‘Kwahiyo mama ikawaje…?’ nikamuuliza nilipoona anataka kuhadithia
jambo jingine
‘Mnataka tuendelee na hali ya mama, ok…..’akasema na kutulia
vyema.
‘Siku ile marafiki zangu wakanisaidia hadi mama tukafika
hospitalini. Mama alikuwa vile vile, na hata wakati tunamteremsha na kumbemba
hadi ndani kwa dakitari, sote tulijua
ndio mwisho wa kumuona mama tena. Lakini cha jabu docta alipomchunguza akasema
mama kapoteza fahamu tu,.
‘Usiwe na wasiwasi mama yako yupo hai, sijui kwanini
unalia…’akaniambia docta aliponiona nikilia.
‘Mhh, …’nikaguna tu huku nikimuomba mungu mama yangu sije
akafariki na kuniacha kwenye madeni ya fadhila,…nsjua hakuna anayeweza kulipa
fadhila za mama, lakini angalau nipate muda wa kukaa na mama kidogo nimuonyeshe
kuwa mimi ni mtoto wake.
Mama akalazwa hapo hospitalini wakimuwekea dripu za maji, mimi nikiwa
nimekata tama kabisa, baadaye dakitari akanijia na kuniambia, mama yangu
kapoteza fahamu tu, wao wanajaribu kuona kwanini fahamu za mama zimepotea, na
wanajaribu kumzindua kwa vifaa vyao lakini hajazindukana bado…je ni kitu gani
kilitokea hadi mama yako akapoteza fahamu…?’akaniuliza
‘Hilo la kupoteza fahamu sijui maana imetokea baadaye sana,..ila
alidondoka akagonga kichwa ..nikampa dawa ya maumivu, na akaendelea vyema tu,
tukawa tunaongea kwa muda mrafu sana, baadaye ndio hivyo akapoteza fahamu….’nikasema
‘Pamoja na hilo yaonekana mama yako ana matatizo kichwani, …hujui
lolote kuhusu historia yake ya nyuma,..labda ana matatizo ya kupoteza fahamu
mara kwa mara au ana matatizo mengine…?’akaniuliza
‘Kiukweli mimi sijui sana ila alinihadithia kuwa huko nyuma mimi
nikiwa mchanga alipoteza kumbukumbu, akawa hakumbuki chochote, na hilo tatizo
lilikuja kumalizika....’nikasema
‘Basi ngoja tumlaze hapa tuone tatizo nini, vipimo vingine
bado….’akasema huyo docta, na kuniambia kuwa mimi naweza kuondoka na nije kesho
yake, lakini mimi sikuondoka, nikabakia hapo hadi usiku, mama hakuzindukana kabisa hata baada ya juhudi
mbalimbali walizomfanyia madakitari. Mama
alibakia hivyo hivyo kwa siku mbili na ikaonekana hawezi kuzindukana tena,
lakini wakimpima bado yupo hai…
Siku ya pili nilikawia sana kurudi nyumbani, kwani ilibidi
nihangaike na madakitari kuhakikisha kuwa wanampima mama na kuona tatizo hasa
ni nini, na hatimaye nikaahidiwa kuwa yupo dakitari bingwa atakuja kumuona, na
huenda ikajulikana tatizo lake ni nini...
Mimi moyoni nikahisi kuwa huenda wanapoteza muda tu, kwa vile sina
kitu cha kuwapa, kama ningekuwa na kitu nina uhakika mama angelikuwa keshapimwa
na kugundulika tatizo lake…. Na fikira hizi ziliniandama kichwani na kujiona
sina maana. Sina maana maana mimi nimeshindwa kumsaidia mtu aliyenisaidia kwa
hali na mali….niliumia sana moyo wangu.
Nilijaribu kutafuta vibarua ili nipate chochote, lakini kutokana
na hali yangu ya kimwili, kila ofisi niliyofika, waliniangalia mara mbili na
kusema `wewe nenda tutakuita baadaye kama kuna nafasi..’ Niligundua kabisa kuwa
hawo waajiri walishanihisi vibaya. Ni kipindi kile mtu ukikonda sana wanajua
unao…
Siki zilivyozidi kwenda hali yangu ilizidi kuwa mbaya sana, kwani
udhaifu wa mwili ulikuwa umenijia kwa kasi, mwenyewe nilijiona kama buwa, mwili
hauna nguvu, na hata akili ikawa haifanyi kazi vizuri, kwani nilijikuta naongea
peke yangu bila kujijua kama mtu aliyechanganyikiwa. Na watu walishaanza
kuninyanyapaa wakijua mimi ninao. Ilifikia muda nikienda kuongea na watu kwenye
kundi, ili kupoteza muda, watu wanaanza kutafuta mwanya wa kuondoka eneo hilo
na baadaye najikuta nimebakia peke yangu.
‘Rafiki yangu nakushauri kitu kimoja, ulishawahi kupima afya yako,
kwani nakuona hali yako sio njema, kwani unasumbuliwa na nini hasa?’ aliniuliza
yule rafiki jirani yangu aliyenisaidia kumpeleka mama hospitalini.
Siku hiyo rafiki yangu alikuja hapo ninapokaa, ili kunijulia hali
na kunipa pole ya kuibiwa na kutaka kujua hali ya mama, japokuwa walikuwa
wakijitahidi kwenda hospitalini kumuangalia mama, lakini siku nyingine
wanashindwa, wanakuja kuniuliza mimi.
Hutaamini kuwa, siku ile niliyokawia kurudi nyumbani, nikiwa
hoapistlini kumbe huku nyuma, watu tena walikuja wakakusanya kila kitu
kilichokuwepo mle ndani. Na nilipodadisi nikagundua kuwa alikuwa ni mke wangu.
‘Sasa kwanini huwaambii polisi kuhusu kuibiwa , maana mtu
unayemshuku ni mke wako, na ni kweli alionekana, … watu walimuona akija na
gari, hata mke wangu kasema alimuona lakini wakati huo ndio anatoka,..na
alipokuja kutaka kujua, mke wako akamwambia mke wangu kuwa hayamuhusu, yeye
anajua ni nini anachokifanya, basi mke wangu hakutaka makubwa akanipigia simu,
nilimwambia amuambie mjumbe, ..mjumbe hakuwepo…na muda huo mke wako
alishaondoka na gari na vitu…’akatulia
‘Nilikupigia simu na ukawa haupatikani..basi tukashindwa la
kufanya ,na mke wangu hakuweza kumzuia, …’akatulia
‘Unaju mke wangu yeye alijua labda ni makubaliano yenu, au
mumepanga muhame…’akaniambia rafiki yangu.
‘We acha tu…hii safari ya pili, alikuja kumalizia vitu
vilivyokuwepo,hata sijui kavihamishia wapi,…wala sihangaiki kwasasa, na siwezi
kwenda polisi..’nikasema
`Safari hiyo ya mwisho alihakikisha anachukua kila kitu, hata
kitanda hakuna hata sijui nitalala wapi’…nikasema
‘Hata kitanda hakukuachia, sasa utalala wapi…?’ akaniulizia rafiki
yangu, baada ya kuniuliza swali la kwanza kuwa naumwa nini, nikawa kimya ..
‘Mimi nakushauri nenda polisi,….’akasema
‘Hapana, hata polisi hawataiamini..’nikasema
‘Kwanini wasikuamini na hali inaonyesha, au unajua kwanini mke
wako kafanya hivyo, labda katafuta sehemu nyingine ili muende mkaishi naye
huko…?’ akauliza
‘Hata sijui, mimi hapa
najiona kama mfu tu, naona kama walimwengu wameamua kunitenga, yaani kuacha
wewe rafiki yangu, sijui kama kuna mtu atakuwa karibu na mimi tena, watu
wananikimbia watu wanaogopa hata kunipa mkono kusalimiana na mimi…’nikasema
‘Mhh, lakini ni muhimu ukapime, unajua siku hizi wapo wataalamu
wakijua una tatizo wanajua jinsi gani ya kukupa ushauri nasaha…utajiona huna
tatizo kabisa…’akasema
‘Mhh,….mimi hapa mawazo yangu ni kwa mama, sijui kama atapona,
yeye ndiye mtu wangu wa karibu anayefahamu tatizo langu,…sijui ..sijui rafiki
yangu, nahisi kama siku zangu nazo zinahesabika..mama akifa na mimi namuomba
mungu aichukue roho yangu….sizani kama nitaishi tena..’ nilijikuta nasema hayo
maneno ambayo yalimfanya rafiki yangu aniangalie kwa wasiwasi.
‘Nakushauri tena rafiki yangu, nenda ukapime ujue hali yako…mimi
nahisi una tatizo la kiafya, na huwezi ukalijua mpaka ukipima, hata kama ni huo
ugonjwa wanaokudhania watu, si ndio itakuwa bora, kwani ukijijua unajipanga
vyema, na hata hivyo nasikia kuna dawa za kurefusha maisha…’akasema
‘Mimi sina huo ugonjwa, uhakika huo ninao…labda kama kuna tatizo
jingine..’nikasema na rafiki yangu aakniangalia kwa mashaka.
‘Lakini utajuaje kama hujapima..kwani kuna tatizo gani kupima,
wanapima bure tu..nenda hospitali ya Lugalo nitakuunganishia kwa jamaa yangu
mmoja askari…’akaniambia huku akiniangalia kwa mashaka. Nilishamshuku kuwa hata
yeye keshaingiwa na wasiwasi na mimi, sikumlaumu sana, kwani yeyote ambaye angeliniona
kwa muda huo angelijua lazima nina tatizo, ninao….
‘Nitakwenda kupima na majibu yangu nitayabandika usoni , ili kila
mtu ajue kuwa sina huo ugonjwa kama watu wanavyonidhania mimi, labda…siwezi jua
, kama huo ugonjwa unaweza kuingia akilini na kunidhoofisha kia-akili ,
ukapunguza nguvu za kufikiri …..’nikamwambia huyo rafiki yangu.
‘Unajua rafiki yangu haya yote yametokana na msongo wa mawazo,
matatizo mengi yaliyofulululiza…imefikia hatua nikashindwa hata kufikiri jinsi
ya kuishi, jinsi ya kuondokana na umasikini nilionao,…labda huo ugonjwa
umepitia huko na kama ni hivyo basi ninao, …’nikasema nay eye akaniangalia tu
‘Kama ni huo ugonjwa, … wa kupunguza kinga za mwili , na
unapatikana kwa zinaa, au ….labda niupate kwa mke wangu, na nakiri kuwa tangu
tuanze matatizo na mke wangu tuna zaidi ya mwaka hatujuani,…sasa , ok, nitapima
tu rafiki yangu kama ulivyonishauri…ili niwathibitishie wanajamii, waache
kuninyanyapaa’ nikasema nikiwa nimedhamiria kufanya hivyo.
Alipofika hapo akakaa kimia kwa muda kama anawaza jambo halafu
akaniangalia na kusema;
‘Unakumbuka siku ile tulipokutana kule Lugalo Hospitali…’
akaniuliza huku akitabasamu, nikatikisa kichwa kumkubalia kuwa kweli nakumbuka.
‘Basi nilikwenda baada ya ushauri huo wa rafiki yangu, nilipofika
hospitalini nikakutana na dakitari nikamwelezea nini dhumuni langu, na yeye
akanipa ushauri nasaha, akijua kuwa kweli nimeathirika, Nikamsikiliza , huku
akilini nikimuomba Mungu, kuwa kama kweli ninao namuomba sana anipe ujasiri wa
kuishi ili niweze kuhangaika ili mwisho wa siku nipate hela za kumtibia mama
yangu.
Nikajikuta natoa machozi, mbele ya dakitari, hakujua kwa nini
natoa hayo machozi, yeye nahisi alihisi kuwa huenda nawaza kuhusu huo ugonjwa,
akasema
‘Nakuomba usijali kwasababu kuumwa ni kawaida tu, na ukimwi ni
sawa na magonjwa mengine, na dawa yake kubwa ni kufuata masharti, kwahiyo
usihofu na usianze kujitwika mzigo kabla
haujatua kichwani…’ alisema mengi , lakini kiakili nilikuwa sipo hapo
kabisa.
Yaani hata ungeniuliza mengi aliyooongea hapo, nisingeliweza
kukuambia, maana sikujua kaongea nini, akili ilikuwa inawaza jinsi gani ya
kupata pesa za kumuuguza mama yangu tu..Hata hivyo kama akitokea dakitari ,
nitamlipa nini ….
Basi siku ile nilipofika kwa dakitari, damu imeshatolewa, sikujua
muda ulivyokwenda,….nilisikia tu nesi akisema
‘Twende huku ukachukuliwe damu…’ akasema yule dakiatri, na
tulitoka naye hadi chumba cha maabara, wakaanza kutafuta mishipa ya damu,
ilikuwa taabu, maana mwili umekunjamana utafaikiri mzee wa miaka nenda
rudi..hatimaye wakchukua hiyo damu, nikaambiwa nirudi kesho yake kuchukua
majibu. Niliwaomba kama inawezekana niyapate muda ule ule, lakini wakasema
haiwezekani muda ulikuwa umekwisha na kulikuwa na matatizo ya umeme. Basi
nikatoka kuelekea nyumbani.
Nilifika kwangu , nikatandika mkeka ambao ndio peke yake
alioniachia mke wangu, hakuna cha nguo wala kipande cha shuka, nikanyosha ule
mkeka na wakati nauweka vizuri nikaona barua ndefu kidogo, nilipoiangalia vyema
nikagundua kuwa ni barua kutoka kwa mke wangu.
‘Uliyekuwa mume wangu, natumai hustahili
kubakia na chochote zaidi ya huu mkeka, kwani utakufaa wakati wa kwenda kuzikiwa, na najua kuwa wasamari
wema watakusaidia sanda yako. Nasema haya sio kwa kuwa nakuchukia kiasi hicho,
la khasha ila ni kwasababu ya kusimamia upande wa mama yako ambaye ndiye chanzo
cha hali mbaya tuliyo nayo. Utakubalije mtu aje akuangamize wewe na familia
yako, kama na wewe sio njama moja.
Nimeamua kuchukua kila kitu ili mupate
muda wa kuwanga usiku, na sizani kuwa mnastahili kulala, kwasabau usiku hamlali….
Mama yako kakulogezea ukimwi, angalia unavyokwisha,…mimi nimeshapima na
kuonekana nipo salama, kwani nilikuwa na wasiwasi kuwa huenda umeniambukiza na
mimi. Nakushauri uende ukapime, ili uhakikishe kuwa ninachokuambia ni sawa,
kuwa mama yako kakulogezea ukimwi..lakini humwi…wewe hulioni hilo,….
Nakutakia maisha mema ..ipo siku
utanikumbuka kwa haya ninayokuambia
Mimi niliyekuwa mke wako
*********
Niliichana-chana ile karatasi kwa hasira huku nikumkumbuka mama
yangu ambaye alijitolea maisha yake kwa ajili yangu, mama ambaye alinipenda
sana, eti leo ageuke kuwa mchawi wa kumloga mwanae, ….
Niliyawaza hayo maneno ya mke wangu kwenye barua, ….nilitamani
huyo mke wangu angelikuwa mbele yangu, ningelimfanya kile ambacho asingeliweza
kukisahau maishani. Nikiwa pale kwenye mkeka mbu wakinitafuta kumbukumbu za
maisha yangu na mama hasa tulipohamia sehemu nyingine baada ya kufukuzwa na
mgambo zikanijia…zilinijia kaam njozi…
Tulipokimbia siku ile kuwakimbia mgambo, tulihamia sehemu ya mbali
kabisa na pale ,kwani tulisikia kuwa mgambo wanatutafuta sana, wakisema
wanamtafuta mwanamke mmoja anayevaa kininja. Nikajua kuwa ni mama, lakini mama
hakuwa na wasiwasi akasema waacha waje wanikamate lakini mwanangu sitakutupa,
nitakulea hadi uwe dume, dume litakaloniletea wajukuu..basi akianza kuongea na
mimi tunacheka, na kusahau machungu ya dunia.
Maisha ya makazi mapya yalikuwa magumu sana, kwani tulikuwa hatuna
njia ya kupata kipato, hatuna mtaji wa kuanzia biashara, hatuna eneo la kulima
hata mchicha. Basi tukaona ni bora tugeuke kuwa ombaomba mitaani. Na hali ya
kuomba ilikuwa ngumu, tulikuwa tukinyanyaswa na hata kupigwa. Na wakati
mwingine unaomba unapata kitu kidogo, mwisho wa siku jamaa wenye nguvu zao
wanakuja kutuibia, na nilishamwambia mama asipigane nao, maana wanaweza kumuua,
na mimi nitabakia na nani, akakubaliana na mawazo yangu, akawa hapigani tena.
Siku moja tulihangaika kutwa nzima hatukupata chochote, mimi
nikawa na njaa sana, nikaanza kumlilia mama kuwa nisikia njaa, siwezi
kuvumilia, mama akanionea sana Huruma mwanae, akaniambia tuondoke pamoja ,
ilikuwa jionijioni, tukafika makazi ya watu. Ujue mara nyingi tunajificha nje
ya makazi wa watu kwasababu tunatafutwa na mgambo.
Basi tulifika kwenye nyumba, maeneo yanayojulikana kama uzunguni,
tukijua huenda hawa matajiri watatupa chochote hata makombo, kwani wao wanakula
na kusaza, mabaki wanayatupa majalalani, hawajui kuwa kuna ambao hayo mabaki
wanayatafuta lakini hawayapati.
Tulikwenda nyumba moja, akatokea mama mmoja wa Kihindi, au
kisomali au Kizungu, hakuwa na sura mbayo moja kwa moja ungesema ni taifa gani,
lakini ni Mtanzania, kwani anaongea Kiswahili vizuri, ila lafudhi yake utajua
sio Mtanzania asilia. Mama akamuomba atupe chochote, akasema basi subirini
niingie ndani nitawapa chochote.
Yule m-mama akaingia ndani , na alikawia kutoka nje, mama machale
yakamcheza, akaniambia;
‘Mwanangu hapa naona hakuna usalama, na kama kutatokea fujo kimbia
moja kwa moja hadi mfichoni kwetu usijali litakalo tokea….mungu atakulinda…’akaniambia
Wakati anamalizi yale maneno mara ghafla, ikasimama nyuma yatu
landrover, ikiwa imejaa mgambo na askari wa kawaida, nikageuka kushoto , halafu
kulia ili nipate mwanya wa kukimbia, …wakanidaka kabla sijakimbia.
Mama alipoona hivyo akawa mbogo, wakaanza kumpiga mama kama
wanapiga mwizi, na ajabu kubwa niliyoiona ni kuwa mara nyingi wakimkamata mama
walikuwa wakipenda kumkanyaga mama kichwani. Mtu wamekamata kadondoka chini
wanamkanyaga kichwani. ..Nililia sana,
Na leo hii nalikumbuka hili tukio ni kijua kuwa , hawo mgambo na
wanadamu wengine ndio waliomfikisha mama yangu hapo alipo, ndio walionifikisha
hata mama hapa nilipo, dunia ilitutenga kwasababu ya umasikini wetu, kwani
jamani tuliomba tuwe hivi…tulikosa nini. Wakati nalia na kuomba wasimuue mama
yangu, nikawa naimba wimbo wa Huruma nikisema;
‘Mama nakupenda mama, mama naomba usife,
nitaishi na nani kwenye hii dunia..,’
Rafiki yangu , machungu ni mengi yaliyonipata siku ile, ila kwa uhakika
nakumbuka dakitari aliniambia mama ana matatizo sana kwenye kichwa, kuna athari
zimejitokeza kichwani kuna uvimbe kichwani…, ila bado waanzidi kuchukua vipimo
vingine kuhakikisha kama hakuna tatizo jingine …
‘Sasa tutafanyaje kuhusu huo uvimbe..?’ nikamuuliza dakitari
‘Kwakweli kwa hapa nchini,mmh …wewe subiria kwanza vipimo vingine
kama ni huo uvimbe tu, mama yako atahitajika kufanyiwa upasuaji, na tatizo ni
kuwa upasuaji kama huo, hauwezekani hapa kwetu, ….unapatikana India..’akasema.
‘India…?’ nikauliza
‘Ndio..utakuja kuambiwa kila kitu baada ya vipimo vyote kukamilika..’akasema
WAZO LA LEO: Urafiki mwema ni ule unaokuja wakati wa
matatizo wakati mtu hujiwezi, hana mbele wala nyum,au wakati mtu unaumwa, anahitajia
msaada wa hali na mali, hapo ndipo utakapogundua ni nani rafiki yako wa kweli. Wengine wanasubiria mtu afe ndio wanafunga
safari toka walipo na kujifanya wanajali, waanupendo, upendo gani wa kupenda
maiti…ukishaondoka duniani, upendo kama huo hauna maana tena kwa marahemu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment