Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Monday, January 15, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-58




 Ilipofika asubuhi, nikiwa nimechoka, macho yana usingizi, maana ilikuwa hakuna kulala…mjamaa yeye alikuwa anakoroma tu, usingizi kwa kwenda mbele. Hata asubuhi ilikuw kazi sana kumuamusha.

‘Leo sijisikii vizuri mwili umechoka sana…’akasema

‘Ndio maana tunataka twende hospitalini…’nikasema

‘Hapana wewe nipe zile dawa zangu, leo hata kazini nitachelewa kwenda ..’akasema

‘Sikiliza…’nikasema na kabla sijaendelea kuongea yeye akasema;

‘Kuna ndoto mbaya  niliota usiku.., lakini sikumbuki ni ndoto gani,...sikumbuki kabisa, lakini ilikuwa ya kutisha inavyoonekana, sitaki…hata kuikumbuka maana sio nzuri, muhimu nimegundua ni ndoto tu....’akasema huku akijaribu kukumbuka

‘Uliotaje..?’ nikamuuliza

‘Yaani najaribu kukumbuka lakini haiji akilini….na bora nisiikumbuke tu..’akasema

‘Kwanini…?’ nikauliza

‘Ni mbaya…’akasema akiniangalia mimi kwa macho yaliyojaa wasiwasi, ni kama haamini, au…

‘Nikuulize hukumbuki kabisa kilichotokea jana..?’ nikamuuliza

‘Jana..hapana..sikumbuki zaidi ya ndoto mbaya, hata hiyo ndoto haiji akilini, …’akasema

‘Jana wewe hukuwahi kuingia maktaba usiku ukachukua kitu?’ nikamuuliza

‘Kitu…! Kitu gani…hapana, mimi sijaingia huko kabisa, hilo usinidanganye, nakumbuka nilipotoka matembezi na mdogo wangu, ila kuna sehemu, nakumbuka kuwa nilitoka na mdogo wangu, mdogo wangu yupo..?’ akauliza

‘Ndio..hilo unakumbuka sio..?’ nikauliza

‘Sasa hapo sijui..ni ndoto ama ni kweli, kama mdogo wangu yupo basi, inawezekana ikawa ni kweli, lakini mengine sitaki kukumbuka…’akasema


‘Na ulipolala hukuwahi kuamuka hata kwenda kujisaidia hata mara moja?’ nikamuuliza

‘Nilala kama gogo, nahisi nilikuwa nimelewa,ni kama nililewa, hivi nilikunywa, kwanini hukunikataza....’akasema.

‘Basi kuna tatizo, kama hukumbuki uliyoyafanya jana basi ujue unahitajika kwenda kumuona docta hakuja jinsi hapo...’nikasema

‘Kwani kuna nini kimetokea mke wangu..?’ akaniuliza akionyesha mashaka sasa

‘Nakumbuka kama ulitoka nje, ukaenda maktaba...ukachukua kitu’nikasema

‘Mke wangu hapana…nakumbuka niliporudi kazini nililala ..hata hiyo kunywa pombe mimi sikumbuki kabisa..ila kuna kitu nahisi kuwa mimi nilikuwa na mdogo wangu, hapo sina uhakika…’akasema

‘Hakuna shida, wewe jitahidi sana kutuliza kichwa, ili uweze kukumbuka vyema, na ili akili yako iwe sawa, inabidi twende hospitalini wakafanye uchunguzi wa kina maana hali kama hiyo sio nzuri…’nikasema.

‘Mimi siumwi mke wangu hali kama hiyo walisema inaweza kutokea , na itapita, usiwe na wasiwasi, ilimradi tu, nikumbuke, maana hata ukinirudisha hospitalini, itasaidia nini, itaisha yenyewe tu...’akajitetea.

‘Ulitakiwa mara kwa mara uwe unakwenda kiliniki, hujaenda, na ukumbuke kuwa uliambia kukitokea jambo lisilo la kawaida pia uende haraka ukamuona dakitari, na unaona hali uliyo nayo, unapoteza kumbukumbu, unafanya mambo usiku na hukumbuki kuwa ulifanya, ....ni muhimu tukamuone dakitari, hilo halina mjadala...’nikasema.

‘Oh…kwanini lakini, haya bwana, kama unaona hivyo ni vyema, tutakwenda tu mke wngu,.....’akasema.

‘Na utakwenda huko ukafanyiwe uchunguzi wa kina, ili tuone tatizo ni nini, kwahiyo unajiandaa kwenda kukaa huko kwa muda...’nikamwambi na hapo akashituka na kusema;

‘Hapana, kwenda tutakwenda kw vipimo, halafu tunarudi nyumbani, ...siwezi kupoteza muda wangu huko, kuna mambo mengi ya kushughulikia, bila kuyamaliza hayo mambo, sitakuwa na amani...’akasema.

‘Wewe unasema hivyo, lakini mimi niliyeshuhudia mambo ya usiku, siwezi kukubali, ukalala hapa nyumbani tena.. ni lazima ukafanyiwe uchunguzi wa kina, kwa hiari , au...’nikataka kusema neno lakini yeye akakatiza na kusema

‘Sawa mke wangu nimekuelewa, nitakwenda,...nitafanya yote wanayotaka wao, sitaki mke wangu uishe kwa mashaka,..na kukosa amani kwa ajili yangu, mengine nitayafanyia huko huko hospitalini, . nakupenda sana mke wangu ...’akasema huku akionyesha kutokufurahishwa na uamuzi huo....

‘Ujitahidi sana, kufuata msharti ya dakitari...’nikamwambia

‘Sawa mke wangu, usijali, nitajitahidi sana,....maana nataka kuondokana na hii hali,...unajua mke wangu niliacha kwenda kiliniki nikijua kuwa sina tatizo tena,...najua docta atanilaumu sana, lakini ...aah, hata hivyo najiona nimepona. Mke wangu nataka nipone kabisa tuchape kazi kama zamani. Tukae tufanya kazi, sitaki nije kuonekana sijui kulea familia yangu...’akasema.

‘Hamna shida, siku ukikumbuka yote yaliyopita ukaniambia ukweli moja baada ya jingine, ndio nitafahamu kuwa kweli umepona, na hutarudi hapa nyumbani mpaka nihakikishe hilo...’nikasema.

‘Kwani sijakuambia kila kitu mke wangu, sizani kama kuna jambo sijakuambia, eti mke wangu kuna kitu sijakuambia kweli, kuhusu nini hasa, ...?’akauliza akiniangalia kwa mshangao

‘Kwa swali lako hilo inaonyesha bado haupo sawa,… hujapona, ukipona utakumbuka kuwa hujaniambia ukweli wote, na ni muhimu sana kwangu, ni muhimu sana kwa ajili ya familia hii, umesikia, ukweli wote ndio kibali cha kuwa wewe umepona vinginevyo, utadumu sana huko hospitalini...’nikasema.

‘Mhh, kweli , hakuna shida...’akasema na tukaondoka kuelekea hospitalini.

**************

Baada ya mume wangu kufikishwa hospitalini nikarejea nyumbani na kwanza kabisa nilihakikisha kuwa kila kitu kipo kama kawaida, na ule mto na shuka lililotobolewa na risasi nilivikunja vizuri, na kuvihifadhi mahala salama, kama vitahitajika kama ushahidi. Hata ile bastola, mimi nilihakikisha siugusi bila soksi ya mkononi, vyote hivyo nikavihifadhi sehemu salama.

Nilijua kabisa sauti ya mlio huo wa bastola itakiwa imesikika kwa majirani, na nilishapanga jinsi gani ya kuwajibu, niliwaambia hakuna tatizo,....sikutaka kuwaambia lolote, kwani kila kauli utakayotoa, inaweza kuwa ushahidi baadaye, japokuwa wengi walipoona mume wangu akitoka na kufuatili na kuona tunaelekea hospitali walijua ni hayo matatizo ya mume wangu ...

Docta jirani yetu ambaye alinipigia simu , nilimuambia kuwa ni yale yale matatizo ya mume wangu..

‘Lakini nimesikia sauti ya mlio wa bunduki, ..kulitokea nini..?’ akauliza

‘Ni utundu wake tu, ina maana hukuiondoa hapo ilipokuwa...’nikasema

‘Nilikuwa mbioni kufanya hivyo, lakini si unajua mambo yalivyofungamana…’nikasema

‘Utakuja kukumbuka ushauri wangu, sasa umeamuaje…?’ akasema na kuuliza

‘Kama nilivyokuambia, hali yake bado, kwahiyo asubuhi tunampeleka hospitalini…’nikasema

‘Akibisha, wewe niambie nitajua la kufanya..’akasema

‘Sawa nitafanya hivyo…’nikasema

Dunia haina dogo, hata mwandishi mmoja wa habari jirani, alifika kutaka kujua zaidi nikamwambia hakuna cha zaidi, hakuna tatizo, na ole wake akiandika mambo ya kizushi...na wananifahamu hakuna lolote lililoandikwa kwenye magazeti.

Tuendelee na kisa chetu....

*****************

Kutokana na afya ya mume wangu kubadilika hivyo…, mimi ilinibidi nianze kufikiria mipangilio mingine. Kuna muda nilitaka niachane na haya mambo kabisa, lakini kwa vipi…maana kuna mambo ya kisheria ndani yake, na hata nikisema niache yabaki kama yalivyo, nigange yajayo…lakini, hali halisi ikawa inanisukuma nifanye hata yale nisiyoyataka kuyafanya.... Ndio nikakaa kwenye kiti na kuanza kuandika…

‘Afya kwanza…’ mkataba wa asili ulitaka hilo, lazima nitimize hilo kwa ajili ya mume wangu, na hata wakili wangu alinisisitizia hilo, hata hivyo, hata bila mkataba kiubinadamu, nilitakiwa kuwajibika  kwa mume wangu japokuwa mengi yalishajitokeza yaliyonifanya nianze kubadilika kinafsi,..chuki ilishaanza kugusa nafasi yangu.

‘Lakini lazima hili tatizo liishe, ..’ hiyo ilikuwa fikra ya pili, kuwa pamoja na hayo, lazima nifikirie namna gani ya kulimaliza hili tatizo kabisa ili maisha yaendelee sasa kwa vipi

‘Kwa vipi…’nikatulia kuwaza

‘Ehee..hapa kuna mambo mawili…’nikasema

‘Jambo la kwanza…labda mimi nikubali yaishe.. na je nikikubali hilo, je kutakuwa na madhara gani…?’ nikaandika kwenye laptop yangu…

 Je nikikubali …mkataba wao unasemaje....?’ nikajaribu kukumbuka mkataba wao unavyosema, japokuwa sikutaka kabisa kuugusa huo mkataba, nikakumbuka kama nilivyowahi kusoma

‘,…kwenye mkataba wao, kama nitakubali yaishe inabidi nikubali maamuzi ya mume wangu,..kwanza kuwa kakosa na mimi nimeshamsamehe, na kwa maana hiyo moja kwa moja ninakubaliana na yale waliyoyapitisha kwenye mikataba yao mingine eti kwa masilahi ya familia, na yaliyomo humo…

-Mume kama mume anashika hatamu…’sio mbaya mimi sikatai,yeye ashike hatamu tu, lakini kwa msingi gani, sasa…wa haki , au wakutumiwa yeye kwa masilahi yaw engine, maana hapo anatumiwa tu, halijui hilo…

-Haki za watoto, ikiwemo huyo mtoto wa nje, na kwa vile ni wa kiume yeye atakuwa kiongozi wa familia…: Mhh, haiwezekani..hili haliwezekani hata kidini, …siwezi kulikubali, lakini lipo kwenye mkataba, na nikikubaliana na mume wangu hili linapita bila kupingwa…

-Nikikubali pia, ina maana nimekubaliana na mkataba wao mwingine ambao mume wangu ndiye anausimamia kama kiongozi wa familia, kwenye huo mkataba mwingine ambao moja kwa moja unafungamana na mkataba wa asili wa familia, umewapa watoto wa marehemu hisa, kutoka kwenye urithi wao…

Hawa watu wana kichaa…sitakubaliana na hili.

‘Njia ya pili ni ya kwenda mahakamani, na ikifikia hapo, ndoa, hakuna…uadui mimi na mume wangu….’

Simu ikaingia ujumbe wa sauti….

Tuendelee na kisa chetu…

*******

‘Mimi ni Yule jamaa mliyekutana naye kule uwanja wa ndege,..nilikuambia tutakuja kuongea, na sababu kubwa ni kuwa polisi wamenitaka kunihoji, na pia nasikia wanahitajia mimi niwe shahid kwenye kesi…’akasema

‘Kesi ipi…?’ nikamuuliza

‘Najua madam wewe ni mkurugunzi, unamiliki hisa kubwa kwenye familia yako, lakini humo pia kuna hisa za watoto wa marehemu, hilo halipo wazi, na..kutokana na ushahidi nilio nao, hilo litakuja kuwa wazi..achana na hilo, lakini pia, watoto wa marehemu wanastahiki kumiliki kampuni ya mume wako..kwa wingi wa hisa walizo nao, na mume wako, hana pesa ana madeni, kwahiyo uwezo wa kufany alolote hana


‘Na zaidi anakabiliwa na kesi ya mauaji, mimi ninao ushahidi wa kutosha wa kumweka ndani,…ni swala la mimi tu kukutana na huyo mpelelezi wao, lakini huyo mpelelezi wao, sipatani naye…ndio maana nikaona nioane na wewe, tuone tutasaidianaje..’akasema .

‘Mimi kwa ushauri wangu wewe kama raia mwema unawajibika kushirikiana na polis, na haki itajulikana au sio..kwahiyo kwani kuna ubaya gani ukiutoa huo ushahidi polisi…?’ nikasema

‘Ina maana upo tayari kuacha mume wako afungwe, maana ushahidi wangu ni kumfunga mume wako, lakini pia upo tayari kuachia hisa zako ziende mikononi mwa watoto wa marehemu…mimi nina ushahid kuwa wao, hizo hisa wamezipata kimagendo, je hutaki nikusaidie kwa hilo,…’akasema

‘Ushahidi gani ulio nao, wa kusaidikisha hayo…?’nikauliza

‘Nina ushahid hapa nikiutoa mume wako anafungwa,..na wewe pia utaonekana kama mlishirkiana hilo ni lakwanza lakini pia nina ushahidi wa kuwa hisa zao, japokuwa zipo kwenye mkataba, lakini unaweza kuutumia kuhalalisha kuwa hazikupatikana kwa haki,..je hutaki nikusaidie kwa hilo, na pia nimsaidie mume wako..huyo wakili mtoto wa marehemu ananitafuta sana, lakini hatujaweza kukutana mimi na yeye, sasa kabla ya kukutana na yeye, ..nimeona nikupigia simu…’akasema

‘Nimekuuliza huo ushahidi upoje…?’ nikauliza

‘Tukikutana utaweza kuuona, haina shida kabisa, mimi nawajali, sitaki mume wako ambaye ni mgonjwa asumbuane na polisi, na bila huo ushahidi ambao polisi wanautafuta kwa hivi sasa, bado hawataweza kumkamata mume wako, lakini cha muhimi ni wewe kuliweka hili liwe siri, ukilivujisha basi mimi sina budi, itabidi niwasiliane na polis, unaona ilivyo, kwahiyo iwe siri…’akasema

‘Kwani mume wangu ni muuaji, hajaua bado, alikuwa mgonjwa, nilikuambia hilo, …’nikasema

‘Huo ushahid utasema…hakuna shaka na hilo….’akasema

‘Kwahiyo unataka nini…?’ nikamuuliza

‘Nitakupigia…’akasema na kukata simu.

Alipokata simu, kwanza nikatuliza kichwa, kitu kilichonishtua ni kuhusu huyo wakili, kijana wa marehemu…kama huyu mtu atakutana na huyu mlinzi wanaweza kujenga ubia ambao unaweza ukawa mbaya sana wa kunisumbua mimi, sasa nifanye nini

Hapo hapo nikashika simu na kuwasiliana na wakili wangu:

‘Kuna swala hili la familia ya marehemu, siku zinakaribia, natakiwa kukutana nao ili kumalizana kuhusu huo mkataba wao, unaodai kuwa wao wana hisa kwenye kampuni ya mume wangu, ..na seehmu kwenye kampuni yangu..’nikasema

‘Hilo niachie mimi….’akasema

‘Lakini ni muhimu nikutane nao, maana waliniona kirafiki..kuacha huyo ndugu yao mwingine…’nikasema

‘Nitaongea na wakili wao kuhusu, hilo, ili niende mahakamani kuweka pingamizi, ili twende kisheria…’akasema

‘Lakini..hapo huoni nitakuwa sikuwasikiliza, maana wao walikuja kwangu wakasema wapo tayari kuridhia makubaliani, bila ya kwenda mahakamani…’nikasema

‘Wao wamesema hivyo, kama ukikubaliana na mkataba huo, au sio, huoni kuwa wamekutega, kwa namna moja kwa njia ya kumsaidia mume wako,..hulioni hilo..hata hivyo, huo mkataba upo kisheria, ni lazima sheria ndio iutengue, na huwezi kuutengua bila kupitia kwenye haki za kisheria, na hapo inabidi mimi nikutane nao…na ili uoekane huo ni batili, ni lazima twende mahakamani…’akasema

‘Kwahiyo tufanyeje…?’ nikauliza

‘Kwa hivi sasa wewe subiria kwanza, wao waanze, maana wao ndio wanadai mirathi, ni wajibu wako kwenda mahakamani kudai wanachostahiki kukidai..’akasema

‘Sawa….lakini kuna kitu kingine ambacho kinanifanya nitaharuki…’nikasema bado nikiwa sina uhakika kama kweli hilo ninaweza kumuambia wakili wangu au la..lakini wakili wangu ndiye kila kitu kwa mambo hayo

‘Kitu gani…?’ akauliza

 Huyu mlinzi sasa ananiweka roho juu, sio tu kwa ajili ya mume wangu lakini kwa namna moja anataka kugusa haya ya mikataba, na hayo wanayodai  wanafamilia hawa, kuwa wana hisa ndani ya kampuni zetu, inatakiwa kumdhibiti huyu mtu mapema, kwani akiungana na wakili mtoto wa marehemu itakuwa ni vita nyingine, ..nikasema

‘Kuna mtu mmoja ananitishia kuhusu mume wangu, muda hivi kanipigia simu anataka kuonana na mimi, nataka  na wewe uwepo, japokuwa kasema kuwa hataki mtu mwingine awepo, ila nataka uwepo wako usiwe wazi, …’nikasema

‘Anadai nini kwani…?’ akaniuliza

‘Anataka eti nimfunge mdomo, ili asiwe shahidi kuwa mume wangu, kwani ana ushahidi wa kubainisha kuwa mume wangu alikuwepo siku ya tukio…na huenda akawa anahusika kwa hayo mauaji ya Makabrasha…’nikasema

‘Kwani mume wako kashitakiwa tayari , au kuna dalili hizo za kushitakiwa kuwa  anahusika…?’ akauliza

‘Hapana , lakini kuna tetesi kuwa itafanyika hivyo,…’nikasema

‘Ili mimi niingilie kati, ni lazima kuwe na mashitaka, mimi nakushauri hivi, kama anataka kuongea na wewe usimkatalie kama una nafasi, kama huna nafasi, haina haja kabisa kusumbuka naye..’akasema

‘Wasiwasi wangu ni kuwa anaweza kumtumia mume wangu kama kitega uchumi, na hali aliyo nayo mume wangu akitaka pesa, nitafanyeje…na docta kasema hali aliyo nayo sitakiwi kumkwaza..sasa je akimuendea mume wangu kwa kumrubuni itakuwaje..na..?’ nikauliza na kabla sijaendelea wakili akasema

‘Kwani ni nani huyo…?’ akauliza na nikamtajia, kuwa ni mlinzi kwenye jengo alilofarikia makabrasha, na nikamtaja jina lake

‘Huyo mtu ni hatari…yeye ndiye anashukiwa kama mtumiwaji wa Makabrasha, aliwahi kuwa mtu wa usalama akafukuzwa, akaenda kuajiriwa nchi ya jirani na huko nako akafukuzwa, na hata kufukuzwa kwake hakupo wazi sana kuhusu kosa lake, ila walisema kwa usalama wa kikazi…inatilia mashaka, ni mjanja sana…’akasema

‘Sasa nifanyeje…?’ nikauliza

‘Natamani sana kukutana na huyo mtu kwenye uwanja huo wa sheria, nione huo ujanja wake …’akasema wakili

‘Kwanini…?’ nikauliza

‘Watu wakorofi kama hao wananipa changamoto kwenye kazi yangu, sasa wewe subiria, akikupigia simu tena, fanya kama nilivyokuelekeza nitakuwa hewani, nikiona alama ya kuwa mpo naye, sawa..mengine yatafuata kuanzia hapo…’akasema

************

 Basi siku hiyo ikawa inakwenda salama, na kabla sijajipanga kwenda  kumtembelea mume wangu hospitalini,  mara simu yangu ikaita,…nilipoangalia nikaona hakuna jina au namba (anonymous) ..ina maana muitaji ni mtu asioyefahamika.

Kwa haraka nikaweka simu yangu kwenye kurekodi, mazungumzo, na kuiweka hewani

‘Nipitie Maringo hoteli, ukienda kumuona mgonjwa, nitakusubiria nje ya hoteli….’akakata simu.

‘Kajuaje kuwa nakwenda hospitalini…?’ nikajiuliza

 Kwa kukisia tu anaweza akawa ndio huyo jamaa, lakini sikuwa na uhakika, na nisingeliweza kumpigia simu maana namba ya simu haisomi..nikawaza kiusalama nifanye nini.

‘Docta, nakwenda kmuona mgonjwa, je tunaweza kuongozana..?’ nikampigia docta jirani yangu

‘Mimi nipo hospitalini kwangu, kama ni muhimu kuja huko nitakuja…’akasema

‘Basi hamna shida..’nikasema,

Huyo mtu ni hatari…yeye ndiye anashukiwa kama mtumiwaji wa Makabrasha, aliwahi kuwa mtu wa usalama akafukuzwa…, ni mjanja sana…’nikakumbuka maneno ya wakili akimuelezea huyo mtu

‘Hata kama ni mjanja mimi ni mjanja zaidi yake…’ nikasema kimoyo moyo, kwanza nikaegesha laptop yangu ambayo ipo nyumbani, ambayo inatumia waya za hewani, iwe na mawasiliano na simu zangu za mikononi, na chombo kingine nitakachokuwa nacho,..kwahiyo nikiwa naongea na huyo jamaa, tukio hilo litachukuliwa moja kwa moja kwenye laptop yangu, japokuwa ipo nyumani…,

Nikaseti nywele zangu na kuchukua kibanio maalumu, na kuzibana nywele zangu, hicho kibanio, sio cha kawaida….

Pia nikachukua simu zangu mbili zote zinauwezo wa kuchukua matukio ya sauti zikiwa na chaji ya kutosha, na kwenye begi langu nikaweka kitufe kingine chenye kazi hizo-hizo…hicho huwezi kukibaini kwani kinalengeshwa kwenye mkanda wa hilo begi..…

Nikatoka nyumbani na kuingie kwenye gari langu…kuelekea hospitalini, lakini nikikumbuka kuwa natakiwa kupitia Maringo hoteli, ili kukutana na jamaa huyo mwenye ushahidi na wakati nipo kati kati ya bara bara, nikapigiwa simu

‘Nani mwenzangu…?’ nikauliza

‘Mimi ni wakili wa familia ya Makabrasha..’ akasema

‘Unataka nini..?’ nikauliza

‘Kijana wa marehemu kanipigia simu, kuwa anataka kuonana na wewe na mimi nikiwepo, ana mambo muhimu ya kifamilia, …na kwa vile mume wako anaumwa, anataka wewe uwajibike nayo, kwani muda wa kuwakilisha mirathi unakaribia…’akasema

‘Siwezi kuliongelea hilo, kwa vile mambo yote alikuwa akiyashughulikia mume wangu, na yeye kutokana na hali yake hawezi kuongea kisheria ikakubalika..’nikasema

‘Katoka kuongea na mgonjwa muda mfupi uliopita, na mgonjwa kasema kutoa na hali yake kuwa mbaya, anashindwa kufanya lolote, lakini kwa vile wewe upo, basi unaweza kuongea naye…’akasema

‘Kaongea na mgonjwa, ni nani kamruhusu kuongea na mgonjwa,…?’ nikauliza

‘Mgonjwa mwenye ndiye alishinikiza kuwa anataka kuongea na huyo jamaa, sijui ilitokeaje mpaka ikafikia hapo…’akasema

‘Madocta wana akili kweli..’nikasema kwa hasira

‘Ilibidi, huwezi kuwalaumu madocta, unajua mume wako akitaka kitu hataki kukataliwa, na kwa hali aliyokuwa nayo haikuwa na jinsi…lakini waliongea kwa amani tu.., hata madocta wanasema baada ya huyo jamaa kuongea na mgonjwa,  imesaidia sana, kwani hata shinikizo la damu limetulia…’akasema

‘Sawa nimekusikia..’nikasema hivyo tu nikijua hapo kuna jambo linatengenezwa

‘Tatizo jingine polisi wanataka kuongea naye…na mimi nimewazuia..’akasema

‘Kuongea na nani..?’ nikauliza

‘Na mgonjwa…’akasema

‘Kuhusu nini tena…?’ nikauliza sasa nikianza kuhisi kichwa kikiniuma

‘Kuhusu mauaji ya Makabrsha…’akasema

‘Kwani mume wangu anahusika nini na hayo mauji..?’ nikauliza

‘Wanadai wana ushahidi mkubwa wa kuonyesha hilo, kuwa mume wako anahusika…’akasema

‘Wameupatia wapi huo ushahidi..?’ nikauliza

‘Mimi sijui..ila wanasema wanao huo ushahid na sasa wanahangaika kutafuta mashahidi wa kutosha, na wana uhakika safari hii ni lazima huyo muuaji atahukumiwa kwa kosa la kuua, kuna shahidi mmoja tu bado hawajampata nasika yeye, alimuona muuji kabisa..’akasema

‘Ni nani huyo, shahidi…?’ nikauliza kwa hamasa

‘Sijui..nasikia hata mtoto wa marehem kaniambia anamtafuta huyo shahidi ili haki itendeke, kasema atashirikiana na polisi kuhakikisha huyo mtu kapatikana..’akasema

‘Hujanitajia huyo mtu…’nikasema

‘Watu wanahisi labda ni mmojawapoo wa walinzi, kuna mlinzi mmoja kachukua likizo, hapatikani, hayupo yumbani kwake, wanahisi labda kasifiri kijijini kwako, polisi wanamtafuta…’akasema

 Hapo nikakata simu...kwani kuna simu nyingine ilikuwa inataka kuingia…ilikuwa ya mpelelezi anayeshughulikia kesi ya mauaji ya Makabrasha…


WAZO LA LEO: Anayepitia uchungu ndiye anayeweza kuhadithia uchungu huo ulivyo;
Ni mimi: emu-three

No comments :