Nikiwa chumba alicholazwa mama, dakitari akafika akiwa na faili la
mama, akaniangalia usoni halafu akasema;
‘Vipimo vyote vya mama vipo tayari…’akasogea na kumkagua mama kwa
macho halafu akanielekea huku kashika faili
‘Kama ulivyoambiwa, mama yako ana uvimbe kichwani..na uvimbe huo
unahitajika kuondolewa, …kunahitajika upasuaji…’akatulia
‘Na kama unavyojua hapa nchini kwetu hatuna huduma kama hiyo, wataalamu
wa upasuaji wapo eeh, lakini, bado hatujafikia hatua ya kufanya upasuaji huo…’akatulia
`Ili mama yako apone anahitaji kupelekwa India huko ndipo upasuaji
huo unawezekana…kiujumla tatizo alilo nalo mama yako,likiachiwa litasababisha
matatizo mengine,…sio na kutisha ila ndio hali halisi, uvimbe huo
ukiachiwa,mama yakoataathirika ki-akili, hatakuwa sawa, atapooza viuongo…,
lakini wenzetu huko India wanaweza kulitatua hilo tatizo kwa upasuaji, na nimewasiliana
nao wanasema hilo linawezekana….’ Akasema
Tuendelee na kisa chetu
***********
‘Oh docta kumbe mama anaweza kupona na kumbe tatizo lake linawezekana kutibiwa, …Sasa docta
si nyie basi ndio mnaweza kufanikisha hiyo safari ya mama ili akafanyiwe huo upasuaji
au,…’nikasema nikionyesha furaha, na docta akaniangalia akafanya kubenua mdomo kama anatabasamu, akasema
‘Mhh, …kufanikisha ..mmmh hapana sisi kazi yetu tumemaliza…’akasema
docta sasa akiendelea kulikagua lile faili (kabrasha)
‘Lakini mama yangu anahitajika kwenda India…si ndio na huko atafanyiwa upasuaji, na nyie ndio mnaojua taratibu zote au sio...’nikasema nikimuangalai
docta, na docta akanitupia jicho , halafu kwa haraka akaendelea kulikagua lile
faili.
‘Ndio hivyo,..mama yako anahitajika kwenda India, na safari hiyo ni gharama ,...'akasema
'Si ndio docta mtu kama mimi nitawezaje,....najua serikali, itasaidia au sio docta...?' nikauliza na docta akatabasamu akaniangalia na kusema;
'Mimi, kama docta nimekamilisha kazi yangu, kazi iliyobakia ni wewe kutafuta uwezekano wa yeye
kufika huko…'akasema
'Ina maana ni mimi natakiwa kufanya kazi hiyo,...docta mimi, nitawezaje ....mhh?' akawa kanivunja nguvu.
'Ndugu, nikuambie ukweli, kuna wagonjwa kama mama yako wengi..na matatizo kama hayo na mengine na wanahitajika kwenda huko huko,...wanasubiria ruzuku
ya serikali, lakini lini, siunajua tena, serikali kama serikali haina pesa, fungu la namna hiyo ni dogo, sana sana wanategemea ufadhili,…'akasema
'Si ndio hapo, wao watatafuta wafadhili , mimi nitawapatia wapo hao watu...'nikasema
'Unajua kwanini nimekuambia ... tatizo la mama yako linahitajia uharaka..ndio maana
nikakuambia wewe hivyo, ili uweze kufanya juhudu za ziada, vinginevyo haya,
subiria hiyo ruzuku ya serikali,..sasa sijui lini….’akasema docta
Yalikuwa maneno ya dakitari ambayo niliyaona kama sindano ndani ya
moyo wangu. Nikajiuliza kwanini hii mitihani yote iniandame mimi, nilijiuliza
mara mbili tatu kichwani,
Hivi huyu dakitari kasema hivi kwasababu anajua kuwa mama hatapona
au kasema hivi kwa vile anajua kuwa sina uwezo huo na kwahiyo mama ataishia
kufa tu bila msaada wowote.
Nikamwangalia yule dakitari huku machozi
yakinilengalenga, na huyo dakitari akanitizama usoni halafu akatizama lile
faili aliloshika, halafu akamwangalia mama pale kitandani alipolala, na aliponiona amchozi yakilenga lenga machoni akaniuliza
‘Kwani wewe huna jamaa mkaambizana mkachangishana, kwasababu kwakweli
upasuaji kama huo hapa nchini hakuna, na huo upasuaji unahitaji umakini sana,
mimi nimemchunguza mama yako kwa makini na ninauhakika kama atakwenda India
atapona kabisa,..’akasema
‘Kwahiyo ninachokushauri wewe nenda katafutaneni wanandugu..mchangangishane..., au njia nyingine, tafuteni wafadhili,
ili ipatikane hiyo pesa, kwa haraka zaidi, `the
sooner the better’, umenielewa lakini…’ akatikisa kichwa, na kuangalia saa
yake, hii iliashiria kuwa nampotezea muda wake, kwani dakitari kama yeye ana
wagonjwa wengi, ana hosptalini nyingi za kwenda kuwahudumia wagonjwa, na
pengine, wagonjwa ambao wana uwezo wao!
‘Sawa dakitari kuhusu hiyo safari nimekuelewa,...tatizo ni hizo gharama... na sijui niseme nini, ina maana kama
hazikupatikana hizo pesa, kwa ajili ya gharama za usafiri, eeh na matibabu…,
hakuna njia nyingine ya kumtibu mama yangu? nikamuuliza na docta akaangalia saa yake
'Njia sahihi ni upasuaji,...nimeshakuelezea 'akasema
'Sasa docta utanisaidiaje, unaniona nilivyo, hali kama hii,..docta yaani mimi sina kazi kabisa..., sina ndugu, sina
pesa, na sina uhai....nipo kama mfu….oh,..nakuomba docta mnionee huruma, nisaidieni....’nikafikia hadi kupiga magoti
Docta akaniangalia na kutiskia kichwa, akageuka na kuanza
kuondoka;
‘Sasa docta,…utanisaidiaje….maana ndio nitajitahidi kuombaomba,
lakini nakuomba na wewe kama una njia za kunisaidia unisaidie tu, mama yangu
akifa na mimi ni heri nife tu…’ nikajikuta nalia kama mtoto mdogo. Niliposema
kauli hiyo dakitari akasimama na kunigeukia akasema;
‘Sikiliza ndugu kulia hakusaidii, …njia zipo nyingi za kufanya kaam nilivyokuambia,ni kweli tatizo kama hili ni gharama, mtu mwenyewe ni shidaah...sasa kama huna ndugu, huna uwezo,…nakushauri nenda
kwenye redio au runinga tangaza kuwa una tatizo kama hili, linahitaji msaada wa haraka,
kuna watu wakisikia hivyo watatoa misaada, wapo watu wanasaidia…’akasema na kuniangalia kwa
makini sijui kwanini alikuwa akiniangalia hivyo
'Docta nimeshakuelezea hali halisi.....mimi ni masikini, ukijua tulipotokea huwezi amini, mimi na mama tulikuwa omba omba...basi nikapata mfadhili nikasoma nikapata kazi, ..baadaye nikapunguzwa kazi, na hapo matatizo yakaanza kujipanga, hili baada ya jingine, unavyoniona hapa, ......watu wanahisi nina ukimwi..lakini hii ni shidaa tu docta...'nikasema
'Uliwahi kupima afya yako hilo ni muhimu sana..'akaniambia
'Ndio nimeshapeleka vipimo, na leo natakiwa kwenda kuchukua majibu ya vipimo...lakini docta mimi siumwi...'nikasema
'Anyway, tuache hayo ya kwako, muhimu kwasasa ni mama,...fanya kama nilivyokuambia..'akasema
'Lakini docta sina jinsi..naomba msaada wako....nipo chini ya miguu yako, nisaidie, nakuomba sana docta..'nikawa sasa nalia kiukweli.
‘Nikuambie kitu, usijiweke katika hali ya unyonge kihivyo...., matatizo hayo yapo, watu wanaipitia kwenye matatizo mbali mbali, ...lakini matatizo yasikufanye uwe mtumwa wake...tatizo likitokea muhimu ni kutafuata njia ya kulitatua,....sio kukata tamaaa, jaribu kila njia..'akatulia
'Sasa docta nyia ndio wenye nafasi ya kunisaidia..'nikasema
'Sikiliza, matatizo hayaepukiki, sasa hivi tatizo lipo mezani kwako,..unalo… huwezi ukabakia kulia
tu...ujue matatizo ndio changamoto ya kukuwezesha wewe kufanya jambo…ukilia itasaidia
nini, na tafadhali usinipigie magoti, maana mimi sio mtatuzi wa hilo tatizo, nakuomba uinuke..’akasema akinishika mkono niinuke lakini sikuwa na hata nguvu ya kufanya hivyo nikabakia vile vile nimepiga magoti…na yeye akasema;.
‘Wapo watu wanaweza kukusaidia , tatizo watajuaje kama wewe unahitajia msaada kama huo, cha muhimi ni wewe kwenda kulitangaza hilo tatizo lako, ili wasikie….mimi
kazi yangu nikukusaidia kutafuta tatizo na nimejitahidi sana kwa kutumia vifaa
vyangu binafsi, gharama zangu binafsi, ...'akawa anafungua fungua lile faili.
'Nimefanya zaidi ya uwezo....kama ungelikuja kwenye hospitali yangu
gharama ingelikuwa kubwa sana, lakini kwa vile nimeamua kumsaidia mama, ndio maana
nimejitolea kutoa hadi vifaa vyangu binafsi kwa vipimo toka hospitali yangu
mwenyewe ambavyo ni gharama sana,…je ulitaka nikusaidiaje…au unataka nikuambai kile kitu na gharama zake ili ujue nimekusaidiaje...’akasema
'Nashukuru sana docta kwa msaada wako lakini bado nakuhitajia..'nikasema
‘Nimeshakusaidia vya kutosha,…zaidi ya hapo mimi sina uwezo
huo, huko sio sehemu yangu tena kuna wahusika wengine…natumai umenielewa…samahani nawahi wagonjwa wengine….’ akasema yule
dakitari nakuomba tafadhali kuwa anawahi sehemu nyingine. Sikuwa na jinsi bali
niliinuka pale nilipokuwa nimepiga magoti, huku nikipepesuka nikiwa kama bua,
nilitembea hadi pale alipolala mama, nikamshika mkono.
‘Mama nifanyeje mwanao, hapa nilipo sina kazi, sina ndugu wa
kutegemea…, sina pesa …mama sasa, oh, nifanyeje, mama ukifa na mimi
nitakufuatia nyuma, maana sitakuwa na raha maisha yangu yote, nitakosa raha
kwasababu nimeshindwa kuokoa maisha yako…mama nifanyeje mwanao, ningelikuwa na
nguvu, ningelikwenda hata kuiba,…ningefanya dhambi hiyo….lakini nikaibe wapi…’nikajikuta
machozi yakinitoka kama maji
‘Mama hapa nilipo sina nguvu,…sijala, siku ya ngapi leo naishia
kula kitumbua…na maji… hata kutembea natembea kwa shida, watu wanadhani nina
ukimwi kwa jinsi nilivyokonda,..lakini sio ukimwi, ni shida, njaa,…na yote haya
ilikuwa ni kuhakikisha wewe na family yangu mnaishi vyema, lakini imekuwa
bahati mbaya. …’nikatulia kidogo nikiamuangalia mama alivyolala,
hatikisiki..kinachoonyesha yupo hai ni yale mashie tu.
‘Mama, mke wangu ndio huyo kanitoroka na mbaya zaidi kaondoka na mwanangu…ni
sawa uzalendo umemshinda, ni sawa, huenda mtoto angelikuwepo ingekuwa ni tatizo
jingine…lakini najua kabisa mama, kama ningelikuwa mimi naumwa kama wewe hivyo,
katu usingeliweza kuniacha, kama ningelikuwa mgonjwa kama wewe najua wewe ungelikuwa pembeni mwangu ukiniuguza,
maana wewe ni mama yangu, mama nakupenda, lakini nifanyeje…’nikatulia nikivuta
kwikwi.
‘Mama watu wanakimbia wakidhania, nina ukimwi…mama jana nilikwenda
kupimwa, na leo nikitoka hapa nakwenda kuchukua majibu kama kweli ninao basi mama
nakuaga kabisakuwa hatutaonana tena, na kama sina huo ugonjwa nitahakikisha
kuwa nazipata hizo pesa ukatibiwe,…. ikibidi nitakwenda kuiba….’ Nikamshika mama
mkono na kuubusu mkono wake huku machozi yakimdondokea mkononi.
Nilitoka mle hospitali nikiwa kama nipo gizani, macho yalikuwa
yamejaa utando wa giza na machozi, akili ilikuwa haifanyi kazi tena, mwili
ulikuwa kama sio wangu.
Nilitembea huku na yumbayumba, na kuelekea barabarani, nafikiri
watu walikuwa wakinishangaa, nilishazoea kushangawa na watu, nilijonea sawa
tu.Nilikuwa hata sijui naenda wapi, kwani wakati huo akili zangu zilikuwa
zikiwalaani wale mgambo waliomkanyaga mama kichwani, niliwaona kama wao ndio
wamemsababishia yote hayo kwa mama yangu . Moyoni nijaa chuki, na nilidhamiria
kama nikiwakuta hawo mgambo tena nitafanya la kufanya nikafie gerezani.
***********
Nikiwa natembea kutoka pale
hospitalini, mara ghafla nikasikia magari yakifunga breki miguuni mwangu,
nikabakia kubabaika, nisijue nifanyeje, kumbe nipo katikati ya barabara bila
kujijua…, na hali kama hii ikanikumbusha siku ile nilipodondoka kwenye lori
ambalo nilipanga kutoroka nalo siku ile nilipotoroka shule ya watoto watukutu.
Kumbukumbu hizo zilinijia muda huo nipo kati kati ya barabara, sijui
kwanini kumbukumbu hizo zilijia muda ule, nikawa kama nipo kwenye ndoto,
niliwazie lile tukio la siku ile, jinsi nilivyokuwa nimelala kwenye kile
kisehemu nyuma ya lile lori, na jinsi nilivyopitiwa na usingizi …ndani ya
usingizi ule niliota ndoto mbaya…
Ndoto ile ndio iliyonifanya nizindukane na kusahau kuwa nipo
kwenye shemu ambayo ni hatari…unajua ilikuwa ni sehemu ndogo sana, na kwa vile
nilikuwa bado mtoto, niliweza kujibanza mle, bila wasiwasi.
Jamani, ….niwakumbushe kidogo siku ile…kuna tukio muhimu
sikuwahadithia….
Nilijikuta namedondoka chini ya barabara ya lami, na kwa vile gari
lile lilikuwa kwemye mwendo, nilidondoka na kuserereka, na ukumbuke nyuma,
yalikuwepo magari yanakuja kwa kasi na mojawapo lilikuwa `land cruiser’, ambayo
ilikuwa karibu sana na lori letu.
Kwahiyo nilipodondoka, …yule dereva wa `landcuiser’ akawa kashikwa
na mshituko kwani hakutegeema kitu kama hicho, alijaribu kufunga breki, na
kulipindisha gari pembeni mwa barabara, na kufanya vile akawa kanigonga kidogo
na kunusumia nje ya barabara huko huko anapotaka kulipindishia gari lake,
kwahiyo nikawa nimetupwa kama mpira.
Sikujua nini kiliendelea baadaye zaidi ya maumivu kwenye kichwa na
begani, yalikuwa hayakadiriki na giza likatanda usoni na kilichofuata baadaye
ni kupoteza fahamu. Nilipozindukana nilijikuta nimevalishwa mavitambaa mwili
mzima, na shingoni kuna limhogo, mkononi hadi begani nimevalishwa POP, pia.
Nilikuwa kama sanamu fulani lilofungwa mavitambaa kila mahali. Nikafunua macho
kwa shida na mbele yangu nilimuona kasimama mama mmoja.
‘Docta naona kama vile mgonjwa kafungua macho, …ahsante sana
mungu, nilijua tumeua…docta tafadhali mwangalie kama anahitaji msaada wowote..’
akasema yule mama.
Docta alinijia na kunitizama , halafu akaangalia mashine yake ya
mapigo ya moyo, halafu akafunua mboni zangu za macho, akamgeukia yule mama, na
kusema, kuwa mgonjwa bado hajawa vyema, inahitajika muda kidogo kusema lolote.
Nikatamani kuwambia kuwa mimi nimepona, wasiwe na wasiwasi , niliona heri
nipone haraka niondoke mahali hapo, wasije wale mgambo wakaja kunikamata na
kunirudisha huko kituo cha kulelea watoto.
Baadaye nikashikwa na usingizi na ndani ya usingizi huo nilimuota
mama yangu akinikanda kwa maji ya moto mwili mzima, na kunibembeleza kuwa
nitapona, ilikuwa ndoto iliyoanzia kwa mimi kudondoka kwenye mti na kutegeuka
mkono, sasa mama akawa ananikanda maji ya moto, na kuniambia nisitoe kitambaa
alichonifunga, kwani nikikitoa mkono hautopana, …’ mara nikashituka toka
usingizini na kujikuta nimeshikiliwa na docta…alikuwa akinibadilisha vile
vitambaa vya vidonda.
‘Docta nipo wapi mama yangu yupo wapi, namataka mama yangu
haraka..’ nikawa napiga ukulele na kutaka kuinuka, lakini yule docta
akanishikilia na kuniambia nitulie kwani nitajitonyesha, nilale hivyohivyo….,
na wakati nahangaika na yule docta mara akaja mama mmoja, nilikumbuka nilimuona
kabla , alikuwa kaongozana na mwanaume, walikuwa wamebeba matunda na vitu
vingine, nilitamani kuwaambia nina njaa lakini mdomo ukawa mzito.
‘Docta vipi mgonjwa wetu anaendeleaje…? Akasema yule mwanamke.
Nilijiuliza kwanini wanasema `mgonjwa wetu’
‘Hali yake inatia matumaini, unajua kwasababu ni mtoto,
haitachukua muda mrefu …atapona haraka sana, sio kama mtu mzima…’ akasema
docta.
‘Unanipa matumaini sana docta, kwani tulikuwa na wasiwasi sana,
…na natumaini…, hakutakuwa na matatizo zaidi kwani askari wamaona kuwa sio kosa
letu, ni kosa la huyo mtoto, sijui alirukaje kwenye lile lori,…unajua hatukujua
kabisa katoka wapi, karuka toka juu ya lori au…hata hatuelewi, sisi tuliona mtu
huyu, yupo mbele yetu anaserereka, cha ajabu hata lile lori halikusimama
kabisa…’ akasema yule mwanaume.
Wale watu walipomaliza kuongea na dakitari waliondoka, na sikuweza
kuwajua ni watu gani.
Nilikaa pale hospitalini karibu wiki tatu halafu… nikaruhusiwa
nasiku naruhusiwa alikuja yule mwanamke na mume wake, wakanichukua hadi
nyumbani kwao na waliniambia kuwa nitaishi nao mpaka watakapokuja ndugu zangu.
Niliwaambia kuwa sina ndugu, kwani mama yangu nilisikia wakisema aliruka kwenye
gari, na haijulikani kuwa kafa au yupo hai.
Na nyie ndio nawaona kama ndugu zangu , maana msaada mlioutoa
hakuna mtu angadiriki kufanya hivyo..’nikasema
‘Basi usijali wewe tunatishi na wewe hapa na jisikia kama upo
nyumbani..’wakaniambia.
Basi ndio ikawa ahueni yangu maana kweli niliishi nao, wakanipa
kila huduma ninayostahili, utafikiri mimi ni mtoto wao wakanisomesha,
nikamaliza darasa la saba, na nilifaulu kwenda sekondari hadi kidato cha nne,…hapo
nikawa mzembe, kujiamini kuwa nina familia ya kifahari, kila kitu napata,
matokeao yake nikafeli, sikupata matokea mazuri ya kuendelea mbele…
Maisha ni kupanda na kushuka, hutaamini hawa wafadhili wangu kumbe
walikuwa wamejenga na miradi yao yote hiyo ilikuwa ya mikopo, sijui ikatokea
nini, na muda huo ndio namaliza kidato cha nne,
Nakumbuka siku nimetoka kufanya mitihani, nikiwa sijui hili wala
lile narudi nyumbani nakuta watu wanabeba vitu, na jamaa zangu wamesimama
pembeni, nikawasogelea , na kuwauliza kulikoni.
‘Wewe tulia tu, maisha ni kamari leo tumekosa kesho tutapata..’akasema
baba yule huku akionyesha hana wasiwasi tofauti na mkewe.
Kumbe kipindi hicho mambo yao yalikuwa sio mazuri, lakini hawakutaka
kuniambia, biashara zao zilikuwa haziendi, na walikuwa na tabia ya kucheza
kamari kwenye makasino, huko ndipo kulipowaweka pabaya zaidi, wakawa wamefirisika, lakini walijitahidi
kunipa kila kinachowezekana na sikujua kabisa hadi siku hiyo… kiukweli kumbe walikuwa
na hali mbaya ya uchumi. Na kumbe walizembea kulipa madeni waliokopa benki na
kwa watu mbali mbali, na kwahiyo nyumba yao ya kifahari, magari yao waliokuwa
nayo yakapigwa mnada.Wakabakia hawana kitu..
‘Kwahiyo sisi ndio hivyo, tunajaribu kuangalia njia nyingine ya
maisha, sasa..hatuna uwezo wa kukusaidia zaidi, kama unavyoona…’wakasema
‘Oh, sikujua, ….’nikasema
‘Lakini usiogope yote maisha,..’wakasema
‘Basi kwa vile hali halisi inaonekana…na mimi nimeshakuwa mkubwa
niacheni mimi nikahangaike kivyangu..’nikasema
‘Hapana wewe bado hujaweza kuishi peke yako, kaa na sisi,..kuna
sehemu tutajisitiri hadi tujua la kufanya,chochote kitakachowezekana tutasaidiana..’wakasema
‘Hapana ndugu zangu,...wazazi wangu, mimi naona nikizidi kukaa na nyie nitazidi kuwapa mzigo..mimi niacheni nikahangaike, ..., nitajua cha kufanya….’
nilikataa na kuingia mitaani kutafuta maisha.
WAZO LA LEO: Matatizo kwa binadamu ni changamoto ya
kusonga mbele, matatizo hukomaza akili na kuweza kufikiria zaidi.
Tusiyachukulia matatizo kama bahati mbaya, kuwa labda nimelogwa , labda nina
bahati mbaya, tuyachukulia matatizo kama ngazi ya kutupeleka juu, kutufikisha
sehemu nyingine ya zaidi, ambayo ni kufanikiwa kutatua lile tatizo na ni maendeleo.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment