Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, September 2, 2015

RADHI YA WAZAZI-37



Baada ya shahidi mwingine kuitwa na kujieleza akiongozwa na muendesha mashitaka, ilikuja zamu ya wakili mtetezi, ...Wakili mtetezi alisimama, na kujinyosha kidogo, akamsogelea shahidi, akamuangalia, akageuka kuwaangalia watu waliokuwemo,akaonyesha ishara fulani kwa  watu wakacheka...

Wakili huyu alishajijengea jina kwa jinsi gani anavyoweza kujenga hoja zake za kutetea mtu, kwahiyo hapo kila mtu alikuwa askisubiria kwa hamu kusikia atasema nini kubaliana na ushahidi huo,....

Profesa moyoni alikuwa akimuomba mungu wake, ili amjalie wakili huyo aweze kutoa hoja zenye kumsaidia, kwani ushahidi uliotolewa ulikuwa ni mnzito,

‘Bro, hapo kwanza nilikuwa namuomba mungu na pili nillikuwa namshukuru sana huyo wakili kwa jinsi alivyokuwa akinitete....’akasema mdogo mtu akiendelea kumsimulia kaka yake...

‘Japokuwa baadaye nilimuona wakili huyo ni wale wale wanaotanguliza masilahi mbele....’akasema na kaka mtu akashangaa

‘Kwanini..?’ akauliza kaka mtu

‘Utakuja kuona huko mbele, ...ni mambo ya masilahi, hata kaam mtu anajua anachotetea ni haki, kumsaidia mtu, lakini kama hakuna kitu, huna kitu ,maana mkoo mtupu haulambwi, ...hakuna anayependa kufanya kazi bure, jao bure hiyo ina masilahi huko mbele ya mungu....’akasema

‘Ina maana hukuweza kumlipa huyu wakili....hata hivyo, yeye si kazi yake atakula wapi?  Halafu kwanza nikuulize,hivi.. ni nani aliyekuwa akimlipa huyo wakili na wewe ulisema huna pesa...ni mama mtemi au?’ akaulizwa

‘Mhh.....bro, we acha tu,...kiukweli sikuwa na pesa, si unajua pesa zangu ni za muda, upate dili ndio uingize pesa, na pesa ikipatikana haikai, maana haina baraka,....’akasema

‘Sasa ilikuwaje, .....maana hapo naona una wakili jembe....?’ akauliza kaka mtu

‘Wewe ngoja tuendelee na kisa chetu nitakuelezea huko mbele, usivuruge mpangilio...’akasema

Haya endelea...’akasema kaka mtu

‘Sasa nitakusimulia kuhusu  mashahidi wawili walioletwa mwishoni, ambao waliweza kubadili muelekeo wa kesi, ... ili tuje kuhitimisha kisa chetu.....’akasema mdogo mtu...

‘Tuhitimishe!...Mbona mambo mengi bado, nataka kujua jinsi kijana wetu alivyokuja kuoana na binti wa mama mtemi...walikubalianaje na je na huyo mama,...kuna yule binti mliyemtumia alikwenda wapi...na huyo kaka yake...

‘Au sema ilikuwaje, na je huyo kijana wetu watakuja huku kwetu au ndio keshakuwa mzungu....?’ akauliza,

‘Bro ngoja tuendelee...maana nikikuelezea juu juu hutanielewa, na kijana wako msahau, akija mtakosana kabisa ni bora akae huko huko.....’akasema mdogo mtu

‘Na akae,...mimi sina shida,mwenye shida ni mama yake maana nasikia hali ...keshakuwa mgonjwa akimtaka mwanae...’akasema kaka mtu.

‘Oh, masikini.....

Tuendelee na kisa chetu

********

‘Unasema mshitakiwa alionekana akitoka akiwa na bastola mkononi....?’ akaulizwa shahidi na kutikisa kichwa kukubali, huku akisema

‘Ndio muheshimiwa...’akasema shahidi

‘Na  ni ...kutokana na kamera,...au sio, kamera ambazo hata waigizaji wanaweza kuigiza tukio, au sio,...hizo  kamera au hiyo kamera iliwekwa wapi na nani, ...?.’ akaulizwa huyu shahidi na wakili mtetezi, na shahidi huyo akatabasamu na kusema.

‘Kamera hiyo ni hizi kamera za nje zilizowekwa kwa ajili ya kunasia matukio ya uhalifu, na wala sio kuwa ni kuigiza,....’akaambiwa

‘Kwahiyo kamera hiyo haikuonyesha mshitakiwa akifyatua risasi, ilichagua kipi cha kuonyesha au,  ....?’ akaulizwa

‘Haikuonyesha...’akajibiwa

‘Kwahiyo kuonekana kwake akitoka akiwa na bastola mkononi ndio ushahidi wenu kuwa yeye ndiye aliyefanya hayo mauaji....au?’akaulizwa.

‘Tumeonyesha ushahidi mbali mbali...kama nilivyoelezea awali,  hatua kwa hatua, sio lazima ionekane akifyatua risasi, vielelezo vya kiashiria vinathibitisha hilvyo, kuwa mshitakiwa ndiye aliyefanya hilo tendo, na hiyo video ni kama ushahidi mwingine tu wa kuthibitisha zaidi...’akasema

‘Nauliza hivyo kwa vile hapa mumetumia ushahidi wa video, na kinachonishangaza ni kwanini video hiyo isionyeshe tukio la ndani ,...inaonyesha tu mtu akikimbia na bastola, sio kwamba mliamua kulikata hilo tukio, ili muweze kutimiza dhamira yenu....?’akasema

‘Video hizi za matukio ya uhalifu, zimewekwa nje,...kwahiyo haziwezi kunasa matukio ya ndani ya majengo ya watu,...unafahamu sana....mara nyingi matukio ya ndani hutegemea na matakwa ya mumiliki wa hilo jengo, kama mumiliki ameweka video kama hizo, na tunazihitajia kisheria, tungeliweza kuzionyesha hapa, lakini hatukuweza kupata  ...’akasema shahidi huyo

‘Ina maana hilo jengo halina kamera za ndani za kunasia matukio...?’ akaulizwa

‘Zipo...’akasema

‘Kama zipo, hiyo video....ipo wapi?’ akaulizwa

‘Kwa tukio hilo, hatukuweza kupata hiyo video yake,....’akasema

‘Kwanini hamukuweza kupata hiyo video yake, wakati nyie ni watu wa usalama, mna mamlaka ya kuhakikisha inapatikana....au hamukuihitajia kwa vile haikidhi matakwa yenu..?’akasema wakili mtetezi

‘Tumejitahidi iwezekanavyo,...lakini kipindi chote cha tukio hilo,..kamera hizo zilikuwa hazifanyi kazi, ilikuwa ni bahati mbaya ilitokea hivyo....’akasema

‘Unaona...!’ akasema wakili huyo akiashiria kwa mkono

‘Kama ni hivyo, badoo hamjakamilisha kazi yenu, yaonekana kuna mtu, na huyo ndiye muuaji halali, hamkutaka kumtafuta, ....’akasema wakili mtetezi, na wakili muendesha mashitaka akasema hiyo sio kazi ya wakili mtetezi, kazi yake ni kumtetea mteja wake.

‘Kwahiyo wewe kama mpelelezi wa tukio hili hukuweza kupata ushahidi wa moja kwa moja kuwa mshitakiwa alionekana akifyatua risasi ....?’ akauliza wakili huyo

‘Upo ushahidi wa kinadharia, unao-onyesha kuwa bastola aliyokuwa nayo mshitakiwa ndiyo iliyotumika kumuua marehemu, tumeshaonyesha hilo....na mshitakiwa ndiye aliyepatikana na ushahidi huo, kuna alama za vidole, na zaidi kaonekana akikimbia akiwa na hiyo bastola, alikuwa ana kimbia nini... tumekwisha onyesha hayo yote kwenye ushahidi uliopita...’akasema huyo shahidi

‘Swali langu ni je kuna ushahidi gani unaonyesha kuwa mshitakiwa ndiye aliyefyatua hiyo risasi iliyomuua marehemu, maana kumeonekana ushahidi mshitakiwa anatoka akiwa na bastola mkononi je upo ushahidi unaonyesha mshitakiwa akifyatua risasi....jibu ndio au hapana’akauliza

Muendesha mashitaka akaingilia, na kusema maswali ya wakili mtetezi ni ya kupoteza muda, kwani alishaambiwa kuwa kamera iliyoonyesha hilo tukio ni ya nje na isingeliwezekana kupata tukio la ndani, kwasababu kamera ya ndani ilikuwa haifanyi kazi kwa muda huo...ila kuna ushahidi wa vielelezo unaonyesha kuwa mshitakiwa ndiye aliyefanya hilo tukio...

‘Kwa vielelezo gani vinavyoonyesha kuwa mshitakiwa ndiye aliyefyatua bastola,...ndio swali langu hapo, hakuna kielelezohata kimoja kilichoonyesha mshitakiwa ndiye aliyefyatua risasi au sio, maana mumeonyesha kuwa yeye alionekana akikimbia akiwa kashika hiyo bastola, sasa ushahidi upi wa kuonyesha kuwa ndiye yeye aliyefyatua risasi...’akasema wakili huyo

‘Ushahidi upo wa kinadharia kuwa ndiye aliyetenda hivyo,...’akasema huyo shahidi

‘Upi huo....huo ushahidi wa kinadharia mimi sijauona?’ akauliza wakili

‘Bastola ina alama za vidole vya mshitakiwa, mshitakiwa kaonekana wazi akiwa kaishikilia hiyo bastola kwenye hiyo video, akikimbia na hiyo bastola, mshitakiwa alionekana na mashaidi wengi kuwa aliingia, akielekea chumba alichokuwa marehemu...wakiwemo walinzi...hivyo vyote tumeonyesha wewe unataka nini tena...’akasema huyo shahidi

‘ Kama ni swala la kuingia hapo kwenye hilo jengo, mbona waliingia watu wengi tu, na kushikilia bastola sio tija, yoyote anaweza kushikilia, na asitende kosa, walinzi wa hapo wana silaha, mbona hamjawatuhumu wao? Akauliza

‘Unapoteza muda tu wakili mtetezi, tunzungumizia silaha iliyotenda hilo kosa, silaha hiyo haikuwa imeshikiliwa na walinzi,  ....’akaambiwa

‘Sawa...kwa hilo ngoja nikuelezee ilivyokuwa, huyu mshitakiwa aligongwa kichwani kwa makusudi, na huyo muuaji,...kwanini aligongwa kichwani, ni ili apoteze fahamu na muuaji akamshikisha mshitakiwa hiyo bastola mkononi,....hata hivyo, mshitakiwa ...’akasema wakili mtetezi na wakili muendesha mashitaka akamkatisha na kupinga maneno yake hayo kuwa hayo ni maelezo yake hayana msingi.

‘Ndugu muheshimiwa hakimu, ataka kuonyesha kuwa...hawa watu wanamuacha muaji halisi, wanaacha kumtafuta muuaji halisi, wanamg’ang’ania huyu mshitakiwa,najaribu kuwaonyesha hali halisi ilivyokuwa.....’akasema

‘Hiyo sio kazi yako.....’akasema wakili muendesha mashitaka

‘Haya, huyu mshitakiwa mnasema alionekana akikimbia na hiyo bastola, ni kutokana na kuchanganyikiwa,.... alipozindukana,baada ya kugongwa kichwani, akili haikuwa sawa,  aliiona hiyo bastola ikiwa karibu yake, akaichukua akitaka kujihami,...’akasema wakili

‘Hayo ni mawazo yako,utakuja kujengea hoja yako ukitoa ushahidi wako kama unao, sisi tumejenga ushahidi wetu hivyo maana tuna uhakika na hilo....’akasema wakili muendesha mashitaka

‘Kama mna uhakika na hilo,  tuonyesheni ushahidi unaoonyesha mshitakiwa akifyatua risasi...kama mumeweza kuonyesha mshitakiwa akikimbia na bastola,basi yawezekana kuwepo na ushahidi wa kuonyesha mshitakiwa akifyatua risasi, na jengo hilo lina kamera,..ni juu yenu kuitafuta, na kwanini muda huo hiyo kamera isifanye kazi....hamuoni hapo kuna walakini?’ akauliza wakili mtetezi.

‘Hiyo ni sehemu ndogo tu, ya ushahidi unaotaka wewe,....sehemu kubwa tumeonyesha kwa vielelezo, na vyote vinambana mshitakiwa....’akasema shahidi

‘Hiyo ni sehemu ndogo,...!? Hapana hiyo ni sehemu  muhimu sana, kama mnataka haki itendeke....na ni muhimu sana kwa mshitakiwa...’akasema wakili mtetezi,

‘Ndio maana tunasema muda wako wa kutoa ushahidi na vielelezo vyako ukifika fanya hivyo, vinginevyo unapoteza muda tu...’akasema wakili muendesha mashitaka

‘Kwahiyo kwa kifupi  hakuna ushahidi wa moja kwa moja kuwa mshitakiwa ndiye aliyefyatua risasi iliyomuua marehemu....?’akasema wakili

‘Sisi tumeshaonyesha vielelezo vyote vinavyoonyesha kuwa mshitakiwa ndiye aliyefanya hilo tendo, hayo unayoongea wewe au kutaka wewe iwe hivyo ni mawazo yako.....’akasema wakili muendesha mashitaka

‘Nimemalizana na huyu shahidi muheshimiwa hakimu....’, akasema wakili mtetezi,

*******

Baadaye aliitwa shahidi mwingine,...kiujumla bro, hawa watu  walikuwa wakikamilisha tu ushahidi wao,...pale walipoona kuna mapungufu, wanamuita shahidi wao tena...sasa akaitwa dakitari , dakitari aliyepima hilo tukio.

Shahidi huyo akatoa maelezo yake akisimamiwa na muendesha mashitaka na alipomaliza kutoa maelezo yake  ikawa ni zamu ya wakili mtetezi.

‘Katika maelezo yako, umetaja muda marehemu alipofariki,... na kwa maelezo ya muendesha mashitaka aliongezea kusema ni muda ambao mshitakiwa alipokuwepo humo, kwani muda huo unaendana sawa na muda mshitakiwa alipopigwa risasi na kufa, na unasema kifo cha marehemu hakikuchukua muda, mimi hapo inanipa mashaka kidogo....’akaanza wakili mtetezi.

‘Kwanini....?’ akauliza huyo shahidi

‘Jinsi ulivyotaja muda...kuna walakini hapo

‘Kwa vipi...kazi yangu ni kutaja muda wa tukio,...au?’akauliza shahidi

‘Huo muda una uhakika nao...?’ akauliza

‘Ndio... siku hizi utaalamu wa komputa unakuelezea kila kitu....’akasema

‘Umetaka muda sawa, na muendesha mashitaka anasema kuwa hakuna walakini kuwa mshitakiwa ndiye aliyesababisha hayo mauaji, kutokana na muda, kuwa mshitakiwa alikuwa kwenye eneo la tukio,... kwasababu kwa muda huo yeye ndiye aliyekuwa na marehemu, sawa si sawa?’ akaulizwa

‘Mimi nimetoa taarifa za muda, sasa kama mshitakiwa alikuwemo, hizo ni kazi zao,...na utaalamu wangu unaonyesha kuwa kifokilitokea saa ngapi, sasa mengine kama yanakutatizo labda upate maelezo kwa muendesha mashitaka....’akasema

‘Hebu tuangalia mpangilia wa saa...huyu mshitakiwa alisaini kwenye daftari la wageni saa ngapi.?’ Akauliza

‘Waulize wahusika, .....’akasema

‘Hapana nakuuliza wewe.....’akasema

‘Ilikuwa...saa nne na nusu...’akasema muendesha mashitaka

‘Aliposaini akatembea kutoka pale mapokezi hadi chumba hicho, akafika  kwenye chumba alipokuwepo marehemu saa nne na dakika 3I.na sekunde kadhaa,...kutoka pale  mapokezi hadi chumba hicho alitumia dakika moja na sekunde kadhaa...

‘Ndio....’akasema muendesha mashitaka kwa sautii ya kuonyesha anapotezewa muda

‘Huyu mtu alifika na kuanza kuongea na marehemu, wakaanza kubishana, na kwa mujibu wa taarifa za mpelelezi wako , na dakitari hapa anasema marehemu alipigwa risasi saa nne na dakika 32...hebu tuyaangalia haya maongezi yalichukua muda gani..

‘Yaangalia wewe,....’akasema muendesha mashitaka

‘Huyu shahidi anachochoangalia ni muda gani marehemu alipigwa risasi....’akasema

‘Ni muda gani...marehemu alipigwa risasi?’ akaulizwa dakitari

‘Ni muda wa saa nne dakika 32....’akasema

Wakali mtetezi, akatoa karatasi, na kusema, ...

‘Hii ni nakala niliotoa kwenye daftari la wageni....’akasema

‘Hebu tuangalia hizi kumbukumbu kutoka mapokezi,

Turudi nyuma kidogo kabla ya mshitakiwa hajaandikisha kuwa ameingia kwenye hilo jengo kumuona marehemu.

Turudi watu watano nyuma tukiangalia mpangilio, wa saa...angalia watu hawa wa tano nyuma saa zimefuatana kwa utaartibu mnzuri tu, ....haya ikafika kwa hawa watu wawili nyuma ya mshitakiwa alipoandika jina lake..

‘Hebu angalia mtu wa pili nyuma ya mshitakiwa alifika saa nne na dakika 31...sawa si sawa...?’ akauliza na huyo shahidi akamgeukia muendsha mashitaka.

‘Sawa...hebu hebu...kwanza,hii nakala umeipatia wapi...?.’akasema muenddaha mashitaka

‘Daftari ni lile lile, mimi nilichofanya ni kutoa nakala, kama unataka kuhakikisha unaweza kuagiza hilo daftari la wageni kwa walinzi....’akasema wakili mtetezi

‘Sawa...uliza swali lako...’akasema sasa akiwa bado anaikagua ile karatasi

‘Haya hebu angalia,..., walikuja watu wawili nyuma yake, yaani nyuma ya mshitakiwa ...kabla ya mshitakiwa, angalia saa walizoandika...huyu nyuma ya mshitakiwa saa ikarudishwa nyuma, ikaandika saa nne dakika 31.5...’akasema na yule shahidi akawa pembeni akiangalia tu

‘Hapana hiii nakala yako sio sahihi...’akasema muendesha mashitaka

‘Endelea kuangaliamwenyewe, muda ambao, hata mshitakiwa hajafika, ...ndio muda ambao mauaji yalifanyika, kwa mujibu wenu, sasa hebu niambieni....’akasema

‘No, ....nahisi kuna makosa, huenda umebadili saa...’akasema muendesha mashataka

‘Saa hazijabadilishwa,dafatari hilo litawakilishwa kama ushahidi, ili kusije kukatokea mabadiliko yoyote, ...hii ni nakala tu, na Inaonyesha waziwazi hapa, hakuna aliyebadili saa, angalia mwenyewe kwa makini...’akasema wakili

‘Baada ya huyo, ...., ikaja kwa mshitakiwa ikaandikwa saa nne dakika 30,...ina maana saa ikarudishwa nyuma,kwanini ifanyike hivyo...hizi saa zilikuwa zinarudi kinyume nyume au mimi sioni vyema...’akasema wakili mtetezi

‘Nafikiri kuna tatizo hapo, ....’akasema wakili muendesha mashitaka.

‘Tatizo la nani sasa....hii inaonyesha wazi hamukuwa mumefanya uchunguzi wa kina, nina uhakika muuaji hamjampata...’akasema wakili mtetezi.

‘Kwanaza hii  ni nakala tu, ...hatuwezi kuithibitisha, .....yawezekana imetengenezwa...’akasema shahidi na wakili muendesha mashitaka akamgeukia na kuonekana akiwaza jambo

‘Itisheni daftari kwa walinzi, muhakiki,  ......’akasema wakili mtetezi na hakimu akataka aione hiyo nakala, alipoangalia, na kuona hicho alichokuwa akisema wakili mtetezi, akasema;

‘Wakili mtetezi una uhakika na hii nakala yako kuwa kweli umechukua kwa walinzi...?’ 
akaulizwa

‘Nina uhakika muheshimiwa...’akasema wakili mtetezi, na hakimu akamgeukia wakili muendesha mashitaka na wakili huyo akasema

‘Haya ni makosa madogo tu,ya watu wa mapokezi lakini haliwezi kubadilisha chochote, muheshimiwa hakimu mimi , wakili mtetezi aendelee na mswali mengine, sisi tunafuatilia hilo kosa tutakuja na jibu sahihi, ni kwanini imetokea hivyo...mpelelezi wetu aliyefanya hiyo kazi kwasasa hayupo, kaitwa kwenye majukumu mengine, angeuliza hilo swali tulimpomsimamisha kutoa ushahidi....’akasema muendesha mashitaka.

‘Ndugu muheshimiwa hakimu, naomba mtu wa mapokezi aitwe kwanza ili kuthibitisha hili kwanini saa haziendani sawa na mtiririko wa watu...’akasema wakili mtetezi.

Wakili muendesha mashitaka akapinga hiyo hoja na kusema yeye amewaita mashahidi wake anavyotaka yeye, kama wakili huyo anataka kujenga hoja yake, atafanya hivyo kwa muda wake, na akitaka kwa muda huo, atamuita huyo mtu wa mapokezi na kujenga hoja yake.

‘Ndugu muheshimiwa hakimu, hizi saa zilikuja kuandikwa baadaye, yaonekana baaada ya mshitakiwa kupita ndipo saa hizi zikaandikwa, ..kwahiyo aliyeandika hakutizama vyema mtu wa nyuma yake, au hawa watu wawili wa nyuma yake yawezekana walikuwa hawajaandika saa ....au vinginevyo ni mipango iliyofanywa na huyo muuaji, au hata hawa waendesha mashitaka....’akasema wakili mtetezi.

‘Hayo unayasema wewe, unaweza kuthibitisha hilo kuwa sisi tumefanya hivyo...’akasema muendesha mashitaka kwa sauti ya ukali kidogo

‘Kwahiyo basi ukiangalia mpangilia wa saa, marehemu alipigwa risasi wakati mshitakiwa 
anaingia mapokezi,....ukiangalia mfuatano wa saa ulivyo, ...hapa inaoyesha muendesha mashitaka sio swala la kubuni, angalia mwenyewe...’akasema

‘Hayo unayaona wewe...lakini kwa kumbukumbu za daftari hilo yaonyesha mshitakiwa alikuwa mapokezi kwa muda ulioandikwa...na aliweza kufika akafanya mauaji kama muda alivyoanishwa na dakitari.....hizi kumbukumbu zinaweza kuwa zimekosewa, lakini matukio yanakwendana sawa na muda...’akasema wakili muendesha mashitaka , na wakili mtetezi akamgeukia docta

‘Kwa kumbukumbu gani, toeni huo ushahidi, maana ushahidi ni maandishi, ....kama kuna kumbukumbu nyingine tuonyesheni...’akasema wakili mtetezi

‘Haya natumai hilo mtalifuatilia...mawakili, tusipoteze muda....’akasema hakimu.

‘Muheshimiwa hakimu , na nina uhakika wakilifuatilia watagundua kuna makosa yamefanyika kuwa huyu mshitakiwa sio muuaji, muuaji bado hamjamkamata....’akasema

‘Hayo ni tumuachie muendesha mashitaka , endelea na mswali kwa shahidi, kama huna maswali mengine, tuendelee....’akasema hakimu na akawa amewageukia wasaidizi wake wakawa wanateta.

Muendesha mashitaka, akasema;

‘Tatizo la wakili mtetezi, unajenga hoja kwa kutegemea mashahidi wangu, unachotakiwa ni wewe kusubiria muda wako, uwaite mashahidi wako, na ujenge hoja zako....’akasema

‘Ni mpangilio wako, mimi sihitaji mashahidi, hawa mashahidi wako watakuwa mashahidi wangu, kama ulivyoona...’akasema wakili huyo na hakimu akaingilia kati na kusema hataki malumbano, na wakili mtetezi, akamgeukia shahidi

‘Je mshitakiwa hakuwa na jereha kichwani...?’ akaulizwa dakitari

‘Ndio alikuwa na jereha kichwani.....’akasema dakitari

‘Ni jeraha la kitu gani..?’ akaulizwa

‘Ni jeraha lilitokana na kitu kigumu, ....kama chuma, au kitu chochote kigumu....’akasema

‘Pia yawezekana kuwa kitako cha bastola au silaha, ...’akaulizwa

‘Yawezekana pia, lakini siwezi kuthibitisha hilo....’akasema docta

‘Je haikuwezekana kuona kama jereha hilo limetokana na kitako cha hiyo bastola iliyotumika kumuua marehemu....?’ akauliza na muendesha mashitaka akaweka pingamizi kwa swali hilo linamlazimisha dakitari kutoa maelezo yasiyo ya kitaalamu.

‘Yeye ni dakitari, alitakiwa kuanisha usawa, kuchunguza hilo jereha la mshitakiwa kufahamu kama kweli limetokana na kitu gani hasa, sio kwasababu ni mshitakiwa muache kuhakiki...,’akasema.

‘Dakitari keshakuambia hilo haliwezekani kutambua kuwa ni kitu gani halisi...’akasema muendasha mashitaka.

‘Nazungumza hili ili tupate uhakika..., hatuwezi kumuhukumu mtu kwa kosa la uuaji, kama hatuna uhakika yakini,..jereha la mshitakiwa linaonyesha kuwa alipigwa na kitu kigumu kichwani, na kitu hicho ni kitako cha hiyo bastola, .....’akasema wakili mtetezi

‘Lakini pia yawezekana kuwa ni kitu kingine....’akasema muendesha mashitaka

‘Pia yawezekana ni hiyo bastola ...’akasema na hakimu akaingilia kati kuwa mahakama iachiwe hiyo hoja, waendelee na ushahidi mwingine.

‘Ndugu muheshimiwa hakimu,....naishia hapa kwa huyu shahidi, lakini nikiwa sijarizika na ushahidi wao waliotoa, wamefanya haraka kumshitakia mteja wangu kabla hawajakamilisha ushahidi wao, na kama wangelichunguza vyema, ni lazima wangeligundua kuwa kuna mtu mwingine alifika mapema akafanya hayo mauaji..’akasema wakili mtetezi

Hakimu kuona hivyo, akawaita mawakili wote pale mbele akawa anateta nao kwa muda, halafu, baadaye akasema;

‘Kesi inaahirishwa hadi, na itasikilizwa tena baada ya wiki moja....’akasema hakimu

‘Bro, wiki kwangu ilikuwa ni tatizo, nikikumbuka kuwa nilishaagizwa nipelekwe gereza la kifo, kwani gereza nililokuwa nimepelekwa lilikuwa sio stahiki yangu.

Wakati tunatoka, nikamuomba wakili mtetezi wangu aombe niongee na kijana wetu,....akaniambia kijana wetu hataki kuonana na mimi, ila yeye atafanya mpango niongee na mama mtemi

‘Kwanini niongee na mama mtemi...?’ Profesa akauliza kwa mshangao

‘Kwanza sijalipwa pesa yangu,....kutokana na makubaliano yetu, pili kuna mambo mlikubaliana nahuyo mama mtemi hujayakamilishwa,....unajua ni mambo gani, kwahiyo kuna umuhimu wewe muongee na huyo mama haraka iwezekanavyo, kabla ya siku ya hiyo kesi,  vinginevyo, inabidi utafute wakili mwingine...’akasema na kuondoka

NB: Tuishie hapa kwa leo


WAZO LA LEO:  Unapoona upo kwenye ukweli, na unachofanya ni cha haki, usiyumbe, usingalie masilahi kwanza, ni bora ukose hayo masilahi, lakini utete ukweli, hata kama ukweli huo utakufanya ukosane na watu, hata kama ukweli huo utakufanya ukose masilahi, wewe simamia kwa nguvu zako zote. Tukumbuke  ukweli  na haki, vipo juu wakati wote..., kuliko hayo masilahi, masilahi ni mambo ya kupita tu, lakini ukweli na haki vitaendelea kuwa ukweli milele.
Ni mimi: emu-three

No comments :