukweli, wewe hayo kwako waona matatizo, hebu nifikirie mimi,…mimi naishi huko,…Pugu, nimekuwa nikiamuka saa kumi alifajiri, namuandaa huyo mtoto kumleta huko Masaki kwenye shule yao alipokuwa akisomea….ni mtoto wangu nitafanya nini,..mume alinikimbia, kisa huyu mtoto, eti kwanini nimezaa kilema….leo hii jamani,…mnanifanyia hivi….’akatulia akilia.

Hapo hisia za huruma zikanijaa..., lakini nikiangalia saa ninachelewa ni kazi za kuandaa, nitahitajika kwenye kikao na wakubwa kujitetea,..nina matatizo makubwa,....

‘Mimi nimehangaika na huyu mtoto tokea anazaliwa, lakini nilisema hata kama yupo hivyo ni kiumbe wa mungu, mpaka anafikia miaka minne hawezi hata kukaa, kalegea tu kama hana mifupa…alipofika mika sita akaweza kukaa, kutambaa, lakn kusimama shida, miguu haina nguvu.

Nikahangaika naye,..umasikini huu tena, unakwenda wapi, lakini kila hatu akaonyesha ukomavu, na hata alipofika miaka sana akaanza kudai kuwa na yeye anataka kusoma,...

‘Mwanangu kwa hali hi shule gani watakupokea…’nikamwambia,..lkn ya mungu mengi, akatokea jirani mmoja akanielekeza shule moja, nikampeleka huko…ikawa namshikili hadi shule, anasoma jioni namfuatilia,…ni shida….mpaka akamaliza la saba, alipewa mtihani wa maandishi makubwa, akwa miongoni mwa watoto waliofaulu. Ilikuwa furaha iliyoje, hakuna aliyeamini...

Sasa sekondari…ikawa wapi, maana kapangiwa shule za kata ni mbali, na hali yake itakuwaje…ndio huyo huyo jirani yangu akanielekeza kuwa kuna shule hiyo ya huko Masaki…nikaenda huko nikaomba nikapata nafasi,..mdogo wangu usione hivi, nakuambia haya unielewe,…nimeuza kiwanja cha urithi, kumtibia huyu mtoto.., lakini wapi…

Lakini namshukuru mungu, kidogo ndio sasa anaweza kusimama, kutemba kwa shida,…nimekuwa nikimleta kutoka Pugu hadi Masaki, kuanzia kidato cha kwanza, mimi mwenyewe,..nagombea daladala hadi shuleni,…na jioni namfuata namrejesha nyumbani, hadi kafikia kiwango hicho,….mama ni mama tu..,..sasa imefikia hatua hii ya mwisho,….mnakatili jamani,…niliomba kwa mungu asome hadi chuo kikuu awe shahidi…jamani sasa ndio mnanifanyia hivi..?’ akasema huyo mama kwa uchungu.

'Najua hapo moyoni kwako unasema;
‘Si kilema tu huyo, hata akisoma atasaidia nini..lkn nyie wenyewe ndio mlitushauri, wasome, sasa mumeona wamekuwa wengi au sio…mnataka watoto wenu tu ndio wasome wasiwazibie nafasi za elimu ya juu, mnaongoza kwa kishindoa au sio…hewala bwana, acheni watoto wenu tukafe nao majumbani,..nyie acheni watoto wenu, wasome wafika hadi ulaya….’akasema huyo mama hajui mimi nipoje,...watoto wangu wenyewe wanasoma shule za kawaida tu...

Alipofika hapo nikaona nami nisema neno, nikamwambia,….

‘Mama sielewi unachoongea, unanilamu bure tu...kwanza hebu niambie kwa kifupi tatizo ni nini… na kwani huko ulipopita  wamekuambiaje, maana kiutaratibu, na kwanini ukasubiria mpaka matokea yakatoka …..?’ nikamuuliza lakini kabla sijamaliza akasema;

‘Unajifanya kuwa hujapata barua ya maombi yangu kuwa mwanangu ana matatizo,..alihitajia mtihani wa maandishi maalumu, tofauti na wengine, makubwa sana…, ....mwanangu anasikia kwa shida, ana matatizo ya macho anaona kwa shida…ni nusu kipofu…, ni kilema, namshikilia kila siku kuja shuleni,..nimefanya hivyo miaka mine, leo kafika kidato cha nne mnasema eti vielelezo havikukamika, eti….mbona huku nyuma hakumsema hivyo, na kwanini na nyie hamkuniambia mapema, mkaacha mpaka mtihani umefika,…?’akasema

‘Lakini mama..kwanza , mimi sikumbuki vyema hiyo barua yako..., basi samahani subiria nitaongea na wenzangu..lkn hata hivyo umeshachelewa sana mama kutoa malalamiko yako,… na kama barua yako ingelifika kwangu kwa wakati kwanini nisikupatie hizo huduma…,  tusingeliacha kumfanyia itakiwavyo, mbona tunafanya hivyo mara kwa mara lakini nahisi kulikuwa na  tatizo…oh, …sijui kwani ilitokea hivyo…’nikajitetea huku hata sijui nifanyeje,…

‘Muheshimiwa, kwanza unakana kuwa barua yangu haijafika kwako.huo ni uwongo,tatizo la mwanangu linajulikana muda mrefu, miaka minne sasa, yeye alikuwa anasomaje hapo shuleni,ilikuwa na haja gani ya kuomba tena,…lakini ndio hivyo, kama ulivyosema muda umeshapita, nitafanyaje, kakosa kakosa, hata nikilia, dua la kuku sasa,…lakini nataka unisikie,...ujumbe wangu,…’akasema

‘Mama nimechelewa kikao, yaani mama hujui tu…’nikasema sasa nikianza kufunga funga niondoke.

‘Nisikilize kwa makini, huu ujumbe lazima upenye masikioni mwako,...sisi watu wa chini hatuna neno, kilio chetu ni kwa mola..sasa nasema hivi,….’ Akanikazia macho na mimi nikawa simsikilizi sasa nimeshachukua mkoba wangu nataka kuondoka, na yeye akayaongea haya maneno....

NB: Hebu sikiliza maneno ya mja wa mungu, na je maneno haya yataleta athari gani...


WAZO LA LEO: Kila jambo hutokea kwasababu, na mara nyingi likiwa ni kinyume na matarajio yetu anglabu hatushindwi kujitetea, hata kama tunafahamu tumekosea..lakini tukumbuke, mwenyezimungu mungu hadanganyiki…mwenye haki mpeni haki yake, na kama ikichelewa, msiendelee kumnyanyasa, adhabu za mungu zitashuka ukiwa umechelewa.

Ni mimi: emu-three

No comments :