Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, September 29, 2014

DUNIA YANGU-38


Kikosi maalumu cha kupambana na kundi haramu kiliundwa, na majukumu makubwa akakabidhiwa Inspecta Maneno, japokuwa lifanyika kwa njia ya mtego zaidi, na muda huo mrembo Jembe akawa safarini kwenda masomoni.

‘Uliniambia Insepecta Moto amepatikana mbona sikumuona nlipoitwa makaoni?’ akauliza Inspecta Moto alipokutana na Inspecta mwenzake ambaye sasa ndiye atakayeshikilia nafasi yake.

‘Ilikuwa njia ya kukufanya ufike huko ukiwa hujajiandaa, ndivyo nilivyoambiwa..’akasema

‘Hawa watu hawana akili kweli, badala ya kuniacha nimalize kazi niachane nao kwa amani, wanafikiri mimi nitakuwa nao maisha yangu yote, hilo halipo. Sasa kazi umeachiwa wewe, kituo hiki sio kirahisi kama unavyofikiria wewe na hao waliokutuma, nimepata taabu sana, lakini ngoja ujionee mwenyewe..’akasema

‘Usijali hiyo ndiyo kazi yangu na wajibu wangu, nitaitimiza kama ipasavo, usiwe na wasiwasi mkuu…’akasema

‘Vipi yule mrembo niliyakuonyesha siku ile..?’ akamuuliza

‘Achana na mambo hayo…mimi sipo huko kabisa, najua hiyo ndio mitego ya watu wabaya, kazi yangu ni moja tu kupamabana na wahalifu….’akasema

‘Haya tutaona hata mimi nilikuja hapa nikiwa na hamasa kama zako, lakini baadaye mmh, ngoja ujionee mwenyewe….’akasema

‘Hamna shaka mkuu,..hiyo ndio kazi niliyoisomea cha muhimu ni kujua ni nini wajibu wangu…’akasema

‘Yah, wewe huna tofauti na Moto, sasa yupo wapi……kampoteza mke, na sasa hajulikani wapi alipo,…..’akasema

‘Ndio mitihani  ya hii kazi….katimiza wajibu wake….’akasema

‘Mnanikera nyie watu…..hivi mnataka muishi maisha hayo mpaka lini…hebu angalieni wenzenu wanavyotesa, magari nyumba nzuri, mnafikiri vimepatikana kirahisi hivyo…’akasema.

‘Kwahiyo mkuu wewe ulitaka mimi nifanya nini…?’ akamuuliza

‘Tutaongea ngoja nikamalizie kazi moja, nikihakikisha hiyo imekwisha, hamna mtu atakayeniweza…maisha safi kabisa….mtajifunza kutoka kwangu…’akasema
Inspecta Maneno akachukua pikipiki yake ambayo huwa anaitumia kwa kazi maalumu za haraka haraka, akaendesha hadi nyumbani kwa Inspecta Moto, alipofika alikutana na mlinzi , yule mlinzi aliyekuwepo mwanzoni ambaye wanafahamiana alikuwa kaondolewa

‘Umeletwa wewe hapa, mwenzako kaenda wapi?’ akauliza

‘Yupo likizo mkuu….’akasema

‘Sasa kuna mambo nataka kuchunguza huko ndani, sitaki usumbufu,..akija mtu usimruhusu kuingia, …’akasema.

‘Sawa mkuu, lakini…..’akaitikia na alipotaka kusema jambo, inspecta akasema;

‘Hamna cha lakini…umenielewa…’akasema

‘Sawa mkuuu....'

Inspecta Maneno akaingia ndani, akiwa anajiamini kabisa, akijua ni kitu gani alichokifuatilia, akafungua mlango, hadi mlango wa chumbani, akaendelea na kuchunguza huku na kule bado akiwa na imani atakipata hicho kitu anachokitafuta.

‘Haiwezekani, nina uhakika badi kipo humu humu ndani…’akasema akivurumua kila kitu kuhakikisha kila sehemu kaipitia.

Alipohakikisha hakuna hicho kitu akakumbuka, ….juu ya kabati!

Akatoka na kwenda barazani, akachukua kiti, maana lile kabati ni refu, akaweka kiti na kusimama juu yake na hapo akaweza kufikia mwisho wa lile kabati na kuanza kuangalia pale juu, kile kitu hakikuwepo..

‘Nina uhakika niliona kitu hapa juu…’akasema.

‘Ni hiki unakitafuta mkuu….’akasikia sauti, iliyomshitua hadi kutaka kudondoka kwenye kile kiti. Sauti anayoifahamu, na sauti hiyo ni ya watu wawili, wanaofanana wakiongea, mmojawapo ni yule muuaji wa kundi ambaye akitumwa kwako ujue wewe ni maiti, na wapili… akagwaya….

*********

Kesi maalumu ya kiaskari ilifanyika, na kama ilivyotegemewa, Maneno hakuweza kutoa ukweli wote, japokuwa alijua Mrembo Jembe anaweza akawa kawaelezea mengi, lakini kwa jinsi anavyofahamu yeye, mrembo huyo asingeliweza kujua zaidi, kutokana na nafasi yake kwenye kundi, kwahiyo akacheza patapotea kuficha baadhi ya mambo  kwasababu zake binafsi.

‘Mimi naona nikatafute ushahidi ambao nahisi upo kwa Inspecta Moto,kama nitaupata huo ushahidi, tutaweza kuwashinda hao watu kirahisi….’akaomba kibali.

‘Una uhakika na hilo?’ akaulizwa.

‘Ndio mkuu, katika kazi ya hao watu, kila sehemu walikuwa wakipandikiza vifaa fulani vya kunasia matukio, na nyumbani kwa Moto kulikuwa na hicho kifaa, ni kidude kidogo sana, lakini kinachukua vitu vingi,picha za video, muda tukio lilipofanyika, na hata kama utajaribu kudurufu baadaye kunakuwa na kumbukumbu,….’akasema

‘Kwanini mwanzoni polisi hawakukiona,  unahisi hapo kilipowekwa awali kiliondolewa na nani mpaka msikione wakati mnfanya uchunguzi....?’ akaulizwa

‘Inawezekana ni mke wake Inspecta, ….’akasema akionyesha hana uhakika

‘Kwani mke wake Inspecta, alikuwa anafahamu mipango hiyo?’ akaulizwa

‘Yeye kama mwanachama, kuna baadhi a mipango alikuwa akiifahamu kwa nafasi yake, lakini hiyo ya kuweka vitu kama hivyo, hakutakiwa afahamu,..ila kama alikuja kuhis hivo…’akasema.

‘Kwanini mume wake asihisi kuwa kuna kitu kama hicho ndani ya nyumba yake..?’ akaulizwa.

‘Kama nilivyosema ni kifaa kidogo sana, na unaweza kuweka kwenye kitu kingine, kikafanana na hicho kitu, kinaashiri rangi ya kile kitu, kimeengenezwa kwa tabia a kinyonga, na hakuna chombo cha kugundua vitu kama hivo kinachoweza kukigundua…’akasema

‘Tunachojiuliza hapa ni jinsi mke wa Inspecta alivyoweza kugundua…maana kama ulivyosema inahitajia mtaalamu sana kukigundua, au sio?’ akaulizwa

‘Kama shemeji yangu huyo alitafakari kwa makini angeliweza kuligundua hilo, hasa baada ya kutishiwa kwa kuonyeshwa mambo yake binafsi ambayo hakupenda mume wake ayafahamu, ambayo pia yalitumiwa awali kwa yeye kuingizwa kwenye kundi….’akasema

‘Mambo gani?’ akaulizwa

‘Mara nyingi kundi hilo huwalazimisha watu kujiunga kwa kuwanasa kwenye kashfa nzito, kwa wanandoa wanaweza kutafuta matendo yako machafu ya nje ya ndoa, na ikishindikana kabisa wanakupandikizia mtu, ufanye naye uchafu, na kuchukua hayo matendo kwenye kanda za video…’akasema.

‘Kwahiyo kwa huyo mama walifanya hivyo?’ akaulizwa

‘Mhh, ndio, nahisi hivyo….na nahisi pia kuwa huenda, ndio sababu ya kuja kujiua kwake, kwani yeye alitakiwa kutoa maelezo ya mume wake ambayo hakuweza kuyatoa, wakaona njia rahisi ni kumtishia kwa kumuonyeshea machafu yake zaidi yaliyokuwa yamefichwa…’akasema.

‘Lakini si umesema huyu mama alikuwa mwanachama toka awali, kwanini haya yaje baadaye, hadi afikie kujiua, kwanini ashindwe kushirikiana na kundi kama alivyofanya  toka awali?’ akaulizwa.

‘Uwanachama wake ulikuwa sio wa ndani zaidi, ni ule wa kawaida tu kwa kutumiwa, mwanzoni walimuingiza wakati anashikirikiana na yule dada mwenye kampuni ya urembo,na akanaswa kwa kutegwa akiwa na mwanaume aliyetegewa naye….’akasema

‘Huyo mwanaume alitegewa kwake, sio kweli kuwa huyo mama alikuwa na tabia kama hiyo y akutembea na wanaume wa nje…?’ akaulizwa

‘Yule mama alikuwa mwaminifu sana kwa mume wake, ni mwanamke aliyekuwa akijitahidi sana kutimiza wajibu wake wa ndoa…hilo mimi namtetea. Lakini watu hawa wana mbinu za kila namna, wakapitia kwa wanawake wenzake..kwenye vikundi, sherehe, na huko wakamwekea madawa kwenye kinywaji, akajikuta anatembea na huyo mwanaume, na hapo wakaweza kuchukua picha zake mbaya…’akasema

‘Hapo ni wakati walipomtaka kujiunga na kundi au ni baadaye…?’ akaulizwa

‘Ndio chanzo cha yeye kujiunga na hilo kundi, kwani alipoonyeshwa hakuamini, na alikuwa kama kachanganyikiwa, nakumbuka kipindi hicho alikuwa mgonjwa sana, hadi mume wake akaamua ampeleke kwako kwa muda, na aliporudi akatulia, na ndipo alikuja mtu kumshauri ajiunge na hayo wanayotaka hao watu, akakubali, akaamua kufanya hivyo watakavo hao watu.

‘Unafikiri kwanini alikubali..na kwanini hakumuambia mume wake?’ akaulizwa

‘Asingeliweza kabisa kumuambia mume wake..sio rahisi, maana kinachofanyika hapo ni kitu ambacho hutapenda mume wako au mtu mwingine unayemuheshimu akione….wanajua ni nini wanachokifanya…’akasema

‘Kwahiyo na wewe ulifanyiwa hivyo?’ akaulizwa

‘Ni kama hivyo,…maana walijua kuwa sitakubali kirahisi, wakanitegea wanawake na kuninasa, na kwangu haikuwa vigumu sana kunitegea wanawake maana wananifahamu udhaifu wangu, na kiukweli niliwagomea sana, ila pale waliposema wanaupeleka huo ushahidi kwa baba mkwe wangu, hapo, nikashindwa…

‘Kiujumla mkuu, watu hao wana mbinu za kila namna, hata za kukushawishi kuwa muwekezaji na humo wanaweza kukutegea bidhaa bandia, ukaja kukamatwa na polisi, na hao polisi ni watu wao…..’akasema

‘Je katika hilo kuna muda walikuchukua picha zako ukiwa na mke wa Inspecta?’ akaulizwa

‘Mhhh, yaah…ni kweli hilo walilifanyia, lakini….mmmh, haikuwa mbaya ya kuweza kunishawishi, zipo nyingine za wanawake wengine, ndizo zilikuwa mbaya zaidi, na ndizo sikupenda zije kuonekana na familia yangu…’akasema

‘Mahusiano yako na mke wa Inspecta yalikuwa toka awali au ni katika kumshawsishi mke huyo kujiunga au kutoa taarifa za mume wake?’ akauliza

‘Hapana yule mama ni mtu aliyekuwa akijiheshimu sana, na nikuambie ukweli, hata kama ingelikuwa ni wewe kwa mbinu wanazozifanya utakubali tu kujiunga na hilo kundi, wana mbinu za kila namna ikishindikana ndio wanatumia mbinu za kukupandikizia makosa..’akasema

‘Mbona Inspecta Moto walishindwa kumshawishi?’ akaulizwa

‘Alikuwa mbioni,angepatikana tu,….na hata hivyo, yeye hawakumuhitaji sana, maana mke wake alishanaswa, kwahiyo kila walichokitaka kwake,walikipata kupitia kwa mke wake..ila baadaye walianza kumuona kuwa ni tatizo, kwani alishaanza kugundua mengi kuhusu hilo kundi, ndio maana wakaanza kumuandama...’akasema

‘Kwahiyo mke wake aliweza kutoa taarifa zote kuhusu mume wake?’ akaulizwa

‘Za muhimu ndio..kuna muda alikuwa anaogopa,…unajua tena mapenzi ya mume na mke, kuna muda unamuonea mwenzako huruma,  lakini akiogopa wanamuonyesha uchafu wake, na wakimlewesha kidogo tu, anaongea kila kitu…akilewa hana ujanja, ataongea kila wanachokitaka….’akasema

‘Je hadi kuwa na mahusiano na shemeji yako, walifanya hivyo, wakiwa na lengo la kupata hayo wanayoyataka kutoka kwa Inspacta Moto ?’ akaulizwa

‘Sio mara kwa mara, maana wananifahamu msimamo wangu, mimi walinitumia tu kwa kazi nyingine, na hata hivyo, kwanini wanitumie mimi kwa kazi hiyo ndogo huyu shemeji hakuwa mgumu kiasi hicho, hasa walipogundua kuwa akilewa, anaongea yote wanayoyataka….’akasema

‘Wewe huwa walikutumia kwa kazi kama zipi?’ akaulizwa

‘Zinazohitaji utaalamu wa kujua jambo lisilopatikana kwa urahisi, kama wanataka kujua jambo ambalo hawawezi kuwatumiwa watu wengine, ndipo wananitumia mimi, lakini sio kazi ndogo ndogo hizo ambazo wangeliweza kufanya watu wengine, kama mrembo Jembe, ….’akasema kwa kujisifu.

‘Na mwishoni ndio maana wakakutumia wewe kumpata au kumuua Inspecta Moto?’ 
akaulizwa.

‘Ni kweli waliposhindwa wakaniita mimi kuwa nikabiliane na mwenzangu huyo, kwakweli hapo walinivunja nguvu, nilijaribu kuwashawishi kuwa huyo mtu waachane naye , mimi nitajua jinsi gani ya kumuweka sawa, lakini hawakukubali, wakasema ni lazima ama tumshawishi ajiunge na kundi, au apotozwe kabisa, kwani kwa sasa yeye ndiye tishio..’akasema.

‘Kwahiyo ukafanyaje?’ akaulizwa.

‘Nikawa natumia mbinu zangu kupoteza muda, maana kiukweli inspecta ni rafiki yangu na tumetoka naye mbali, kwahiyo ingeniuma sana, sikupenda na baadaye waliligundua hilo, ndio wakampa kazi hiyo mtu wao maalumu, huyo akipewa kazi, hana mzaha…’akasema

‘Ni vitu gani hasa wanavyovitumia kuwaangamiza watu wasiowataka..?’ akaulizwa

‘Mara nyingi wanatumia madawa, kuna sindano zinawekwa kwenye bastola akma risasi,kwenye hizo sindani wanaweka sumu..au hata kwenye dawa kama hizi za capsule,hata kwenye panadon,  ukienda kutibiwa wanakupa basi kazi imekwisha, ..au hata kwenye vinywaji, soda pombe, wao wanakuwa na chupa zao tayari, zinaweka sehemu za manunuzi, ukija kunywa mtu wao,..ukinywa umekwenda na maji….’akasema

‘Ni hatari…huoni kuwa wanaweza kufanya makosa vinywaji hivyo vikaenda kwa watumiaji mitaani?’ akaulizwa

‘Hilo hawafanyi makosa, vnywaji hivyo hutengenezwa siku hiyo na kuhakikisha vinatumiwa siku hiyo kwa walengwa, na kama vimebakia vinaharibiwa haraka sana….hakuna ushahidi unaobakia, nakuambia hao watu ni wataalamu sana, na kila tukio wanalifuatilia kwa kamera za video…’akasema

Inspecta Maneno alihojiwa kwa siku mbili, ili kupata hizo taarifa, lakini mara kwa mara aliachiwa kutoka ili aonekane yupo kazini kama kawaida, lakini chini ya ulinzi maalumu, nia ni kuhakikisha kundi hilo haligundui chochote.

Na siku iliyofuata ndio Inspecta Maneno akaamua kwenda nyumbani kwa Inspecta Moto, kukagua kwa mara ya mwisho kama alivyoomba. Na kitu kilichomshangaza ni kutokumuona Inspecta Moto, huko makaoni ambapo alisikia yupo huko, na alipouliza aliambiwa huyo mtu hajapatikana.

‘Kwanini msako usiendelee kufanyika, maana huyo ni mtu wetu..na kama walimpiga hiyo sindano sizani kama yupo hai, mna uhakika kweli kuwa yupo hai?’ akauliza

‘Hilo linaendelea kufanyika, usiwe na wasiwasi, wewe kuanzia sasa weka fikira zako kwenye hii kazi ya kuwajibika, kuhakikisha hili kundi linamalizwa, usipofanikiwa  kwa hili, ujue utawajibika vibaya sana, umesaliti, na adhabu ya kusaliti unaifahamu..’akaambiwa

‘Naifahamu mkuu, mimi nitatimiza wajibu wangu nipo bega kwa bega kuhakikisha kundi hili linapatikana, mkuu….’akasema.

Na pale alipokuwa kasimama kwenye kiti aliogopa hata kugeuka, akilini akijaribu kuhakiki, kuwa kweli sauti hiyo ni ya mtu anayemfahamu, akasema;

‘Wewe ni nani, umetumwa kuniua sio…..’akasema na kwa haraka akaruka hewani na kujiviringisha kisarakasi hewani kutoka kwenye kile kiti na kutua chini tayari kwa mapambano….

WAZO LA LEO: Siku hizi ubinadamu umekwisha, watu wapo tayari kufanya lolote, ili wapate mali, wamefikia hadi kuua,umesikia visa vya kuua wenye athari za ngozi-Alibino,..achlia mbali hao majambazi ambao wameamua maisha yao yawe hivyo, lakini pia hata kwenye sehemu zetu za kazi, maofisini, mitaani, ndugu marafiki, wanaposhawishika kuwa wakifanya hivyo watapata mali, hawajali tena ubinadamu.


Hivi tukiwa na tamaa hivyo ya mali isiyo halali hata kufikia kuua, ina maana tunajiona kuwa tutaishi milele, …hapana, huko ni kujidanganya, kwani kiujumla mali, utajiri huo ni wa kupita tu, siku yako itafika, na mali hiyo utaiacha kwa fedheha na mateso makubwa, maana adhabu ya dhuluma mateso yake huanzia hapa hapa duniani.

Ni mimi: emu-three

1 comment :

Anonymous said...

Ujumbe Wa Leo murua natamani wapite wasome