Bro, unajua mimi
nilipoteza fahamu siku tatu,...nikiwa kama mfu, maana nilikuwa sijijui,kabisa
..’akaanza kusema Profesa.
‘Siku tatu,
unasema ulikuwa kama mfu,..halafu ukafufukaje..!?’ akauliza kaka mtu
Kisa kinaendelea...
*********
‘Ni siku ile
alipokuja wakili nikiwa nimelazwa hospitali, akiwa na wazo la kutaka mimi kurudishwa
huku kwetu...alipoondoka kumuita dakitari , mimi huku nyuma, hali ilizidi kuwa
mbaya, nikapoteza fahamu....’akasema
‘Ndio ulisema
hivyo,....sasa ikawaje..?’ akauliza kaka mtu
‘Unajua pale
mwanzoni alipokuwa akinielezea makusudio yake alidhania kuwa huenda nimedhira
kuongea naye, kwani alishaambiwa na docta kuhusu hali yangu...kiukweli kutokana
na hasira, masononeko, shinikizo la damu lilikuwa limepanda juu,nikawa nakufa
kisabuni, maana ndani kwa ndani hali yangu ilikuwa mbaya,...’akasema
‘Mhh....’akaguna
kaka mtu
‘Na ndipo alipoondoka
tu, nikapoteza fahamu, na nilipozindukana na kuweza kutoa kauli kwa mara ya
kwanza tangu hali hiyo itokee ni siku nimeshafika hapa nyumbani, ...’akasema
‘Sasa aah.....
siku ile, kama hali ilikuwa mbaya kiasi
hicho kwanini,hukumwambia yule wakili maana alikuwa ni wakili wako au sio?’
akaulizwa
‘Ni wakili
wangu ndio, na ndiye aliyetakiwa kunisaidia, lakini kwa jinsi nilivyokuwa
nimekasirika,...siku ile sikutaka kuongea naye kabisa, niliona wananipotezea
muda wangu tu huku mimi naumia,...bro, niliteseka sana jela, hakuna maelezo
nitakayokuambia yaweze kuelezea hiyo hali,.. hata hivyo japo nilidhamiria
hivyo, lakini ilipofikia nahisi kufa kufa, nilitaka nimuelezea kuwa hali
imekuwa mbaya, hapo nilishindwa kabisa, sikuweza kuongea tena kiukweli....’akasema
‘Sasa
ikawaje...?’ akaulizwa
‘Kwa vile lengo
lao lilikuwa mimi niondolewe hapo nchini haraka iwezekanavyo,walitafuta kila
hila...ningelikufa ingelikuwa ni aheri kwao wangelitimiza dhamira yao,lakini wakakuta
sifi, maana hali kama hiyo ilishatokea mara nyingi, ...’akasema
‘Hali gani..?’
akauliza kaka mtu
‘Hali hiyo ya
kupoteza fahamu, nakuwa kama mtu anataka kukata roho,....lakini baadaye wanakuta
mimi bado nipo hai, kwahiyo walishachoka, ...na wasingeliweza kuniua...’akasema
‘Kwanini
sasa..., unasema walishindwa kukuua?’ akauliza kaka mtu
‘We acha tu,
...bro, binadamu ni mtu wa ajabu sana, akiwa na malengo yake, atatafuta kila
mbinu, bila kujali kuwa na yeye ni binadamu tu...hayo anayoyataka kuyapata kwa
njia ya dhuluma, ni masilahi ya muda tu, ipo siku na yeye yatamkuta, atayaacha
tu....hapo kulikuwa na ajenda ya siri, na walishajua kuwa mimi nikipata mwanya
tu, nitawaumbua....lakini mungu anajua,...mimi nilikuwa mnyonge, sina wa
kunisaidia, ningelifanya nini...’akasema kwa sauti ya unyonge.
‘Mhh, sasa
ilikuwaje...?’ akauliza kaka mtu
‘Nikasafirishwa
kiaina, kurudishwa huku kwetu....’akasema
‘Mhh, sasa
aaah, mimi hapo sielewi, ulisafirishwaje ukiwa huna fahamu,.?’ akaulizwa
‘Bro, wajanja
hawashindwi kitu, walifanya walichofanya nikajikuta nipo bongo ...’akasema
‘Walifanyaje
sasa..??, walikubeba kwenye jeneza...’akasema
‘Walinifanya
kama msukule....’akasema mdogo mtu huku akicheka kama mdhaha
‘Hahaha,...sasa
wewe unachelewesha tu, hebu elezea kitu kinacheleweka, ina maana hata wazungu nao ni wachawi.....?’
akauliza kaka mtu.
‘Walipojua
kuwa mimi nipo hai, ni nguvu tu sinam walinidunga sindano ya kuongeza nguvu, hali
ile ya kupoteza fahamu, kuzindukana ilikuwa inakuja mara kwa mara...wakaona
isiwe taabu,...wakanipiga hiyo sindano...’akasema
‘Mhh, ipoje
hiyo...?’ akauliza
‘Ni ya
kuongeza nguvu, kwa muda....’akasema
‘Ina maana
hata wenzetu wanaweza kuwa na roho mbaya kihivyo...?’ akauliza kaka mtu
‘Nimekuambia watu
wakitaka jambo lao liwe, wanajisahau kuwa na wao ni binadamu tu,,...kuna mambo
walitaka kuyafukia, na mimi ningekufa ingesaidia, ....lakini ikwa mimi sifi, na
wakaona isiwe taabu, kufa nitakufa tu, lakini lini, na je kama nikiweza
kuongea, watu wa habari, au..’akasema na kukatisha akikohoa.
‘Njia gani
hiyo, kwani wangetaka si wangekuua tu, una nini wewe , wewe ni nani mpaka
wasumbuke hivyo...?’ akaulizwa kaka mtu sasa akimtizama mdogo wake kama yupo
salama kwani alikohoa mfulululizo.
‘Bro, sheria
ipo, na sheria inaogopewa, sema watu ni kutikisa kibiriti tu, hata uwe nani,
ukijua kuna sheria inakubana, hata ukifanya makosa bado moyo utakusuta, utakuwa
na mashaka...kuna watu wanafuatilia sana mambo hayo,...usione hivyo, hata kama
mimi sio kitu, lakini watu wanatafuta visababu vidogo tu, kuangushana hasa kisiasa.....’akasema
‘Sasa
ilikuwaje...na je inaruhusiwa?’ akauliza kaka mtu
‘Kuruhusiwa
kwa vipi?’ akauliza Profesa
‘Yaani
mgonjwa kuchukuliwa katika hiyo hali uliyokuwa nayo?’ akaulizwa
‘Hilo mimi
sijui, ..ninachojua na ndivyo ninavyohisi walifanya hivyo, wakitaka mambo yao yawaendee
vizuri,...’akasema profesa
‘Akina nani,
maana hapo nahisi walichoogopa labda ni gharama za kukusafirisha ukiwa maiti...au,
hebu elezea ilivyokuwa...’.akasema kaka mtu.
‘Hivyo ndivyo
ilitakiwa ionekane hivyo, lakini kiundani kulikuwa na ajenda ya
siri,...ukiangalia mlolongo mnzima wa hiyo kesi, hadi kushikwa mimi, ....kuna
mambo mengi yemejificha hapo, kwani mpaka naondoka bado muuaji halisi alikuwa
hajapatikana....’akasema
‘Si ulisema
alishapatikana, ...au alikuwa sio yeye?’ akauliza kaka mtu
‘Alikuwa ndio
yeye kwa kushukiwa tu, .. lakini ilikuwa haijathibitishwa mbele ya mahakama
kuwa muuaji ni nani, jinsi walivyoshukuwa hao watu wawili ni kama
nilivyoshukiwa mimi tu,...lakini je walikuwa ndio wauwaji, kweli, na huyo mtu
wa pili alikuwa ni nani...’akasema profesa
‘Sasa muuaji
alikuwa nani....?’ akauliza kaka mtu.
‘Mimi
nilishaondoka huko,..wao walitaka mimi niondoke huko mapema maana kukaa kwangu
huko kungelifichua mambo mengi...hasa kama hao watu wanaoitwa wa haki za
binadamu wangeliingilia kati, najua wangelidadisi kutaka kujua zaidi, na hapo
bomu lingewalipukia...’akasema
‘Haya
tuyaache hayo, hebu niambie wewe ilikuwaje hadi ukafika huku kwenu..?’ akauliza
kaka mtu.
‘Ili uelewe
vyema turudi siku ile pale alipoondoka wakili kumuita dakitari , alipoondoka mimi
huku nyuma nikapoteza fahamu kabisa,nilishakuambia hilo ...., kwahiyo dakitari
alipokuja, sikumuona, na sikuwa na ufahamu ni nini walikifanya kujaribu
kunizindua,....najua watakuwa walifanya hivyo, lakini ilishindikana, wakajua labda ndio
kwaheri, muda wakakuta nacjezesha mkono...’akasema
‘Hayo
uliyajuaje, ni nani alikuja kukusimulia hayo ya huko, wakati ulishaondoka, na
unasema ulikuwa hauna fahamu...?’ akauliza kaka mtu
‘Haya nilikuja
kuambiwa ni hao watu walionisindikiza kunileta huku..’akasema
‘Ina maana
ilibidi usindikizwe na watu wao, au ni akina nani hao walikusindikiza, na
ulipata wapi mwanya wa kuwauliza,?’ akauliza
‘Ni watu wao
wa usalama,...kama nilivyosema ilibidi kuwe na watu wawili ambao walikuwa
kiegemeo wakati naletwam wanakuwa pande zangu mbili, ili nisije kudondoka...na
watu hao walipewa kazi ya kuhakikisha nimefikishwa nchini kwangu na kuandikisha
maelezo yangu....’akasema
‘Maelezo gani
sasa...?’ akauliza kaka mtu
‘Maelezo..!
ni lazima kuwe na melezo ya kuejeshwa kwagu huku nyumbani nikiwa
mgonjwa,...’akasema
‘Sasa
waliandikaje...?’ akauliza
‘Waliandika
kuwa mimi ni mhalifu wa biashara za mlungula, na pia nilikuwa kule kinyume na
sheria, na nikawa najishughulisha na matendo kinyume na sheria za nchi
hiyo,...nilihukumiwa kufungwa, lakini kutokana na hali ya kiafya kama
ilivyoonyeshwa na dakitari wameona waniwahishe huku.....blablabla...’akasema
‘Najiuliza
sheria inasemaje kuhusu hilo....inakubalika kweli, watu wa huku kwetu
hawakulihoji hilo...?’ akauliza kaka mtu
‘Walihoji
hilo, wawahoji wazungu,...lakini ndio hivyo, mimi sijui....ninachofurahi ni
kuwa nimerudi nyumbani na najua dawa zangu za kienyeji zitaniponyesha tu, si
unaona sasa hivi nimeshaanza kuonekana binadamu...japokuwa bado natisha....’akasema
akiendelea kujiangalia.
‘Sasa hao
watu waliokusindikiza walikusimuliaje, na wewe ulisema ulikuwa unasikia tu,
...?’ akauliza
‘Ndio,...wakati
napelekwa hospitali ya hapa.nilipata nafuu nikaweza kuongea kidogo, nikamuuliza
huyo jamaa mmoja ilikuwaje, ndio
akanielezea kwa haraka,...namfahamu sana huyo jamaa....’akasema
‘Alikusindikiza
hadi hospitalini, au alikusimulia wapi?’ akauliza
‘Walifanya
hivyo ndio, walinisindikiza hadi pale nilipofikishwa hospitali, kuhakikisha
wanaondoka kila kitu kikiwa kama walivyotaka wao, wasije kuonekana walipanga
kwa nia mbaya....’akasema
‘Mhh,
....alikuambiaje...?’ akauliza
************
'Turejee siku
ile nilipopoteza fahamu, pale hospitalini.....'
'Wakati wakiwa wanaulizana wafenye nini, hapo fahamu
ikanirejea, lakini mwili haukuwa na nguvu kabisa....hapo tupo sawa..?.’akaanza
kuelezea mdogo mtu sasa akielezea mkasa mzima.
‘Fahamu zilinirejea
kwa namna ambayo siwezi kujiinua, naona, nasikia lakini siwezi kujibu kitu,
mwili ulikuwa kama sio wangu, akili tu ndio inafanyakazi....
‘Huyu mtu
kapooza mwili mzima, hapa alipo ni kama mzigo tu....’akasema dakitari, nilimsikia
na kiukweli sikuipenda hiyo kauli yake lakini sikuweza kumjibu.
‘Kwa hali
kama hiyo tunaweza kumsafirisha kumrejesha huko kwao....?’ akauliza mtu
mwingine sikuweza kumfahamu maana alikuwa kwa pembeni.
‘Inawezekana
lakini mhh ...au mnatakaje...’akasema dakitari
wakawa wanaongea kwa sauti nisiyoisikia, na baadaye dakitari akatikisa
kichwa kama kukubali.
‘Kwahiyo
inawezekana,mkitaka iwe hivyo, lakini, sijui maana si mumesema huyu mtu ana
kesi ya kujibu, hakimu kalirizia hilo ...?’ dakitari akauliza akionyesha
mashaka.
‘Hakimu
kaizinisha, huyu mtu arudishwe kwao,...ili kukwepa gharama hasa kutokana na hii
hali yake...’sauti ikasema
‘Unajua
docta, kama ulivyosema , kuendelea kumfunga huyu mtu hali yake itazidi kuwa
mbaya, basi maelezo hayo yalisaidia hakimu kukubali, maana kama unavyoona, ina
maana itabidi kila muda awe analetwa huku hospitalini au sio,...sasa tunachotaka
huyu mtu asifie huku kwetu...’sauti ikasema
‘Kwahiyo
mnatakaje....?’ akauliza na maneno waliyokuwa wakiongea sikuyasikia, ila docta
baadaye akasema
‘Kama mnataka
hivyo, Inawezekana tutaona jinsi gani ya kufanya...’sauti ikasema
*******
Profesa aliandaliwa na kweli ikaja nguvu ya
aina yake, akaweza hata kukaa, lakini cha ajabu, pamja na nguvu hiyo kurejea,
lakini profesa hakuweza kuongea, aliweza kuona kinachoendelea, na kusikia tu, na
kwa msaada wa watu aliweza kusimama, akaweza kutembezwa akiwa kashikiliwa huku
na huku, na hata wakati anaingizwa kwenye gari, kupelekwa uwanja wa ndege
aliweza kufahamu hayo yote , lakini kila mara kulikuwa na watu wawili
wakumsaidia kushoto na kulia, ili asije kuanguka.
‘Nilikuwa
naona, nasikia, lakini siwezi kutamka kitu, nilikuwa kama bubu, mdomo
haufunguki,...mwili unaweza kutembea kwa msaada wa mtu huku na huku,
unafikishwa kwenye kiti unakaa kama kawaida, ila ni lazima kuwe na mtu wa
kukuzuia huku, na huku, ili kukitokea mtikisiko usiangukie upande mwingine....’akasema
profesa
‘Nilifikishwa
kwenye ndege nikitembea, kwa msaada wa watu huku na huku walihakikisha
sianguki, ila ionekane nipo hai, nipo mnzima, ni kuchoka tu ...na hao watu wawili
ndio nilikuja nao hadi huku nyumbani...’akasema profesa
Ndani ya
ndege nilipigwa sindano nyingine nahisi ni ya kuniongeza nguvu, na hadi tunafika
hapa nchini, bado nilikuwa na zile nguvu za kuongezewa, na nikakabidhiwa kwa
watu wa usalama wa huku, na ikatakiwa kuwahishwa hospitalini haraka,...’akasema
‘Huyu mtu ni
mgonjwa, ni muhimu afikishwe hospitalini....’wakasema, waliongea walichoongea,
na kweli nikachukuliwa na gari la wagonjwa, kuelekea hospitalini na tukiwa
njiani ndio nikaweza kuongea, na kumuuliza mtu aliyenisindikiza, kwanza
hakuamini, halafu alipoona kweli nimezindukana vyema, akanisimulia ilivyokuwa
‘Alinisimulia
kwa haraka, ....nikawa nasikia tu...aliniambia kuwa yeye alitakiwa aondoke
kesho kurudi kwao lakini kwanza alitakiwa kuhakikisha kuwa nimefikishwa
hospitalini,...ili kutoa maagizo kwa dakitari atakeyanipokea’
‘Maagizo,..maagizo
gani hayo.....’akazidi kusema
Profesa alifikishwa
hospitalini na kukabidhiwa kwa dakitari, haikuchukua muda profesa akapoteza
fahamu...
Profesa
alilazwa hapo hospitalini wiki nzima, kabla hajaweza kujitambua vyema na
alipojitambua ndio akawaomba madocta wajaribu kuulizia kuhusu ndugu zake, ndio ukafanywa utaratibu hadi kaka yake
akapatikana, ....
‘Bro ndio
ilivyokuwa hivyo...’akasema akimuangalia kaka yake.
‘Sasa vipi
kuhusu huyo kijana wetu...?’ akauliza kaka mtu.
***********
‘Bro mimi
hata sitakia kusikia, kuhusu huyo mtoto wako, na kwa angalizo bro...nakuonya uachane kabisa
na huyo mtoto...’akasema
‘Kwanini
unasema hivyo...?’ akauliza kaka mtu
‘Kutokana na
msimamo wake, nina uhakika kama atarudi hapa mkaonana naye, atakutia hasira na
itakuwa ndio mwanzo wa kuchukiana kabisa na yeye...’akaambiwa
‘Mimi sina
haja naye, ...kama amekwisha kusema hana baba, baba yake alikufa, basi...ila
kinachoniuma ni huyo mama yake maana kila mara nikikutana na ndugu za huyo mama
ninachoulizwa ni hicho,wanasema huyo mama sasa hivi kawa kama kachanganyikiwa
kisa ni huyo mtoto, sijui kwanini hamsahau, yeye anadai mtoto wake yupo hai,
lakini mbinu zimefanywa ili asimuone....’akasema na Profesa akatikisa kichwa
kwa kusikitika, halafu akasema;
‘Inaniuma
sana, najuta kwanini nilifanya hivyo, wakati nayafanya hayoo nilijua natenda
jambo jema, kuwa nitamsaidia huyo mtoto, apate elimu, na mimi hapo hapo ndio
nikapata mwanya wa kutokea, ...nisaidie na mimi nifaidikie sikujua haya yote yanaweza
kutokea....’akasema
‘Ndio hivyo
umeniharibia mwanangu kwa tamaa zako, na hivi sasa utafanyaje, maana..majuto ni
mjukuu....hebu fikiria kama ni mtoto wake angefanyiwa hivyo ungelifanyaje...’akasema
kaka mtu.
‘Lakini hata
mimi ni damu yangu, ...nilifanya kile nilichoona ni sahihi kwa wakati
huo,...mfano kama mambo yangekuwa mazuri, akawatambua nyie, ...faida ingelikuwa
kwa nani, tatizo ni kuwa amekataa kuwatambua au sio...’akasema
‘Nikutokana
na malezi uliyomlelea, wewe umeishi maisha hayo ya utapeli, mali na pesa ipo
mbele zaidi ya utu,...hiyo ni tabia mbaya sana, ...nakufahamu sana bwana mdogo,
tokea ukiwa mtoto, ...lakini tuyaache hayo, wewe jitahidi ufuate masharti usije
kujiona umepona...’akaambiwa na kaka mtu.
‘Nitajitahidi
sana, na nataka nianze ile biashara yangu ya madawa, nikipata nafuu nitakwenda
mjini, kuangalia soko langu...’akasema
‘Huko
pasahau,..maana ukienda huko utataka kuiona nyumba, na itakutia hasira...mimi
ningekushauri uweke akili yako kwenye kutunza afya yako....’akaambiwa
‘Ni lazima
nikaione hiyo nyumba, na ...sijui. bro.....labda mungu asinipe uzima,..mhh,
sijui....’akasema
‘Utafanya
nini wewe, nyumba utakufa nayo, unanishangaza kweli...?’ akaulizwa kaka mtu akimuangalia ndugu yake kwa jicho la dharau,
akitabasamu.
‘Ile ni haki
yangu bro, wematumia mbinu kuniibia...lakini ngoja nipone,...na ole wao,,nipate
afya njema, nipate nguvu, bro, usinione nipo hivi, ,...'akasema
'Utafanya nini na hiyo hali, hivi hujioni eeh...?' akauliza kaka mtu
'Mhh, nitafanya nini,...wao waombee tu
nife,...lakini kama mungu atanipa afya angalau kidogo..., nikarudi kwenye hali nzuri, bro, utayasikia
mambo yangu, ile nyumba itarudi.....mimi sio profesa wa bure bro, nafahamu mambo ambayo wewe huyajui..'akasema
'Ya uchawi...?' akauliza kwa dharau
'Kinachoniuma ni kuwa ile nyumba
nilijenga kwa jasho langu, halafu watu waje waichukue kilaini tu, hivi hivi, hata sikubali...nitaizungukia kwa udi na uvumba....’akasema
akijiinua pale alipokuwa amekaa, akasimama, kaka mtu akamuangalia akitabasamu
‘Haya bwana,
....nakujua ulivyo, unapenda sana ligi, mwili wenyewe upo wapi, ni maneno tu.
Yamebakia sahau, wajanja wameshakuzidi...utarudi ukapambane na mama mtemi,
au....wewe, kubali tu yaishe..’akasema kaka mtu
Na mara
mlango ukagongwa, akaja mgeni, wakasalamiana, na huyo mgenii akasema katokea
mjini
‘Umetokea
mjini....?’ akasema kaka mtu akisalimiana na huyo mgeni
‘Ndio
nilikwenda kuchukua mzigo...’akasema
‘Kuna nini
huko mjini...cha zaidi?’ akaulizwa
‘Hakuna cha zaidi...mambo
ni ya yale yale, kampeni za kisiasa...si unajua tena, vipi mgonjwa wetu
anaendeleaje, maana naona uzima unaanza kurejea, kweli binadamu wa ajabu, mimi
nilijua ni maandalizi tu ya kuzika,..’akasema akigeuka kumuangalia mgonjwa, na
Profesa akacheka
‘Sifi bwana,
mtakufa nyie kwanza....’akasema kiutani
‘Kweli wewe
una roho ya paka...’akasema mgeni
‘We acha tu
cha moto nimekiona...hata mimi hapa nilipo siamini kuwa bado nipo
hai....’akasema na huyo mgeni akawa kama
anakumbuka kitu akasema
‘Hivi ile
nyumba yako,mjini uliiuza...au?’
akauliza huyo mgeni na ndugu hawa wawili wakaangaliana, na baadaye kumuangalia
huyo mgeni kwa macho ya udadidi na Profesa akawa wa kwanza kutamka neno
‘Kwanini
unasema hivyo...?’ akauliza profesa
‘Mhh,...nimepita
pale sikuweza kuitambua tena,imezungushiwa mabati, nahisi...kuna matengenezo
yanaendelea humo ndani, ...’akasema
‘Oh, hata
sijui....’akasema kaka mtu akitikisa kichwa na huyo mgeni akageuka kuondoka
akasema
‘Jamani mimi
sikai nilikuja kumuona mgonjwa mara moja mimi naondoka...’akasema na kuondoka
zake.
‘Ngoja
nipone...ngoja nipone...tutaona.’akasema Profesa akitikisa kichwa
Kaka mtu
akamtizama mdogo mtu kama kutaka kuuliza
kitu, lakini akamuona mdogo wake kainama , akajua mdogo wake huyo sasa roho
inaanza kumuuma, na akajua sasa kuna vita nyingine inakuja huko mbele...
NB: Profesa
karudi nyumbani, ni nini kitaendelea huku, na huko je ilikuwaje...na ni vipi
hiyo radhi ya wazazi ikaja kutokea...tuzidi kuwepo kwenye hitimisho la kisa
hiki.....
WAZO LA LEO: Roho inauma pale unapokikosa kitu,
hasa kama kilikuwa chako na sasa kimechukuliwa na mtu mwingine kwasababu mbali
mbali..... , kama ilivyo kukosana kwenye ndoa, ukaacha mke, na mke akaja kuolewa
na mtu mwingine na ukaja kukutana naye na kumuona kawa mnzuri zaidi...moyoni
utaumiaje...thamani ya kitu inaonekana pale unapokikosa.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment