Ilikuwa natembea, nawahi sehemu, sijui nilikuwa naelekea wapi,
Lakini yaonekana…kuna mvua, na jua kwa wakati mmoja,…
Lakini nina haraka sana, sijali mvua
hiyo au jua hilo…niliwapita watu na wengine wakikimbilia sehemu ili
wasilowane..kwahiyo tukawa tunapishana, bila hata kusalimiana, wengine
nawafahamu, lakini hata wao hawakuwa na habari na mimi, kila mtu anatafuta
usitiri wake asilowane, lakini cha ajabu pia jua linawaka.
Na mara nikaguswa na wimbo…
‘Matatizooo. Matatizo, sijui yatakwisha lini…mimi
mama mjane, na watoto wangu yatima…matatizo , matatizo sijui yatakwisha
lini…kila anionaye, hanithamini…watu wananipita kama hawanijui…matatizo, matatizo
sijui yatakwisha lini…’ilikuwa ni wimbo, wenye sauti ya huzuni. Wimbo ule, ...ukanifanya
nisimame.
Nikageuka kushoto hakuna mtu, nikageuka kulia..namuona huyo mama, kakaa huku kajikunyata,
kalowana, na watoto wake pia,..lakini jua lipo , nalo ni kali kweli, watoto
wanatetemeka baridi..jua,...kuna jua lakini haliwasaidii kitu…watoto wanalia…hakuna anayewajili.
‘Mama njaa…mama, tunalowana…’ilikuwa kilio cha
watoto, na mama anawaimbia wanawe…
‘Wewe mama toka hapo , mvua hiyo, itakupatia maradhi,
na hao watoto wanashikwa na homa..’nikasema na huyo mama akageuka, ..na
kuniangalia, huku anatoa machozi,
akasema. Machozi yana rangi, kutofautisha na maji ya mvua, ambayo ilikuwa kitengeneza mifereji usoni mwa huyo mama.
‘Wewe waongelea mvua…hulioni na hili jua, vyote hivyo ni
vyetu..ni nani atatusitiri sisi, kwenye mvua, na kwenye jua…ni nani atatusitiri
kwenye njaa na shida…hakuna, nyie mna haraka zenu, hamuwakumbuki watu kama
sisi, hata kinga ya mvua na jua, hatuna tena…’akasema na kuangalia watu wanavyokimbizana kutafuta sehemu ya kujikinga
na mvua.
‘Lakini huwaoni hao watu…wao wanahangaika kukimbilie kwenye kinga ya mvua…na wewe
fanya hivyo…’nikasema
Na yeye, kama kunionyesha, akainua mikono yake, hauinuki, kumbe kafungwa na mnyororo,
nikaona ajabu, kwanini afanyiwe hivyo..
‘Ni nani kakufunga hivyo..?’ nikauliza
‘Ni walimwengu…ni wanajamii…’akasema
'Oh..wanajamii, haiwezekani...'nikasema sasa najitutumua kumsogelea, ..kumbuka awali nilikuwa natembea kwa haraka...ajabu sasa nataka kwenda kwake, siwezi...miguu minzito, na sio miguu...mchanga, utelezi..mvua...
‘Oh..ngoja nije nikufungue…’nikasema nikijaribu
kumsogelea pale walipo, lakini mchanga, unanifanya nitembee kwa shida, maji…na
mara...
Kitu kikali kikinigonga kichwani kwa nyuma, ..na maumivu yake yakanifanya nisiweze
kuhimili nikadondoka…nikaanza kuona giza, huku yule mama akiendelea kuomba
msaada..sasa akisema;
‘Amuka…ukilala wewe ni nani atatusaidia, ukipotea
wewe ni nani atatusaidia,…kwanini nakutana na mitihani hii jamani…amuka , muka jamani...’sauti hiyo
ilinifanya niingiwe na nguvu, nikajitutumua, kichwa kinauma…maumivu makali..na
mara, nikahisi mwanga mkali ukipenya machoni..
Nikazindukana..lakini huku nalia...
‘Kichwa kichwa…’
‘Docta, docta, kaamuka, analalamika kichwa..'nikasikia sauti kwa mbali.
Ilikuwa suti iliyoashiria kuwa nipo mahali gani,
lakini akili yangu bado ilikuwa haijawa sawa, sijitambui, …naona watu marue rue, na hali hiyo ikaendelea na baadae ikawa sawa, nikawa naweza kuona vyema.
‘Nipo wapi, ooh, kichwa…’nikasema
***************
Nilizindukana na kujikuta nipo hospitalini, kichwa
kimewekwa bandeji kwa nyuma, niliangalia huku na kule, sikumuona mtu ..baadae
akaingia mama mjane…akiwa kaongozana na docta.
‘Oh, pole..unajisikiaje kaka..?’ akaniuliza na docta
akawa ananiweka sawa, akawa ananikagua kichwani.
‘Kwanini hutulii, umeona umejitonesha sasa…’akasema
docta.
‘Kichwa kinauma…’nikasema
‘Kwasababu umejitonesha, tulia hivi hivi…’akasema
akiniweka sawa.
‘Ni kosa langu docta, nilipitiwa na usingizi…’akasema
huyo mama.
‘Lakini ulikuwa unaimba…’nikasema
‘Umenisikia…?’ akauliza kwa mshangao
‘Nilikuwa naota…’ nikasema
‘Lakini niliimba muda, halafu nikapitiwa na usingizi,
nilipoamuka nikakuta unachezesha kichwa,…unalalamika, ..kichwa kichwa…’akasema.
‘Oh…’nikaguna hivyo na docta akawa ameniwekea dripu
ya maji,..na kusema.
‘Sasa tulia…ukitaka upone utulie hivyo
hivyo..’akasema docta na kundoka, nikabakia mimi na huyo mama mjane..
‘Watoto wapo wapi…?’ nikamuuliza.
‘Watoto…!!!, watoto wapo nyumbani…vipi kwani…?’
akaniuliza sasa akionyesha uso wa kushangaa…na kutulia kimia, nikiwaza hiyo
ndoto.
‘Kwani unajisikiaje sasa…?’ akaniuliza
‘Sasa kidogo, sijambo, ila kichwa bado kina maumivu
kwa mbali…nimefikaje hapa..?’ nikauliza.
‘Nasikia waliokuleta hapa hospitalini ni …askari…’akasema.
‘Askari, askari gani hao,…mi-mi nakumbuka, eeh,
kichwa kinauma, kwa nyuma,..ndio..nilipigwa na kitu kigumu kichwani, si ndio
hivyo….nikapoteza fahamu, si ndio hivyo....’nikasema nikitaka uhakika.
‘Nlivyoambiwa ni kuwa, hao maaskari walikuokoa,
ukitaka kuuliwa na mtu..lakini hawajasema ni mtu gani…’akasema
‘Mhh..ni huyo chizi nini..’nikasema.
‘Chizi, chizi gani…?’ akauliza
‘Mhh, hata simjui…’nikasema
‘Maana, kuna mtu namfahamu wanamuita hivyo. Chizi,
lakini ni msafi kweli, ..uchzi wake ni waajabu sana,…’akasema
‘Ni nani huyo..?’ nikamuuliza
‘Mhh, niliwahi kumuona mara moja,..huwezi amini kuwa
kachanganyikiwa, ila wanasema kikicharuka, inabidi watu wakimbizane, maana
anaweza hata kuua, analalamika, ‘moto, moto..’ nikama anaungua vile…’akasema
‘Oh…moto…?’ nikauliza hivyo.
‘Ndio , kwani unamfahamu…?’ akauliza
‘Kama ndio huyo,..basi ndiye nilikuwa namtafuta,
..’nikasema.
‘Wanini, kujitafutia matatizo, unaona
alivyokufanya…’akasema
‘Unajua…huyo ndiye anaweza kuwa ni msaada wa kesi
yetu…’nikasema
‘Umechanganyikiwa, mtu ni kichaa, ..atasikilizwa na
nani, na hata hivyo, yeye atautsaidiaje…?’ akauliza mama mjane
‘Kwanza niambie, huko baharini, ulikwenda kufanya
nini huko, ndio kumtafuta huyo chizi…..?’ akaniuliza mama mjane.
‘Oh…hata sijui,…itakuwaje,..’nikasema hivyo.
‘Jamani mimi nilishakuambia, haya yote yanayotokea,
yanatokea kwa mapenzi ya mungu,kama kapanga iwe hivyo, itakuwa hivyo, na yeye
akitaka, yote yatakwisha, sio kwa ujanja wetu, sio…sasa mpaka wanataka
kukua,,…’akasema mama mjane.
‘Haya...vipi wanasemaje kuhusu mnada..imefikia
wapi..?’ nikauliza bila kumjali maneno yake.
‘Mhh…sijasikia lolote kwa leo….jana ndio ilikuwa
wafike, lakini hawakutokea, japokuwa watu walifika kwa ajili ya huo
mnada..baadae nikasikia, wameahirisha , sasa sijui hadi lini, labda leo mimi
sijui, nimeshakata tamaa..’akasema
‘Mhh…usikate tamaa..nataka nionane na huyo mtu
tu…’nikasema
‘Jana ilibidi niache kila kitu, niliposikia kuwa
umeletwa huku hospitalini, …nikaja na kukuta kwenye hiyo hali..kiukweli nililia
sana, hata waliposema niondoke, sikukubali, nikasema nitakaa hapa hapa,…sasa
nikapitiwa na usingizi,..unisamehe tu…’akasema.
‘Ahsante kwa kunijali, dada yangu…’nikasema
‘Kwani mliponipigia simu, …ukaniuliza ..nikakuelezea
nilivyota, majinamizi, mlikuwa mnafanya nini,…?’ akaniuliza
‘Mhh…sijui…kwa mara ya mwisho niliongea na mpelelezi,
akasema anafuatilia kuhusu kuzuia huo mnada usifanyike, lakini walikosa
ushahidi wa kuweka pingamizi,..ndio nikawa nafuatilia, nipata huo ushahidi,…sasa
siwezi kuwa na uhakika,..nahisi kuna kitu kimetokea, vipi watoto lakini…?’
nikauliza
‘Hawajambo, zaidi ya…hilo tukio..hakuna
kibaya…’akasema alionekana kama ananificha kitu.
‘Docta yupo wapi, ,maana kuna jambo muhimu ni lazima
nilifuatilie,..kabla hawaja….mhh...kichwa jamani, hakitaka nifikiria jambo,
sasa kinaanza kuuma tena.., sijui walinipiga kwa nyundo,..lakini ni lazima
nionane na huyo mtu…’nikasema.
Nikawa nataka kama kujiiunua
‘Unataka kwenda wapi, na hali hiyo…’ sauti ikatokea
mlangoni
***********
Ilikuwa ni sauti ya mpelelezi. Nilitaka kujiinua
nimuangalia lakini kwa jinis nilivyolala, nikashindwa.
‘Mtu wa jamii…hahaha, umeionja joto ya jiwe eeh…,
nilikuambia hizi kazi zina wenyewe, ukajifanya na wewe mpelelezi…hahaha, pole
sana…, je nisingelifika kwa wakati muafaka, unafikiri ingelikuwaje…’akasema.
‘Ulifika tu, kwa mapenzi ya mungu, wala sio kwa ujanja
wako afande..hata hivyo nashukuru sana kama ni wewe ulini-okoa, ilikuwaje
kwani, na huyo jamaa aliyefanya hivi ni nani, alitaka kuniua, au…?’ nikauliza.
‘Hahaha, haya bwana, ni mapenzi ya mungu kweli…maana
huyo jamaa alidhamiria kukua kweli…nilimuwahi kwa risasi,…’akasema.
‘Ina maana umemuua…oh , sasa si umehribu ushahidi
wote..?’ nikauliza.
‘Hapana, sikutaka kumuua, nilimjeruhi mkononi, akiwa tayari anataka kukutwanga
nyundo ya pili kichwani..nisingelifanya hivyo, sasa hivi ungelitw jina jingine…’akasema.
‘Oh…ina maana kweli alikuwa na lengo la kuniua..ni
nani huyo lakini..?’ nikamuliza.
‘Wewe ulikuwa
unakwenda kuonana na nani kwani..?’ akaniuliza swali bila kunijibu swali langu.
Na ili kuwaza kidogo, kichwa kikaanza kuniuma.
‘Mhh…kichwa kinauma sana afande…lakini lazima
nitoke,..nataka nitoke , docta yupo wapi kwani, muda unakwisha au, unakumbuka
wanataka kuufanya huo mnada…’nikasema nikijaribu kujiinua.
‘Unataka kwenda wapi wewe…sikiliza, huyo mtu
uliyekuwa ukimfuata, keshapatikana kama ndio yeye unayetaka kwenda kuonana
naye,…’akasema na mimi hapo nikabakia kimia.
‘Tumempata …’akasema kwa msisitizo bila kumtaja huyo
mtu.
‘Ndio nani huyo, maana sikumbuki kukuambia ni nani
nilikuwa namfuata..?’ nikamuuliza.
‘Si ndiye huyo uliyekuwa ukimfuata,…ameniambia yule
mlinzi wa pale hospitalini…na na ndio nikajua umeelekea wapi…’akasema.
‘Kwani ilitokeaje hadi huyo mlinzi akakuambia, maana
nijuavyo, wao hawakutaka kuliongelea hilo,..?’ nikamuuliza
‘Kuna mambo niligundua wakati nimekuacha pale uondoke,
nilitaka kuwafahamu watu wa zamani wa humo…nikagundua kuwa mmojawapo ni huyo
mlinzi na yule mdada wa mapokezi…nilipomuuliza mlinzi, akasema nimemuuliza
maswali kama uliyomuuliza wewe…na ndio akaniambia wewe umemfuatilia huyo
‘chizi’ na mtu huyo hafuatiliwi ovyo.
‘Oh…lakini kitendo cha kumuhoji,..mpaka kufikia hapo,
ilichukua muda, au sio…hadi kuamua kunifuatilia na kufika kwa wakati muafaka..naona
kama…’nikasema bila kumalizia.
‘Nilichukua pikipiki, nikitaka nikuwahi….wewe
ulitumia usafiri gani,…?’ akaniuliza
‘Bajaji…nilikodi bajaji…likaniacha mbali kidogo na
ufukweni…, nikawa natembea nikiitafuta hiyo sehemu…, sikutaka huyo mtu
anishuku…’nikasema.
‘Ndio maana nikafika wakati muafaka kwa pikipiki…’akasema.
‘Kwahiyo huyo aliyeniumiza mimi kichwani ..ndio huyo
Chizi…?’ nikauliza.
‘Hapana…’akasema na kunifanya nibakia na mshangao
‘Sasa ni nani huyo…?’ nikauliza
‘Unajua yaonekana huyo mtu kwa muda mwingi alikuwa
akikufuatilia, kila unapokwenda, na hukuwa makini kwa hilo…’akasema
‘Haiwezekani,…ni nani huyo anifuatilie…?’ nikauliza
‘Huwezi amini , ni babu yako….’akasema.
‘Mzee mtupe, kwa nini afanye hivyo ..?’ nikauliza.
‘Ni hadithi ndefu, wewe malizana na matibabu, maana
hivi sasa sisi tunakimbizana na watu wa benki, leo ndio siku yao ya mwisho,
tusipowakilisha ushahidi wetu, basi, hakuna jinsi, ni lazima mnada ufanyike….’akasema.
‘Kwahiyo ushahidi mnao, au....?’ nikauliza na huyo
mpelelezi, akatabasamu tu, na muda huo akaingia docta,, akingia na mwingine na
kigari cha kukukota
‘Tunataka kumchukua mgonjwa wetu, tunaomba
mtoke…’akasema docta
‘Kunichukua kwenda wapi..?’ nikauliza
‘Chumba cha upasuaji…’akasema docta
Hapo nikaanza kuhisi vibaya, ni heri
wasingeliniambia, nikahis huenda tatizo hilo ni kubwa sana…labda kichwa
imepasuka hadi kuathiri ubongo..nikawa nawaza sana.
‘Usiogope…hilo tatizo sio la ndani…’akasema docta
‘Oh, sasa kwanini upasuaji…?’ aliyeuliza ni mama
mjane.
‘Samahanini, naombeni mtoke nje…’akasema docta,
akiwaambia mpelelezi na mama mjane, na
wawili hao wakatoka nje.., kiukweli sikuwa na amani kabisa…niliona nina jukumu
kubwa la kufanya.
‘Docta, kwani haya maumivu hayawezi kupata dawa,
yakatulia, ili nikafanya kazi moja muhimu sana, kwanini mpaka nifanyiwe
upasuaji, kuna nini , niambieni…?’ nikamuuliza
‘Kuna tatizo kidogo…kuna damu zimevilia kwa ndani..ni
kidogo tu, kwa juu, , tunahitajika kufanya upasuaji kidogo…ni sehemu nyeti,
tukiachia hivyo, inaweza kulete matatizo..’akasema na muda huo tulishafika
chumba cha upasuaji.
‘Nini…haiwezekani docta..hapana…hamuwezi kuahirisha,
mimi nina ushahidi muhimu wa mahakamani, nisipokuwepo, kesi …tutashindwa na
haki za watu zitapotea bure, hao wapelelezi hawajui kitu bado…,’ nikasema na
sikuweza kumalizia, mara nikazama kwenye usingizi mnzito , kumbe alishaweka
dawa ya nusukaputi.
**************
Ilikuwa sasa nipo chumba cha wagonjwa wa
kawaida,..bahati nzuri siku hiyo alikuja mpelelezi kunitembelea….tukasalimiana,
baadae akasema
‘Leo tunakueleta mgeni maalumu …docta anasema hali
yako ni nzuri, ila bado huwezi kupewa ruhusa…’akasema
‘Mgeni gani..lakini kwanza nataka kujua
kinachoendelea,…?’ nikauliza
Na wakati huo mpelelezi alikuwa akiangalia mlangoni,
kwani mlango ulifunguliwa, na wakaingia askari wawili wakiwa wamemshikilia
jamaa kati kati…huku kafungwa mnyororo…huku na huku…
‘Aaah…naumia ..naumia, nitasema ..nitasema kila
kitu…’huyo jamaa akawa analalamika , akionyesha dalili za kupata maumivu, na
aliponiona tu, akaacha kulia, na kusema;
‘Ni wewe….hahaha…aaah,…ila..ooh, naumia jamani, wewe ndio tiba yangu ,unaona
sasa nafuu, ..aah, imeanza tena,…, hapana,…niacheni, .. nisamehe..nisamehe..ni
kweli..ni mimi, ni mimiii…’jamaa akawa anahangaika, lakini askari wake
walimshika imara, huku wamemfunga na mnyororo.
‘Vipi mbona mnamfanya hivyo,..hamuoni kuwa
mnamuumiza…’nikasema.
‘Tukimuachia hapa, ataumiza watu….na tumemleta hapa
kwasababu anasema bila ya kukuona wewe na mama mjane, hataweza kupona, nyie
ndio tiba yake….’akasema.
‘Kwanini….mbona mimi simjui huyu mtu, …kwani yeye ni nani …?’nikasema, nikiuliza.
‘Mimi nakujua sana wewe, nakujua, akufahamu,
nakuelewa, na najua unachokitaka…niakuambie, hapo ulipo unawaza nini…unajiuliza
mimi ni nani, au sio, hahaha, najua mimi kweli si kweli……’akasema akihema kama
mtu aliyekuwa anakimbia, sasa akiwa kanikodolea macho.
‘Uliniona wapi..?’ nikamuuliza nikionyesha ishara ya
mshangao.
‘Siku ya kwanza ulipofika kwa mama mjane, mimi
nilikuona, unajua, ulifika, kwa mapenzi ya mungu, ila mimi nikajua..…hahaha na
mama mjane…, mama mjane yupo wapi sasa…nimewaambia nini…?’ akauliza
akimuangalia mpelelezi,
Mpelelezi.. akasema
‘Muiteni mama mjane aingie ndani…’akasema mpelelezi.
Mara mama mjane akaingia…alionekana alikuwa analia…nikataka
kumuuliza analia nini, lakini huyo mjamaa akaniwahi
‘Mama mjane…haaaa …nisamehe jamani…’, sasa akawa kama
anamfuata huyo mama wale maaskari, wanaonekana wana nguvu, walivyojazia, ..
wakawa wamemshikilia imara. Nilitamani kuwaambia wamuachilie tu, lakini huenda ni kwa usalama. Baadae huyo mtu
akanigeukia,…
‘Wewe mimi nakufahamu sana…, nilikuona, kila siku
mimi nakuona,…ulivyojiingiza kwenye mambo yasiyokuhusu…ungeshakuwa maiti wewe….hahahaha…
ila..hahaha, wewe ni mjanja , unajua mimi mungu kanipatia kipaji, cha kuona
hata visivyoonekana, na kusikia, saana,
lakini sasa..’akageuka kumuangalia mama mjane, halafu mimi..
‘Nimegeuka kuwa shetani…nimevitumia vibaya…sasa
nakula jeuri yangu….hahaha, jamani,….mama mjane nisamehe…sina uwezo tena, wa
kumrejesha….duniani, oooh, nitakwenda kukutana naye…nina uhakika atanisamehe….khaaah,
…khaaah…’akawa kama anakabwa, na mdomoni kunatoa damu.
Baadae akatulia.. docta akachukua kitambaa na kumfuta
mdomoni, na akawa kama hataki, baadae docta, akamuacha, jamaa akasema;…akiniangalia
mimi…
‘Wewe kwa mara ya kwanza nilikuona, ukiingia kwa mama
mjane nikajua wewe utakuwa ni adui yangu namba moja, wewe ni mjanja sana, ,
…hahaha, hapana nitasema,…kila kitu, msiniunguze jamani… naungua, moto,
moto…haah, msininunguze nitasema..’akawa analalamika hivyo kuashiria anateseka kweli...
‘Mama mjane…naomba unisamehe..’akasema akimuangalia
mama mjane ambaye alikuwa kimia, kakaa pembeni ya kitanda, nilicholala mimi…,
nikamuangalia mama mjane, mama mjane alikuwa akimuangalia huyo jamaa kwa uso wa
huruma…chuki, machozi yanamtoka…hata huwezi kujua lipi ni lipi.
‘Najua nimewakosea sana…kwa ujumla wenu,…nawaombeni
mnisamehe, ili nife kwa amani…sistahiki kuishi tena …mimi sio binadamu wa
kawaida,..mimi ni shetani…’akasema akionyesha meno nje.
‘Mhh, haya niambie,..kama kwa kuniambia hayo
unayotaka kunieleza inaweza kusaidia ….wewe kutokupata taabu hiyo uliyo
nayo…maana bado mimi sijajua unataka kuniambia nini, na kipi kilichokusubi, na
wewe ni nani…..je ni kuhusu deni la marehemu.’nikasema, na kuuliza.
‘Wewe ulinifuata nini kule ufukweni, kwanini, eeh,
ulitaka ninywe damu yako, nimechoka kunywa damu za watu, eeh, niambie wewe,..…eeh,
?’ akaniuliza akinikodolea macho
‘Ina maana ni wewe …’nikakatisha maana niliona
akitolea macho kama kaona kitu cha kutisha..halafu ghafla…
‘Hahahaha…eti wao wananiita mimi nani vile.....mimi sio hivyo, wanavyoniita, hawa wanaonitesa sasa ndio mizimu halisi...ndio nyie ndio halisi...yaah, ni kweli , mimi ni …ni
mtaalamu, ndio jamani ndio mimi...'akatulia kama anasikiliza
'Ndio, nawaambia kuwa…mimi ndiye mtaalamu halisi,..hahaha, …ni ni…ba-ba-bu, mimi sina baba,
yeye si alinikataa,....ndio...ba-ba-bu... mlitaka mimi nifanye nini sasa…hahaha,….niache, haya niunguzeni
nife kabisa..., kwanini mnanitesa hivi,….ni ba-ba, mbona hamsemi ma-ma, alimfanya nini
mama, ndi-ndio…….…hahaha, …hahahaha…hahaha…’jamaa, akaendelea kucheka kucheka,
kucheka…mpaka anaishiwa nguvu.
Ikapita muda, ..jamaa akafungua macho, mdomo, upo
wazi kwa jinsi alivyokuwa akicheka, nikama mdomo umaganda…hauwezi kurejesheka
tena.
‘Ndio hivyo, anateseka kweli…’aliyesema hivyo alikuwa
ni mpelelezi
Docta akasogea pale na kujaribu kuufunga mdomo wa
huyo jamaa, akawa anaukwepesha huyo jamaa, na docta akafanikiwa kuufunga huo
mdomo, jamaa sasa akawa anajinyonga nyonga kuashiria maumivu…
Ukimuangalia utamuonea, huruma nikaona nipoteze
mawazo, nikamgeukia mpelelezi..
‘Sasa ..mumefikia wapi…?’ nikauliza
‘Hawawezi kushinda hiyo kesi bila ya mimi….nimewaambia….haaah,
hapana, nitasema kila kitu..yayayaya, naungua jamani….nitasema, ndio..wapi,
mahakamani, ndio..nitasimama, na nani, …mtaalamu, …kafa ndio…nimebakia mimi, na nani, hapana hahusiki...nani, ba-ba-bu…ndio
mleteni, na nani mwingine,.haya, nitasema, nipeni nafasi hiyo,..yaaah, siwadanganyi tena,..sawa...sawa...ndio..aakkaaaaa …hahaha, ..’sasa akawa anajinyonga,
..na ghafla, akatulia, akalegea,…anataka kudondoka, ikabidi wamshikilie…
Ikapita muda, jamaa sasa wanashindwa kumshikilia huyo
jamaa, maana kalegea..docta akamsogelea, akamshika kumpima….akasema;
‘Kapoteza fahamu…’akasema docta
NB: Ni NINI HIKI TENA…
WAZO
LA LEO: Ogopeni sana duwa ya mwenye kudhulimwa, ole wenu,…yule
anayemdulumu mja wa mungu, …huwezi jua ni nini kisasi cha duwa hiyo
kitakuandama, na mola wetu, huwa anatupatia nafasi nyingi sana za kutubia,
lakini tunapuuzia, tunajiona sisi ni wajanja…Haah, ujanja kwa jasho la mtu,
ujanja kwa haki ya mtu,…halafu unadhulumu hata mayatima,…
Tumuombe mola wetu, atuongoze kwenye njia sahihi,
tuwe waadilifu, tuishi kwa jasho letu, …
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment