Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, November 11, 2016

TOBA YA KWELI-18



‘Dada mimi simtaki huyu mtu,…, simtaki…ataniua…’

‘Ananibaka ananibaka, njoo nisaidie….niokoe niokoe…simtaki simtaki,….’
Ni sauti zilizonivunja nguvu kabisa, zilicheza kwenye ubongo wangu na  kunifanya nihisi kuwa huyu mdada sitaweza kumshawishi kwa vyovyote vile, na nashangaa kitu gani mke wangu alimpendea, na wakati anafahamu  kabisa nilivyokuwa namchukia huyo binti.

 ‘Kwa taarifa yako tu, …nimesikia juu juu, kutoka kwa wife wangu, kuwa huko kijijini watu wengi wanamtaka huyu binti…, sasa kazi kwako , chelewa chelewa utamkuta binti sio wako,….

‘Ina maana wenzangu wameshajipanga, watamchukua, na kiukweli ni binti mnzuri, ana sifa zote za kuwa mke mwema, ila mimi tu….

Kuna muda nilitaka kusema , vyovyote iwavyo, mimi sitaki kuoa, lakini je ni kweli kuwa nitaweza kuvumilia kuishi bila mke…na hata mfano ndio nikataka kuoa, na wakati huo huyo binti keshaolewa, sioni kuwa nitaumia sana, …

‘Aaah, …’nikasema hivyo nikiwa na maana haina haja sana, kwani ni lazima niti kila kitu wanachosema watu…

Unayapuuza maigizo ya mke lakini..mkeo ambaye kafa kwa ajili yako,..mkeo aliyekupenda sana, na usia wake ndio huo umuoe huyo binti, huyo binti ndiye anayekufaa…..

Ni kweli kwa tabia yangu, sidhani kama mtu anaweza kunivumilia, japokuwa kiukweli nilikuwa nimeshabadilika sana, …nilikuwa mtu mwingine, nilikuwa nimeshaanza kuzisahau zile hasira, …je kweli nitaweza kuvumilia hivyo,.

Hapo nikabakia njia panda,…

Niliwaza hayo nikiwa nimekaa upenuni mwa nyumba, sikutaka kuondoka kabisa, niliogopa huyo binti atatoka na begi lake aondoke.

Siku hiyo hakuweza kutoka nje, hali yake ikawa imebadilika, akawa sasa anaumwa kweli...

**********
 Huyo binti hali yake ikawa sio nzuri, akawa hawezi hata kusimama, ikabidi nimuite, na docta akasema hali hiyo itakwisha ni kutokana na shinikizo la damu, ila anahitajia uangalizi wa karibu na kukwepa kitu chochote kitakachomshtua tena..
‘Sasa docta inavyoonyesha binti huyu kaniogopa mimi, na wala sijui ni kwasababu gani..’nikasema.

‘Huenda kuna jambo uliwahi kumfanyia, na muda mwingi amekuwa akiogopa…sasa ilishafikia kikomo, akashindwa kuvumilia tena…ndio ikatokea hivyo…’ akasema huyo docta.

Kwa maelezo hayo ya docta , nikakata tama kabisa na huyo binti.

Nilijitahidi kumsaidia, kumuhudumia, alikuja mzazi wake akitaka kumchukua , nikamuomba asimchukue, aendelee kutibiwa hapo hapo, na mimi nitamsaidia,…sasa ikawa zamu yangu kufanya yale yale aliyokuwa akinifanyia mimi.

Usiku sasa ikawa nakesha kumuomba mungu wangu, nilimuomba anisaidie, huyo binti apone, na anisamehe yale yote niliyomfanyia, na amsafishe moyo wangu uwe na ujasiri wa kuweza kuishi na mimi asiniogope, na ikiwezekana awe mke wangu…hayo ndio yalikuwa maombi yangu.

Akawa anaanza kupona, na hata kutembea tembea japokuwa kwa shida…..

