Tuesday, September 4, 2018

YOTE NI KWA MAPENZI YA MUNGU-42


Ilikuwa siku ya kesi, ni kesi ya kuamua kama pingamizi la kusitisha  mnada likubaliwe au la,….na hakimu alikuiwa mkali kweli, kutokana na kesi ya kwanza ilivyokuwa, watu wanafika mahakamani hawana ushahidi.

Watu wa benk walikuwa wanashinikiza kuwa mnada ufanyike kwa vile walipaji hawana uwezo wa kulipa tena, au wamepuuzia,…

‘Sisi tunachotaka ni hayo madeni yalipwe, na wadaiwa wanapoteza muda bure tu, maana kila kitu kipo wazi, ushahidi wote tulishauonyesha hapa mahakamani kwenye hukumu ya awali, tatizo ni kuwa, bado wanafikiri kuwa deni hilo, au madeni hayo hayakuwa ya marehemu, hayo madeni yana ushahidi,...kila moja lina kumbukumbu zake kisheria,.. na tatizo ni kuwa, hayo madeni yamekaa muda mrefu, hatuwezi kuvumilia tena…’akasisitiza wakili wa benk.

‘Sasa kwa vile inavyoonekana wadaiwa hawana jinsi ya kulipa hayo madeni, tunaomba kwako Muheshimiwa hakimu, tuendelee na taratibu za mnada, pingamizi lao halina nguvu, kwa vile wao hawana ushahid, ushahidi wa kimaandishi,...wanachofanya wao ni kupoteza muda ..’akasema wakili wao.

Wakili anayetetea watu wanaodaiwa akasimama na kusema;

 ‘Muheshimiwa hakimu,…hatujafika hapa kupoteza muda, ..na tuna uhakika mwisho wa siku haki itatendeka, maana sisi tunatetea haki zao za watu waliodhulumiwa, na madeni wanayodaiwa  sio haki ya wadaiwa,..’akasema wakili upande wa wanaolalamika kuwa madeni sio haki yao.

Miongoni mwa wanaolalamika, ni mama mjane, ..ambaye inasadikiwa , kutokana na ushahidi wa benki, mumewe alifariki akiacha deni nyuma yake. Na hilo deni limekaa muda mrefu bila kulipwa!

‘Ndugu muheshimiwa hakimu… benki wanataka madeni yao yalipwe, lakini hawataki kuangalia uhalali wa hayo madeni , tumejaribu kuwaomba tushirikiane nao, ili tuone huo uhalali, lakini imekuwa ni vigumu sana, wanadai wao wana uhakika kuwa hayo madeni ni halali kwa wadaiwa, na sisi tumegundua kuwa, hayo madeni sio halali kwa wadaiwa…’akasema

‘Uhalali kwa vipi, mbona vidhibiti, nyaraka, mikataba ipo, na kila kitu kipo sawa, ulitaka sisi tuhakiki kivipi, je awali kesi ilipofanyika, watu wenu hawakuviona hivyo vidhibiti, waliona ushahidi wote ikiwemo mikataba, je sahihi, na hiyo mikataba sio halali..?’ akauliza wakili wa benki.

‘Hivyo vidhibiti, au nyaraka, vina walakini..’akasema wakili mtetezi.

‘Walakini gani, je mahakama iliyopitisha hukumu haikuona hilo tatizo,..?’ akauliza wakili wa benki.

‘Tutakuja kuliona hilo tatizo, hapa mbele ya mahakama, na kitu cha kujiuliza, ni kwanini  haya madeni yote wanaodaiwa ni  marehemu, nyie kama benki kwanini hamjiulizi hilo swali…’akasema wakili anayetetea wanaodaiwa. Na hapo wakili wa benki akasema;

‘Kwenye madeni haijalishi huyo mdaiwa ni marehemu au yupo hai,…ndio maana wadaiwa waliweka dhamana, dhamana maana yake ni nini, kama itatokea mdaiwa hawezi kulipa, basi dhamana hiyo ndiyo italipa hilo deni, ikitokea mdaiwa kafariki, dhamani hiyo ndio inalipa hilo deni, ni utaratibu wa kawaida tu..’akajitetea wakili wa benki.

‘Sawa…lakini kwa kukumbusha tu, hebu turejee miaka ya nyuma wakati benki yenu ilipokumbwa na tatizo la wafanyakazi wasio waaminifu, …benki yenu iliwafukuza wafanyakazi karibu wote, ambao mliwashuku kuwa ndio chanzo cha tabia hiyo chafu… ‘akasema wakili na wakili wa benk, akaingilia kati na kusema;

‘Hilo ni jambo la kawaida, kwenye taasisi, au kampuni, watu kama hao hutokea,..benki au kampuni yoyote inaweza kuwafukuza wafanyakazi wake hata wote..kama hao wafanyakazi sio waadilifu, lakini taratibu za kikazi zipo pale pale, maana kumbukumbu zipo…’akajitetea.

‘Ndugu wakili …ni zamu yangu kutoa maelezo, usiwe unaniingilia,…nataka kuelezea, mkasa huo ulivyokuwa, hadi watu wasio na hatia kupewa madeni yasiyo haki yao…’akasema wakili na hakimu akasema aendelee, na wakili mwingine atulie.

‘Na ukiangalia lini madeni hayo yalitolewa , utagundua ni kipindi kile benki hiyo ilikuwa na matatizo, hiyo  benki ilikumbwa na kashfa nyingi, … na muda huo mtandao wao wa kimahesabu, uliharibika…, kwanini uliharibika , na kwanini hawataki kuliweka hilo wazi , kwasababu wanafahamu kuwa walioharibu huo mtandao wao ni hao watu waliowafukuza...’akasema

Wakili wa benki akataka kuoingea, na alipoona hakimu hamruhusu, akaanza kuongea tu.

‘Sio kweli, mtandao kuharibika sio sababu ya kuharibika kwa kumbukumbu za kikazi,.. kumbukumbu zote za kuambatatisha madeni hayo zipo, …na mtandao kuharibika sio kupotea kwa ‘data’..na ukiangalia, pamoja na kuharibika kwa baadhi ya nyaraka, lakini kumbukumbu za madeni ambayo yalihakikiwa, bado zipo, na yana nyaraka zake zote, yale ambayo hayana nyaraka stahiki, tuliwaita tukakubaliana…’akasema.

Wakili wa utetezi wa madeni, akasema;

‘Tuna ushahidi wa kutosha kuwa madeni hayo yote, yalikuwa ni mbinu za wafanyakazi wenu mliowafukuza kazi…na uzuri wake, wengi wao bado wapo hai….’wakili aliposema hivyo, wakili wa benki alitoa pingamizi akitaka kuingilia kati, na hakimu akasema;

‘Mnaweza kuutoa huo ushahidi…?’ akauliza hakimu

‘Ndio muheshimiwa hakimu, tunao ushahid wa kutosha…’akasema wakili

‘Leteni huo ushahidi…tusipoteze muda mwingi, maana kesi hii ilishatolewa hukumu, na kilichosababisha hukumu kutolewa kwa masilahi ya benki, ni nyie wadaiwa kutokuwa na ushahidi wa malalamiko yenu…sasa je mnao huo ushahid wa madai yenu, kuwa hayo madeni sio halali kwenu..?’ akauliza hakimu.

‘Tunao  ushahidi huo muheshimiwa hakimu…’akasema wakili

‘Leteni huo ushahidi wenu…’akasema hakimu.

‘Ushahidi wetu upo kwa kupitia mashahidi….’akasema na wakili. Hapo wakili wa kutetea benki akaingilia katu na kusema;

‘Muheshimiwa hakimu, tatizo ni lile lile kama ilivyokuwa awali, watu hawa wanapenda kuongea tu, bila kutoa stakabadhi, au kumbukumbu za maandishi, sisi kama benki hatuwezi kukubali maneno matupu, na nina shaka kuwa hao mashahidi watakuwa wametengenezwa tu…’akasema wakili huyo.

‘Kama nilivyokwisha kutangulia kuelezea, kumbukumbu za kibenki walizo nazo zina walakini, na uwalakini huo unatokana na hao watu waliokuwa wakifanya kazi kipindi hicho, na ndio maana tunataka wao wenyewe walithibitishe hilo, kuwa kweli ni wao walitengeneza hayo madeni…’akasema na hakimu akasema kwa mshangao.

‘Wao wakubali kuwa ni wao walitengeneza hayo madeni, kwa vipi, yawezekana kweli, msije mkawa mumewatesa ili wake kutoa ushahidi kama huo..?’ akauliza hakimu.

‘Wao wenyewe kwa ridhaa yao, …wengien wamesema ni kutokana na imani yo kuwasuta, kwa vile walitenda, na dhuluma imewafanya wajisikie vibaya,…dhuluma imewatesa wao wanyewe, kwahiyo sasa wanataka kukiri mbele ya mahakama yako tukufu, na kama mtu kateswa, yupo huru kusema …’akasema wakili.

