Muungwana lake moyoni.
‘Ni kweli nimeamua kuoa…na nimemuoa huyo huyo uliyeambiwa..’ilikuwa
kauli ya jamaa yangu mmoja, sikuamini niliposikia kaoa, na kumuoa yule yule….,
na nilipokutana naye nikamuuliza, hakusita kunijibu, japokuwa mwanzoni hakuonekana
na raha.
‘Hongera,..’nikanyisha mkono kumpongea,kwanza akatabasamu na
baadaye akatikisa kichwa.
‘Nashukuru, ahsante…’akasema
‘Lakini wengi wanauliza imekuwaje jaje, maana siku zote
ulikuwa ukimkashifu huyo mdada, na ulimweka kwenye kundi baya, na ukafikia hata
kusema, atakayemuoa huyo kala hasara, je umakubali kula matapishi yako wewe
mwenyewe..?’ nikamuuliza
‘We acha tu, …na awali nilikuwa naona aibu sana, lakini
baadae nikajirudi , nilijiuliza ni kwanini nione aibu, ni kwanini nijiskie
vibaya, hapana, ….sasa nasonga mbele, huyo ni mke wangu, na nimeanza kumpenda,
hata yeye haamini…’akasema
‘Mhh hongera, …lakini bado sisi tunajiuliza kulikoni?’
nikamuuliza
‘Kwanza aminini kuwa lipangwalo na mungu halikwepeki, hilo
kwangu nimeliamini sasa kwa ushuhuda… ama kwa kujitetea, ni kuwa, ..mmh,
ilitokea tu, siku moja, nikaingia kwenye anga zake, na..tahamaki nikanasa, ...’aktulia
kidogo.
‘Rafiki yangu mimi siwezi kuongea kwa undani zaidi, lakini
siri ya kwanini nimemuoa, ipo ndani ya moyo wangu. …kwani nimeamini uzuri wa
sura, umbo,..havina maana sana kwenye ndoa, …muhimu ni nini unachokipata kwake,…nimerizika,
na sijuitii tena…na ..we acha tu, nampenda sana mke wangu…hamjui ni nini
ninachokipata kutoka kwake…siamini na nashukuru mungu! ’aliyatamka hayo maneno
akitabasamu.
‘Sasa mbona awali nilikuona kama huna raha…?’ nikamuuliza
‘Usoni, sawa…si unajua tena, uso umeumbwa na aibu..kwa yale
niliyokuwa nikiyasema, nikawa namkashfu binti wa watu…nimejuta na nimemuomba
sana msamaha…usoni ndio hivyo, ,lakini moyoni, nipo ok…muungwana lake moyoni au
sio…’akasema na sikupenda kumdadisi zaidi, nikaona niliandike hili kwenye shajara yangu, kwa nia ya kutoa
maadili kwa wanandoa, na wanaotaka kuoa.
Kwani kuna marafiki zangu wanatarajia kuoa na kuolewa, …mimi
nawatakia kila la heri, ndoa zao zifanikiwe vyema… na wanaotarajia, kutafuta,
wachumba, wafanikiwe kuwapata wachumba wema,..Ila nina ushauri tu. Tukumbuke
kuwa kizazi huanzia kwenye ndoa, mkishaoana mjue nyie ni chumbuko la jamii
nyingine huko mbeleni, kwahiyo tuweni makini sana hapa kwenye kuchagua
wachumba.
Tunapofikia umri, wa kuoa, au kuolewa, tufikirie huko mbele
ya safari, ya kuwa, sasa mimi natafuta mtu tutakayejenga jamii ijayo, je nataka
jamii yangu iweje, maana nyie ni kizazi, na chimbuko la kizazi chenu ndio jamii
ijayo, kikiwa kizazi chema, jamii itakuwa njema, na kikiwa kizazi kibaya,
jamiii itakuja kuwa mtihani…Sababu ni nyie!
Vurugu nyingi duniani zilianzia hapo, …watu wanafikia
kuchukiana, kuuana, na matokea yake ni visasi visivyokwisha, matokea yake ni
jamii yenye ubinafsi,..hakuna upendo, kila mtu anajijali yeye mwenyewe, chanzo
ni nini, hukutaka kuchunguza, ..hukutaka kumtafuta mke au mume mwema.
Uliyekutana naye ulimuona ‘hakuna mwingine’ kisura mrembo,…nani kama yeye, mrs
world,… mwenye mwendo wa tausi, kumbe sura na huo mwendo wa nanihii… ulikuwa ni
ulimbo tu. Umenasa.
Sina nia ya kuwakatisha tamaa wale wenye taswira zao na
malengo yao ya kufunga ndoa, lakini ushauri wangu ndio huo,..tuweni makini sana kwenye kuwachagua wenza
wetu wa maisha, tujaribu sana kufikiria mbali, tukitafakari jamii tunayoiandaa,
…
Namuomba mwenyezimungu awape mapenzi mema watarajiwa , na
atujalie sisi sote tuwapate wake wema, na waume wema, Aamiyn
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment