Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Thursday, November 16, 2017

MKUKI KWA NGURUWE-27



Alikuwa ni baba….baba ananipigia simu…nikawa najiuliza kuna nini tena...kwa pale ilikuwa sio vizuri kupokea simu, labda nitoke nje, nikamuangalia docta, docta akawa haniangalii,...na simu ikaita mpaka ikaacha yenyewe...

 Haikuita tena...tulishaingia chumba alicholazwa mgonjwa na...nikawa nasita kidogo, na docta, akanigusa begani, nikageuka kumuangalia.. akaniashiria nisogee, nitembee kuelekea kule kwenye kitanda….alipolala mgonjwa.

Mapigo ya damu yalikuwa yanakwenda kwa kasi, ni kama nina wasiwasi, au kuna kitu kinakuja kutokea, ...sijui kwanini niliwaza hivyo...

Mume wangu alikuwa kalala kwenye kitanda huku akiwa kanyooka kabisa, na ilionekana kama kawekewa vyumba pembeni ili asitingishike,..lakini tofauti na ilivyokuwa mwanzo, safari hii kitanda kilikuwa kimeinuliwa kidogo, ili yeye kuweza kulala kama vile ameinuka sehemu ya begani na kichwani…

Nikasogea,…nilimchunguza, nikagundua kuwa, shingoni alikuwa kavalishwa, plastiki la kuzuia shingo isicheze cheze, na jinsi alivyowekwa ni kama mtu kakaa mwenyewe kimtindo. Na pale alipokuwa kalazwa, aliweza kuangalia mlangoni, kwahiyo tulipoingia tu, alituona.

Rafiki wa mume wangu yeye akawa kasimama, nilijua alifanya hivyo, ili kunifanya mimi nitangulie mbele yake, yeye akawa anakuja taratibu nyuma yangu, huku akinigusa kwenye mkono, kuniashiria kuwa nisogee pale alipokuwa mume wangu , na hata ilifikia hatua ya kuninong’oneza akisema;

‘Nenda pale kitandani kamsalimie mume wako,....mpaka nikifundishe,..., na kumbuka niliyokushauri .....’ nikaelewa ana maana gani, nilisogea huku macho yangu yakiwa yanamwangalia mume wangu.

Kwa pembeni karibu na ofisi ya docta, walisimama madakitari wawili wakihakikisha kila kitu kinakwenda salama, na mmoja wapo alikuwa dakitari wake bingwa wa maswala ya mifupa, alikuwa kashika makabrasha yake akimuelekeza msaidizi wake ni nini cha kufanya baada ya hapo....

Mimi sikuwa na haja na watu hawo kwa muda huo, mawazo na akili  yangu ilikuwa kwa mume wangu, na macho yangu yalikuwa yamelekea pale alipo mume wangu, na nikawa namsogelea huku tumetizamana machoni.

Macho yangu na ya mume wangu yakawa yanaangaliana, kwanza niliona usoni kama anashituka,au kama ananishangaa kuniona, na baadaye mdomoni akaonekana kutabasamu, lakini niliona kama tabasamu la kulazimisha,..lakini kadri tulivyokuwa tukimsogelea ndivyo lile tabasamu lilivyozidi kuongezeka, na sasa likawa tabasamu halisi, na alikuwa wa kwanza kutamka neno.

‘Hatimaye mke wangu umefika...’akasema.

 Na kauli hii ilinifanye nigeuke kumwangalia rafiki wa mume wangu , ambaye alikuwa nyumba yangu kama vile wafanyavyo walinzi, nahisi aliogopa nisije nikaongea jambo lisilotakiwa kwa wakati huo.

Kiukweli sikuwa nimependa jinsi anavyonifanya, nakuwa sina uhuru wa kuongea, lakini kwa namna nyingine niliona ni bora iwe hivyo, maana ananifahamu vyema, sina uvumilivu wa kumezea jambo, kama ni jambo la kuongewa, ni lazima litaongewa tu, sipendi kunyamaza nyamaza.

Nilimwangalia mume wangu huku nikitabasamu , lile tabasamu la kimodo, ili tu mume wangu aone kuwa nampenda, namjali, na sina kinyongi naye, kwakweli kwa hali ilivyo, tabasamu hilo lilikuwa kama la kubandikwa mdomoni, lakini nilijitahidi kuliigiza ipasavyo…

Nilipogeuka kumwangalia rafiki wa mume wangu, nilimuona naye akitabsamu, kama vile ananionyeshea kuwa na mimi nitabasamu hivyo hivyo,na akawa ananionyeshea ishara kuwa nisogee mbele karibu sana na mume wangu. Nami nikasogelea kile kitanda alicholala mume wangu , na kumuinamia..

Kwa ujumla mume wangu alikuwa amepungua sana, na hali hii ya kupungua, kukonda ilianza kujitokeza hata kabla ya hili tatizo, na baada ya hili tukio, nimeona kapungua kwa haraka sana, hali hii imezidi kumfanya akonde zaidi, hata mashavu, yalishaonyesha kubonyea, moyoni nikasema akipona tu nitahakikisha mashavu yanakuwa dodo...ni lazima nimrejeshe kwenye hali yake ya kawaida....

‘Nimefika mume wangu unaendeleaje?’ nikamuuliza nikiwa nimemkaribia, na kumuinamia nikambusu kwenye paji la uso, yeye akaguna kidogo na kusema;

‘Mhh, hata sijui niseme nini, kuwa sijambo au naumwa, mwenyewe unaiona hi hali niliyo nayo, maana hapa nilipo ni kama nusu mfu, mwili wote sio wangu tena, kama unavyoona, mwili wote chini hauna kazi,ni kama sio mwili wangu,....’akasema akionyeshea kwa ishara.

‘Utapona usijali..’nikaema

‘Unajua, eti wanasema ni swala la muda, lakini kwa hali kama hiii ....dakika,saa , siku ni kama mwaka, nateseka sana mke wangu,sijui hii ndio adhabu yenyewe, mungu wangu nisamehe sana.., nimekosa, sitarudia tena.....’akawa anaongea na mimi nikawa namwangalia tu.

Kiukweli macho yake yalionyesha huruma, na alivyokuwa akiongea, hata ingelikuwa nani angelimuonea  huruma, …pale nilipo huruma ilinishika, na  nilihis machozi yakianza kunijia, nikakumbuka maneno ya docta...

‘Hakikisha humuonyeshi mume wako kuwa anaumwa sana, zuia kulia, jenga tabasamu la kumuonyesha kuwa hajambo...muonyeshe kuwa hali aliyo nayo ni ya kawaida tu...’

‘Mume wangu mbona umeshapona tu, ..hatua uliyofikia ni kubwa sana, maana ukiona hilo gari lako lilivyoharibika, huwezi kuamini kuwa kuna mtu katoka hai, lakini mungu wako bado anakuhitajia uwepo dunia, sisi tunaokupenda tunakuhitajia sana..namshukuru mungu kuwa upo salama, na hali uliyo nayo ni ya kutia matumaini, cha muhimu ni kufuata masharti ya madakitari...’nikasema.

‘Eti masharti ya dakitari,..masharti gani hayo, hapa nilipo nitafanya nini cha kuvunja hayo masharti, maana kama unavyoona mwili wenyewe hausogei, nitavunja msharti gani, kinachofanya kazi hapa ni akili tu...kuwaza tu, ..haya na huko kuwaza nitawezaje kujizuia, wakati nafahamu fika , kuwa haya yote yametokana na dhambi ....nimewakosea watu.’akasema na hapo nikageuka kumwangalia rafiki wa mume wangu, akanionyesha ishara ya kuwa makini.

‘Mume wangu hakuna dhambi hapa duniani isiyoweza kusameheka,kama umetubu ..mimi nina imani kuwa kila binadamu anakosea, na wewe kama binadamu huwezi kujiaminisha moja kwa moja kuwa utaweza kutenda kila jambo sawasawa, ....kama ulitetereka, basi ..imetokea na huna jinsi nyingine, cha muhimu ni kujitahidi kutuliza kichwa chako na mawazo yako ukayaelekeza kwenye kupona, na wamesema kupona kwako itategemeana na wewe mwenyewe...’nikasema.

‘Mmh, kupona kwangu itategemea na mimi mwenyewe, sijui kwa vipi,...na wakati nimeshakuambia nimewakosea nyie watu wangu, ..nimewakosea watu muhimu sana, katika maisha yangu..nimekukosea wewe mke wangu …nisamahe sana...’hapo akatulia kidogo, na nilipomwangalia machoni, niliona kama analengwa legwa na machozi, akasema;

‘Mimi nimeshakusamahe  mume wangu…’nikasema

‘Mke wangu umesema umenisamehe, kwanini ulikuwa huji kuniona mara kwa mara, maana hata kama nilikuwa sina kauli, siwezi kuongea, lakini nilikuwa naona kila kitu kinachotendeka…?’ akauliza na hapo ikabidi nigeuke kumuangalia docta.

Docta aliniashiria niwe makini hapo, na kabla sijasema kitu, akaendelea kusema

‘Unajua.., wote waliokuwa wakija nawaona, lakini wewe sikuweza kukuona, , nilikuona mara moja tu, siku ile...hali hii inanipa shida na kunifanya nisiamini kuwa kweli umenisamehe....hivi kweli umenisamehe mke wangu..?’akasema na alikuwa kama analalamika, na hali hiyo ikanifanya nigeuka kumwangalia tena rafiki wa mume wangu ambaye alijifanya kama haniangalii mimi, alikuwa akisoma kadi iliyokuwa imewekwa mezani.

‘Mume wangu, mimi nilikuwa nafuata masharti ya madakitari, kwani wao waliniambia kuwa huhitajiki kusumbuliwa, na ilitakiwa usikutane na watu wengine zaidi ya madakitari wako, hadi zipite siku saba, ili uweze kutuliza kichwa chako... ni masharti niliyopewa mimi, na ndivyo nilivyofanya, sikutaka litokee jambo la kukufanya usipone haraka...’nikasema.

‘Sio kweli, kama ni hivyo mbona rafiki yako wa karibu mara nyingi nilikuwa nikimuona akifika hapa...na aliniambia kuwa anaondoka na mtoto, kwenda kusoma, kwanini aondoke na mtoto bado mchanga, hivi nyie mna akili kweli...’akasema.

‘Alifika akakuambia hivyo..?’ nikauliza nikionyesha mshangao.

‘Ina maana wewe hujui kuwa keshaondoka, ...usinidanganye wakati wewe ndiye mfadhili wake, mimi sikuona umuhimu wa yeye kwenda kusoma kwa sasa, wakati ana mtoto mchanga,nilimshauri asubiria kwanza, lakini hakunisikiliza, nikajua mumepanga wote...’akasema.

‘Haina shida, huko Ulaya unaweza kusoma na mtoto, unaweza kusomea nyumbani,...hilo lisikutie mashaka, anajua ni nini anachokifanya yeye sio mtoto mdogo....’nikasema.

‘Kweli Ulaya ni ulaya, lakini mimi namuwazia sana mtoto, yule mtoto bado mchanga bwana, wewe hulioni hilo..yeye angelisubiria angalau miezi mitatu hivi, lakini haelezeki, htaaki kusikia, kaamua kaamua basi, rafiki yako mnajuana wenyewe,....’akasema.

‘Yule niachie mimi, namfahamu sana, ni rafiki yangu, usiwe na shaka na yeye, alishaambiwa huko mtoto hatakuwa na shida, kila kitu wamemuandalia....’nikasema.

‘Mimi sina shaka na yeye nina shaka na mtoto, mtoto yule bado mchanga, safari na hali ya hewa ya huko, mmh, mimi sijui....’akasema na kutulia, na baadaye akasema;

‘Yeye alikuwa anakuja, anasimama pale mbele kwenye kiyoo, ananiangalia kwa muda halafu anaondoka, mimi nilikuwa namuona…’akasema na mimi nikageuka kuangalia kwenye hilo dirisha.

‘Nikawa najiuliza kwanini haingii ndani  na mara ya mwisho nikaona niongee na dakitari ili aruhusiwe aingie, inaonyesha alikuwa ana hamu sana ya kuniona, ..rafiki yako ni mtu mnzuri, ila akiamua jambo, hapo humuelezi kitu, hajali tena hisia za wengine..’akasema

‘Mhh, ndivyo alivyo…’nikasema maana naona imekuwa maongezi ni kuhusu huyo rafiki tu, sikutaka kumkatili.

‘Ila kiukweli kauvunja moyo wangu…kuondoka na mtoto, unajua yule tumeishi naye, tunamjali sana, kwanini hukumshauri wewe…lakini sawa mwache aondoke, si atarudi,....’akasema

 Hapo nikawa nataka kuongea jambo,  kuuliza maswali, lakini nikaogopa, nikaona nikae kimiya,maana nilipomwangalia rafiki wa mume wangu ambaye alikuwa kwa mbele, eneo la kichwani kwa mgonjwa, na alikuwa akiniangalai moja kwa moja ninavyoongea, akaniashiria nisiseme neno.

‘Mke wangu, mimi inanipa shida sana naona kama wewe hujanisamehe kiukweli, na nilikuambia ukinisamehe nahis hivyo,..siku ile kweli ulitamka na ilionekana hivyo, ila kila hatua nahisi kama hujanisamehe..’akasema

‘Kwanini unasema hivyo mume wangu..?’ nikauliza

‘Kama hujanisamehe sizani kama mimi nitakuwa na amani, na huenda nikarudi kuzimu , unajua nilikufa…ni maombezi tu, kuwa nirudi ili nimalizie toba, nihakikishe kuwa kila kitu kipo sawa…sasa kwa hali kama hiyo, sioni umuhimu wa haya yote...’akasema na mimi hapo nikashindwa kuvumilia nikajikuta nimetamka neno ambalo lilimfanya rafiki wa mume wangu kuniangalia kwa sura ya kunisuta;

‘Mume wangu mbona hujafanya kosa, kwani kuna kosa gani kubwa la kukufanya usononeke kiasi hicho...nimeshakuambia kuwa nimekusamehe, japokuwa sijui kosa gani ulilolifanya...’nikasema na nikaona akishtuka, na kunikazia macho, nikaona kama anabadilika.
Docta rafiki , akahisi kwa haraka akatoka kule alipokuwa kasimama na kunisogelea, sikuwa nimemuona, hadi pale aliponishika mkono, nilipogeuka nikamuona yeye akinionyesha ishara ya kuwa makini.

‘Mhh, mke wangu…unasema nini, ..ndio maana nilikuwa na wasiwasi sana, mungu wangu, ina maana kweli hujui kosa lako ni nini…mmmh,… hapana usinichekeshe,..ina maana kweli kosa lenyewe hulijui, halafu umekubali kunisamehe ..haah , kwahiyo ulikuwa wanichezea shere, unaigiza tu, nilijua tu…’akasema

‘Mume wangu mimi najua , kuwa umenikosea kwa yale mambo yetu ya nyumbani, unakwenda unakunywa, unakutana na wanawake huko..sasa sijui huko mnamalizana vipi, hiyo ni siri yako,..kama ni hivyo, basi  mimi nimekusamehe ilimradi umefahamu kosa lako ni nini, ila sipendi kujua zaidi kama, ulipitiliza utajua wewe na mungu wako, ila mimi nimekusamahe, ni wapiti njia au sio..…’nikasema

‘Oh…kumbe hata kosa lenyewe unasema hulijui, hapana sio wapiti njia, mimi sikuwa na tabia hiyo…mimi nazungumzia kosa hilo jingine…kwahiyo sio kweli, niambie ukweli..., au unajifanya tu kuwa hulijui kosa langu, kwa vile kuna watu hapa, huyu ni rafiki yangu tu…’akasema akimuonyeshea docta.

‘Mume wangu haina haja, yamepita basi…’nikasema

‘Hayajapita, ni lazima unisamehe kiukweli,  je hujaongea na mwenzako, mkakubaliana jambo..au kwa vile hayupo leo hapa,…najua angelikuwepo hapa ingelikuwa ni bora zaidi, ili alithibitishe hilo…lakini si atakuja tu, nitahakikisha anaongea kila kitu, hata hivyo mimi sina muda, sijui muda wangu..maisha haya hayana muamala..nataka niutue huu mzigo...’akasema na kutulia.

‘Mume wangu mimi nimekusamehe, na kwangu afya yako ni bora kuliko, hayo ya kupita tu, amini kuwa nimekusamehe, nisingelipenda kujua mengine zaidi, inatosha, unanisikia, wewe tuliza moyo wako ili upone haraka…’nikasema

‘Hapana mimi nataka kauli yako, nijue ukweli wako, je ni kweli kuwa hulifahamu hilo kosa,… aah..pumzi inakata kwanini docta…ni lazima niliongee hili  leo hii,…niambie ni kwanini usilifahamu wakati wewe ndiye uliyemtuma kwangu ..?’ akauliza

‘Kumtuma nani…?’ nikauliza na docta akaniashiria nikubali tu.

‘Rafiki yako…’akasema

‘Rafiki yangu …ok, ndio, mara nyingi namtuma…alikuambiaje…’nikasema

 Hapo mgonjwa, akatulia akionyesha kama anawaza jambo halafu nikaona kama anabadilika, anapata taabu ya hewa kitu kama hicho, mimi niligeuka kumuangalia docta, na docta wakati huo alikuwa anashughulika na kitu kingine.

Nikageuka tena kumuangalia mume wangu, akawa yupo sawa, …ila ni kama anajilazimisha,…akasema

‘Siamini kama hujui kosa langu,..nilijua tu , hukupenda, lakini unajua tena ulevi..na hapo imekuwa sababu ya madhambi mengi tu….ooh, kwanini hii hali haitulii, niongee na mke wangu…’akasema akijaribu kuinua kichwa kumuangalia docta, na docta akamsogelea na kusema;

‘Kama hujisikii vizuri usijilazimishe…’akasema docta

‘Usiniingilie haya docta,..hata kwangu ni mhimu kwangu kuliko chochote,..huenda nisipate muda tena…’akasema akimuangalia docta. Na docta akawa kama anataka kumzuia asiendeleee kuongea lakini hakuweza, akaniangalia mimi huku akionyesha wasiwasi, na kwa muda ule, mume wangu alikuwa akihangaika kama hewa inamuwia ndogo, lakini aliendelea kuongea.

‘Mke wangu, unafikiri mimi nilipenda kufanya hivyo, ilikuwa kazi kubwa sana kukubali hayo…, na nilikubali tu kilevi levi, lakini moyo haukutaka, na ni kwa vile ni rafiki yako, na ni kwa vile kasema mliongea naye ukakubaliana ila iwe siri,..hapo ukichanganya na ulevi, nikajikuta nimeingia kwenye mtego, ningelifanyaje hapo mke wangu nakiri kuwa ni kosa maana sikutaka kuhakiki kutoka kwako…’akatulia huku anaonekana anapata shida

‘Docta….’nikasema

‘Achana na …na huyo do-docta nisikilize mimi..unasikia , nisikilize mimi mumeo…’akasema, na mimi nikamuangalia, ndio akaendelea kuongea.

 ‘Ulevi, mawazo..na kauli yake, ikanihadaa…unasikia, nasema haya kiukweli…nisamahe tu, najua nimekosea sana, kwani sheria ya ndoa inanibana,…’akasema na nikaona akizidi kuhangaika.

‘Mhh…sikupenda mke wangu…ndio maana najuta sana, inaniuma sana, sijawahi na sikutarajia kufanya hilo, nimekuwa mwaminifu kwako mke wangu, wengi wakiniona nipo na mwanamke wanafikiri vibaya, lakini napoteza nao mawazo tu…’akasema na kukokhoa, halafu akatulia na nilitaka niongee lakini akaanza kuongea yeye.

‘Rafiki yako, ananiliwaza, tunaongea ananipa faraja, nikamzoea hivyo, lakini sikuwa na nia mbaya kwake…ila siku , oooh,…ikatokea , hata sijui ilikuwaje, nashindwa kuelezea, kauli yake ikaniponza,, yaani inaniuma sana, nilishindwa mke wangu, nikiri kuwa , ooh, nilitaka m-tttt.ooh wa-waaah, aaah..’akashindwa kuendelea na hapo rafiki wa mume wangu alifika na kumuinamia akamwambia;

‘Rafiki yangu acha kuongeza zaidi, mke wako ameshakuelewa, hukukusudia kabisa kujiingiza kwenye dhambi hizo, ulishawishika vibaya, kama ulivyosema, unakumbuka nilivyokuambia, acha kabisa kuongea hayo mambo....ni kosa na kama ni kosa limeshafanyika, ...basi’akasema…kukawa kimia, mimi nilikuwa mwili umekufa ganzi

Muda kidogo,akafunua mdomo na kusema;

‘Mke wangu hana kosa,…wewe huna kosa nisitoe kisingizio kuwa kwa vile..hapana, maana muda wote najizuia,…lakini  rafiki yaka…alichosema, kilikuja kipindi kibaya nikiwa sijitambui…kwahiyo kwa hali kama ile, basi ikawa hivyo, kwahiyo, nisamehe tu mke wangu….’akasema

Docta akamwambia;-

‘Basi keshaelewa, tulia, sasa lala..au unataka ulazimishwe kulala kwa madawa…’akaambiwa, mimi kiukweli akili ilikuwa sio yangu, nilikuwa kama naota ..

‘Sogea pe-pembeni bwana,.. mimi nataka kuongea na mke wangu…nisipoongea leo, sitaongea tena, unanielewa, nilifunga kuongea, nikiwaza mengi, nikutubu, nikiwazia ya huyo rafiki yake, hataki kunisikiliza…sasa nipo peke yangu ni bora kufa tu, maana sitaeleweka, nakutegemea wewe mke wangu, basi…baba yako, hatanisikia, kampuni,…hata sielewi, ..’akasema.

 Na hapo docta akageuka kule walipo madocta, nahisi alitaka kuwaashiria kitu , lakini wale madocta walikuwa wameinama wakiangalia kitu mezani.

‘Mke wangu unanifahamu sana, wakati wote nimekuwa nawajibika, nimekuwa mwaminifu kwa kazi, tukirudi nyumba wewe na laptop na mimi na laptop, hao ndio wapenzi wetu, haahaa…ni hivyo, basi mimi nikaongeza pombe, kumbe …ndio imenifikisha hapa…’akatulia

Pale nilipo najaribu kufunua mdomo lakini siwezi, nimebakia kimwili tu…na yeye akaendelea kuongea;

‘Mhh..sa-sa.., japokuwa wakati mwingine nateseka kama binadamu wa kawaida, unatamani kitu, unataka mtoto…..unajua tena…inabidi uvumilie, ndoa ni ndoa..mke yupo, lakini utafanyaje, nisingeliweza kumlazimisha mke wangu…’akasema na hap akawa kama anaongeza kitu kichwani mwangu, natamani nianza kuonega kwa jaziba, lakini siwezi.

‘Mke wangu ….kiukweli sikupenda, maana nakupenda sana mke wangu, na sikutaka kukuumiza mke wangu, japkuwa nilikuwa naumia, natamani, ndio nikaanza kulewa, kulewa ikawa ni shida, maana ndio imefanya akili ikaharibika…ila simlaumu mtu, aah, najilaumu mwenyewe dhambi ni zangu, usiponisamehe, basi acha nikaangamie, unasikia, nisimlaumu mtu, kabisa....’akasema

‘Mume wangu inatosha, sawa nimekuelewa, inatosha, mimi nimekosa, samahani kwa hilo sitarudia tena sikujua kuwa nakuumiza hivyo, nisamehe mume wangu, oh…ina maana haah, basi, ..hata, basi, hata..sielewi, inatosha mume wangu, basi …’hapo sikuweza kujizuia, nikaanza kulia.

‘M-mke -wangu, usilie….najua hujakosea, sikiliza…’akawa anahangaika kutaka kama kuinuka hawezi..

‘Ohoo, unafanya nini sasa wewe, utamuua mume wako, nilikuambia nini..’akasema docta akijaribu sasa kufanya lolote kuidhibiti ile hali

‘Mke wangu…mke wangu nisamahe tu…nimeongea hayo kukuonyesha kuwa sikutaka..ila nili..zidiwa, na kwa vile alisema mlikubaliana, upo radhi..basi, …’akatulia

‘Tulikubaliana nini..…’ hapo nikasema kwa ukali, mpaka docta akashtuka na kuniangalia kwa macho yasiyoaamini,..haraka akanishika mdomoni nisiendelee kuongea.

‘Ndio..alisema hivyo..ndio maana nikashindwa,...nikashindwa,....najuta sana kukubali kufanya hivyo , kwanini nilishindwa kujizuia,mbona wakati wote niliweza , kwanini safari ile nikashidwa ...nimeumia sana,…nisamehe sana mke …mke…tamka neno kuwa umenisamehe, niwe huru na mateso haya, aah, aah, aah,….. ’ madocta wakawa wameshafika;

‘Nini tena, hebu,..hebu….’nikasukumwa pembeni, maana pale nilipo sikuweza hata kuinua mguu.

‘Sogea, sogea, basi hatuwezi kumruhusu kuongea tena, ni vyema ukatoka nje, ...ngoja tumpe dawa,  anahitajia kupumzika....’akasema

Hapo ndio nikagundua kuwa nimeharibu, nimeshindwa kuvumilia, kama alivyonitaka docta, badala ya kujenga nimebomoa, nikajua sasa nimeua…mume wangu akawa bado anajitahidi kuongea, nikasikia akilalamika,

‘Mbona sijamalizana na  mke wangu, sijamwambia, nilichotaka kumwambia...nipeni dakika mbili niongee na mke wanguuu-uh...’akasema mume wangu, lakini maneno yake hayo ya mwisho yalikuwa kama ya mtu aliyelewa, na akatulia, kumbe kuna dawa waliipitishia kwenye mpira, ilikuwa dawa ya usingizi....

‘Mbona inachelewa….’akasema docta akiwa na maana ile dawa ya kumfanya alale imechelewa kufanya kazi

‘Mungu wangu nimefanya nini....’nikajikuta nimesema  hivyo, nikijua kuwa nilishindwa aliyoniambia rafiki wa mume wangu  nikageuka kumwangalia rafiki wa mume wangu, ambaye alikuwa akibenua mdomo, kuashiria kuwa hakuna tatizo.

Nikageuka kumwangalia mume wangu ambaye alikuwa keshafumba macho, na madaktari walikuwa wakiendelea kumkagua, na hapo kichwani nikaanza kukumbuka maneno yake, maana muda ule wakati anaongea kuna muda akili ilikuwa kama imeganda, sasa maneno yanaanza kujirejea kichwani;

‘Mke wangu, unafikiri mimi nilipenda kufanya hivyo, ilikuwa kazi kubwa sana kukubali,...kwa vile ni rafiki yako, na kwa vile kasema wewe ndiye uliyemtuma,

‘Oh, mungu wangu…’nikajikuta nimesema hivyo

Mimi ndiye niliyemtuma, ..aka-aka…sio hivyo, hatukukubaliana hivyo, kwa mume wangu hapana, hili halipo, kwa shameji yake, nimtume mimi, haiwezekani, sio kweli , sio kweli, labda kama …rafiki yangu aliamua kutumia kauli hiyo kutimiza malengo yake…lakini haiwezekani sio rafiki yangu…

‘Au mume wangu hana maana hiyo, labda ana maana ya jambo jingine labda sio hivyo, mungu wangu, mungu wangu sio kweli jamani…’maneno hayo nikayasema kwa sauti , na docta akayasikia, lakini wenzake walikuwa wakihangaika na mgonjwa..

Docta akaniashiria nitulie…hutaamini bado nilikuwa sijaweza kuinua mguu, nipo pale niliposukumiwa na wale madocta, …miguu haiana nguvu

Na muda huo nahisi kama kuna vitu vimeingia kichwani, maneno ya mume wangu yanajirudia rudia kichwani;

‘Mke wangu unanifahamu sana, wakati wote nimekuwa nawajibika, nimekuwa mwaminifu kwako na kazi yangu,nimekuwa nikijizuia kutenda dhambi yoyote, japokuwa wakati mwingine nateseka kama binadamu wa kawaida...


‘Oh…mbona sielewi, kuna nini hapa, ina maana ni kweli,…’nikasema kwa suti ndogo, kama namnong’oneza mtu..

‘Sio kweli, kachanganyikiwa tu mgonjwa sio kweli…’nikasema sasa kwa sauti, mpaka wote pale ndani  wakageuka kuniangalia mimi.

Docta akanisogelea na aliponiangalia tu, akagundua kuwa nimeshabadilika na muda wowote naweza kudondoka, ..akanishikilia nikaona anamuashiria docta mwingine aje kusaidia..akawa anamuagiza kitu, sikuelewa ni kitu gani.

‘Ina maana ni kweli, aaah, hapana sio kweli jamani …docta niambie kuwa sio kweli..hana maana hiyo kabisa, eti docta ni kweli jamani...?’nikasema huku nashikilia kifuani, kiukweli pale nilihisi maumivu makali yalikuwa upande wa kushoto…nipo kama nimechanganyikiwa.

‘Mke -wangu,wakati mwingine kama binadamu wa kawaida natamani nitende dhambi, lakini najizuia, naogopa, ...lakini safari ile nikashindwa,...nikashindwa,....najuta sana kukubali kufanya hivyo , kwanini nilishindwa kujizuia,mbona wakati wote niliweza , kwanini safari ile nikashindwa....’

Maneno hayo yalijirudia rudia kichwani...yakanifanya niishiwe nguvu kabisa, kama isingelikuwa ni docta ningedondokea sakafuni, ..

‘Inatosha...haina haja, kumpiga sindano.’akasema docta akimwambia mwenzake sikujua ana maana gani, na mimi nikawa naongea tu..


‘Umefanya nini na mume wangu, ...mumefanya dhambi gani wewe na rafiki yangu, ina maana ni kweli ..ina maana ni kweli…hapana sio kweli jamani haiwezekani kabisa,…

Nikamwamgalia mume wangu ambaye wakati huo alikuwa katulia, kalala, na akili yangu pale ikanituma kuwa keshafariki…sijui kwanini niliwaza vile…;

‘Ina maana nimeongea vibaya, nimemuua mume wangu. Mume wangu usife nataka niusikie ukweli wote, jamani…sio kweli jamani, sio kweli, kwanini hivi jamani..mume wangu usife uje uniambie ni kwanini..’ sasa nikawa naongea kama mtu aliyechanganyikiwa..

‘Hajafa, tulia, …ukiendelea kuongea hivyo ndio utamuua…’akasema docta...na muda ule akawaashiria kitu, na mara nikahis sindani ikipigwa..haikuchukua muda,  giza litanda usoni…lakini kabla sijafunga macho mlangoni nilimuona baba akiwa kasimama, kama anasubiria kuambiwa aiingie, sijui alifika muda gani ….


WAZO LA LEO: Mambo yakijirudia sana mwishowe  watu huja huamini, hata kama ilikuwa sio kweli. Ndivyo akili zetu zilivyo., ni wachache sana wanaoweza kusubiria hadi ukweli uwe bayana hasa kwa mambo yanayokwanza mioyo yetu. Tunaweza kujiaminisha kuwa ni kweli, kwa vile tu linaongelewa sana, kwa vile tu mtu mashuhuri kalisema, nk..lakini hatujiuliza kwanza, je ni kweli, je kama sio kweli itakuwaje, na tujiulize hivyo huku tukifanya tafiti yakinifu…bora ya kuwa na subira kuamini jambo huku ukitafuta ukweli kuliko kukimbilia kuamini halafu ije kuwa sio kweli..

Ni mimi: emu-three

No comments :