Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Saturday, January 13, 2018

MKUKI KWA NGURUWE-57



Ilikuwa ni muda wa usiku, nahisi ilikuwa ni saa sita na nusu hivi, kwani niliangalia saa ya ukutani, tatizo, siwezi hata kugeuza kichwa, lakini niliona ni saa sita, mshale unaonyesha hivyo.

Cha ajabu mwili hauna nguvu, na pumzi ilikuwa ndogo sana, nipo wapi hapa, ni jela au ni chumba gani hiki hakina hewa…nikajiuliza, nikijaribu kugeuza kichwa siwezi, lakini naona, kwa hisia

Mara ghafla mishughuliko, kama kuna kugombea jambo..sijatahamaki mara mkono ukanishika shingoni, unanikaba, na mwingine , na mwingine..ikawa inakuja mikono mingi kunikaba, lakini simuoni mtu ila nahisi ni mikono ya watu inanikaba kila nilipojaribu kugeuza kichwa au kujitetea, sikuweza, mwili ulikuwa haukubali ilikuwa kama mtu aliyenyweshwa madawa ya kulevya au nusu kaputi.

Akili ilikuwa inaona, au nahisi hivyo, kuwa kuna mikono mingi inanikaba, tena ya kiume..na pia  ya kike, ni nani hao, wanataka kuniua,..wote walikuwa wamenishikilia na kila mmoja akiapiza kivyake, kuwa ananiua kwa vile..hiki na kile, na sauti hazisikiki vyema, ila sasa mmoja ndio akasema

‘Nataka ufe kwa vile unakuwa kikwazo kwetu…ila tunakupenda, na kukupenda huko, ili usihangaike ni bora ufe tu…’ilikuwa suti ya kike, iliyochanganyikana na sauti ya kiume kama wanaongea kwa pamoja.

Mikono hiyo mingi iliendelea kunikaba, na mara kwa mbali, nikamuona mtu…anakuja taratibu, akatabasamu, na kusema;

‘Nilikuambia mimi ndiye rafiki yako wa ukweli, sasa nikuokoe au nikucha wakuue..?’ akauliza hivyo, na mimi nikawa najitahidi kujiokoa, sitaki huyo mdada aniokoe namuona kama mnafiki kwangu ,ananihadaa tu, ananivunga, nikawa nataka nijiokoe kivyangu,..hapo sasa pumzi ndio kama inishia, sasa nataka kukata roho.

Yule mtu, ni mdada, lakini mrefu..akaniuliza tena..tena,

 'Hutaki, nikuokoe unajua wewe ni rafiki yangu, nakupenda sana,na kila kitu nafanya kwa ushauri wako,wewe ndiye ulinijenga, akili yangu ikawa inakuwaza wewe, usemacho kwangu ni kama askari anayepewa amri,..ua, naua, kamata , nakamata , sasa iweje…sasa niambie nikuokoe au niache ufe..'

‘Mna-na-fiki wewe…’nikajaribu kusema hivyo, kinafsi niliweza, lakin mdomoni siwezi hata kufunua mdomo mkavu,..kwa sababu ya kukabwa, ulimi umetoke nje...na Yule mdada, akainua mikono, kama vile na yeye anataka kunikab au kunikoa, mimi nakataa, sitaki afanye anachotaka kukifanya,…,

 Ni wakati huo nimeshakata tamaa, namuomba mungu anisamehe makosa yangu ili nife kwa amani,…sasa sina uwezo tena hata wa kuongea, kauli imeshakata,..mara kikaja kitu kama mwanga, kikanipiga usoni, nikashituka,...nipo wapi, .. ooh, kumbe ilikuwa ni ndoto.

‘Ndoto mbaya hii…ooh..’nikasema sasa nikijaribu kuweka fikira zangu vizuri, mwanga ulikuwa ukitokea dirishani,ni mwanga wa taa za nje...!

Jasho lilikuwa linanitoka, haraka nikainua mikono yangu na kushika shingo, sikuona dalili yoyote ya maumivu, ya kukabwa,..na nikageuka huku na huku kunyosha shingo, sikuhisi kuumia, na wakati huo macho bado mazito kufunguka, naogopa nitayaona haya majitu.

Baadae nikafungua macho…nipo chumbani kwangu , kitandani,…hapo nikajitahidi na kujiinua kidogo, nikajikuta nipo sawa, nikajinyosha, halafu nikageukia ubavu wa pili, upande ule aliolala mume wangu,

Hakuna mtu!!

Mume wangu hayupo kitandani, na nina uhakika alikuja usiku ule tukalala naye, japokuwa alikuwa kalewa, sikuweza kumkatalia, kwa ile hali, lakini awali sikuweza kupata usingizi hadi niliposikia anakoroma kuashiria kuwa kalala, na ndipo usingizi ukanishika,, sasa mume wangu hayupo kitandani

‘Labda katoka kidogo,..’nikajipa matumaini

Usiku ule walipofika na mdogo wake, niliongea naye kumuuliza hali ya mgonjwa, maana ni mgonjwa sasa, ..

‘Shemeji yupo safi tu, ila anaongea sana…’akaniambia

‘Sawa sasa ni usiku sana, ila kesho kama nilivyokuambia,huyu ni wa hospitalini…’nikasema

‘Amekataa, anasema yeye haumwi, sijui tutafanyaje…’akasema

‘Basi nitamuita rafiki yake docta, aone atatusaidiaje, ila kwasasa ukalale naye..’nikasema

‘Hapana, shemeji,..kasema anataka kulala na wewe kwa vile wewe ni mke wake, nilimuambia hilo wakati tunakuja, kakataa katakata…kasema ukimkitaa, atakufanya kitu ambacho hutamsahau…’akasema

‘Atanifanya nini..?’ nikauliza

‘Kasema hivyo tu…’akasema

‘Oh,…sasa akileta vurugu usiki itakuwaje..?’ nikauliza

‘Wewe shemeji usijali, hakikisha simu yako ipo karibu, akifanya fujo, au hali ikiwa mbaya, wewe nibeepu tu, weka namba yangu tayari, na mlango usifunge kwa kubana,…’akasema

 Kwahiyo tukaishia hapo, na kweli nilifika na kumkuta mume wangu ameshatangulia kitandani, na sasa kalala…

 ‘Sasa kaenda wapi huyu mtu..?’ nikajiuliza hali ya ndani kulikuwa kimia kabisa, husikii kitu …nikakaa kimiya kidogo, nikisubiria huenda kweli katoka kujisaidia, lakini hakutokea kabisa, moyoni nikahisi ni yale yale, nilikuwa nikiogopa, na nikikumbuka hiyo ndoto ndio nikawa na mashaka kabisa

Uzuri watoto walikuwa hawapo, wapo shule za bweni, kwahiyo upande huo nilikuwa na amani nako, sasa ni mimi na mume…na shemeji yupo chumba kingine.

‘Uwe makin na huyo mtu, hata ukilala usilale kupitiliza…’nikakumbuka ushauri wa docta rafiki wa mume wangu.
Nilipokumbuka hilo kwa haraka, akili ikanijia, nikaona nifanye jambo , jambo ambalo niliwahi kuliona kwenye sinema, lilinijia hilo wazo tu. Taa ya ndani ilikuwa inawaka, lakini sio ile ya mwanga mkali, huwa sipendi kulala na giza,

Kwa haraka nikaamua nifanye hivyo, sijui kwanini niliamua kufany ahivyo, ila nilifanya hivyo tu, sijui…

Kwa haraka nikachukua mto wangu wa kulalia,na mashuka ya akiba nikayaweka pale nilipokuwa nimelala, nikayafunika kama mimi niliyelala, na mimi mwenyewe nikatafuta sehemu ya kujibanza, nikajaribisha na kuona ninaweza kujibanza hapo bila ya yoyote kuniona.

‘Najihami tu…’nikasema hivyo.

Nilikaa pale kwa muda bila kuona mtu akitokea, nikawa najiuliza je ni kweli ninavyowaza au ni wasiwasi tu.

‘Ngoja kwanza nikahikishe labda jamaa kaenda kulala chumba cha maongezi,..’nikajisema moyoni, kwahiyo taratibu nikafungua mlango na kuchungulia huko…hakuna mtu…nikasikia kitu kama kimegonga, kwa haraka nikarudi kwenye maficho yangu na kutulia, kukapita muda, hakuna mtu aliyetokea


Nikakumbuka jambo,…kila kitu kinahitajia ushahidi au sio, ngoja niweke ushahidi kama kuna lolote laweza kutokea.

Kuna video, niliyokuwa nimeweka chumbani, ni katika kutafuta ushahidi tu, lakini baade niliizima, ni videi inayochukua matukio…nikasogea kwenye lattop yangu nikaisha na kuiweka hai, ili ichukue matukio yote humo ndani.


Mara nilisikia kitu kimegonga upande ule wa makitaba, ...oh, kumbe mume wangu yupo huko, huenda aliamua kwenda kupoteza muda, nikataka kwenda huko, lakini nikaona ngoja nitulie kama dakika tano hivi, huenda kuna kitu anakitafuta, nikasikiliza lakini sikusikia tena…nikatoka mafichoni, na sasa nataka kwenda huko maktaba

Mara ....nikasikia kama mchakato, wa mtu kutembea, na niliposikia hivyo, nikakimbilia ile sehemu yangu ya maficho. Huwezi jua, huenda ana lake jambo ngoja nione anataka kufanya nini.

Nikawa najiuliza kama mume wangu alikwenda tu kupoteza muda, ...akaja akaikuta ile hali, anaweza kuniona simwamini...hapana nitamtania tu  kuwa nilikuwa namfanyia mzaha. Nikatulia, huku nikiwazia mataayrisho ya kesho kuwa kesho ni lazima nimtafute fundi, abadili vitasa vyote vya makabati, na hata ikibidi nyumba nzima, maana hakuaminiki tena...

‘Bastola...’ oh nilipokumbuka hivyo mwili mnzima ukazizima, woga!!

‘Mungu wangu , kwanini sikuiondoa pale…’nikajilaumu

 Hapo moyo wangu ukawa unanienda mbio, sijui kwanini nilisahau, kwani nilipanga, kuja kuiondoa ile bastola kwenye kabati na kuificha sehemu nyingine, lakini kutokana na mishughuliko, na hayo mambo ya kufuatilia, nikawa nimesahau kabisa,

Nakumbuka mume wangu walipoondoka na mdogo wake hawakuchukua muda, walirudi, wakiwa wanaongea kwa furaha, na nilipopata muda wa kuongea na shemeji yangu, yeye alisema kaka yake muda wote walikuwa akiongea kwa furaha, hakukuonekana tatizo lolote...

**********
‘Inabidi kujihami tu...’nikasema kujipa moyo nikiwa bado mafichoni

 Kila hatua nilihis nipo hatarini, na kila nikitaka kumbipu shemeji, nahis kama nitaonekana muoga, simuamini mume wangu, basi nikaona niache tu, nione kwanza mwisho wake ni nini

Muda ukawa umepita sikuona dalili za mume wangu kutokea.

‘Au kaenda kulala na shemeji au kule kwenye chumba chake kingine…anapolala akiwa kalewa…’nikasema hivyo kimoyo moyo

Nilipoona muda unakwenda nikataka kutoka na kumfuata mume wangu huko huko kama ni chumbani kwake au kwenye maktaba yetu,  na mara mlango wa maktaba ukafungulia!

Mume wangu akajitokeza…akiwa na pajama la kulalia, mkononi kashika kitu,

Kwanza sikuweza kukiona hicho kitu alichokishikilia, kwa jinsi alivyokishikilia usingeliweza kuona na pale nilipo ikawa siwezi kujisogeza,  na kwa vile nilikuwa nimesimama kwa muda, mwigi kwenye shemu ndogo, miguu ilishaanza kuuma, lakini hata hivyo niliogopa kijitikisa sikutaka mume wangu ajue kuwa nipo pale.

Mume wangu akawa anakuja ule muelekeo wa kitanda, alikuwa akitembea mwendo ule wa kunyata,yaani utafikiri ule mwendo wa kwenye picha wa kunyata, taratibu, na kila hatua ilikuwa kama mtembeaji anahakikisha kuwa mguu umefika pale alipopataka,..akasogea hadi karibu na kitanda, na hapo nikaona kashikilia nini,...moyo ulinilipuka, nikawa nahisi kuishiwa nguvu..

Yale yale niliyokuwa nikiwaza, na hapo nikazidi kujilaumu,  kwanini sikufanya kama nilivyoambiwa, haya mambo ya kuzarau, sasa naona matokeao yake ...huwa kila anachoniambia rafiki wa mume wangu nimekuwa na tabia ya kukizarau, na nimejikuta nikipatwa na matatizo na baadaye ndio najiona nimefanya makosa, ni aheri ningelimsikiliza ushauri wake.

 Tatizo huyu rafiki wa mume wangu, ni mtu anayejitahidi sana kunisaidia, japokuwa ni mume wa mtu, lakini bado anaonyesha ile hali ya kunipenda, hata wakati mwingine najisikia vibaya kutokana na matendo yake. Na kuna wakati anajisahau kabisa kuwa yeye ni mume wa mtu na anataka kufanya yale tuliyokuwa tukifanya tukiwa wapenzi, kwakweli kwa hilo sikutaka upuuzi huo.

 Sasa kupuuzia yale anayonishauri matokea yake ndio haya...

Wakati huo mume wangu alikuwa ameshafika eneo la kitandani na hapo akainua kile alichokishikilia na sasa kikawa kinaonekana dhahiri,

Bastola…!!

Sasa akawa kaishikilia bara bara, japokuwa mikono yake inakuwa kama inatetemeka,..sasa anailenga ile bastola pale nilipokuwa nimelala, niliona mikono yake ikitetemeka, sijui kwanini

Kwa haraka nikamchunguza kwenye macho yake, awali alipokuwa kasimama nisingeliweza kuyaona vyema, kwani mwanga wa taa ya ndani ulikuwa ni hafifu, ila aliposogea karibu na kitanda pale aliposomama sasa ndio nikamuona na ni kutokana na mwanga wa taa nje.

Taa ya nje ilinipatia nafasi ya kumchunguza vyema machoni alikuwa kafungua macho, ila ukiangalia kwa makini macho yake yalikuwa meupe,...sio ya kawaida, nikakumbuka zile hadithi za watu wanaofanya kazi wakiwa usingizini,..

Kweli mume wangu hapo hayupo sawa, na ilivyo, hutakiwi kumshitua, ..unaweza ukamsababishia mshituko wa moyo, na hata kusababisha kifo, kwahiyo nikatulia kimiya, nione ni jambo gani anataka kulifanya,..

**************

 Mume wangu hajui kutumia vyema bastola, niliwahi kumfundisha lakini hakupenda kabisa kuitumia, nahisi ndio maana mikono yake ilikuwa ikitetemeka,..ila nilimfundisha jinsi gani ya kuweka risasi na kutoa, kwahiyo yawezekana atakuwa keshaweka risasi kabisa kwenye hiyo

‘Hii imepangwa itokee, ili iwe fundisho kwangu...’nikasema kimoyo moyo.

‘Jembe njoo huku...’sauti ikatoka mdomono kwa mume wangu, ilikuwa kama ya kuwewesa..na anaongea kama mtu aliyelewa hivi.

Huyo jembe ni nani..?’ nikajiuliza, nikakumbuka ..jembe ni mdogo wake, lakini hapo hayupo, mbona anamuita kama vile yupo naye karibu.

‘Jembe, ..nakutegemea wewe....lakini hili ngoja nilifanye mimi mwenyewe, sitaki wewe uje kuingia matatani, na kama unaogopa ondoka....’ikatoka ile sauti, ni kama ya wale wanywa  madawa ya kulevya. Niliweza kuisikia kwa shida, hapa nikuelezea kwa vile nilivyoelewa, lakini alivyokuwa akiongea ni maneno ya kutafuta.

‘Na-na-taka ku-ku-limaliza hi-li ka-ka-bisa, tuwe huru...’akasema huku akisogeza ile bastola palen nilipoweka mto, na kama angegusa kwa mkono angeligundua kuwa hakuna mtu, lakini nikamuona akisogea nyuma, akapiga magoti.

‘Oh, Jembe nisaidie jamani.. , nashindwa kufanya hili....nashindwa kumaliza hii kazi, namuonea huruma, lakini jembe , nisipofanya hivi tutakosa kial kitu,...kazi yangu yote na juhudi zangu zote zitapotea bure, mtaishije, nitaishije,..nirudi kuwa masikini hapana, sikubali, ni bora nimfuate Makabrasha, ....’akatulia.

‘Unasikia eti, wana-se-sema  Makabrasha ka-fa…yu-le, afe…hapana, kama ni hivyo, basi hata mimi nataka kumfuata huko huko…najua hata mimi ndio njia yangu…nitakufa, lakini abla ya kifo changu, nataka niachie familia yangu jambo la kunikumbuka.

‘Sitaki ubaguzi..ooh, mtoto wan je..nani kasema hayo..sasa ili huyo mtoto wa nje naye atahaminiwe, basi nataka huyu kizuizi aondoke,… Jembeeh, unanisikia,..sasa nisaidie tumalize hii kazi, mbona husogei, sogea huku...mkono hauna nguvu kuvuta hiki kiwashio…traigaaaaa..’akasema.

‘Oh, wewe sasa unaogopa eeh,,..ngoja mimi nimalize hii kazi mwenyewe, maana wiki imeshapita, kinachofuata hapo ni nini....ni mkataba wa zamani, ukipatikana huo, mimi sina changu, hivi huo mkataba wa zamni ni upi,...ananishangaza kweli, kweli mke wangu kachanganyikiwa, mimi siujui huo..sija—labda makarasha atanisaidia, mimi sijui....’akatulia

‘Sikiliza jembe, tusipolimaliza hili, tutakosa kila kitu, tukilimazlia hili, tutakuwa huru, na mimi nitamfuata Makabrasha, nimekutana naye, kasema huko alipo kuna amani…yupo wapi huyu mtu…’akatulia

‘Ananiita, unasikia, suti yake hiyo, ananiita…hahahah..ngoja nimalize hii kazi, anasma nimalize hii kazi halafu nimfuate huko alipo…’akatulia kama anasiliza

‘Mke nakupenda lakini …wewe ni kikwazo..bora nije kuishi na huyo mwingine, hana shida,..kwanza …anadai yeye ndiye kanizalia dume, hivi ni kweli eeh, yawezekana ni yeye,..hahaha, kanizalia dume, kama ni kweli, basi kweli ananipenda, tofauti na wewe mke wangu ambaye anaogoma kunizalia dume..Tatizo wewe mke wangu,..unathamini tu mali, wazazi wako, familia yako..na kunifanya mimi bweeege.’akasema

Pale nilipokuwa  nimejificha, nilihisi hasira, nikahisi nijitokeze nikafanye lolote , lakini mwili ulikuwa kama umekufa ganzi, nikabakia kuumia ndani kwa ndani, kumbe....kumbe, ni kweli mume wangu ana mwanamke mwingine nje na huyo mwanamke anampenda kuliko mimi, sasa ni nani,…ni..ni…hapana mbona hamtaji!

‘Ni mwanamke gani huyo…?’ nikajiuliza

‘Tatizo mwanamke wewe unayenipenda sikuoni…upo wapi…ni nani wewe..mbona inakuwa kama jinamizi, nashindwa ku-kumbuka, ni nani wewe..nakuwa kama mtu anayempenda shetani, ..jini mahaba, asiyeonekana, umekwenda wapi wewe…je ni kweli ni wewe ulinizalia jembe…’akatulia

‘Ni kweli maana ni kwanini mke wangu alitaka kumtupa mtoto ..kwa vile hana uchungu naye..yaah, nimegundua, mke angu hanipendi, kama hampendi mtoto wangu hata mimi hanipendi, sasa nakuua…ufe,..ufeee...na hii silaha yako…na mimi,…hahaha’

‘Sasa jembe mimi namaliza kazi, nikimaliza kazi, kinachofuata tukamtafute mtoto wetu, ...tutakuwa na jembe jingine, dume la kazi....ukiwa na jembe ndani ya familia raha, watoto wote nawapenda, lakini wa kike watapendwa na wengine zaidi, watachukuliwa, nitabakia na nani sasa....mungu kanisaidia nimepata mtoto wa kiume, eti nimuachie hivi hivi..hapana, ni lazima ..ni lazima, tukamchukue, sasa jembe mimi namaliza kazi ..

‘Wewe sihutaki kunisaidia eeh ...mimi naifanya hii kazi peke yangu, wewe ....unisaidie jambo moja, nikikamatwa, unilelee watoto, nikifa, halikadhalika, nakuachia kila kitu kikiwa sawa,...hata nikifungwa, wewe chukua jahazi, najua kwa sasa kila kitu kipo makini, ahsante Makabrasha, nakuja nisubirie, nakujaa.....’akasema

Akasogea karibu kabisa sasa na pale nilipoweka kanyaboya akaelekeza ile bastola kwenye mto, akaisogeza karibu sana, na kusema;

‘Samahani sana mke wangu ...nalifanya hili kwa vile sina namna nyingine, na nikimaliza hili na mimi nikiona vipi nitajimaliza mwenyewe, kwa manufaa ya familia…’akawa sasa anakaza kidole cha kuvuta kiwambo cha bastola

‘Najua..nitapatilizwa na kusakamwa sana..lakini kama wanavyodai wamemfanya hivyo Makabrasha, kwanini hililisifanyike , na kuna shida gani maana kila kitu sasa kipo makini, kila kitu kipo makini au sio best Makabrasha, nakushukuru sana...’akasema na kuisogeza bastola karibu kabisa na mto....

‘Kila kitu kipo makini....’akawa anayarudi hayo maneno mara kwa mara sasa, nikawa najiuliza hayo maneno yana maana gani, kwanini ameyependa kuyarudia, amejihakikishia vipi kuwa kila kitu kipo makini, nikawa najiuliza huku nikimwangalia mume wangu, nikiwa pale nimejibanza,

‘Makabrasha kafa…nani kasema kafa, wehuu nyie…, basi kama kafa nimemuua mimi, mwenyewe, hivi hivi….hahahha. Kama nimemuua rafiki yangu aliyenithamini, kwanini nishindwe kukua, wewe…hahahaha, kwaheri…

Mara mlio ukasikika, ...mlio ulitetemesha ndani,....na mlio ule ulimshitua hata huyo aliyeusababisha, na yeye akadondoka chini, na mimi pale nilipokuwa ilikuwa kama mtu kaniziba masikio ghafla,.

Hata hivyo nikajitahidi, maana ni lazima nifanya jambo, kwani huenda mlio huu umesikika hadi huko nje, itakuwa ni kashifa,...nikatoka pale nilipokuwa nimejificha, na kwa haraka nikaenda pale alipodondokea mume wangu, alikuwa amedondoka sakafuni, sasa kalala, ..ametulia....anahema kwa mbali, na sauti kama ya  kukoroma, ya kuashiria kuwa mtu yupo kwenye usingizi,...

Nikaiangalai ile bastola ipo wapi ilikuwa imemtoka mkononi na kudondokea kitandani, na hapo nilitaka kuichukua lakini nikatulia, kwani nilisikia mlangoni ukigongwa.

‘Shemeji kuna nini huko....’alikuwa mdogo wa mume wangu, na mara simu ikaanza kuita….

NB: Kwa leo naishia hapa, naogopa na kuogopa,

WAZO LA LEO:  Tuwe ni wenye kuhurumiana, na kusaidia, hasa pale tunaposikia kuwa mwenzako yupo kwenye mitihani ya maisha huo ndio upendo wa kweli. Mitihani ya maisha ipo mingi, lakini mtihani wa maradhi ni mgumu sana, kwa mgonjwa mwenyewe na muugazaji, Ni wangapi wanakuwa wepesi kusaidia mtu akiumwa, ni vigumu sana kuwaona,..lakini mtu huyo huyo akisikia mwingine kafa, hata kama ni nauli atakopa,..najiuliza tu, je twawapenda watu wakiwa maiti zaidi ya wakiwa wagonjwa! Najiuliza sana sana hili. Tupo pamoja..


Ni mimi: emu-three

No comments :