Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, September 19, 2018

YOTE NI KWA MAPENZI YA MUNGU-50



Askari, wakawa wanafuatilia, kuzima hizo fujo, na kuwatoa watu nje..walitaka pia kuona kuna tatizo gani.

Na baadae huyo mtu aliyekuwa akiendeshwa kwenye kigari cha wagonjwa, akawa keshafikishwa mbele akiwa ndani ya kigari hicho..., nyuma yake yupo docta, anakisukuma hicho kigari, na muda huo hakimu alikuwa kasimama, akitaka kuondoka,…

'Kuna vurugu gani, kesi ijayo, sitaki kuona hili likitokea, kama watu hawana busara, wasifike hapa mahakamani..'akasema hakimu kwa hasira.

Akamuona huyo mtu, akisogezwa mbele, hakutaka hata kufahamu huyo mtu kaletwa wa nini, ...kwa haraka akaanza kutembea kuondoka, huku akisema;


‘Hatuwezi kufanya lolote kwa muda huu, lolote ulilo nalo wewe kwa sasa, itabidi lisubirie muda mwingine, …’alisema hakimu huku anatembea kuelekea mlango wake wa kutokea,

.
Huyo mtu aliyekaa kwenye hicho kigari, akasema kwa sauti kubwa;


‘Samahani muheshimiwa hakimu, lakini hili haliwezi kusubiria kesho,…ilimradi kauli imeshatoka, ya kunishutumu mimi, na hatujui kesho itakuwaje, ninaogopa isije kutokea kama ilivyowahi kutokea huko nyuma, watu wameondoka na kuacha maswali nyuma,…naomba tafadhali, unisikilize japo kidogo tu…’huyo mtu kwenye kigari akasema

Hakimu akawa anatembea kuondoka, na huyo jamaa akazidi kusema kwa sauti kubwa

‘Mimi ndiye....alimaarufu,.. Dalali…’Aliposema hivyo, hakimu akasimama, na kwa haraka akageuka kumuangalia huyo mtu, alitulia kidogo akimuangalia ...


‘Dalali…ndio wewe ndiye uliye- ….’akasema hakimu na huyo jamaa hakusubiria hakimu amalizie, akasema;


‘Ndiye mimi muheshimiwa hakimu, ndiye mimi niliyeshutumiwa na mengi, kutoka kwenye kinywa cha kijana anayedai kuwa yeye ni mtoto wangu…’akasema huyo mtu, na hakimu akawa sasa kasimama.


‘Mimi imenibidi nijitokeze tu, ili haki iweze kutendeka, siwezi kuvumilia tena, nahisi kuna njama za kuupotosha ukweli, na tukiendelea kunyamaza, mabaya yanaweza kutokea, nahisi wakati sasa umefika kuusema ukweli wote,...kwahiyo muheshimiwa hakimu tafadhali, nipe angalau muda kidogo,...naogopa kwa hali ilivyo, kesho inaweza isinikute nikiwa hai…’akasema huyo jamaa.


‘Kwanini unasema hivyo, kuna nini kimetokea na kwanini upo katika hiyo hali,,…?’ akauliza hakimu, sasa akiangalia saa yake.


‘Nimetishiwa uhai muheshimiwa hakimu, yanayotokea kwangu, ni majinamizi tu, nafanya bila kujijua nafanya nini...'akasema

Hakimu sasa akageuka kumuangalia huyo mtu

'Na cha muhimu ni iliyotolewa na huyo kijana, sasa kwa vile una haraka, mimi nasema hivi, sio kweli kuwa mimi nimechukua hilo deni, sio kweli kuwa mimi ndiye nilikopa hizo pesa, sio kweli kuwa mimi nilijua kilichokuwa kinaendelea kwenye hilo deni, nayatamka haya yasikike,…ili hata wakinua leo, kauli yangu iwe ndio hiyo…’akasema huyo jamaa.

Hakimu akaangalia saa, na kuanza kuondoka, huku akisema;


‘Sawa kauli yako imenakiliwa, kesi itaendelea kesho, au siku itakayopangwa kwa leo hatuwezi kufanya lolote..unasikia, sheria za mahakama zinafuatwa, kesi hii imesitishwa kwa leo…’akasema hakimu , akaanza kuondoka, lakini ghafla akasimama , na kwa sauti kubwa akasema;


‘Ila wewe itabidi uwe mikononi mwa watu usalama, watu wa usalama, hakikisheni huyo mtu analindwa kwa nguvu zote, hadi kesi itakapoendelea tena…’akasema huyo hakimu, na huyo akafunguliwa mlango, na kutoka eneo hilo la mahakama.


Watu wa usalama kwa haraka wakamfuata huyo mtu aliyeingia ambaye lijitambulisha kuwa yeye ni …alimaarufu, Dalali na kuondoka naye.


Kisa kinaendelea..


*********

Kesi hiyo ilibidii ipangiwe siku iliyofuata,hiyo ni kutokana na kilio cha watu wengi ambao walianza kulalamika kuwa kesi hiyo inachukua muda, huku wao wakidhulumiwa haki zao, wana mashaka na haki zao, kwani wamepewa madeni yasiyo halali yao…


Na wakati huo huo,  waendesha mnada walikuwa wakilalamika,kuwa na wao wanazuiliwa kutekeleza majukumu yao, wakati wana kibali rasmi, cha kuendesha minada hiyo kwa niaba ya benki..


Na watu wa haki za binadamu, wanajamii,…haki za akina mama na watoto na wao walishaanza kupaza sauti, kuwa matajiri, wanatumia mapesa yao, kuhakikisha, haki za wanyonge hazipatikani…


Jambo hili likaingia kwenye siasa, …wanasiasa nao, wakaona hiyo ndio sehemu ya kujijengea majina, wakaanza kupaza sauti, kwa wananchi…


‘Haki..haki..haki…haitendeki ipasavyo….’


Kwa mashinikizo hayo, yakaifanya idara ya mahakama kuingilia kati, na kesi hiyo ikapewa kipaumbeme… hakimu akaona kesi hiyo iendee siku iliyofuatia.


‘Kutokana na ratiba zetu, siku ya kesho haina kesi nyingi, kwahiyo kesi hiyo itaendelea, na natumai , siku hiyo ndio itakuwa siku ya mwisho ya kusikiliza ushahidi wenu, na muhakikishe kila kitu kinakuwa tayari,…ili tuone kama tunaweza kuihitimisha hiyo kesi, au la, hatutaki idara hii kuingiliwa na watu wengine…’akasema msemaji wa hakimu akiongea na mawakili wa pande zote mbili.


Na wakati hayo yakiendelea, Majaliwa alikuwa bado kapoteza fahamu, na alikuwa chumba cha wagonjwa mahututi, ….na ndiye alionekana kuwa shahidi muhimu wa kuhitimisha hiyo kesi, watu wengi walikuwa wakimzungumzia yeye, na wengi walitaka wawepo kwenye hiyo kesi.


‘Kama shahidi huyo muhimu anaumwa hajitambui, tutaendeleaje na hii kesi hapo kesho, tunaona tusubiria labda..?’ akauliza wakili wa benki.


‘Tutaendelea na mashahidi wengine, kuna huyo mmoja aliyejitokeza,…hatuwezi kumpuuza, na ikizingatiwa kuwa yeye katajwa kama ndiye muhusika wa hilo deni la mama mjane…’akasema, msemaji wa hakimu.

‘Sio kweli…’akataka kusema wakili wa benki lakini akanyamazishwa,


‘Hayo tutayasikia huko mahakamani, lengo la kikao hiki ni kuwaarifu tu, kuwa kesho muwe mumejiandaa, hatutaki kupoteza muda kwa kesi moja tu…’akasema huyo msemaji .


**           


Basi kesi ikaendelea siku iliyofuatia,…na siku hiyo watu walijaa..isivyotegemewa, na ikaonekana mahakama haiwezi kukusanya watu wengi kiasi hicho,…, ikabidi kikosi cha kuzuia fujo kifike kuwatawanya hao watu waliojazana na wengi bado walikuwa wakiendelea kufika.


‘Kama hamtaki kutulia, inabidi muondoke eneo hili…’wakaambiwa watu, na wachache wakatawanyika, wengine wakatafuta sehemu pembeni ya mahakama wakakaa, wakisubiria ni nini kitatokea.


Sauti mahakamani ikasikika, …


‘Dalali…unakumbuka uliwahi kuambiwa ueleze ukweli wa deni ambalo benk wanadai kuwa ni deni la marehemu, aliyekuwa mume wa mama mjane ambaye ni mmmoja wa watu wanaodai kuwa deni hilo sio la kweli…’akaulizwa.


‘Ndio nakumbuka sana muheshimiwa …’akasema


‘Lakini kwa mara zote ulizofika mahakamani, au kuhojiwa na polisi wewe…, hukutaka kusema ukweli,…’akaambiwa.


‘Mimi nilisema yale yaliyostahiki kusemwa kwa wakati huo…’akasema Dalali.


‘Sasa kwa vile ukweli umeshajulikana, kuwa wewe ndiye uliyefanikisha deni hilo,sasa swali je hiyo sahihi ya kaka yako ilitoka wapi, kama ni wewe uliyefanikisha deni hilo…?’ akaulizwa…?’ akaulizwa Dalali.


‘Kabla sijajibu hilo swali, nataka tuwe wakweli , je hilo linawezekana  kweli..tuweni wakweli tu…, kwa taratibu za benki, zilivyo kwa mtu kama mimi, au kwa mtu yoyote kuweza kuchukua deni, achilia mbali, kwa niaba….lakini hapa kuna swala la sahihi ya mtu, kuna  dole gumba, la muhusika, je mimi nilikubaliwaje kuchukua , au kuweka sahihi kwa niaba..je ni kweli sahihi hiyo ni yangu, kwa niaba ya kaka yangu, ambaye ni marehemu…?’ akauliza.


‘Utuambie wewe sasa, maana sisi hatukuwepo, na wewe umetajwa kuwa ndio wewe ulifika kuchukua hilo deni, ukaleta kumbukumbu zinazohitajika, na wewe ulifanikisha hilo…’akaambiwa.


‘Jibu ni kuwa haiwezekani,…si ndio hivyo,..huo ndio ukweli, haiwezekani, na kama alivyosema, msemaji mmoja, maswala la mikopo yaliwekewa kitengo maalumu na waliohusika walifika kwenye kitengo hicho maalumu, sasa mimi sikumbuki…kwakweli, naomba nifahamishwe vyema, ilikuwaje….?’ Akauliza.


‘Sisi tutakufahamisha nini, …wewe kwa vile umetajwa kuwa ndiwe uliyehusika kwa hilo, tunataka utuambie wewe ulifanyaje, au ilikuwaje..’akaambiwa.



‘Kabisa… kabisa mnakubaliana na kauli hiyo,..ya maneno tu,  kuwa mimi ndiye nilihusika na hilo, kwanini mumuamini kiasi hicho,..!  Jamani, fanyeni kazi yenu vyema, mimi sielewi hapo….’akasema na kukaa kimia.


‘Tunakusikiliza wewe, hatuna muda wa kupoteza leo….leo, hatuwezi kuchukua siku nzima kwa hii kesi moja tu…’akasema hakimu.


‘Ina maana kuna mbinu zilitumika, muheshimiwa hakimu, sio bure tu, ..na hizo mbinu haziwezi kufanywa na mtu nje ya benki,…kwani benki wana taratibu zao, na mtu wan je huwezi kuzivunja, au sio, sasa iweje mimi mtu wa nje nishutumiwe kwa kauli ya mtu mmoja tu…’akasema, na hakuna aliyemjibu.


‘Ni sawa,…mimi nakiri kuwa kweli nilikuwa natumika kwa niaba ya bro ambaye ni marehemu, nilikuwa nachukua pesa kwa niaba yake…lakini nasema kwa kuapa, sikuwahi kujaza au kupeleka fomu ya kuomba mkopo kwake, akajaza akaweka sahihi, nikarejesha benki,…hilo halipo jamani…’akasema



‘Kwahiyo…unataka kusema nini…ni nini kilichokuleta hapa?’ akaulizwa

‘Kwahiyo, mimi nasema hivi, kama hilo deni lilitolewa,… mimi sijui lilitolewa vipi, na ndio maana nikawa nimesimamia kwenye ushahidi wa benki nikiamini huenda ni kweli hilo deni lilitolewa kwa bro, labda bro alichukua na hakutaka mimi au mkewe alijua hilo…’akasema


‘Usitake kutuchanganya hapa…’akasema wakili wa kutetea madeni.


‘Sio kuwa nawachanganya, huo ndio ukweli jamani,…hapa ni mahakamani, mimi naongea kama Dalali, najua dhima ya hili kama nitadanganya, mimi sijui lolote zaidi ya nakala za benki kuwa deni hilo lilichukuliwa na marehemu, sasa kama kulikuwa na mbinu nyingine kiukweli mimi sijui…’akasema Dalali.


‘Kwahiyo huyo shahidi aliyepita, alidanganya , kwa kusema wewe ndiye unahusika na hilo deni…?’ akaulizwa


‘Alisema hivyo kuwa mimi ndio muhusika wa hilo deni…?’ akauliza


‘Unauliza kama hujui, kwanini sasa umefika hapa kuikana hiyo kauli, …huyo shahid alisema wewe ndiye uliweka sahihi, ya hilo deni kwa niaba ya kaka yako, na wewe ndiye ulifanya utaratibu wa kupata dole gumba..’akaambiwa.


‘Mimi ndiye niliweka sahihi, hapo kwenye hiyo stakabadhi ya benki, kuna onekana sahihi yangu, kuwa nimechukua kwa niaba…sio kweli…huyo shahidi aje ayaseme hayo maneno mbele yangu, anithibitishie kwa ushahid kuwa mimi ndiye nilifanya hivyo…mimi sikubaliani na shutuma hizo…’akasema Dalali.


‘Unasema hivyo kwa vile wewe unajua kuwa msemaji hyupo hapa, hajiwezi,…si unajua huyo shahid ni  mahututi, hataweza kuja kupingana na wewe hapa, na wewe unachukua nfasi hiyo kupoteza muda hapa…’akaambiwa.


‘Lakini hii ni mahakama, kauli yangu inukuliwe,..kuwa mimi sijui lolote kuhusu hilo deni zaidi ya ushahid wa benki kuwa deni hilo ni la marehemu kaka yangu, sasa kama kuna vinginevyo, kuwa kuna njama zilifanyika, mimi nanawa mikono, sizijui kabisa…’akasema.


 Dalali akaigiza kama ananawa mikono…alipomaliza kufanya hivyo akaendelea kuongea;


‘Na kusema ukweli mbele yenu , mimi sikuwa na ufahamu wowote wa hilo deni, wakati kaka yupo hai…hilo deni nimelisikia siku walipoleta benki barua ya kujulisha kuwa kaka yangu anadaiwa…’akasema


‘Kaka yako hakuwahi kukuambia benki kuna deni, …awali hakuwahi kukuambia kuwa benki pesa yake inachukuliwa bila ya yeye kufahamu…?’ akaulizwa


‘Ni kweli ipo siku, kaka aliliongelea hilo, kuwa anashangaa kuna pesa imetolewa bila ya ridhaa yake, akaandika barua, na benki wakasema watafuatilia…na…siku moja wakati…ni.ni siku ile ilipotokea ajali,..hapana siku kabla, ..ooh, sijui kichwa changu kipoje…’akawa anajikuna kuna kichwa.


‘Ilikuwaje siku hiyo…?’ akaulizwa.


‘Ndio alinipigia simu akilalamika…kuwa kuna tatizo benki, nirudi haraka na gari,..kwa muda huo nilikuwa nalichunguza gari,…na kiukweli, sikuweza kupata muda wa kulichunguza, ila nilihisi gari lina matatizo…’akasema.


‘Je hayo matatizo ndio yalisababisha gari, kupata ajali…?’ akaulizwa.


‘Kiukweli…labda nijilaumu mimi…wakati najaribu hilo gari, nilihisi kuna tatizo..nikaona nilipeleke gari gereji…sasa wakati nimelifungua, ndio nikasikia simu..ya bro..kuwa nirejee nyumbani haraka, kuna tatizo benki…’akasema.


‘Ni nani alikupigia simu…?’ akaulizwa.


‘Unajua hilo nimeliwaza sana, nimejaribu kufanya uchunguzi wangu binafsi...tatizo,kiukweli kwa siku ile,…sikuwa makini kukagua ile namba, niliyopigiwa simu, ..na sikumbuki ilikuwa namba gani, ila …nilijua ni bro…’akasema.


‘Ina maana namba ya kaka yako haipo kwenye simu yako, hukuangalia kuwa ni namba ya kaka yako au la..?’ akaulizwa.


‘Namba hiyo ninayo kwenye simu yangu, ila mimi .nasema hivi, siku ile nilipokea bila kutizama mpigaji, na nikasikiliza, na mimi nikajua ni kaka…kwa haraka , nikijua labda kuna tatizo kubwa, ikabidi nifunge gari, na kuendesha gari kurudi nyumbani, muito wa kaka ulionyesha kuwa kuna tatizo kubwa sana…’akasema.


‘Wakati unaendesha gari kurudi nyumbani ilikuwaje…?’ akaulizwa.


‘Kuna hali,…nilihisi sio ya kawaida,…lakini akili yangu ilikuwa mbali, kuwazia, hicho alichoniitia kaka yangu…na nikafika nyumbani, kaka akiwa kakasirika kweli, na muda huo ameshajiandaa kuondoka…’akasema.


‘Hukumuambia kuhusu tatizo hilo la gari…?’ akaulizwa.


‘Hakutaka hata kuongea na mimi…kwa haraka akasema nimpe ufunguo, akaweka mizigo yake kwenye gari..na kuanza kuondoka….’akasema.


‘Hukumzuia kuondoka na gari hilo, ukiwa  unafahamu kuwa gari hilo lina matatizo…?’ akaulizwa.


‘Sikuweza,..kaka akikasirika huwezi kuongea neno mbele yake, usubirie mpaka atulie,..sikuweza kabisa na ilipotokea ajali, nilijilaumu sana, kuwa mimi nimehusika, kwanini sikuweza kufanya hivyo, kumzuia…’akasema


‘Kiukweli,... kaka alipoondoka, nilimuuliza shemeji kuna tatizo gani, shemeji akasema hata yeye haelewei kitu..basi mimi nikaomba mungu tu..kaka aweze kuende salama na aweze kurudi salama…lakini siku hiyo haikupita ndio tukapokea taarifa ya hiyo ajali…kwakweli kwa hilo hadi leo mimi najilaumu sana..., ni mimi nimesababisha kifo cha kaka…’akasema sasa akijizuia kulia

‘Kusababisha kwa vipi sasa…?’ akaulizwa


‘Nilishindwa kumzuia, nilijua gari hilo lina matatizo, lakini yeye hakutaka kunisikiliza ningelifanya nini sasa…’akasema


‘Wanasema wewe ndiye ulikuwa wa kwanza kufika kwenye hilo gari,...baada y aajali kutokea, kweli si kweli…?’ akaulizwa.


‘Kwa vipi…!?' akauliza kwa kushangaa. Halafu akaendelea kuongea...


'Unajua...mimi nilifika kwa haraka baada ya kupokea taarifa, ...nilifika na kukuta  gari linawaka moto mkali sana…na niliuliza kaka yangu yupo wapi, je kaweza kutoka kwenye hilo  gari, watu wakasema hawajaona mtu akitoka,..'akatulia kidogo.

'Mimi nikawa sasa nataka kwenda kwenye hilo, gari, moto ni mkali kweli..  watu wakanishikilia,…kwa watu walioweza kuiona hiyo ajali, watakuwa ni mashahidi wangu, waulizeni watu waliokuwepo siku hiyo, mimi ninashangaa kusikia eti …nilikuwa wa kwanza kufika kwenye hilo gari, ku-ku, kiukweli inaniuma sana…’akasema.


‘Baada ya hapo ilikuwaje…baada ya moto kuzimwa, ..wewe ulifika kwenye gari…?’ akaulizwa.


‘Ndio, lakini kwa kuitikia wito wa askari,…..ili niweze kuutambua mwili wa kaka,..maana ...walisema, aligonga nguzo, akapoteza fahamu, na huo moto unawaka, hakuwa na fahamu, na ilitokea kwa kasi sana, walivyosema watu..mimi nuilifika kwenye hilo gari kwa muito wa askari, kuhakikisha kuwa mwili huo ni wa kaka yangu, nitakuwaje wa kwanza kufika hapo…’akasema.


‘Mbona unarudia uwongo ule ule..’akaambiwa


‘Sio uwongo jamani…mimi sasa hivi nasema ukweli ulivyo, nifiche ili iweje,…na huyo anayejiita ni mtoto wangu, aje hapa athibitishe hilo...'akasema


'Athibitishe nini sasa, kwani alikuwepo kwenye hiyo ajali..?' akaulizwa

'Athibitishe kuhusu hilo deni, maana …mimi sijui lolote kuhusu hilo deni…’akasema hivyo na watu wakaishia kuguna, na ...mara watu wakawa wanaongea kila mtu na lake mpaka hakimu akaingilia kati.


‘Kwahiyo unataka kusema huyo kijana wako anadanganya, na kwanini unasema ‘huyo anayejiita, mtoto wako..’,?' akaulizwa


'Ndio anayejiita,...nina sababu zangu kusema hivyo....'akasema hivyo.

'Ni kweli kuwa hata yeye hata yeye kasema hujawahi kumkubali kuwa yeye ni mtoto wako, ni kwanini wewe, unamkana kuwa huyu sio  mtoto wako, wakati mama yake kaandika hivyo, kuwa wewe ndiye chanzo cha huyo mtoto…?’ akaulizwa.


‘Sijasema nimemkana…na ndio ni eeh, eeh,…kwa kauli ya marehemu nikiwa na maana, mama wa huyo kijana,..'akasita watu wakiguna.


'Nimesema hivi , mimi sikatai, spingi kauli ya huyo mama, …ni kweli, eeh...aliwahi kuniambia ana mimba yangu…lakini hatukuwahi kulithibitisha hilo, na …kutokana na mageuzi, kuwa mimi nimeoa,…nina familia yangu, siwezi kukubaliana na hilo, ..kwani kukubali hilo ni kuleta uhasama ndani ya ndoa yangu…’akasema.


‘Lakini hayo yalitendeka kabla hujaoa, si ndio hivyo, kuwa wewe uliwahi kumbaka huyo mdada, na mbele ya mahakama ulikana hilo, alipokushitakia, kwenye kesi, aliyokushitakia wewe…’akaambiwa


‘Mbele ya mahakama iliamuliwa tukalimalize hilo nyumbani, maana kulikuwa bado na utata mwingi, na sikuweza kukubali au kukataa…’akasema hivyo,


‘Ni ikawaje…?’ akaulizwa


‘Alipoitwa kwenye kikao cha kifamilia hakuwahi kufika, alikuwa anaumwa,…’akasema

‘Sasa kwanini mke wako aje kukwazika na jambo kama hilo, hukuwahi kumwambia uliyowahi kuyafanya ujanani mwako, sizani kama hayo ya ujanani, yatamfanya mke wako akwazike,…na kuleta uhasama kwenye ndoa yenu…’akaambiwa.


‘Ni kweli…lakini…mnielewe hapo, mimi sikuwahi kukaa na kukubaliana na huyo marehemu kuwa huyo mtoto ni wa kwangu, kutokana na historia ilivyokuwa, na niliongea hayo hata mbele ya mahakamani,..na angelifika siku hiyo ya kikao cha kifamilia pale nyumbani sizani kama ingelileta shida,…kama ni mtoto wangu, ningekubali tu…’akasema.


‘Je hukuwahi kumfanyia hayo aliyosema yeye kuwa wewe ulimfanyia…?’ akaulizwa.


‘Ujana una mambo mengi…..na na…kwa vile kijana mwenyewe hajataka kulikubali hilo, kwanini mimi ning’ang’anie…'akawa anaongea tofauti na swali lenyewe, 

'Yeye, kama anaona kweli mimi ni baba yake alitakiwa tukae meza moja tulijadili hilo, yeye kama alivyokuwa mama yake ni kiburi tu…sasa mimi nifanye nini…’akasema.


‘Kwahiyo wewe na yeye bado mna uhasama…?’ akaulizwa.


‘Yeye ndio ana uhasama na mimi, mimi sina uhasama na yeye…na visa vyote hivyo anavyovi-fanya vya kunitia mimi matatani, kunitega,kwa mambo mbali mbali ili mimi nionekane muhalifu,…havitasaidia kitu , maana kama ni kosa lilishafanyika, na hayo yalikuwa mimi na huyo mama yake, na niliwahi kumuomba msamaha, …’akasema.


‘Kwa kusema hivyo, unamaanisha, huyu kijana ndiye kakutega na hilo deni, kuwa wewe uliweza kulipokea hilo deni kwa niaba ya kaka yako..wakati kaka yako hana ufahamu na hilo…si ndio hivyo?’ akaulizwa.


‘Narudia tena, tafadhali mnielewe…mimi sijui lolote kuhusu hilo deni, zaidi ya ushahid wa benki, kama yeye kanitega kwa hilo deni, mimi sijui..sina ushahidi wa hilo, na nisiwezi kumsemea hivyo,....ila kumbekeni maswali yangu ya awali,...'akasema


'Maswali gani...?' akaulizwa

'Inawezekanaje deni hilo lifanyike hivyo,..kwa mujibu wa sheria za benki, na lipite hivyo kirahisi,..yawezekanaje kwa mtu wa nje kama mimi, nije kuyafanya hayo,...hebu jkaribuni kulifikiria hilo, ..ni hekima ndogo tu,..kiukweli mimi sina ushahidi wa kumnyoshea mtu kidole,..ila jiulizeni hilo...’akasema.


‘Kwanini sasa akutaje wewe kuwa ndiye uliyeweka sahihi kwa niaba ya kaka yako, ?’ akaulizwa na kabla swali halijamalizika, yeye akasema;

‘Mimi  hapo kwakweli sijui…kwanini anisingizie mimi hivyo..., ndio maana nilitaka niliongee hili mbele yake, anielezee ilikuwaje,...lakini kwa bahati mbaya nilipofika tu yeye, sijui kwa kuniogopa akapoteza fahamu..’akasema.


‘Kwanini akuogope?’ akaulizwa.


‘Labda ni kutokana na..mimi sijui, kwanini ilitokea hivyo, labda alimuona mama yake, au mzimu wa mama yake..ukamuonya kuwa anachokifanya sio sahihi,…nimesikia akisema kuwa mama yake alimkanya kuwa asije kunilipizia kisasi mimi..kwa haraka hapo utafikiria nini,..wanawake wa siri kubwa mioyoni mwao..’akasema.

'Una maana gani kusema hivyo...?' akaulizwa

'Nawaza tu..kutokana na historia ya huyo mama, ilivyokuwa...mengi yalisemwa juu yake, na ..sio kuwa yote yalikuwa ni kweli..lakini kuna ambayo mimi nayafahamu, ..siwezi kuyasema hapa...'akasema


‘Je ni kweli kuwa wewe uliwahi kumfanyia mama yake huo ubaya, na unyama wa kumkata ulimi, kwa kifaa chenye kutu..?’ akaulizwa.


‘Hayo, mengine kiukweli mimi siyajui, na…na kiukweli, …jamani siku ile ilikuwa na mikanganyko mingi, nililewa…sikujua nilitendalo…sasa mimi siwezi kukubaliana na hilo moja kwa moja,....ni kweli kuwa niligombana naye, na siku ile, alitamka maneno ya kunikera, yaliyonifanya nikasirike sana…'akasema


'Je ni kweli uliwatuma watu wafanye hivyo...?' akauliza

'Lakini mimi sikuwaambia wamkate ulimi...sikuwaambia wa..wa...muue, hapana hayo sijui yalitoka wapi,,,niliwaambia wamfundishe adabu tu ..’akasema.


‘Ina maana hayo aliyoyaandika huyo mama kuwa wewe ndiye ulimfanyia hivyo, na wakati yanafanyika hivyo wewe ulikuwepo, kaandika uwongo,..je ni kweli kuwa wakati kitendo hicho kinafanyika wewe ulikuwepo maana yeye aliandika hivyo…?’ akaulizwa.


‘Nasema hivi mimi…siwezi kuyakataa hayo madai,,… kipindi kile , ujana, ulevi, na…na kuogopa, ilibidi nifanye mambo ambayo sikutaka yafanyike, ..lakini sikumbuki kitendo hicho cha kumkata ulimi, mbona ni unyama mkubwa sana huo,…aah, hapana, labda wale wahuni tu, sio mimi…’akasema.


‘Kwa kauli yako hiyo , kwa hivi sasa inatufanya tukutilie mashaka, kuwa wewe sio mkweli…hayo maneno aliyaandika marehemu, ..na inavyoonyesha kwenye maandishi yake yeye alikuwa akikupenda sana,..sasa kwanini akusingizie kitu kama hicho…?’ akaulizwa.


‘Jamani, hayo ya mimi na yeye, ningeliomba tuyaache,..kiukweli mimi nakiri kumkosea, lakini aliyoyafanya, yeye ndiyo yalinitia hasira…hamjui alinifanyia nini, na sio vizuri mimikumuongelea vibaya marehemu, wakati hayupo hapa duniani,..…mengine kayaficha hakuyaandika,…nahisi kwa kwa masilahi ya mtoto wake, je nyie mnataka yasemwe, sio vizuri jamani…’akasema.


‘Ni hasira gani za kufikia kumfanyia binadamu unyama huo wote, hapo ndio sisi hatukuelewi, hasira zilitokana na nini…?’ akaulizwa.


‘Jamani, sijui nisemeje…labda mnataka nionekane kuwa mimi ni mnyama, au sio ili nifungwe, ninyongwe..si ndio hivyo, sawa..., kama hilo litasaidia eeh, ili nisamehewe dhambi zangu, sawa...mimi nipo tayari…nifungeni tu, au ninyongeni tu…lakini siwezi kuyaongea hayo mengine sio vizuri…’akasema.

Alikaa kimia baadae akaongeza haya maneno….


‘Na…mengine niliyafanya,..naweza kusema ni akili za ujana ..na kutokujitambua, na, na..nilifanya vile…ili kujiokoa kwenye mikono ya kaka yangu, …’akasema.


‘Kwa vipi…ujiokoe kwenye mikono ya kaka yako…?’ akaulizwa.


‘Kiukweli kama kaka yangu angeliligundua hilo..misaada yote kwa ajili yangu, maana mimi nilikuwa nasaidiwa na yeye, ...na..nilikuwa na ujana mwingi,..ila nijua kuigiza, ili kaka anione ni mwema sana,..kiukweli kaka aliniamini sana,...sasa ninani angelikubali hiyo misaada isitishwe, na nina imani, ..angehakikisha kuwa mimi nilifanya hivyo kwa huyo binti....ningelifikishwa…kwahiyo kwa akili za kitoto, niliona bora,..huyo mwanamke atokomee, asioekane hapo karibu...’akasema.


‘Kwahiyo kumbe kweli ulidhamiria kumuua, au huko kumtokomeza kulikuwa na maana gani..?’ akaulizwa

‘Mnataka mimi nisemeje sasa…ule ulikuwa ni ujana. Jamani, nimeshawaambia hilo, hasira zilinizidi kupita kiasi...kiukweli nyie hamjui tu, mtu nilimuamini, nikajitolea…nikamuhifadhi sehemu, kwa gharama zangu, tena za kudanganya hapa na pale,halafu, hapana  …inaniuma sana,…’akatulia


‘Unajua sisi bado hatujakuelewa, yeye kakiri kuwa yeye alikupenda sana,ndio maana hakutaka kabisa uje kufanyiwa lolote baya, lakini wewe unavyoongea ni kama haupo hivyo, ni kwanini…?’ akaulizwa.


‘Hivi mumesikia, ni kwanini nilitamfutia sehemu...tatizo ni kuwa yeye alikuwa mfanyakazi wa ndani...sasa, mnajua wenyewe nina maana gani,...na...unajua mengine sikutaka kuyasema...'akatulia, halafu akaendelea kusema;

'Ni kweli nimeyasikia hayo, kuwa kweli alinipenda hivyo, ..na hata akawa radhi kesi yetu imalizikie nyumbani, akanisamehe,  na mimi kuonekana sina hatia, maana kama kweli angeliamua, ningefia jela,…najua kiukweli mimi nina hatia, na nipo tayari …kuwajibika kwa hilo…lakini..’akasema na kutulia.


‘Hilo umelikubali, ..kuwa kweli ulimfanyia huyo mama unyama huo aliandika,  sasa huoni madhara yake yamekimbilia kwa mtoto kalifahamu hilo, ..unafikiri kama ungelikuwa wewe mama yako kafanyiwa hivyo, ungelikaa kimia..?’ akaulizwa na hapo akabakia kimia.

Muulizaji akaendelea...

‘Kijana wako kwa kauli yake alisema hivi…’Aliyechukua huo mkopo, aliyeweka sahihi, si mwingine,… bali ni Dalali, baba aliyemuangamiza mama yangu…’..na kweli wewe umekiri kuwa wewe ulimfanyia mama yake hayo mabaya,.. sasa tunajiuliza wewe uliwekaje sahihi, na sahihi inayoonekana ni ya kaka yako..

Pili,.dole gumba liliwekwaje...maana dole gumba ni la kaka yako...na wewe ndiye inasadikiwa, kwa kauli ya kijana wako, ndio wewe ulifanikisha hilo kwa vipi, tuambie, ili tujue kuwa wewe ni mkweli na unataka kesi hii iishe...'akaambiwa

Na tatu, nilini haya yalifanyika ni baada ya kaka yako kufariki, au yalifanyika kipindi bado yupo hai, ..sasa kwa mara ya mwisho, sisi tunataka kauli yako, ili tusije kulaumiana tena kwa hilo, je yeye, kijana wako kadanganya, kwa hiyo kauli, sio kweli kuwa wewe unahusika na hilo deni, au wewe ndiye unadanganya, sisi tuna ushahidi wote hapa, …?’ akaulizwa hilo swali.

Dalali, akabakia kimia...kama anawaza jambo...halafu akainua kichwa na kumuangalia hakimu...ndio akaanza kuongea...


NB: Nimeshindwa kumalizia

WAZO LA LEO: Ndani ya hasira yupo ibilisi.. hasira mara nyingi humvuta mtu akafanya yale anayoweza kuja kuyajutia baadae, wengine wanasema wakiwa na hasira ni bora waseme sana, au wafanya jambo, hata la kuumiza,…wengine hufikia kulia tu... Je baada ya matendo hayo, unakuwa umefaidika na nini hasa..hujaumiza watu wengine huenda walikuwa hawana hata kosa…tujue fika,..hasira ni hasara,


Ni nini iliyobora ukifikwa na mtihani huo, kwanza,…tulia, fikria kwa makini, huku ukimuomba msaada mola wako, ili akupe utatuzi wenye busara, kumbuka jambo moja, kila jambo lina sababu yake, je hilo jambo lililokufanya ufikwe na hasira ulishalifahamu ni kwanini lilitokea, je ni kwa dhamira mbaya ya mtendaji au ni bahati mbaya….


Ni mimi: emu-three

No comments :