Baada ya
shahidi mwingine kuitwa na kujieleza akiongozwa na muendesha mashitaka, ilikuja
zamu ya wakili mtetezi, ...Wakili mtetezi alisimama, na kujinyosha kidogo,
akamsogelea shahidi, akamuangalia, akageuka kuwaangalia watu waliokuwemo,akaonyesha
ishara fulani kwa watu wakacheka...
Wakili huyu
alishajijengea jina kwa jinsi gani anavyoweza kujenga hoja zake za kutetea mtu,
kwahiyo hapo kila mtu alikuwa askisubiria kwa hamu kusikia atasema nini
kubaliana na ushahidi huo,....
Profesa moyoni
alikuwa akimuomba mungu wake, ili amjalie wakili huyo aweze kutoa hoja zenye
kumsaidia, kwani ushahidi uliotolewa ulikuwa ni mnzito,
‘Bro, hapo kwanza nilikuwa namuomba
mungu na pili nillikuwa namshukuru sana huyo wakili kwa jinsi alivyokuwa
akinitete....’akasema mdogo mtu akiendelea kumsimulia kaka yake...
‘Japokuwa baadaye nilimuona wakili
huyo ni wale wale wanaotanguliza masilahi mbele....’akasema na kaka mtu
akashangaa
‘Kwanini..?’ akauliza kaka mtu
‘Utakuja kuona huko mbele, ...ni
mambo ya masilahi, hata kaam mtu anajua anachotetea ni haki, kumsaidia mtu,
lakini kama hakuna kitu, huna kitu ,maana mkoo mtupu haulambwi, ...hakuna anayependa
kufanya kazi bure, jao bure hiyo ina masilahi huko mbele ya mungu....’akasema
‘Ina maana hukuweza kumlipa huyu
wakili....hata hivyo, yeye si kazi yake atakula wapi? Halafu kwanza nikuulize,hivi.. ni nani
aliyekuwa akimlipa huyo wakili na wewe ulisema huna pesa...ni mama mtemi au?’
akaulizwa
‘Mhh.....bro, we acha tu,...kiukweli
sikuwa na pesa, si unajua pesa zangu ni za muda, upate dili ndio uingize pesa,
na pesa ikipatikana haikai, maana haina baraka,....’akasema
‘Sasa ilikuwaje, .....maana hapo
naona una wakili jembe....?’ akauliza kaka mtu
‘Wewe ngoja tuendelee na kisa chetu
nitakuelezea huko mbele, usivuruge mpangilio...’akasema
Haya endelea...’akasema kaka mtu
‘Sasa nitakusimulia kuhusu mashahidi wawili walioletwa mwishoni, ambao
waliweza kubadili muelekeo wa kesi, ... ili tuje kuhitimisha kisa
chetu.....’akasema mdogo mtu...
‘Tuhitimishe!...Mbona mambo mengi
bado, nataka kujua jinsi kijana wetu alivyokuja kuoana na binti wa mama mtemi...walikubalianaje
na je na huyo mama,...kuna yule binti mliyemtumia alikwenda wapi...na huyo kaka
yake...
‘Au sema ilikuwaje, na je huyo kijana
wetu watakuja huku kwetu au ndio keshakuwa mzungu....?’ akauliza,
‘Bro ngoja tuendelee...maana
nikikuelezea juu juu hutanielewa, na kijana wako msahau, akija mtakosana kabisa
ni bora akae huko huko.....’akasema mdogo mtu
‘Na akae,...mimi sina shida,mwenye
shida ni mama yake maana nasikia hali ...keshakuwa mgonjwa akimtaka mwanae...’akasema
kaka mtu.
‘Oh, masikini.....
Tuendelee na
kisa chetu
********
‘Unasema
mshitakiwa alionekana akitoka akiwa na bastola mkononi....?’ akaulizwa shahidi
na kutikisa kichwa kukubali, huku akisema
‘Ndio
muheshimiwa...’akasema shahidi
‘Na ni ...kutokana na kamera,...au sio, kamera
ambazo hata waigizaji wanaweza kuigiza tukio, au sio,...hizo kamera au hiyo kamera iliwekwa wapi na nani,
...?.’ akaulizwa huyu shahidi na wakili mtetezi, na shahidi huyo akatabasamu na
kusema.
‘Kamera hiyo
ni hizi kamera za nje zilizowekwa kwa ajili ya kunasia matukio ya uhalifu, na
wala sio kuwa ni kuigiza,....’akaambiwa
‘Kwahiyo
kamera hiyo haikuonyesha mshitakiwa akifyatua risasi, ilichagua kipi cha
kuonyesha au, ....?’ akaulizwa
‘Haikuonyesha...’akajibiwa
‘Kwahiyo
kuonekana kwake akitoka akiwa na bastola mkononi ndio ushahidi wenu kuwa yeye
ndiye aliyefanya hayo mauaji....au?’akaulizwa.
‘Tumeonyesha
ushahidi mbali mbali...kama nilivyoelezea awali, hatua kwa hatua, sio lazima ionekane akifyatua
risasi, vielelezo vya kiashiria vinathibitisha hilvyo, kuwa mshitakiwa ndiye
aliyefanya hilo tendo, na hiyo video ni kama ushahidi mwingine tu wa
kuthibitisha zaidi...’akasema
‘Nauliza
hivyo kwa vile hapa mumetumia ushahidi wa video, na kinachonishangaza ni
kwanini video hiyo isionyeshe tukio la ndani ,...inaonyesha tu mtu akikimbia na
bastola, sio kwamba mliamua kulikata hilo tukio, ili muweze kutimiza dhamira
yenu....?’akasema
‘Video hizi
za matukio ya uhalifu, zimewekwa nje,...kwahiyo haziwezi kunasa matukio ya
ndani ya majengo ya watu,...unafahamu sana....mara nyingi matukio ya ndani
hutegemea na matakwa ya mumiliki wa hilo jengo, kama mumiliki ameweka video
kama hizo, na tunazihitajia kisheria, tungeliweza kuzionyesha hapa, lakini
hatukuweza kupata ...’akasema shahidi
huyo
‘Ina maana hilo
jengo halina kamera za ndani za kunasia matukio...?’ akaulizwa
‘Zipo...’akasema
‘Kama zipo,
hiyo video....ipo wapi?’ akaulizwa
‘Kwa tukio
hilo, hatukuweza kupata hiyo video yake,....’akasema
‘Kwanini
hamukuweza kupata hiyo video yake, wakati nyie ni watu wa usalama, mna mamlaka
ya kuhakikisha inapatikana....au hamukuihitajia kwa vile haikidhi matakwa
yenu..?’akasema wakili mtetezi
‘Tumejitahidi
iwezekanavyo,...lakini kipindi chote cha tukio hilo,..kamera hizo zilikuwa
hazifanyi kazi, ilikuwa ni bahati mbaya ilitokea hivyo....’akasema
‘Unaona...!’
akasema wakili huyo akiashiria kwa mkono
‘Kama ni
hivyo, badoo hamjakamilisha kazi yenu, yaonekana kuna mtu, na huyo ndiye muuaji
halali, hamkutaka kumtafuta, ....’akasema wakili mtetezi, na wakili muendesha
mashitaka akasema hiyo sio kazi ya wakili mtetezi, kazi yake ni kumtetea mteja
wake.
‘Kwahiyo wewe
kama mpelelezi wa tukio hili hukuweza kupata ushahidi wa moja kwa moja kuwa
mshitakiwa alionekana akifyatua risasi ....?’ akauliza wakili huyo
‘Upo
ushahidi wa kinadharia, unao-onyesha kuwa bastola aliyokuwa nayo mshitakiwa
ndiyo iliyotumika kumuua marehemu, tumeshaonyesha hilo....na mshitakiwa ndiye
aliyepatikana na ushahidi huo, kuna alama za vidole, na zaidi kaonekana
akikimbia akiwa na hiyo bastola, alikuwa ana kimbia nini... tumekwisha onyesha
hayo yote kwenye ushahidi uliopita...’akasema huyo shahidi
‘Swali langu
ni je kuna ushahidi gani unaonyesha kuwa mshitakiwa ndiye aliyefyatua hiyo
risasi iliyomuua marehemu, maana kumeonekana ushahidi mshitakiwa anatoka akiwa
na bastola mkononi je upo ushahidi unaonyesha mshitakiwa akifyatua risasi....jibu
ndio au hapana’akauliza
Muendesha
mashitaka akaingilia, na kusema maswali ya wakili mtetezi ni ya kupoteza muda,
kwani alishaambiwa kuwa kamera iliyoonyesha hilo tukio ni ya nje na
isingeliwezekana kupata tukio la ndani, kwasababu kamera ya ndani ilikuwa
haifanyi kazi kwa muda huo...ila kuna ushahidi wa vielelezo unaonyesha kuwa
mshitakiwa ndiye aliyefanya hilo tukio...
‘Kwa
vielelezo gani vinavyoonyesha kuwa mshitakiwa ndiye aliyefyatua bastola,...ndio
swali langu hapo, hakuna kielelezohata kimoja kilichoonyesha mshitakiwa ndiye
aliyefyatua risasi au sio, maana mumeonyesha kuwa yeye alionekana akikimbia
akiwa kashika hiyo bastola, sasa ushahidi upi wa kuonyesha kuwa ndiye yeye aliyefyatua
risasi...’akasema wakili huyo
‘Ushahidi
upo wa kinadharia kuwa ndiye aliyetenda hivyo,...’akasema huyo shahidi
‘Upi huo....huo
ushahidi wa kinadharia mimi sijauona?’ akauliza wakili
‘Bastola ina
alama za vidole vya mshitakiwa, mshitakiwa kaonekana wazi akiwa kaishikilia
hiyo bastola kwenye hiyo video, akikimbia na hiyo bastola, mshitakiwa
alionekana na mashaidi wengi kuwa aliingia, akielekea chumba alichokuwa
marehemu...wakiwemo walinzi...hivyo vyote tumeonyesha wewe unataka nini tena...’akasema
huyo shahidi
‘ Kama ni
swala la kuingia hapo kwenye hilo jengo, mbona waliingia watu wengi tu, na
kushikilia bastola sio tija, yoyote anaweza kushikilia, na asitende kosa,
walinzi wa hapo wana silaha, mbona hamjawatuhumu wao? Akauliza
‘Unapoteza
muda tu wakili mtetezi, tunzungumizia silaha iliyotenda hilo kosa, silaha hiyo
haikuwa imeshikiliwa na walinzi, ....’akaambiwa
‘Sawa...kwa
hilo ngoja nikuelezee ilivyokuwa, huyu mshitakiwa aligongwa kichwani kwa
makusudi, na huyo muuaji,...kwanini aligongwa kichwani, ni ili apoteze fahamu
na muuaji akamshikisha mshitakiwa hiyo bastola mkononi,....hata hivyo,
mshitakiwa ...’akasema wakili mtetezi na wakili muendesha mashitaka akamkatisha
na kupinga maneno yake hayo kuwa hayo ni maelezo yake hayana msingi.
‘Ndugu
muheshimiwa hakimu, ataka kuonyesha kuwa...hawa watu wanamuacha muaji halisi,
wanaacha kumtafuta muuaji halisi, wanamg’ang’ania huyu mshitakiwa,najaribu
kuwaonyesha hali halisi ilivyokuwa.....’akasema
‘Hiyo sio
kazi yako.....’akasema wakili muendesha mashitaka
‘Haya, huyu
mshitakiwa mnasema alionekana akikimbia na hiyo bastola, ni kutokana na
kuchanganyikiwa,.... alipozindukana,baada ya kugongwa kichwani, akili haikuwa
sawa, aliiona hiyo bastola ikiwa karibu
yake, akaichukua akitaka kujihami,...’akasema wakili
‘Hayo ni
mawazo yako,utakuja kujengea hoja yako ukitoa ushahidi wako kama unao, sisi
tumejenga ushahidi wetu hivyo maana tuna uhakika na hilo....’akasema wakili
muendesha mashitaka
‘Kama mna
uhakika na hilo, tuonyesheni ushahidi
unaoonyesha mshitakiwa akifyatua risasi...kama mumeweza kuonyesha mshitakiwa
akikimbia na bastola,basi yawezekana kuwepo na ushahidi wa kuonyesha mshitakiwa
akifyatua risasi, na jengo hilo lina kamera,..ni juu yenu kuitafuta, na kwanini
muda huo hiyo kamera isifanye kazi....hamuoni hapo kuna walakini?’ akauliza
wakili mtetezi.
‘Hiyo ni
sehemu ndogo tu, ya ushahidi unaotaka wewe,....sehemu kubwa tumeonyesha kwa
vielelezo, na vyote vinambana mshitakiwa....’akasema shahidi
‘Hiyo ni
sehemu ndogo,...!? Hapana hiyo ni sehemu muhimu sana, kama mnataka haki itendeke....na
ni muhimu sana kwa mshitakiwa...’akasema wakili mtetezi,
‘Ndio maana
tunasema muda wako wa kutoa ushahidi na vielelezo vyako ukifika fanya hivyo,
vinginevyo unapoteza muda tu...’akasema wakili muendesha mashitaka
‘Kwahiyo kwa
kifupi hakuna ushahidi wa moja kwa moja
kuwa mshitakiwa ndiye aliyefyatua risasi iliyomuua marehemu....?’akasema wakili
‘Sisi
tumeshaonyesha vielelezo vyote vinavyoonyesha kuwa mshitakiwa ndiye aliyefanya
hilo tendo, hayo unayoongea wewe au kutaka wewe iwe hivyo ni mawazo
yako.....’akasema wakili muendesha mashitaka
‘Nimemalizana
na huyu shahidi muheshimiwa hakimu....’, akasema wakili mtetezi,
*******
Baadaye
aliitwa shahidi mwingine,...kiujumla bro, hawa watu walikuwa wakikamilisha tu ushahidi wao,...pale
walipoona kuna mapungufu, wanamuita shahidi wao tena...sasa akaitwa dakitari ,
dakitari aliyepima hilo tukio.
Shahidi huyo
akatoa maelezo yake akisimamiwa na muendesha mashitaka na alipomaliza kutoa
maelezo yake ikawa ni zamu ya wakili
mtetezi.
‘Katika maelezo
yako, umetaja muda marehemu alipofariki,... na kwa maelezo ya muendesha
mashitaka aliongezea kusema ni muda ambao mshitakiwa alipokuwepo humo, kwani
muda huo unaendana sawa na muda mshitakiwa alipopigwa risasi na kufa, na
unasema kifo cha marehemu hakikuchukua muda, mimi hapo inanipa mashaka kidogo....’akaanza
wakili mtetezi.
‘Kwanini....?’
akauliza huyo shahidi
‘Jinsi
ulivyotaja muda...kuna walakini hapo
‘Kwa vipi...kazi
yangu ni kutaja muda wa tukio,...au?’akauliza shahidi
‘Huo muda
una uhakika nao...?’ akauliza
‘Ndio...
siku hizi utaalamu wa komputa unakuelezea kila kitu....’akasema
‘Umetaka
muda sawa, na muendesha mashitaka anasema kuwa hakuna walakini kuwa mshitakiwa
ndiye aliyesababisha hayo mauaji, kutokana na muda, kuwa mshitakiwa alikuwa
kwenye eneo la tukio,... kwasababu kwa muda huo yeye ndiye aliyekuwa na
marehemu, sawa si sawa?’ akaulizwa
‘Mimi
nimetoa taarifa za muda, sasa kama mshitakiwa alikuwemo, hizo ni kazi zao,...na
utaalamu wangu unaonyesha kuwa kifokilitokea saa ngapi, sasa mengine kama
yanakutatizo labda upate maelezo kwa muendesha mashitaka....’akasema
‘Hebu
tuangalia mpangilia wa saa...huyu mshitakiwa alisaini kwenye daftari la wageni
saa ngapi.?’ Akauliza
‘Waulize
wahusika, .....’akasema
‘Hapana
nakuuliza wewe.....’akasema
‘Ilikuwa...saa
nne na nusu...’akasema muendesha mashitaka
‘Aliposaini akatembea
kutoka pale mapokezi hadi chumba hicho, akafika kwenye chumba alipokuwepo marehemu saa nne na
dakika 3I.na sekunde kadhaa,...kutoka pale
mapokezi hadi chumba hicho alitumia dakika moja na sekunde kadhaa...
‘Ndio....’akasema
muendesha mashitaka kwa sautii ya kuonyesha anapotezewa muda
‘Huyu mtu
alifika na kuanza kuongea na marehemu, wakaanza kubishana, na kwa mujibu wa
taarifa za mpelelezi wako , na dakitari hapa anasema marehemu alipigwa risasi
saa nne na dakika 32...hebu tuyaangalia haya maongezi yalichukua muda gani..
‘Yaangalia
wewe,....’akasema muendesha mashitaka
‘Huyu
shahidi anachochoangalia ni muda gani marehemu alipigwa risasi....’akasema
‘Ni muda
gani...marehemu alipigwa risasi?’ akaulizwa dakitari
‘Ni muda wa
saa nne dakika 32....’akasema
Wakali mtetezi,
akatoa karatasi, na kusema, ...
‘Hii ni
nakala niliotoa kwenye daftari la wageni....’akasema
‘Hebu
tuangalia hizi kumbukumbu kutoka mapokezi,
Turudi nyuma
kidogo kabla ya mshitakiwa hajaandikisha kuwa ameingia kwenye hilo jengo
kumuona marehemu.
Turudi watu
watano nyuma tukiangalia mpangilio, wa saa...angalia watu hawa wa tano nyuma
saa zimefuatana kwa utaartibu mnzuri tu, ....haya ikafika kwa hawa watu wawili
nyuma ya mshitakiwa alipoandika jina lake..
‘Hebu angalia
mtu wa pili nyuma ya mshitakiwa alifika saa nne na dakika 31...sawa si
sawa...?’ akauliza na huyo shahidi akamgeukia muendsha mashitaka.
‘Sawa...hebu
hebu...kwanza,hii nakala umeipatia wapi...?.’akasema muenddaha mashitaka
‘Daftari ni
lile lile, mimi nilichofanya ni kutoa nakala, kama unataka kuhakikisha unaweza
kuagiza hilo daftari la wageni kwa walinzi....’akasema wakili mtetezi
‘Sawa...uliza
swali lako...’akasema sasa akiwa bado anaikagua ile karatasi
‘Haya hebu
angalia,..., walikuja watu wawili nyuma yake, yaani nyuma ya mshitakiwa
...kabla ya mshitakiwa, angalia saa walizoandika...huyu nyuma ya mshitakiwa saa
ikarudishwa nyuma, ikaandika saa nne dakika 31.5...’akasema na yule shahidi
akawa pembeni akiangalia tu
‘Hapana hiii
nakala yako sio sahihi...’akasema muendesha mashitaka
‘Endelea
kuangaliamwenyewe, muda ambao, hata mshitakiwa hajafika, ...ndio muda ambao mauaji
yalifanyika, kwa mujibu wenu, sasa hebu niambieni....’akasema
‘No,
....nahisi kuna makosa, huenda umebadili saa...’akasema muendesha mashataka
‘Saa
hazijabadilishwa,dafatari hilo litawakilishwa kama ushahidi, ili kusije
kukatokea mabadiliko yoyote, ...hii ni nakala tu, na Inaonyesha waziwazi hapa,
hakuna aliyebadili saa, angalia mwenyewe kwa makini...’akasema wakili
‘Baada ya
huyo, ...., ikaja kwa mshitakiwa ikaandikwa saa nne dakika 30,...ina maana saa
ikarudishwa nyuma,kwanini ifanyike hivyo...hizi saa zilikuwa zinarudi kinyume
nyume au mimi sioni vyema...’akasema wakili mtetezi
‘Nafikiri
kuna tatizo hapo, ....’akasema wakili muendesha mashitaka.
‘Tatizo la
nani sasa....hii inaonyesha wazi hamukuwa mumefanya uchunguzi wa kina, nina
uhakika muuaji hamjampata...’akasema wakili mtetezi.
‘Kwanaza hii
ni nakala tu, ...hatuwezi kuithibitisha,
.....yawezekana imetengenezwa...’akasema shahidi na wakili muendesha mashitaka
akamgeukia na kuonekana akiwaza jambo
‘Itisheni
daftari kwa walinzi, muhakiki, ......’akasema wakili mtetezi na hakimu
akataka aione hiyo nakala, alipoangalia, na kuona hicho alichokuwa akisema
wakili mtetezi, akasema;
‘Wakili
mtetezi una uhakika na hii nakala yako kuwa kweli umechukua kwa walinzi...?’
akaulizwa
‘Nina
uhakika muheshimiwa...’akasema wakili mtetezi, na hakimu akamgeukia wakili
muendesha mashitaka na wakili huyo akasema
‘Haya ni
makosa madogo tu,ya watu wa mapokezi lakini haliwezi kubadilisha chochote,
muheshimiwa hakimu mimi , wakili mtetezi aendelee na mswali mengine, sisi tunafuatilia
hilo kosa tutakuja na jibu sahihi, ni kwanini imetokea hivyo...mpelelezi wetu
aliyefanya hiyo kazi kwasasa hayupo, kaitwa kwenye majukumu mengine, angeuliza
hilo swali tulimpomsimamisha kutoa ushahidi....’akasema muendesha mashitaka.
‘Ndugu
muheshimiwa hakimu, naomba mtu wa mapokezi aitwe kwanza ili kuthibitisha hili
kwanini saa haziendani sawa na mtiririko wa watu...’akasema wakili mtetezi.
Wakili
muendesha mashitaka akapinga hiyo hoja na kusema yeye amewaita mashahidi wake
anavyotaka yeye, kama wakili huyo anataka kujenga hoja yake, atafanya hivyo kwa
muda wake, na akitaka kwa muda huo, atamuita huyo mtu wa mapokezi na kujenga
hoja yake.
‘Ndugu
muheshimiwa hakimu, hizi saa zilikuja kuandikwa baadaye, yaonekana baaada ya
mshitakiwa kupita ndipo saa hizi zikaandikwa, ..kwahiyo aliyeandika hakutizama
vyema mtu wa nyuma yake, au hawa watu wawili wa nyuma yake yawezekana walikuwa
hawajaandika saa ....au vinginevyo ni mipango iliyofanywa na huyo muuaji, au
hata hawa waendesha mashitaka....’akasema wakili mtetezi.
‘Hayo
unayasema wewe, unaweza kuthibitisha hilo kuwa sisi tumefanya hivyo...’akasema
muendesha mashitaka kwa sauti ya ukali kidogo
‘Kwahiyo
basi ukiangalia mpangilia wa saa, marehemu alipigwa risasi wakati mshitakiwa
anaingia mapokezi,....ukiangalia mfuatano wa saa ulivyo, ...hapa inaoyesha
muendesha mashitaka sio swala la kubuni, angalia mwenyewe...’akasema
‘Hayo
unayaona wewe...lakini kwa kumbukumbu za daftari hilo yaonyesha mshitakiwa
alikuwa mapokezi kwa muda ulioandikwa...na aliweza kufika akafanya mauaji kama
muda alivyoanishwa na dakitari.....hizi kumbukumbu zinaweza kuwa zimekosewa,
lakini matukio yanakwendana sawa na muda...’akasema wakili muendesha mashitaka
, na wakili mtetezi akamgeukia docta
‘Kwa
kumbukumbu gani, toeni huo ushahidi, maana ushahidi ni maandishi, ....kama kuna
kumbukumbu nyingine tuonyesheni...’akasema wakili mtetezi
‘Haya
natumai hilo mtalifuatilia...mawakili, tusipoteze muda....’akasema hakimu.
‘Muheshimiwa
hakimu , na nina uhakika wakilifuatilia watagundua kuna makosa yamefanyika kuwa
huyu mshitakiwa sio muuaji, muuaji bado hamjamkamata....’akasema
‘Hayo ni tumuachie
muendesha mashitaka , endelea na mswali kwa shahidi, kama huna maswali mengine,
tuendelee....’akasema hakimu na akawa amewageukia wasaidizi wake wakawa
wanateta.
Muendesha
mashitaka, akasema;
‘Tatizo la
wakili mtetezi, unajenga hoja kwa kutegemea mashahidi wangu, unachotakiwa ni
wewe kusubiria muda wako, uwaite mashahidi wako, na ujenge hoja zako....’akasema
‘Ni
mpangilio wako, mimi sihitaji mashahidi, hawa mashahidi wako watakuwa mashahidi
wangu, kama ulivyoona...’akasema wakili huyo na hakimu akaingilia kati na
kusema hataki malumbano, na wakili mtetezi, akamgeukia shahidi
‘Je mshitakiwa
hakuwa na jereha kichwani...?’ akaulizwa dakitari
‘Ndio alikuwa
na jereha kichwani.....’akasema dakitari
‘Ni jeraha
la kitu gani..?’ akaulizwa
‘Ni jeraha
lilitokana na kitu kigumu, ....kama chuma, au kitu chochote kigumu....’akasema
‘Pia
yawezekana kuwa kitako cha bastola au silaha, ...’akaulizwa
‘Yawezekana
pia, lakini siwezi kuthibitisha hilo....’akasema docta
‘Je haikuwezekana
kuona kama jereha hilo limetokana na kitako cha hiyo bastola iliyotumika kumuua
marehemu....?’ akauliza na muendesha mashitaka akaweka pingamizi kwa swali hilo
linamlazimisha dakitari kutoa maelezo yasiyo ya kitaalamu.
‘Yeye ni
dakitari, alitakiwa kuanisha usawa, kuchunguza hilo jereha la mshitakiwa
kufahamu kama kweli limetokana na kitu gani hasa, sio kwasababu ni mshitakiwa
muache kuhakiki...,’akasema.
‘Dakitari
keshakuambia hilo haliwezekani kutambua kuwa ni kitu gani halisi...’akasema
muendasha mashitaka.
‘Nazungumza
hili ili tupate uhakika..., hatuwezi kumuhukumu mtu kwa kosa la uuaji, kama
hatuna uhakika yakini,..jereha la mshitakiwa linaonyesha kuwa alipigwa na kitu
kigumu kichwani, na kitu hicho ni kitako cha hiyo bastola, .....’akasema wakili
mtetezi
‘Lakini pia
yawezekana kuwa ni kitu kingine....’akasema muendesha mashitaka
‘Pia
yawezekana ni hiyo bastola ...’akasema na hakimu akaingilia kati kuwa mahakama
iachiwe hiyo hoja, waendelee na ushahidi mwingine.
‘Ndugu
muheshimiwa hakimu,....naishia hapa kwa huyu shahidi, lakini nikiwa sijarizika
na ushahidi wao waliotoa, wamefanya haraka kumshitakia mteja wangu kabla
hawajakamilisha ushahidi wao, na kama wangelichunguza vyema, ni lazima
wangeligundua kuwa kuna mtu mwingine alifika mapema akafanya hayo mauaji..’akasema
wakili mtetezi
Hakimu kuona
hivyo, akawaita mawakili wote pale mbele akawa anateta nao kwa muda, halafu, baadaye
akasema;
‘Kesi
inaahirishwa hadi, na itasikilizwa tena baada ya wiki moja....’akasema hakimu
‘Bro, wiki kwangu ilikuwa ni tatizo,
nikikumbuka kuwa nilishaagizwa nipelekwe gereza la kifo, kwani gereza nililokuwa
nimepelekwa lilikuwa sio stahiki yangu.
Wakati tunatoka, nikamuomba wakili
mtetezi wangu aombe niongee na kijana wetu,....akaniambia kijana wetu hataki
kuonana na mimi, ila yeye atafanya mpango niongee na mama mtemi
‘Kwanini niongee na mama mtemi...?’ Profesa
akauliza kwa mshangao
‘Kwanza sijalipwa pesa yangu,....kutokana
na makubaliano yetu, pili kuna mambo mlikubaliana nahuyo mama mtemi hujayakamilishwa,....unajua
ni mambo gani, kwahiyo kuna umuhimu wewe muongee na huyo mama haraka
iwezekanavyo, kabla ya siku ya hiyo kesi,
vinginevyo, inabidi utafute wakili mwingine...’akasema na kuondoka
NB: Tuishie
hapa kwa leo
WAZO LA LEO: Unapoona upo kwenye ukweli, na unachofanya ni
cha haki, usiyumbe, usingalie masilahi kwanza, ni bora ukose hayo masilahi,
lakini utete ukweli, hata kama ukweli huo utakufanya ukosane na watu, hata kama
ukweli huo utakufanya ukose masilahi, wewe simamia kwa nguvu zako zote.
Tukumbuke ukweli na haki, vipo juu wakati wote..., kuliko hayo
masilahi, masilahi ni mambo ya kupita tu, lakini ukweli na haki vitaendelea
kuwa ukweli milele.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment