Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, May 22, 2018

YOTE MAPENZI YA MUNGU-1


Kisa kilianzaje….

Mnada ,mnada …. Kwa niaba ya bank,… kampuni yenu pendwa ya Auction Mart, tunapenda kuwatangazia mnada wa hadhara, tarehe …., wa kuuza nyumba kubwa ya kisasa, ili kulipia deni la benki… fika ujionee mwenyewe…., fika ununue nyumba ya kisasa yenye kila kitu, ikiwa na uwanja mpana, na sehemu kubwa ya kuegesha magari…’ aliendelea kutoa wasifa wa hiyo nyumba hiyo, huyu mpiga debe.

Watu wakawa wametega masikio,.. huku kila mmoja wetu akijiuliza hiyo nyumba ni nyumba gani yenye hizo sifa nyingi hivyo, na kwanini mwenye nyumba akafikia kiasi hicho cha kuachia nyumba yake ipigwe mnada, au yeye mwenyewe kapenda ifanyiwe hivyo tu, kwa malengo yake.

Nikasikia jamaa mmoja akisema;

‘Hiyo itakuwa ni ile nyumba ya Yule jamaa aliyekuwa ulaya, …’akasema.

‘Jamaa wa Ulaya…!!’ nilisema hivyo kwa mshangao…..

‘Kwanini,..mbona yule jamaa alikuwa anajiweza sana…’mmoja akasema na kukawa na maongezi , unajua tena wabongo kujadili watu ni hulka yetu,…hata hivyo kelele za pale zilinifanya nisifuatishe hayo maongezi yao, kwani nilishaelewa ni nyumba gani hiyo:

‘Nyumba ya mtu wa ulaya,…’

Maeneo ya hapo kwetu, ukisema nyumba ya yule mtu aliyekuwa ulaya anatambulikana sana…na hata mimi mwenyewe niliwahi  kupita maeneo hayo  lakini ni siku za nyuma…kipindi hicho ndio ilikuwa inamaliziwa maliziwa kwenye ujenzi wake,…na kila mtu aliyeiona hiyo nyumba, alibakia kuisifia..na ukiuliza hii nyumba ni ya nani watu waliishia kusema;

‘Ni ya mtu mmoja  kutoka ulaya….’ Ikawa imetambulikana hivyo…’nyumba ya mtu kutoka ulaya..’ baadae nyumba ya mtu wa ulaya…!

Ni siku nyingi, ni miaka naweza kusema hivyo… na huyo jamaa mwenyewe niliwahi kuonana naye kipindi hicho hicho cha nyuma, na kwa vile alikuwa mkarimu, nilibahatika kupata lifti ya gari lake, …ni muda kwakweli,  baada ya hapo sikuweza kuonana naye tena.

Sasa kwanini nyumba yake inataka kuuzwa…ilinipa maswali mengi kichwani,.., ina maana labda alijenga nyumba hiyo kwa mkopo ,au hata sijui ilikuwaje, na je hana familia inayoishi  hapo, mbona nasikia kama kulikuwa na watu wanaishi kwenye hiyo nyumba,..labda ni wapangaji….

Na kama inauzwa huenda, hao wenye nyumba labda hawapo tena hapa nchini, na kama wapo hapa nchini basi watakuwa wanaishi kwenye nyumba nyingine.

‘Ngoja nikaitembelee hiyo nyumba, nijionee mwenyewe, na huenda na mimi nikawa dalali wa kumtafuta mnunuzi,…’nikasema hivyo nikitaka na mimi niwe mdadisi kidogo kupoteza muda.

Ni kweli udadisi huo ulinisukuma hadi nikafika kwenye eneo la hiyo nyumba, na kiukweli, kila jambo mungu ndiye mpangaji, hisia nanguvu za kunifanya nifike pale, zilikuwa sio bure,..niliyokutana nayo huko, yalifanya nikiandike hiki kisa, ni ya huzuni, utapeli, mauaji, na kwa kifupi, ni dhuluma tupu.

*************

Haya ilikuwaje…

Siku hiyo nikawa natembea kwa haraka huku nikiongea peke yangu.

‘Nahisi jamaa alienga hiyo nyumba kwa mkopo, na kwa vile ana pilika pilika nyingi huko Ulaya huenda kapitiwa au ni njia moja wapo ya kuuza hiyo nyumba, apate malipo alipe mkopo na kubakiwa na chochote kitu,..!’

 Mbwembwe za mpiga hiyo mbiu, ziliwavuta wengi kwakweli, sikuwa peke yangu niliyevutika kwenda huko, watu wengi walielekea huko kila mtu akiwa na lake kichwani, na sikuweza kuongea na yeyote, maana kila mmoja ana lake….

 Sio mbali sana, ni sehemu ya kutembea kwa miguu tu…hutaamini kipindi nilipofika eneo hilo awali, kulikuwa na uwazi mkubwa, kabla ya kufikia hiyo nyumba, sasa hivi karibu yote imejaa nyumba,hata njia za kupita zimebadlika, ikabidi kuzunguka kidogo,…hatimaye nikaiona hiyo nyumba kwa mbele yangu, huwezi kuipotea, ipo na mjengo wa kitofauti. 

Nyumba yenyewe ilijengwa kama juu ya mlima hivi, sehemu ile imeinuka kidogo…kwahiyo ili ufike kwenye eneo lenyewe,  ilipojengwa hiyo  nyumba, inabidi uwe kama  unapanda kimlima kidogo.

Sikuwa na wasiwasi, kwasababu hiyo nyumba  ilikuwa inapigwa mnada nilijua sitapata kizuizi cha kuweza kuingia ndani na kuikagua, japokuwa imezungushiwa ukuta mkubwa,…

Nilipofika, niliwakuta watu wakiikagua hiyo nyumba , lakini wengi kwa muda huo walikuwa nje ya geti, nikahisi huenda watu hawaruhusiwi kuingia ndani ya geti, lakini sio hivyo, wao walishaingia na sasa walikuwa wakihakiki kwa macho tu, wengine wakiipiga picha..siku hizi tena, kila kitu kupigwa picha, selfie ..ndio hivyo!.
‘Vipi jamani naruhusiwa kuingia ndani…?’ nikauliza
‘Ruhusa…unaweza kuingia geti lipo wazi…’nikaambiwa!
 Kwenye ukuta wa hilo geti nikaona tangazo…



‘Kwa niaba ya…….’

Sikutaka hata kuendelea kulisoma tangazo lenyewe nikaingia ndani…
Mashallah, …kiukweli ilikuwa ni nyumba kubwa, na mjengo wake kwa mbele tu, ulikuwa ni  wa kipekee, wanasema ramani hiyo jamaa alikuja nayo mwenyewe kutoka ulaya,…na mafundi wake walikuwa wa kimataifa, na ilijengwa kwa gharama kubwa sana …na kile aliyeulizwa kuhusu muundo wa nyumba hiyo aliishia kusema huo ni muundo, wa kutoka ulaya.

‘Huu ni muundo wa huko huko Ulaya, unaona toka chini ilivyo,…imeanza na mawe magumu, hakuna matofali zaidi ya waya za nondo....inakuwa kama imewekezwa juu ya mawe ukiangalia kwa nje…basi ndani baridiii..utafikiri upo ulaya…huhitaji kiyoyozi..jamaa aliona mbali huyo… lakini ndio hivyo tena…!’akasema jamaa mmoja alipoona naangaza macho kuangalia yale mawe yalivyopangwa, ni mawe makubwa,magumu…

‘Ndio hivyo tena…’na mimi nikasema hivyo nikiwa kama nataka kuuliza, lakini huyo jamaa simu yake ikawa inaiita, kwahiyo akageuka upande mwingine na kupokea  simu, sikuweza kuongea naye, na kwa vilenimefika mwenyewe nikaona nijionee mwenyewe.

Watu walikuwa wakiingia na kutoka, na kila mmoja aliyetoka huko ndani aliongea la kwake, lakini mimi kichwani nilitaka kufahamu hatima ya familia hiyo, wapo wapi,.pamoja na mengine, ukiwa mwandishi unakuwa na jicho la tatu.

Nikawa natembea hatua za taratibu huku macho yakifanya kazi yake ya kupiga picha eneo, na nyumba yenyewe,…

‘Mimi ndio maana naogopa kukopa, sasa mtu kakopa pesa nyingi kiasi hicho cha kuwezesha kujenga nyumba ya gharama kiasi hiki, leo hii inapigwa mnada, na je wao wenyewe watakuwa wanaishi wapi, maana hali kama hiyo inaweza ikamfanya mwenye nyumba akadondoka kwa shinikizo la damu!’ nikasikia mmoja akisema huku akikimbilia nje.

Na mimi kwa muda huo nikawa kama tajiri anayetaka kuinunua hiyo nyumba, natembea taratibu nikigeuka kushoto na kulia,…huku nikivutiwa na bustani na mua yaliyopandwa pembezoni mwa njia…

Sasa nikifika kwenye mlango mkuu wa nyumba yenyewe…marumaru ziliwekwa kwenye njia,  zenye nakshi nzuri, na moyoni nikatamani , kama ningelikuwa na pesa, mhh, ningeli inunua hii nyumba,….hahaha…itakuwa mwendo wa mamilioni kama sio bilioni, ikawa ni ndoto za Alinacha, kuwaza kwa hamasa ya ‘Ngeli…’ ningekuwa, ningeli…ndio hivyo tena.

Kiukweli ni nyumna nzuri, na mazingira yake yanavutia, utafikiri upo wapi vile, u-la-ya…..!
Sasa nikawa nipo kwenye mlango wa geti dogo la kuingilia kwenye nyumba yenyewe, hapo …nikageuka kulia , kwa mbele zaidi nikaona eneo kubwa limepandwa miti na migomba, na ..ndege walipita huku na kule, wakifurahia mandhari

Sasa ..nikageuka kushoto, mara nikasikia sauti!

Mwanzoni nilijua ni watu waliokuja kuitizama hiyo nyumba lakini haikuwa hivyo, ni hali kama upo kwenye magofu hivi, unahisi kama kuna watu lakini huwaoni, ..ndivyo nilikuwa nahisi kwa muda huo,..hata hivyo, kulikuwa na sauti nyingine, sauti halisia...ni kama mtu analia au watu wanalia,....

‘Hapa kuna tatizo, nahisi…’nikasema na kweli nikahisi nywele zikinisisimuka,…nikasita kutembea, nikageuka nyuma kuhakikisha kama sipo peke yangu, maana nahisi kama hakuna amani tena..nikaona watu, nikajipa moyo kuwa hakuna matata…

Kukawa kumetanda ukimia kidogo…hapo  nikainua hatua moja , mbili  , tatu, nikafungua lile geti dogo la nyumba,…lilikuwa wazi unasukuma tu kidogo,…hiloo, likafunguka,  na hapo tena nikakutana na ngazi za maru maru za kuelekea juu, ni kama tano hivi, ili uufikie mlango wa nyumba yenyewe,..moyo ukawa na wasiwasi, sijui kwanin, nahisi ni kutokana na ile sauti kama ya mtu analia…

Sijui kwanini, nilianza kuhisi mashaka,…wasiwasi na hata woga,…

Nikaona nisipoteze muda,… nikaanza kupanda zile ngazi ya kwanza, ya pili ya tatu,nne, tano… nikawa sasa nauangalia mlango, nikataka kugeuka kulia na kushoto, lakini sikuweza maana  macho yangu yalinasa kitu,…pale mlangoni kuna tangazo jingine, sio kubwa kama lile la kule nje...

Nikalisogelea sasa…lakini sikuweza kulisoma hilo tangazo, macho yangu yakawa yamenasa kitu kingine, na akilini niliendelea kuhisi kama kuna hali ya watu wasioonekana hivi....mwili unasisimukwa, na macho yangu kwa muda ule,yakanasa kitu kingine kitu ambacho,..kilichonivutia zaidi...

Na kwa..., kupitia kwenye mlango, uliokuwa nusu wazi, nikaona jambo...akili yangu sasa ikawa kama imefunguka na zile sauti za kama upo kwenye gofu, lililohamwa, halafu unahisi kuna majimizi hivi, zilikaniondoka,..ila bado moyo wangu ulikuwa na wasiwasi, ….

Nikasimama …kwanza sikuamini, maana nilijua humo kwenye hiyo nyumba hakuna mtu mwingine tena,…mpaka inafikia kunadaiwa ina maana wenyewe watakuwa hawapo inawezekana wapo kwenye nyumba nyingine au wapo ulaya, au labda hapo kuna wapangaji bado au walinzi, ….mhh lakini niliowaona walinipa mshawasha wa moyo, nikasahau hata kulisoma lile tangazo.

Ni akina nani hawa…? nikajiuliza.

Sasa nimesimama usawa wa kitu kama kibaraza…nikawa najongea ili niweze kuona kupitia kwenye ule upenyo wa mlango uliopo wazi…

Kule ndani niliwaona watu,…walikuwa watatu, ni mama mmoja akiwa kakaa mkao wahuruma, ule mkao wa mtu kukaa chini, miguu imejikunja na kichwa kinakuja kulala kwenye magoti…na pembeni yake kulikuwa na watoto wawili,….ule mkao sio wa kawaida…na hali zao sio za kawaida, zinatia huruma.

Mama Yule alikuwa kama analia, ….! Nina uhakika alikuwa analia….

Kwanini analia, nikawa najiuliza sasa….na cha ajabu watoto wake walionekana kama wanambembeleza, inawezekana ni  watoto wake…sikuweza kuiona sura ya huyo mama kwa haraka , kwani kichwa kiliinamishwa  na kuficha sura,…oh masikini, yaonekana wamakutwa na janga wakiwa hawajajiandaa, moyo wa huruma ukanijia,..au labda  wamefiwa, hata kama wamefiwa kwanini wapo kwenye hii nyumba, na mbona wapo peke yao…!

Nikawa nimepigwa na butwaa,…..

 Mtoto mkubwa alikuwa upande wa kushoto kwake, akiwa naye kakaa chini na mkono wake mmoja wa huyo mtoto upo kichwani kwa mama yake, na mtoto mwingine yeye alionekana sio mkubwa sana, alikuwa naye kakaa akiwa kajiegemeza ubavuni kwa  huyo mama, na alikuwa kainama kuficha uso, huenda na yeye alikuwa analia.

Hali hii ikanifanya hisia zangu zote zipotee, hisia z nyumba nzuri, hisia za…sasa nahisi napambana na hisia za huzuni, moyo wangu ukaelekea kwenye Nyanja yangu ya jamii

‘Huenda humo pia kuna msiba,…’ nikajisema na mwili wangu ukazidi kusisimukwa…

 Hata hivyo akili iliniambia hapa kuna zaidi ya hilo la nyumba, kuna jambo kubwa nyumba ya pazia, na nyumba imekuwa ni sababu tu iliyoniwezesha kufika hapo, ….nikavuta pumzi na kumuomba mola wangu, maana hali kwangu mimi kinfasi nilishahisi mashaka,…ni namna nilivyojengeka kuhisi jambo, na nikihis jambo ujue kuna jambo.

Ndio nikaanza kusikia yale mazungumzo...

‘Mama sasa sisi tutakwenda kuishi wapi…?’ Nilisikia sauti ya mtoto ikiwa kama inalia na kulalamika.
‘Hata sijui…’sauti ya mama akajibu kwa mkato kama kukerwa vile.
‘Kwanini wanataka kuuza nyumba…sisi tutakwenda kuishi wapi, …?’ ilikuwa ni sauti ya  mtoto mdogo wa pili.

*********

‘Hodi  tena sijui ni wenyeji au ni ….’ Nikasema sasa nikisukuma mlango, ili niweze kuingia ndani… nikaona sasa nakabiliwa na mtoto mdogo machoni kajawa na hasira, nikashikwa na butwaa, na aliyeweza kunisaidia ni huyo mama, akamshika mtoto wake, ….

NB: Mambo yalianzia hapo....tuendee….!


WAZO LA LEO: Sio vyema kujengeana dhana mbaya, tukawa tunajenga hisia ambazo hatuna uhakika nazo..tukasambaza mapicha, maelezo kwa nia mbaya tu…. Jiulize je kama sio kweli, na hapo ulishasema na kunadi kuwa huyo mtu yupo hivi na vile..na sasa hivi kwasababu ya mitandao, habari huenea kwa haraka sana. Hebu jiulize ungelikuwa ni wewe umefanyiwa hivyo ungejisikiaje. Dhana mbaya kiukweli hazijengi, na madhara yake ni kuleta chuki na uhasama katika jamii. 
Ni mimi: emu-three

No comments :