Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Saturday, December 24, 2011

Akufaaye kwa dhiki ndiye rafiki wa kweli-68 Hitimisho 12




Wote walimgeukia mama na kumwangalia, hata shangazi alimgeukia, huku akimuashiria kuwa aongee, kwani huo ndio wakati muafaka wa kusema kila kitu ambacho watoto wanataka na kwa muda mchache kukawa kimiya.

Na kwa muda ule Rose akatulia kimiya kumsikiliza mama yake kuwa atasema nini, katika uzoefu wake na mama yake , huwa sio mwepesi wa kushindwa, huenda ni kutokana na uzoefu wake wa kibiashara ambapo hupambana na watu wa aina mbalimbali, na kwa msingi huo, Rose alikuwa hawezi kusimama na mama yake wakabishana kitu na akashinda, hata kama kina ukweli ndani yake, na mwisho wa siku huamua kujiondokea,

‘Sasa una kwenda wapi, ina maana umenizarau, …’alikumbuka siku moja walipokuwa wakibishana kuhusu yeye kuolewa na Adam, alipoona hawaelewani, aliinuka na kujiondokea, na kumuacha mama yake akiwa kakasirika.

‘Mama najua hata kama tutapewa siku mbili za kubishana, mimi sitaweza kubishana na wewe, wewe ulichoamua ndicho hicho hicho na utakibishia hadi uone umeshinda, sasa ni bora mimi nijiondokee, lakini hata hivyo, sitakubali kamwe kuolewa na mtu nisiyemtaka…’akasema Rose.

‘Mama leo ule ubishi wako umeishia wapi,na nashngaa mama kukuona leo ukitoa chozi, sikumbuki kukuona hivyo kabla, samahani kama kwa kukuuliza hivyo nimekukwaza kiasi hicho, ila naomba, na sio mimi tu, ni pamoja na ndugu yangu, ambaye sijui ilikuwa nia yako ipi hata tufikia umri huu bila kujuana, tunaomba utupe maelezo ya kina kwanini haya yote yametokea…’akauliza tena Rose huku akimwangalia Maua kama ana cha kuongezea, lakini alipomuona Mua yupo kimiya naye akatulia na kumwangalia mama yake, ambaye alishaonyesha ishara ya kuongea kitu.

********
Mama kabla hajajibu, alijikuta katika njia panda, kwanza kuna mambo alitakiwa asiyaongee kabisa, ambayo yanafungamana na ndoa yake, lakini yana msingi wa hayo mazungumzo, bila kuyasema haitaeleweka kitu, je ayaseme na kusaliti ndoa yake, au akaongope kiaina…? Akajiuliza kilini kwa muda, lakini kwa vile yeye ni mtaalamu wa biashara na anajua jinsi gani ya kupambana na wateja wake, akajipa moyo na kusema, nitaongea lile litakalokuja kichwani, akakohoa kusafisha koo na kusema;

‘Sikiliza Rose, usinione nipo kimiya ukafikiri labda sina cha kukujibu, na usinione natoa machozi ukafikiri mimi sio binadamu wakawaida, kuwa hata kama kuna uchungu, siusikii, mimi ni binadamu wa kawaida, na machungu ninayo sana, ….’akawa anasita maana hali ya kulia ilikuwa imemtinga, lakini akajipa moyo na kusema,

‘Rose na Maua wanangu, kwanza inabidi niseme, samhani kwa haya yote, huenda mkanielewa, au msinilewe, lakini maji yameshamwagika hayazoleki, yameshatokea yaliyotokea, siwezi kusema ngoja turudi nyuma niyageuze, ….kama binadamu nilifanya yale niliyoona ni sahhihi kwa muda huo, sikujau nini kitatokea baadaye, lakini kwa muda huo niliona ndio njia sahihi…’akawaangalia wale watoto halafu akakohoa kidogo na kuendeela kusema;

‘MaJibu yapo mengi sana, na yana msingi, sio kwamba nilifanya hayo bila sababu za msingi, la hasha, ila je hiyo sababu kwako mutaiona ya maana, je mutaamini kile nitakachokuambieni, ..hayo na maswali mengine ndiyo yanayonifanya nishindwe kuwapa jibu la haraka, maana hapa sio mahala pa kubishana tena, ni mahala ambapo tunatakiwa tuelezane na mwishoo wa ukweli na tukubaliane…’akasema mama kwa kujiamini sasa huku akimwangalia Rose, na alipogeuza macho kuwamngalia Maua, akajikuta anasita kuongea kwa ile sauti ya ujasiri, maana hapo uchungu ulimwingia…

Maua akahisi hilo na kusema `Mama we ongea tu, tunasikiliza na tunaombe utuambie kila kitu ili nasisi tuelewe….’

‘Na ndivyo ninavyotaka kusema, ila nikikuangalai moyo wangu unajaa uchungu sana, unisamehe sana mwanangu, naomba unisikilieze na unielewe, sikuwa na nia mbaya kiasi hicho…’akaanza kulia na wote wakakaa kimiya wakimwangali akifuta machozi na kupitisha leso machoni kuyafuta…hakumbuki kujisikia hivi kabla…

‘Sawa sisi sote ni wakubwa sasa, sio watoto wadogo, tunajua upi ukweli na upi sio ukweli, inawezekana kweli tusikuelewe, lakini ni vyema tukasikia hizo sababu, ili nafsi zetu zitulie, mimi sizani kwamba mzazi, hasa mwanamke unaweza akaamua kumtelekeza mwanae,tena mtoto mchanga bila sababu ya msingi,…hapo mimi bado sijaelewa, na sijui ulinikabi..dhi kwa shangazi nikiwa na umri gani, maana mimi nimejitambua nipo kwa shangazi,…ina maana ulinikabidhi nikiwa mchanga,….maana shangazi hakuwahi kuniambia ukweli…sasa ukweli tuusikie kutok kwako, …labda kulikuwa na makubaliano fulani kati yako na shangazi,…’akasema Maua.

‘Maua….na Rose, naomba mnielewe nitakayozungumza, …..Maisha yetu haya yamejaa fadhaa nyingi, na hasa pale unapokuwa namalengo yako, na huenda malengo yako haya yakawa kinyume na jamii ilivyozoea, lakini kila mmoja ana malengo yake fulani. Ili kuyafikia inabidi uhangaike, na wkati mwingine inabidi uchukue maamuzi magumu, hapo ndipo unapokutana na mitihani , ….’akaanza kuongea mama huku akionyesha hisia fulani.

‘Kama nilivyoanza kusema, kuwa kuna sababu nyingine huenda kabisa msinielewe, kwasababu nyie ingawaje mumeshafikia umri huo, bado hamjui maisha yalivyo, …maisha yetu tuliokulia yalikuwa yana mitihani tofauti na haya ya kwenu, hamkupitia maisha yetu, mumepitia maisha rahisi kidogo, vitu vimerahisishwa, na niseme kuwa mumekuta mambo yapo, lakini hamjui jinsi gani mambo hayo yalivyokuja, ….mumekuta kila kitu kipo wazi kwako, lakini ilikuwa sio kama umri wetu tukiwa kama nyie, ilibidi ujitume , ujitoe, na hata ukosane na jamii, ili ufikie maisha kama mliyotiona nayo.

Rose akamwangalia mama yake, akitaka kusema kitu,lakini shangazi akamuonyesha ishara ya kutulia, na Rose akatabasamu kiaina.

‘Mimi na baba yenu , nikiwa na maana baba yenu aliyenipa ujauzito wenu, tulikutana kwa muda mfupi tu na urafiki ukaanza kwa muda mfupi tu, na wakati huo sikuwa na malengo ya kuoana na yeye, …nilihamasika na kutaka urafiki naye, …sikuwa na malengo ya …’Mama aktuli hapo akitafuta neno la kusema.

`Niseme kwa wakati huo sikufikiria mengine kuwa yatatokea na kunifanya niweze vinginevyo. Nilimkubalia kuwa rafiki na hata kukubali kuolewa nay eye kwa haraka haraka tu. Kwani kwa muda ule sikutaka kumuumiza kwa kumwambia ukweli, na aliponitamkia kuwa anataka kunioa, nilikubali moja kwa moja, kuwa sawa, sikujua kabisa kuwa mbele yangu nitakutana na nini…’akasema mama huyo huku akiwa kainama chini.
‘Siku nilipomtamkia kuwa sawa nipo tayari kuolewa na yeye, nilishakutana na mtu mwingine, ambaye alishanibadili muelekeo, lakini yeye hakuwa muwazi sana, tulikuwa naye kibisahara tu. Siku kama leo nikamkubalia baba yenu kuwa nipo tayari kuolewa, na kesho yake nikasafairi hadi Uganda, kwani kulikuwa na bidhaa nilizozifuatilia, na wakati naingia ndani ya ndege, kuna mtu alikuja akanipa kifurushi chake akaniambia ni msaidie kukibeba anakuja atanikuta sehemu ya kukaguzi, nilikubali kwasababu kilikuwa kibegi kidogo tu na nikijua ni mama mwenzangu, …na hilo lilitokea haraka haraka sana’akasema na kutulia kidogo.

‘Nilipofika sehemu ya ukaguzi nikaweka vifaa vyangu na kukishikilia kile kibegi mkononi, huku nikimsubiri huyu mwanamama aliyenipa hicho kibegi. Mpaka muda wa kukaguliwa ulipofika, ikabidi niende nacho sehemu ya ukaguzi, sikujua wapi nikiweke, ukijua nimepwa dhamana ya watu. Nilipofika kwenye sehemu ya ukaguzi, nikakaguliwa vitu vyangu, na kile kibegi nikawa nimekishikilia mkononi,yule mtu wa kukagua akaniuliza mbona hicho simpi , nikamwambia sio changu, kuna mtu kanipa nimshikie lakini hajaonekana, …,’

Yule mkagauzi akaniangali kwa mashaka na baadaye akaniambia anataka kukikagua , kwani muda umekwisha na alionyesha dhahiri mashaka fulani na hicho kibegi nikamwambia , sitaweza kumpa hadi mwenyewe afike, tukasubiri kidogo namuda ukawa umeenda, na hatua iliyobakia ni kuingia ndani, na nisingeliweza kuingia nacho, nikampa yule mkaguzi, nikimwambia kuwa huo mzigo uhifadhiwe hadi huyo mtu atakapotokea…’

Yule mhusika akaupokea lakini akataak kuukagua kwanza, na mara nikaoana akionong’onezana na mwenzake, na mara wakaitwa maaskari, nikajikuta nipo chini ya ulinzi, nilipouliza sababu nini nikaambiwa kuwa kile kibegi kuna madawa ya kulevya, yamefungwa ndani ya begi na kushonewa, kitaalamu sana, kiasi kwamba ilikuwa sio rahisi kuyagundua….nikashikwa na butwaa…

‘Unasema madawa ya kulevya, mungu wangu, Ilikuwaje…’akauliza Maua akiwa na shauku ya kutaka kujua, akipeleka akili yake kwenye taarifa na picha za filamu alizowahi kuziona kwa watu waliokamatwa na mdawa…akaingiwa na hamu ya kusikia nini kiliendela toka hapo, na wote wakamwangali mama akiwa anaendelea kuongea.

‘Wakati nasubiri kupelekwa jela, au sijui wapi, nikapata simu yangu iliyokuwa kwenye kibegi ikaita, nikawaomba wale maasakari walionishikilia niipokee, nilipoiangalia nikaona imetokea Uganda, sikujua vipi na ni nani ,mawazo yakanituma ni moja wa mawakala wangu wanatka kujua kuwa nitafika leo au kesho.

‘Halloh, nikaipokea na sauti ya kiume ikaongea;

‘Mama Chakarika, vipi unakuja lini huku….’ Akasema huyo mwanaume nisiyemkumbuka vyema, na hilo jina la mama chakarika ndilo wanalolijua huko Uganda.

‘Sijui maana nipo kwenye matatizo, ambayo hata sijui yamekujaje..’nikasema.

‘Matatizo gani, sema kama unahitaji msaada wangu, nikusaidie na nina maongezi na wewe muhimu sana, kuna tatizo gani? Akaniuliza huyu mwanaume.

‘Kwanza wewe ni nani…?’ nikauliza kwa hamasa.

‘Mimi ni Mzungu , mfanya biashara mwenzako…’akasema huyo mtu. Na niliposiki ahilo jina nikagwaya, kwani huyo jamaa aanyeitwa Mzungu ni tajiri mkubwa sana, na nilikutana naye mara kadhaa, katika maswala ya kibishara, nakumbuka kuna kipindi nilikwama kidogo akanisaidia, lakini sikuwa na ukaribu sana na y eye. Wengi wa wafanyabishara wanamjua na akina mama wengi wanamtamani, kwani bado hajaona. Nilijiona nina bahati kubwa sana na hapo hapo ikabidi nimwambia nini kilichotokea.

‘Oh, hilo balaa, kwanini hukuwa mwangalifu, usikubali hata siku moja kupkea mzigo ukiwa unasafiri bila kuukagua, haya yanafanyika sana…sasa ngoja nitakupigia baada ya nusu saa…’akasema huyo mtu na kukata simu. Nusu saa ilikuwa kwangu kama mwaka, na kweli baada ya nusu saa akanipigia simu.

‘Sikiliza nimeongea na mtu wangu wa huko, yeye atakuja hapo atayamaliza. Huyo anawaju watu wa aina hiyo wapo wengi sana, ni wakili, hilo ni swal dogo, hapo uwanjani kuna mitambo a kunasa mzinguko ya watu, atafanya kila njia aone nini kilitokea na kama kweli ulipokea huo mzigo na huyo mtu atapatikana , kwani mawakala wote wa mambo hayoo wanajulikana…’akanipoa faraja hilo, nikawa kama mtu aliyepewa dhahabu.

‘Sasa wewe tulia usiwe na wasiwasi, kwani huku nilishatayarisha mambo fulani, ya kibishara na mengine, na nakuhitaji haraka iwezekanavyo, kwahiyo hilo swala nataka limalizwe kiharaka, na najua ni gharama, lakini hiyo gharama sio muhimu sana kuliko hilo ninalokuhitajia…’akasema huyo mtu, na sikuwa najua nini ananihitajia, nikasubiri kama alivyoniambia.

Mara akaja mtu akaongea na askari, baadaye nikaitwa pembeni nikaongea naye akanitambulisha kuwa ni wakili wa Tajiri Mzungu, akaniambi mambo yanakwenda vyema, nisiwe na wasiwasi lakini safari ya leo haitawezekana mpaka kesho…’ akasema huyo mtu.

‘Ina maana hakuna kupelekwa jela au mahakamani..?’ nikauliza.

‘Jela …mahakamani sijui …., hilo sijawa na uhakika nalo, lakini usitie shaka maana huna kosa, hilo litabainika mda sio mrefu, kama kweli huna mahusioano na hawo watu wauza madawa ya kulevya, na hilo ndilo wanalifanyaia kazi kuwa huenda una ushirika na hao watu, sasa hivi wanafanya uchunguzi, mwanzoni walishagundua kuwa kweli umepewa hicho kibegi, kutokana na mitambo yao…sasa wanachofanya ni kuhakikisha kuwa kweli huna mahusiana na hawo watu, sio njama mumepanga na huyo mtu…’akasema yule wakili.

‘Nipenge njama na nani, mtu mwenyewe hata simjui..imetokea haraak sana, kiasi kwamba..oooh, sijui kwanini nilikubali haraka kiasi hicho, najiona mjinga kweli kweli…’akasema mama.
‘Ndio hivyo kwenye sheria hakuna kusema mimi nilikuwa sijui…unapokamatwa ni kweli unatakiwa ufikishwe mahakani, na kabla ya kufikishwa mahakani, utatakiwa kupelekwa rumande, jela..na hilo ndilo nalifanyia kazi, lisitokee, kwani ukifikishwa huko hutaweza kusafiri karibuni na Mzungu anakuhitaji kama nini sijui…sasa subiri hapa nataka haya yafanyike haraka kabla hamjachuliwa na karandinga kupelekwa jela….’akasema huyo mtu

‘Jela mungu wangu,hapana, kwanini nipelekwe jela, wakati sina kosa… huko naomba ufanye kila njia nisifike huko, mungu wangu…’nikasema kwa woga, nikiwa siamini kuwa nitaokoka, na nilijua nikipelekwa huko nimekwisha, …nikaanza kuomba kila aina ya maombi, ili niokoke najanga hilo….’akasema mama akionyesha hali ya kuogopa utafikiri ndio siku hiyo. Na baadaye huyo wakili akaondoka kufuatilia hayo maswala na kuniacha chini ya ulizi wa hawo maaskari . Mama alipofika hapo akatulia kwa muda, kiasi kwamba wote wakawa na haraka ya kujua nini kilitokea baadaye na alipotulia zaidi Maua akauliza;

`Ilikuwaje baada ya hapo….

‘Ilikuwaje mwanangu, mambo yalitokea haraka haraka….nikawa nasubiri huyo wakili atakuja na majibu gani, huku naomba hilo gari, su karandinga lisifike mapema…lakini mara tukasikia kuwa karandinga la kutucuhukua limeshafika kutuchukua, nikajua sasa nimekwisha, naenda kulala jela….’akasema mama

‘Oh, mama ukapelekwa kufungwa, lakini kwanza siulitakiwa kufikishwa mahakamani, na huyo wakili alitakiwa kukuchukulia dhamana…’akasema Maua. Na mama akamwangalia Maua kwa makini, na huzuni ikamwingia kwa jinsi alivyomfanyia, akaomba moyoni, akubali kumsamehe, na atahakikisha kuwa haachani naye tena…

Na wakati mama anafungua mdomo kuongea mara simu ya Rose ikasikika ikilia, na Rose akaipokea bila kuangalia ni nani kampigia, akiwa kwamgalia mama yake kwa makini, kutokana nay ale mazungumzo,….alikuwa akijaribu kuyachuja, …akaiweka simu sikioni huku bado kamwangalia mama yake, mwanzoni alifikiria kuwa huyo aliyepiga hiyo simu ni yule dakitari aliyekuwa akimshughulia mgonjwa wao, maana ndiye aliyempa namba yake, na mwingine anayejua hiyo namba ni mama yake tu…

‘Haloh,…’akasema Rose, na upande wa pili ukawa kimiya kwa muda, akaitizama ile namba, akashangaa, maana haikuwepo namba, ilionyesha `private namber’…akashituka kidogo , halafu akasema tena huyu nani hasemi kitu na hata simu haionyeshi namba yake, akasema kwa sauti

`Halloh, nani wewe…’ Na mara sauti ya upande wa pili ikasema;

‘Nisikilize kwa makini, nipo karibu na mtu wako, na ninauwezo wa kumfanya lolote lile, lakini kabla ya kufanya hivyo, nataka tuongee mimi na wewe, fika hapo hospitalini, sehemu ya mapokezi, utanikuta, ukichelewa, usinilaumu….’simu ikakatwa…

Rose akainuka haraka kutaka kuondoka, lakini Maua akamshika mkono, na kumuuliza vipii kuna nini, kimetokea nini, mbona baada ya kusikiliza hiyo simu amebadilika na kuinuka harakaharaka, Rose akamtizama Maua kwa muda, alitaka kusema kitu, lakini akaona haina haja, akageuka kuwatizama mama na shangazi na kusema;

‘Mimi ni docta, na huko hospitalini kumetokea dharura, wananihitaji mimi kama docta…’akasema

‘Ina muhusu mgonjwa wetu, au..?’ akauliza mama kwa mshangao.

‘Ndio, lakini sio kwamba ana hali mbaya, lakini kwa vile niliwahi kuwa naye huko nilikotoka, wananihitaji kwa mambo fulani fulani, hawajaniambia ni mambo gani, ngoja niende huko nitajua nini nini, ile msitie shaka, nikirudi nitawaambia, kikao tukiahirishe hadi nikirudi, nataka kusiki akila kitu …’akasema Rose huku akiondoka, lakini Maua akawa na mashaka, na kusema ,
Ngoja tuongozane na mimi nataka kuja kumuona huyoo mgonjwa wetu..’

‘Hapana, huko kuna utaratibu wake, huwezi kuamua tu kwenda kumuona huyo mgonjwa mpaka uwe ni miadi nao, utafikaje pale bila muda uliopangiwa , ndio unaweza ukafika na kubakia nje mpaka muda uliopangiwa, sasa imesaidia nini , ni bora usubiri hadi muda tuliopangiwa, na tutakwenda kumona muda huo kwa pamoja,..usijali , mambo yatakwenda vyema na mumeo atakuwa na hali nzuri kabisa ndugu yangu…’akasema Rose, na kuondoka mle ndani.

NB:Je ni nani huyo kampigia simu Rose? Tuwepo pamoja katika hitimisho la kisa hiki. Najua wengi wapo mapumzikoni, na hasa wale wanaonisaidia kwa kunitumia maoni, maoni yenu ndiyo yanayonipa hamasa ya kuandika haraka haraka, na mkikaa kimiya nahisi mambo niliyoandika hayakuwafurahisha…lakini TUPO PAMOJA

Ni mimi: emu-three

1 comment :

Anonymous said...

Tupo siku-kuu, ndio maana unaona hatuandiki kitu, lakini tipo pamoja, vipi kuhusu mambo yako umepata sehemu au vipi mpango wa modemu?