Marejeo..niliamua kuikimbia nyumba yangu kuepusha shari...niliondoka huku nikijua huenda nimeshamu-ua mke wangu, ..na docta aliyekuja kumtibia alikuwa taabani kwa kipigo changu...nikaenda kupata hifadhi kwa rafiki yangu, na kufika huko tu nikapotewa na fahamu..
Baadaye hali ilirejea , nikakutana na mshauri wangu wa kiimani, akanikumbusha kile nilichoahidi,..kutubia madhambi yangu ili iwe ni tiba ya matatizo yangu, matatizo yaliyonifanya nisiwe na raha hapa duniani, japokuwa nina mali, mke mnzuri...lakini...
Je nitaweza, kulifanikisha hilo.. kwani kila hatua ilikuwa ni ngumu na yenye mitihani migumu,...na sasa nipo kwenye kizingiti kigumu...KUSAMEHE WALIONIKOSEA..!
Walikosea hadi kuingilia ndoa yangu..na kuharibu, ...na kuharibu kile nilichokuw nikikitafuta!
Tuendelee na kisa chetu
*************.
Nilipofika nyumbani
kwangu, kabla hata sijalifikia geti la kuingilia, nilihisi mwili ukinisisimuka,
kwangu mimi hiyo ni ishara kuwa sipo
salama, kuna adui karibu..mimi ni mpiganaji, na nilipokuwa jesini, nikijihisi
hivi, najua sipo peke yangu, kwani adui karibu, na natakiwa nijihami kwa
haraka,lakini sasa sipo vitani…nipo uraiani, natakiwa nisionyeshe hali yoyote
ya mashaka.
Nilichofanya kwanza
nikujaribu kuchukua tahadhari zote,..nikavuga nikichunguza mzunguko wote wa
eneo langu kwa macho huku natembea , kuelekea mlangoni, na hadi nafika mlango
wa geti nilishajua kuna nini kuzunguka eneo.
Kulikuwa na watu ….lakini
hakuna niliyemtilia mashaka, kwani walikuwa wakiwa na shuguli zao pembezoni mwa
ukuta,…nikawa kila mara nawatupia jicho kw uficho kuona kama kuna yoyote
anashauku na mimi, lakini hakuna aliyeonyesha dalili hizo.
Nikashika mlango wa
geti na kuusukuma,..siku hizi hata mlinzi hakuna!
Nikaingia ndani na
kukagua maeneo yote ya kuzunguka nyumba yangu, lakini kwa macho, mpaka nilipojirizisha kuwa hakuna tatizo, ndio
nikashika kitasa cha mlango, ile na ile nakigusa tu,nikasikia sauti ikilia
nyuma ya nyumba.
Kwa haraka
nikakiachilia kile kitasa na kwa haraka
nikakimbilia nyuma ya nyumba…nilisikia mtu akidondokea nyuma ya ukuta, nikajua
kweli kulikuwa na mtu huku nyuma, nikachunguza sehemu zote, na nilipoona hakuna
zaidi, nikarudi mlangoni nikafungua mlango, kwa ufunguo wangu ninaotembea nao.
Kwanza nilishikwa
na butwaa, …
Ndani kulikuwa shangala baghala… utafikiri kulikuwa
na vita vya dunia, vitu vimevunjika, …hakutamaniki..sikuamini kuwa ni mimi niliyefanya
yote hayo, nahisi kama kuna mtu alikuja akaongezea kama anatafuta kitu…
Nikajaribu kupanga
panga vitu,lakini akili haikunikaa sawa, nikajiona nimechoka, napoteza
muda…haraka nikaacha hiyo kazi na kutoka nje, nikitafakari la kufanya kwanza.. Nikaona
kabla sijafanya lolote nijua hali ya mke wangu.
Simu sikutaka
kuiwasha kabisa,….ukiwa kwenye shughuli zangu, simu ni nzuri sana, lakini pia
ni chanzo kikubwa cha kukufichua wapi ulipo, nikaona niachane na simu kwa muda,
haraka nikaelekea kwa jirani yangu ninayelewana naye..huyu mara kwa mara
tunakutana na kuongea…, nilipofika kuulizia kama wana taarifa yoyote kumuhusu mke
wangu nikaambiwa;
‘Si nimesikia kuwa
mke wako yupo hospitalini anaumwa,…na ana hali mbaya sana, kwani wewe ulisafiri,
kweli jana pia nilisikia watu wakijaribu kukutafuta sana, hupatikani umezima
simu yako, ni kwanini unafanya hivyo..’akasema kwa kunilaumu.
‘Kwani umesikiaje, kuwa mke
wangu ana hali gani…?’ nikauliza
‘Sijasikia zaidi..,
nilitaka kuja kwako kuukulizia, lakini niliposikia kuwa haupo, nikaona
nisubirie tu…hata hivyo, mbona watu wanasema ndani kwako, yaonekana kama kuna
majambazi waliingia, kwa jinsi kulivyoonekana, nilitaka leo nifike mwenyewe
niingia maana tunajuana, lakini ndio bahati hii umekuja…’akasema
Lakini kuna watu
waliamua kuingia ndani na kuchungulia dirishani wakikutafuta, wakaona ndani vitu
vimevunjwa vunjwa….kwani kulitokea nini..?.’nikaambiwa na jirani huyo na mimi
sikutaka kusema lolote nikauliza;
‘Mke wangu kalazwa
hospitalini gani?’ nikauliza, na jamaa akataja jina la hospitali ambayo,
inamilikiwa na mbaya wangu, niliposikia hivyo kwa haraka nikageuka kuondoka,na
huyo jirani yangu akasema;
‘Na pia nimesikia
kuwa unatafutwa na polisi…’ akasema akiniangalia kwa mashaka.
‘Natafutwa na
polisi kwanini…?’nikauliza nikijifanya nashangaa, huku nikianza kutembea
kuondoka.
‘Mimi sijui…unajua mimi
naumwa sijaweza kutoka nje wiki sasa.., hayo nimeyasikia tu…sasa sijui umefanya
nini….’akasema huyo jirani yangu akiniangalia kwa mashaka wakati huo mimi
nilishafika mlangoni naondoka zangu.
‘Uwe makini jirani…’akasema
Sasa moyo ukaanza
kunienda mbio, nikajua yawezekana jirani yangu huyu naye anajua jambo, kumuhusu
mke wangu, lakini hakutaka kuniambia moja kwa moja…na kama polisi wananitafuta
yeye ndiye atakuwa wa kwanza kuulizwa, kwani wengi wanajua tunafahamiana kwa
karibu kama majirani…sasa hawa polisi wananitafutia nini..ni kuhusu mke wangu
au…ooh, yawezekana,
‘Kwa kumuumiza
dakitari…’nikasema
‘Sizani kama mkewe
wangu ataweza kunishitaki, kuwa nimempiga..na kama ana hali mbaya, au …hwezi
kuwa kafariki, haiwezekani…, sasa natafutwa na polisi kwa kosa gani?’
nikajiuliza huku nikitembea kurudi nyumbani kwangu, na kabla sijafungua mlango
nikahisi kuna mtu ananichunguza, nikafanya kama nafungua mlango halafu kwa
haraka nikageuka kuangalia nyuma…hakuna mtu.
‘Ni lazima kuna mtu
ananichunguza..’nikasema, lakini sikutaka kuchunguza zaidi , nikaingia ndani.
Nilikaa ndani kwa muda, nikijaribu kuwaza,..sikutaka kuwasha simu yangu kwanza,
baadaye, nikatoka nje,wazo jingine likanijia kichwani.
‘Niende huko
hospitalini…’nikasema
Nilipotoka nje,
nikaona mlango wa geti ukifungwa kwa haraka, kuashiria kuwa kulikuwa na mtu
ndani, sasa alikuwa akitoka, ..kwa haraka nikakimbilia pale getini na kufungua
mlango kuangalia huyo mtu ni nani…..sikumkuta mtu yoyote.
‘Hawa watakuwa ni
polisi au ni watu gani, au wezi nini…’nikasema niktamani niwashe simu nimpigia
mlinzi wangu aje..lakini sikuona haja, kuna mlinzi wa jirani huwa akija usiku
anaangalia sehemu zote, na mimi nachangia katika malipo, ndio maana sikuwa na
haja na mlinzi wangu binafsi.
