Nilishaanza kumshuku shemeji yangu kuwa anafahamu mengi, na siku
ya leo niliona ndio siku pekee ninayoweza kumbana , na kusema ukweli wote, lakini
sikutaka niongee naye peke yangu, nilishaongea na watu wa usalama, ambao
nafahamiana nao,na niishawaeleza ni nini lengo langu, na nikaona niwaite watu
hao waje kunisaidia ...
Endelea na kisa chetu
*********
Shemeji yangu huyo alipooa nafanya kweli akageuka huku na kule
akitaka kukimbia, na kabla hajafanya hivyo nikamuonyeshea ishara ya
kumuonya..., akatulia nikamaliza kuongea na huyo ofisa upelelezi, ambaye
nilishamgusia kuhusu hayo mambo yanayoendelea katika nyumba yangu na yeye
akaahidi kuwa atalifuatilia hilo tatizo kwa karibu.
‘Shemeji ...ina maana unataka sisi tufungwe?’ akauliza shemeji
yangu huyo sasa akionyesha ile sura adimu ya chuki, sura kama hizo kwa wengine
ni nadra kuonekana.
‘Ukweli wako ndio utakaokusaidia wewe na kaka yako, nilishawapa
muda wa kutosha, sasa wakati umefika, kama kweli unataka kumuokoa kaka
yako na wewe mwenyewe sema ukweli, niambie kila kitu nitakachokuuliza kabla
huyo jamaa hajafika..’nikamwambia.
‘Lakini shemeji mimi nitakuambia nini, nimeshakuambia kila kitu ninachokifahamu
mimi, mengine sina uafahamu nao, sio kila kitu kaka alikuwa akiniambia,
ananiita ananituma na kama hilo tukio, ..mimi nilikuwa sijui kitu..shemeji
kiukweli hivyo sio sahihi kabisa..’akasema.
‘Sawa ...basi kama umeshaniambia kila kitu ngoja hawo polisi
wafike, wao wana utaalmu zaidi yangu mimi, baada ya hapo, najua sitakusumbua
tena, unasikia,.tatizo wewe unafikiri mimi ninatania ..’nikasema na mara mlinzi
akaja, na kutuambia kuwa kuna jamaa wamefika wanataka kuonana na mimi.
‘Ni watu gani?’ nikauliza.
‘Wanasema wao ni watu wausalama, wamenionyesha vitambulisho
vyao...ni kweli ni watu wa usalama…’akasema huyo mlinzi, na hapo shemeji yangu
ambaye alifikiria nafanya utani, akasimama na kushika kichwa, na mimi nikamwambia
huyo mlinzi.
‘Waambia waje huku bustanini’nikasema huku nikiweka ile mashine
yangu vizuri, sikutaka mazungumzo hayo yaishie hewani.
‘Shemeji umafanya makosa makubwa sana, kaka akilisikia hili, na
hayo matatizo yake sijui kama mtaweza kuishi nyumba moja,...ina maana kweli ni
wewe shemeji, sasa unataka kaka afungwe,...aheri hata mimi mnzima nikifungwa
haijalishi kitu , lakini mume wako ni mgonjwa..huo ndio ukweli wenyewe, kama
ana matatizo…’akawa anasema kama anataka kulia.
‘Muda wa utani umekwisha ndugu zanguni, , maana mimi wakati
nawaonea huruma nyie mnafanya kweli..hamnionei huruma na mimi, hamfahamu kuwa
hata mimi ni binadamu,.., sasa ngoja na mimi nifanye kweli tuone mwisho wake
utafikia wapi, nina ushahidi wa kutosha wa kukuweka wewe na kaka yako ndani
..’nikasema.
‘Ina maana hata kaka, mumeo humpendi tena,...unataka umweke ndani
hujali kuwa anaumwa, siamini hilo shemeji?’ akauliza.
‘Wewe ndio utakwenda ndani kuisaidia polisi, ....kaka yako
atasubiri hadi hapo atakapopona, mjue mna makosa mengi ,kwanza kwa kuniibia,
pili kwa kugushhi mikataba halali, tatu kwa mauaji ya Makabrsha , nne kwa wizi,
na jingine hilo la jana la kutaka kuniua,..na mengine mengi...’nikasema na mara
hawo jamaa wakafika mmoja akiwa na pingu tayari mkononi kuonyesha yupo kazini.
************
‘Mungu wangu kumbe ni kweli…’akasema hivyo sasa akionyesha ule
uwoga wa dhahiri, sikufahamu kuwa shemeji yangu ni muoga hivyo mpaka nikamuonea
huruma, lakini hiyo ndio njia pekee ya kuupata ukweli.
‘Wakaribishe huku…’niliona wale wageni wakiaka kuingia ndani,
ikabidi niwaite kwa sauti, watuone kuwa tupo huku bustanini..
‘Shemeji, mimi sitaki kwenda jela, kwasababu sihusiki kabisa, yote
niliyafanya kwasababu ya kaka..kwasababu ya kumsaidia kaka, angalia ali yake
ilivyo, ...muhurumie kaka, shemeji...’akasema sasa akininong’oneza, na mimi
sikumjali.
`Ukitaka usalama wako ongea ukweli, maana mengi yanafahamika, wao
watakachofanya ni kupima ukweli wako,...sema yote unayoyafahamu, ukipindisha na
kusema uwongo, jela inanukia, jela sio mchezo, isikie hivyo hivyo, mimi
nimeionja na niliwekwa sehemu wanayosema ni nzuri, lakini taabu niliyipata
siwezi hata kusimulia....’nikasema na wale jamaa wakafika
Kwanza walijitambulisha na wakaonyesha vitambulisho vyao. Mimi
nikajifanya navikagua, halafu nikasema
‘Karibuni sana, niambieni shida yenu, maana mnatutisha,
silaha,..pingu, ni mimi mhalfu tena..’nikasema nikijifanya kunyosha mikono
kujisalimisha, na wao wakacheka kiogo, na kusema;
‘Haaah, hapana sisi tupo kazini, ni kweli..kazi yetu ni hiyo kuwatafuta
wahalifu, sasa tutashukuru na sisi tukisikia utambulisho wenu…’akasema
mmojawapo, na mimi nikajitambulisha na kumtambulisha shemeji yangu.
‘Sawa karibuni..’nikasema
‘Kwanza tunachohitajia hapa ni ushirikiano wenu, tupate ukweli kwa
hayo tutakayoyauliza, …’akasema
‘Sawa ..’nikasema
‘Mama mwenye nyumba,..wakati, umeshikiliwa kituo cha polisi, na
hata kupelekwa Segerea, ulisema kuwa nyumbani kwako kulitokea upotevu wa vitu,
kweli si kweli..?’ akauliza
‘Ni kweli…’nikasema
‘Je hebu kwa kutukumbusha tu, kulipotea vitu gani…’akasema
mwingine.
‘Ni kweli, kuna vitu vilipotea, na ni vitu muhimu sana, mojawapo
ni mikataba wangu halali, na zaidi hata silaha yangu...’nikaanza kuongea ,
japokuwa nilishaongea naye, lakini sikutaka shemeji yangu afahamu kuwa nawafahamu
hawo watu.
‘Una maana ile silaha iliyotambulikana kuwa ndiyo iliyomuua
Makabrasha?’ akauliza huyo ofisa usalama.
‘Ndio ..’nikasema.
‘Kwahiyo kumbe kwa kupitia hivyo vitu tunaweza sasa kumpata muuaji
halisi wa Makabrasha, ..’akasema huyo
mwingine
‘Na huyu umesema ni shemeji yako..?’ akauliza
‘Ndio…’nikasema na shemeji yangu alikuwa kanywea kweli kweli
haamini kinachotokea.
‘Huyu hapa ni shemeji yangu, kiukweli ni mtu niliyeishi naye hapa
namtambua vyema, ni mtu mwaminifu sana..’nikasema.
‘Hebu tuambie ndugu, ujue tunachokiuliza hapa tumekifanyia kazi,
na hatutaki kupoteza muda mwingi hapa…wewe na kaka yako mnaelewanaje..?’
akaulizwa swali.
‘Ni..ni..kak yangu, tunaelewana tu…’akasema
‘Kwahiyo shughuli zake nyingi unazifahamu…?’ akaulizwa
‘Zile anazoniambia, nazifahamu…’akasema
‘Sasa kutokana na uchunguzi wetu, wewe ni mtu wa karibu sana na
kaka yako, kuna mambo mengi sana mumekuwa mkishirikiana naye…huwezi kutuficha,
lakini tunahitajia kauli yako kukupima je unahusika au huhusiki…’akasema mmojawapo
‘Kuhusika kwa lipi..?’ akauliza shemeji, naona kaamua kujikakamua.
‘Wewe ndiye uliyekuwa ukitumwa na kaka yako, kuchukua vitu mbali
mbali, na katika upotevu wa vitu, kama alivyosema shemeji yako, makabati, au
nyumba haikuvunjwa, ina maana kuwa mtu aliyefanya hayo yote ni mtu wa
nyumbani,…kama kaka yako alikuwa hospitalini mtu mwingine anayeweza kuifanya
hiyo kazi ni wewe…’wakasema
‘Kazi ipi…?’ akauliza
‘Sikiliza sisi hatuja kupoteza muda, tunakuuliza kitu amacho hata
wewe unakifahamu, unasikia, tuna namna nyingi za kukufanya useme ukweli wote,
lakini kwanza tunahitaji ushirikiano wako,… hapa tunamstahi shemeji yako tu,
lakini tukifika huko utaimba yote kama wimbo unaoufahamu sana..’akaambiwa.
‘Sasa mnataka niseme nini?’ akauliza huku akijaribu kujitutumua,
naona alishaniona sio mtu wake tena, alishaniona mimi ni msaliti wake.
‘Kwanza kuna mkataba wa shemeji yako uliibiwa, je upo wapi?’
akaulizwa
‘Mimi sijaiba huo mkataba,...muulizeni kaka....’akasema.
‘Kwahiyo kaka yako ndiye anafahamu wapi huo mkataba upo, au
sio..?’ akauliza
‘’Mimi sijui…’akasema
‘Ok, shemeji tunaomba tuondoke na huyu mtu, sisi tunakuhakikishia
tukifika naye huko atataja kila kitu, sisi tulishamchunguza nyendo zake kwa
kirefu, tuna ushahidi wote kuwa anahusika kwa kiasi kikubwa sana,kuna mambo
mengi anayafahamu,na ameyafanya sasa hatuna muda wa kupoteza tena ...’akasema
Na mimi nikamuangalia shemeji yangu huyo ambaye alikuwa kama
kamwangiwa maji. Alikuwa hataki hata kuniangalia, nahisi chuki dhidi yangu
zilikuwa kubwa, lakini sikuwa na njia nyingine.
‘Shemeji hiyo ndio nafasi yako ya mwisho, kama unamjali kaka yako
sema ukweli, kama unaona kukaa kimiya ndio kutamsaidia kaka yako haya, mimi
nitawaruhusu muondoke nao, na unafahamu ni kitu gani kitakukuta huko mbele,
unamkumbuka yule rafiki yako aliyejifanya anaweza kuvumilia mateso ya huko,
alikuambia nini kilichompata,....kama wewe unajiamini zaidi yake niwaruhusu
muondoke ....’nikasema na yeye kwanza akaniangalia kwa jicho lenye chuki,
halafu akasema.
‘Haya mimi nitawaambia ukweli lakini naombeni mumuache kaka
yangu , kaka yangu anaumwa, na mengi aliyafanya bila kujitambua..’akasema
‘Hiyo sio kazi yako, sisi tunalifahamu hilo ndio maana tunakuuliza
wewe, hatujakwenda kumuliza kaka yako kwasababu anaumwa,...kama tungelikuwa
hatulitambui hilo, kaka yako sasa hivi angelikuwa jela. Sasa kwa vile
wewe ni mzima huna matatizo unahitajika utuambie ukweli, kwani wote lenu
ni moja....’akaambiwa, na akatulia kimiya kwa muda kama anawaza, halafu
akasema;
‘Haya ulizenu maswali yenu nitawajibu, kwa kile
ninachokifahamu...’akasema
‘Swali la kwanza, tuambie mkataba wa wanandoa hawa wawili ulioibiwa
upo wapi?’ akaulizwa.
‘Mimi sijui huo mkataba ulioibiwa ni upi, ...’akasema
‘Wewe unafahamu mikataba mingapi?’ akaulizwa
‘Mimi nilishaiona mikataba zaidi ya mmoja, sasa sijui upi ni upi?’
akasema.
‘Kwa hivi sasa wewe una mikataba mingapi?’ akaulizwa
‘Nina huu mmoja alisema nimpelekee huko hospitalini....’akasema
‘Ulishawahi kutumwa kuchukua mikataba kama hiyo kabla?’ akaulizwa
‘Ndio…’akasema
‘Ulipotumwa hukuambiwa ni kitu gani, …?’ akaulizwa
‘Niliambiwa nikachukue nyaraka, imeandikwa mkataba…wa hivyo na
hivyo, na upo mahali fulani, na ufunguo huu hapa, mimi namtiii kaka yangu,
nafanya hivyo…’akasema
‘Kwahiyo ulipochukua hiyo mikataba ulimpelekea nani..?’ akaulizwa
‘Kaka…’akasema
‘Kulikuwa na mkataba uliokuwa nao wewe , ambao haujaonekana mpaka
sasa, mkataba huo ndio shemeji yako anaoutafuta, kwa uchunguzi wetu, unao wewe,
tunahitajia huo mkataba ambao ni ule wa mwanzao uliotumwa kuuchukua, sisi tunao
ushahidi kuwa unao wewe...’akasema huyo ofisa.
‘Nimesema nilishamrudishia kaka....’akasema na kukatisha
‘Sema ukweli, ilivyoupata huo mkataba, uliingiaje kwenye nyumba ya
mtu , na ukifahamu mwenyewe yupo, ....ina maana uliuiba au sio?’ akaulizwa.
‘Kaka ndiye alinituma niuchukue...mimi sijaiba, kaka ni mwenye
nyumba pia...’akasema.
‘Ehe, uliwezaje kufungua makabati, ya shemeji yako?’ akaulizwa.
‘Nilipewa ufunguo na kaka, ....’akasema
‘Hebu tuonyeshe hizo ufungua’akaambiwa, na akatoa zile ufunguo
alizo nao akazionyesha kwa hawo watu, waliziangalia tu, kwa mbali bila
kuzigusa, halafu wakauliza
‘Kwahiyo hizo ufunguo zote ulizo nazo, alikupa kaka yako, na
zinaonekana ni za kuchonga?’ akauliza
‘Ndio alinipa kaka, lakini mimi sijui kama ni za kuchonga,...’akasema.
‘Alikutuma pia ukachukue na ule mkataba uliokuwa huko ofisini kwa
shemeji yako?
‘Ukazipeleka wapi hizo mikataba, ulizotumwa
‘Nilimpelekea kaka..’akasema
‘Kuna mkataba mmoja unakosekana, wewe bado unao,..tunauhitajia
huo..usitupoteze muda…’akaambiwa na hapo akasita kidogo
‘Kaka yako ndiye alikutuma hiyo mikataba sio..wa nyumbani, na wa
ofisini, au sio../’ akaulizwa
‘Ndio…’akasema
‘Kwa ujumla nakala za mikataba yote uliichukua wewe, baada ya
kutumwa na kaka yako…kweli si kweli…?’ akaulizwa
‘Ndio alinituma yeye, kwanza huo wa nyumbani alikuwa nao yeye
mwenyewe, alikuwa na nakala mbili, sikujua kuwa mmoja ni wa shemeji, baadaye,
akaniambia nizipeleke kwa Makabrasha...’akatulia.
‘Nilipofika kwa Makabrasha akaniambia nihakikishe kuwa hakuna
nakala inayobakia, mimi nilikuwa nimeshaficha nakala moja,...bila kaka
kujua,..’akasema
‘Kwanini ulifanya hivyo?’ akaulizwa.
‘Nilitaka nitoe nakala nyingine, kwani nilihisi baadaye inaweza
ikahitajika, kaka huwa anachanganyikiwa, baadae anaweza kuhitaji nakala au
kumbukumbu, huwa naan ahivyo kwa akiba…ila kiukweli mimi sikuwa nafahamu malengo
yao ni nini....’akasema
Ulijua lini malengo yao....?’ akaulizwa
‘Kuna siku waliniita kwenye kikao wakaniambia kwanini wameamua
kuziharibu hizo nakala zote...’akasema
‘Walikuambiaje , lengo lao ninini?’ akaulizwa na hapo akaa kaa
kimia, na hapo yule ofisa akauliza swali jingine.
‘Na kule ofisini uliwezaje kuingia , wakati muda wote kuna
walinzi?’ akaulizwa
‘Niliingia muda wa kawaida tu, yule mhudumu alikuwa hayupo, na
mimi niliwaonyesha kibali kuwa nimetumwa na shemeji, nikaweza kuingia kwasababu
nilikuwa na ufungua, alionipa kaka....’akasema.
‘Kibali gani hicho, ina maana ulikwenda kwa shemeji yako ukamuomba
hicho kibali?’ akulizwa
‘Aliwahi kunipa kibalia kabla,,...nikawa naendelea kukitumia..kuna
siku nafika kwa ajili ya matengenezo ya ofisi yao’akasema.
Hicho kibali hakina tarehe?’ akaulizwa, na kukaa kimiya, na yule
ofisa akauliza swali jingine.
‘Ina maana uligushi tarehe....?’akasema huyo mpelelezi
‘Kilikuwa hakijaandikwa tarehe....’akasema
‘Kwahiyo kumbe kaka yako alikuwa ana ufunguo zote za ofisini na za
makabati ya mke wake?’
‘Mimi sijui, hilo swali ingelifaa mumuulizeni yeye mwenye kaka,
yeye alinipa ufunguo akanituma niende ofisini akanielekeza wapi pa kuipata hiyo
nakala ya mkataba, mimi nikafanya kama alivyoniagiza....’akasema.
‘Wewe kwanini hukumwambia shemeji yako ?’ akauliza
‘Kwanini nimuambie, kama kaka angetaka nifanye hivyo angeniambia
nimwambie, kaka kafanya hivyo kama mume wake, na mume wake ana haki kwenye
kampuni za mkewe, kuna ubaya gani hapo eeh , ‘akasema na kuniangalia mimi , na
mimi nikawa nimemkazia macho, akaangalia pembeni.
‘Ohooo, kwa vile yeye ni mwanaume, sio…safi kabisa, mlishalipana
hilo, ..’akasema mmojawapo.
‘Kaka aliniambi ahivyo…’akasema
‘Kuwa yeye ana mamlaka popote, hata kama kampuni sio yake,wewe
hujui kuwa kampuni hiyo uliyokwenda kuchukua huo mkataba ni ya shemeji yako sio
ya kaka yako ...huoni kuwa ni makosa?’akaulizwa
‘Hayo muulizeni kaka yeye mwenyewe , mimi nimejitolea kuwaambia
yale ambayo hata kaka hakutaka niwaambie, ...najua nimefanya makosa sana
kuwaambia, kaka hatanisamehe kwa haya, lakini sina jinsi...’akasema kwa
uchungu.
‘Swali jingine, je kaka yako ndiye aliyekutuma kuchukua bastola kwenye
kabati la shemeji yako?’ akaulizwa na hapo akatulia kidogo, halafu akasema.
‘Lakini kaka sio yeye aliyemuua Makabrasha, ...’akasema
‘Una uhakika gani na hilo?’ akaulizwa na kukaa kimiya, na huyo
ofisa hakutaka kumshinikiza kwa hilo, kwa vile wao wanafaahmu zaidi, wakauliza
swali jingine
‘Kama sio kaka yako basi ni wewe uliyemuua Makabrasha?’ akaulizwa
‘Sio mimi wala sio kaka..’akasema
‘Unaposema sio kaka yako au wewe, ina maana unamfahamu muuaji, ni
nani aliyefanya hivyo?’ akaulizwa
‘Kwakweli mimi sijui,....’akajibu na kutulia na yule ofisa
akatabasamu na kutikisa kichwa, halafu akauliza swali jingine
‘Tuambie ilikuwaje siku hiyo ambayo Makabrasha aliuwawa,, maana
usipotuambia ukweli , ujue hapo wewe utakamatwa kama muuaji, wewe na kaka
yako’akaambiwa.
‘Mimi sio muuaji, ..sijamuua Makabrasha, japokuwa ni kweli mimi
ndiye niliyekwenda kuichukua hiyo bastola kwenye kabati la shemeji,
...nilifanya hivyo nikiogopa kuwa shemeji kwa jinsi alivyokuwa na hasira ,
angeliweza kuitumia kumuua kaka, nikaona bora niichukue hiyo silaha nikaifiche
mbali kabisa na wao’akasema
‘Kwahiyo hukutumwa na kaka yako kuichukua hiyo bastola?’ akaulizwa
‘Hapana kaka hajanituma kuchukua hiyo bastola, niliichukua
mwenyewe baada ya kuiona hapo, siku aliponituma kurudisha hiyo mikataba
mipya...wakati nafungua kabati la shemeji nikaiona hiyo silaha, na najuta
kwanini niilichukua hiyo silaha’akasema
‘Ulipoichukua hiyo silaha uliipeleka wapi?’ akaulizwa
‘Niliificha ofisini kwetu, na siku moja, nikaichukua kwenda nayo
porini kuitupa...’akasema na huyo ofisa akatabasamu, na kumwangalia mwenzake,
ambaye alitikisa kichwa kama kukubali kitu.
‘Kwanini ufanye hivyo?’ akaulizwa
‘Kwa wazo hilo hilo kuwa ikiwemo mle ndani inaweza kuleta majanga,
na bora niitupe mbalii kabisa,..’akasema
‘Ikawaje sasa, ...?’ akaulizwa
‘Nikiwa ndani ya gari, nikiwa naelekea huko porini , nilifika
mahali gari likawa halina mafuta, ....kituo cha mafuta kilikuwa karibu tu,
lakini gari lilikuwa haliwezi kufika hapo, kwahiyo nikaona nichukue galoni
niende kununua...’akasema .
‘Unaweza kutuambia ni kituo gani hicho, na una risiti na mafuta
uliyonunua siku hiyo, kama ushahidi?’ akaulizwa
‘Mh,hata sikumbuki, na hata jina la kituo, sikumbuki, na nakumbuka
sikuchukua risiti...’akasema
‘Ehe, ikawaje?’ akaulizwa
‘Niliporudi kwenye gari langu sikuuona ule mkoba wangu
uliokuwa na silaha, ulikuwa haupo,....inaonyesha kuwa kuna watu walikuja kwa
haraka wakafungua kiyoo, wakauchukua, sikuwa makini kufunga viyoo vya gari,
ningelijua ningelifunga hivyo akasema
‘Endelea…’akaambiwa
‘Nahisi kuna mtu alikwua akanifuatilia, kwasababu ni nani
angelijua kuwa ni na vitu kama hivyo,...nilijaribu kuangalia huku na kule
lakini sikuona dalili ya mtu, nikajua nimeibiwa, na silaha ya watu
imeshachukuliwa, sikujua nifanye nini, nikaamua kukaa kimiya, ..hadi hapo
niliposikia kuwa hiyo silaha ndiyo iliyofanyia hayo mauaji,..huo ndio ukweli
wenyewe, ..’akasema
‘Hiyo hadithi yako hukuipanga vyema, inabidi ukaipange vyema, hiyo
hadithi yako haina vina wala mizani, itakutia matatani, usiposema
ukweli,..’akaambiwa.
‘Ndio ukweli wenyewe huo....’akasema
‘Sema ukwei ni nani uliyempa hiyo silaha, ujue ulichukua silaha ya
watu inayomilikiwa kisheria, na silaha hiyo ikatumiwa kufanyia mauaji, na
muuaji mpaka sasa hajapatikana, kwanini wewe usikamatwe kwa kosa hilo, tuambie
ukweli ulivyo..’akaambiwa.
‘Ukweli ndio huo, sina ukweli mwingine, ...’akasema
‘Inavyoonekana ni kuwa kaka yako alikutuma hiyo silaha, ili ukampe
mtu fulani, ambaye ndiye aliyemuua,
Makabrasha, sisi tunafahmu kuwa ni wewe uliifanya hiyo kazi,
ulitakiwa uifanye wakati kaka yako anaongea
na marehemu....’akasema
‘Hapana,kaka hajawahi kunituma hiyo silaha, kaka kipindi hicho
anaumwa, hajui kabisa kuhusu hiyo silaha, ....na mimi sijaua mtu, na siwezi
kufanya hivyo..kwanini tumuue mtu kama yule ambaye anatusaidia sisi, hilo
hamlioni jamani, Makabrasha alikuwa ni mtu wetu wa karibu,....’akasema akiwa na
wasiwasi.
‘Anaweza akawa mtu wenu wa karibu lakini mkaona hawafai tena,
akifa yeye, hisa zake mtazichukua nyie, kwasababu akiendelea kuwepo, hisa zote
mtazipoteza kwa vile alikuwa anawadai pesa nyingi sana, na madeni yake alipanga
yalipwe kwa hizo hisa,..hiyo ndio mipango yenu,...’akasema huyo mtu wa usalama.
‘Hapana hatujamuua Makabrasha, sijui ni nani aliyefanya
hivyo...tunasikitika sana kwa kifo chake...’akasema
‘Ni nani aliyemchukua kaka yako kutoka hospitalini hadi kwa
Makabrasha?’ akaulizwa
‘Ni mimi, alinipigia simu kuwa niende kumchukua,...kwani ana
mazungumzo muhimu na marehemu’akasema
‘Kwahiyo alikutuma pia ukachukue hiyo silaha, umpe mtu mwingine
kama unakataa kuwa sio wewe na huyo mtu mwingine ni nani,..usipomtaka huyo mtu
ni wewe, nakuuliza haya ukijua sisi tunafahamu kila kitu, lengo ni kukupima
yawezekana haya uliyafanya kwa kumsaidia kaka yako ...’akasema kabla hajamaliza shemeji
akamkatisha na kusema;
‘Mbona mnanitungia uwongo, sijafanya hivyo, hata silaha yenyewe
sijawahi kuitumia,...’akasema.
‘Unaweza usiweze kuitumia ukabahatisha,kwani ina ugumu gani ,
yoyote anaweza kutumia, kama anafahamu jinsi ya kufyatua risasi, hata hivyo
hatujasema wewe ndiye uliyemuua, kuna mtu uliye mpa hiyo silaha, ndiye
aliyefanya hayo mauaji, na unamficha, na kwahiyo wewe utashitakiwa kama ndiye
uliyefanya hayo mauaji ...’ akaambiwa.
‘Mimi nimeshawaambia huko ukweli, na kwanini tumuue Makabrasha
wakati ni mtu anayetusaidia?’ akauliza.
‘Hilo swali unatakiwa ujibu wewe,...’akaambiwa.
‘Mimi nimeshawaambia ukweli,....’akasema.
‘Hilo litajulikana baadaye, kama unasema ukweli, sisi tumeshaujua
ukweli, nia yetu hapa ni kukupima, na ukweli ndio utakao-kuokoa
wewe...’akasema.
‘Nimeshawaambia ilivyokuwa,...mnataka niseme ukweli gani zaidi ya
huo’akasema.
‘Hujatuambia ni nani uliyempa hiyo silaha, ...hilo unatuficha, ili
hali sisi tumeshamfahamu, ’akaambiwa.
‘Mimi nimeshawaambia hiyo silaha sijampa mtu...’akasema.
‘Ehe, ulipomchukua kaka yako wewe ulikwenda wapi..hebu elezea
hapo…maana ni lazima umfikishe pale, wewe ulipomfikisha ulikuwa wapi
ukimsubiria kaka yako....?’ akaulizwa.
‘Mimi nilimsubiria nje, barabarani..’akasema.
‘Ni nani aliyekuona ukimsubiria,maana hapo usipokuwa na ushahidi
wa kutosha, utaingia matatani...’nikamwambia.
‘Yule mlinzi wa nje wa hiyo hoteli iliyopo karibu na lile jengo,
nilicheza naye drafti, hadi kaka alipokuja, na tukaondoka naye...’akasema. Na
huyo jamaa akaandika jambo kwenye karatasi yake, na kusema.
‘Hilo nilishalifuatilia, ni kweli...ulionekana ukicheza drafti na
huyo mtu, lakini kabla ya hapo...mhh, sawa hilo tuliache hivyo kwanza au sio
mwenzangu..?’ akasema akiangaliana na mwenzake..
‘Yap, weka akiba..’akasema mwenzake.
‘Lakini bado hatujamalizana na kipengele hicho, kuna ukweli mwingi
unatuficha hapo, na hatujui kwanini unafanya hivyo, tutakuja kuuliza sana
sehemu hiyo muda ukifika....’akasema na kukatisha.
`Swali la tatu, hiyo nakala ya mkataba wa zamani uliokuwa nao wewe
upo wapi?’akaulizwa
‘Niliurudisha kwenye kabati la kaka.....’akasema
‘Lini?’ akaulizwa.
‘Leo asubuhi...wakati shemeji walipompeleka kaka, mimi nilibakai
nyuma, nikaurudisha ..kimia kimia, niliuweka pale ulipokuwa,...’akasema.
‘Kwanini ulifanya hivyo?’ akaulizwa
‘Niliogopa kuwa kaka akifahamu nina nakala nyingine ya huo mkataba
atagomba, kwani wao walitaka nakala zote ziharibiwe, ..lakini pia nilisikia
kaka akihangaika kuutafuta huo mkataba wa zamani,na pia nimesikia shemeji
akiuulizia huo mkataba, nikaona jambo jema kuondoa hili tatizo nikuuweka huo
mkataba wa zamani, ili kaka akija akiuona, aurudishe kwa shemeji mambo
yaishe...’akasema
‘Hapo pia kuna kitu unakificha, kama wewe uliona kuwa mkataba huo
ni tishio kwenu, hasa kwa kaka yako, na mkakubaliana kuwa mikataba yote
iharibiwe, ibakie hiyo mipya, ni kwanini ukaamua kuurudisha hapo tena,....kuna
nini kilikusukuma kufanya hivyo, au ulitaka kuuficha hapo kwa muda ili baadaye
uje uuchukue, maana ulishajua kuwa kule kwako hakuna usalama tena,..’kaulizwa
‘Mimi niliamua kuurudisha kwa nia njema kabisa…,kama
nilivyowaambia...’akasema
‘Kwahiyo huo mkataba kwa sasa upo wapi?’ akaulizwa
‘Nimefika leo kuuangalia, nimekuta kabati halifunguki, kwahiyo
sijui kama upo hapo hapo, ila nina uhakika niliuweka hapo hapo....’akasema
‘Swali kubwa hapo ni kwanini uliurudisha?’ akaulizwa
‘Nilitaka kaka aje auchukue mwenyewe,...., sikutaka tena kuendelea
kujihusisha na mambo ya familia, na niliona nafanya makosa, na nilitaka kaka na
shemeji waje waelewane....’akasema.
‘Waelewane, kwani walikuwa hawaelewani…kwasabababu ya mkataba au
kwasababu ya matendo ya kaka yako…?’ akaulizwa na kukaa kimia.
‘Ina maana huo mkataba hadi hivi sasa upo kwenye hilo kabati...?’
mimi nikamuliza na akaniangalia akionyesha uso wa kunikasirikia , akasema;
‘Ndio upo humo kwenye kabati..., lakini kabati halifunguki kabisa,
kama vile kitasa kimebadilishwa, kama likifunguka mtauona, upo .... maana mimi
ndiye niliyeuweka leo asubuhi,...na kuna kitu changu kingine, sijui kama kipo
humo au vipi....’akasema na mimi kwa haraka nikainuka na kuomba niende kwenda
kuuangalia kama kweli ndio huo mkataba wetu wa zamani.
‘Nenda kahakikishe, halafu uje, tuendelee, maana huyu mtu
asipotuambai ukweli, leo tunakwenda naye..’aaksema huyo ofisa.
‘Mimi nimeshawaambia ukweli, naomba niende nikamuone kaka, yeye
ndiye aliyenituma… na jinsi ninavyochelewa nampa mashaka, na wasiwasi, na hivyo
vitu havitakiwi kwa afya yake...’akasema
‘Yeye ndiye aliyekutuma nini, huo mkataba, au sio…kuna mengine
kakutuma hujatuambia…au sio?’ akaulizwa
‘Ndio alinituma huo mkataba na vitu vingine,....’akasema
‘Shemeji wewe nenda kahakikishe hilo,..huyu haendi mahali, hadi
hapo kitakapoeleweka, kuwa tunakwenda naye kituoni, au anafunguka ukweli wake
wote, na ukweli wake ndio utakaomfanya sisi tumwamini, na akifanya hivyo basi
sisi tutakuwa upande wake, kumlinda..’akasema huyo ofisa.
Mimi nikawa nimeshaanza kutembea kuelekea ndani , moyoni nikiwa na
hamasa kuupata huo mkataba wa zamani, …mkataba utakaoleta haki ndani ya familia
yangu,…na huku nyuma nikasikia shemeji akiniambia;
‘Shemeji ...ukiona kitu changu ndani ya huo mkatana nakuomba
tafadhali, unipatie, nahisi nimekiacha ndani ya huo mkataba...’akasema na mimi
sikumjali nikaharakisha kwenda kufungua hilo kabati na wale watu wa usalama wakiendelea
kumuhoji, hawakujua kuwa nimeacha mshine ya kurekodia matukio, ikiwa inafanya
kazi....
NB Ni hayo kwa leo, natumai leo mumefurahia sehemu hii kama
mumefurahia,naomba comments nyingi sana..
WAZO LA LEO:
Katika maisha yako jifunze kuwa mkweli, kusema ukweli na kutenda yaliyo haki, hiyo
ndio njia ya kuiweka nafsi yako huru, kujiamini na na kutokuwa na wasiwasi…na
matokea yake huwa ni chanya,…na hutajuta katika maisha yako yote, kinyume chake
ni mashaka, na mwisho wake ni kuzalilika tu.
Ni mimi:
emu-three
No comments :
Post a Comment