Hiyo ndio sehemu niliyomuhadithia kaka
yangu, ndugu zanguni,...’akasema huyo mzee tuliyemkuta kwenye hiyo nyumba,
akaendelea kusema
‘Sasa mengine yalikuja kutokea baada
ya huyo kijana kurejea hapa nchini,.....’akasema
‘Kijana yupi..?’ nikamuuliza
‘Kijana ambaye alikuwa akiishi na
profesa huko nje, kijana ambaye alikuja kuungana na mama mtemi .....’akasema
‘Kwanini alirejea nchini,..?’
nikamuuliza
‘Unajua hayo yalitokea kama mapinduzi,
....kila taifa lina hili tatizo, la vijana wengi kukosa ajira, na wenyeji wa
nchi husika mara nyingi hudhania kuwa ajira zao zimechukuliwa na
wageni,.....ndio maana wao hawana kazi....hili lilitokeapia huko ....’akasema
‘Huko Ulaya!?’ nikamuuliza
‘Ndio, huko Ulaya,.... vijana wa nchi hiyo
aliyokuwa akiishi profesa nao walikuja juu, wakiandamana kutaka wageni
waondolewe makazini...ili wao wenyeji wawezi kuajiriwa,...kwanini wageni
wakapate ajira wakati wao wenyeji hawana ajira....na ukumbuke kuwa wenzetu,
wana taratibu za kuwalipa watu wao wale wasiokuwa na ajira japkuwa kiasi
wanacholipwa ni kidogo....’akasema
‘ Basi kutoka na ghasia hizo,
wanasiasa wakainglia kati, ikabidi upite mchujo wa raia wa kigeni upite, na
wale walioonekana kuwa wanaweza kurejeshwa makwao, warudishwe, na wengine
walifanyiwa utaratibu wa kupata ajira kwenye balozi za nchi hizo kwa wale walioonekana wanafaa kufanya
kazi hizo, na mmojawapo alikuwa kijana wetu,...’akasema huyo mzee
‘Kwahiyo kijana wetu akarudi na mkewe...’akaongezea
‘Na mkewe....?’nikamuuliza kwa
kushangaa
‘Ndio walishaoana na huyo mtoto wa
mama mtemi na wakati wanakuja huku walikuwa tayari wana mtoto mmoja, na wa pili
walimpatia wakiwa huku huku kwetu...’akasema huyo mzee na kutulia kama vile
keshamaliza kisa , na mimi nilipoona hivyo nikamuuliza;
‘Sasa hiyo hali ya kuchanganyikiwa
ilitokeaje maana katika maelezo yako tumesikia zaidi kuhusu wewe, hukutuelezea
kuhusu huyo kijana ambacho ndicho tunachokihitajia...?’ tukamuuliza
‘Najua...ila nilitaka muone chanzo
halisi , ni wapi kijana wetu alitokea....kama angelikuwa na uwezo wa kuongelea
mambo yake angeliwaelezea zaidi kwa upande wake,...’akasema
‘Kwahiyo ....?’ nikataka kuuliza na
huyo mzee akaonyeshea mkono kama kuninyamazisha akasema;
‘Nitawaelezea msijali, ...jinsi
ilivyokuja hadi kijana akawa hivyo....si mlimkuta barabarani kapanga mavitabu, anatoa ‘lecture’...moja baada ya
nyingine au sio.....’akawa kama anauliza
‘Ndio baadaye akaanza kuporomosha
matusi...’mwenzangu akasema
‘Yah...ndio muone nini maana ya
mzazi...na sio kwamba mzazi, au wazazi wake walisema au walitaka awe
hivyo..hapana mungu mwenyewe kataka kuonyesha uwezo wake....’akasema
‘Kwa vipi....?’ nikamuuliza
‘Hii ni sehemu ya pili,...ambayo
nitawaelezea yaliyotokea huku Tanzania......’akasema huyo mzee
******************
‘Ilibidi niwaelezee
kuhusu Profesa , maana yeye ndiye aliyesababisha hayo yote...’akaendelea kusema
Profesa kila
mara alikuwa akikiri hilo, na hata kufikia kutubu, kuwa bila yeye hayo yote
huenda yasingelitokea...hata hivyo, hadi kufikia kijana kuchanganyikiwa hiyo
ili ni baadaye ni kipindi ambacho kijana ana fahamu zake ana utashi wake,
usingeliweza tena kumbebesha lawama profesa
‘Muda ulifika
Profesa akawa sasa anaendelea vyema, na mara nyingi alikuwa akitumia dawa zake
za mitishamba, na ikafikia hatua afya yake ikaanza kuimarika, na hata akaanza
biashara yake ya kuuza dawa za kienyeji, na hata kupeleka mjini.
Na mara ya
kwanza alipofika hakutaka kabisa kupitia eneo alipokuwa kajenga, alijitahidi
kufuata masharti ya kaka yake, lakini mara pili hisi zikamvuta, akashindwa
kuvumilia.
Siku hiyo,
alimua kupitia tu angalau aone hiyo nyumba ipoje, kwani alishasikia kuwa
imekarabatiwa na kutengenezwa upya.....
‘Ngoja
nipitie tu nikapaone...’siku hiyo akasema na kweli akapitia huko.
Alipofika eneo hilo, kwanza alijiona kama
kapotea kwani mji ulikuwa umebadilika, mitaa mingi ilikuwa imeboreshwa , bara
bara ambayo kipindi hicho ilikuwa haina lami, sasa ina lami, akajisema moyoni,
kweli maendeleo yapo.
Akatembea
hadi pale kulipokuwepo nyumba yake,
hakuweza kuamini, japokuwa nyumba yake kipindi hicho ilionekana kubwa ya
kisasa, lakini sasa alichoona ni nyumba nyingine iliyojengekea kisasa zaidi....na
hakuna mabanda ya mbele tena, kilichoonekana ni ukuta mkubwa wenye nyaya za
usalama juu yake..
‘Mhh, hawa
wajanja wamefanya hivi ili nione kuwa ilikuwa sio nyumba yangu..’akasema huku
akiisogelea, na alipofika kwenye eneo la geti la kuingilia ndani, akagonga hodi
na mara akatokea mlinzi, kwanza hakumsemesha akawa anaangaza macho ya
kushangaa.
‘Unasemaje...?’
akauliza huyu mlinzi na profesa akawa anaendelea kukagua akitafuta mwanya wa
kuangalia kwa ndani.
Nyumba
ilikuwa imebadilika kabisa, imefanyiwa ukaratabati wa hali ya juu, sio ile
nyumba yake tena aliyokuwa akiifahamu, ni nyumba imara ya kisasa zaidi, ikiwa
na kila kitu cha nyumba ya kisasa.
‘Mhh kweli ni
kama imejengwa upya....lakini hawawezi kunipiga changa la macho, hii ni nyumba
yangu...’akasema kwa sauti na yule mlinzii aliyekuwa kasimama akimuangalia
akabakia kushangaa, akamuuliza
‘Nyumba yako
kwa vipi,...umechanganyikiwa nini. wewe....?’ akauliza huyo mlinzi
‘Hahaha
nimechanganyikiwa, ..hebi nikuulize wewe umekuja lini hapa mjini...?’ akauliza
‘Hata kama
nimekuja jana, juzi au mwaka juzi, inakuhusu nini wewe, ....?’ akauliza huyo
mlinzi
‘Maana
hufahamu chochote kuhusu hii nyumba awali ilikuwa ni ya nani....?’ akauliza
profesa
‘Mimi
nafahamu hii nyumba ni ya wenye hii nyumba ....’akasema
‘Wewe
ulikuwepo eneo hili wakati hii nyumba haijakarabatiwa..?’ akaulizwa
‘Sikuwa
nafanyakazi hapa, nilikuwa sehemu nyingine, lakini nilikuwa napita mara kwa
mara.....’akasema huyo mlinzi akionyesha hamasa ya kutaka kujua zaidi.
‘Kabla
haijakarabatiwa ulikuwa ukifahamu kuwa nyumba hii ilikuwa ni ya nani.....?’
akauliza
‘Mimi sijui,
na hainihusu....kwanini unauliza hivyo...?’akasema na kuuliza
‘Basi kwa
taarifa yako hii nyumba ilikuwa ni ya jamaa mmoja aliyejulikana kama
profesa....’akasema
‘Hahahaha....unanichekesha
kweli, mimi nijuavyo hii nyumba ilikuwa ya mzungu, ambaye alikuja kuwauzia hawa
wenye hii nyuma kwa hivi sasa.....ambao ndio wameamua kuikarabati kama
inavyoonekana kwa sasa....’akasema
‘Sawa, ipo
siku mtakuja kuujua ukweli.....’akasema Profesa na kutulia kidogo.
‘Ukweli wa
nini.....ili iweje, aah,....?’akasema huku akitaka kugeuka kuendelea na
shughuli zake
‘Samahani
nilikuwa naulizia huyu mtu anayeihi hapa yupo wapi?’ profesa akamuuliza huyo
mlinzi
‘Hayupo
kaenda kazini....’akasema huyo mlinzi bila hata kugeuka kumuangalia muulizaji.
‘Na mkewe, au
hana mke?’ akauliza Profesa na huyo
mlinzi akageuka sasa akiwa mkali, akasema;
‘Kwanini
unawaulizia, unataka nini kwao...una shida gani kwao?’ akauliza kwa hasira
‘Mimi ni
mgeni wao, nahitaji kuonana nao...’akasema profesa.
‘Ndio hivyo, nimekuambia
hawapo wamekwenda kazini....umenielewa au...’akasema huyo mlinzi akiwa kakunja
uso, na profesa hakutaka kuongea zaidi akageuka kutaka kuondoka, halafu
akasimama akageuka tena kuangalia muelekea wa hiyo nyumba, hakuweza kuona ndani
kwasababu ya hilo geti moyoni akawa anasikitika, na baadaye akasema;
‘Mhh, hiki
ndio ilitakiwa iwe kinua mgongo changu, kwa umri kama huu, ningekuwa na kiota
cha kunisitiri, naona mabanda yote yaliyokuwa hapa mbele wameyabomoa, yalikuwa
yakinisaidia sana kwa kukodisha.....lakini ...ipo siku, na ...tutapambana tu....’akasema
na yule mlinzi akawa anamuangalia huyo mgeni kwa macho ya kujiuliza, halafu
akasema;
‘Kwani wewe ni nani...?’ akauliza huyo mlinzi
‘Ipo siku
utajua tu....’Profesa akasema na kugeuka kuondoka , alirudi sehemu ambapo
alikuwa akiuzia dawa zake, akaendelea kutafuta wateja, maana kazi ya kuuza dawa
kama hizo inahitaji kuhangaika kweli, na ilibidi kufanya mazingaumbwe na vioja
mbali mbali ili kuwaita watu waje kuvutika nazo.
Siku hiyo
hakutaka kurudi mapema kijijini, sio kwasababu ya biashara, lakini alikuwa na
hamu ya kuwaona wamiliki wa nyumba yake, aliendelea kuuza dawa zake hadi jioni.,
Na ilipofika jioni, akafunga funga shughuli zake na haraka akarudi tena mitaa
ya iliyokuwa nyumba yake.
Alipofika
akamkuta mlinzi mwingine sio yule aliyeonana naye mchana, ikabidi kwanza aanze
kumdadisi.
‘Samahani
afande, eti mwenye nyumba hii kesharudi....?’ akauliza
‘Kwanini
unauliza hivyo, wewe ni nani?’ mlinzi akauliza
‘Mimi natokea
huko kijijini, mwanzoni alikuwa akiishi jamaa yangu hapa, ndio nataka kujua
kama yupo au kasafiri...?’ akauliza
‘Jamaa
gani...?’ akauliza
‘Alikuwa
mangaji wa hii nyumba, lakini kabla hajakarabatiwa....’akasema
‘Alishandoka,
mbona siku nyingi sana...hii nyumba sasa hivi inamilikiwa na watu wengine
kabisa....’akasema
‘Inamilikuwa
sio imekodishwa, sio kuwa hawa wanaoishi hapa ni wapangaji, na wenyewe wanaishi
ulaya...?’ akauliza
‘Walikuwa
wakiishi ulaya ndio, sasa wamekuja kuishi wenyewe, hakuna mpangaji, wanaishi
wenye nyumba....’akasema
‘Ohoo, kumbe
wanaishi wazungu, ndio maana wameitengeneza hivi...’akasema profesa na huyo
mlinzi akataka kuachana naye, lakini profesa akamuuliza swali jingine.
‘hivi
unamfahamu aliyekuwa mumiliki wa hii nyumba kabla haijauzwa....?’ akaulizwa
‘Namsikia tu,
mimi sikuwahi kuonana naye.....’akasema
‘Unamsikia
tu,...alikuwa nani, unamsikiaje?’ akaulizwa
‘Namsikia tu,
alikuwa naye anaishi huko Ulaya, akaishiwa , akawa naumwa sana, ikabidi auze
nyumba yake ili awezi kujitibia, nasikia alikuwa tapeli,...akaja kuumwa huu
ugonjwa, akarudishwa huku akiwa kazidiwa, na ameshafaiki dunia,....huu ugonjwa
unawamaliza sana watu wetu....’akasema huyo mlinzi
‘Nani
alikuambia hivyo?’ akaulizwa
‘Watu wengi
wanaomfahamu mbona wanalifahamu hivyo, ....’akasema na mara akaangalia kwa
ndani, akasema
‘Ulikuwa na
shida gani ndugu...?’ akauliza sasa
‘Nataka
kuonana na huyo mumiliki wa hii nyumba, umesema ni mzungu au?’ akauliza
‘Kama ni kazi
hakuna kazi , walishaniambia hawataki watu kuja kuwasumbua, niwaeleze kabisa
kuwa hakuna kazi....’akasema mlinzi
‘Mimi natokea
kijijini, nahitajia kuonana na mwenye nyumba hii nina mashitaka dhidi
yao....’akasema profesa kwa ukali
‘Mashitaka ,
mashitaka gani...?’ akauliza mlinzi
‘Wewe niitie
au niingie nionane nao mimi mwenyewe....’akasema kwa ukali, na mlinzi akaingiwa
na hamasa, akamuangalia huyo mgeni kwa makini, halafu akasema;
‘Niwaambie
wewe ni nani..?’ akauliza
‘Profesa.....’akasema
na huyo mlinzi akamuangalia huyo mgeni kwa makini na kusema,
‘Wewe ni
profesa,...mmh, najua maprofesa ni watu waliosoma, wana kazi zao, ....sasa wewe
mbona ....’akasema na profesa akasema
‘Unaniitia su
niingie mwenyewe....’akasema kwa ukali
‘Hebu
subiri...’akasema na kufunga mlango vizuri, akarudi kibandani kwake akachukua
simu na kupiga, akawa anaongea, na sauti ilikuwa haisikiki vyema ila alisikia
jina lake likitajwa;
Baadaye
mlinzi akafungua mlango akasema;
‘Kaniuliza
maswali mengi, kwani mwenyewe alikuwa na miadi ya kuonana na rafiki yake
anasoma chuo kikuu, lakini anasema huyo mtu hajafikia ngazi ya uprofesa, sasa
akahisi anatania tu kwani ana ndoto ya kusoma hadi uprofesa, lakini wewe sizani
kama unasema chuo kikuu......’akasema
‘Niingie au
nikaje na askari, ndio utaniruhusu niingie...?’ akauliza profesa
‘Ingia ndugu,
Profesa......wanakusubiria ndani...’akasema sasa akimpisha huyo mgeni huku
akimuangalia kwa mashaka
‘Huko kwenye
mfuko umebeba nini....?’ akauliza
‘Dawa zangu,
nauza dawa....una matatizo ya ngiri,...tumbo kijaa gesi, nguvu za
kiume,....’akaongea kama anavyonadi dawa zake akiwa kazini..
‘Hapana
ndugu, kama lengo lako ni hilo kuwauzia dawa, watu hao hawahitaji dawa hizi za
kienyeji, ...’akasema
‘Sitaki
kuonana nao kwa ajili ya dawa, kama una shaka na hilo, nahifadhi mzigo wangu
hapa, nataka kuonana nao kwa maswala mengine kabisa...’akasema sasa akikagua
mandhari ya ile nyumba maana alikuwa ameshaingia kwa ndani, akageuka upande
ambapo kulikuwa na mti na kiti cha kubembea, mti ule na kiti kile bado
kilikuwepo, akasema
‘Kiti changu
bado kipo, naweza kwenda kukaa kidogo....?’ akauliza yule mlinzi akamuangalia
huyo mgeni kwa mashaka,akasema;
‘Unaweza
kwenda kuwaona, kama hunatajali, maana siruhusiwi kuongea na wageni hapa
getini, ...’akasema na profesa akaona asipoteze muda, akatembea huku bado
akikiangalia kile kiti, hadi alipofika kwenye geti jingine la nyumba.
Lilikuwa ni
geti la nguvu, unabonyeza kitufe linajifungua, na hapo unaiona nyumbe yenyewe
sasa, na kulikuwa na mtoto akicheza mpira kwenye bustani, alikuwa na sura ya
kizungu ,moyoni akajua kweli wenyeji ni wazungu.
Akasoegelea
mlango akagonga mara mbili tatu na mara mlango ukafunguliwa na binti, ambaye
alimuangalia huyo mgeni akionyesha mshangao usoni, akasema
‘Wewe ndiye
profesa...?’ akauliza
‘Ndio,
wenyeji wapo wapi, na wewe ni nani?’ akauliza kwa sauti la lafudhi ya kizungu,
kuonyesha msisitizo, na huyo binti akawa kama anajizuia kucheka, akashika
mdomo.
‘Kwanini
unacheka....?’ akauliza
‘Hapana samahani
unavyoongea tu, unanichekesha...’akasema
‘Wewe ni
nani...?’ akauliza
‘Mimi ni
mfanyakazi wa ndani wa nyumba hii subiria nikuite wenyewe....’akasema sasa
akionyesha mashaka...
‘Kama
nakufahamu vile....’akasema Profesa , alijisemea tu kiutani
‘Hapana
hunifahamu....’akasema huyo binti, na kufunga mlango, hakumkaribisha ndani,
ukapita muda, na baadaye akarudi na kusema;
‘Karibu
ndani....’akafungua mlango na profesa akaingia ndani
‘Wenyeji wapo
wapi...?’ akaendelea kutumia lafudhi ile ya kizungu, na yule binti akafanya
vile vile akitaka kucheka lakini akaweka mkono mdomoni kujizuia
‘Wanaogelea....’akasema
‘Kwani hii nyumba
imewekwa bwana la kuogelea ...!?’ akauliza Profesa kwa mshangao na huyo binti
akatabasamu na kusema
‘Ndio....lipo
kwa nyuma huko,...’akasema huku akiendelea kunyosha nguo kwa haraka yanekana
zilihitajika kuvaliwa na wenyewe nyumba.Na kwa muda huo profesa alitarajia
kuulizwa unatumia kinywaji gani, lakini binti alikuwa akihangaika na kunyosha
nguo tu....
‘Naweza
kupata maji ya kunywa...au..?’ akauliza profesa na binti akaangalia nyuma ya
profesa kama kutoa ishara, hakusema neno, na profesa akageuka nyuma na akaona
mashine ya maji iliyoandikwa Cool Blue,
na vikombe vya plastiki vya kutumia mara moja, akasema
‘Oh,
afadhali,yaani nina kiu.....basi wewe endelea tu na kazi yako mimi nitajisaidia
mwenyewe...’akasema na kuanza kunywa maji, alikunywa maji kwa tani yake, halafu
akasema
‘Sasa basi
tumbo limejaa,....maji baridiiii...mmh ’akasema na kurudi kukaa kwenye sofa
akakunja nne akimuangalia yule binti akiendelea na usafi na kwa nje kwa kupitia
dirishani akamuona binti au mwanadada wa kiziungu akiwa na vazi la kuogelea, akipita
na kuotea alikuwa kabalia mawani usoni, akajaribu kuchunguliza zaidi kwa nje
lakini hakumuona tena.
‘Huyo
mwanadada huko nje mzungu ndiye mwenye nyumba au....?’ akauliza profesa
akichungulia kule dirishani na yule binti akageuka kuangalia huko nje kwa
kupitia dirisha hilo la viyoo lakini hakuona kitu, hata hivyo akatikisa kichwa
kukubali.
‘Mhh, nilijua
tu, hata hivyo nitapambana nao...’akasema profesa na huyo mdada akawa
anaendelea kunyosha nguo hakusema kitu.
‘Wewe ulianza
kufanyakazi na hawa watu toka lini?’ akauliza
‘Siku nyingi,
tangu walipofika toka huko ulaya....’akasema huyo binti
‘Kwahiyo
kumbe unawafahamu sana....nitafurahi nikipata muda tukaongea wote kama
hutojali...’akasema
‘Kuhusu
nini...?’ akauliza huyo binti, bila kumuangalia
‘Nitakuja
kukuambia, ngoja nionane nao kwanza....’akasema na kuendelea kuangalia humo
ndani kwa makini, halafu akasema;
‘Mhh, kweli
wameiboresha, mwanzoni haikuwa na ukubwa huu, na humu
wamepaongezea......’akasema na huyo binti akainua uso na kumuangalia, Profesa
lakini hakusema kitu.
Profesa sasa
akawa anaendeela kukagua mandhari ya hapo ndani kwa macho, .....na binti akawa
anaendelea na shughuli yake, wote wakiwa kimia.
Kilikuwa ni
chumba kikubwa cha maongezi kilichopangiliwa vizuri kabisa na kulikuwa na
masofa ya kisasa makubwa kweli....na katikati kulikuwa na meza kama ya mkutano,
imepangwa viti kuiznguka, na maua yasio asili yakiwa yamepangwa vizuri juu ya
hiyo meza...kulikuwa na matunda kwenye mabeseni,
Profesa
akaingiwa na hamu ya kutaka kuchukua moja, lakini akavutiwa na kitu kingine,
kwenye, ukutani kulikuwa na runinga kubwa, ikionyesha matukio mbali mbali, na
moja ya tukio na jamaa aliyefukuzwa huko ulaya kwa makosa mbali mbali, akawa na
hamasa ya kutaka ni wapi huko, na akilini na yeye akawa anakumbukia tukio lake....
‘Mhh, mbona
sisi hatuwafukuzi huku kwetu, kwao wanatudharau, wanatufukuza huku kwetu
tunawakumbatia, tunawaita tunawaona kama mungu mtu.....’akasema akisonya, na
huyo binti akatabasamu.
Akiwa bado
anaangalia kwenye runinga ambayo iliwekwa kwa sauti ndogo, mara sauti ikasikika
, ilikuwa sauti ya kike , na ilikuwa ni lafudhii ya kizungu ikiongea, na
ilionyesha alikuwa akimuongelesha huyo mfanyakazi.
‘Huyu mgeni
yupo wapi...’sauti ikauliza
Profesa
ambaye alikuwa kazama kwenye mawazo, akiangalia runinga, akajiinua pale alipokuwa
amekaa, kwani alikaa mkao wa kujiegemeza kama kulala upande upande, na haraka akageuza
kichwa kuangalia wapi sauti hiyo imetokea.
Profesa hakuweza kumuaona huyo aliyeongea, akahisi hueda
huyo mtu alishapitiliza na kuingia kwenye chumba ambacho kilionekana mlango
wake upo wazi, akamtumpia jicho huyo binti mfanyakazi, ambaye kwa muda huo
alikuwa akiendelea kunyosha nguo kwa haraka, ili kuwa na uhakika Profesa
akauliza,....
‘Yupo
wapi....?’ akawa anamuuliza huyo binti huku akiagalia kile chumba ambacho
mlango uo wazi, na huyo binti aliendelea na kazi yake bila kusema kitu.
Profesa akawa
sasa kakaa vizuri akijua kuwa mwenyeji wake sasa hivi atajitokeza na kwahiyo
anahitajika kujipanga jinsi gani ya kukabiliana naye, kwanza alishajiandaa
kutoa vitisho, kuwa nyumba hiyo alitapeliwa, kwani hati yake bado anayo....kwa
vile mauzo yalifanyikia ulaya, hati ya nyumba ilikuwa haikuchukuliwa, lakini
yaweza ikawa imepitwa na wakati..
‘Nitaanza na
hilo kujaribu,....’akasema na mara akasikia mtu akikohoa, ilikuwa ni kutokea
chumba kile ambacho mlango upo wazi...
Taratibu,
akageukia upande ul na kumuona huyo mwanadada wa kizungu akiwa kasimama
mlangoni, akiwa kageukia mlango wan je, kama vile anajua kuwa mgeni huyo bado
yupo huko nje. Profesa akataka kusimama ili amuone vizuri, lakini huyo
mwanadada akawa anatembea kuelekea pale alipokuwepo huyo mfanyakazi wa ndani..
‘Huyo mgeni
bado yupo nje....?’ akauliza huyo mwandada wa kizungu na huyo mfanyakazi
akanyosha mkoni kuonyesha pale alipokuwa amekaa Profesa na huyo mwanadada wa
kizungu, akataka kama kugeuza kichwa mara moja kwa haraka na kurejea kuangalia
kile alichokuwa akikiangalia, alikuwa akiangalia nguo alizokuwa akinyosha
mfanyakazi, halafu akachukua nguo mojawapo akasema
Kulikuwa na
kizuizi pale alipokaa Profesa na hao wenyeji wake, na ilimfanya Profesa asiweze
kuwaona vizuri, kama huyo mwanadada angelikuwa kasimama pale alipokuwa kasimama
huyo mfanyakazi ingelikuwa ni rahisi kwa profesa kumuona vyema.
‘Hii kamwekee
mume wangu ,ndiyo atakayoivaa...sawa eeh...’akasema huyo mwanadada wa kizungu, halafu
sasa akawa kama anataka kugeuka upande ule alipokaa mgeni, lakini akasita na
kuendelea kupanga hizo nguo alizokuwa akinyosha huyo binti, na kusema;
‘Mgeni
samahani kidogo, ...,sijui tukusaidie nini...’
‘Nashukuru,
wewe ni mwenye nyumba nataka kuongea na mume wako .....?’ Profesa akaanza
kusema akitaka kusimama, lakini alipoona huyo mwanadada anaendelea kufanya
jambo a huyo mfanyakazi, akarudi kukaa, profesa akajipa moyo akisema kimoyo
moyo;
‘Mambo mazuri
hayataki haraka..’akasema huku moyo ukimuenda mbio, akilini alihisi kitu lakini
hakuwa a uhakika nacho, akawa anasubiria....
Profesa akiwa
anasubiria moyoni akijaribu kujipa uhakika kuwa nyumba hiyo inamilikiwa na
wazungu, aligeuza kichwa chake kuendelea kuangalia runinga, alijua kabisa huyo
mwanadada wa kizungu hawezi kuongea lolote mpaka huyo mwanaume wake aje, huyo
mwanaume wake alikuwa bado akiogelea au akifanya jambo huko nje, na moyoni
akasema
‘Ni lazima nipambane
nao, hata kama ni wazungu.....’akasema na wakati anaongea kimoyo moyo huku akiangalia
kitu kwenye runinga, akahisi kuwa kuna mtu yupo karibu yake, ni yule mwanadada
alikuwa tayari keshafika kwenye sofa lililokuwa upande wa pili, .kuliani kwake,
akageuza kichwa ili kumuangalia huyo mwanadada wa kizungu na sasa wakawa wanaangaliana
uso kwa uso na huyo mwanadada,....
Profesa
alijikuta akishtuka, na kubakia kutoa macho ya kutokuamini hicho anachokiona
‘Ni
wewe....’profesa akasema huku akibakia mdomo wazi, na yule mwanadada aliyekuwa
ameshakaa, akasimama akionyesha wasiwasi naye akiwa katoa macho kuashiria kuogo,akawa
kashika mdomo, na kwa sauti yenye kigugumizi akasema;
‘What the hell,... Who is this man..?’
aliuliza huyo mwanadada wa kizungu akiwa bado katoa macho na kule kwenye mlango
wa kutokea nje, kukatokea sauti ya kiume, huenda alikuwa ndio mume wa huyo
mwanadada wa kizungu ikiuliza:
‘Kwani kuna
tatizo gani....’sauti ikasema,na hiyo sauti ikamfanya Profesa azidi kupatwa na
mshituka,...na kwa vile alishakuwa na tatizo la shinikizo la damu, akahisi
mapigo yakienda mbio,....pumzi ikawa kama haitshi, ila alijitahidi na sasa yeye
akasimama huku mkono mmoja ukishikilia lile sofa, akitaka kugeuka kuangalia
huko sauti ya kiume ilipotokea....
NB: Ni nani
huyo
WAZO LA LEO:Tabia njema ni pamoja na jinsi gani ya
kukirimu wageni, ..hata kama tuna haraka, au hatuna muda wa kuongea na huyo
mgeni lakini tuwe na namna njema ya kumfanya mgeni ajisikie vyema, asione
kadharauliwa, ..kwani kwa kufanya hivyo, kuonyesha hutaki mgeni, huna muda wa
kuongea, au kwa wenye uwezo kuhisi kuwa mgeni kaja kuomba, tunajikosesha
baraka.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment