‘Na je mume wangu ana taarifa?’ nikauliza.
‘Sina uhakika na hilo, sijaongea na mume
wako bado, ..’akasema.
‘Wakili wako atakuwa keshafika, mtaonana naye leo hii hii…
Alikuwa docta rafiki wa mume wangu , na
baada ya hapo akaondoka, na mimi nikawa mikononi mwa askari wa Magereza…
Tuendelee na kisa chetu….
*************
Nikaingia jela, na kuonyeshwa hiyo sehemu niliyoambiwa ni ya
usalama zaidi na kuahidiwa kuwa hapo sitasumbuliwa na kitu chochote…
‘Nataka nionane na wakili wangu haraka iwezekanavyo…’nikasema
‘Akija utaonana naye hakuna shida, lakini hata akija dhamana sio
rahisi kupatikana kutokana na kosa lenyewe..’nikaambiwa.
‘Dhamani ni haki yangu, sina kosa, hata nyie mnalifahamu hilo,
mnafahamu kabisa mimi sijaua, mnachofanya ni kunizalilisha tu mimi, hamjui na
nyie ipo siku mtazalilishwa hivi hivi, …’nikasema
‘Sisi hatujui hayo, hapa kazi yetu nikuhakikisha tumekupokea kama
mfungwa, mengine hayatuhusu, muhimu tii sheria za hapa, kuna kitu kingine
unahitaji,..maana tumeambiwa tuhakikishe upo salama, na nakuhakikishia hutapata
tatizo lolote hapa,.. …’akasema askari mmoja.
‘Sihitaji kitu…’nikasema na mlango ukafungwa nikabakia peke yangu.
*******
Nilibakia mle ndani, kiukweli niliwekwa mbali na wafungwa
wengine,lakini hakukuwa na amani, akili iliteseka, na unawaza mambo ambayo
hayana mtu wa kukusaidia, huna vitendea kazi, huna simu…inabakia kuwaza tu.
Hata hivyo, niliona sina jinsi, nikubali ukweli kuwa sasa nipo
jela, ..je nifanye nini, kwanza nikaanza kuliwazia hili tukio kiundani, nakujiuliza je nimekosea wapi, tatizo ni nini
hasa, ni mimi au ni walimwengu,…au ni mume wangu…na ni kwanini nafikwa na
mitihani hii yote,..nilijiuliza hadi kichwa kinauma, maana awali nilikwuwa
nawaza tu bila mpangilio
‘Ni kwanini wamemuua Makabrasha..?’ hapo nikatulia na kujaribu
kupata usingizi. Hakukuwa na usingizi baadae nikagundua kuwa mtu mwingine
kaletwa upande mwingine wa chumba, naye alikuwa akihangaika kivyake, hakutaka
hata kuniangalia….yeye baadae nikamuona kalala, ni kama mzoefu vile
‘Ni nani kamuua Makabrasha..?’ ilikuwa ndilo swali langu la mara
kwa mara
Huenda haya mauaji yanatokana
na matukio ya nyuma, ...ambayo yameanzia kwa mume wangu, au kwangu, mtu
akayafuatilia na baadae akaona huu ndio muda muafaka wa kulifany ahilo , ili
kuichafua familia yangu, sasa ni nani huyo
‘Ni adui zake…’ ndivyo polisi wanavyoamini hivyo, na adui za
Makabrasha wanavyoona polis kwa ushahidi ni mimi….
‘Kwa mume wangu haiwezekani kwa maana kuwa Makabrasha alikuwa rafiki ya mume wangu, na
ndiye anamtumia kufanikisha malengo yake, kama hiyo mikataba na…hapana kwa mume
wangu haiwezekani, kwanza mtu mwenyewe yupo hospitalin, na sizani kama ana watu
anaoweza kuwatumia, pesa ya kufanya hivyo ataipatia wapi..’nikawa naongea kwa
kimoyo moyo.
‘Je ni mambo ya kisiasa…’nikasema na kuinua kichwa, nikagundua
kuwa yule mtu mwingine alikuwa kalala, lakini sasa anakuwa kama ananichunguza
kinamna fulani, sikumjali,…nikaendelea kuwaza.
Kutokana na maelezo ya rafiki yangu hili jambo limekwenda zaidi na
kuingiza siasa ndani yake, kwahiyo haya yanaweza yakawa yamepangwa kisiasa,
lakin kwa vipi, ili iweje, wakati huyo ni mtu wao muhimu sana, hapana kwa
upande huo sizani kama wanaweza kumuaa, sasa ni nani...
‘Huyu Makabrasha kama anatumiwa, na hao wanasiasa ni kwanini wamuue…?’
nikajiukuta nimeongea kwa sauti mpaka nikajishutikia, na niligundua yule mtu
mwingine upande ule alikuwa kama ananisikiliza
Nikamzarau na sasa nikawa makini ili nisiongee kwa sauti, ..jamani
ukiwa mahali kama hapo, unakuwa kama umechanganyikiwa fulani hivi, usiombe
kukaa sehemu kama hizo, hakuna mawasiliano na wanadamu wenzako.
‘Mkataba…eeh’ nikasema na kukuna
‘Kuna huo mkataba wa pili, wa huyu rafiki yangu aliotakiwa yeye kuweka
sahihi, je huo mkataba ulikuwa malengo gani, kwanini uwe wa kulazimishana,...ili
iweje, kwa manufaa ya nani, kama ni Kwa Makabrasha kwanini wakamuua, na kama
Makabrasha alikuwa jembe la wanasiasa kwanini wamuue…hapa ina maana gani,
..kuwa aliyemuua Makabrasha sio hao wanasiasa, ni watu ambao hawana umuhimu
naye sasa ni akina nani’
‘Hapo ndio wewe unaingia..na kushukiwa kuwa huenda ndio wewe
ulifanya mauaji hayo…’ nilikumbuka kauli ya docta rafiki wa mume wangu.
‘Hapa kwa vyovyote iwavyo, rafiki yangu anafahamu mengi
yanayohusiana na huu mkataba,..namfahamu ni mjanja sana, atakuwa keshafahamu
kitu, …na huenda na yeye ni muhusika mkuu, na anaweza akafahamu lolote
kuhusiana na huyo mtu aliyekuwa akiongea na Makabrasha, na huyo mtu ndiye
muuaji, sasa ni nani huyo…’nikawaza kimia kimia.
‘Rafiki yako hahusiki kwa vile aliondoka kwa Makabrasha..akatoweka,
ushahid upo kuwa alikuwa uwanjani kajificha,…mmh, kajificha wapi…
‘Hayo mauaji yalifanywa
baada ya yeye kuondoka kwahiyo yeye hahusiki kwa hayo mauaji, labda awe katuma
watu wake waje kufanya hivyo...na watu wake ni akina nani,...watu wake wengi
nawafahamu,...nitaongea nao,....lakini kwa vipi ...hapa si mpaka mimi nitoke
humu, lini... na muda ni muhimu sana...’nikajikuna kichwa huku nikiwaza.
Nikasimama, na kujinyosha, niliona yule jamaa kule akijiinua
kuniangalia, mimi sikumjali..nilijinyosha nikachukua mazoezi kidogo, ilimradi
mwili ufanye kazi, hadi nikachoka na kujilaza.
‘Ni nani mwingine anaweza kuhusika, labda docta, rafiki wa mume
wangu, lakini kwa nini ahusike, ana nini na huyo mtu, hapana, huyu haweze
kabisa, ..sasa ni nani….mhhh, ?’
nikajiuliza bila majibu.
Kichwa sasa kimechoka kuwaza, nitaka kama nipate dawa ya usingizi,
nitaipataje, maana kwa hali kama hii nitawehuka…nikasimama, nikakaa, nikasimama
nikaaa..yaani kiukweli akili ilikuwa sio sawa..baadae nikajilaza tena na wakati
nataka kupata usingizi..mara…
Nikasikia nikiitwa, na
kuambiwa wakili wangu ameshafika, na wamemruhusu nikaongee naye kwa muda mfupi
tu, kwani muda wa kuongea na watu wa nje ulishapita ila nimepata upendeleo tu..
Kwa haraka nikasimama na mlango ukafunguliwa, nikatoka hadi sehemu
ya kuongea na wageni, nikamkuta wakili wangu akinisubiria, na aliponiona tu
akaanza kuongea;.
‘Samahani sana, ilibidi kwanza nihakikishe kuwa mzazi wangu yupo
sehemu stahiki, si nilikuambia anaumwa, kwahiyo kutokana na hili tukio, ikabidi
tubadilishe mipangilio yetu yote,..ikiwemo kumchukua mgonjwa, nije naye huku
Dar, hili halikuwepo kwenye mipangilio yetu.
‘Anaendeleaje..?’ nikamuuliza
‘Ni hivyo hivyo, na uzee nao..lakini uzee sio tija ya kuwa mtu
aumwe, ni maradhi tu, na kwa vile mwili ni mzaifu, madawa yanachukua muda
kufanya kazi yake, tunapambana, huku tukimuomba mungu..’akasema
‘Poleni sana…’nikasema
‘Ilikuwa ni kazi kubwa sana kumshawishi hadi akakubali tuje naye
huku, hakunielewa ni kwanini najali kazi zaidi, hakuelewa umuhimu wa hili
tukio, lakini mwisho wa siku akakubali,
‘Haya...., sasa tuingie kazini, maana nimejitahidi kupitia kwa
watu wote muhimu, kuanzia kwa wale waliokukamata,…mpaka nimefika eneo la tukio…nikaongea
na watu mbali mbali mle kwenye lile jengo, nikaja kuongea na wapelelezi nia ni
kupata picha na hali halisi, na mtizamo wa watu kabla sijafika kwako
....’akasema.
‘Wamekudanganya nini hao watu?’ nikauliza.
‘Kiufupi ni kesi ngumu..’akasema
‘Lakini mimi kiukweli sijaua, siwezi kukuficha hilo…’nikasema
‘Najua, hujaua, polisi bado wanahisi unaweza ukawa umefanya hivyo,
unajua kazi ya polisi ilivyo, ni mpaka wajirizishe, shuku shuku ni moja ya kazi
zao ili kumpata muuaji, na kukushikilia kwako ni njia moja wapo ya kumpata
muuaji,..’akasema
‘Kwanini wanitese mimi,maana huku nikutesena, napata hasara kiasi
gani,..nazalilika, familia yangu inaingie kwenye kashfa, hawalioni hili...’nikasema
‘Ushahidi mkubwa wanao kuwa wewe unaweza kuhusika,...lakini
kinachowachanganya, ni muda wa muaji,..muda ndio imekuwa kikwazo kwao, kukuweka
wewe kuwa mtuhumiwa mkuu…’akasema
‘Wanajua hilo..’nikasema
‘Sasa kutokana na hilo wanakuja kukuona huhusiki moja kwa moja na mauaji
hayo, ila wanafikiria kuwa wewe utakuwa ulimtuma mtu, ayafanye hayo mauaji , na
ulifika hapo kuchukua nyaraka fulani hapo ofisini ndio wakakuwahi…swali kwanini
ujipeleke mwenyewe…’akatulia.
‘Nilijipeleka, mimi nilikuwa sijui lolote ni waongo hao…’nikasema
‘Pili, silaha yako ndiyo iliyotumika kwenye hayo mauaji, japokuwa
hakuna alama zozote za vidole kwenye hiyo silaha, ya kwako au ya mtu mwingine,
silaha haina alama yoyote, na wewe walikukuta umevaa kinga za mikononi.
‘Kwahiyo, swali ni kwanini ulivaa kinga,…na silaha haina alama za
vidole , ina maana ulifany ahivyo makusudi…’akasema
‘Wanasema pia ulipofika ulisema una miadi na marehemu…lakini
kwenye kumbukumbu cha kitabu cha marehemu haupo, yeye ana kitabu cha kumbukumbu
cha watu alitakiwa kukutana nao, hakuna jina lako, na imegundulikana kuwa
ukurasa wa siku hiyo umechanwa, na hawajaona ukurasa huo mahali popote huenda
ingesaidia jambo…’akasema
‘Kwahiyo bada ya kumtafuta muuaji, wanahangaika na mimi au sio…’nikauliza
‘Wanasema kwa wadhifa wako unaweza ukawa uliwatuma watu wako,
ukawapa silaha yako, na huenda kilichokupeleka hapo ni kuharibu ushahidi pamoja
na kuchukua nyaraka ambazo alikuwa nazo Makabrasha, swali ni kwanini uende
mwenyewe wakati..umeagiza mauji yafanyike, na kwanini ukadanganya kuwa ulikuwa
na miadi na huyo mtu, …’akasema
‘Unaona eeh, wao wanajikanyaga tu kutaka kuniharibia jina langu,
kama wanatumiwa basi wataumbuka wenyewe…’nikasema
‘Swali jingine ni kwanini uliwadanganya kuwa ile bastola sio
silaha yako…wakati silaha yako unaifahamu…hapo wakahisi kuna kitu
unawaficha..’akasema
‘Lakini ni kweli, mimi nilikuwa sina uhakika bado, maana silaha
yangu niliicha kabatini…’nikasema
‘Uliposema silaha yako ipo kabatini walikwenda kuhakiki, wakaona
kabati lako limefungwa, hakuna dalili zozote za uvunjwaji, kwa maana huyo mtu
aliyeichukua hiyo silaha yako ana ufungua, ni nani mwingine mwenye ufunguo wa hilo
kabati unapoweka hiyo silaha..?’ akaniuliza.
‘Hakuna mwingine…nakala zote ninazo mimi, mume wangu hakuwa na
haja ya ufunguo wa kabati hilo…’nikasema.
‘Kwahiyo huyo mtu aliyeichukua hiyo silaha yako,ndio huyo huyo,
aliyeweza kuiba mikataba,..yawezekana mtu huyo anafahamu siri zako za ndani,
sasa ni nani huyo, unaona hapo, kwahiyo ni lazima wawe na shaka na wewe..’akasema
‘Kiukweli hata mimi mwenyewe nashindwa kuelewa hapo, ni nani huyo..?’
nikawa kama namuuliza wakili
‘Ndio hapo polis hawataki kukuachia....’akasema wakili.
‘Zaidi ya mume wangu ..hakuna anayejua kuhusu hizo funguo, hata
rafiki zangu hawajui hilo, ..wafanyakazi wa ndani hawafiki huko, huko nafanya
usafi mimi mwenyewe…na mume wangu ni mgonjwa, asingeliweza kulifanya hilo,
japokuwa hajambo lakini bado hajaweza kutembea vyema, na asingeliweza kutoka
hospitalini wasimuone….’nikasema
‘Na hii inafanya jambo hili liwe gumu kidogo, kwani watu
tunaowafahamu waliopo karibu na wewe na wanaoweza kufahamu nyendo zako ni mume
wako, mwingine kwa mbali ni rafiki yako, ambaye yupo mbali sana na tukio
lenyewe, kiushahidi, maana muda wote alikuwa na watu wanaoaminika, mwingine ni
nani unayemuhisi....?’ akaniuliza.
‘Sana sana ni docta, rafiki wa mume wangu, ambaye hawezi kuhusika
kabisa....’nikasema.
‘Kwasasa kila mtu anaweza kuhusika, cha muhimu ni kukusanya
ushahidi, ...lakini kwa sasa, kwa vile nimepewa muda mchache tu, ngoja
nikafuatilie kuhusu dhamana yako kwanza, na kwa hivi sasa unatakiwa kukumbuka
kila kitu, ili tukikutana tena, uniambie kwa uwazi, usinifiche
chochote, ni muhimu sana kwa sasa...’akasema wakili.
‘Nasikia dhamana imekataliwa...ni kweli…?’ nikauliza.
‘Mimi ni wakili wako, kama imekataliwa nitakuambia mimi mwenyewe,
usiwasikilize watu wengine, na kwa tahadhari, usiongee na mtu mwingine yoyote
kwa hayo yaliyotokea, zaidi yangu mimi, unanielewa hapo..tukishirikiana vyema.., hili
litakwisha japokuwa lina ugumu wake kidogo...’akasema na kutaka kuanza kuondoka.
‘Ni ni kweli kuwa haya mambo yamekuwa ya kisiasa zaidi….?’ Nikauliza
‘Yawekana ikawa hivyo, ila kwa hivi sasa ni mapema kulisema hilo,
maana kwangu mimi natakiwa niwe na ushahidi unaoweza kumtosheleza hakimu, sio
maneno ya kusikia ..unanielewa, nia ni kukuondoa kwenye makosa kisheria, sio
kupambana na makundi…’akasema
‘Inasemwa hivyo kuwa huenda ni maadui wa baba yangu wa kisiasa
wanatumiwa mwanya huo kujenga kashafa,kwa vile baba yupo kwenye siasa, ..’nikasema
‘Nikuambie kitu, hadi hivi sasa upande huo wana kundi limeundwa
kwa ajili ya kutafuta ni nani kamuua mtu wao, ..Marehemu alikuwa mtu muhimu
sana kwao, na wametumia pesa nyingi kumgharamia , kwenye masomo nk..haiwezekani
wao, wakamuua..lolote laweza kutokea, ..kama ni kisiasa, lakini kiushahdi haina
mshiko..’akasema
‘Kwahiyo…?’ nikauliza
‘Kwa hivi sasa acha nifuatilie mambo ya dhamana yako kwanza, ni
muhimu sana hilo, kabla siku haijaisha,
.., mengine yanaendelea kufanyiwa kazi, unasikia wewe kwa leo nakuomba tu, utulie
kwanza, najua upo kwenye wakati mgumu lakini kwa kosa kama hili, hatuna ujanja
wa kulazimisha mambo, niamini mimi,…’akasema
‘Nakuomba kitu kimoja, usije ukamwambia mume wangu, najua wazazi
wangu wameshafahamu lakini mume wangu ni mgonjwa, haya mambo yatazidi
kumchanganya,...’nikasema.
‘Wote hawo wanashafahamu, wazazi wako walinipigia simu, japokuw
mtu wa kwanza kunipigia simu alikuwa ni mume wako, niliongea naye na yeye , na
akaniomba sana niweze kukusaidia upate dhamana haraka iwezekanavyo...’akasema
‘Haiwezekani, ni nani alimuambia mume wangu kwa haraka hivyo alijuaje,
kwanini watu wanachukua mambo kwa haraka hivyo, hwafahamu kuwa huyo mtu ni
mgonjwa, na docta, amesema hakuwahi kuongea naye leo, ni nani huyo..?’
nikauliza.
‘Ndio hivyo, ili ujue kuwa, dunia sasa hivi haina dogo....wa
kwanza kunipigia simu alikuwa ni mume wako, na baadae ndio wakanipigia wazazi
wako, wazazi wako ndio walionifanya nihangaike kumchukua mgonjwa nije naye…’akasema
na kuondoka.
Nb: Tulikuwa tunamalizia sehemu hii, ilikuwa ndefu kidogo, ndio tukaigawa sehemu tatu, tukijaliwa tutaingia sehemu nyingine, kufichua utata huo, ni nani kamuua Makabrasha na kwa nini....
Swali,: bashiri ni nani anaweza akawa kamuua Makabrasha, kati ya wahusika hawa: Mdada(mke wa mgonjwa), mgonjwa (mume wa mdada), Rafiki wa mdada(anayesafiri masomoni), Docta rafiki wa mume, wanasiasa ili kujenga kashfa...toa maoni yako, na ni kwanini unaona hivyo.
Tuzidi kuwa pamoja.
WAZO LA LEO: Ukiona
mtu anafurahia madhila na taabu za wengine , na anatamani watu hao hata wafe, watu
ambao wasio na hatia, wanateseka, wazee , akina mama na watoto ambao hata
hawajui kinachoendelea, wewe unafurahia, unatoa maneno ya dharau, chuki,
unadhihirisha ile chuki yako ya ndani…eti kwa vile sio wenzako, ujue mtu huyo
ana roho ya shetani ndani yake.
Haijalishi mtu huyo anayeteseka,
anayedhulumiwa haki yake yupo kwenye kundi gani, ilimradi hayo yanayompata sio stahiki
yake, na hakuna hukumu kisheria iliyopitishwa dhidi yake, ilibidi watu wapaze
sauti ya kuwatetea,…lakini watu wanafurahia, wengine wakiuwawa, wakiteseka,
wakidhulumiwa, utafikiri hao wanaofurahia hivyo wataishi milele,..hakuna
atakeyeishi milele, marejeo yetu ni kwa yule aliyetuumba, na siku itafika
hukumu ya kweli itatimilizwa.
Tukumbuke sisi sote ni wana-wa -Adamu, na chanzo chetu ni kimoja,
sasa iweje damu ya ndugu yako inamwagwa, watu wanadhulumiwa haki zai, sisi
tunafurahia, kwa kisingizio cha makundi, bado tunaiona ni wacha mungu…hapana
huo sio ucha mungu,na wenye tabia hiyo, sio mtoto wa Adamu, na kama wewe sio
mtoto wa Adamu, utakuwa mtoto wa nani..
No comments :
Post a Comment