‘Ndugu yangu liogope chozi la kutoka moyoni…hili ni chozi la
huzuni, chozi la majuto, chozi la kukosewa, chozi la kulalamika…huwezi
kulitafsiri, maana linakuja tu..na huja kwa jambo maalumu sio hivi hivi tu..kwa
aliyezoea kulia, …hili sio chozi lake..’aliendelea kunihadhithia rafiki yangu.
Hiki ni kisa cha kweli kilichonitokea mimi na familia yangu...’akasema huyo rafiki yangu anayenisimulia kisa hiki....
‘Unajua mimi sikupenda kuyahadithia haya, lakini nataka mlione
chozi la namna hii linavyofanya kazi yake maana sio chozi la kawaida,…na nakuhadithia hiki kisa, sio kwa nia ya
kuwalaumu hao walionitelekeza, huenda walifanya hivyo kwa nia ya jinsi walivyoona ni sahihi kwao, ila maamuzi hayo yalitoka kipindi ambacho niliwahitajia sana…maana
nilitarajia mengi baada ya kuwafanyia
kazi zao kwa kujitoa kwa moyo wangu wote, na nini walikuja kunilipa sasa,…
'Malipo yangu ndio hayo kuwa mimi sihitajiki tena....'akasema
'Pole sana...'nikamwambia
‘Yote namuachia mungu…’akasema na kutulia.
'Hebu sasa niambie kwa kirefu, ilikuwaje kwenye hiyo kampuni hadi ikafikia hapo...?' nikamuuliza
Tuendelee na kisa chetu...
*************
Kwa kuhadithia tu, mimi nilianza
kufanya kazi kwenye kampuni hiyo, ikiwa na mapungufu mengi tu, na waliniita hapo kwa vile walisikia kuwa mimi ni mtaalamu kwenye hiyo idara ...ni kweli na nilipofika hapo na kuyaona hayo mapungufu, nikaamua kutumia
ujuzi wangu na uzoefu wangu kuhakikisha kila kitu kinakuwa sawa…na nilifanya
hivyo nikijua huenda huko mbele kutakuwa na neema. Hayo ndio yalikuwa matarajio yangu.
Katika kuwajibika huko, niliweza kuokoa mamilioni ya pesa, pesa
hizo hazikuwa zimejulikana, kutokana na mahesabu yao na kumbukumbu zao, kutokuwa sawasawa, na bosi
aliposikia hivyo alifurahi sana, nikajua labda tutapewa kifuta jasho (bonasi,..lakini
haikutokea, sikukata tamaa, nikajua ipo siku.
Kazi zikaendelea, lakini kutokana na hali halisi ya mabadiliko,
ya kinchi, nisema hivyo... ambayo sio kwa kampuni hiyo peke yake tu,…biashara haikuwa nzuri
sana, kwahiyo kukawa sasa na tetesi kuwa huenda watu wakapunguzwa, mimi sikuwa
na wasiwasi na hilo..., maana kama niliweza kuokoa mamilioni ya pesa, kwanini kampuni
inipunguze mimi.
Ndio maana baada ya kupata taarifa hiyo, niliumia sana, niliumia
kwa vile nilishafika mahali nikawa napanga maisha, nakopa huku na kule ili
watoto wasome,..najua mwisho wa mwezi nitapata fungu langu, japokuwa lilikuwa
lapatikana kwa nusu nusu...lakini unakuwa na uhakika hata ukikopa utakuja kulipa.. Sikujali, nilijua ndio hali halisi…
Sasa kilichoniuma zaidi
ni pale nilipopigiwa mahesabu ya nini nilipwe,..hapo ndio unaweza kuona jinsi gani haya makampuni ya watu binafasi yalivyo na dhuluma...
‘Wewe mwenyewe unaifahamu hali halisi, kwanza nilikuwa
sijakuajiri, kweli si kweli... ulikuwa kama kibarua tu,…kwahiyo kutokana na hali halisi,...sipendi, unaonaee..nifaneje sasa, na sitaki uondoke mikono mitupu, etu usubiria mpaka nikijaliwa, lini sasa..kwahiyo mimi nimeona hivi.. tutapiga
mahesabu yako ya mwezi huu…umefanya siku ngapi vile…’akajifanya kama hajui.
Mimi nikabakia kimia.
‘Eeeh mwezi uliopita umelipwa pesa yako yote…?’ akauliza kama vile hajui hilo
‘Bado, …nimelipwa nusu mwezi…’nikasema kwa sauti ya unyonge, nimeshavunjika nguvu, nilikua kwa juhudi zangu nilizofanya, angalau...ningelipewa hata asante
‘Ok, sasa..tutachukua hiyo nusu mwezi ilibakia na tutaongeza na
siku hizi za mwezi huu ulizofanya, tutakulipa,…nitahakikishe umelipwa hizo pesa
zako, sitaki uondoke mikono mitupu…’akasema
‘Ina maana, ndio malipo hayo ya
mwisho…?’ nikauliza
‘Wewe mwenyewe si unaona hali halisi, nitakulipa nini, shukuru
kuwa mimi nitafanya juhudi upate hizo…nusu mshahara uliobakia, na siku hizi za
mwezi huu ulizowahi kufanya..na..kiukweli sikutegemea kuwa kazii hii itachukua
muda wote huu, mimi nilitarajia utafanya miezi mitatu, ..tumalizane…’akasema
Sikutaka kusema lolote kuwa kama ningefanya hivyo anavyodai
yeye, asingeliweza kuyapata hayo mamilioni ya pesa, nikabakia kimia, nikiumia
kimoyo moyo..
‘Nitamwambia mshika pesa wangu akupigia mehesabu yako, na
akulipe, lakini hakikisha kazi zako zote ulizotakiwa kufanya umemaliza…najua
sina shaka na wewe, lakini kwa kukumbushia tu, sitaki mtu aondoke hapa kabla
hajamaliza kazi zake,..na nitakulipa baada ya kukaguliwa kuwa kweli umemaliza
kazi zako…’akasema
Sikuamini hayo maneno, ina maana kafikia sehemu ya kutokuniamini
tena…moyoni nilitaka kumuambia, kama ungelinijua nilivyo, usingelisema maneno
hayo, hata kama unaniondoa mimi nitafanya kazi yako yote…kimujibu wa taaluma
yangu, ..ndivyo nilivyo, sina haja ya kuwa na kisasi na yeye.
Yaliyofuata hapo baadae huwezi amini, nilioanza kuonekana kama
mtu ambaye naweza kuharibu kazi, naweza kuiba, naweza kufanya jambo na
kukimbia,…sikuamini…
Haya ngoja turudi siku ile…ambayo, nilitakiwa nirejee nyumbani,
nikutane na muuza duka,..siku ya kulipa ada..siku ya…mke wangu anategemea
nitakuja na mkopo, ili aweze hata kuanzisha duka,…siku ambayo nilipewa hiyo
taarifa kuwa kazi sasa basi.
*************
Siku ile naikumbuka sana, kwani ni siku ambayo….nilianza hata
kuumwa maradhi ya moyo…
Wakati naondoka kazini, nilipanga nisipitie njia ile ya dukani,
kama nitawahi kufika, kama nitafika maduka yamefungwa itakwua ahueni kwangu…na
hata hivyo huko kwa dukani nikipita salama, nitakwenda kusema nini kwa familia
yangu…kiukweli nilikuwa na wakati mgumu sana.
Siku ile…, pamoja ya
kutoka kazini kwa muda ule ule wa saa kumi na moja, cha ajabu siku ile usafiri
ukawa ni rahisi,…hakukuwa na wingi wa abiria, nikapata gari, japo la kusimama,
mwili hauna nguvu, lakini utafanya nini..tumbo halina kitu, ningelikula nini,
wakati bajeti imebana.
Cha ajabu siku hiyo
nikafika nyumbani mapema sana, tofauti na siku nyingine…akilini nawaza nikifika
nitaanzaje kumwambia mke wangu…mawazo hayo yakawa sasa ndio yameuteka ubongo
wangu…unajua mkiwa mnaishi pamoja, unajau ni kitu gani uongee na mwenzako kwa
wakati gani,…nilimpenda mke wangu na familia yangu sikupenda kabisa ije kuumia,
nipo tayari kufa kwa ajili ya famili yangu.
Kwa jinsi nilivyotekwa na mawazo hayo ..ya jinsi gani ya
kufikisha ujumbe huo kwa familia yangu,…, nilisahau kabisa lile wazo la kupitia
sehemu nyingine kumkwepa mwenye duka, maana njia ya kufika nyumbani ni lazima
upitie kwenye hilo duka, lakini kuna njia nyingine ya kuzunguka…wakati natoka
kazini, nilipanga nipitie njia ya kuzunguka…lengo ku mkwepa huyo muuza duka.
Ndugu yangu, sio kwamba mimi ni muoga kiasi hicho, ila kiukweli
huyo jamaa sifa zake za ukatili, zinajulikana sana, kwanza alikuwa jambazi, na…sio
kwamba natania, ipo siku moja alishikwa mwizi, ..kwa macho yangu nilimuona
jamaa huyu akionyesha unyama wake kwa huyo mwizi, aliyetaka kuvunja duka lake
ili aweze kuiba, ilikuwa alifajiri mimi nawahi kazini
Walikuwa wawili mmoja akaweza kuponyoka na kukimbia, sasa huyu
aliyeshikwa, ambaye alijiona ni mbabe, ndiye alikutana uso kwa uso na huyu
muuza duka,…mwizi alikuwa mtu kashiba, ana miraba minne, na akaamza kukabiliana
na huyu muuza duka, lakini hakuweza.
‘Huyu niachieni mimi mwenyewe, nataka niwaonyeshe kuwa mimi
siibiwi..na hakuna atakyefanya hivi hapa tena….sitaki utani mbele ya mali yangu…’akasema,
kwanza alikuwa na kisu akakurusha pembeni.
Mwizi kuona hivyo, akajua huyo muuza duka ni rahisi kwake, ,…wakaanza
kutupiana ngumi na huyu mwizi kwanza mwizi alionekana kumzidi muuza duka,
lakini hakuna aliyeingilia,..watu walikuwa wamesimama pembeni.
‘Ukinishinda, umepona, ..nikikushinda umekufa….’akasema huyo
muuza duka, kifua wazi, na bukuta la kulalia…bukta lake lina sehemu ya
kuhifadhia kisu –ala.
Ikawa kila mwizi akipatwa na konde moja usoni, anabwagika chini,…anajizoa
hara haraka, kawa sasa kama kalewa… watu wakawa wanacheka…mwizi gani kila ngumi
anakwenda chini…lakini mwizi akawa anapmbana akijua ndio kupona kwake, kufa au
kupona…
Ikatokea wakati mwizi
akarusha ngumi, mkono ukadakwa na huyo muiza duka, kwa jinsi alivyoshikwa
tulisikia mlio wa kooo….mkono ukavunjwa na hapo hapo, huyo mwizi akarushwa hewani,
alizungushwa hewani kama mzigo tu, na kubamizwa chini, na watu walishangaa huyu
mtu ana nguvu gani ya kuweza kumbinua huyu mwizi hewani, mwizi ambaye kiumbile
anamzidi huyo muuza duka…ilibakia historia.
‘Mimi sina huruma na pesa yangu,…pesa yangu ina thamani ya utu,
ukinichukulia pesa yangu, umevunja utu wangu na mimi sitakuwa na huruma na utu
wako..nitakumaliza tu…hilo nimeapa, sasa wewe mwizi utakuwa fundisho hapa mtaani, nitakuonyesha
kile ambacho watu hawakijui kunihusu mimi…’akasema
Huyo mwizi anagugumia mkono umevunjwa, muuza duka akawa bado
hajaridhika,…akasogea pale alipoweka kisu chake, akakichukua mwizi hata hawezi
kuinuka, kukimbia, ..muuza duka akamrejea na kumshika huyo mwizi sikio
akalikata sikio…
‘Hiyo kwanza ndio alama yako kuwa wewe ni mwizi, mimi nilikuwa
jambazi, na jaambazi ukikamatwa ujue ni kifo, sasa mimi nimeacha, sitaki
kuibiwa tena, wewe wataka nirejee kwenye wizi…’akasema
Na hapo hapo akakitumbukiza kile kipande cha sikio mdomoni
akakitafuna..sasa sijui atakimeza au la,… kwa haraka ageuka kwa kasi ya ajabu,
kile kisu, kikapita kooni kwa huyo mwizi, damu zikaruka,…
‘Aaah…’ mwizi akapiga ukelele.
Tukajua koromeo limekatika…bahati mbaya kisu hicho kilkwepa
koromeo, kikakata sehemu ya koo … lakini kilifanya kazi yake ..mwizi yule akalala
chini, anakoroma kama mtu anayekata roho.
‘Hufwi eeh,..umechafua kisu changu halafu hujafa… ngoja nikuone
kama hutakufa…’jamaa akaingia dukani, na kuchukua chupa ya mafuta ya taa…mimi
hapo sikuweza kuvumilia tena…huyo,
nikaondoka zangu kuwahi kazini..
Nilipokumbuka hayo,
nikajua huyu mtu hana mzaha kweli kwenye pesa yake, na kweli kwa maana kwa yoyote
eliyewahi kumkopa akachelewa kumlipa pesa yake cha moto alikiona.., kwanza akija
kwako utapokea kipigo, na kipigo hicho yeye
mwenyewe anakuruhusu upigane naye, halafu anachukua kitu chochote ambacho
kinaweza kulipa deni lake,..
Sasa sijui mimi yatanikuta hayo au….kwahiyo sio kwamba
niliingiwa na wasiwasi huo bure… jamaa huyo ana visa vingi, akipigana na
mtu,..ngumi yake ikikupata lazima utaenda chini, yeye anadai, alishaambiwa
asitumie mkono wake kupiga mtu, hasa wa kushoto..alishawahi kumvunja kaka yake
mkubwa wake taya, kwenye ugomvi ugomvi
*********
Sasa ghafla bin vuu,..nikawa nipo maeneo ya duka…nilishasahau,
kuwa nilipanaga nitumie njia nyingine ili kumkwepa huyo muuza duka, ..mawazo ni
kitu kingine kabisa, na ilipangwa tu , lazima nipitie hapo dukaniu.
.
Nilipofika hapo , nikawa
sina jinsi, nikasema moyoni potelea mbali, mungu atanilinda, nikasogea pale
dukani, …sikumuona huyo jamaa, yupo kijana wake, ajabu mara nyingi huyu jamaa hamuamini mtu, nikajua labda yupo chooni, ..hata hivyo nikasema afadhali.
Nilisema afadhali, ..sio kuwa nitakuwa namkwepa hivyo kila siku,
nilikuwa na maana nahitajia kwanza nifike nyumbani,…, nipate muda wa kujipanga,
jinsi gani ya kukabiliana naye,..najua ni lazima nionane naye ..hata hivyo
akili ilikuwa imechoka sana..nilihitajia nikalale kidogo hadi kesho .
'Bosi wako yupo wapi…?’ nikamuuliza hapo kwa kujiamini kidogo.
'Katoka hapa sasa hivi…, anasema anawafuatilia wadeni wake, kakasirika
kweli kweli…’akasema huyo kijana wake.
'Mungu wangu...'nikasema hivyo tu kuondoka pale dukani kwa
haraka…, nikikimbilia nyumbani kwangu sio mbali sana na hapo dukani,…na hisia
zangu, ni kuwa huenda familia yangu ipo chini ya ulinzi ya huyo jamaa au
keshawafanyia kitu kibaya. Pamoja na kumuogopa hivyo, kama atakuwa kaifanyia
kitu kibaya familia yangu, tutapambana…
Nafika eneo la nyumba yangu, nasikia sauti ya jamaa akifoka huko
ndani, nikajua sasa..kumekucha, sasa naingia vitani, japokuwa nafahamu fika
kupambana na huyo mtu siwezi lakini nitajitahidi …
Na kwa namna nyingine nikaona labda kuepusha shari, ni bora
nirudi nilipotoka, nikakae sehemu hadi usiku ndio nirudi, lakini je hapo alipo
hajafanya chochote kibaya, ikawa ndio wasiwasi wangu huo..
Nikawa sasa natamani nigeuke nirudi nilipotoka, na kabla
sijafanya lolote la maamuzi yangu, mara mlango ukafunguliwa, jamaa huyo katoka. Akaniona, au sijui
hakuniona maana kilichofuata baadae ilikuwa ndio jibu halisi…
Alipojitokeza pale
malngoni, uso umebadilika kawa mweusi, …jicho limemtoka nikajua sasa napambana
na simba…kurudi nyuma siwezi, kusogea mbele siwezi nikawa nimeganda, nasubiria
kitakachofanyika
Jamaa huyu anakuja usawa wangu, nikawa nimejiandaa, huku moyoni
nasema, kiukweli ilibidi iwe hivyo, kumuomba mungu, maana sikupenda iwe shari..,…
‘Mungu wangu nisaidie kwa hili, haya yote sio kwa kusudio langu.
Je mimi sikutimiza wajibu wangu kazini,.., je mimi nimefanya dhambi gani hadi
niondolewe kazini, nimefanya kosa gani hadi nije kuzalilika hivi…najua kabisa ningelikuwa
kazini, haya yasingelitokea…naomba msaada wako, ewe mola wangu…’nilijikuta
nasema hivyo tu, kwa hisia za ndani,..sijui ila nahisi ilikuja hali ya chozi
kama lile la ofisini
Nilishangaa….mimi sina kawaida ya kutoa machozi…na niliona ajabu
tukio hilo liniathiri kiasi hicho,…najiona nipo kwenye mabadiliko mengine
makubwa.
Basi kwa muda jamaa alishafika usawa wangu…nikitarajia kipigo,
najua nitajitetea, lakini najua kiundani siwezi kupambana na mtu kama huyo…
Ajabu kabisa jamaa akanipita kama hanioni,…upepo tu, nikayumba…
sikuamini hilo…karibu anipige kikumbo, huyooo kwa haraka akawa anaondoka…
Mimi ilinijia kwa mshangao, sikumini kabisa kama jamaa huyo
angeliliweza kunipita bila kufanya jambo, bila hata kunifokea…kwa vile
sikuamini, taratibu nikageuka kwa
mashaka, kumuangalia kama kweli ndio anaondoka,...
Ile nageuka, kumbe naye sijui alikuwa akiwaza nini, naye kumbe
akagauke, tukawa tumeangaliana, lakini kwa umbeli, alishanipita na kwa vile
alikuwa akitembea kwa haraka ilikuwa ni umbali wa hatua kadhaa,..hapo ndio
sijui, alikuwa hajaniona au..na kwanini alipogeuka alikuwa akainiangalia kama
kushangaa vile…na alipogeuka tulikutanisha macho.
.
Hakusimama na wala hakurudi nyuma…
Ilipita dakika mbili hivi bado nimesimama, na akili iliporejea
kwenye msimamo wake, ndio nikakumbuka kuingia ndani kuiona familia yangu…nikatembea
kwa hatua za haraka haraka, kawaida nikifika nyumbani nagonga mlango kupiga
hodi..
Sikufanya hivyo….nikasita kufanya hivyo, nikajikuta nasita hata
kushika kitasa…nahisi mwili ukinisisimuka, …ni hali ngeni kwangu..hata hivyo,
nikashika kitasa na kuzungusha , mlango ukawa wazi..
Ile natupa macho ndani, naangalia sakafuni, namuona mke wangu…na
mtoto kasimam akiwa kainamisha kichwa…
NB….ILIKUWAJE…Ndugu zangu, nahis kama nisipopata kitendea kazi,
kisa hiki na hicho kingine kitechelewa kidogo maana sehemu niliyoitegemea ,
nilipokuwa nimejishikiza sitakuwepo tena…mniombee tu, nipate sehemu nyingine.
WAZO LA LEO: Yakikukuta
matatizo, shida , mitihani, kamwe usikate tamaa, wewe elekeza imani yako kwa mwenyezimungu,
kwani yeye anatosha kukuongoza na kukusaidia kwenye hatua nyingine.
Ni mimi:
emu-three
2 comments :
UPO WAPI NDUGU YANGU
Kama umeshindwa endeleza niuzie hii blog...
Post a Comment