‘Nina uhakika
nikienda hospitalini, nitaishia mikononi mwa polisi, na kama hawa watu
wananitafuta kuna jambo… na jinsi wanavyonitafuia visa vya kunikamata, sasa
naona wamenipata, lakini sikubali….’ Nikafunga mlango na geti, nikatoka nje …hutaamini
nilikuwa na gari langu, nililiuza, …
Nikatembea kuelekea
kituoni….,lakini kabla sijafika mbali nikahisi kuna mtu ananifuata kwa nyuma!
************
Nilichukua bajaji , lakini kabla sijaingia
kwenye bajaji , jamaa wawili wakaja wakanishika, wakajitambulisha kuwa wao ni
watu wa usalama, wakasema ninahitajika kituo cha polisi kwa kuhojiwa. Sikufanya
ubishi, nikaongozana nao hadi kituoni.
‘Umeshitakiwa kwa
kupiga na kujeruhi…’akasema askari
‘Nimempiga nani…?’
nikauliza
‘Dakitari…’akasema
‘Amesema ni kwanini
nimempiga..?’ nikauliza.
‘Hajui sababu…,
yeye anasema alikuja kwako kumtibia mke wako , ukaanza kumpiga,…’akasema polisi.
‘Sio
kweli…’nikasema , nikadanganya, nikawa nimevunja miiko ya toba, kwani
niliambiwa kipindi chote hiki niwe ninasema ukweli…nisidanganye, lakini kwa hali ilivyokuwa sikukubali kwenda
jela.
‘Sio kweli kwa vipi
una maana docta anaweza kuja kukusingizia
uwongo, unafahamu ni docta gani tunayemzungumzia..’akasema.
‘Yawezekana…kutokana
na jinsi tunavyoishi, mimi nimekuwa na maadui wengi, kila mmoja anataka
kuniharibia maisha yangu,…na huyo ni mmojawapo, huenda kapigwa na watu wengine
akahisi ni mimi nimewatuma…’nikasema.
‘Hata hivyo docta
alikuja baadaye akasema kaifuta kesi, ila kutokana na uchunguzi wetu
kunaonekana kuna tatizo, wewe mtu una matatizo, …tuambie ukweli, ni nini
kinachoendelea, maana tulifika kwako hali tuliyoikuta yaonyesha wazi, hakuna
usalama, ..’akasema polisi.
‘Kuna jingine
lolote au niondoke..’nikasema, na Yule askari aliponiona sitanii, akasema;
‘Sawa unaweza
kwenda, lakini bado tunakuchunguza kama kuna jambo linaloondelea na hutaki
kutoa ushirikiano , ujue utakuwa hatiani…tumekuwa tukikufuatilia, na mara kwa
mara umekuwa ukiponyoka kwenye mikono yetu,lakini nakuhakikisha ipo siku….’akasema
huyo askari.
Mimi sikumjibu nikaondoka zangu hadi
hospitalini.
*************
Nilipofika hospitalini, sikuruhisiwa kumuona
mgonjwa, niliambiwa docta amesema mgonjwa asisumbuliwe, na yoyote Yule.
‘Lakini mimi ni
mume wake…’nikasema.
‘Tunafuata amri ya
docta…’akasema nesi.
Nilikaa pale kwa
muda, na mara docta akafika, ..Nilimuangalia huyo docta akishuka kwenye gari
lake, alikuwa na plaster puani, nikakumbuka ile ngumi niliyompiga…nikahisi
vibaya, kiukweli nilifanya vibaya lakini hasira, hata ingelikuwa ni wewe, unaambiwa
huyu ndiye mwizi wako..
Docta, akawa
anakuja usawa na pale nilipokaa, aliponiona wala,hakuonyesha dalili za
kunikasirikia, akanisalimia ,…na akanitafadhalisha kuwa nimpe muda kidogo
aingie ofisini kwake baadaye ataniita, ..na kweli haikupita muda, baadaye alinikaribisha
kwenye ofisi yake,
‘Mkeo bado hayupo
vyema..na kwa hali aliyo nayo, tunashindwa kuendelea na matibabu mengine..ila
tangia jana alikuwa akitaka muonane naye…’akasema.
‘Kwani ana tatizo
gani?’ nikamuuliza.
‘Mhh…siwezi
kukuambia lolote kwasasa maana bado yupo kwenye uchunguzi, lakini mengie
alisema,…atakuja kukuambia yeye mwenyewe…’akasema.
‘Sijakuelewa…kwanini
wewe kama docta usiniambie tatizo lake ni nini….?’ Nikamuuliza.
‘Mimi natii agizo
la mteja wangu ambaye ni mgonjwa wangu..hata kama ni mkeo siruhusiwi kumwambia
lolote mpaka yeye mwenyewe atoe hicho kibali, ilimradi ana fahamu na akili zake
timamu…’akasema.
Nikasimama kutaka kutoka,..na yeye akasema;
‘Kuna jambo
nilitaka kuongea na wewe, lakini naona ukaongee kwanza na mke wako ila
nikuambie ukweli,…mimi sipendi ugomvi mimi na wewe,…yaliyotokea sawa, labda
ulifanya ukijua ….au ukitaka kulipiza kisasi,..lakini nikuambie unafanya makosa
sana…’akasema.
‘Umesema hutaki
kuongea na mimi mpaka niongee na mke wangu, ..unataka tuongee kwanza….?’ Nikamuuliza.
‘Aaah,.. hilo ni juu
yangu mimi na wewe..ulichonifanyia jana kimeniuma sana, kuwa wewe umekimbilia
hasira,..unafikiri mimi siwezi kupambana na wewe...unataka mimi na wewe tuonyesha ubabe si ndivyo unavyotaka, lakini kwanini umesahau, … nilitaka kukushitakia lakini
baadaye nikaona haina maana, maana huenda sio kosa lako…’akasema.
‘Ni kosa la
nani….?’ Nikauliza.
‘Ufahamu!…ufahamu
wako ni mdogo sana….’akasema na mimi nikawa napambana na hasira, niliona
kanizarau,..lakini nikaona nikiendelea kujibishana na yeye nitaharibu kila
kitu, kwanza nipo ofisini kwake, pili keshanishitakia….basi nikasema;
‘Naweza kwenda
kumuona mke wangu tafadhali..’ nikasema
‘Sawa unaweza
kwenda kumuona, ila wewe na mimi hatujamalizana...mimi na wewe tutapambana kiume..wewe si unajiona mbabe sio....tutaona...kwa mahali pake, sio hapa, nakuapia umeingia choo cha kike, hayo unayoyataka hutayapata na nitahakikisha unakuja kunipigia magoti.....'akasema na mimi nikatikisa kichwa dharau.
'Usijali....'nikasema
' Na kama angalizo, uwe makini sana na kauli zako mbele ya mkeo.., hakikisha huongei jambo
la kumkwanza..ndio maana sikuhitajia mtu yoyote kuonana na yeye, lakini kwa
vile anahitajia kuonana na wewe, sikuona kwanini nikuzuie, bado yupo kwenye uchunguzi,
….’akasema
‘Sawa , usiwe na
wasiwasi na mimi, huyo ni mke wangu..’nikasema na kuondoka kuelekea huko kwenye
chumba alicholazwa mgonjwa, nikiwa na mafundo mengi kichwani…niktamani nirudi nipambane na huyu mtu, katika maisha yangu sipendi kutishiwa, ni bora tupambene nijue moja...moyoni nikaahidi kupambana na huyu mtu ...
Nilifungua mlango
alipolazwa mke wangu….chumba kilikuwa cha baridi, na mlio uliokuwa ukisikika ni wa kipozoe cha hali ya hewa, na mbele yangu kulikuwa na kitanda,..lakini kimezungushiwa pazia,..moyo ukanilipuka…
NB: Ni nini
kitaendelea, jamani tuombeane heri, maana mitihani ni mingi, ndio maana
nachelewa sana kukiendeleza hiki kisa
WAZO LA LEO: Katika maisha ya ndoa kunaweza kutokea mitihani kwa
wanandoa, kiasi kwamba kila mmoja akawa na chuki na mwenzake. Yaweza ikawa ni
sababu za kiuchumi, au ikawa ni sababu yoyote ile, tahadhari, kwa vyovyote
iwavyo, sio vyema mmojawapo kwenda kumtangaza mwenzake nje ubaya.
Kufanya hivyo ni kukiuka miiko ya ndoa, muhimu
nyote wawili, kaeni ongeeni, ikishindikana watafuteni wakubwa, wazazi wenu, au
washauri wa kidini. Msiwape watu faida kwani wengine watautumia mwanya huo
kuwaharibia kabisa.
\Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment