Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Wednesday, May 23, 2018

YOTE NI MAPENZI YA MUNGU-2


 Mama yule sasa akanigeukia lakini akiwa kainamisha kichwa chini, ….akainua kichwa kidogo, kiasi cha kunitupia jicho,..sasa nikaweza kuuona uso wake, nilichokiona kwake ni taswira ya huzuni na kukata tamaa. 

Ukimuangalia huyu mama kimavazi, kiukweli, nguo zake zilikuwa kuu kuu, na hali aliyo nayo ni kama mtu aliyechanganyikiwa, nywele aliziacha zikawa timu timu, niliziona awali,japokuwa aliponiona alikimbilia kufunika kichwa chake.

 Alivyoniangalai ile ya haraka, niliona  machozi,….hapo nikawa na uhakika kuwa kweli alikuwa analia.

‘Habari zenu….’nikasalimia na wote walibakia kimia, nahisi walishachoka na hizo salamu.

‘Samahanii jamani nilikuwa nauliza tu, lakini naona kama hampo sawa,  kuna msiba, au kuna tatizo gani limetokea..?’ nikauliza.

‘Msiba…?!’ akauliza huyo mama kwa mshangao, sasa akiniangalia mimi machoni, kuashiria anashangaa na hiyo kauli yangu. Kijana wake yule mdogo akawa sasa anakodolea macho, yaliyojaa hasira, kwa muda ule nilijiuliza, ina maana kijana yule keshanikasirikia, keshaniona mimi ni mbaya wake, japokuwa hakuwa na ufahamu kuwa mimi sio dalali.

‘Kwa jinsi mlivyo,…mama unalia na hali yenu yaonyesha kama mpo kwenye majonzi  makubwa…’nikasema, na yule mama akageuza kichwa kuangalia kwingine halafu akasema;

‘Hapa hakuna msiba kama ni msiba labda uulete wewe…, sisi tupo salama tu, hatujambo kwa majaliwa ya mola wetu…, ila…. Hata hivyo, samahani tunaomba usizidi kutuongezea machungu zaidi….’akasema.

‘Hapana mimi sina lengo hilo,…ila, kama binadamu kwa hali niliyowaona nayo, inaniwia vigumu kuondoka bila kuwajulia hali, nia yangu ni njema tu…’nikasema.

‘Sawa umeshatujulia hali, tumekuambia hatujambo, si inatosha jamani, au kuna jingine … unataka tukusaidie nini…?’ akauliza huyo mama naona alikuwa hayupo sawa.

‘Nataka kufahamu kama nyie ndio….sina uhakika, nyie mlikuwa wapangaji wa humu ndani au…?’ nikauliza.

‘Wapangaji wa hii nyumba mhh!!....’akasema  kwa mshangao hayo maneno huku akiniangalia

‘Nauliza tu…unajua tena, kwa hali niliyowakuta nayo lazima niwe na ubinadamu wa kutaka kufahamu zaidi…na pia…’nikasema na kabla sijamaliza akasema;

‘Hapana sisi sio wapangaji,….’akasema hivyo, sasa akitaka kama kuondoka.

‘Oh, sasa mnfanya nini humu..au ..samahanini lakini…’nikasema

‘Na mimi nikuulize wewe ni nani wakutuuliza maswali hayo yote…mbona unatutia mashaka, maswali kama hayo niliwahi kuulizwa na watu wa usalama au ndio kuna jipya limtokea tena..?’ akauliza

‘Samahanii kwa hilo,…kiukweli hali mliyo nayo imenigusa, nilikuwa nimekuja…’kabla sijamaliza akasema

‘Basi yatosha, ulikuja kukagua nyumba, si ndio hivyo, basi umeshafanya hivyo, au kuna kitu kingine wataka kuniuliza kuhusu hii nyumba, nikuambie…nyumba ni hii ndiyo unatakiwa kupigwa mnada, ikague tu…’akasema

‘Mhh…samahanini lakini, …sina nia mbaya…’nikasema

‘Sawa nimekuelewa,…’akasema

‘Nauliza tu, nilitaka kufahamu zaidi labda nyie mlikuwa mkiishi humu ndani kama wapangaji au..…?’ nikauliza

‘Kama wapangaji, sawa uonavyo wewe, si ndio hivyo tena, kwa vile ni wapangaji hatuna haki tena,….na..lakini kwanini unataka nini lakini, wewe ni nani…?’ akasema hivyo na mimi ikawa zamu yangu kushikwa na mshangao.

‘Nia ni kujua zaidi tu, hasa nyie ambao, nimewaona kwenye hii hali, hilo la nyumba, aah, tuwaachie wenyewe, nataka kujua zaidi kutoka kwenye masahibu gani yaliyowakuta…?’ nikauliza

‘Tulikuwa aah…bwana, mimi naona uondoke tu, kwa leo siwezi kuongea lolote….’akasema hivyo.

‘Mhh, unajua shemeji, mimi ni msamaria mwema tu, …natunga sana hadithi, visa, na…najaribu kuwa karibu na jamii, na nikiona watu wapo hivi, inanigusa sana, natamani kuyaandika yale yaliyowasibu…’nikasema

‘Tunashukuru…’akasema hivyo tu

‘Kwahiyo, nyie ni nani hasa, na kuhusu kuishi  hapa kwenye hii nyumba, sasa eeh,. unajua nakumbuka jambo moja, mwenye nyumba hii alikuwa akiwajali sana watu, na zaidi ..nakumbuka siku moja nilikutana naye, akasema yeye anaijali sana familia yake, kwa kila hali, na wale waliopo kwenye mikono yake, hata wapangaji wake, nakumbuka sana hiyo kauli, sasa nashangaa kidogo..'nikasema.

'Unashangaa nini sasa...?' akauliza huyo mama akianiangalia kwa macho ya kujiiba

'Nyie hali mliyo nayo,...'nikasema hivyo nikiwazia jinsi gani ya kuweza kupata maelezo kutoka kwa huyu mama, maana inavyoonekana hataki kuongea zaidi.

‘Wewe umeshasikia kuwa nyumba hii  inapigwa mnada…wenye nyumba hii hawana chao tena,...wawe wapangaji au nani,...inabidi watafute sehemu nyingine ya kuishi,  nyumba hii sasa sio mali yao…tulishapewa notice, nyumba hii sasa ni mali ya hao watakaoinunua, …kama ni wewe haya kagua uondoke zako, mtuachie na majonzi yetu,….’akasema huyo mama.

‘Mimi sijui kabisa kinachoendelea,…na kiukweli, nilivutika tu niliposikia tangazo…kutoka kwa mpiga mbiu kuwa nyumba hii inanadiwa,… inauzwa, na inatokana na deni, alilokopa, hajalipa…’nikasema.

‘Kama umesikia hivyo basi inatosha wewe unataka nini tena zaidi….’akasema huyo mama na mtoto wake huyo mkubwa,akamkatisha na kusema kwa sauti kama ya ukali.

‘Mwenye nyumba hii hajakopa pesa yoyote, waongo hao…mwenye nyumba hii alikuwa ni baba yangu..’akasema na kabla hajaendelea mama akamziba mdomo.

'Baba yako...alikuwa una maana gani!?' nikauliza kwa mshangao, hakusema neno , kwa vile mama yake alikuwa kamziba mdomo.

‘Mungu wangu, ina maana,…oh…kumbe,…ina maana nyie,ni…..oh, nimekumbuka hata sura za watoto zinafanana,..na baba yao, oh…sasa jamani mbona, ungeliacha tu mtoto aelezee, msiwe na mashaka na mimi…’nikasema.

‘Huyu mtoto anaongea tu,….’akasema sasa akizuia machozi.

‘Hapana sasa naanza kuelewa, …kwani baba yenu yupo wapi kwa hivi sasa bado yupo Ulaya, alisafiri tena eeh….?’ Nikawauliza wale watoto, na wote wakainamisha vichwa chini….
Ikawa kama nimetonesha kidonda kilichoanza kupona.

Mama akaanza kulia, na baadae watoto….

*************

Nikabakia na mshangao….baadae huyo mama akasema;

‘Baba yao ni marehemu….’

‘Unasema….Mungu wangu, …ina maana…oh, kwake tumetoka na kwake ndio marejeo yetu, poleni sana, nisameheni tu sikujua jamani…’nikasema

‘Ndio hivyo, kama ulikuwa hujui sasa umeshafahamu…’akasema huyo mama.

‘Oh poleni sana, mimi sikujua siku nyingi sijapita maeneo ya huku, nashangaa hata huo msiba sikuwahi kuusikia…’niliishiwa cha kuongea.

Kiukweli sikuwahi kusikia kuwa mwenye hiyo nyumba sasa ni marehemu,….sikumbuki kabisa kusikia hata mtu mmoja akisema hivyo…watu walikuwa na hamasa tu ya kuiona hiyo nyumba…kwa nia tofauti wengine wakijifanya madalali, ili waende kwa matajiri waje kupata cha juu,  wengine wakiitamani tu.. wengine ndio hao akina pangu pakavu, tilia mchuzi kupata taarifa za umbeya.

‘Ina maana huyu…hata siamini, Yule jamaa sasa ni marehemu…’nikabakia nimeduwaa.

‘Mbona ni muda mrefu sana mume wangu alishatangulia mbele ya haki, na wengi walishasahau, ila mwenye kovu usizani kapoa, mimi nimekuwa nikiombeleza miaka yote hiyo…na haya yanayotokea sasa yananizidishia machungu, na kuzidi kunikumbusha marehemu mume wangu,….’ Hapo akaanza kulia

Halafu akasema

‘Nina imani, …kama angelikuwa hai haya yote yasingelitokea…’akatulia na akavuta pumzi ya kutaka kulia zaidi

‘Pole…poleni  sana na mnisamehe tu, sikuwa na lengo la kuwakumbuishia msiba huo…’nikasema

‘Najua ndio basi tena,sitamuona tena… sasa sina jinsi inabidi nikubaliane na hali halisi.., inabidi nikateseke kama wanavyotaka wao, wanafikia kusema si ulikuwa unaringa, sasa kipo wapi, si…ulikuwa hivi....jamani, lini nilifanya hivyo, ‘akatulia akijizuia kulia.

‘Hiyo ni ya kawaida kutoka kwenye vinywa vya wanadamu , wengi hawawezi kuzuia hisa na ndimi zao, huo ni mtihani kwakweli…’nikasema

‘Lakini nina uhakika  kama angelikuwepo hai haya yote yasingelitokea…nina imani hiyo kabisa, hii sio bure tu…kuna mkono wa mtu…’akasema huyo mama kwa uchungu.

‘Mkono wa mtu, …una maana uchawi au…?’ nikauliza

‘Hapana mimi nipo mbali kabisa na imani hizo za kishirikina, uchawi upo, lakini mimi sina maana hiyo kabisa,…ila wewe elewa  hivyo tu…’akasema

Akilini nilikumbuka yale maneno  mazito ya mtu wa imani akisema; ‘mpende umpendaye ipo siku mtaachana naye, kipende ukipendacho ipo siku utakiacha, ipende uipendavo hii dunia ipo siku utaicha,…itakayobakia kwako ni amali yako njema tu,…

Na wakati nawazia hayo Yule mama alikuwa bado analia, nikamsogelea na kuanza kumliwaza kwa kusema;

‘Tukubali tu shemeji, japokuwa ni hali ngumu, utafanya nini tena mola akiamua,..tunabakia kusema 
Yote ni mapenzi ya mungu, au sio…’nikasema  hivyo na huyo mama,akahema kwa nguvu halafu akanitupia jicho, hakusema neno…

‘Ni kweli, YOTE NI MAPENZI YA MUNGU…’akasema akiwaangalia wanawe.

‘Poleni sana na mola aiweke roho ya marehemu huyo mahali pema peponi,  roho ya mpendwa wetu huyo, alikuwa ni mtu wa watu kwa kweli….’nikasema hivyo , na mama huyo japo alijitahidi kutulia lakini hali ya kutaka kuendelea kulia ilikuwepo, hata watoto walikuwa wanalia kimia kimia. Iliniuma sana, kama ningelijua nisingelianzisha hilo….

‘Shemeji cha muhimu sasa sio kulia zaidi, kwa kuonyesha mapenzi yako kwake, wewe uzidi  kumuombea  marehemu maghafira na najua , nimjuavyo mimi, mume wako atakuwa mahali pema peponi, yeye alikuwa mtu mwema sana, alikuwa mtu wa watu,……’nikasema

************

Ni kweli huyo jamaa alikuwa mtu mkarimu sana, pamoja na kutokea hukoo alipokuwa ulaya hakuonyesha ile hali ya kuringa, hakuweza kukupita njiani na gari lake kama anakufahamu ni lazima atasimama akuchukue, na hata kukufikisha nyumbani kwako, lakini sasa ndio hivyo hatunaye tena…Yote mapenzi ya mungu. Kweli wema hawana maisha.

‘Ni kweli yote ni mapenzi ya mungu, lakini haya yanayotokea sasa, yanatuzidishia machungu, maana kila alichokiacha sasa kinachukuliwa, hebu fikiria hata haya makazi yetu ya hapa duniani, sehemu ya kujisitiri aibu zetu nayo ndio hiyo wanataka kuichukua,...'akatulia kidogo

'Hebu jiulize...hawajiulizi hilo...hawana mawazo hayo tena,..je sisi tutakwenda kuishi wapi, au wanataka na sisi tuwe marehemu, lakini siku kama hazijafika, hatutaweza kufa au sio, sasa kwanini wanatufanyia hivyo….’akasema huyu mama akiangalia juu, kuiangalia hiyo nyumba!

‘Oh…’nikaguna hivyo na huyo mama akaendelea kuongea kwa sauti yenye huzuni

‘Hawa watu sijui mwishowe wanataka nini kwetu, walianza kutunyang’anya kimoja baada ya kingine, mara mashamba , mume wangu alikuwa na mashamba yake aliyanunua akiwa hai, hayo yote yamechukuliwa…’akasema

‘Yamechukuliwa na akina nani…?’ nikauliza

‘Hahaha, unauliza ni akina nani....'akasema huyo mama akiniangalia moja kwa moja

'Ndio....'nikasema

'Ni ndugu zake, ambao walikuwa karibu naye,..hao, walikuja kugombea mali za kaka yao, huku wakigawana bila aibu,....'akasema

'Kwa utaratibu gani...?' nikauliza lakini hakunijibu hilo swali yeye, akaendelea kuongea

'Waligawana na…na yote hayo yalifanyika kipindi mimi sijitambu, nimekuja kugundua hayo, wakati huo mali zoe zimeshachukuliwa, ..mashamba....nitafanya nini tena, maana na wao wameuza kwa watu wengine...'akatulia

'Mimi...nimekuja kujitambua muda umeshapita sana...haya.., mimi nitafanya nini, nikasema hewala chukueni kama ni halali yenu, sasa hata hii nyumba jamani…’akatulia kidogo

‘Yamegawanywa kivipi, maana kuna utaratibu za mirathi au sio…?’ nikauliza

‘Waligawana bwana....hawakujali hayo...watoto si wadogo...kila mmoja akija na visingizio vyake, mara hili shamba lilikuwa la familia, na mmoja akifa shamba linatakiwa kurudi kwa familia, zipo hat za makubaliano hayo,..mara hili eneo walinunua kwa umoja wa familia eti walichangiana ndugu wakanunua kwa pamoja  kwahiyo sasa linakuwa mikononi mwa familia..mara....mimi akili bado ilikuwa hajakaa sawa..

'Sasa ulifanyaje ulipotulia

‘Mimi Sikutaka hata kugombana nao, maana hadi sasa kama unavyoniona, sijakaa sawa,..bado akili haijaka sawa jamani,mimi kwa muda mrefu  nilikuwa kama mfu, sijitambui…na hata hivyo,  ningelisema nini…’akatulia

‘Nauliza hivi, si kuna hati za mashamba si zilikuwepo, wewe si unajua wapi zilipo au…’nikasema

‘Hati….zilikuwepo,…lakini si walizichukua, muda huo mimi sijitambui...aah..hayo tuyaache tu, ila  nikajiuliza ina maana sisi sasa sio miongoni mwao tena, sio familia yao tena, jamani hata mimi labda,…mimi si mjane, sina haki, lakini hawa mayatima hawana haki na mali hizo…, ’akatulia 
akiwageukia watoto wake mmoja mmoja!

‘Lakini hebu ngoja nikuulize kipindi hicho mume wako ananunua hayo mashamba, wewe hukuwepo, hukushirikishwa,…?’ nikamuuliza

‘Nilikuwepo sana, lakini si unajua tena sisi wanawake, na na….. usijifanye hujui kuhusu wanawake, inapofikia kwenye mashamba na mali, siwezi kumlaumu mume wangu kwa hilo…kiukweli yeye aliniambia ananunua hiki na kile na wakati mwingine tunakwenda naye, lakini yeye kwa upendo aliokuwa nao kwa ndugu zake, kila kitu aliwaweka wao mbele…’akatulia

‘Ina maana kwa namna fulani, ..sema tu ukweli, labda mume wako, kipindi hicho hakukujali au hakujali kukushirikisha kwenye mambo kama hayo, alikudharau kwa vile wewe ni mwanamke…?’ nikauliza.

‘Sio kuwa hakunijali, hapana…aliona kwa vile ndugu zake wapo, na yeye ni kaka yao mkubwa, basi wanakwenda pamoja, mimi napewa tarifa tu, …baadae nakuja kuonyesha eneo, sikuwa na lawama kwa hilo, nilijua mume wangu anaanya hayo kwa nia njema…’akatulia

‘Ok….nimekuelewa, lakini…’kabla sijauliza akaendelea kuongea.

 ‘Unajua mume wangu aliwaamini sana ndugu zake, aliwafanya wao ni sehemu ya familia yake na alitaka maendeleo  ya wote kama familia moja, yeye hakupenda ubinafsi, na ndugu zake walikuwa muhimu sana…kila akinunua sehemu anawagawia na ndugu zake, lazima akinunua eneo anawanunulia na wao…kwa masilahi ya familia, na maendeleo yao pia..’ akasema

‘Ikiwemo na wewe pia au sio..?’ nikauliza

‘Mimi si ndio yeye, alichofanya yeye kipindi hicho ni kama nimekifanya mimi, sikuwa na wasiwasi wowote na hilo…’akasema

‘Kwahiyo wewe una ushahidi kuwa mume wako ndiye alinunua hayo mashamba, na kama alifanya hivyo  si kuna hati na kitu kama hicho, mume wako hakukuonyesha, au ilikuwaje katika manunuzi, mume wako hakuwahi kuandikishana na hao wauzaji…..?’ nikamuuliza

‘Kipindi hicho sikuwa natilia maanani, hayo sijui hati, kuandikishana, nilijua wao wote ni kitu kimoja,…hao ndugu zake niliwaona ni kama mume wangu tu.. sikujua haya yatakuja kutokea, sikujua kuwa hawa ndugu watakuja kunibadilikia hivi,….mimi sikuwa na wazo hilo kuwa nichukue hati, au….niliwaona hawo shemeji zangu kama alivyo mume wangu kabisa kabisa…’akasema kwa uchungu.

‘Sasa kwanini walikuja kubadilika….?’ Nikamuuliza na yeye akaona kama kukerwa na hilo swali langu.

‘Hayo mimi sijui…na kiukweli tabia hiyo hawakuwa nayo kabisa kipindi kaka yao yupo hai…’akasema.

'Sasa....'nikataka kuuliza

‘Mhh, kubadilika ile ya ku...…….walianza kubadilika pale walipooa…nakumbuka hata alipokuwepo mume wangu, ndugu zake hawa waliishi kwa ushirikiano na kaka yao, lakini baadaye walianza mabadiliko fulani,….hasa pale walipooa, hata hivyo kwa muda huo walimuogopa kaka yao….walikuwa wakimuheshimu sana kaka yao...’akasema

‘Kwahiyo unataka kusema labda tabia hiyo ya ubinafsi ilichangiwa na wake zao..?' nikamuuliza kwa umbeya ili kutaka kujua hisia zake

‘Mimi siwezi kuwasingizia wake zao maana msimamo ni mtu mwenyewe, kama mume unatakiwa uwe na msimamo wako ujue nini majukumu ya familia, usiyumbushwe, lakini  kwa hisia hizo zipo, ila kwngu mimi siwezi kusema zaidi ya hayo mungu ndiye anajua zaidi ya hayo....’akatulia.

‘Sasa hao wake wenza kwa shemeji zako, hawakuwa na ushirikiano mwema kama walivyokuwa shemeji zako, maana mlitakiwa muwe pamoja au sio, kwani haya yanaweza kuwakuta hata wao au sio..?’ nikamuuliza

‘Wewe hujui sisi wanawake, tuyaache hayo tu....'akasema

'Hapana shemeji, ...nataka kujua zaidi,..huwezi jua...'nikasema

'Sikiliza..., kama umekuja kutizama nyumba ndio hiyo, kama una hitaji kuja kununua haya bahati ni yako, au kama u dalali haya..….’akasema.

'Hapana mimi si mnunuzi...wala sio dalali kama nilivyokuambia awali...'nikasema

*************
Alikaa kimia kidogo halafu akasema;

‘Kilichonishangaza hata kushindwa kuamini ni pale tu mume wangu alipokwisha kulazwa kaburini, hayo mimi nimekuja kuhadithiwa baadae maana kipindi kirefu mimi nilikuwa sijitambui….’ hapo akanifanya nitege masikio

‘Ilikuwaje…?’ nikauliza

‘Hao walioitwa ndugu, ambao niliishi nao  kwa upendo akiwemo kaka yao, walibadilika, uroho wa mali ya kaka yao uliwatawala, ....hawakukumbuka tena ule upendo wa  kaka yao,

Huwezi amini hadi sasa ule upendo wa shemeji zangu kwangu haupo tena…yaani hata siwezi kuamini, hata wengine wananisingizia mabaya, hata siamini, niwezeje kumuaa mume wangu…yaani inaniuma sana...’akatulia pale mtoto wake mkubwa alipomshika akimuashiria asiendelee kuongea zaidi.

‘Mama akiongea hayo anazidi kulia…’yule mtoto mkubwa akasema akiniangalia mimi, alikuwa na kama umri wa miaka tisa hivi kwa kumkadiria.

Pale nilipo niliwaza, nifanyeje, maana nataka niujue ukweli, lakini kila ninavyozidi kumuuliza ndio kama namchochea kulia zaidi, na mtoto huyo keshanipa kama angalizo, nisiendelee kumuuliza mama yake maana namfanya aendelee kulia. Hata hivyo sikukata tamaa, nilijua muda ndio huo, baada ya hapo huenda nisipate nafasi hiyo, nyumba itakuwa imeshauzwa.

‘Je nifanyeje….’nikajikuta nimesema hivyo kwa sauti. Yule mama akaniangalia, halafu akasema;

‘Huna cha kufanya shemeji…hili hakuna anayeliweza,...zaidi ya yule asiyeshindwa, hakuna mwanadamu tena wa kuliweza hili...iliyobakia tumuachie mola...nimeshanyosha mikono yangu juu, nikisema haya yote ni kwa mapenzi yake, kama ni hali yangu, ....nitaipata, lakini kama mungu kapitisha hivyo...basi ...ni kwa mapenzi yake...’akasema hivyo..

‘Lakini nataka kufahamu zaidi…’nikasema

'Inataka kufahamu nini, ili iweje,...ina maana wenzako, wasomi...hapana, hili liache tu.....liache tu,....

NB: Nataka kufahamu zaidi, najua na wewe unataka kufahamu zaidi, tusubirie sehemu ijayo


WAZO LA LEO: Dunia hii ni ya kupita tu..tuipende tuipendavyo, ipo siku tutaicha,…mali zetu na majumba yetu, tuchume tuchumavyo, hata kwa ufisadi, lakini ipo siku mali hiyo tutaicha, tuwapende wapenzi wetu tuwapendavyo, wake zetu, waume zetu, watoto wetu, wazazi wetu, lakini ipo siku tutaachana nao. Tukumbuke jambo muhimu, ni nini cha kuondoka nacho, chenye faida kwetu,…ambacho hutaweza kukiacha, kitakuwa msaada wako, huko tuendapo… kwenye safari hiyo isiyo na marejeo,…ni AMALI NJEMA TU.
Ni mimi: emu-three

No comments :