‘Hamna cha
wakili mnzuri hapo ushahidi upo wazi, yeye ndiye kaua, kutokana na vielelezo
tulivyo navyo, ....’akasema muendesha
mashitaka
‘Ukiangalia video
inaonyesha wazi, anaonekana mshitakiwa akiwa anakimbia akiwa na silaha,kwanini
akimbie, ndilo swali la kujiuliza hapa, na anakimbia akiwa kashikilia hiyo
silaha...hapo hana sehemu ya kuokokea, hata akiwa na wakili mnzuri,...
‘Na mara nyingi
kama silaha ina alama za vidole za mtuhumiwa, ni ushahidi wa kutosha wa kumtia
mtu hatiani, labda ithibitike kuwa alishikishwa, kwahiyo huo kwetu ni ushaidi
muhimu unathibitisha na kuhalalisha kuwa huyo mshitakiwa ndiye muuaji, sasa
mnataka ninii zaidi....’akasema. muendesha mashitaka wakiwa wanajadiliana na
wenzake
‘Lakini hakuna
ushahidi wa moja kwa moja kuwa ndiye aliyefyatua risasi, yeye mshitakiwa anadai
alipigwa na kitu kichwani akapoteza fahamu na kweli jereha linaonekana kichwani,..hatuwezi
kusema kajipiga mwenyewe ili kuharibu ushahidi,...sehemu kama ile mtu huwezi
kujipiga mwenyewe,....’akasema mpelelezi.
‘Yah....’akasema
muendesha mashitaka
‘Na pia
anasema alipozindukana alikuwa kachanganyikiwa, ...., akaiona hiyo silaha
karibu yake, kwa kutaharuki akaichukua na kukimbia nayo....’akasema mkuu
kuongezea
‘Hapo unaweza
kusema anajitetea tu, na hoja kama hiyo ni ya kufundishwa na huyo wakili
wake,...japokuwa kweli ana jeraha kichwani,..labda alipigwa na marehemu wakati
wanapambana, labda alipigwa na mtu mwingine baada ya kutoka hapo....’akasema
mpelelezi.
‘Na labda
tungesema huenda alipigwa na marehemu wakipambana, lakini kwenye eneo la tukio hakukuwa na dalili za watu kupambana,
tumechunguza hilo...inaonyesha muuaji, alifika na kumpiga marehemu risasi, bila
hata maehemu kujitetea, ni mauaji ya dhahiri ....’akasema mpelelezi
‘Ana jeraha
kichwani, lakini hakuna dalili ya kuwa walipigana na marehemu,....hapa
inamaanisha nini.....’akasema mkuu aliyekuwa akiwasikiliza.
‘Hapa ina
maana kulikuwa na mtu wa tatu, na huyo mtu wa tatu anaweza kuwa ndiye
muuaji,...sasa huyu mtu wa tatu ni nani.....’akasema mpelelezi.
‘Kwahiyo
kazi yote uliyofanya ni bure, inabidi kumtafuta muuaji, au...?’ akauliza mkuu
‘Sio bure,
hapa tukithibitisha kuwa yeye sio muuaji, yaani mshitakiwa, tunaangalia njia
nyingine ya kumpata muuaji, na atapatikana tu, kama sio huyu mshitakiwa ,
akiatikana ni kiasi cha kuunganisha ushahidi na huyo muuaji mpya, matendo na
sababu ni zile zile...’akasema mpelelezi
‘Yaweza kuwa
tofauti, kutegemeana na mtu mwenyewe, huenda katumwa tu kuua,...muuaji wa
kukodiwa,.....na hapa tunacheza na muda...’akasema muendesha mashitaka
‘Ok,...tusipoteze
muda, mimi naona tuanzie kwenye orodha ya majina ya watu walioingia pale kwenye
jengo siku ile..., maana hapa ndipo wakili wao, alipoweza kukushika shati
wakili,.....ilikuwaje kwenye saa zisiendane, na kuonekana kama zimebadilishwa,
maana hapa yaonyesha kabisa kuna jamboo limefanyika,.....’akauliza mkuu.
‘Tulipowauliza
wahudumu waliokuwepo, walisema mara nyingi, yule mtu anayeingia ndiye anayeandika
saa , na wao huwa makini kuthibitisha hilo kuangalia kama kweli aliyeandika
kaandika muda sahihi, lakini wakati mwingine kuna kupitiwa...’akasema
mpelelezi.
‘Kwahiyo
kweli, hakuna aliyejaribu kubadili mtiririko wa saa kwa makusudi..?’ akauliza
muendesha mashitaka
‘Hakuna,....saa
hizo waliandika wenyewe watu walioingia, na hata tulipowaonyesha wale walinzi
waliokuwepo hao mapokezi wakisimamia hilo, walishangaa, hawakuwa wameligundua
hilo kabla....’akasema
‘Yawezekana
hili limefanywa kwa makusudi, au huyu wakili mtetezi, asije akawa kafanya ....’akasema
mkuu na kukatiza
‘Hapana ,
wakili huyo hajafanya kitu, maana kama ingekuwa kumebadilishwa ungeooana,
hakuna dalili kama hizo...’akasema mpelelezi.
‘Sasa ni nani
kafanya hivyo...maana mshitakiwa hawezi kufanya hivyo, ukiangalia yeye kaandika
sawa tu, tofauti kidogo na mtu wa juu yake,...angekuwa kaweka saa tofauti na
mtu wa juu yake, kama walivyofanya hao waliopotosha saa tungesema ni yeye....’akatulia
mpelelezi kama kagundua kitu
‘Hapa
tuwaangalia hawa watu wa juu, hawa watu watano, walioleta tofauti ya saa, ni
akina nani....hawa wanaweza kuwa na sababu...ni nani hawa watu....?’ akauliza
‘Mmoja ni
kijana wetu, na yupo kijana mwingine walikuwa naye....’akasema
‘Kijana wenu!
Ni nani huyo...?’ Na, ina maana mlikuwa na mtu humo, wakufuatilia au ilikuwaje
mbona hujaniambia hilo....?’ akauliza muendesha mashitaka na mkuu naye akawa
kama ndio kwanza anasikia hiyo taarifa
‘Siku ya
kuchukua huo mzigo ambao ni pesa, hatukuwa na uhakika ni saa ngapi,au ni wapi....na
hatukuwa na uhakika kuwa watatumia jengo hilo, mwanzoni walipanga kuwa huyo
mpelekaji atapeleka hizo pesa kwa huyu marehemu, na kuna mtu atakuja
kuzichukua....’akasema mpelelezi
‘Lakini
wakaja kubadili, kuwa marehemu azipeleke kwenye hilo jengo, tatizo walipobadili
hivyo, marehemu hakutupa taarifa kuwa kaambiwa apelike hizo pesa maeneo
hayo....’akasema
‘Unahisi ni
kwanini alifanya hivyo?’ akaulizwa
‘Hapo
hatujui ni kwanini, maana alikubali kushirikiana nasi...’akasema mpelelezi
‘Yawezekana
marehemu alishakuwa na mpango wake,..unajua alishafahamu kuwa huo mzigo una
pesa,...kwahiyo huenda, alitaka kufanya awezevyo nay eye aambulie
kitu....’akasema mkuu.
‘Hiyo
yawezekana...maana wakati anaondoka hapo alimuaga mwenzake kuwa anakwenda kufanya
dili.....’akasema
‘Dili, akiwa
na maana gani?’ akauliza mkuu
‘Dili ni
namna ya kuingiza pesa kwa mpango fulani, uwe wa kujadiliana au
kibiashara,....’akasema
‘Mwenzako
hakusema lolote, kama alifahamu ni dili gani na kama aliweza kuona ni kitu gani
mwenzake aliondoka nacho....?’ akaulizwa
‘Mwenzake
anasema kulikuwa na mzigo ,na mwenzake alipokea simu, ikimuelezea huo mzigo
aupeleke wapi, na .....kwa vile yeye hashughuliki sana na mizigo ya kutoka nje,
hakuwa makini ni kitu gani...’akasema
‘Huoni
kwamba mwenzake ana kitu anaficha, maana pale mambo mengi yapo kimaandishi au
sio....?’ akaulizwa
‘Ndio na
ndizo taratibu zilivyo, lakini cha ajabu huo mzigo, haukuwa na kumbukumbu
yoyote, kama ilivyo kawaida yao, mzigo unaandikishwa umetoka kwa nani,
unakwenda kwa nani,...lakini mzigo huo ulikuwa ni wa maneno tu, fanya hivi,
peleka hapa, na kwahiyo walikiuka taratibu, kisheria....’akasema mpelelezi.
‘Je marehemu
alipofika kwenye hilo jengo alipoambiwa apelike huo mzigo, aliandikisha jina
lake muda gani?’ akaulizwa
‘Cha ajabu
basi marehemu hakuandikisha jina lake halisi.....na tulipowauliza walinzi,
waliokuwepo, walisema kwa muda huo kulikuwa na watu wengi,...kulikuwa na hali
ya msongamano , kila mtu akitaka kuwahi, kwahiyo hawakuwa makini sana,....
‘Sasa
kilichotusaidia ni kamera, kamera ilionyesha marehemu akiandika jina lakini
tulipoangalia hakukuwa na jina lake, ina maana aliandika jina la uwongo....’akasema mpelelezi
‘Kwanini....?’
akauliza muendesha mashitaka
‘Angalia
mtiririko wote huo,huko kazini, hawakufuata taratibu za huo mzigo, ina maana alikuwa na ajenda fulani,
ama kwa masilahi yake au kutokana na hao walivyomuelekeza...na huenda ndicho
kilichosababisha kifo chake...’akasema mpelelezi
‘Ok, kwenye hiyo
kamera, hakuna namna ya kunasa muda,...ni kamera ya namna gani, kwani nyingi
unaweza ukafuatilia tukio, unapanga kwa masaa, kwa sehemu nk...hiyo kamera
ipoje,...ili tujue hasa huyo mshitakiwa alifika saa ngapi.....?’ akauliza
muendesha mashitaka.....
‘Kamera
waliyoweka sio za kisasa, huyu mtu aliweka kamera ili tu kuonyesha kaweka
kamera,...ni ya kizamani na kuukuu....tuliliangalia hilo tukio kwa utaalamu
wote, lakini, hatujaweza kufanikiwa...’akasema mpelelezi
‘Kamera yake
ni ile ya kuchukua tukio kama video tu, inaonyesha tuki kwa muendelezo, na
huwezi kulichambua hilo tukio kwa saa, kwa eneo nk...tulijaribu kuingia ndani
zaidi kuona kama tunaweza kupata ule mtiririko wa picha moja moja..lakini
hatukuweza, maana hata mashine yenyewe ni mbovu....’akasema mpelelezi
‘Ni mbovu,
lakini hilo jengo ni jipya, au sio, sasa Iliharibika kwa vipi,..iliharibika
muda gani, au iliharibiwa makusudi...?’ akauliza mkuu
‘Inavyoonyesha
ni kipindi marehemu akiandika,.... maana wakati anaandika utaona ile kamera
ikicheza cheza, halafu, ikazima,....halafu ikawaka, halafu ikazima,...kukawa
hakuonyeshi kitu, sasa toka hapo hadi watu kama ishirini hivi hakukuwa na picha
yoyote....’akasema
‘Mhh....kwanini
iharibike kipindi marehemu anaandikisha jina....hapa kuna sababu, ni nani
anayesimamia huo mtambo, hawakujisajili idara ya usalama....?’ akauliza mkuu.
‘Kwa muda
huo, mtambo huo ulikuwa unajiendesha wenyewe, ....huwa yule mtu wa kuhudumia
huo mtambo, akisha uweka sawa, anaondoka, na kama kuna tatizo ndio anaitwa,....’akasema
mpelelezi.
‘Lakini
mtambo wao haukusajiliwa kwenye watu wa usalama kama wengi wanavyofanya, maana
nijuavyo mitambo hii lazima iwe na uangalizi makaoni mwa ofisi za usalama kwao
kama wana kampuni ya ulinzi au kwa usalama wa kipolisi,...?’ akaulizwa
‘Niliwauliza
hilo swali, kwanini, wakasema ndio walikuwa mbioni kufanya hivyo, hata fomu
wanazo walizokuwa wamejaza kwa ajili ya kujiunganisha kwenye usalama wa
kipolisi...’ akasema mpelelezi
‘Kwahiyo
sasa walikuwa wanatumiaje hiyo kamera, ipoje...?’ akauliza mkuu
‘Wao kamera
yao ilikuwa humo kwa mumo,wana mtambo wao na unatumika humo humo ndani, na
walinzi waliopo ni wafanyakazi wao, waliowaajiri kwa kazi hiyo, kwahiyo
wanalipwa mshahara kama wafanyakazi wa kawaida...hawakukodi kamuni za usalama, ..ndio
tatizo hapo...’akasema mpelelezi
‘Sasa huyo
aliyekuwa akishughulika na hiyo mitambo, siku hiyo alikuwa wapi...?’ akauliza
‘Alitoka
kama kawaida yake, huwa anakuja muda kwa muda, akihitajika, hasa mtambo ukileta
matatizo,..na ilipotokea matatizo siku hiyo alipigiwa simu, lakini simu yake haikuwa
hewani, hakupatikana mara moja, na baadaye yeye mwenyewe akapiga simu kwa
kutumia namba tofauti akasema simu yake imeibiwa ....’akasema
‘Je ni kweli
hayo anayoyasema, kuwa aliibiwa simu, maana mimi nimeshaanza kumuhisi
vibaya...’akaulizwa
‘Ni kweli
simu yake ilibiwa,....kuna ushahidi,... alipoibiwa alitoa taarifa kwa mawakala
wa simu,...wakazuia takwimu zake,..na ni muda kabla ya muda wa haya matukio, na
kumbe wakati anahangaika huko kutoa taarifa, na kupata line nyingine huku wanamtafuta...’akasema mpelelezi.
‘Hapa kuna
jambo...huyu mtu tunahitajia kumweka chini ya ulinzi, nahisi anafahamu kitu,....nyie
mnaonaje,... inawezekana huyu mtu kapangwa...’akasema mkuu
‘Na pia
yawezekana kuwa huyo mtendaji, muuji, alijua kuwa huyu ndiye mtaalamu wa hapo,
akamwibia simu yake, akijua hakutakuwa na mawasiliano, akaingia kwenye hilo
jengo akaharibu mawasiliano ya kamera..lakini je yawezekana hilo, tukiangalia
muda wa kufanya hayo yote....’akauliza muendesha mashitaka
‘Aliibiwa
mitaa ya .....mmh, kweli hapo ni lazima kuwe na ushirikiano zaidi ya watu
wawili, kwa minajili hiyo basi kulikuwa na mtu mwingine wa kufanya hayo, akiwa
kwenye jengo, wakati huyo mwingine akiiba simu nk, ...’akasema mpelelezi
‘Mshitakiwa
hawezi kuwa mshirika....?’ akauliza mkuu
‘Mshitakiwa?...
Mimi naona kama hivyo,...niliona hivyo, lakini nitalipompekenyua
zaidi,nikagundua kuwa huyo hana utaalamu wa hiyo mitambo.....’akasema mpelelezi
‘Kwa
minajili hiyo, huyo mshirika awe na sifa ya utaalamu wa hiyo mitambo...ni nani
tunaweza kumshuku, aliyewahi kuingia hapo mwenye utaalamu huo, hebu tuangelia
katika walioingia kabla ya marehemu,
hata baada lakini wawe karibu na huo muda...’akasema mkuu
‘Tukiangalia
kwa mshitakiwa, yeye alifika baadaye, kuna watu walikuwa wakimfuatilia,
wanasema alifika hoteli ya karibu, akaingia na kutokea mlango wa nyuma,
hawakuligundua hilo hadi walipoona muda umekwisha, wakawa wamempoteza na
kumpata kwake ndio muda huo anakamatwa....’akasema mpelelezi.
‘Kwahiyo hao
hawakuweza kutusaidia, ....eeh, hebu turudi kwenye hili dafutari la
mapokezi..hawa watu watano,ni nani na nani....nahisi hapa tunaweza kupata kitu,
hisia zangu zinanituma hivyo’ akasema mkuu
‘Mmoja ni
kijana wetu, wengine hawa wawili ni wateja wa humo humo,na wengine wawili....mmoja tumempata, ni
mtu wa kuingia na kutoka, hana lolote,alifika kuuza bidhaa zake tu, na huyu
mwingine hatujampata , jina ni geni...yawezekana hakuandika jina
sahihi....’akasema mpelelezi
‘Na kamera
ndio hiyo ilikuwa haifanyi kazi...huyu huyu, ambaye yaonekana aliandika jina
bandia, ni nani...., walinzi wanasemaje kumuhusu yeye, hawana kumbukumbu yoyote
ya kutusaidia...?’ akauliza mkuu na muendesha mashitaka akaongeza kwa kusema
‘Na je kamera
za nje hazikuweza kunasa mtu wa kumshuku aliyeingia, tukiangalia kumbukumbu za
watu wakorofi...?’ akauliza muendesha mashitaka akijikuna kwa kutumia
kalama kichwani
‘Unajua
kamera hii nje imenasa hao watu
walioingia eneo hilo, lakini watu walioingia eneo hilo, kuelekea kwenye hilo
jengo ni wengi sana...labda tungekuwa tunamuhisi mtu fulani, tungeliweza
kumnasa kwa kumsearch--- kwa picha, hilo lingeliwezekana, lakini ukumbuke ni watu
zaidi ya mia waliingia eneo hilo, na katika kutafuta watu tunaoweza kuwashuku,
hakuna tuliyempata...’akasema mpelelezi.
‘Huyu ambaye
hakuandika jina halali ni nani, mpelelezi, fanya kazi hiyo tumpate, na nilikuwa
nauliza huyu kijana wako aliyekuwa kwenye hilo jengo ni nani, na alikwenda kwa
matilaba yenu, au alikuwa na mambo yake binafsi...?’ akauliza muendesha
mashitaka.
‘Huyu kijana
wetu, alikwenda kwa mambo yake na huko akamkuta huyo kijana mwingine, ....na
kijana wetu anasema huyo mwenzake aliondoka akamuacha yeye hapo, ....’akasema
‘Ok, tujue
kwanza kuhusu kijana wa mshitakiwa, ....’ akasema muendesha mashita na mkuu
akionekana kuwaza jambo.
‘Huyu kijana
wa mshitakiwa alipomuona mshitakiwa
anaingia akatoa taarifa kwetu, na huyu ndiye aliyesaidia, maana watu wetu
walishampoteza huyu mshitakiwa, kwahiyo sisi tukawasiliana na watu wetu kuwa mshitakiwa kaonekana akiingia
kwenye hiyo hoteli,na wao wakaelekea huko, lakini walikuwa
wamechelewa....’akasema mpelelezi
‘Ni nani
huyo kijana wenu, ni maofisa usalama, au ni hawa wa kupachika siku moja
moja....?’ akauliza muendesha mashitaka
‘Sio ofisa
usalama, unakumbuka nilikuambia kuwa kuna vijana tuliwashirikisha na wakawa
tayari kuisaidia polisi, huyu alikuwa mmojawapo, yeye anafanya kazi kwenye ile
ofisi ya yule mtaalamu,....’akasema
‘Mtaalamu
huyu mwenye kampuni ya mitandao ...?’ akauliza mkuu
‘Ndio
mkuu...’akasema mpelelezi
‘Ni nani
huyo?’ akauliza muendesha mashitaka akimuangalia mkuu,halafu mpelelezi
‘Ni kijana
wa huyo mshitakiwa...’akasema mpelelezi, na aliposema hivyo, mkuu akainua
kichwa kumuangalia mpelelezi, kama kuonyesha kushutika hivi, lakini hakuonyesha
dalili ya moja kwa moja, akamgeukia muendesha mashitaka kama kutaka kumuuliza
kitu, lakini akasita, akamgeukia mpelelezi na kumuuliza.
‘Mbona
hukuniambia hilo hata kwenye ripoti yako hukuyaandika hayo, sikuona hilo kabisa
au nimekosea,...?’ akauliza mkuu, na mpelelezi akawa kama anatafakari jambo, na
muendesha mashitaka akauliza
‘Huyu kijana
wa mshitakiwa anasemaje ulipomuuliza, alifika hapo kwasababu zake, au alifika kwa kazi maalumu,,...?’ akauliza
muendesha mashitaka.
‘Sisi
hatukumtuma, alitumwa na mtu mwingine,...’akasema
‘Alitumwa na
mtu mwingine !? ni nani huyo alimtuma...?’ akauliza mkuu
‘Alitumwa na
Mama mtemi!! ...’akasema mpelelezi
‘Alitumwa
nini,au kufanya nini....maana haya sasa nayaona megeni hukuyaandika,
hukuniambia...?’ akauliza mkuu
Wakati huo muendesha
mashitaka akawa anaandika kwenye kumbukumbu zake na mkuu akawa anaangalia jinsi
muendesha mashitaka anavyoandika, kwa kuonyesha wasiwasi, na mpelelezi hakujibu hilo swali kwanza japo
mkuu wake ndiye aliyemuuliza, akisubiria muendesha mashitaka amalize kuandika
anachoandika.
‘Mkuu, haya
sikuyaandika kwasababu.....’akatulia, akisita kuongea na muendesha mashitaka
akamkatiza kwa kumuuliza swali jingine.
‘Samahani
kwanza hapo,....umesema huyu kijana wa mshitakiwa alimkuta kijana mwingine ,
huyo kijana mwingine sio miongoni mwa vijana wenu...?’ akaulizwa
‘Hapana,
...yeye ni rafiki wa huyo kijana wa mshitakiwa,...’ akasema mpelelezi,
akimtumpia jicho mkuu wake, aliyekuwa akiangalia saa
‘Ni nani
huyo kijana mwingine rafiki yake kijana wa mshitakiwa, na mlimuuliza huyo
kijana mwingine alifika hapo kwa shughuli gani, haiingiliani na hili tatizo....au
walipanga kukutana na huyo kijana wa mshitakiwa au ilikuwaje...hebu weka sawa
hapo nikamilishe ninachoandika...samahani mkuu kwa kukukatiza?” akauliza
muendesha mashitaka.
Mkuu akatikisa
kichwa kukubali, huku naye akionyesha shauku kusikia jibu la mpelelezi, wote
wakawa wanamuangalia mpelelezi, wasubiria...mpelelezi akawa anafungua
makabrasha yake hakutaka kulijibu hilo kwa haraka,na hapo kumfanya mkuu wake
aonyeshe kama kukerwa, na kabla mkuu hajasema neno, kwani alitaka kusema neno,
mpelelezi akageuka kamuangalia muendesha mashitaka akasema, ....
‘Ni kijana
wa mkuu...’akasema mpelelezi na mkuu akashituka kiasi kwamba kule kushituka
kwake kulimfanya atake kama kusimama
‘Ni kijana
wangu! Kijana wangu mimi,.... haiwezekani, ...una uhakika na hilo,...ilikuwa
saa ngapi, nakumbuka alikuja kwangu, tukawa.... no no, ungeniambia mapema,
kwanini hukuniambia mapema, kabla huja.....siwezi kuamini, sio yeye....’mkuu akasema
sasa akishindwa kuficha hisia zake, akasimama huku akiangalia saa
‘Kwanza
nimechelewa kikao,...na mpelelezi,umenichanganya,..hukutenda majukumu yako
ipasavyo, itabidi tuliongee hilo, sipendi kazi ya namna hiyo, ya kunificha
ficha baadhi ya mambo.....sasa mimi naondoka, nina kikao na wakuu...’akasema
akipanga panga makabrasha na kuweka ndani ya mkoba wake.
‘Mkuu, ngoja
tumalize hili kabla hujaondoka...’akasema muendesha mashitaka alipomuona mkuu
huyo akijiandaa kuondoka, lakini mkuu hakumsikiliza akainua mkoba wake na
kuanza kundoka
Naye mpelelezi
akawa anafungua makabrasha yake kama vile anataka kuendelea kuonyesha ushahidi
zaidi...akasema
‘Mkuu nina sababu za kufanya hivyo....’akasema, na
mkuu alishaanza kuondoka akageuka kumuangalia mpelelezi akasema
‘ Sijarizika
na utendaji wako,...sina muda tena, wekeni mambo sawa tutakutana baadaye, na
mara simu ya mkuu ikalia, na mkuu kwa haraka akainua simu yake kuangalia
mpigaji, na kusema....
‘Ni mke
wangu! Oh, nilisahau kumpigia simu,...`sory mke wangu..nilikuwa kwenye
kikao....nani, kijana wetu,.... yupo hapo,mwambie asiondoke mpaka nije,nina
mazungumzo na yeye....’akawa anaongea huku anatembea kutoka nje...na wenzake
wakawa wanaangaliana, macho yakiongea
.....
WAZO LA LEO: Kuna wazazi huwa wepesi sana
kuwatetea watoto wao, hata kama wanajua kuwa watoto wao ni wakorofi, wakiambiwa
`mtoto wako ni mwizi, au mtoto wako ni muhuni au ni jambazi....’, yeye (mzazi)
huja juu na kumtetea mwanae....,badala ya kuungana na jamii kumsaidia huyoo
mtoto, yeye hukimbilia kujenga chuki na jamii,...tukumbuke kuwa kufuga mwizi,
kutetea maovu, hata kama yanafanywa na mtoto wako ni sawa na kufuga nyoka
mwenye sumu kali, ipo siku atakugeukia wewe mwenyewe...
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment