Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Friday, June 22, 2018

YOTE HAYO NI KWA MAPENZI YA MUNGU-13



‘’….sikiliza kama wewe unataka kuyachokonoa haya mambo sawa endelea, …ila … Ila mimi  nakuasa kitu kimoja, …hayo unayotaka kuyafanya wewe, unanisikia eeh, yalishafanyika, sitaki kurudia rudia, matokea yake yakawa hivyo…unasikia,…’akaninyoshea kidole, na kumuonyeshea yule mtoto.

Mimi sikusema jambo, nikawa namsikiliza tu.
‘Sasa eeh,… kuanzia sasa, wewe ndiwe utakuwa na dhamana ya huyo mtoto, na familia kwa ujumla, … umesikia nilivyo kuambia…lolote likitokea …mimi simo..tusije kulaumiana...’akasema akionyesha kama ananawa mikono.

 Mimi nikawa na muangalia tu, baadae naye akatulia, hapo na mimi nikaanza kuongea, nikasema;.

‘Hivi kwanini nyie watu mnapenda kuwatumia watoto kwenye mambo yenu, ya kishirikina….’nikasema hivyo na huku namuangalia kwa makini
Nilimuona , akaonyesha dalili ya kushtuka kidogo, lakini akajikausha, halafu akatoa lile tabasamu lake la dharau, akatikisa kichwa, halafu akasema.

‘Eti nini…?’ akauliza akiwa haniangalii moja kwa moja usoni…

‘Umenisikia vyema, …haya yanayofanyika, kwa jinsi ninavyoona mimi, hivi vitisho..kumtesa mtoto, kuna jambo, na nahisi haya yamefanyika kwa makusudi fulani,…, na wewe iavyoonekana, unajua hili jambo,…’nikasema nikionyesha kujiamini na yeye hapo akakunja uso, halafu akatikisa kichwa , baadae akatabasamu na kusema;

‘Unajua nini… kwa vile ni mimi ndiye niliyekwenda huko kwa huyo mtaalamu, siwezi kunyamaza, hata useme nini, mimi nafahamu madhara yake, kufahamu kwangu ndio huko zaidi ya hayo, ni yako wewe…unasikia, . wewe hujui tu…’halafu akamgeukia shemeji yake, akasema;

‘Shemeji mimi naogopa sana hili jambo,… hivi likitokea la kutokea, tutasema nini, utanilaumu mimi, utamlaumu nani, mimi sikukuambia…sitaki ije kuwa lawama kwangu, najua hata mimi nitaumia, maana hao, ni watoto wangu, ni damu yangu, kaka na mimi haina tofauti …’akasema, akimuangalai shemeji yake, halafu mimi.

Mimi nikaendelea kukaa kimia, huku nikiangalia simu yangu ikiwa pale mezani,..nilikuwa nasuburia taarifa muhimu kutoka kwa vijana wangu, niliona wamechelewa kunipatia taarifa muhimu…nikaona niendelee kumchokoza huyu jamaa.

‘Wewe ni baba yake au sio…?’ nikasema kwa kuuliza

‘Sikiliza Bro, ni kweli mimi ni baba yake, na nimejitoa kwa kila hali, sasa ni nini nakipata kwa dhamana hiyo…eeh,…, ni nani anayejali kujitolea kwangu huko, hebu niambie…, na sasa hata wewe unafikia kusema hayo maneno ya kipuuzi kabisa.., unajua inaniuama sana…’akasema.

‘Maneno gani ya kipuuzi, wewe unayaona hivyo, lakini ni lazima ukweli usemwe au sio, na hayo niliyokuambia ni ukweli mtupu…’nikasema

‘Ukweli gani…?’ akaniuliza akinikazia macho

‘Kuhusu hivyo vitisho kwa mtoto, ina maana gani hapo…kuwa labda na wewe unajua kinachoendelea, ndio maana kila tukijaribu kuitafuta haki, wewe unatishia, kwanini ufanye hivyo, kama huhusiki…’nikasema

‘Kuhusika kwangu ni kama nilivyokuambia, ni kwa vile niliongea na huyo mtaalamu, akaniambia jinsi inavyotokea, kuna kosa gani kwa hilo, ina maana ningelitakiwa nikae kimia, au..hapana siwezi kufanya hivyo, maana hawa watoto ni wangu pia, na siwezi…..’nikamkatisha hapo na kusema;

‘Ndio ulikutana naye kabla..mkaongea naye, mkapanga..yawezekana kuwa hivyo, au sio..ndio mlipokwenda na shemeji yako, mka…’akanikatisha

‘Kwanini nifanye hivyo..?’ akauliza kwa haraka.

‘Naongelea hili kwa mtizamo wa haya yanayotokea,..kwanini uwe mshabiki sana wa mambo hayo…’nikasema na hapo, akanikodolea macho, nilijua labda atakasirika, lakini badala yake akatabasamu, na kusema;

‘Unajua…mimi sivyo, kama unavyofikiria wewe…nawafahamu sana nyie watu,…mimi nakustahi tu, maana nimekutana na watu wengi kama wewe…, ila mimi, …bado nazidi kusisitiza…bado nazidi kutoa angalizo, maana mimi nafahamu madhara yake…’akasema

‘Najua unalifahamu hilo, …lengo la watu wako, ni kumtesa mtoto ili mfanikiwe malengo yenu,..sasa niwaulize tu,..mtapata faida gani, nyie si muna watoto hebu fikiria hayo yangelitokea kwa mtoto wako ungelijisikiaje, eeh…’nikasema

Na kwa muda ule mtoto alishaamuka, akawa anajitahidi kukaa , lakini kwa jinsi anavyoonekana, nahisi bado yupo kwenye mateso ya joto la homa, sikutaka kumtia mama yake wasiwasi, nikatulia kwanza,…na mama yake, sasa akawa anamuangalia mtoto wake kwa mashaka pia, …akamsogelea

Mama mjane alipomshika mtoto wake tu, …nikajua sasa mtoto keshaanza kuchemka tena. Kwa hali ile, mama, akawa sasa anaonyesha kuchanganyikiwa,…naona alishachoka na mates ohayo ya mtoto wake..mimi nikajipa moyo, moyoni nikawa namuomba mungu, namuomba anipe hekima. Ni kweli kwa hali ile ungelisema basi, ngoja tuache tu..lakini je hiyo ndio njia sahihi,…

Jamaa alipomuangalia shemeji yake, akasema;

‘Kama mtoto keshaanza kuumwa kivile anavyoumwa,..na ikifikia kupoteza fahamu.., mimi sina zaidi…na alisema ikifikia joto kuisha ghafla, na mtoto kuwa baridi ndio basi tena…maana hiyo dawa haitakuwa na nguvu tena…mimi nilishawaambia..msije kunilaumu, mimi sipo, kwanza ngoja niondoke zangu …’akasema sasa akitaka kusimama kuondoka;

‘Unakwenda wapi sasa, na kwani sisi tumefanya nini kibaya, eeh, niambie wewe mliyepanga hayo, sisi tumefanya nini kibaya,…..?’ nikamuuliza.

‘Mimi nimekuelezea inavyotakiwa iwe, hujataka kunisikiliza, sasa nikae hapa nikisubiria nini..maana mimi sijui malengo yenu ni nini,..na hao mizimu wanajua lengo lenu ni nin, mimi utanidanganya, je hao…nyie jamani, mnataka nini.. kumuua huyu mtoto au…mbona mna tamaa ya mali hivyo,…mimi sitaweza kulivumilia hilo…na kama baba, bora wewe uondoke humu ndani…au sio shemeji…’jamaa akasema akimuangalia shemeji yake

‘Mimi sitatoka hapa mpaka tumalizane mimi na wewe…’nikasema

‘Wewe kama nani…?’ akaniuliza sasa kwa sauti ya ubabe.

‘Kama mtu anayejali wanyonge, anayejali haki za mjane na mayatima, ..na kwa hili nitahakikisha haki imepatikana, …’nikasema

‘Hahaha…unajua, ..shemeji, huyo …unajua, ..hata sijui niseme nini, yule mtu wa kutetea mayatima na wajane, anaitwa nani…alikuja hapa, alisema nini, kauli zao ni hizo hizo…mimi sioni ajabu, maana kila mtu anatafuta riziki mezani kwake,..na huyo na wenzake, kazi zao ni hizo, sisi hatuna pesa za kuwalipa, msipoteze muda wenu bure….’akasema.

‘Hahaha, nani kakuambia nafanya haya kwa ajili ya malipo..sikiliza Dalali…hilo la mtoto kuumwa wala usijali kabisa, mimi nitabeba dhamana yake…kama kweli sote tunamuamini mungu, basi mtoto huyo, hayo ya mateso yatakwisha…, atakuwa kwenye kinga ya yule aliyemuumba,…labda mmoja wetu hapa awe anahusika kwa hilo…’nikasema bila kujali maneno yake.

‘Unasema…nini,…!!? Nani anahusika hapa, usitake kutuchanganya hapa, anayehusika na lolote dhidi ya mtoto ni wewe unayetaka kuleta mambo kinyume na matakwa ya mizimu…?’ akauliza kama kukasirika.

Mimi pale nikamsogelea yule mtoto, nikamshika, mwili ulishaanza joto, na niliona kama  joto linazidi kuongezeka…sikukata tamaa, nikachukua gilasi ya maji, nikaanza kuyaombea …huku nahisi machozi yakitaka kutokana na maombi yangu,…niliona taswira ya huyo mtoto kwenye hisia, akiwa hajiwezi, …nilihisi vibaya sana, ..baadae nikamsogelea yule mtoto…nikamshika shavuni…joto kali sana.

Sikujali tena,…sikutishika kama awali… nikamwambia huyo mama mjane;
‘Mpe mtoto haya maji anywe, kwa nguvu za muumba, hayo yote kama ni kwa nguvu za giza yatatoka hayo mapepo na mashetani, na vibwengo, mizimu na watu wake…, kama ni kwa majaliwa yake yeye aliyetuumba,..basi tumuomba yeye atusaidie, amponyeshe huyu mtoto kwa uwezo wake…’nikasema na mama akampa mtoto yake maji..

Haikupita dakika moja…Mtoto alitokwa na jasho, utafikiri kamwagiwa maji, kwa muda mfupi tu…akalala…

***********

‘Sasa tuanze kuulizana maswali, kumbuka mimi ninachotaka kutoka kwako ni ukweli, na sina nia mbaya, unasikia, …’nikasema, jamaa sasa ananitolea macho kama mtu aliyeona kitu cha kutisha

‘Shemeji vipi mtoto…’jamaa akasema akimuangalia mtoto…mimi nikasema;.

‘Mungu atamjalia, na atamlinda, sisi tuendelee au sio..’nikasema

‘Oh….afadhali kama mtoto katulia basi, afadhali lakini mimi naomba jambo moja, kwanini tunafanya haya, wakati tunafahamu kuna hatari, maana kutulia huko ni kwa muda tu, kama bado lengo lenu ni lile lile..hali itaendelea kuwa hivyo…’akasema

‘Wewe unajuaje hayo..?’ nikamuuliza

‘Majibu yangu ni yale yale….’akasema

‘Sikiliza, wewe sasa naanza kukuhisi vibaya..’nikasema

‘Kwanini…?’ akauliza

‘Sema ukweli wako, wewe kuna kitu unakifahamu na unatuficha, nahisi kuna njama mumezipanga wewe na wenzako…’nikasema na yeye hapo akajirudi, akatulia.

‘Kitu gani yakhe…kauli zako ni hizo hizo, jaribu nyingine, mimi sina zaidi ya hayo niliyokuambia, unielewe kabisa, au…unataka nifanye nini, ili uniamini…?’ akauliza

‘Huko kwa huyo mganga, ulionyeshwa na nani, sio kwamba mnafahamiana naye siku nyingi…?’ nikamuuliza

‘Kuonyeshwa na nani kwa vipi…?’ akauliza
‘Wewe ulisema mtoto alipoanza kuumwa, ulishauriwa uende huko, au sio..au wewe uliona ufanye hivyo ili mukamilishe mipango yenu..?’ nikamuuliza

‘Ni kweli kwenda huko nilishauriwa na mtu, mimi nilikuwa simfahamu huyo mtu..’akasema

‘Ni nani alikushauri uende huko…?’ nikamuuliza

‘Haikuhusu, ni nani, siwezi kukuambia…’akasema

‘Inanihusu, ..nataka kumfahamu huyo mtu mliyeshirikiana naye…, la sivyo, ni wewe ulipanga uende huko, ili kufanikisha malengo yenu…ndio maana nasema wewe unafahamu ni nini kinechoendelea, wewe unajua ….’nikasema

‘Nijuavyo mimi ni hivyo nilivyowaambia…’akasema

‘Sio kwamba mlipanga na huyo mtu, mnayemuita mtaalamu ili haya yafanyike ili mfanikiwe kwenye malengo yenu…?’ nikauliza

Malengo gani, wewe mtu mbona unaropoka sana, nakushauri kitu, uwe makini na hayo maneno yako…nitake radhi tafadhali, …tatizo wewe huelewi mambo ya mizimu ndio maana unaongea lugha chafu kama hizo, siwezi kukulaumu, nakusamahe tu....ungelifahamu mambo hayo, wala usingethubutu, sasa sikiliza…’akasema sasa akininyoshea kidole.

‘Hao mizimu kama wanaitakia mema hii familia, familia ya marehemu, walitakiwa wasifanye hivyo, nijuavyo mimi, eeh,.. marehemu aliipenda sana hii familia, …na akajenga nyumba hii imara ili waje kuishi familia yake na hadi vitukuu, na vitukuu, kweli si kweli…?’nikasema kama kuuliza.

‘Huko tunarudi nyumba, na kupote muda, samahani lakini….’akasema

‘Nakuuliza sasa ni kweli si kweli, nataka kusikia kauli yako … wewe hukuwahi kumsikia kaka yako akisema hivyo..kuwa hii nyumba wataishi hadi vitukuu, je kwanini sasa iuzwe….?’nikamuuliza

‘Kaka eehn …ndio, niliwahi kumsikia akisema hivyo, tena mara nyingi sana, lakini sasa, unajua ndio maana sisi hatukuamini, mpka tukafika mahakamani, unielewe ndugu yangu…’akasema

‘Sasa kwanini hao mizimu wawe kinyume na kauli ya kaka yako, kama sio maadui wa kaka yako…na..kwanini unavurugwa akili na vitu kama hivyo hadi ufikie kuikana kauli ya kaka yako,… ?’ nikamuuliza

‘Jibu ni lile lile….’akasema
‘Ndio maana  mimi nakutilia wewe mashaka, unanifanya nikushuku vibaya, maana kama kweli wewe ungelikuwa upande wa kaka yako, ungeipigania hiyo kauli yake,..hadi hatua ya mwishi na ili, twende sawa, nahitaji muda wa maswali mimi na wewe…’nikasema

‘Sikiliza, mimi sijaikana kabisa kauli ya kaka… na sikuwa tayari kufanya hivyo,…mimi ninachotaka kukifanya ni kuhakikisha, kwanza hii familia ipo salama, pili roho ya marehemu inastarehe peponi, mimi nina uhakika kutokana na hili deni kaka huko alipo anateseka,..na…na sitaki kitu kitokee kwa hii familia pia….’akasema akionyesha uso wa uchungu, na mikono ikiwa mbele kama ananiomba mimi.

 Aliponiona mimi nipo kimia, akamgeukia shemeji yake, akasema;.

‘Shemeji mbona upo kimia, kwanini hunisaidii…hivi umesahau tulivyohangaika hadi hayo yanatokea kwa mtoto eeh,…muda wote najaribu kukuuliza ili unisaidie, lakini yaonekana kama nipo kivyangu, ..haya bwana,…niachie nihangaike na watoto wangu, sitachoka kwa hilo…’akasema.

‘Shemeji yako, anafahamu kabisa kuwa hilo deni sio stahiki ya mume wake, shemeji yako, anajua kabisa, hii nyumba haitakiwi kuuzwa, ila hana jinsi ya kufanya, jinsi ya kufanya ni sisi tumsaidie yeye, je kumsaidia kwake ndio huko…kumtesea mtoto wake…’nikasema

‘Ni nani anayemtesea mtoto wake…hayo ni maneno yako..na siyapendi. Nisikilize, mimi sitai hizo kauli zako, ..shemeji yeye anaogopa kujibu tu hapa, alishasema kama ni nyumba iuzwe tu, yeye hataki tena hayo mambo, alishakubaliana na mizimu…ili wao wawe na amani…sasa ni wewe unayekuja kuharibui…’akasema

 ‘Tunapoteza muda…au sio…’nikasema

‘Ingelikuwa nimekwenda mwenye ungesema labda, lakini  nimeshakuambia mimi nilikwenda an ndugu yake shemeji, na kwa msisitizo mimi narudia tena, ile hali ya mtoto haitakiwi ijirudie zaidi ya tatu,….’akasema na simu yake ikatoa mlio wa ujumbe wa maneno, akaitizama

‘Sasa ….., unaona  eeh,….’akawa anasoma huo ujumbe, huku anaongea…na akatikisa kichwa kama anakubali kitu.

‘Shemu, mambo ya mahakama, yakianza hapa, mimi sijui itakuwa….tafadhali ndugu zanguni, mimi inaniuma sana, mimi sasa ndiye baba yake, nitaulizwa kwa hili,….mnielewe jamani,  shemeji hebu mwambie huyu ndugu yako...’akasema akimwangalia shemeji yake

‘Tafadhali…’shemeji akaanza kuongea, nikaona nikimpa muda huo naye ataungana na shemeji yake mimi nikasema;

‘Sasa kwani tatizo lipo wapi hapa,  kwanini unaogopa hayo maswalii yangu,  mbona unakuja juu kama unajihami, una wasiwasi gani, je mimi kwa kuulizana hayo maswali tutakuwa tumekiuka hiyo miiko…ina maana hiyo miiko inasema tusiulizane maswali, tusitake kujua ukweli, kama ni hivyo basi kuna kitu kingine zaidi ya hicho, mimi nimeshamuomba mungu, mizimu imeondoka, haya tuendele…’nikasema

 Kabla hatujaanza kuongea mara tukasikia sauti ya ukelele kutoka ndani…sasa ni yule mkubwa, alikuwa kalala ndani, mara akatoka, akiwa katoa jicho, ….la kuashiria anaogopa

‘Ni nini na wewe..?’ akauliza mama yake

‘Simba….mama, simba anataka kunitafuna….’akasema akionyesha ndani,…mimi nikawa nimetulia huku namtupia jicho la kujiiba huyo jamaa, ambaye alionyesha na yeye uso wa kushangaa,…kiukweli huwezi kumshuku lolote, kama anaigiza basi huyu jamaa ni mtaalamu.

‘Hakuna simba wewe ulikuwa unaota tu..’akasema mama mtu lakini usoni alionekana kuwa na uso wa mashaka.

‘Hebu nikaangalie huko ndani mimi mwenyewe, tusije kusema hakuna , kumbe kweli kuna kitu…’akasema huyo baba mtu akitembea kuelekea huko ndani, alipokuwa kalala huyo mtoto, baadae akarudi…akasema

‘Hakuna kitu, hizo ni ndoto, lakini ndoto kama hizo, kaulizie, hayo ni mashetani…hebu kijana wangu usiogope, hakuna simba, niambie vizuri, wewe uliota nini…?’ akawa kachuchumaa akiongea na huyo mtoto.

‘Sijaota, nimemuona simba huko ndani…alitokea mlangoni, akawa anakuja pale nilipolala kitandani, nimemuona kwa macho yangu,..sijaota mimi..’akasema

‘Yupoje huyo simba…?’ akamuuliza

‘Mkubwa kama ng’ombe, ana meno ya kutisha…’akasema

‘Unaona..haya haya….aliyasema huyo yule mtaalamu, hao..sasa ni mashetani…ni lazima yaje kwa mbinu hizo, …maana hatutaki kuwatii mizimu…unajua nikuambie kitu ndugu yangu, mizimu wao wanatupenda, ..na mara nyingi wanapambana na hayo mashetani, sasa tusipokuwa upande wao, na wao wanayaachia hayo madude yapambane na sisi, ili tujifunze…’akasema

‘Mashetani sio..ndio ndio hao hao mizimu  umekubali wewe mwenyewe sasa…’nikasema
‘Nimeshakuambia kuna mashetani na mizimu…mashetani ndio hao wabaya, wanataka kuumiza, lakini mizimu wanasaidia, wanapambana na hao mashetani,..mizimu wao wanatusaidia kutukumbushia…’akasema.

‘Kwa kumtesa mtoto..au ni watu wanatumia mbinu hizo, kumtesa mtoto, ili mama yake aogope, na kukubaliana na matakwa yenu…’nikasema, nilikuwa napoteza muda, maana kuna jambo muhimu nilikuwa nalisubiria, na sikutaka huyu jamaa aondoke.

‘Chunga kauli yako ndugu, mizimu wanakuwa mwilini kwa nia ya kukumbushia tu, maana deni ni lazima lilipwe, halina ujanja wa kukwepa…’akasema akinionyeshea kidole.

Kukawa na ukimia kidogo,halafu mimi nikasema;

 ‘Ndio tuendelee…sasa, kuna taarifa nazisubiria, mimi ninataka wewe, na huyo mtaalamu wako, muwe mashahidi mahakamani, muyaelezee hayo maneno mahakamani, ili tujirizishe kuwa kweli hamjapanga hizo mbinu…’nikasema

‘Mimi sikuelewi, hebu niambie kwanini unarudia rudia hayo maneno, una uhakika gani na hicho unachokisema, maana hiyo sio kauli nzuri, nani kapanga hayo, mimi najua kuzungumza na mizimu…?’ akaniuliza akigeuka kidogo kumwangalia mtoto, au shemeji, halafu akageuka kuniangalia mimi lakini kwa jicho la pembeni.

 ‘Wewe unajifanya hujui….unajifanya hujui ni kitu gani kinachoendelea kwa huyu mtoto, na kwanini yeye atumiwe kwenye shinikizo la hilo deni,, yeye kama mtoto…hajui kabisa kinachoendelea..’nikasema nikimkimuangalia moja kwamoja usoni, nia yangu ni kumchanganya kichwa, akasirike. Mtu akikasirika huropoka ovyo…

Ilikuwa kama nimemmwagia maji, akataka kusema kitu, lakini kikawa hakitoki, akatikisa kichwa, halafu akasema;

‘Unajua mimi nilikuheshimu sana, nilikuona ni mtu wa maana, sasa sijui nikuite nani, nimejaribu kukulezea kwa busara, lakini wewe hutaki kunielewa, na sasa unataka shari na mimi, unajua wewe hunifahamu mimi nilivyo, mimi ni mtu mpole sana, nina tabia ya subira lakini ikija kunitoka, hutaamini,….’akasema akitikisa kichwa.

‘Nakufahamu sana, wewe ni dalali, na mbinu zako za udalali zinajulikana, ukitaka kitu ni lazima ukipate, si ndio hivyo ulivyo…, kwa njia yoyote ile utakipata, umekuwa ukisema maneno hayo, kweli si kweli..?’nikasema.

‘Ni nani kakuambia hayo, ni kweli ndivyo nilivyo, lakini sio kwa dhuluma, halafu dhuluma kwa familia yangu, jipange vingine ndugu yangu…’akasema

‘Nitakuja kulithibitisha hilo, kuwa wewe una tabia hiyo ndio maana ulikwenda kwa huyo mtaalamu..’nikasema

‘Shemeji huyu mtu  ni nani kwako…..?’ akauliza

‘Unataka kujua mimi ni nani eeh…?’ nikamuuliza, nikawa kama najipapasa hivi, akawa ananiangalia,..nikajifanya kama nimekumbuka, nikasogea pale nilipoweka simu, nikaichukua, nikawa naangalia kama simu bado inauwezo wa kupokea hayo mazuungumzo, ilikuwa imesimama, nikaiweka sawa.

 Kabla ya hapo, nikapiga namba ya askari mmoja ninayemfahamu, nikaongea

‘Upo kituoni…mimi ni afande wako..hahaha, hii namba ngeni ndio, ile ya mwanzo nimeiacha, kabisa, ni lazima..sasa..’nikasema

‘Nataka unisaidie jambo dogo, unaweza kuja na gari, kuna yule mtu niliyekuwa nikikuambia, ninaye hapa…’nikasema, na kutulia

‘Ndio nataka twende naye hadi huko kwa mtaalamu wake, maana anawatesa sana hawa watoto..’nikasema

Jamaa sasa akawa ananiangalia kwa mashaka.       Na wakati huo huo, nilimuona mama mjane akihangaika na mtoto, nikamtupia macho, ..na mara mama huyo akasema;

‘Jamani mimi nimechoka na haya mambo, mtoto anaumwa, na keshaanza kuwa baridi sehemu ya miguuni, japokuwa usoni kuna joto sana..miguu utafikiri haina uhai,…jamani, mtoyo wangu jamani, hii sio kawaida…’akasema mjane

‘Mimi nilishasema, sina namna ya kufanya kama hali ya mtoto ikijirudia, kama homa ikimpanda tena, dawa tuliyopewa haiwezi tena kufanya kazi,…. hiyo ni  kutokana na mtaalamu alivyosema,…mimi kwa hivi sasa siwezi kufanya chochote ni miiko niliyopewa, ile dawa haitakiwi tena kutumika,…’jamaa akasema na hapo ndio akazidi kumchanga mama mjane

Mtoto alikuwa kalegea, ilionyesha kabisa pale mama alipompakata yule mtoto shingo kama sio yake, kalegea kupitiliza

‘Jamani mwanangu imekuwaje…’akasema huyo mama, na mimi kwa haraka nikasogea, sasa kumshika mtoto yule mtoto, sasa sio joto tena, mtoto keshakuwa mkavu, kakauka kabisa,..macho kayatoa

‘Mungu wangu..’mimi nikajikuta nimesema hivyo

‘Mumeona eeh,mimi niliwaambia..’akasema jamaa
Mama naye kuona vile, akadondoka….akapoteza fahamu…

NB: Imebidi sehemu hii nikatishe hivyo


WAZO LA LEO: Binadamu tumefikia hatua ya kuthamini mali zaidi ya utu wa mtu, watu wengine wapo tayari hata kuwafanya watoto wao mazezeta, ili tu watajirike, wengine, wanaua kabisa,..tujiulize hizo mali zitatufanya tushi milele, ..haiwezekani, kila nafsi ni lazima ije kuonja umauti na mwisho wa yote ni hukumu, ambapo kila ulichokifanya hapa duniani utakuja kuhukumiwa nacho…..wengine mateso yao wanaanzia kuyapatia hapa hapa duniani, je hatujawahi kuyaona hayo? 
Ni mimi: emu-three

No comments :