Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, July 9, 2014

DUNIA YANGU-3


‘Hawa watu wanasema wana akili zaidi yangu kwa vile wamekwenda kusoma Ulaya, Marekani, na wapi sijui, lakini hawajui mimi nina akili zaidi yao, ngoja niwaonyeshe mimi nilivyo na akili zaidi yao,....’akasema akikumbuka yeye alitaka kwenda kusoma nje, lakini baba yake alikataa, baba yake alimwambia anatakiwa kuwa hapo kwani ana mambo mengi ya kujifunza kwanza

Lakini hata hivyo, alipelekwa kwenye shule ya hali ya juu, akasoma, na darasani alikuwa miongoni mwa watu waliokuwa wakifanya vyema, hakumuangusha baba yake, na siku moja baba yake akamwambia;

‘Akili uliyo nayo najua baadaye utaitumia vyema, nataka ujue utawala, ujue jinsi ya kuongoza watu, lakini pia nataka ujue uchumi, ili uweze kuwa mzalishaji mnzuri, ...’akasema baba yake.

‘Nitajitahidi baba , lakini mimi nilitaka kwenda kusoma nje, nijifunze mambo ya mitandao, napenda sana komputa...’akasema

‘Hayo yote utajifunzia hapahapa usijali, siku pesa inaongea,...’akasema baba yake
Ni kweli pesa inaongea, elimu zote hizo alizipata humu humu nchini, na japokuwa alikuwa na hali fulani ya ugumu, lakini alipokuwa na komputa, aliweza kugundua mambo mengi, na baba yake akagundua kuwa mtoto wake ana kipaji cha mambo hayo, lakini hakutaka kumuingiza huko moja kwa moja,alitaka mtoto huyo awe mrithi wake..

Alipokuwa akiyawaza hayo, akakishika kile kijitabu, na kufungua ule ukurasa ambao alishaanza kuandika kwa kifupi jinsi wazo lake litakavyokuwa, jinsi gani anaweza kuyaweka mambo yake kwa pamoja...akachora dunia, na kuiangalia kwa makini,halafu akachora mikono mingi, ikiizunguka hiyo dunia, akaiangalia ile picha kwa makini , kwa muda mrefu....halafu akatabasamu..

‘Ni ujanja mdogo tu ukiwa na akili kama zangu, halafu tena uwe na pesa...hahahaha’akasema na kuanza kuandika mawazo yake kwenye maandishi, aliandika kwa muda mrefu,...vidole vyake vilikuwa vyepesi sana, kwa muda mfupi akawa amendika mambo mengi..

Baadaye akatulia, na akilni alijua kabisa licha ya hayo mawazo yake, licha ya hayo malengo yake, licha ya kuwa ana pesa,...lakini yeye peke yake hataweza, ...hata pesa alizo nazo, hazitatosha, kunahitaji pesa nyingi zaidi...

‘Mmmh, kweli pesa hazitoshoi hata uwe na pesa za kuijaza hii dunia,..lakini kianzio kipo...’akasema na kuanza kupiga mahesabu yake, na alipofikia mwisho akajikuta anahitaji pesa mara mbili ya hizo alizonazo...

‘Haiwezekani....’akasema,

‘Hata hivyo, hata nikiwa na pesa kuna tatizo jingine,...nahitaji vichwa, nahitaji rasilimali watu, na watu hao wawe na utashi wa hali ya juu, wawe na ujasiri...’akasema na kuandika hayo mawazo

‘Wakati mwingine, kama ikibidi, kutakuwa na kumwaga damu..’alipowaza hivyo, akainua kichwa na kuangalia kile kisu, na rangi nyekundu iliyokuwa kwenye kile kisu, ilionekana kama inavuja,...hizo ni hisia zilizokuwa zikimjia akilini

‘Kwahiyo nahitaji watu ambao wapo tayari hata kuua....hilo sio tatizo nitawajenga, kila kitu kinawezekana kama ukiwa pesa, ....’. Akatikisa kichwa na kusema;

‘Ukiwa na pesa, ukawa na utajiri kama huu huwezi kushindwa kitu, sijui kwanini wazee hawa walikuwa wakiishi kwa shida, wakati pesa wanazo, utajiri wanao lakini waliukalia, sasa mimi nitautumia, tatizo ni muda, tatizo ni namna ya kuanza, tatizo ni hawa watu , rasisilimali watu watakavyonielewa,...’akasema na kuanza kuandika mambo mengine kwenye hicho kitabu, hadi ukurasa ule ukajaa tena.... 

Kabla hajafungua ukurasa mwingine mpya, akaona afanye marejeo kidogo, akafungua ukurasa ule wa mahesabu ya pesa, akaongeza mistari mingine na kuweka kiasi cha pesa, na pesa anayohitajika ikazidi kuongezeka,...akaangalia kiasi cha pesa kilichopo benki, akakigawa mara nne,  kwanza fungu la kujiwezesha, pili fungu la kuwezesha, tatu fungu la kuwekeza, nne, fungu la dharura...pesa imekwisha....

‘Pesa haitoshi, mmmh, haiwezekani....’akasema na kuguna

‘Ina maana pesa zote zimeisha kwa haya mambo manne tu, haiwezekani, ....’akasema

‘Lakini huyu baba aliwezekaje kuwa na pesa nyingi kama hizi...hii miradi aliwezeaje kuimudu mwenyewe, .....?’ akajiuliza

Alifungua ukurasa mwingine, ambapo kuna watendaji wa kampuni za baba yake, akawaangalia hao watu, aliona wengi ni wazee, akaanza kuangalia kisomo chao, akaguna, na kuanza kuandika mapendekezo yake, alipomaliza akasema;

‘Hawa hawanifai...nataka vichwa vingine,....hawa hawataweza kupokea mafunzo yangu, nataka watendaji wanaoweza kubuni mambo mapya, wasiogope kuthubutu, hilo nitalifanyia kazi...’akasema na kuandika maazimio, halafu akafungua ule ukurasa wake wa kwanza, lakini mara akakumbuka jambo, akasema.

‘Kwanza lazima niongee na hawa mameneja wote, pili nihakikishe hakuna kinachofanyika mpaka mimi nitoe idhini, na tatu pesa zote kuanzia sasa zitaingia kwenye account yangu....’hapo akacheka na kuikuza picha yake ya dunia ikiwa na mikono mingi...

‘Bila hivi wajanja watanizidi,...mmh, kwanza niongee na huyu mhasibu wa mzee, mmh, hata yeye ni mzee, kwanini baba alipenda kuwaweka watendaji wake wa karibu wazee, huyu nitamuondoa,...ngoja kwanza niongee naye, nione kama kuna pesa nyingine zimeingia,.....’akampigia huyo meneja fedha, na kumuuliza, na aliambiwa hakuna fedha iliyoingia tangu baba yake afariki maana wawekezeja wengi, hawajakuwa na amani, na utawala mpya...

‘Kwanini, nyie sasa mnafanya nini maofisini?’ akauliza

‘Kazi zetu zipo kila siku kuwe na pesa au kusiwepo na pesa, kuna mambo mengi tunafanya, ...’akasema huyo mzee

‘Naona, hamuwezi kazi...kama hakuna pesa, sihitaji watendaji wengi...nataka uje ofisini kwangu na mahesabu yako yote,....na uje na wazi jipya la kunihakikishia utendaji wako, kama huna wazo jipya, sizani kama utanifaa...’akasema

‘Nitakuja tu kijana..mzee, bosi....’akasikia huyo mzee, akishikwa na kigugumizi, na hapo Diamu akatabasamu na kusema;

‘Hivyo ndivyo nataka, nikiongea, watu wanagwaya, mzee, sasa ananiita mzee,...hahahaha...’akacheka na huku akifungua ule ukurasa wa mawazo yake, na akawa anakumbuka maneno ya mama yake;

‘Mwanangu uwe makini na hao wazee wa siku nyingi, hao watakuwa kikwazo kwenye mambo yako, hao wanafahamu kila kitu kuhusu mzee wako, kuna muda walihisi kuwa mzee , baba yako kauwawa, hao wazee wanaona mbali sana, .. cha muhimu ni kwenda nao taratibu ukiweza waondoe mmoja mmoja, ila uwe makini, wanaweza kukuharibu kabisa....’akasema mama

‘Mimi siogopi mtu...’akasema

‘Sio swala la kuogopa, ni swala la kukuharibia...’akasema mama

‘Mimi nitajua jinsi gani ya kuwaweka sawa, usijali mama, huyu mtoto wako haogopi kitu, baba alinijenga kuwa jasiri...nitajua ni nini cha kuwafanya....’akasema

Wakati anawaza hivyo, mara mlango ukagingwa na huyo mhasibu akaingia ni mzee , ni makamo ya baba yake, na wakasalimiana, na wakaongea, na yule mhasibu alijaribu kumuelezea ni kwanini wawekezaji hawataki kuwekeza, lakini ndani ya akili ya diamu, hakutaka kuelewa, alijua kila jambo lina njia, haiwezekani, ...halafu akasema;

‘Ok, sasa naanza kuelewa, kumbe hilo nalo ni tatizo, hapa sasa nahitajia kichwa kipya, cha ushawishi, ni lazima hawa watu warudi kwenye mstari, ni lazima wote waje kwetu, sioni kwanini mzee, hebu niambie kuna mbinu gani tunahitajika kutumia?’ akauliza

Yule mhasibu akajaribu kumuelezea kitaalamu, kuwa yeye anahitajika kuonyesha kuwa kweli anaweza kusimamia mitaji yao, je kweli anaweza kuhakikisha mitaji ya hao watu itakuwa salama, na kuna kikao kitakaa kuamua kama wataendelea kuwekeza hapo kwenye kampuni au watakwenda kuwekeza kwingin....blabla...., hakutaka hata kusikia zaidi.

‘Mzee, hivi ni mimi nahitajika kuwaonyesha au wao waonyeshe kuwa wananotaka kuwekeza kwangu, hivi hawa watu hawajui kuwa mimi nimeshikilia mpini,...kumbe eeh, lakini hivi kwanini wasumbue, kwanza hadi sasa mimi nina mitaji yao tayari, mtu akisema hataki kuendelea na mimi, mtaji wake hapati,...hilo nataka walielewe, pili, mitaji yao, nikuitumia mimi,  bila wao kupata hata senti moja, watanifanya nini?’ akauliza

‘Watakushitaki, kuna mikataba kisheria, hilo kijana wangu usijaribu kufanya, watu hao wana mawakili wao, na kwanini ufanye hivyo, muhimu ni kuwahakikishia tu, uwe na ushawishi, kivitendo, sisi tumeishi miaka mingi kwenye miradi ya kampuni ya baba yako tutakusaidia,...’akasema mzee

‘Hahaha, mikataba kisheria...sheria, eeh, na mwanasheria wetu ni nani, ni yule mzee, mmh,wazee, wazee kila kona wazee...nitataka kuongea naye, usijali mzee, tupo pamoja, nitahitaji uzee wako kwa muda, lakini baadaye, nitajua la kufanya ....’akasema akiandika kitu kwenye kijitabu chake.

‘Mzee, wewe niachie mimi hayo, ila nahitaji mahesabu yote, nahitaji kila kitu ulichokuwa ukikifanya, kesho ukija hapa tutakaa nataka kujua kila kitu ulichokuwa ukikifanya, usiache hata jambo moja, ...umenisikia mzee wangu...?’ akasema

‘Lakini utakuwa muda mfupi kuweza kufanya hilo, nakushauri muhimu tuwe na ajenda ya kushawishi wawekezaji kwanza, tusianze mambo ya ndani yatakayoleta sintofahamu, wakahisi kuna migongano...ni muhimu sana hilo kibiashara...’akasema mzee

‘Mzee wewe, unaweza kwenda...mimi najua ni kitu gani nafanya, wewe utaona mzee, hapa yupo kichwa, Diamu, unafahamu maana ya jina hilo....’

‘Nakumbuka baba yako alipotaka kukupa hilo jina nilikuwepo, akasema anataka jina tofauti, akasema atakuita jina la kipekee, na mama yako ndiye akalitaja jina hilo, lakini wazee wengi walipinga, kwani sio majina ya kifamilia,....’akasema

‘Basi mimi nafahamu maana ya jina hilo, jina hilo maana yake ni damu ya shetani...hahaha...’akasema na kucheka, na yule mzee akamwangalia kijana yule kwa mshangao na kusema

‘Mwanangu hiyo sio maana yake usijiumbie ubaya....ujue jina linaweza kukufanya uwe na tabia hiyo hiyo unayofikiria wewe,...’akasema mzee

‘Yah, mimi nahisi nipo hivyo, ....kwani hao nikisema ndio nimekuwa, hata hivyo, sioni ajabu, mzee, wewe hunifahamu mimi nipoje ndani, lakini ipo siku utanifahamu,...’akasema akimuangalia yule mzee kwa macho makali, hadi yule mzee akakunja uso kuonyesha wasiwasi, akageuka na kuanza kuondoka, na Diamu akamuangalia yule mzee wakati anatembea, akatikisa kichwa na kabla yule mzee hajafunga mlango Diamu akasema;

‘Mzee, pia, natumai kwa muda uliokaa na mzee wangu, umewekeza mahali,..nataka ukakae kwenye miradi yako, ujitegemee, unalionaje hilo wazo, waachie vijana wawajibike, au nitakuwa nimekosea?’ akauliza na yule mzee, akasema;

‘Utakuwa umefanya haraka kuchukua maamuzi hayo, sikatai, hata hivyo nilishaomba iwe hivyo kwa baba yako, baba yako akakataa, akasema ananihitaji sana, sasa kama wewe unaona hivyo, basi lakini kwa kuanzia sisi ni watu muhimu sana, maana tunafahamu wapi baba yako alipotoka hadi hii leo, hujui siri ya mafanikio ya baba yako, huwajui maadui zake, kijana unatuhitajia sana sisi ....’akasema mzee huyo kwa sauti ndogo ya kutia huruma.

‘Mimi nafanya hivyo kwa nia njema tu, sio kwamba siwahitaji, nawahitaji sana, lakini yatakayotokea mnaweza mshindwe kuvumilia,...sitaki kupata laana nyingine, hapana, hata hivyo, uongozi wangu utakuwa wa mikikimikiki, sijui kama watu kama nyie mtauweza,...nataka tusaidiane jambo kwanza utaniambia unahitaji kiasi gani cha kukuza mtaji wako, tuone tutasaidiana vipi, ninaweza kukuhitaji tena na tena, maana mzee alisema wewe ni muaminifu sana, umeishi naye kwa uaminifu mkubwa...’akasema

‘Hamna shida, ila kwa ushauri wangu wa mwisho ni kuwa mageuzo unayotaka kuyafanya, usiyachukulie kwa pupa, hata nyumba haijengwi kwa siku moja, ni vyema ukaenda hatua kwa hatua kidogo kidogo, mwishowe utaweza kusimamia shughuli zote kwa makini zaidi,...wawekezaji ni muhimu sana kwenye kampuni, ukiwakosa hali itakuwa mbaya...’akasema huyo mhasibu

‘Mzee, usijali, hakuna kitakachoharibika, ila nawaonya wenye nia mbaya, kama kuna mtu ataanza kuleta balaa, akafanya fitina, mimi nitamuona, nitahakikisha anakwenda kusikojulikana.....nimeshajiandaa kwa hilo...’akasema na yule mzee akasema

‘Hakuna mwenye mawazo hayo, ni kusaidiana tu, ila kwa hilo unalotaka kulifanya utajiharibia, na sisi wazee kama unatuona hatufai kwenye ofisi yako tutaondoka tu, ila utakuja kutukumbuka...’akasema

‘Sawa mzee, cha muhimu ni kujua kuwa kila jambo lina muda wake, umri nao unakushitaki, huoni mzee kuwa unahitajika kumpumzika, ni muhimu wewe ukaa-kaa nyumbani,...nakushauri hivyo, kaa jipange nipa mahesabu yako, ili upate kianzio cha uzeeni, au sio mzee...?’akasema na yule mzee, alifunga mlango bila kusema neno.

‘Hahaha mzee kazeeka kupita kiasi kwa muda mfupi tu,....mzee wangu kaondoka itakuwa yeye, ngoja kwanza, hata hivyo kanipa wazo, wazo jipya, hapa ni lazima niwarejeshe hao wawekezaji kwenye mstari, ni lazima kwanza nimtafute huyu mtu wa kushawishi, .....’akabponyeza kitufe kwenye simu ya mezani, na mara sauti ikasema;

‘Bosi nakusikiliza...’ile sauti anayoipenda kuisikiliza ikasema;

‘Njoo hapa mara moja kuna kazi nataka unifanyie mara moja....’akasema
Yule binti akafika, na kusimama mlangoni, akionyesha lile tabasamu lake analolijua mwenyewe, huwa akilitoa hilo tabasamu watu kama akina Diamu, hawakatizi ni lazima watasema neno.

‘Ingia ukae hapa kwenye kiti, kuna mambo nataka tuyafanyie kazi, nataka unisikilzie kwa makini, ukifika nyumbani leo nataka ukae, upasue kichwa na ubuni mbinu na kesho nataka jibu,....unakumbuka nilipokutoa....?’akauliza

‘Bosi nawe bwana, kwanini unasema hivyo...mpaka uanze kuninyanyasa...’akasema huyo binti akijibaragua kimadoido.

‘Aaah, sio kukunyasa kama unavyofikiria wewe, mimi ninachotaka ni kutumia vipaji, wewe una kipaji, au sio....?’ akawa anauliza

‘Kipaji gani bosi, mimi sio muimbaji....?’ akauliza

'Hicho ulichokuwa ukikifanyia kazi,nataka ukumbuke zile mbinu za mitaani, jinsi gani ulivyoweza kuwapata watu wakubwa, ambao walijifanya hawapatikani, jinsi ulivyoweza kuwaachanisha waume na wake zao,....’aliposema hivyo, yule binti akacheka hadi bosi akabakia ameduwaa, na baadaye bosi akauliza

‘Unacheka nini,...mimi nipo kikazi zaidi...’akasema Diamu

‘Nimecheka maana sikutegemea bosi kama wewe utafikiria hayo mambo yangu kama yana faida, ...’akasema

‘Hahaha, kila kipaji kina faida, watu hawajui,...mimi nataka kufanya mambo ambayo hayajawahi kufanyika, vipaji, akili, ujanja, umbeya,....ni rasilimali...’akatulia kidogo

‘Bosi...’akasema huyo binti

‘Nataka ufikirie, nakuhitajia kwa kazi maalumu, kwanza nataka uelewe kuwa mimi nimekuchukua kwenye hii ofisi sio kwa ajili ya kuangalia urembo wako tu, nataka huo urembo wako uwe ni mtaji, una kazi muhimu sana,...kwa hivi sasa nahitajia sana mbinu zako za mitaani,nataka kuutumia uzuri wako kifaida, unasikia, kaa uwaze uchanganue uje na wazo tofauti ...’akasema

‘Kweli bosi hata mimi nilikuwa na wazi kama hilo lakini nilikuwa naogopa kukuambia, kama utakubaliana name, mimi nitafanya lolote unalotaka maana wewe ndiye unayeniweka hapa mjini...’akasema akijerembua

‘Kuna watu nataka waingie kwenye mtandao wangu, wamejifanya kutokuwekeza kwenye kampuni yetu, kisa hawaniamini, na sasa hivi tunahitaji pesa nyingi sana, sio kwamba hatuna pesa, pesa zipo, lakini tunahitajia pesa zaidi, kabla ya kuanza wazo langu nililo nalo kichwani ni lazima tutafute pesa,....’akasema

‘Wazo gani bosi, mbona kila siku unasema unawazo, unawazo..ni wazo gani hilo?’ akauliza

‘Wazo hilo litakuja kutajwa wakati muafaka, ila nataka wewe uwe mtu wangu wakaribu sana, maana tumetoka mbali, wewe ndiye uliyenifundisha mambo fulani, ukanitoa tongo tongo za aibu, ukanijengea ujasiri nisokuwa nao kabla, ...wewe na mama ni watu muhimu sana kwangu siwezi kukutupeni, ila na wewe usiniangushe,...’akasema

‘Siwezi kukuangisha bosi wangu...’akasema huyo binti

‘Ninachotaka nikutumia kipaji chako, nataka nianze kwa hilo kwanza, vipaji, vipaji ni mtaji nyie hamjui tu,...mmh, hilo ni muhimu sana kwasasa..., unasikia, jikumbushe, na pia kaa fikiria, unipe mawazo, nataka mawazo yenye kujenga, unasikia, usikae tu hapa ukitegemea nikulipe, hapana, ni lazima na wewe uonyeshe kipaji chako au sio, ...’akasema

‘Lakini....’akataka kusema neno baadaye akasita

‘Lakini nini, unajua wewe ulikuwa mitaani, ukawa unakutana na watu mbali mbali, wengine wakubwa, uliniambia hata waheshimiwa ulikuwa unakutana nao, na hao ndio walikufanya ung’are zaidi,ukajenga, una gari la bei mbaya,  ..mmmh, sasa nataka tukae tupange, nina wazo jipya kwako, litaleta tofauti,isiwe gari tu, nyumba tu, sasa fikiria zaidi ya hayo, wewe nenda ....ngoja nifikirie kwanza...’akasema

‘Lakini bosi mawazo si mazuri, usiumize kichwa sana, mbona una utajiri wa kutosha, utajiri ulio nao unaweza kula wewe na wajukuu zako, kwanini uumize kichwa?’ akauliza yule msichana na yule jamaa akamuangalia bila kusema kitu, baadaye akasema;

‘Nina wazo kubwa sana, na hilo wazo tukiliweka kwenye matendo, likafanya kazi, dunia itaniheshimu, kila mtu ataniheshimu, hata wewe mwenyewe utaniheshimu...’akasema

‘Bosi mbona hata hivyo mimi nakuheshemu sana tu...’akasema

‘Bado,...sijapata heshima inayostahili,....’akasema

‘Kwahiyo bosi nifanye nini?’ akauliza

‘Hilo sasa ni tatizo, watu ninaowataka mimi, ni kuwa nikiwaagiza jambo, wanajua ni nini cha kufanya, akili zao zinatakiwa ziwe pana, ...naona kwanza unahitajia shule, nitakuepeka shule, shule maalumu, ukitoka huko, sitapata maswali kama hiyo, ...nikisema fanya hiki, natarajia matokeo, mimi nataka vichwa, watu wanaofikiria, wabunifu...’akasema.

‘Sawa nimekuelewa bosi,....’akasema yule binti huku akitabasamu, alisubiri kidogo, alipoona bosi wake kazama kwenye mawazo, akasimama akatembea kuelekea pale alipokaa bosi wake na kuanza kumkanda kanda mgongoni,  

Mhh, unaona hiki ni kipaji...sasa nataka haya uyafanyie kazi, kila atakayeingia kwenye anga zetu, ni biashara...lakini zaidi ya hayo, kila tunalolitaka tunapata, nataka wewe ukishaiva unakuwa mwalimi wa wengine....unaona raha hii unayonipa, ukiwapata hawa waheshimiwa, hawa matajiri, watakubali tu...inatosha, ...’akasema na yule binti akaacha na jamaa akasema

‘Unaweze kwenda mrembo, lakini kumbuka, kesho, nataka jibu, nataka unipe mipango yako,....kesho nataka wazee wote wafungashe virago, kesho...., nataka kuanza kulifanyia kazi wazo langu, kesho, kesho.....’

NB: Hivi huyu jamaa vipi, hebu tuone mawazo ya watu kama hawa, ambayo ndio yapo kila mahali kwa sasa,


WAZO LA LEO: Akili aliyotupa mungu ni kwa ajili ya kutuwezesha kuishi kwa amani, vipaji alivyotupa mungu, ni kwa ajili ya kutuwezesha tuweze kuyamudu maisha yetu ya kila siku, je ni wangapi wanatumia vipaji vyao vyema, kwenye malengo mema. Kila mtu ana kipaji chake, basi tufikiri njia njema yenye manufaa kwa mtu mwenyewe  na kwa jamii.
nnmimi: emu-three

No comments :