*************
 Sijui hiyo siku  ilitokeaje,…kuna matukio mengi kama haya ya ajabu ajabu yalikuwa yakinitokea lakini hili liliacha kumbukumbu kubwa katika maisha yangu…

Ilikuwa mchana mchana, nikawa nimekaa nje, navuta hewa kwenye bustani ya nje, na akili ikanikumbusha enzo hizo, mke wangu alipokuwa akihudumia hayo maua, nikawa nimezama kwenye mawazo …na ghafla nikaona tena taswira ya mke wangu akitokea upande wa pili..

Yaani pale niliposimama nyuma ya hayo maua, ndipo nilimuona sasa akiwa kasimama, na alikuwa akiniangalia, lakini kwa kujificha,…nikashangaa,…na akili pale ikawa imetaharuki, akili inawaza kuwa hilo ni kweli, huyo ni kweli mke wangu, haraka nikasogea…ili nimuone vyema, lakini kila nikisogea na yeye hujisogeza kujificha..

‘Mke wangu umerudi…’nikasema

Nikafanya haraka ili niende kumlaki, nikasogea upande ule wa pili..yaani huwezi amini, akili yangu iliona hivyo,… na kilichofuatia baada ya kumkaribia huyo mke wangu, nikamvaa na kumkumbatia…nikawa nimemganda, na kilichonishtua ni sauti..

‘Shemeji unaniumiza….’oh, shemeji tena…kumbe alikuwa huyu binti, huyu binti alishajiweza na akajikongoja kutoka nje, …mimi nilipohisi kuwa ni yeye kwa haraka nikamuachia, nikageuka kutaka kuondoka. Na sauti nyuma yangu ikasema;

‘Shemeji mimi naona nimepona nataka niondoke, maana kwa hivi sasa nionavyo mimi hata wewe umeshapona, na kwa hali ilivyo mimi siwezi kuendelea kukaa tena hapa, …kama unavyoona, vituko vyako vinanitisha, hadi nafikia hivi..na zaidi sasa nimekuwa nikiota ndoto mbaya-mbaya  dhidi yako,nyingi zikinikumbusha kipindi kile ulichotaka kunifanyia mambo mabaya, kwakweli shemeji mimi siwezi tena kukaa hapa….’akasema

‘Najua shemeji yangu, nilikukosea sana…lakini ..’nikajitetea.


‘Shemeji yangu hakuna cha lakini..mimi bado hali hiyo inanitesa..kumbuka sana,..ilikuwa mbele ya dada, sasa nipo peke yangu, hivi likitokea la kutokea, atalaumiwa nani, wakati nilishaambiwa niondoke…hapana shemeji , ngoja niondoke tu….’akasema

 Nilijilamu sana, kwanini mimi ilinifikia hali ile, kiukweli kipindi kile nilishakuwa mnyama….hapo ndio nikakumbuka tukio la siku ile , siku ile ambayo nilimfanyia huyu binti jambo la aibu, na athari yake ndio inaendelea hadi leo….

************
 Binti huyu alikuja hapa kwangu, kama kawaida yake alikuwa akija kumsaidia dada yake,…awali alikuwa mdogo, lakini jinsi siki zilivyokwenda  akawa anakuwa haraka haraka, kajaliwa mwili wa kukua haraka,..ikawa sasa akija ni binti mrembo na mimi baba tama, nikawa naanza kumtamani, lakini muda wote alikuwa karibu na dada yake, nikaanza kumtongoza kiaina mara namletea zawadi hii na ile…, na hata ikafikia muda nikaanza kumuomba awe mpenzi wangu…

Siku nilipomtamkia hivyo, alishtuka sana na hakuamini …alishawhi kusikia kuwa nina tabia mbaya, lakini hakutarajia kuwa na yeye yanaweza kumkuta hayo…

Sasa siku hiyo aliposikia namtamkia hivyo, alibakia mdomo wazi,…baadaye akakimbia na kwenda kwa dada yake, sijui waliongea nini… ila sasa akawa hataki kabisa kunikaribia mpaka dada yake akahisi kuna jambo, lakini sijui kama aliwahi kumuelezea dada yake au vipi, mimi kwa kipindi hicho sikuwa najali!

Moyoni sikukubali kushindwa,…nikawa kila nikipata mwanya namuandama, na yeye ananikatalia, kwangu mimi kukataliwa ni kutangaza vita…nikaanza kumchukia, maana sio kawaida yangu kukataliwa…, wengi nikiwabembeleza kwa pesa wananikubalia tu, sasa kwanini huyu….sikukubali.

Siku moja nilibakia mimi na yeye, ili kuondoa aibu nikanywa pombe, na alipojitokeza tu, kwanza nikampa zawadi niliyokuwa nayo, akaikataa, nikaanza kumbembeleza akakataa, nikaona asinipoteze e muda nikamdaka, ikawa kukuru kakara, ilichukua kama dakika kumi, huyo binti akipambana na mimi....hakukubali

Nikaanza kumpiga, kumpiga kweli mpaka akadondoka chini, …akiwa sasa hajiwezi, na mimi na pombe tena, hata sijui ninachokifanya, kichwani sio mimi, alipodondoka, sikujali kama kapoteza fahamu au vipi, nikataka kuanza kufanya mambo yangu….

Mara nikasikia sauti ya mtu akipiga hodi,..

Binti alikuwa kalala sakafuni, mimi nikawa sasa nasita kuendelea, … hapo ikawa salama yake, huyo binti aliniponyoka akakimbia,….na siku hiyo hiyo aliondoka, hata bila kumuaga dada yake… na dada yake alikuja kuhisi , lakini kipindi hicho mke wangu hakuwa na nguvu za kunikabili..nilikuwa siambiliki..mbogo, …nina pesa, utasema nini kwangu…

Baadae iliwahi kuja, lakini hakutaka hata kunikaribia, na kipindi alichofika ilikuwa mimi na mke wangu tumeshakwaruzana, na alipofika yeye ndio ikawa zaidi , ni kama alikuja kuongeza mafuta ya taa kwenye moto..mimi hapo nikajua yeye ndiye chanzo,…nikampiga marufuku kuwa simtaki hapo nyumbani, lakini mke wangu akasema ;

‘Huyu ni ndugu yangu, atakuja kila nikimuhitajia…’sikuweza kuipinga hiyo kauli, lakini moyoni, ikatokea kumchukia sana huyo binti…

Kumbe yaliyotokea kati yangu na uyu binti mke wangu alikuja kuyafahamu, lakini mke wangu aliniacha hivyo akijua ni nini nilichokuwa nahangaika nacho kwa kipindi kile, japokuwa kiukweli alikuwa akiumia sana.
***********
 ‘Umenisikia shemeji….mimi naomba kesho niondoke…’ sauti hiyo ilinizindia kutoka kwenye hayo mawazo

 Nilimuangalia yule binti….sasa angalio langu kwake, lilikuwa la aina yake, angalio la sasa lilikuwa la macho ya huruma na upendo, moyo wangu kwakweli ulikuwa umeshalainika,. Huyu sasa alikuwa sio yule binti niliyemchukia tena, huyu ni mwanamwali mwingine kabisa, binti ni mrembo, na nikimuangalia sana, simuoni yeye, ila ninyemuona ni aliyekuwa mke wangu,…

‘Sasa nifanyeje…?’ nikajikuta najiuliza , kumbe nimeongea kwa sauti.

‘Hamna cha kufanya shemeji,..naelewa hali yako, ama kwa swala la nauli kila kitu kwasasa ninacho.. mimi nikutakie tu maisha mema, na nashukuru sana kwa yote, wala usijali shemeji yangu…, kwa hayo yaliyotokea huko nyuma,..nikijaliwa nikipata muda nitakuwa nakuja mara moja moja, lakini hilo siwezi kukuahidi kabisa…maana sijui ya huko mbele…’akasema.

Moyoni nikasema kwanza huyu mtu anastahiki nimuombe msamaha kwa yale niliyomtendea, hajawahi kusema kuwa keshanisamehe, hilo ni muhimu sana kwangu…nataka kwanza nisikie kauli yake ya kusema kanisamehe.

Kama kawaida yangu nikitaka kumuomba mtu msamaha nafanya hivyo… nikapiga magoti mbele yake…na kwa muda huo huyo binti alikuwa kasimama tu, akiniangalia , na hilo tendo la mimi kupiga magoti mbele yake akalipokea kwa mshangao mkubwa, niliona machoni mwake…

‘Nisamehe sana …shemeji nakuomba, nipo chini ya migu yako, nakuomba sana sana, unisamehe,..kiukweli kama sio wewe hadi leo ningekuwa mtu mwingine, ..na nimegundua kuwa bila wewe sizani kama nitaweza kuishi peke yangu humu kwenye hii nyumba,sitaweza kuishi kwa amani…nakuomba sana unisamehe, na nakumba usiondoke tafadhali….’nikasema

Kwanza alitulia, akibabaika…halafu akasema;

‘Shemeji ….naomba usinipigie magoti,…mimi sio mtu wa kupigiwa magoti, sina hadhi hiyo kabisa,…..ama kwa kukusamehe, mbona mimi nilishakusamehe tu shemeji yangu..najua sio wewe, nilijua sio wewe ni ibilisi tu, na kila siku nimekuwa nikikuombea, ili mungu akuongeze,…lakini sasa shemeji..naomba uinuke, …na ujue ukweli kuwa sasa muda umefika, wa mimi kuondoka, na unielewe kuwa na mimi nahitajia maisha yangu…’akasema.

‘Maisha yako…eeh, ehee, unajua shemeji hapo na mimi nilikuwa na maongezi tena mazuri sana, kuhusu maisha yako,…unajua wewe ndiye mtu wangu uliyebakia,..unaona ndugu zangu wote, wamenikimbia,sina kitu, hata marafiki wapo tena, sina kitu…umebakia wewe tu…, wewe ni zaidi ya ndugu….na nataka maisha yako yawe hapa, uishie hapa…’nikasema

‘Hapana shemeji…wewe unastahiki uje uoe,…na hilo dada alilisisitizia sana kuwa akiondoka hapa duniani, atafurahi sana ukioa mapema, nakumbuka kabisa alisema hivyo, …ila kwa mimi shemeji haitawezekana kabisa kuendelea kukaa humu, ninaomba unielewe tu...’akasema.

‘Umekumbuka sasa eeh, dada yako kumbe aliwahi kukuambia hayo,..japokuwa sikutaka kuoa, lakini kwa ajili yake, basi mimi nataka nije kufanya hivyo, sasa unaonaje ukikaa hapa ili niweze kulifanikisha hilo…?’ nikasema na kumuuliza.

‘Nakumbuka sana jinsi dada alivyosema, kila nikipokuwa naye karibu aliniambia mengi,na moja wapo ni hilo kuwa mimi nijitahidi  kukusaidia mpaka hapo ukiwa na hali nzuri ndio mimi nirudi kwetu kijijini…ndivyo alivyoniomba hivyo…, hakuna zaidi, hajasema niwe naishi hapa na wewe milele,…mpaka uje kuoa tena… hapana, halafu siwezi kuendelea kukaa zaidi humu, maana mimi sio ndugu yako, watu wananifikiria vibaya…’akasema

‘Sasa nakuomba kitu kimoja, nakuomba uniache niwazie hilo, ila nakuomba sana usiondoke kesho, nitaka tuongee, tafadhali sana….’nikasema.

‘Kesho shemeji mimi naondoka….siwezi kukaa zaidi hapa tena…’akasema huku akiondoka kurudi ndani.

************
 Ilikuwa kwenye chakula cha usiku, aliniandalia yeye, ..maana sasa alishaweza kufanya kazi zake kama kawaida, …na aliweka chakula mezani kwa haraka akataka kuondoka, hapendagi kula na mimi mezani…

‘Shemeji nakuomba leo ..tule pamoja hapa mezani, nataka kuongea na wewe jambo moja…’nikasema na yeye kwanza alionekana kusita, lakini kwa heshima akafanya hivyo.

Nilimuanzia maongezi ya mbali..kwa kuongea mimi najua sana, najua jinsi gani ya kumweka mtu sawa…na hatimaye nikamuelezea dhamira yangu,..kuwa mimi ninataka kumuoa yeye, awe mke wangu wa ndoa…hapo sasa…

‘Eti nini…wewe baba wewe..hapana,….mimi nimekuwa nikiishi hapa , kwasababu tu ya dada, na wala sikuwahi kuwa na wazo kama hilo hata siku moja…, nakuomba tena sana ondoa wazo kama hilo, usije kuja kuumia moyo wako….mimi sitaweza kuishi na wewe, siwezi na haitawezekana…’akasema akionyesha kweli ana nia hiyo.

‘Shemeji….nakuomba sana sana, urudishe moyo wako nyuma,..najua mengi yamepita, lakini niangalie na mimi, ..na kiukweli kama ukiondoka, ukaniacha… huku nyuma utasikia mengine, siwezi kuishi bila ya wewe..nakupenda sana …na nakuona wewe kama mke wangu, kila nikikuangalia nakuona wewe kama jilio jipya la mke wangu ’nikasema

‘Mhh.. shemeji huko umeenda mbali, siwezi kuwa mke wako.. hapana..nimekuwa mimi nikikusaidia wewe kwa vile dada nilimpenda sana, lakini kiukweli sijawahi kufikiria kitu kama hicho, nakuheshimu sana shemeji yangu,.. eti leo mimi nije kuolewa na wewe, hapana..hata wazazi wangu hawatakukubali hilo…’akasema,

‘Kwanini sasa..kwa vile mimi …nina matatizo au..nitakufanya kitu kibaya..shemehi mimi nimeshabadilika,..mimi sio yule mtu wa zamani,…nimetubu, nimemrejea mola wangu, ..na toba yangu,..inatoka moyoni..nakuomba unielewe…’nikasema

Mdada huyo akatikisa kichwa kukata, kata kata….

Ikawa kazi kubwa sana ya kumshawishi huyu binti, nilitumia kila njia ninayoifahamu mimi, na ikafikia hatua ya kupiga hata magoti..mimi nikitaka kitu, naigiza kila jambo,..hutaamin, hata chozi lilinitoka,

Baadaye  huyo binti akasema anahitajia muda wa kuliwazia hilo, na hapo ikanipa moyo kuwa huenda atanikubalia ombi langu..unajua tena.., ile hali ya kuishi naye karibu-karibu, nahisi hata yeye,  ilishamjengea namna fulani ya upendo..lakini huenda uwoga…

Basi asubuhi ndio nilitarajia ataondoka, akaja kuniaga, kiukweli alishapanga kuwa ni lazima aondoke, ..ila sasa hata akiondoka najua anaondoka na jambo jingine kichwani,…aliniambia anaondoka na wazo hilo kichwani mwake, yeye kama yeye anaweza asiwe na maamuzi, anaomba kwanza aende nyumbani akaongee na wazazi wake kwanza .

‘Shemeji unipe muda, kwanza ni swala la kunishtukizia,…najua , nakufahamu, kiukweli,…sina la kusema,..itakuwa vigumu sana kuja kukuzoea,..lakini siwezi pia kusema hapana, sikutaki,..ngoja kwanza nilifikishe hilo ombi kwa wazazi wangu na kama wao watanikubalia, basi …kwa heshima ya dada yangu nitakubali niishi na wewe….’ Akasema

‘Uishi na mimi kama mke na mume…’nikamalizia mimi, na yeye kwa aibu akageuka pembeni.

‘Tuombe mungu tu…’akasema hivyo, na siku hiyo akaondoka kurudi kwao…

NB: Mhh, mbona inazidi kuwa ndefu hii stori….msijali, tutakuja kumalizia sehemu iliyobakia, tukijaliwa

WAZO LA LEO: Ili tufanikiwe kwenye shughuli zetu, shughuli za kimaisha, zenye hitajio la mafaniko fulani, yawe ni ya kumtafuta mwenza wa maisha, yawe ni yakutafuta maisha bora, yawe ni ya kuishi na familia yako vyema, ujirani mwema nk…tukumbuke sana kumweka mungu wetu mbele, tuombe sana, tumuombe mola ukweli wa kumuomba, kwani yeye ndiye anayefahamu shida zetu na njia ipi sahihi ya kufanikiwa, yeye ndiye anayemfahamu mwenza wetu wa kimaisha,..omba na usichoke kuomba.
Mola wetu tunakuomba, utukubalie maombi yetu, tuwe na wenza wema, maisha mema, afya njema na Baraka tele…Aamin.

Ni mimi: emu-three

No comments :