Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, July 23, 2018

YOTE NI KWA MAPENZI YA MUNGU-24


‘Sii hii hapa..inaita, ulisema haipatikani, eti mtaalamu kajificha, hahaha, kwanini ajifiche, eeh… tatizo lako wewe,  humfahamu vyema huyo mtu, mtaalamu sio mtu wa kuogopa ogopa mambo, hahaha …uwongo mwingine bwana.  hauna maana kabisa ndugu yangu…’akasema sasa akiwa anacheka, na mpelelezi  akamsogelea;

‘Nataka nihakikishe, hebu nipe hiyo simu…’mpelelezi akasema na Dalali kwa haraka akampa simu huyo mpelelezi, na mpelelezi akaichukua hiyo simu, akajifanya anaikagua ile namba, na niliona akibonyeza kiwambo cha spika ya nje.., wakati huo Dalali, yupo kwenye kucheka.

‘Hahaha…umeiona afande eeh, hiyo hapo inaita eeh…, hiyo sasa ndio namba yake halali, sio ile uliyokuwa ukiishuku,..sasa kama inaita, hiyo namba nyingine ni ya nani, hebu niambieni…’akasema Dalali.

‘Labda ana simu mbili je…’akasema …mpelelezi, halafu kwa haraka akasema;

‘Hebu tusikie akipokea kama ndio yeye…’akasema mpelelezi, simu ilikuwa inaendelea kuita tu, haipokelewi..

‘Sawa hamna shaka,  ngoja… atapokea sasa hivi, mara nyingi anakuwa na wateja wengi…kwahiyo anaweza asipokee hapo hapo…ila nakuthibitishia afande hii ndio namba yake aliyonipatia mimi…’ na mara sauti ikasikika..

Tuendelee na kisa chetu.
*********
‘Halloh, nani mwenzangu…’sauti hiyo ilitufanye sote tuangaliane, na Dalali hakujua kuwa mpelelezi kaweka sauti ya spika ya nje…kwahiyo sauti hiyo tuliisikia sote…na Dalali alivyoona hivyo…, akageuka kutuangalia,…

‘Sauti ya kike, huyo mtaalamu ni mwanamke kumbe.…’akasema mpelelezi.

‘Labda yupo nyumba ndogo…’nikasema kiutani, na Dalali akanitupia jicho, huku akijigonga gonga, kuipokea hiyo simu.

‘Ni..ni-na...eeh, …nataka kuongea na Mtalaamu…’akasema

‘Wewe ni nani…?’ sauti ikauliza na mtaalamu akabenua mdomo kidogo, nikajua ni kwanini anafanya hivyo.

‘Ninaweza kumpata mtaalamu, nina shida naye, ….’akasema

‘Ni wewe shemeji,….nimeigundua sauti yako,.. hebu niambie,mwenzako yupo wapi..’sauti ya kike ikauliza

‘Kwa-kwani, hayupo hapo nyumbani..?’ akauliza Dalali.

‘Angekuwepo nisingelikuuliza hivyo…watu wengi wanamtafuta, kwani kuna nini kimetokea, mbona mnaniweka roho juu,..mimi,…nilijua wewe upo naye, mbona sauti inasikika hivyo..’akasema

‘Kwani kuna nini, hakuna kitu shemeji …nita-nitakupigia baadae?’ akauliza Dalali, na alipoona sote tunasikiliza akasema hivyo na kukata simu.

 Akawa kainamisha kichwa chini, hakutaka kutuangalia machoni.

‘Kwanini umekata simu Dalali…., kwanini hujaongea na shemeji yako..?’ nikauliza

‘Kuongea na yeye kuhusu nini, huyo ni mke wa mtu, na sisi tunamtafuta Dalali, au sio…sikiliza…nahisi kuna tatizo limetokea..’akasema Dalali.

‘Basi ungelimuuliza huyo shemeji yako…, si rafiki yako, na mkewe anafahamu kuwa mpo naye,..awali ulisemaje..?’ nikamuuliza

‘Kwani mimi nilisema nini kibaya,…mimi najuana naye kwenye kazi zangu za udalali,..na nikaja kujuana naye zaidi, pale mtoto alipoanza hayo matatizo yake..’akasema Dalali.

‘Naomba hiyo namba yake…tafadhali..’nikasema

‘Namba ya nani..?’ akauliza Dalali akionyesha uso wa kushangaa.

‘Namba ya mtaalamu..’nikasema

‘Yanini..?’ akauliza

‘Nataka niongee naye, huyo shemeji yako..’nikasema

‘Afande,..huyu anataka mimi nionakane mbaya, kuwa nagawa namba za watu, halafu anataka kuongea na mke wa mtu, je mtaalamu akijua nimefanya hivyo, mimi nitakuja kueleweka vipi ..’akasema Dalali.

Dalali, akawa akimuangalia mpelelezi, na mpelelezi akabakia kimia tu. Na mimi nikasema;

‘Isiwe shida, hiyo namba yake ninayo, nilishapewa na watu wangu..’nikasema na sasa nikawa naitafuta kwenye simu yangu, sio simu ile niliyokuwa nimeiweka mezani..hii ni simu ndogo tu naitumia kwa dharura.

Nikasogea pale mezani nikachukua hiyo simu ya mezani nikaifauta namba…na kuiweka kwenye hiyo sim ndogo,nikawa naipiga hiyo namba..Dalali akawa ananiangalia kwa uso wa mashaka.

‘Halloh nani mwenzangu..?’ ilikuwa sauti ile ile ya kike

‘Naomba kuongea na Mtalaamu..’nikasema

‘Wewe ni nani..?’ akauliza

‘Mimi ni mmoja wa wagonjwa wake, kuna maagizo alinielekeza ..sasa kuna kitu nimekwama..tafadhali ni muhimu sana nataka kuongea naye, nisije kuvunja miiko..’nikasema na kukawa na ukimia fulani, baadae akasema;

‘Mtaalamu hayupo…’akasema

‘Oh,… kaenda wapi jamani nataka kuonana naye ni muhimu sana kwangu..’nikasema

‘Nimesema hayupo na wala sijui wapi kaelekea…kwani kuna kitu labda naweza kusaidia..?’ akauliza

‘Kwani na wewe unafahamu maswala ya matatizo  ya mizimu..kama utaweza kunisaidia nitashukuru sana..?’ nikamuuliza

‘Oh…hayo sijui kwakweli…kama ingelikuwa ni dawa hapo ningeliweza kujua jua kidogo…’akasema

‘Yamenitokea tena, na sijui nifanye nini… mimi haya mambo nilikuwa siyataki, lakini mke wangu akang’angania tu….sasa hata sijui tufanyeje…’nikasema, huku nikimuangalia Dalali, alikuwa akitaka kufanya kitu kwenye simu yake lakini anashindwa,..

‘Oh..kwakweli hayo mambo hata mimi siyajui, hayo ni mambo ya maruhani, ..na ni mpaka mwenyewe awepo apandishe ndio akuelekeze, siwezi kukusaidia kwa hilo, samahani…’akasema.

‘Oh, sasa huu ni mtihani,…samahani…nitakusumbua sana kwa maswali…’nikasema

‘Wewe uliza tu kama naweza nitakujibu..’akasema

‘Haya…mambo niliambiwa ni mizimu ya marehemu, anataka mambo fulani yafanyike, ..na mimi sikupenda kwakweli…kuna madhara yoyote naweza kupata..?’ nikauliza.

‘Kama uliambiwa yafanyike, nakushauri kaka yangu,..sijui ni kaka au ni baba, yafanye kama ulivyoelekezwa tu…, hayo mambo ya mizimu yana miiko yake,…’akasema

‘Ndio kuna miiko niliambiwa…sikupenda haya mambo kwakweli..’nikasema

‘Ina maana ni ya kutengeneza au ni ya kutumiwa au ni ya…mambo ya jadi..?’ akauliza

‘Mhh..hapo ndio nakwazika, …sikutaka kufahamu zaidi…’nikasema

‘Unajua kama ni ya jadi, ina maana wahenga wanahitajia jambo fulani, na ..kwa hilo ni muhimu ufanya wanavyotaka,..ila kama ni ya kutengeneza…ili upate jambo fulani..ni bora utekeleze hivyo vinginevyo yatakugeukia wewe mwenyewe…’akasema

‘Hapo sasa ndio sielewi, maana aliniambia ni mizmu, inamadai, marehemu ana kitu alikiacha, sio deni, lakini ni kitu aliahidi kwa mtu..’akasema

‘Kama ni kitu au ni deni ni lazima ifanyike ilivyosema mizimu,..kama ni deni ni lazima lilipwe, na kama ni maagizo kuwa jambo fulani lifanyike ni lazima lifanyike la sivyo …kuna matatizo mwaweza kuyapata…mabaya ni hayo ya kutumiwa,..sasa sijui wewe ni lipo kati ya hayo…?’ akauliza

‘Ni hilo la maagizo,…’nikasema
‘Unajua kuna watu wengine, wao wanapenda tu wafanyiewe kutimiza haja zao..wengine ndio hivyo ni kweli wanatokewa na matatizo,..kwahiyo kila mtu na tatizo lake, ndivyo nilijuavyo mimi…’ akasema.

‘Mhh…mimi hapo sasa nakuwa na wakti mgumu…sasa kwanini mtu aje kutengenezewa mambo ya hatari hivyo, mimi sitaki kabisa mambo hayo, ila kwa hili sikuwa na jinsi...’ nikasema.

‘Mimi nakushauri tu,…kama nilivyokuambia, sina ujuzi nayo zaidi, nisije kukudanganya…’akasema

‘Hakuna mtu mwingine ambaye aliwahi kufanyiwa, ambaye anayafahamu hayo mambo, ili niweze kumuulizia..?’ nikauliza

‘Mhh, ..mbona wapo wengi tu, mimi siwezi kukumbuka kila mtu na mambo kama hayo ni siri za watu na kila mtu anakuja na mambo yake,....siwezi kukusaidia kwa hilo..’akasema

‘Kuna jirani yangu mmoja naye alikuwa na matatizo hayo kwa mtoto wake anasumbuliwa sana, ..sijui naye nitamkuta labda anaweza kunisaidia…’nikasema

‘Ni nani huyo..?’ akauliza

‘Ni Dalali mmoja hivi….’nikasema, huku nikimuangalia Dalali, kiukweli alionekana hana raha, na mpelelezi alikuwa akimtupia jicho kuhakikisha hafanyi kitu.

‘Ok…kama ni huyo dalali ninayemfaamu mimi,..huyo ni rafiki yake mume wangu mkubwa, ukimpata huyo anaweza kufahamu wapi alipo huyo rafiki yake, lakini sasa, kuna tatizo…’akatulia

‘Tatizo gani tena…?’ nikauliza

‘Huyo Dalali, kanipigia simu, kasema na yeye hajui wapi alipo huyo rafiki yake, nay eye anamtafuta…, ila nikushauri kitu. mpigie au umpitie huyo huyo Dalali, anaweza kukusaidia …kweli naliwahi kusikia kitu kama hicho…’akasema

‘Kitu gani…jamani huenda kikaweza kunisaidia na mimi…?’ nikauliza

‘Kuna matatizo yake ya kifamilia… ana mtoto wake anasumbuliwa hivyo hivyo..ila sijui zaidi maana nilisikia juu kwa juu, mara nyingi wawili hao wakikutana nakuwa sipo….’akasema.


‘Yeye alinunua au ni tatizo tu la …kama unaweza kufahamu..?’ nikauliza

‘Hapo siwezi kukujibu..sijui kwakweli…’akasema

‘Unajua ni hivi kuna dawa huwa nilipewa ikitokea basi naitumia,sasa nimevukisha muda, niliambiwa isizidi mara tatu, sasa imeshazidi, hata sijui nifanyeje,, naogopa kuitumia tena..’nikasema

‘Mhh, hayo ndio masharti yake,..ila kiushauri , muone huyo huyo rafiki yake, ..anaweza kukusaidia…mengine wanasema tu, ukiona vipi humpati, wewe itumie tena tu hiyo dawa…huenda ikasaidia,…lakini sijui zaidi ya hapo mimi sijui..’akasema

‘Sawa ngoja nimpitie huyo rafiki yake, nashukuru sana kwa msaada wako, na kama umesema ni rafiki yake huenda akawa anafahamu fahamu kidogo…’nikasema

‘Huenda, …maana wanafahamiana sana,…wewe kamuulize tu na huenda keshamtafuta kwenye simu, mimi nitaendelea kumtafuta mume wangu, maana kuna watu wanamtafuta sana, nikimpata nitakupigia…’sauti ikasema

‘Ahsante sana…, nikimkosa huyo rafiki yake…, nitakupigia tena huenda ukanisaidia, maana hapa naogopa kweli na …nahitajia msaada wake kwa haraka..’nikasema

‘Pole sana…’sauti ikasema na mimi nikakata simu.

***************
‘Dalali, Dalali..wewe ulisema nini, kuwa huyo mtu hamjuani sana, mkewe anasema wewe ni rafiki yake mkubwa…’akasema mpelelezi.

‘Urafiki wetu ni kwenye kazi hizo za Udalali…’akasema

‘Na huyo  MTAALAMU, ni shahidi wangu wa pili….’mimi nikasema hivyo kwa sauti nikisisitizia neno ‘mtaalamu’.

‘Shahidi wa nini sasa…?’ akauliza Dalali, akiniangalia kwa uso uliojaa mashaka.

‘Kuthibitisha madai yangu..kuwa hilo deni sio halali ya marehemu,  na wewe na Dalali mnaweza kuahamu jambo..’nikasema,

‘Hahaha,..unajua usijifanye mbumbumbu…hilo deni linatoka benki na benki wana taratibu zao, sasa mimi nitahusikanaje na hilo deni eeh…’akasema akiniangalia, baadae akamgeukia mpelelezi na kusema

‘Afande hii kweli inaingia akilini, hebu nisaidie hapo kidogo,..na naah…mimi kwenda kwa mtaalamu eeh….ni kutokana na tatizo la mtoto,..unasikia sana,… vinginevyo, ..mimi ningeendelea kujuana na huyo mtu kwenye kazi za udalali tu..’akasema

‘Kwahiyo kujua jinsi gani hizo dawa zinatumika,…na ikitokea ufanye vipi, eeh… ni kutokana  na hilo tatizo, kabla ya hapo ulikuwa hufahamu chochote kuhusiana na matatizo kama hayo..?’ nikamuuliza.

‘Sikuwahi…mhhh, usilinganishe tatizo la mke wangu na hili, tatizo la mke wangu ilikuwa ni mashetani, alikumbwa na mashetani…lakini hili la hapa, ni mzimu ya marehemu ..yenyewe ilikuja kuwakilisha huo ujumbe wa hilo deni…’akasema

‘Swali ni kwanini awali ulikana kuwa wewe na huyo mtaalamu hamkuwa na usuhuba..?’ akaulizwa na mpelelezi.

‘Afande hayo ni mambo ya uganga wa kienyeji, sio mambo ya kujitangaza-tangaza ovyo….hakuna mtu anapenda kusema mimi najuana na mganga wa kienyeji, kweli s kweli, japokuwa watu hao wanatusaidia sana,….na kutokana na kazi zangu watu wanaweza kunifikiria vibaya..’akasema

‘Kwahiyo , kiuhalisia, huyo mtaalamu ni rafiki yako wa siku nyingi..?’ akaulizwa

‘Sio kivile…ni katika namna tu, siwezi kuelezea zaidi..’akasema

‘Dalali unanifahamu…mimi sipendi uwongo, kwa jinsi unavyolielezea hilo inaonekana kabisa kuna kitu unaficha, …mimi ninaweza kuamua kulichunguza hilo nikapata ukweli wake,…sasa nikiamua kufanya hivyo nikaja kugundua, sizani kama nitakuelewa, ..’akasema mpelelezi.

‘Afande mimi nifiche nini..siwezi kukuficha kitu afande..huyo mtu kujuana kwetu ni kutokana na kazi yangu ya udalali tu.. zaidi ni pale huyo mtoto alipoanza kuumwa..’akasema Dalali.

Mpelelezi akanigeukia mimi, …na mimi sikupoteza muda, nikamtupia swali Dalali,

‘Ni wapi unaweza kufahamu Dalali yupo..?’ nikamuuliza

‘Mimi sijui…’akasema

‘Afande unaweza kuniruhusu nikasoma mawasiliano yake kwenye simu yake..?’ nikauliza na hapo Dalali, akashikilia simu yake imara,…na afande akasema;
‘Hilo sio rahisi, labda Dalali awe kashukiwa na jambo fulani, je wewe unamshuku Dalali, kwa kosa lolote..?’ akaniuliza afande.

‘Mimi nataka kufahamu wapo alipo huyo mtaalamu, huyo mtaalamu  ..ni shahidi yangu muhimu sana..’nikasema

Mpelelezi akageuka kumuangalia Dalali, akasema;

‘Kuna namna moja ya kukuweka wewe salama; ama utuambie wapi alipo huyo mtaalamu, au utupatie hiyo simu yako…tusome jinsi gani mlivyokuwa mkiwasiliana naye..’akasema mpelelezi.

Dalali, akabadilika sura…halafu akasema

‘Kwanini mnataka kufanya hivyo, mimi nina kosa gani..?’ akauliza

‘Ndugu yetu hapa kakushuku kuwa wewe unaweza ukawa na namna fulani ya hilo deni,…shutuma hizo kakuelekeza kwako na kwa mtaalamu…’akasema mpelelezi

‘Kama una shutuma kama hizo, basi yeye afuate taratibu,…si taratibu zipo jamani,.. je mimi ni mhalafu, ni mhalifu wa kosa gani, hayo yapo wazi au sio afande…?’ akauliza Dalali sasa kwa kujiamini.

‘Unashukiwa…’akasema mpelelezi

‘Je huu ndio utaratibu..afande,…maana mimi sina wasiwasi kwa hilo..kama wewe utaona kuwa huo ndio utaratibu sawa, mimi nitakupatia hii simu usome kila kitu, lakini kama sio utaratibu, mimi nitalifikisha hili jambo huko kituoni kwenu..’akasema mpelelezi,

Mpelelezi akaniangalia mimi..

‘Afande..wewe upo kazini, unamekuja kumuhoji Dalali, na katika kazi yako, unaruhusiwa kumchunguza mtu, kuhakiki maelezo yake, je hapo umekosea..?’ nikauliza

‘Huwezi kunifundisha kazi, na ukiona sifanyi jambo fulani, ujue kuna namna ambayo ..natakiwa kuifuatilia, sioni kama kuna umuhimu wa mimi kuchukua simu yake huyu jamaa na kuanza kuisoma, labda unithibitishie kuwa huyu mtu ni mhalifu..’akasema Mpelelezi.

‘Nimeshakuambia kuwa Dalali, ndiye anaweza kutufikisha huko alipo huyo mtaalamu, na mtaalamu ni shahidi wangu ..’nikasema

‘Kwenye kosa gani..?’ akauliza Dalali.

‘Nafuatilia uhalali wa deni..’nikasema

‘Deni la nani..?’ akauliza

‘NI deni linalokisiwa eti ni la marehemu, kitu ambachp nataka kukihakikishia kuwa sio sahihi kwake hilo deni sio la marehemu..’nikasema

‘Wewe kama nani..?’kauliza Dalali

‘Kama mtu niliyeteuliwa na mama mjane kulifuatilia hilo na kulinda haki zake mama mjane na mayatima, ..’nikasema

‘Na mimi ni nani wa marehemu..kabla sijamuuliza Shemeji kuthibitisha kauli yako..?’ akauliza Dalali.

‘Wewe ni ndugu yake marehemu..’nikasema

‘Mimi na wewe ni nani ana uchungu zaidi kwa marehemu..?’ akauliza Dalali

‘Huo ni mmoja wa ushahidi wangu mahakamani..’nikasema

‘Kwa vipi sasa mbona hueleweki.?’ Akauliza

‘Kama nilivyoelezea awali…unataka nikufafanulie tena..’nikasema

‘Wewe bwana usilete ubabaishaji hapa, mimi nimeshaelewa lengo lako, ni kutafuta pesa tu, ..hupati kitu hapa..’akasema

‘Kutafuta pesa za nini…?’ nikauliza

‘Si za uwakili au…wewe hapa siumesema unafuatilia uhalali wa hilo deni, sasa unafanyaje hilo…eeh, niambie,..au,..usiniambie kuwa wewe unafanya kazi hii bure, ujue mimi ndiye mwenye mamlaka ya wewe kulipwa..’akasema

‘Wapi nilisema nafanya hii kazi kama wakili, au wapi niliandikishiana na wewe kuwa naifanye hii kazi kwa malipo kadhaa..?’ nikauliza

‘Ndio maana niliwahi kusema wewe ni tapeli..kwanini uje kuingilia familia hii na kujifanya unatafuta ukweli, wakati mimi mwenyewe sijakuruhusu..shemeji hawezi kufanya jambo bila ridhaa yangu, mimi ndiye msimamizi wa hii familia.

‘Na huo ndio ushahidi wangu mahakamani…’nikasema

‘Afande unemuelewa huyu mtu…’akasema Dalali akiniangalia mimi machoni, na afande akawa kimia,na mimi nikasema;

‘Tuambie ni wapi mtaalamu kajificha..’nikasema

‘Mimi sijui…’akasema

‘Basi tupatie simu yako, tusome ujumbe,..maana kuna ujumbe umetumwa kwako, utakaousaidia sis kufahamu wapi huyo mtu kajificha..’nikasema

‘Una uhakika na hiyo shutuma yako..?’akauliza Dalali kwa kujiamini

‘Kama huna wasiwasi na hilo, kwanini unaogopa kutoa hiyo simu yako..?’ nikauliza

‘Kwasababu hii simu ni yangu, kuna mambo yangu mengi ya kikazi, na mimi sikuamini,..unaweza ukawa ni tapeli wa kutaka kufanya jambo…’akasema

‘Kwahiyo wewe huamini kuwa mimi nafanya hili jambo kwa masilahi ya familia, kwa nia ya kutafuta ukweli wa hilo deni..?’ nikamuuliza

‘Mimi sikuamini, ..maana sijakutafuta kwa kazi hiyo, sijui labda shemeji aniambie..’akasema akiashiria kwa shemeji yake bila kumuangalia usoni.

‘Utanitafutaje wakati unafahamu fika kuwa wewe unahusika kwa namna fulani …’nikasema

‘Kuhusika kwa vipi, mimi sasa nataka uwe muwazi kwangu, je unanishuku, je mimi nina kosa gani, uweke wazi, kwa uthibitisho, vinginevyo mimi sasa nitalifikisha hili jambo mbele ya sheria..’akasema kwa kujiamini kabisa

‘Nitathibitisha ukinipatia hiyo simu yako, tukasoma ujumbe uliondikiwa na mtaalamu…na hiyo simu kuanzia sasa ni  ushahidii wangu mahakamani, afande, mimi ninakuarifu kuwa simu hiyo ina ushahidi wa ninachokishuku kwa huyu mtu..’nikasema

‘Kwahiyo wewe unanishuku, kuwa nina kosa..kosa gani…?’ akauliza Dalali

‘Ukinipatia hiyo simu nitalithibitisha hilo,..hiyo simu ina ushahidi wangu muhimu wa kulithibitisha hilo..’nikasema, na mara …

Dalali sasa akamgeukia shemeji yake, na kusema

‘Je shemeji wewe umemchukua huyu mtu …?’ akauliza

‘Kumchukua…?’ shemeji akauliza kwa mshangao

‘Ndio nataka kufahamu je umemchukua huyu mtu kuwa wakili wa kutafuta ukweli wa hilo deni,..niambie ukweli shemeji, maana mimi nina haki ya kulifahamu hilo,..vinginevyo wewe uniambie kuwa mimi huniamini..’akasema sasa akimuangalia shemeji yake usoni.

NB: Tuishie hapo kwa leo.

WAZO LA LEO: Unapojikuta upo kati kati ya kutoa ushahidi wa pande mbili, ushahid ambao, ukiutoa unaweza kuleta sintofahamu kutoka kwa pande mbili, za marafiki wako wakubwa…marafiki ambao ni maadui wenyewe kwa wenyewe..ina maana ukisema hivi utamkwanza mwingine na ukisema hivi utamkwanza mwingine,..je utafanya nini…?
Wakati wote fahamu jambo moja, HAKI ina thamani kubwa sana, na haki husimamiwa na UKWELI. Ongea yaliyo ukweli hata kama utavunja urafiki wako kwa rafiki yako mkubwa , na haki hiyo itakuja kukulinda baadaye kwa huyo huyo rafiki , pale ukweli utapokuwa bayana.



Ni mimi: emu-three

No comments :