Siku hiyo
nilikuwa nimekaa sebuleni, nikiwa nimekunja nne, pembeni kuna chupa ya
kinywaji, sina wasiwasi pesa zipo japo kidogo,..unajua tena masikini akipata
inakuwaje...na wakati nainua gilasi ya kinywaji kwa madaha, mara nikahisi mwili ukinisisimuka, nikainua
kichwa na kutizama ujio wa mlangoni. Huwa sijui ni kwanini, ....
‘Unajua bro,
kutokana na utaalamu huu wa madawa, na mazoezi,...huwa nimeshajengeka kuwa na
hisia fulani,...najua wengi, ingelikuwa huku watasema una kitu kama mashetani
au ...vyovyote iwavyo ila nina hiyo tabia,...ni tabia ya kuhisi jambo kabla
halijatokea, hasa ikiwa ni hatari,...kwahiyo nilivyohisi mwili unasisimuka,
nikajua kuna jambo, na kweli haikupita muda mara kule mlangoni, nikaona watu wakiingia.
Pale
nilipokuwa nimekaa nilikuwa naona mlango wa kuingilia, na nilichagua sehemu
hiyo mahususi kwa ajili ya kujihami, ...nilitaka mtu yoyote akiingia nimuone,
ni kujihami tu maana muda mwingine nikiwa chumbani siwezi kuona anayeingia na
kutoka
Hata hivyo
wakati nachukua chumba, kwa siku mbili tatu, nilishawaambia kuwa sitaki mgeni.
‘Nina kazi
naifanya sitaki usumbufu, kwahiyo akija mgeni au mtu yoyote kuniulizia
msimwambie nipo hapa, ....’nikawaambia
‘Sawa bosi,
upendavyo, jisikie upo nyumbani...’akasema huyo muhudumu, lakini ka hisia zile
nikahisi kuna jambo..
‘Mhh, nahisi
hatari....’nikasema na kusimama kidogo, lakini nikajipa moyo kuwa hata kama ni
hatari, bado huyo mtu hawezi kuja kuniona moja kwa moja, ,...ni lazima
muhudumu, atakuja kuniambia kwanza. Nikainua chupa kabla sijapiga fundo,
nikahisi hiyo hali tena, nikatikisa kichwa kuondoa hiyo hali, nikasema kwa
sauti ndogo
‘Hata hivyo,
huku nani atanifuata, ....mmh nihahisi ni owoga tu, .....’na kabla sijamaliza
kujiongelesha kichwani,nikaona mlango wa sehemu ile niliyopo ukifunguliwa, hapo
nikatega macho, na masikio...
Alikuwa ni mtu wa mapokezi ! Kwanza nilijua
yupo peke yake , nikajiandaa kumwambia sitaki wageni, ....lakini kumbe nyuma
yake kuna mtu!
Ni nani huyo
yupo nyuma yake, huyo mtu alisimama nyuma ya huyo mtu wa mapokezi, kama vile anajificha nyuma yake, sikumuona
mapema....
‘Oh,....alikuwa
ni mwanamke...., mwili ukanizizima, nikataka kuinuka niende chooni, lakini
isingeliwezekana kwani choo, kipo muelekeo wa huko wanapotokea hawo watu.
‘Nimekubamba....’ilikuwa
sauti ikitokea nyuma kwa huyo mwanamke,
na sauti yake ilinifanya nidondoshe ile gilasi niliyokuwa nimeshikilia, na
kushikwa a kikohozi cha muda.
‘Mhh,...kohokoho...
u-u-u-menibamba! Kwanini, karibu...hamna shida, unajua , nipo hapa nasubiri
kukutana na bosi wangu mpya...kohokohokoho, karibu madame.....’nikasema huku nikijikanganya.
‘Najua....yah,
, tena sana, kila bosi wako lazima aingie mkenge wako au sio...ndio zako
hizo,..., hahaha....angalia usitie hasara kwa kuvunja gilasi za watu kwa
uwoga...’akasema huku akimuashiria yule mtu wa mapokezi aondoke, utafikiri ana
mamlaka naye, na yule muhudumu kweli akageuka na kuondoka.
Huyu mama
alisubiri kuhakikisha yule muhudumu kaondoka kabisa ,halafu akasogea pale
nilipokaa, akasema huku akitabasamu kwa dharau.
‘Siku hizi
huonekani eeh,....umepotea kabisa maeneo ya kule kwetu,....’akasema akishika kidevu
huku akibenua mdomo kwa dharau...
‘Mbona nipo
tu, ni kwa vile umesema huna kazi na mimi,sasa nitakuonaje huko kwako,....au
kuna kazi nije...’profesa akasema sasa akijitutumua kuondoa ule uwoga uliokuwa
umemtinga.
‘Mhh,...
kumbe umekuja kujificha huku, ukitumbua pesa za mlungula...au sio...?’akaniambia
huyo mama huku akivuta kiti na kukaa , alikaa mkabala na mimi, ili tuwe
tunaangaliana,sikupenda akae hivyo .Akawa sasa ananiangalia moja kwa moja
usoni,bila kupepesa macho.
‘Hapana,...sio
pesa ya mlungula,... nilifanya kazi sehemu moja,nikapata vijisenti, na kwa vile
nina miadii na bosi wangu mmoja ndio nikaona nije nipumzike hapa...ni kawaida
tu..leo hapa kesho pale, si unajua mimi sina kazi ya kudumu....’nikazidi
kudanganya
‘Hahaha,...watu
kama nyie mtapata kazi ya kudumu,...halafu unasema eti umekuja hapa kupumzika
wakati umepanga kwenye hii hoteli, leo siku ya ngapi....usinifanye mimi mjinga....’akasema
akizidi kumuangalia profesa moja kwa moja usoni.
'Ndio
hivyo...’akasema profesa akishindwa kuendelea kuongea
‘Ok, sina
haja ya maneno mengi,....ila nafahamu unajua kwanini nimekuja hapa kukuona au
sio...?’ akasema
‘Aaah,
kuhusu pesa yako au sio...’akasema profesa huku akitoa pesa mfukoni, ilikuwa
dola elifu tano, akaziweka mbele ya huyo mama, na huyo mama akaziangalia kwa
macho ya dharau na kusema;
‘Unakumbuka
deni langu,.... ulisema utalipa sehemu nyingine mwisho wa mwezi huu uliopita,
na mwezi umeshapita sijapata hizo pesa,unataka nikuelewe vipi...na hiki ni kitu
gani unanipa.....hiyo ndio malipo yangu, naona unanitania...’akasema huyo mama
akizingalia zile pesa bila kuzigusa.
‘Ndio maana
nipo hapa kukutana na bosi wangu, nitakuja kwako nikitoka hapa kama sio leo ni
kesho...huyo bosi wangu, ananizungusha kidogo, lakini nina uhakika ...’nikasema
nikitikisa kichwa kama kukubali.
‘Bosi wako
,bosi wako..huyo bosi wako ni nani....?’ akauliza
‘Huna haja
ya kumfahamu,...si unajua tena...’akasema profesa
‘Nataka pesa
yangu, wakati unaichukua hukunipa muda...unakumbuka...ukajifanya
mjanja,..hahaha, utaninyaa, nakuambia, utanisimulia..bado,.....’akasema
‘Nakuomba
uniamini, nipe wiki moja hivi...ukiniona kimia, nakuahidi nitakuwa nimeshapata
pesa yako usijali...nilipanga kila wiki niwe napunguza, lakini mambo hajawa
safi,....lakini ipo njiani inakuja...’nikasema nikinyosha mkono kuzichukua zile
pesa, nikijua hataki kuzichukua.
‘ Wiki
moja!,...nikupe wiki moja...hahaha, unanitania sio,....Sikiliza wewe mwizi wa
mlungula,....’akasema sasa akiwa kasimama, na jinsi mkono wake ulivyokwenda
haraka na kuzichukua zile pesa utafikiri
ulimi wa mjusi ukidaka wadudu wanaopita hewani.
‘Labda wewe
hujanielewa, sipendi utani, usione nimefika hapa ukafikiri nimebahatisha,
nafahamu nyendo zako A to Z, najua sasa mpo kwenye mpango wa kumla mtu pesa
zake, sasa sijui kwa vipi,....’akasema akizifutika hizo pesa sehemu ya maziwa
yake bila kuzihesabu.
‘Hizi hazipo
kwenye mahesabu,ni gharama ya kukufuata...unasikia....’akasema
‘Hapana
napunguza deni,.....’akasema profesa
‘Mimi hilo
sijui,na sijali jinsi gani unazipata hizo pesa, na wala sitaki kuingilia wizi wako.....,
ilimradi unanilipa pesa yangu kama ulivyoahidi...’huyo mama akasema
‘Nitakuletea
pesa yako madame,..., wewe uniamini
tu....na sio za wizi ni jaso langu...’akasema profesa hukuu akichelea huyo mama
asije kuleta vurugu hapo, na watu wakawaona.
‘Poa,...mimi
naondoka, nakupa siku hizi mbili, au tusema tatu, nikija , au popote
utakapokwenda ujue ninakuja kwa shari... sitakuja hivi hivi,nikuache hivi hivi...leo
nimeiheshimu hii hoteli, wananifahamu na nawafahamu ni watu wangu...’akasema
sasa akiwa sasa anasimama.
‘Ila
kumbuka, safari nyingine nikija, ...nitakuja nikiwa nimekamilika, usinione sasa
ni mtu mzima ukafikiri siwezi kukumudu...kwanza wewe hunipi shida...ni mdwebedo
tu...hujai hata kiganjani...’akasema na kugonga meza kwa nguvu, hadi vinywaji
vilivyokuwepo vikamwagika
‘Oh...tafadhali
madame...utafanya watu wanifikirie
vibaya....’nikasema , na yeye bila kujali,huyoo, akaondoka zake nikabakia
najikunguta kinywaji kilichonirukia, usoni na nguoni. Mwili ulikuwa umeanza
kunietemeka.
*********
Nilibakia
nimeduwaa maana sikuweza kafahamu vipi huyu mama aliweza kugundua kuwa nipo hapo,kwani hapo ni sehemu niliyoitafuta
ya kujificha, nikiwa nafanya vitu vyangu, na kiujumla pesa nilikuwa nayo
kidogo tu, lakini ilikuwa haitoshi kumlipa huyo mama, kutokana na makubaliano yetu
...akawa sasa kachukua kaakiba kangu niliko kuwa nak...
Nikaangalia
huku na kule kuhakikisha kama hakuna aliyewahi kuona hilo tukio, na hakukuwa na
watu sehemu hiyo, watu walikuwa wamekaa kwa nje,....na ukiwa kwa nje huwezi
kuona huku ndani.
Hapo sasa nikaona
hakuna amani na siku imesharibika, nikasimama na kuanza kutafakari la kufanya.
‘Huyu mama
kanipa siku tatu,...na mzigo mwingine tuna
utarajia lini, oh,...ni baada ya wiki,...baada ya wiki, sasa nifanyeje..’nikajikuta nakuna kichwa, nikiwazia la kufanya.
‘Nitapatia
wapi pesa za kumnyamazisha huyo mama, japo kidogo....?’ nikawa najiuliza
Mara wazo la
haraka likanijia kichwani, nikachukua simu yangu ya mkononi kutaka kupiga simu, lakini nikakumbuka jambo, nikarudisha
hiyo simu mfukoni, ...nikatembea hadi mapokezi
‘Muhudumu,...umefanya
nini sasa, nilikuwambia sitaki mgeni, mbona unamleta yule mama bila taarifa...maana
yake nini....,mnakiuka masharti ya mteja au...?’ nikauliza kwa hasira
‘Huyu mama
kasema mliwasiliana naye, na huyu mama huwa ni mteja wetu mkubwa wa hapa,tunamuamini
sana, hawezi kutudanganya, na kasema upo hapa ukimsubiria, hatuwezi
kumdanganya...na alishakuona ukiingia mara kwa mara hapa, kwahiyo anafahamu
kuwa upo hapa...’akasema muhudumu
‘Ina maana anaingia
hapa hotelini mara kwa mara, kufuata nini...?’ nikauliza na yule muhudumu
akakaa kimia,
‘Mhh...ina
maana kila siku yupo hapa,na alishaniona nikiwa humu...haiwezekani...!? 'nikasema.
‘Ndio...alishakuona
na akasema wewe ni mfanyakazi wake, na kwa vile ni mteja wetu mkubwa tukamuamini..’akasema
‘Mhh,mbona
hamkuniambia....ooh, itabidi niondoke hapa haraka, siwaamini tena nyie watu...’akasema
‘Kwanini
tukuambie, kwani kuna tatizo...mimi najua ni mtu wako mnafahamiana...na kasema
wewe ni mfanyakazi wake...anajua wewe upo japa kwa kazi maalumu aliyokupa....umfanyie...’akasema
‘Kwani
nadaiwa shilingi ngapi, nipeni bili yangu...nadaiwa shilingi ngapi?’ profesa
akauliza
‘Kwanini
uondoke haraka hivyo...na akija tumuambieje...?’ akauliza huyo muhudumu
akionyesha uso wa mshangao
‘Nataka
sehemu nyingine, sehemu ambayo sitaki wageni, na nikisema sitaki wageni kweli
sitaki wageni, ...’akasema profesa
‘Sawa kama
ni hivyo, tutafanya hivyo...endelea kukaa, akija tutamwambia haupo....au
tusemeje bosi...’akasema muhudumu
‘Unajua
umenivurugia mipango yangu ya pesa,
nipeni bili yangu niwalipe niondoke zangu...hamna maana nyie kabisa...’profesa
akasema na muhudumu akaenda kuongea na bosi wao, haikupita muda akaleta bili na
profesa akalipa,na kuondoka zake.
********
‘Lakini
bwana mdogo, naona kama umeruka sehemu, unakimbilia kusema umepata pesa,
hujasema umezitoa wapi, ulizipata wapi,..ilikuwaje...?’ kaka mtu akauliza,
alipoona mdogo wake msimuliaji akijinyosha.
‘Nitakuelezea
tu bro..., wewe usijali, naongea kutegemea na kumbukumbu zinavyokwenda imebidi
nianzie hapo maana tukio la kuzipata pesa mwazoni lilikuwa rahisi lakini hatua
ya pili iliingia nyongo...’akasema huku akiashiria kwa mkono
‘Ilikuwaje
ikaingia nyongo...?’ kaka mtu akauliza
‘Unajua dili
hii haikutakiwa kuharakisha kihivyo, lakini tamaa zetu zilitufanya tufanye
hivyo, na matokea yake, ikaharibu mambo...’akasema
‘Kwa vipi
hebu anzia pale mlipokuwa mkipanga jinsi gani ya kufanya, mkakutana na yule
msichana wa bar....halafu ..., hatujaona
hilo tukio, jinsi mlivyofanya hadi mkaweza kumtoa huyo mtu pesa...’kaka mtu
akasema
‘Hilo
utalisikia tu huko mbele..., ngoja twende ninavyotaka mimi,...’akasema mdogo
mtu
‘Haya
endelea utakavyo....’kaka mtu akakubali kwa shingo upande.
‘Ni hivi bro,...kiukweli
tulipopata mkupuo wa kwanza,...lakini haikuwa pesa ndefu kama ilivyotarajiwa,....maheabu
yetu mwanzoni kutokana na mtaalamu yalikuwa makubwa,... lakini hatukufanikiwa.
Unajua kazi
hizi za dhuluma, hakuna kuaminiana kwani hata nilipompelekea mtaalamu, kiasi
hicho hatukuelewana, yeye akaendelea kudai ushuru wake, lakini ningepata wapi
hicho kiwango alichokuwa akidai, hakuniamini kabisa hadi pale alipohakiki kwa njia zake....
Basi
tulichopata ndicho tulichogawana, nikajikuta nina pesa ndogo tu,...nikaona cha
kwanza kwenda kumlipa huyo mama...nina penda sana pesa ikiingia mkononi,
ninakuwa mchungu kuitoa, lakini nikikmbuka ya huyo mama, sikuweza kuvumilia,
kwa haraka nikakimbilia kwake...
Nilifika kwa
huyo mama huku mabega yapo juu, kwa madaha,nikamuuliza
‘Hivi
unanidai shilingi ngapi...?’ nikamuuliza
‘Unataka
kusema nini, umekuja na pesa yangu au..?’ akauliza na kabla sijamjibu nikatoa bulungutu
la dola elifu ishirini,...nikawa nahesabu na huyo mama akawa ananiangalia kwa macho
yenye uchu
‘Nakuda-dai,....hesabu
vizuri....dola,laki-, eeh, ....aah, hebu vizuri....’akawa ananifuatilia
ninavyohesabu, na akishindwa kunitajia kiasi anachodai, kwa uchu wa zile
pesa,mpya mpya kutoka benki
‘Hizo ni za
mkupuo wa kwanza,...baada ya wiki mbili hivi nitakuletea mkupuo mwingine,
nataka tumalizane kabisa...kukuonyesha kuwa sina shida..ilikuwa ni namna ya
kukuweka sawa....siuanona mwenyewe...’akasema profesa
‘Umepatia
wapi hizi pesa, ohoo,umemuibia mtu mwingine nini eeh...sawa,mimi sijali,ninachotaka ni pesa
yangu,...’akasema akiwa haamini, akiwa kazishikilia hizo pesa mkononi
‘Mhh,
uliuliza nini, ...ok,..nilishakupa jumla ya deni langu sitaki kurudia rudia tena,
....madeni ya wengine mtajuana nao,ila....wakisema niwasaidie,nitawasaidia, na
tutakuja kwako...’akasema
‘Aaah,....wewe
angalia chako..ukiwasemea wengine...nitashindwa kukulipa deni lako, hao wengine
achana nao,....,unasikia, ...tutaongea mimi na wewe nikija kumalizana, au
sio....’nikamwambia, lakini kwa muda huo alikuwa akianza kuzihesabu zile pesa.
‘Unasema
...ndio tutaongea, ngoja kwanza nizihesabu hizi pesa, maana kwenye pesa hakuna
kuaminiana...’akasema akihesabu
‘Wewe
niamini tu, nikipata nyingine, ambazo natarajia hivi karibuni, nitakuja , ni
kama baada ya wiki moja hivi,...’nikasema nikianza kuondoka
‘Aaah, unanichanganya,
hebu subiri.....’akasema mimi sikutaka kumpa nafasi maana anaweza kunza kudai
nyingine na mimi nikakosa hata salio,
‘Nina
haraka, kuna miadi mingine mahali, wewe niamini tu, kuwa nitakuletea nyingine
kama hizo au zaidi ya hizo....’nikasema huku nikiharakisha kuondoka, na huyo
mama akabakia akihesabu pesa yake.
‘Unaona bro,
hayo ndio mambo ya mlungula...unapata pesa, lakini pesa zenyewe ni haramu
hazikai...’akasema mdogo mtu akishika kidevu akikumbukai hiyo enzi
*********
‘Ina maana
huyo mama mlishakubaliana kulipana hizo pesa...au ilikuwaje na ulikuwa unadaiwa
kiasi gani na huyo mama....?’ akauliza kaka mtu
‘Kiasi gani ...hahaha
alikuwa akinidai pesa nyingi, aliweka na riba juu kunikomoa....tatizo ndio hilo
, unapata pesa, na aliyekupa hizo pesa akikuzidi ujanja, inabidi umlipe, na
unamlipa pesa nyingi zaidi...sasa uone ubaya wa kazi kama hizo ulivyo, sasa nalipia pesa nilizowahi kuzila, napata
huku narejesha huku, nabakiwa sina kitu,..
‘Bro hayo ni
maisha ya shida, maana huyo mama alishanikaa kooni, na nilijua nisipofanya
hivyo, nitauhama huo mji, na sio kuuhama tu, huenda nikaishia jela,na hakuna
sehemu ninayoiogopa kama jela, asikuambie mtu jela sio mahali pa kwenda
‘Nilishawahi
kufungwa kabla..., lakini sikuwahi kukaa sana, nafungwa nakaa wiki, wiki mbili,
na muda mrefu ulikuwa mwezi mmoja, kabla ya kifungo hicho kikubwa nitakachokuja
kukusimulia ilivyokuwa...lakini bro, huo muda mfupi wenyewe..., nilikiona cha moto,mtu
kama mimi, profesa kulala jela, niliumia sana, lakini ndio maisha,...’akasema
‘Hebu kwanza
nikuulize,unaposema uliwahi kufungwa kabla,...ina maana maisha yako ya ulaya
ilikuwa hivyo,maisha ya wizi......ukamchukua mtoto kwa maisha hayo -hayo, ,...?’
akauliza kaka mtu kwa hasira.
‘Bro,nilishakuambia
kuwa mwanzoni, sikuwa na shida, kipindi wahisani wananipa pesa za mtoto,sikuwa
na tatizo, matatizo yalianza pale kijana alipoanza kazi...
‘Naa, ni
kweli kuwa niliwahi kufungwa kabla,hiyo ilikuwa kabla sijamchukua huyo mtoto, ilikuwa ni tatizo la madawa , kuna mteja nilima dawa,
akakosea matumzi, yakamuathiri huyo mteja, nilikaa wiki moja tu, akaja huyo mteja
kunitoa mwenyewe, ...akanisamehe, yakaisha....’akasema
‘Haya
endelea na simulizi la maisha yako ya dhuluma, kwani nina hamu ya kusikia
kuhusu kijana, ilikuwaje, ...’akasema kaka mtu
‘Bro...maisha
ya huko ni ujanja ujanja tu...’akasema
‘Ujanja gani
huo, dhuluma ni ujanja, hayo ni maisha ya kujitakia, na hayo yaliyokukuta, wala
usimlaumu mtu....unalipa kile ulichovuna, ....na bado hujafika mbele ya
muumba,...hujatubu, maana kutubu kwake, ni hao uliowadhulumu, wakusamehe, sasa
wapo wapi....’akasema kaka mtu.
‘Bro, we
acha tu,...nani arudi ulaya,...eti niende kuwatafuta ili nitubu, ..hahaha, sijui kama nitarudi hai....hao walichukua
pesa za mnada wa nyumba ni bahati yao...ila kiukweli, ulaya sio mahali pakukimbilia
hivi hivi tu, kama huna utaratibu maalumu, ukienda huko, utaumbuka....’akasema
‘Umeona
eeh.....’akasema kaka mtu
‘Nione mara
ngapi bro,..niulize mimi,maana nimeishi maisha yote, ya raha, ya shida, ya
jela...kila aina ya maisha huko nimepitia, nimewahi kuajiriwa,nikafanya kazi za
ofisini, nikaona ugumu wake....na kule hufanyi siku nzima, ni masaa, ukitoka
hapa unakwenda hapa, ukipata pesa inashia kwenye kodi,hakua ujanja wa kukwepa
kodi huko .....kwahiyo hakuna mtu wa kunidanganya...’akasema
‘Ehe
endelea.....’akasema kaka mtu.
‘Niendelee sio....’akasema
kinywa maji
******
‘Pesa tuliyopata
kwa huyo jamaa ilikuwa kiduchu tu..., na yule binti ilibidi aondoke,...sio tu
kutokana na vitisho, lakini hata muajiri wake, alishapata malalamiko
kabla,kumbe muajiri wake alikuwa akisiburia kisingizio, ili apate mwanya wa
kumfukuza kazi huyo binti.
‘Basi
tukamlipa pesa huyo binti, kiasi, sio zote,..na akafanyiwa mpango sehemu nyingine
ya kazi..., kutokana na urembo wake, haikuwa ni tatizo, akapatiwa sehemu
nyingine, ikawa ni ahueni yetu, lakini bado kulikuwa na tatizo, kwani bado
alikuwa akinidai, na akasema kaka yake ndiye atakuwa mkusanyaji wa hilo deni...ikawa
ni tatizo
‘Bro,nikajikuta
kwenye wakati mgumu,maana wote wanaonidai, walishaona dalili kuwa nina
pesa,kwahiyo wakawa wananiandama,ndio maana nikatafuta sehemu ya kujificha,ili
nikionekana tu,niwe na cha kudanganyia....’akasema
‘Pesa
tuliyopata ikawa ndio hiyo, kinyume na tulivyotajia, kwani ilikuwa ni ndogo
sana...lakini jamaa alishaingia kwenye anga zetu, na alishaahidi kulipa
nyingine baada ya wiki moja
‘Kwanini
sasa,..... unajua bwana mdogo unachanganya mada...hujaenda
kimpangilio...’akauliza kaka mtu
‘Kulikuwa na
tatizo lilitokea...hasa kuanzia huko benki na likaja kumuhusisha mkewe...’akasema
‘Kwa vipi na
wewe ulisema huyo jamaa anaweza kutoa pesa nyingi tu bila matatizo...na bila
mkewe kujua,?’ akauliza kaka mtu
‘Kutokana na
mtaalamu ndivyo ilivyokuwa , lakini kumbe akaunti ya huyu jamaa ilikutwa ina
matatizo, benki walikuwa wanahitaji maelezo ambayo alikuwa hajakamilisha, na
barua kutoka benki, ikaja na aliyeipokea akawa ni mkewe,hilo ni la kwanza
Pili,
jingine kubwa likatokea,ambalo liliharibu, na kusababisha sintofahamu, kati yao
wawili, yaani jamaa na mkewe, ikabidi akaunti hiyo sasa ijulikane rasm kwa
mkewe na mke, na azimio jingine likapitishwa...na sio hayo tu kuna kisanga kwa
familia hii, utakuja kuona ndio maana tulikuwa na uhakika wa kupata hizo
pesa....’akasema
‘Ilikuwaje...?’
akauliza kaka mtu
‘Bro, Subiri
nitakuhadithia, sehemu ijayo,ngoja nipumzike kidogo....
NB, UTAKUJA
KUONA SEHEMU HIYO, SEHEMU IJAYO, NGOJA TUWEKE MAMBO SAWA, SIUNAJUA MAMBO YA
SALIO NA MIMI BADO NIPO KWENYE MAWE
WAZO ZA LEO: Toba ya kweli kwa mkosaji, kwanza
ni kukiri kuwa kweli umekosea, ukakiri kuwa hutarudia tena, halafu ukamwendea
uliyemkosea ukamuomba msamaha, ukamrejeshea ulichomdhulumu,...wengi
wanadhulumu, mafisadi, wanatajirika, lakini hawajui kuwa chumo hilo ni deni,
hapa duniani na kesho ahera, kamwe asikudanganye mtu, kuwa kuna mtu wa kubeba
dhambi za wengine, ..! Kumbuka, kila mtu atauchukua mzigo wake mwenyewe!
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment