Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, February 26, 2016

SIKIO LA KUFA HALISIKII DAWA-11


Mzee aliondoka nikabakia peke yangu…nakajua sasa mimi ni mpweke, sina wa kumtegemea tena, na sina majaliwa mengine ya hapo kijijini.. na kabla sijatanabahi ndio mlango ukafunguliwa…..!
Lakini kabla ya tendo hilo la kufunguliwa mlango, ulipita muda mchache kama dakika kadhaa…na muda huo ulinifanya niwaze sana, nilie..nisononeke…..

************

Akili ya mwana-adamu ni ya ajabu sana…mzee alipoondoka tu hapo hapo akili ikaanza kufanya kazi, ni kipindi cha muda mfupi tu, lakini niliweza kuwaza mambo mengi  na niliwaza hayo hata kabla mlango haujafunguliwa…!

Jambo la kwanza lilinijia akilini ni kuwa natakiwa niondoke hapo nyumbani  haraka kabla sijakutana na mama mwenye nyumba,…..yeye alikuwa hanitaki….najua hilo akilini,….chuki na hasira alizokuwa nazo mama huyo angeliweza hata kunifanya chochote, nilishindwa kuelewa ni kwanini alipotukuta pale kitandani na nikiwa na mumewe hakufanya fujo, ilivyo kwa wengi wangelileta fujo,  yeye hakufanya hilo kabisa ni kama vile alijua nini anachikifanya.

Hakutaharuki, zaidi ya kusema maneno aliyosema na kutupiga picha… ni kama vile ulikuwa mpango wa kuninasa…na hii ilinipa mawazo mengine akilini kuwa huenda hili lilipangwa…..ina maana walifanya mpango huo na mumewe, hapana…sizani!.

Wazo la kuwa huenda mumewe alifanya hivyo ili upatikane ushahidi halikuniingia akilini, …kwasababu mume huyo alikuwa mkarimu, mwenye huruma sana kwangu,  sasa iweje wapange na mkewe kuwa kupatikane ushahidi nifukuzwe….

Kwa jinsi ilivyotokea pale…mume mtu ndiye alianza uchokozi na mimi sikuwa na mpango huo, nilimuheshimua sana huyo mbaba…na kama angelichelewa kuja huyo mke mtu,  mumewe,alikuwa akielekea kubaya,….alishashindwa kuvumilia, lakini mimi sikuwa tayari kwa hilo…

‘Sasa mimi nilikuwa na kosa gani hapo….kwanini wanione mimi ndiye mbaya,…lakini hapo hapo nikazidi kujiuliza ni kwanini mkewe asilete vurugu..hili lilinisumbua sana kichwa kuliwazia,hata hivyo sikuwa na uwezo wa kulipatia jibu,  sikuwa na muhimu ni kuondoka hapo nyumbani haraka…

Kitu kingine nilichojiuliza kwa haraka, ni kuhusu kuonekana kuwa mimi ndiye mkosaji, ni kwanini wao walikimbilia kuniona mimi ndiye mkosaji, ni kwanini wasimshutumu mume mtu… labda ni kutokana na historia iliyopandikizwa kwangu kuwa mimi ni mbaya huko kwetu,…. sina cha kujitetea sina wa kunitetea, mtetezi wangu alikuwa  huyo mzee, sasa naye kajitoa, sasa  kweli  nakamilika…. mimi sasa nimekuwa…sikio la kufa….

‘Sasa nitakwenda wapi!....hata kama nikiamua kuondoka…?’ nikajiuliza

‘Hata kama sina pa kwenda ni lazima niondoke kwenye hii nyumba kabla mambo hayajaharibika…’nikasema

Hakukuwa na jingine bali ni  kuanza kupanga vitu vyangu  ili niondoke kwa haraka na ikiwezekana wakiingia humo wakute nimeshaondoka…tatizo ni muda, tatizo nilikuwa sijui waliongea nini huko,..na nini kitafuata….ila hisi ziliniambia kuwa…kwa muda wowote watafika na kunitimua sizani kama baba mwenyenyumba anaweza kumshawishi mkewe…..

Nilijua kwa hivi sasa alikuwa na wakati mgumu wa kuitetea ndoa yake,….na hata kama ingelikuwa mimi , ningetetea ndoa yangu kwanza, sasa sijui walikubaliana nini, na huenda baba mwenye nyumba keshanigeuka,  huenda kapindisha maneno, au walipanga ili niondoke hapo nyumbani….sijui, labda…niliwaza hilo nikijaribu kuhisi jinsi mbaba huyo atakavyojitetea ili kuikoa ndoa yake,..nasema huenda japokuwa huyo mbaba hakuonekana kuwa na tabia hiyo.

Nilikumbuka kuwa mke mtu alimwambia mumewe aende akampe talaka yake, …nilijua kabisa kauli hiyo ni ya kutingsha kibiriti…..,lakini kwa vyovyote itakavyokuwa, mume hawezi kufanya hivyo, asingelikubali kuitoa hiyo talaka ..na ndivyo ilivyokuwa ndio maana huyo mzee aliitwa haraka,

Nilijiuliza ni kwanini huyo mzee aliitwa, badala ya wawili hao labda kuwaita wazazi wao, ili wasuluhishwe, kwanini  aitwe huyo mzee  kwanza, kuna sababu ya msingi….kama mpango wao tu, basi walitaka kuutumia ushahidi huo ili mimi niondoke…lakini kwanini….!

Kwa tabia ya huyo mbaba, nimjuavyo mimi….yeye sio muongeaji, pili hapendi majungu kukaa na kuanza kuteta mtu, na siku zote ikitokea tupo wawili, haongei sana labda kwa swala la wajibu….na alijitahidi sana kujiweka mbali kama hakuna ulazima, isipokuwa siku nikiwa naumwa…na hata mkewe alipofikia kumshuku hivyo, niliona ajabu sana…

Sasa ni sababu gani ya kuweza kufanya mipango ya pamoja  ili upatikane ushahidi  ili nifukuzwe humo ndani…, sizani, hiyo itakuwa mbinu ya mama mwenye nyumba, …sikutakiwa kuliwaizia hilo nilichotakiwa kukifanya ni kuondoka, maana sitakiwi tena kuwepo  hapo...

Najua mzee aliitwa, kama kweli sio mpango, mume alimuita huyo mzee, au mke ndiye aliyemuita huyo mzee ili kuwe na suluhu, na ili suluhi ipatikane ni mimi niondoke…kwani tatizo ni mimi, na sio mume aliyenitaka …..na waliamua kumuita huyo  mzee kwani ndiye aliyenidhamini,au kama ni mkewe alimuita huyo mzee, nia yake ilikuwa  kuonyesha huo ushahidi  alioutaka huyo mzee.

Mzee alipofika, mama mwenye nyumba hakuwa na la zaidi ….sijui labda mama mwenye nyumba alisimamia kwenye msimamo wake kuwa anataka talaka yake na mumewe akaanza kujitetea, na mama mwenye nyumba akaamua kuutoa huo ushahidi….

Nakumbuka mzee alipoingia tu, alionekana kukasirika, hakuonyesha ule uso wa upendo tena, ina maana alishakabidhiwa mtu wake, na mzee hakuwa na jinsi ….kwa jinsi alivyoonekana ni wazi kuwa huenda  alishaafiki  uamuzi kuwa mimi niondoke hapo japokuwa mzee hakunitamkia hayo,hakusema ni nini walikubaliana huko…hakutaka hata kusikia hiyo siri niliyokuwa nimekusudia kumwambia…yeye alisimamia katika kuiokoa ndoa ya watu. Mawazo haya yalikuja kwa haraka sana kabla mlango haujafunguliwa

'Hivi kwanini mzee hakutaka kunisikiliza nalo  lilinikwanza sana, utafikiri huyo mzee ni baba yangu, nilijiuliza sana kwanini mzee hakutaka kunisikiliza kama ilivyokuwa kawaida yake, hakutaka  kunielewa, hata kama kuna maamuzi hayo…ya kuwa mimi niondoke,…kwanini hata hakutaka kusikiliza hiyo siri….

‘Kwanini ..kwanini…mzee hukunisikiliza….’

‘Kwanini mzee…mimi nilitaka unielewe,…’ nilisema kwa sauti,..sikupenda mzee wa watu ajisikia vibaya kwa maamuzi yake ya kunitetea, sikutaka mzee aungane na wengine ili nionekane mimi ni mbaya kama walivyokuwa wakiniona wengine..kama ni kuondoka iwe ni kwa nia njema tu, ya kuikoa ndoa ya watu ,mzee huyu umenisaidia sana, kwa ujumla ananidai….,kwa fadhila zake… hata kama nikiondoka lakini ingelikuwa ni vyema angenielewa, tu…

‘Sasa  kwanini mzee umeondoka….hata bila kukushukuru…’ nikajikuta naongea mwenyewe tu….ni kiukweli, sikutaka tena…kuwepo hapo, sijui…maana ningeenda wapi,….na kama nikiondoka kwenye hiki kijiji, sizani kama nitaweza kurudi tena…ni vipi nitakutana na nyuso za watu wa kijiji hiki…., nilijiona mchafu, nilijiona sifai kwenye jamii, lakini nikajiuliza kwa kosa gani, kwani  mimi nilifanya nini kikubwa ambacho wengine hawajakifanya

Labda mimi sikustahiki kuwemo humu duniani, na hapo wazo la kujiondoka hapa dunia, hata kufa likaanza kunijia akilini…nilitamani kabisa nitoweke hapa duniani, nisionane na nyuso za watu….

‘Bora nife tu….’nikasema na hapo hapo nikasema kwa sauti

‘Ina maana hata mzee, na yeye kayaamini hayo…..’nikasema huku sasa nikiwa naanza hatua za kwenda kuanza kupanga  vitu vyangu niondoke…..

‘Hata mzee jamani….ni yeye peke yake aliyewahi kunielewa…’ nikasema tena huku kichwa kikianza kuniuma, niliwaza sana…na wazo la mzee likaaka sana kichwani, nikimuoena huruma jinsi nilivyomsumbua ….. mzee wa watu,

Nitamlipa nini mzee wa watu….hata shukurani sijawahi kumpa…., na sasa keshaondoka, na sitaweza kumshukuru .., mzee ambaye alionekana mwenye hekima, huruma na upendo, alinifanya mimi kama binti yake na alinisikiliza yale niliyomuambia awali,…

‘Sasa kwanini mzee hukuvuta subira kidogo, nikakufichulia siri…siri ambayo…ooh,..’nilijikuna kichwa nikitafuta wapi pa kupenya , wapi …dunia ipasuke nimezwe…..

Niliona nisiendelee kulia, kujitesa na mawazo… kwani nilijua mzee ana sababu kubwa ya kuyafanya hayo yote, na kwa haraka nikajua sababu hizo….nilichanganua sababu hizo kichwani kwa haraka, ujue hayo ni mawazo yaliyonijia kichwani kwa muda mfupi,hata  kabla mlango haujafunguliwa…na kipindi hicho sikuwa nimejuwa kuwa  kuna mtu angelikuja, na mimi sikupenda mtu aje, nilihitajia muda wa kujiandaa na kuondoka, na kutokomea kusikojulikana…

Niliyachanganua sababu za mzee kuamua hivyo alivyoamua,..haya niliyachanganua kichwani, ili kujirizisha kuwa mzee wa watu hana hatia, hajaamua tu….nikawaza kichwani kwa haraka…
Kwanza, ukumbuke mzee alishapata ushahidi kutoka kwa mama mwenye nyumba,…sijui walichoongea wakati mzee alipofika kusuluhisha hilo tatizo ili kuiokoa  hiyo ndoa,…na sikujua mzee huyo aliitwa saa ngapi, nahisi alipigiwa simu.

Ila  ninachojua ni kuwa mama mwenye nyumba huyo kabla….hilo nililijua kabla kuwa mama huyo aliwahi kwenda kwa huyu mzee kumlalamikia kuwa mimi sio mtu mwema, na mzee hakulichukulia haraka, ila nakumbuka niliambiwa kuwa mzee alimuahidi huyu mama kuwa kama utaupata ushahidi unaonyesha kuwa mume wake ana mahusiano na mimi, na akamuonyesha mzee huo ushahidi,  basi  mzee hatakuwa na msamaha na mimi, yeye mwenyewe atanichukuliwa hatua kali, na hatua hiyo ni mimi kufukuzwa hapo nyumbani…

‘Ushahidi…mmh, najua tu, picha…!’ nikasema kwa sauti. Nilijua kwa vyovote  huyo mama atakuwa alimuonyesha huyo mzee huo ushahidi wa picha.

Pili kutokana na taarifa alizozipata huyo mzee kutoka huko kijijini kwetu alipokwenda kutafuta ukweli, huko alikutana na hao wanaume wanne na pia wazazi wangu,na watu wengine mbali mbali, na wote walisadikisha kuwa mimi nilikuwa na tabia mbaya, nilishindikana, sikuwasikiliza wazazi wangu…. lakini kubwa zaidi ni kuhusu kuwa eti…

‘Eti mimi nitakuwa nimeambukizwa ugonjwa wa ukimwi na nimeambukizwa na mmoja wa hao wanaume, kwani nilitembea naye na wengi wanaamini hata hiyo mimba ni huyo mwanaume sijui kwanini wanaamini hivyo…’nikasema kwa sauti ndogo

Nilisikia kuwa huyo jamaa alikuja kujitangaza baadaye wakati mimi nimeshaondoka huko kijijini kuwa kaathirika,…mimi niliposikia uvumi huo kwa mara ya kwanza sikuamini…lakini sasa imekuwa hivyo, lisisemwalo lipo…wanakijiji wameambiwa,…na hata kuthibitisha.

Kwahiyo mzee alichokuwa akihitajia kutoka kwangu ni kauli yangu tu, kuwa  kweli nimetembea na hao wanaume wanne..,na mmojawapo ni huyo jamaa….. na zaidi ya hayo yeye alishawaahidi wanakijiji kuwa kama nimeathirika kweli, na kama nilitembea na hao wanaume wanne …na ikagundulikana kuwa lengo langu ni kuusambaza huo ugonjwa, hatua kali dhidi yangu zitachukuliwa…na hatua hizi ni mimi kufukuzwa hapo kijijini, kauli hiyo aliitoa kwa raia-wanakijiji, waliofika kumlalamikia.

‘Mimi nawaahidi kuwa itagundulikana kuwa ni kweli…huyo binti katembea na hao wanaume wanne, mimi sitakuwa na msamaha kwake,…na ikizingatiwa kuwa mmojawapo kaathirika, …basi nitasimamia upande wenu, …hilo nawaahidi,..’akasema mzee

‘Mzee chonde chonde…’wakazidi kusisitiza

‘Kwani pamoja na hayo, huyu binti ana tofautii gani na mabinti zetu hapa kijijini, au ni kwa vile ….?’ Akauliza mzee

‘Mzee huyu binti ni mrembo, ana mvuto, na ni kishawishi kikubwa hapa kwetu, anaweza kuutumia urembo wake huo kuwashawishi vijana wetu, au waume zetu, huoni hilo ni hatari kabisa, mzee, tumia hekima zako umuondoe huyu binti….’aliambiwa

‘Sasa niwaambie kitu…kama ni mkosaji, kama mnahisi ana tabia hiyo, ya kuweza hata kuwarubuni waume zenu, na sijui kwanini waume zenu warubuniwena huyo binti kwa hali kama hiyo…hawana huruma….sawa, sasa nipeni ushaidi wa kulithibitisha hilo...’aliwaambia

‘Sisi tulifika hadi huko kijijini kwao, kuna taarifa zimeenea kuwa huyo mwanamke ni mhuni kupundikia, tunaweza kumuita malaya,…katembea na wanaume zaidi ya mmoja, …yaani mzee, huyo ni kicheche…ana tabia mbaya na la kuogopewa tumesikia kuwa mmoja wa mwanaume aliyetembea naye keshagundulikana kuwa kaathirika, …kama huamini nenda mwenyehuko kijijini  ukalithibitishe hilo….kuna ushahidi wa kutosha,..utauona mwenyewe….’akaambiwa

‘Hayo mumesikia…hayo ni ya kuambiwa, mimi naongea na huyo binti mara kwa mara, niliwahi kumuulizia kuhusu hilo na alisema hayo ni maneno ya huko kwao,…ni tabia za atu kuwavumishia watu uwongo,….ni  kwa vile tu wanamchukia, yeye yupo mbali na tabia hizo…sasa sijui, kwanini hakuwahi kuniambia ukweli huo…’akasema mzee

‘Uliwahi kumuuliza kuhusu hao wanaume wanne, kuwa aliwahi kutembea nao…?’ akaulizwa

‘Kwanini niingie undani wa hayo, nitakuwa kama simuamini, yeye kaniambia kuwa hana tabia hizo chafu,nikimuhoji sana kihivyo, ataniona simuamini,….na kiukweli mimi nimemuamini..na kutokana na hali aliyo nayo, sikutaka kumweka kwenye hali ya majonzi…jaribuni kujiweka kwenye hiyo hali yake…’akasema mzee

‘Sisi mzee tunakuhakikishia hilo, na ushahidi utakuja kuupata…lakini hata hivyo, ni lazima tukutane tulijadili hilo, maana naona wewe mzee unalichukulia kirahisi tu…huwajui hawa vijana wetu wa siku hizi….waongo, hawana ukweli…’akaambiwa

Kwa malalamiko hayo, wazee na wajumbe wa kijijji walikutana, na mzee akawekwa kiti moto kuuliziwa,na Mzee mbele ya baraza la kijiji , aliwathibitisia kuwa huyo binti hana makosa , mambo yote nasingiziwa tu;

‘Huyu binti ni mhanga wa udhalilishaji, akina mama, mabinti zetu wanadhalilishwa,…wanabebeshwa mimba na wanaume waliofanya hivyo wanawakana.. na wanakuwa hawana namna ya kujitetea, watakwenda wapi…niambieni,… huyu binti nimemchunguza nimegundua kuwa ni mmoja wa wahanga hao, ndio maana mimi nimeamua kumtetea, ili tuweze kuangalia jinsi ya kumsaidia, na ikibidi tuonane na wazazi wake, na huyo aliyembebesha mimba awajibike…’akasema.

‘Lakini mzee…..’wakazidi kumlalamikia, hapo ni kabla ushahidi haujapatikana, ushahidi wa watu na mzee kwenda huko kwetu, na ushahidi wa mama mwenye nyumba….

‘Sasa ushahidi umepatikana, na mzee keshaniona mimi ni muongo….. unatarajia nini hapo, mimi nina usalama hapa kweli,  kwanza nitapitaje mitaani, nikikutana na watu nitakuwa nikinyoshewa vidole , …..hapana ni lazima niondoke hapo haraka, lakini niondoke niende wapi…’ nikazidi kuwaza

Vyovyote itakavyokuwa nitamshukuru sana huyu mzee, kwani hata Wanakijiji wa hapo waliona ajabu sana kwa jinsi mzee huyo alivyoamua kunitetea, kwa jinsi nilivyosikia  mzee huyu ni mmoja ya wazee wanaoheshimika hapo kijijini kwa msimamo mkali, msimamo wa kupinga mambo machafu yanaoharibu vijana na wanajamii hapo kijijini,…yeye akachaguliwa kuwa mzee mshauri na kiongozi wa kusimamia tabia njema za hapo kijijini.

Lilipotokea hilo na mzee kuonekana tofauti na tabia yake, wenzake wakajiuliza kulikoni na wabaya wake wakaona ndio sehemu ya kumuharibia, wakaomba kikao kiitishwe kulizungumzia hilo jambo, na wao wakaonyesha msimamo wao kuwa wanapinga huyo mdada kuendelea kukaa hapo kijijini. 

Kwa shinikizo hilo ndio maana mzee akawa hana budi, akaona ni heri  kulifuatilia hilo tatizo kwa undani zaidi licha ya kuwa ndoto yake ilikuwa imemuonyesha kuwa mimi sina hatia.

Yeye mzee hata hivyo aliwaambia wenzake, ….hasa wale ambao muda mwingi walikuwa wakitafuta mwanya wa kumchafua …aliwaambia wazi wazi kuwa yeye kama yeye hawezi  kukubaliana na hizo shutuma mpaka kuwe na ushahidi wa dhahiri,….akawapa changamoto wapinzani wake hao kuwa walete huo ushahidi kulithibitisha hilo;

‘Kama mkileta huo ushahidi na kugundilikana kuwa huyo binti ana kosa mimi sitasita kuwa pamoja nanyi, ilii huyo binti achukuliwe hatua stahiki kutokana na taratibu zetu za hapa kijijini, na hatua ya juu, inayomfaa kuhakikisha kuwa tumemfukuza huyo binti hapa kijijini…lakini kwa hali kama hii, ya maneno tu, hatuwezi kufanya hivyo, tutakuwa tumekosea sana….’akasema
Baadhi ya wajumbe, waliamua kuutafuta huo ushahidi, ….

Haya wajumbe wakafanya kazi yao japokuwa sikuambiwa zaidi..ila tetesi zilinifikia kuwa kwa uchunguzi uliofanywa uliashiria kuwa mimi nina makosa…hakuna aliyekuwa na tafsiri nyingine,…walisema huko kwetu ukinitaja mimi ni gumzo la binti aliyepotoka…na nimekimbia kwa kashfa…

Nilishindwa kujua kwanini, kwani mimi ni wa kwanza, wapo wengi waliopata ujauzito hata bila kuolewa, wakakataliwa na waliosadikiwa kuwapa mimba, na taratibu zilifanyika yakaisha, lakini kwanini mimi ikawa tofauti…huko kijijini na sasa hapa.. hakuna aliyeangalia utu au ubinadamu, kila mmoja aliyesikia hayo alikuja na msimamo mmoja kuwa mimi niondoke hapo kijijini, sifai, nitaharibu jamii….nitawaambukiza vijana na waume wa watu ukimwi..

Eti mimi nina ukimwi, sijawahi kupimwa,..kama kweli ninao, mimi sijui kama nina huo ugonjwa, lakini watu wameshaanza kuninyanyapaa…oh…eti ni kuwa huyo mwanaume, kati ya hao wanne kaniambukiza, lakini angalau wangetafuta ushahidi wa kitaalamu, nipimwe basi…ili, nionekane ninao….’nikawaza hilo huku nikijawa na wasiwasi,

‘Huenda kweli ninao, mimi sijui, labda kwa vile naumwa umwa hivi,…kiukweli kila mara naumwa hiki, mara kile,  mara damu inanipungukia, lakini mbona hata docta alisema ni kawaida tu, inatokea  tu….,na sijui…na hata hivyo...sijawahi kupimwa, kwa ajili ya ugonjwa tu….. maana mara zote ninapokwenda kupimwa, sikumbuki kuchukuliwa kipimo hicho,…ila nakumbuka wakati naongezewa damu….sijui , ila docta mmoja aliwahi kuniuliza kama niliwahi kupima huo ugonjwa nikamwambia hapana…na hakusema zaidi

Inawezekana ninao…lakini kwa vipi..ooh, hata sijui…jamani sijui…ilikuwaje,…hata mimi najiona kinyaa, kwa hicho cha kutembea na hao wanaume wanne..ilikuwaje,….nawaambia kiukweli hata mimi sjui, ni siri…ni siri ambayo nilishindwa kuing’amua, lakini ipo siku …ipo siku kama nikikutana na hao wanaume wawili

Kwahiyo kwa hivi sasa msiniulize kwanini ilitokea hivyo……jamani sijui ilikuwaje….lakini kama ni hivyo kama kweli ilitokea hivyo…., basi ninao, na nashindwa kuelewa kwanini madocta hawakuniambia…au ndio wamevujisha kuwa ninao…sasa kwanini hakuniambia mimi mwenyewe…nikaanza kuingiwa na mawazo mengine, wasiwasi..mashaka ambayo sikuwa nayo, kuwa huenda kuwa kweli nina huo ugonjwa.

Ndio maana wanakijiji waliofuatilia kuchunguza kuhusu hizo kashafa dhidi yangu waliona kuwa kweli mimi ni mkosaji, na hakukuwa na dalili za kuonyesha kuwa kuna kusingiziwa au unyanyasaji, taarifa zilikuwa kuwa mimi nilikuwa mjeuri, sikuwasikia wazazi wangu nikawa natembeza uhuni mitaani, na mambo ya aibu,hayo ndiyo yamezagaa kijijini kwetu,….kwahiyo huko nikionekana itakuwa ni kuzomewa tu,….…na mzee wa watu aliposikia hilo akawa hana namna tena, na yenye kama  kiongozi muaminika,akatakiwa kutoa kauli…

Yeye kabla hajachukua hatua yoyoye aliamua kujirizisha ndio maana alifunga safari ya kwenda huko kwetu, na alikwenda huko baada ya mama mwenye nyumba mfadhili wangu kuja kwake tena kumlalamikia kuwa mimi sasa nayafanya hayo hadharani, nimekuwa mkaidia nimekuwa kama mke ndani ya nyumba, sifanyi kazi, nasingizia kuumwa, natumia nafasi ya kuumwa kwangu ili nikutane na mume wake…

‘Una uhakika na hayo unayoyasema ina maana humuamini mume wako…’mzee akasema

‘Wanaume hawaaminiki..hasa wakipata uchochoro…huna mwanamke ni rahisi sana akiwambiwa , na hata bila kutongozwa anajiuza..anajirahisi, na mume wangu sio malaika, ni lazima katekwa na huyo binti..ule urembo umemzuzua..mtu anakaa khanga moja, hajali kujisitiri, unafikiria nini…’akanisingizia mengi, kitu ambacho sio kweli, mimi nikiwa hapo nyumbani nikijua wapo, nahakikisha nimevaa gauni kubwa , pana, siunajua magauni ya akina mama wakiwa wajawazito..sikuwahi kuvaa nguo fupi….labda kama ilitokea siku chache!

‘Mimi nimeshaongea na mume wako kanihakikishia kuwa hawezi kufanya uchafu huo,…na mume wako namuamini sana…lakini kama una uhakika, ..nitafutie ushahidi,…kama utaniletea ushahidi, ….siwezi kuvumilia tabia hizo nitamfukuza, sitajali kuwa mimi nilimdhamini…’nasikia alisema mzee huyo siku alipokutana na huyo mama.

 Haya limetokea, na mama mwenye nyumba keshaupata huo ushahidi….mzee alipoitwa ina maana alionyeshwa huo ushahid, ushahidi wa picha, na kuambiwa haya mtu wako uliyekuwa ukimtetea ndiye huyu, ona anachofanya na mume wangu, ….mzee kuiona hiyo picha hakuamini, akamuuliza baba mwenye nyumba…vipi kulikoni…

‘Wewe , si uliniambia ….’ukumbuke haya nayawaza tu kichwani, sikuwa nimeyafahamu kwa muda huo…lakini ndivyo ilivyokuja kujulikana baadaye, kwa siku hiyo sikuwa nimekijua walichokiiongea, ila kwa pale niliwaza hivyo …..

Nahisi baada ya malumbano makali, ikaonekana kuwa mimi sifai, na mzee akaona ni heri mimi niondoke, lakini kabla hajaungana na wengine  akaona  kwanza aje kulithibitisha hilo kwa kutaka kusikia kaulii yangu..kauli yangu tu, ndiyo aliyoitaka kama ningelijua hilo ningetafuta mbinu za kutokumjibu, lakini nilimuamini sana huyo mzee nikaona nimuambie ukweli …nimjibu anavyotaka yeye...ila mengi ya nyuma ya pazia yalikuwa ni siri ambayo hakuvuta subira nimsimulie, angeliyajua hayo, nahisi angepasuka kwa hasira….sasa itabakia kuwa siri yangu

Hata hivyo mimi nilijua kuwa ujio wa mzee ungelilenga moja kwa moja swala la hiyo ndoa, kuwa nimefumaniwa,….. Lakini cha ajabu mzee hakutaka kuliongelea hilo la mimi kutembea na mume wa mtu, hakutaka kunitupia shutuma hizo , yeye akaja na jambo jingine kabisa,  kutaka kujua kama kweli nilitembea na hao wanaume wanne.. na aliposikia kauli yangu akaaondoka

Je ni hiyo kauli tu!,…hapana ni zaidi ya hilo,..mimi kwa muda huo sikutaka kuyajua zaidi, nilichotakiwa kukifanya ni kuondoka hapo,…sikutaka kukabiliana na wenye nyumba tena, nilijua ni nini kitatokea, naogopa nitazidiwa kwa maneno nitajibu na majibizano yatazaa vita, …na mimi sikuwa na nguvu tena ya kugombana na mtu, niliyo nayo yanatosha, nikakumbuka kauli ya mzee wakati anaondoka alisema;

‘Kwa jibu lako hilo, kwa kauli yako hiyo kuwa ulitembea na wanaume wanne, na si mmoja, si huyo mwanaume wako tu, na nilijua hao wanakusingizia, ndio niliona ushahidi lakini waweza kutengenezwa..nilitaka kauli yako, na wewe umelithibitisha hilo, mmmh, sasa….hapana, hapoo  tena siwezi kuvumilia….’ na ndio, akaondoka

Kumbe alipoondoka hapo alikwenda moja kwa moja kuitisha kikao chao cha wajumbe wa kijiji. Wajumbe hao walikuwa wakisubiria kikao hicho, kwani  aliyekuwa kikwazo  cha kufanyika kikao hicho cha maamuzi ni huyu mzee, ….ni huyo mzee,…

Sasa kikao kinaenda kuitishwa, je mzee atasema nini kwenye hicho kikao, kwani yeye ndiye aliyekuwa kaweka pingamizi, je atanitafutia sehemu nyingine…niende kuishi kwake, yeye hana uwezo wa kunichukua kwake kwani nyumbani kwake kumejaa, ana familia kubwa…siwezi kwenda kwake, kamwe..ni aibu, nitaishije huko… nitakuwa mzigo mwingine kwake…

Kwa vyovyote iwavyo, uamuzi wa kikao hicho, ninajua utakuwa  nifukuzwe hapo kijijini, na nikifukuzwa nitakwenda wapi….Nirudishwe kijijini kwetu..na je mzee anaweza kunitetea tena kwa lipi…sizani…! Labda watapanga kunirejesha nyumbani kwetu….!

‘Hapana kwetu siwezi kurudi hata kama ni kwa dawa…..’, nilishawaambia,

‘Kwetu hasa kwa wazazi wangu sirudi , ni bora kufa….’ Niliwaambia mapema, kwahiyo wazo la kunirejesha kwetu halipo,…wanalifahamu hilo,…labda watumie nguvu, na wakitumia nguvu, je wazazi wangu wapo tayari kunipokea, hasa baba , baada ya kashifa zote hizo …sizani ,mimi namfahamu mzee wangu ana msimamo mkali, akiamua kaamua….

‘Hapana huko sirudi,….na kama wakifanya hivyo,watarudisha maiti yangu….’nikajisemea na ndipo mlango ukafunguliwa..na kukatiza mawazo yangu, nikatoa macho ya uwoga….!

NB; Hii ni nyongeza kabla ya kukutana na huyo mtu aliyeingia, sijui ni baba mwenye nyumba au mama mwenyenyumba au ni mzee alirudi tena, au ni walinzi wa kijiji walikuja kunifukuza. 

Nimeamua kuifafanua sehemu hiyo kwa undani zaidi ili watu waelewe, kuna watu wameniuliza nafikiri sasa watakuwa pamoja nami.
   
Ni mimi: emu-three

No comments :