‘Muheshimiwa hakimu, umesikia alivyosema, …ina maana hao watu kama watakiri, basi ni kutokana na mateso waliyoyapata, hayo mateso ni mateso gani, na tunakataa kauli ya wakili huyo, ..sio kweli kuwa kumbukumbu hizo zilitengenezwa, maana zina vitu muhimu vya kuthibitisha, zipo sahihi, na lipo dole gumba…’akasema wakili.

Alipoongea huyo wakili wa benki, wakili wa utetezi…akatabasamu kidogo, halafu akasema;

‘Ukweli wote utajieleza, usiwe na shaka na hilo, tatizo la benk walijua hao marehemu wameshafariki, kwahiyo hakuna mtu wa kuja kuwatetea,..na pia walijua hawataweza kupatikana..’akasema wakili wa kutetea madeni.

‘Haya waite hao mashahidi, lakini pia tunahitajia kumbukumbu za kimaandishi…’akasema hakimu.

Waliitwa mashahidi baadhi ya wafanyakazi wa benki…ambao, walitakiwa kutoa kauli yao kuhusiana na hali ya benki ilivyokuwa kipindi hicho, na wengi wao waliwanyoshea kidole, viongozi wa vitengo waliokuwepo kipindi hicho…, baadae ikaja zamu ya mzee mtupe..

Mzee huyo alifika akiwa kafungwa mkono,..kuonyesha kuwa ana jeraha … na swali la kwanza likawa;

‘Mzee, umefanya nini huo mkono wako…?’ akaulizwa.

‘Niliumizwa kwa risasi…’akasema.

‘Na nani…?’ akaulizwa.

‘Na polisi…’akasema , na aliposema hivyo wakili wa benki akacheka na kuonyesha ishara kuwa, ‘mnaona’

‘Kwasababu gani, polisi walikupiga risasi huo mkono wako…?’ akaulizwa.

‘Nilikuwa natimiza wajibu wangu wa kumlinda mtu aliyeniajiri…’akasema

‘Wewe ni askari…?’ akaulizwa

‘Sio lazima mtu awe askari ndio afanye hiyo kazi, hata hivyo, niliwahi kuwa askari enzi zangu, kama unataka kuhakiki ubora wangu wa kikazi,…niliwahi hata kupigana vita vya Idd Amini, niliporejea nikaacha kazi, kwasababu za kiafya…’akasema

‘Kwahiyo hiyo kazi ya ulinzi, uliipewa kwa vile unajua jinsi gani ya usalama wa mtu, au sio..je sheria za kazi hiyo inazifahamu..?’ akaulizwa.

‘Ndio, nazifahamu sana, lakini ningeishije…ndio niliacha kazi kwasababu ya afya, lakini maisha yangu yalikuwa magumu sana,  sina ujuzi, zaidi ya ujuzi wa kijeshi..na nataka niishi, …naeleza haya, ili mnielewe kuwa hayo niliyoyafanya sio kwa kupenda, ni hali halisi ya maisha…’akasema.

‘Unacho kibali cha kuifanya hiyo kazi, ya kumlinda huyo mtu uliyekuwa ukimlinda, unayo leseni …?’ akaulizwa.

‘Ndio ninacho kibali…na mwajiri wangu ana barua ya mkataba wa kumlinda, kwahiyo niliifanya hiyo kazi kwa mujibu wa mkataba…’akasema akitoa vielelezo vyake.

‘Kabla ya kufikia kumtaja huyo bosi wake ni nani, ngoja tuhakiki, baadhi ya ubadhirifu wa watendaji, ambao walipewa dhamana, lakini hawakuweza kutimiza wajibu wao,…’akasema wakili

‘Lakini je huo ubadhirifu kama ulivyouita, unahusiana na hilo deni, inahusiana na kesi yenu..?’ aliyeuliza sasa ni hakimu

‘Ndio muheshimiwa hakimu, tunakwenda hatua kwa hatu, kuhakiki ukweli wa madai yetu…’akasema wakili..

Vielelezo vile vilipitiwa, na vilivyofikishwa kwa wataalamu wa kazi hiyo ambayo wanatoa vibali, muhusika wa kutoa hivyo vibali,  akasema;

‘Vielelezo hivi ni halali, lakini vilitolewa kimakosa…’akasema

‘Kwa vipi hebu tuelezee…’akaambiwa

‘Aliyevitoa vielelezo hivi ni mmoja wa watu waliofukuzwa kazi kwa tabia hiyo chafu ya kutoa vibali, kimakosa, kwasababu mbali mbali, na moja ya vibali vilivyogunduliwa kuwa vilikuwa na makosa ni hiki hapa..hata kwenye kumbukumbu zetu za ofisini utaliona hilo…’akasema muhakiki wa hivyo vibali.

‘Sasa tutamleta huyo aliyetoa vibali hivyo, ili uhakika ukamlike..’akasema na wakili wa benki akapinga kuwa hilo haliendani na kesi husika,  hakimu akamuangalia mtu wa benki, kwa makini, halafu akasema

‘Hebu mleteni tuone huo ukweli wake, tunataka kuhakiki hiyo shutuma…’akasema hakimu.

Hakimu alipsema hivyo, wakili wa benki, akawa analalamika,  akidai kuwa hilo sio kosa la mshitakiwa, kwani yeye alipewa vibali hivyo kihalali, sasa kama mtoaji katoa kimakosa sio kosa la mtuhumiwa. Na ushahidi huo hauendani na kosa linalozungumziwa…

Hakimu alishapitisha kuwa shahidi huyo aitwe…

‘Ngugu muheshimiwa hakimu, nataka kuionyesha mahakama yako tukufu, kuwa kesi hizi zimekuwa zikikwama kutokana na watu waliopewa majukumu yao, kutokuwa wadilifu…taratibu zinafuatwa, lakini kwa hila…mtoa kibali anatoa kibali kwa masilahi, binafsi,au nyaraka zinatolewa lakini zimegushiwa…tutakuja kuliona hilo..’akasema wakili

‘Na kutokana na hilo, wenye haki zao, wameshindwa kesi, na kesi mojawapo ndio ya mama mjane, na wengine ambao wana madeni ya ndugu zao, na ndugu zao hao ni marehemu,…mama mjane mume wake, aliambiwa alindoka akiwa kaacha deni lililosadikiwa ni la mume wake, lakini sio kweli, hizo ni njama zilizotengenezwa kiujanja kama tutakavyokuja kuoonyesha hatua kwa hatua…’akasema wakili.

‘Mnao ushahidi wa kimaandishi…’akauliza wakili wa benki

‘Tutakuja kuuona bila shaka…’akasema wakili anayetetea wanaodaiwa.

‘Kutokana na  watendaji wabovu, …taasisi iliyopewa kukusanya madeni, imekuwa akitumia vibali hivyo,, vielelezo hivyo, nayaraka hizo,…ambazo zilitengenezwa kwa hila, udanganyifu,.na kugushiwa kitaalamu...’hapo wakili wa benki akaweka pingamizi, kuwa wakili huyo anatoa kauli za kashifa athibitishe maneno yake hayo.

‘Ndugu muheshimiwa hakimu,  tutamuita mmoja wa kutoa vibali hivyo, athibitishe haya, aliyekuwa mtoa vibali vya walinzi binafsi…’akasema na wakili wa benk akapinga, akisema huyo mtu atasema kwa vile alifukuzwa kazi,na huenda atasema hivyo kwa shinikizo, kwa kulipiza kisasi tu, na..hata hivyo mambo ya ulinzi yanahusiani vipi na hilo deni.

‘Ngoja tumsikilize kama kweli anafanya hivyo kwa kulipiza kisasi au la..nia ni kuhakiki hayo madeni, lakini hayo madeni yalitengenezwa na kundi la watu…wakili, usiwe na shaka na hilo, hapa naanza kukuonyesha madeni hayo yalivyokuwa yakitayarishwa, na nani sasa…’akasema wakili.

Hakimu akataka kumsikia huyo mtendaji atasemaje, ikabidi huyo mtendaji aitwe kutoa ushahidi…huyo jamaa alipoitwa, kila mtu alishikwa na butwaa..

‘Jina lako ni nani…?’ akaulizwa

‘Mimi naitwa Mkwatue..bin…’akataja jina la baba yake.

‘Baba yako anafanya kazi gani..?’ akaulizwa

‘Alikuwa mganga wa kienyeji…’aliposema hivyo watu wakacheka, hakimu akagonga rungu lake kunyamazisha watu.

‘Kwa jina maarufu alikuwa anaitwa nani…?’ akaulizwa

‘Mtaalamu…’akasema, na watu wakacheka,..

‘Haya hebu tuambie..wewe ulipokuwa umeajiriwa kazi yako ilikuwa ni nini…?’ akaulizwa

‘Kazi yangu ilikuwa kutoa vibali vya walinzi, walinzi jamii, walinzi ambao wanawalinda watu, kwa sababu mbali mbali…’akasema

‘Je wewe kipindi hicho, uliwahi kutoa kibali kwa huyo mzee Mtupe…?’ akaulizwa

‘Ndio muheshimiwa…’akasema

‘Ulitoaje, …?’ akaulizwa

‘Alifika na maombi yake ya kutaka kibali, kibali chake hakikupitia kwa wengine kama ilivyokuwa kawaida,..hata hivyo, ni nani angelipinga hilo,..mimi mwenyewe nilipitisha sehemu zote hadi mezani kwangu...'akatulia

'Kwanini ulifanya hivyo..?' akaulizwa

'Nia ni mzee afanye kazi yake kihalali...'akasema

'Kihalali...?' akaulizwa

'Ndio kama, ana hicho kibali, basi kazi yake ni ya halali, au sio...'akasema

'Kwahiyo wewe ndiye mtu wa mwishi wa kuidhinisha hicho kibali, ?' akaulizwa

'Ndio, hata ukiangalia hivyo vibali kuna sahihi yangu...'akasema.

'Hayo maombi yalipofika kwako wewe ulifanya nini..?' akaulizwa.


'Nifanye nini, maana sio kitu kigeni kwangu,, niliweka sahihi yangu sikuwa na haja ya kuhakiki,kwa vile mimi nilishafahamu ni kibali cha nani na kwanini…’akasema

‘Ulishafahamu kwa vipi…?’ akaulizwa

‘Tulipanga na wenzangu…’akasema na watu wakagunda

‘Je nyaraka hizo zilikidhi masharti yote…?’ akaulizwa

‘Mhh…kiukweli sikujali hayo,…nilipitisha tu, kwa vile yeye ni babu yangu, ..’akasema

‘Babu yako…babu yako kwa vipi?’ akaulizwa.

‘Ndio ni babu yangu, ….mzee mtupe, alizaliwa tumbo moja na baba yake baba yangu…’akasema

‘Baba yake baba yako, ..ukiwa na maana baba yake mtaalamu au sio, na kwahiyo mzee mtupeo kwako, ni babu yako, au sio..?’ akaulizwa

‘Ndio muheshimiwa…’akasema, wakili akacheka, akimuangalia wakili wa benki ambaye alionekana kushikwa na butwaa.

‘Unaona hii ni familia iliyojipanga,…hapo sasa mtoto, baba , babu… na walihakikisha udugu wao hautambulikani, kwanini walifanya hivyo...kuna jambo limejificha hapo...na je ni nani alikuwa anajua hilo, kuwa mzee mtupe ana udugu na mtaalamu, hawa watu walikuwa hawaivani, au sio, ilivyoonekana kwenye jamii…?’ akauliza na watu wakaguna, na wengine wakasema

‘Hakuna…aliyejua,...’akasema na hakimu akainua rungu akitaka kuligonga, lakini hakufanya hivyo, akawa anamuangalia huyo shahidi na mzee mtupe.

‘Swali kwanini walifanya hivyo…hayo tutakuja kuyaona huko mbele,  hatua kwa hatua…’akasema wakili na wakili wa benk akasogea kuongea na wasaidizi wake..

Wakili upande wa benki, akawa anateta na wasaidizi wake,..., huku wakili wa kutetea haki za wanaodaiwa  akiendelea.


Hayo yakiendelea huko, …mimi nilikuwa bado nimelazwa, nipo hospitalini, nikiwa naendelea na matibabu.

************

 Siku hiyo ya kesi, nikiwa hospitalini, aliletwa tena yule mtu mbele yangu,…

‘Oh, umeletwa tena, wewe si ulisema unataka kwenda kutoa ushahidi mahakamani…?’ nikamuuliza

‘Wamenikatalia wanasema ushahid wangu hautakubaliwa kwa vile eti nina matatizo ya akili…’akasema

‘Je itakuwaje, maana wewe umsema bila yaw ewe ukweli hautagundulikana…wewe ndiye unafahamu kila kitu, je unayo nyaraka yoyote, ushahidi wa kimaandishi utakaotusaidia mahakamani..?’ nikamuuliza

‘Mimi nipo sawa kwa hivi sasa, ila nilitaka kuonana na wewe kwanza…’akasema na docta akaingilia kati na kusema;

 ‘Mimi nimeamua  kufanya anavyotaka yeye, yeye ana imani akionana na watu wawili, mtu wa jamii, na mama mjane basi atapona kabisa, , …na kupona kwake, ndio kutasaidia wengi, sasa nimelata kwako, muongee naye, ili tuone kweli kapona..’akasema docta.

‘Lakini mimi sio docta…’nikajitetea..

‘Usijali, ..mimi ni docta, nitasikiliza, na anavyoendelea kuongea, nitajua ukweli wa utaalamu wangu kama kweli kapona na ushahidi wake unaweza kukubalika au la…’akasema docta.

Yule jamaa leo alionekana tofauti, hajafungwa, lakini kuna askari wapo tayari, kama lolote likitokea..

‘Nimekuja,…nataka tuongee, najua wewe umeshaufahamu ukweli, najua …ulitakiwa ufe ili ukweli usijulikane, na mimi nimeshaahidi kuwa nitasema ukweli wote…’akasema sasa akiongea vizuri tu.

‘Je unataka kuniambia nini, maana benki wao wanahitajia ushahidi wa maandishi, sio maneno, na wewe kwa hali yako, kisheria haitakubalika kutoa ushahidi, na leo nasikia kesi inaendelea huko…’nikamuuliza na yeye akasema;

‘Wewe si unataka ushahidi eeh, ushahidi wa kukusaidia mahakamani, au sio…ili huo ushahidi uweze kuhakiki ukweli wa hilo deni, au sio, mimi ninaweza kusadikisha hilo, na benki wanalijua hilo ..?’ akaniuliza na kusema.

‘Swali langu umelielewa, wewe utasadikishaje, je unazo nyaraka, kumbukumbu za kibenki, za kulisaidikisha hilo, muhimu benki wanataka kumbukumbu za maandishi….?’nikamuuliza.

 ‘Kazi hiyo nitaifanya huko mahakamani, ila kwasasa nimekuja kwako kwa kukuomba msamaha, nataka nianzie kwako, kabla muda haujafika, je umenisamehe…?’ akasema na kuniuliza hivyo.

‘Mimi hujanikosea, uliowakosea wapo, ila  kama kweli utasaidia ukweli kupatikana, na ukweli ukapatikana, msamaha wangu upo wazi..na msamaha wa hao uliowakosea utakuwepo tu…muhimu ni haki itendeke..’nikasema hivyo.

‘Haya, mimi waniepeleke huko mahakamani,…nitasema kila kitu, sidanganyi safari hii, nitamtaja muhusika mkuu wa hujuma hiyo bila kuficha, na jinsi hujuma hiyo ilivyofanyika…’akasema sasa akionyesha uso wa wasiwasi.

‘Docta, unasemaje..?’ nikamuuliza docta

‘Kitaalamu, mimi siwezi kusema uwongo, kwa hatua aliyofikia, hajambo, na anaweza kuongea ikakubalika,..lakini yategemea pia, …je akifika huko hali ikabadilika,…’akasema

‘Kwanini ibadilike…?’ akauliza huyo jamaa

‘Siku zote inakuwaje, si unaonekana mzima baadae hali inabadilika…’akaambiwa

‘Sio sasa…hali yangu kwa hivi sasa yategemea ukweli nitakaousema, nikichelewa na hali ikarejea tena, ndio basi,..naombeni tafadhali mniwahishe huko mahakamani…’akasema huyo jamaa.

Baadae huyo mtu akapelekwa mahakamani, …, nilitamani sana niwepo huko mahakamani, lakini docta alisema mimi bado sihitajiki kutembea,

Kesi siku hiyo ikafanyika na nilikuja kuambiwa kilichotokea siku ya pili yake, na aliyekuja kuniambia ni mama mjane.

‘Vipi mbona huna raha, mahakamani imekuwaje…?’ nikamuuliza na badala ya kunijibu akaanza kulia..

Nb: Huyu mama mjane alilia nini....naona nisiwachanganye niishie hapa kwanza.

WAZO LA LEO: Haki ina nguvu, ..haki itashinda tu, na hata haki ikizuiwa, ni swala la muda tu, ipo siku haki itafanya kazi yake na ukweli utabainika tu.



Ni mimi: emu-three

No comments:

Post a Comment

Changia hoja kwa kutoa maoni yako hapa: Au tuma kwa e-mail> miram3.com@gmail.com