Hii ni blog maalum kwa kumbukumbu za kimaisha, na matukio yenye mafunzo ndani yake, ndio maana nikaiita 'diary'(shajara). Pia tunakaribisha mijadala yenye kuelimisha

Na kwa kuifanya iweze kuvutia zaidi tunaandika matukio hayo kwa mfumo wa visa, hadithi au tamithilya..

Wewe ukiwa mdau muhimu, unaweza kuchangia na wenzako kwa kutoa hoja (comments). Pia unaweza kutoa maneno ya hekima, utaalamu, au dukuduku lako (kilio chako)kwa jamii ili kuweza kukidhi mahitajio yetu.

MUHIMI, SOMA , CHANGIA, NA TOA kisa chako, au lolote lenye mafunzo ili tuliweke hewani.

TUPO PAMOJA DAIMA


Tushirikiane, Tusaidiane, Tupendane, Tuvumiliane, Tusaidiane, Tusameheane.

Kwa visa motomoto tunapatikana pia kwenye mitandao ya kijamii ya: Facebook, na Twitter, bofya hapa upate visa zaidi;

https://www.facebook.com/emu.three, na kwa ajili ya kuitangaza hii blog, ingia hapa:

https://www.facebook.com/diaryyangu/

`u-like' na pia unaweza kutwitter hapa;

https://twitter.com/emuthree



Tuesday, August 29, 2017

DUWA LA KUKU...43


‘Kabla hujaendelea mbele naona muda unakwisha,  nauliza maana mpaka hapo ulipofikia, sijasikia kuwa ni nani mwenye huu mzigo, hiyo mimba ni ya nani,...’alikuwa mama Ntilie akinionyeshea mimi kidole tumboni, na hapo akili ya kufuatilia hiki kisa ikapotea na kurejea kwenye hali yangu,…

Mzee mzima akageuka na kuniangalia, akatikisa kichwa na kusema;

‘Yaani sijui nisemeje…kama nilivyoelezea awali mambo ya usiku mimi nilikuwa siwezi kuyaona, sasa siwezi kudanganya, …’akasema.

‘Yawezekana ni yako..ndio maana unavuta vuta muda…’akasema mama Ntilia

‘Mhh..hebu kwanza tuendelee na muendelezo, kama kuna swali mtakuja kuuliza baadae maana huko mbele ndio tutapata ufumbuzi, wa swali lako…na mimi nitawaambia maamuzi yangu ambayo yamenifanya nifike hapa hii leo, najua wengi watanishangaa lakini haina budi…’akasema mke wa jamaa

Yule mbaba akamuangalia mke wake kwa macho ya huruma, na alipoona kuwa yeye ndio anasubiriwa kuendelea kuongea,  kwanza akakohoa…

Tuendelee na kisa chetu.

********

 ‘Baada ya kupokea simu hiyo kutokwa kwa yule mlinzi nilichanganyikiwa, kumbe sikuchukua ile bahasha yenyewe, nilikuwa nimechukua bajasha nyingine, lakini pale nilipoichukua bahasha hiyo hakukuwa na bahasha nyingine, labda hiyo yenye video alikuwa kaiweka kwingine,…Ilichobakia hapa ni kuchukua hatua…

Kwanza nikageuka kumwangalia mke wangu, yeye alikuwa kainamisha kichwa chini, nikageuka kumuangalia kijana, kijana alikuwa akinitazama mimi  na ile bahasha bado ipo mikononi mwake, alipoona namuangalia akheuka kumuangalia mama yake hapo akafanya kosa, mimi kwa haraka nikatembea kwa kasi na kumkabili kijana, na kubakua ile bahasha mkononi mwa kijana, yaonekana hakulitegemea hilo, na kabla hajasema kitu,.nikisema kwa hasira.

‘Sasa unaona …babu yako keshajua kila kitu, haya nikutokana na mambo yako ya kitoto, nilikuambia uniamini mimi, haya nenda kwa babu yako akusaidie na huu mkanda ndio unataka mama yako akauangalia, haya ngoja nimpe akaangalia yaliyomo , tuone matokea yake yatakuwaje..’nikasema na kutembea kuelekea kwa mke wangu nikimkabidhi huo mkanda, lakini mke wangu hakuinua mkono kuipokea hiyo bahasha.

‘Chukua sasa uangalie kilichopo, ambacho ndicho huyo kijana wako kampalekea baba yako…’nikasema moyoni nikiomba ujanja wangu ufanye kazi, ni ujanja wa kuwajulia hawa watu tabia zao..nilijua kabisa mke wangu hawezi kuchukua kwa haraka hivyo.

‘Kwanza ni nini kipo ndani ya hiyo bahasha…aah, hayo ni mambo yenu sitaki hata kuyaona…’akasema na moyoni nikasema bao moja tayari, nikageuka kumuangalia kijana na kusema.

‘Haya unasemaje sasa….?’ Nikamuuliza

‘Baba, …huko kwa babu …’kabla hajasema kitu, mara simu ya  mke wangu ikalia, na mke wangu akaipokea na kusikiliza;

‘Unasemaje baba…?’ akauliza.

‘Mjukuu wako nipo naye hapa, kuna nini..?’ akauliza

‘Mzigo gani..?’ akauliza

‘Kwahiyo unataka kusema nini…?’ akauliza

‘Ok, sawa atakuja muonane naye…’akasema na kugeuka kumuangalia kijana, na kusema;

‘Babu yako anasema uende mkaonane naye…’akasema

‘Huo mzigo keshaupata..?’ nikauliza lakini mke wangu hakujibu kitu, akawa anamuangalia kijana wake kwa makini,

‘Hebu sasa niambie una tatizo gani mpaka uende, na….na kitu gani hicho ulichompelekea babu yako..?’ akamuuliza.

‘Mama  kila kitu kimejielezea humo, sikutaka kuongea, sikutaka hii hali ya kuulizwa ulizwa maswali, mimi sipendi kuulizwa ulizwa maswali,…na…’akasema sasa akimuangalia baba yake ambaye alikuwa kashikilia hiyo bahasha.

 ‘Huyu mtoto wako hana akili, hajui alivyoharibu, anatuvizia na kutupiga picha tukiwa tunagombana,..kila tukio analiweka kwenye video, hiyo ni tabia gani …sasa ndio kaamua kumpelekea baba yako ili aone jinsi gani hatupo sawa, nia yake ni nini kuvunja ndoa yetu,…’nikasema na sasa nikitaka njia ya kutoka humo ndani.

‘Basi kama ni hivyo, basi,  ngoja tuone kilichomo, halafu nitajua la kufanya…’akasema mke wangu akiangalia ile bahasha niliyo nayo mkononi.

‘Hakuna cha maana hapa, hivi sio vitu vya kuweka, maana vikitua kwa watu wabaya tutapata shida sana…tatizo ni hiyo aliyoipeleka kwa baba yako,..sijui itakuwaje…’nikasena sasa nikiiweka ile bahasga kwenye koti langu.

‘Kama ni hayo uliyoyaelezea sizani kama kuna tatizo, labda kuwe na jamabo jingine ambalio wewe hutaki kulisema, eti kijana wangu niambie ukweli…’akasema mama.

Kijana akawa katulia tu, …na mara simu ya mke wangu ikaita;

‘Nini tena baba, mara ya pili unanipigia simu..nipo kwenye kikao…, ndio..tupo wote hapa kuna nini kwani baba…?’ mke wangu akauliza.

‘Unasema unataka kuja huku, eeh, kuhusu nini…?’ akauliza na kusikiliza.

‘Bahasha gani hiyo, kutoka kwa kijana wangu, ya nini..?’ akauliza na kutulia kimia akisikiliza

‘Hapana, sina habari yoyote..’akasema mke wangu huku akimuangalia kijana, na kijana akageuka kutaka kuondoka na mama akamuashiria kwa mkono asiondoke.

Na alipomaliza kuongea na simu akamuambia kijana…

‘Unakwenda wapi subiri babu yako anakuulizia, …’ akasema

‘Hapana mama mimi nataka kuondoka,…sitaki tena kukaa humu ndani…’akasema sasa akitoka kwa kasi humo ndani, kama anakimbia..

Mimi nikawa namuangalia mke wangu kutaka kujua atasemaje , lakini hicho cha babu yake kuja hapa, kama kauona huo mkanda nafahamu kabisa ni nini kitakachoendelea, na kama keshauona huo mkanda ni bora nisikutane naye kabisa,, ili kuwa na uhakika nikauliza;
‘Baba yako anasemaje..?’ nikauliza

‘Anataka kuja hapa nyumbani,  na anataka sote tuwepo,…’akasema.

‘Sote tuwepo…! Na wakati kijana ndio huyo kakimbia, kagundua upuuzi alioufanya hauna maana, kwani baba kasemaje kuhusu hicho kikao ni kuhusu nini hasa…?’ nikauliza

‘Hajasema, ngoja….’

Baadae mke wangu akaamua kumpigia baba yake kuwa kikao hicho anachokitaka yeye kwa leo hakitawezekana..

*************
Nilibakia na mke wangu, nikisubiria amalize kuongea na simu, na wakati anaongea na baba yake mara simu yangu ikalia..nikaipokea kwa haraka;

‘Nani mwenzangu..?’ nikauliza,na huyo mtu akaongea kwa sauti kama ya kuigiza, mimi moja kwa moja nikajua ni yule mlinzi

‘Unataka nini, si umefanya ulichotaka, sawa bwana, najua malipo ya wema wangu kwako ndio hayo, sasa umepata faida gani…?’ nikamuuliza na kusikiliza alichokuwa akiongea, sikuamini kuwa mtu huyo anaweza kunifanyia hivyo.

‘Unasema nini…?’ nikasikiliza kwa makini anachokiongea

‘Unasema unataka nikulipe niini…acha uhuni wewe mtu…wewe kama haja yako ni pesa, sio lazoma utumie njia hiyo, unasikia,…aah, hapana hatuendi hivyo,…hebu jiulize, je nikiamua kumwambia bosi wako kuwa, huoni utapoteza kazi yako, au unasemaje nimwambie…’nikasema na simu ikakata.

Huyu mlinzi anasema kuwa ile bahasha hajaipeleka, kapeleka bahasha nyingine tu, na hiyo bahasha anayo yeye mkononi, na amegundua kuwa ndani ya ile bahasha kuna video, video ambayo ni hatari ikiingia mikononi mwa watu hasa watu wa mitandani na magazeti, na pia ikifika kwa mzee, baba mkwe wangu, kwahiyo kwa hivi sasa anayo hiyo video, kama nitaka yeye anahitajia pesa nyingi tu, hakusema kiasii gani,  vinginevyo atamkabidhi bosi wake, na kumuomba msamaha …’akakata simu.

Niliwaza sana hilo, na wakati nawaza hayo nikawa namuangali mke wangu, sikutaka kabisa ajue hicho kinachoendelea kati yangu na mlinzi wa baba yake,….na baadae mke wangu akamaliza kuongea na simu, akaja na kuniangalia usoni…

 ‘Mzee anasema tuhakikishe leo tunakutana na yeye, atakuja yeye mwenyewe …’akasema

‘Kwani hilo lina tatizo, tatizo ni kijana wako, je tunaweza kumpata..?’ mume akauliza

‘Hilo sio tatizo, baba keshaongea naye, na kakubali kuwa atakuwepo kwenye hicho kikao, kwani yeye ana mengi ya kuelezea,...na anao huo ushahidi wa hicho anachotaka kukisema…’akasema

‘Oh, kwahiyo kumbe bado hajanielewa..’mume mtu akasema na kutizima nje, akilini akijua ana majanga mawili tayari, sijui aanze lipi kwanza.

‘Akuelewe vipi, baba gani wewe, mwenye tabia ya ajabu, hata ingelikuwa mimi, ningelifanya hivyo hivyo..sasa ujiandae, nafahamu maamuzi ya baba, na  nikuambie ukweli safari hii, tutasigishana,..ya kuwa mimi nitakuwa pamoja na wazazi wangu, vinginevyo…’akatulia

‘Vinginevyo nini…?’ nikauliza
‘Vinginevyo, …nitayaongea hayo kwenye kikao,….na najua hicho kitakuwa kikao cha mwisho baada ya hapo sitaki tena kikao na wewe…’akasema na kuanza kuondoka

‘Je kikao kitafanyika saa ngapi mbona unaondoka…?’ nikauliza lakini mke wangu hakujibu akawa keshaondoka, na mimi nikabakia peke yangu nikijiandaa kwenda kukabiliana na huyo mlinzi.

*******************
Wakati hayo yakiendelea, mbaba akiendelea kusimulia yaliyomsibu,


Mimi ghafala akili ikahama, nikawa nawaza mengine tofauti, ikafika muda hata sisikii hicho wanachokiongelea sijui kwanini mawazo hayo yaliteka akili yangu…



Nilijiuliza ni kwanini mimi ndiye yanikute hayo yote….mimi nimezaliwa masikini, wazazi wangu walikuwa omba omba, kula yetu na maisha yetu yalitegemea kile tutakachopewa na wasamaria wema,..na kwa bahati ndio nikapata hiyo kazi ya ufanyakazi wa ndani,…lakini badala ya kupata kile nilichotegemea ndio nikazidi kuingie kwenye mtihani mkubwa.



Mama yangu niliyemuacha huko kijijini, akisubiria angalau jasho la binti yake, akaishia, kuangamizwa kwa kuchomewa banda lake na yeye kufariki kutokana na majeraha ya huo moto, je ana kosa gani, je walifanya hivyo ili iweje,..



Nasikia kumbe lile kundi la uharamia, la vijana hao waliotelekeza dhuluma hiyo lilikuwa likisimamiwa na huyo huyo marehemu, nia na lengo lake ilikuwa kupora ardhi ,lakini hata baada ya adhima yake hiyo kutekelezwa, akajikuta bado anagombea eneo hilo na hasimu wake.


Hayo nilikuja kusimuliwa na wale watu wa dini waliokuja kunitembelea wakinitafuta mumiliki halali wa eneo hilo, na hilo lilikuja kukubaliwa baada ya watu kushindwa kulimiliki. Kwani hao waliotaka kulimiliki kwa dhuluma, hawakuweza hata kujenga nyumba, kila walichofanya kilishia kibaya.


Lakini hayo hayakunisumbua sana, kilichonisumbua sana akilini ni mawazo ya hatima yangu, tumboni nina kiumbe, je ni mtoto kweli,...na kama sio mtoto itakuwa ni nini...na huenda akawa ni mtoto, atakuwaje nikijifungua, na  mpaka hapo , maelezo yote ya huyo mbaba, hakuna sehemu inayofichua ukweli wa hii mimba, ni nani anahusika, sio hoja kwangu, hoja ni je atazaliwa kiumbe wa namna gani


Nikawa najiuliza sana hilo swali, lakini hata nikijiuliza ni nani atafahamu, hapo nikaona nimuachie mola mwenyewe,, ..kila nilichowaza hapo hakikuwa na ufumbuzi, ..nikiisia kujiuliza tu, kwanini mimi…kwanini mimi nizalilishwe hivyo, kwanini mimi yanitokee hayo yote, nimekosa nini jamani…’hapo machozi yakawa yanazidi kunitoka kwa wingi.



 Sasa nikaona mawazo hayo hayatanisaidia, ndio nikazama kwenye imani ..nikawa sasa namuomba mola wangu nikisema kimoyo moyo…


.
'Ewe mola wangu, nisamehe kwa dhambi hii, mimi sijui nimetenda madhambi gani hadi haya yanikute, wewe peke yake ndiye unaye ujua ukweli wa haya yote, mimi ni kiumbe dhaifu tu,..uwezo wa kuyabeba haya kwa hivi sasa sina tena.., kama kweli wapo watu wenye uwezo wao waliamua kuyafanya haya, wewe unawajua, na sipendi kusikia tena walitaka nini kwangu, na hata hivyo, mimi sina nia ya kuwaombea mabaya,...wasamehe tu... na sina lengo la kulipiza kisasi, ninachokuomba uwasamehe tu hilo kwangu ni faraja…’nikapandisha viganga vyangu usoni na kuyafuta machozi.


‘Nakuomba mola wangu uwasamehe, hususani huyu baba hapa, nawatambua hawa kama walezi wangu, najua walichokifanya ni kibaya, lakini ni katika kuhangaika kwao, walijua wakifanya hivyo labda watafanikiwa lakini ni shetani tu kawazidi nguvu, mimi nakuomba uwasamehe, na nitajua kuwa umewasamehe kama nilivyowasamehe mimi, nikisikia wamesameheana na kurejeana kama mke na mume....' hapo ni machozi tu yanatoka,..hata nilipojitahidi kuyazuia sikuweza.


‘Nakuomba  ewe mola wangu, na huyo kijana wao, apone, aondokane na mitihani inayomakabili arudi na kuungana na wazazi wake..hili kwangu litakuwa ni faraja kubwa sana, na huyo binti naye aachiwe awe huru, kwani na yeye ni miongoni mwa waathirika wa mitihani hii ambayo, wewe peke yake ndiye unajua ni kwanini ilifanyika kwetu, huyo binti kadhulumiwa na yeye, lakini najua na yeye atasamehe , na kusamehewa,..nakuomba ewe mola wangu wangu unitimizie maombi yangu hayo, ..sijui nifanye nini ili unitekelezee hayo maombi yangu…’nikainua viganja vyangu na kufuta machozi yangu tena.

Hapo nikahisi hicho kiumbe tumboni kikinikwangua, nilihisi maumivu na baadae yakapoa, nikaendelea na mawazo yangu sasa yakiwa ya kuomba tu.....

‘Pamoja na hilo, …nakuomba mola wangu, kinyume na imani za hao watu walionifanyia hivyo, nakuomba tena na tena hii mimba, huu, uja uzito uwe ni faraja, kwangu, nimzae mtoto aje kunifuta haya machozi, zaidi ya wewe sina wa kumtegemea, zaidi ya huyo mtoto hakuna wa kunifuta haya machozi.....’hapo sikuweza kuvumilia  nilijikuta nikilia kilio cha kwikwi , na muda huo ndio watu wote mle ndani walikuwa wamenigeukia..mimi....hapo sijijui nimezama kwenye duwa, kwenye maombi kwa mola wangu

 Kumbe wawili hawa wapo mbele yangu  wamepiga magoti  mimi sijui...ao wanajua nalia kutokana na hayo yaliyotokea, wao wananibembeleza ili niwasamehe..sijui ...na ndipo akili ikafunguka,, na kutoka kule kwenye imani, na mawazo niliyokuwa nayo yakapotea na kuwaona wawili hao wamenipigia magoti baba na mama mfadhili.

‘Kwanini…mnafanya hivyo…?’ nikauliza, huku nikihangaika kujifuta machozi...

‘Kwanini wewe unalia, ina maana muda wote ulikuwa kwenye mawazo, na hata hujui  tulichokuwa tunaongea..?’ akauliza mama Ntilie

‘Oh, kwakweli,  nilipotea, nisameheni sana, ila…mimi sina kinyongo na nyie wazee wangu naombeni msimame, msifanye hivyo, mimi sio mtu wa kupigiwa magoti, hamuniamini kuwa mimi nilishawasamehe nyote, mimi nawauliza tu, je nyie wawili mumeshasameheana..?’ nikawauliza

Wote mle ndani wakashikwa na mshangao, na mama Ntilie akasema

'Inaonekana hukuwepo humu ndani kabisa...'akasema mama Ntilie.


Na wawili hao wakaangaliana, na tabasamu likatawala kwenye midomo yao, na kwa pamoja wakasema

‘Ndio….kwa ajili ya familia, kwa ajili yako, na kwa ajili ya mola wetu tumesameheana…’wakasema, hapo kiukweli nilijikuta machozi yakitoka  tena lakini sasa kwa furaha, kilichoendelea hapo ni furaha, .....na baadae tukaongea kidogo wao wakaaga kuondoka kwani walikuwa wakisubiriwa na familia zao,  na kabla hawajaondoka simu ikapigwa, kijana wao kaachiwa, yupo huru, ila yule binti bado kashikiliwa, hata hivyo, hata yeye atachiwa baadae.

Mambo hayo yalitokea siki hiyo hiyo...

Kwahiyo familia hiyo ikaondoka ikiwa na furaha...na hakuna aliyefikiria kuniuliza vipi hatima yangu itakuwaje,..hilo sikujali, moyoni nilijua, kama hayo yametokea, ina maana duwa langu kwa muumba limeshapokelewa, ...najua hata mimi mambo yangu yatakuwa mazuri,..mungu hamtupi mja wake...imani yangu ilisema hivyo


‘Siamini,...ina maana hao watu wamesameheana, kiukweli.. kwani ilikuwaje…, unajua mimi nilipotea, nikazama kwenye mawazo ilikuwaje, hebu niambie jamani...?’ Hayo nilimuuliza mama Ntilie, wakati wawili hao wameshaondoka..

Muda wa kunisimulia hayo haukupatikana, wageni, wateja..ikawa kazi siku hiyo ikapita, na kesho yake ukaingia ugeni...


NB: Tutakutana kwenye hitimisho


WAZO LA LEO: Tujiepushe sana na tabia ya kiburi, hasa ukijaliwa mali, nguvu, cheo au na neema yoyote ile, usijione wewe umefika, usijione kuwa umevipata hivyo kwa ujanja wako, jiulize wangapi wenye uwezo kama wako, walikuwa na akili sana madarasani, walikuwa na namna nyingi sana, lakini hawajapata kama ulivyopata wewe, sio kwamba wao ni wajinga hawaju njia za kupata kama ulivyopata wewe, ..ni neema za mola ambaye humpa mja wake kwa kadri aonavyo ni sawa, basi ukipata mshukuru mola wako, na saidia wenye kutaka msaada, na shukuru na kuwaombea wasio nacho wapate kama wewe au zaidi yako.

Ni mimi: emu-three

No comments :